Hadithi ya kusisimua: Vita ya wachawi

Hadithi ya kusisimua: Vita ya wachawi

HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-7

ILIPOISHIA:
“Mbona hiyo adhabu ni ndogo kuliko uliyotaka kuitoa?”
“Tufanye isiyoendana na tukio la kumtia mimba mtoto wetu.”
“Nilikueleza awe mbali na wanawake kwa kumuua nguvu za kiume.”
“Tutafanyaje bila kumshirikisha Atu ambaye siamini kama atakubali.”
“Tutatengeneza uongo kwamba akifanya hivyo basi mpenzi wake hawezi kumuacha. Kwa vile hatujaonesha kukemea kilichotokea itakuwa njia rahisi kutimiza dhamiri yetu.”
SASA ENDELEA…


“Basi tufanye hivyo.”
Walikubaliana kumwita Atuganile na kumweleza kitu cha kumfanyia mpenzi wake kama kuongeza mapenzi kumbe kummaliza. Aliitwa Atuganile aliyekuwa akiosha vyombo.
“Atu,” mama yake alimwita kwa sauti.
“Abee mama.”
“Njoo mara moja.”
Atuganile aliacha kuosha vyombo na kusuuza mikono yake na kuwafuata wazazi wake waliokuwa wamekaa pembezoni mwa nyumba wakizungumza.
“Abee,” aliitikia huku akifuta maji kwenye khanga aliyojifunga.
“Kaa hapo,” alisema baba yake, naye alitii amri na kukaa kitako.
“Atu,” mama yake alimwita.”
“Abee mama.”
“Nina imani umejua kilichotokea wewe na mpenzi wako?”
“Ndiyo.”
“Tuna imani unampenda sana Ambakisye?’
“Ndiyo mama.”
“Sasa kuna dawa tutakupa ambayo ukikutana na mwenzako kimwili hakikisha unajipaka mkononi na kumpaka sehemu za siri ili asiweze kukuacha.”
“Jamani Ambakisye hana tatizo bali wazazi wake sasa hiyo dawa ya nini?”
“Sisi ndiyo tunajua hebu fanya zoezi hilo kisha tuangalie nini kinaendelea.”
“Sawa wazazi wangu.”
“Lini unaonana naye?”
“Hata leo.”
“Basi subiri,” mama yake alisema huku akinyanyuka kuelekea ndani, baada muda alirudi akiwa na karatasi na kumpa Atuganile.
“Hakikisha unampaka baada ya tendo na si kabla.”
“Sawa mama.”
“Haya malizia kuosha vyombo uwahi kwa mwenzio.”
“Sawa mama.”
Atuganile alinyanyuka na kuingia ndani kuweka dawa yake na kurudi kuendelea na kazi ya kuosha vyombo ili baadaye aende kwa mpenzi wake.
****
Ambakisye akiwa anajiandaa kutoka kumfuata mpenzi wake alisikia mlango ukigongwa, alipotoka alimuona mpenzi wake mlangoni.
“Ha! Atu.”
“Ndiyo mimi mpenzi.”
“Karibu mpenzi.”
“Asante,” Atuganile alisema huku akiingia ndani.
“Yaani ndo nilikuwa najiandaa kuja nawe umetokea.”
“Leo nimemaliza kazi mapema nikaona nije mwenyewe.”
“Nimefurahi kusikia hivyo.”
“Hivi kweli Amba upo tayari kuoa mwanamke mwingine?” Atuganile alimuuliza huku akikaa kitandani.
“Atu nikueleze mara ngapi mi nakupenda lakini lililoamuliwa na wazazi wangu lipo nje ya uwezo wangu.”
“Kwa hiyo upo tayari kuoa mwanamke mwingine na kuniacha mimi?”
“Hata kama nitamuoa mapenzi yangu yote yatakuwa kwako.”
“Sasa mimi nitaishi hivi mpaka lini?”
“Kwa kweli huo ni mtihani walionipa wazazi wangu.”
“Hivi kwa bahati mbaya mchumba wako akifa utakuwa tayari kunioa?”
“Hilo halina tatizo, wewe ndiye mke wangu mwingine ni kulazimishwa.”
“Halafu mchumba wako anaitwa nani.”
“Bupe.”
“Bupe nani?”
“Ambokile.”
“Kwao unapokaa unapajua.”
“Si nilikuambia Kijiji cha Kilasilo.”
“Kesho nina safari ya Kilasilo nimetumwa nilitaka unipeleke na baiskeli yetu, lakini nina wasiwasi mchumba wako atakuona ukinisindikiza nami siwezi kwenda peke yangu.”
“Usiwe na wasiwasi nitakusindikiza tu kwa vile yeye amekukuta kama akisusa si itakuwa nafasi yako.”
“Nimefurahi kusikia hivyo, kweli unanipenda mpenzi wangu.”
“Hata wewe unajua.”
Baada ya mazungumzo ambayo yalitawaliwa na siri nzito mioyoni mwa wapenzi wawili toka katika familia zao. Walizama kwenye mahaba mazito mwisho wa safari Atuganile alimpaka dawa aliyopewa na wazazi wake sehemu za siri bila kujua anamuumiza mpenzi wake.
Baada ya kustareheshana kama kawaida Ambakisye alimsindikiza mpenzi wake mpaka kwao na yeye kurudi kulala bila kupeleka dawa aliyopewa na wazazi wake akaitege mlangoni kwa mpenzi wake.
Atuganile aliamini huenda dawa aliyomfanyia mpenzi wake itasaidia Ambakisye asioe.
Siku ya pili alikutana na wazazi wake na kuwaeleza kila kitu kimekwenda kama walivyomuagiza.
“Hukukosea?” mama yake alimuuliza.
“Sikukosea nilikuwa makini sana.”
“Basi kazi yako umemaliza tuachie sisi.”
“Sawa mama.”
Kwa vile asubuhi ile alikuwa na safari ya kwenda Kilasilo alipotumwa na bibi Tumwambilile. Walikubaliana na mpenzi wake wakutane mbele ambako hakuna mtu atajua safari ile wamekwenda pamoja. Atuganile alisubiri wazazi wake waende shamba alichukua baiskeli na kutoka nayo. Kwa vile alikuwa akijua kuendesha alimpitia Ambakisye ili kumjulisha anatangulia.
Ambakisye alimfuata mbele na kupakizana kwenye baiskeli na kuelekea Kijiji cha Kilasilo, Atuganile alianza kwa kumpakia mpenzi wake alipochoka Ambakisye alichukua baiskeli na kumpakia mpenzi wake mpaka walipofika.
Walifika Kijiji cha Kilasilo saa sita mchana, kwanza Atuganile aliomba apelekwe Mto Kiwira sehemu ambayo watu wanatumia kwa huduma muhimu za kufua, kuoga na kuosha vyombo.
Alipofikishwa aliteremka mtoni na kujifanya ananawa na kuchukua maji ya mto na kuweka katika kichupa kidogo na kuchuma majani yaliyoingia mtoni kisha alirudi mjini ambako alimuomba mpenzi wake amsubiri sehemu na yeye kuchukua baiskeli na kwenda mbele na baadaye kurudi kwa mpenzi wake huku akitengeneza uongo.
“Yaani nimefanya kazi bure,” Atuganile alijifanya kusikitika.
“Kwa nini?”
“Wamesema amekwenda Isaki mpakani.”

Itaendelea
 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-8

ILIPOISHIA:
"Yaani nimefanya kazi bure," Atuganile alijifanya kusikitika.
"Kwa nini?"
"Wamesema amekwenda Isaki mpakani."
SASA ENDELEA


"Basiturudi nyumbani."
Walikubaliana kurudi nyumbani, walifika nyumbani majira ya saa moja na nusu usiku, baada ya kuagana, Atuganile hakwenda nyumbani kwao, alichepuka na kukimbilia kwa bibi Tumwambilile. Alipofika alimpa mzigo aliotumwa.
"Bibi mzigo huu hapa."
"Ulienda na nani?"
"Na Ambakisye."
"Ulimwambia unaenda kufanya nini?"
"Nilimwambia nimetumwa na mama, lakini nilifanya vitu vyangu bila kujua chochote."
"Jina la mchumba wake?"
"Bupe Ambokile."
"Basi mjukuu wangu kapumzike kazi yote niachie mimi ila kitakachotokea ibakie siri yako hata wazazi wako usiwaambie."
"Siwaambii ndiyo maana nilikuja peke yangu."
"Basi majibu utayapata kwa siku mbili kuanzia kesho."
"Nitafurahije bibi, nimeumia sana kumkosa Ambakisye."
"Najua ndiyo maana kazi yako sikumpa mtu yeyote, nitaifanya mwenyewe."
"Nakuamini bibi, nitakupa zawadi nzuri."
"We iandae tu."
Atuganile aliagana na Bibi Tumwambilile na kurudi nyumbani ambako aliwakuta wazazi wake waliotaka kujua alikuwa wapi siku nzima.
Alidanganya alimsindikiza mpenzi wake Ambakisye Kijiji cha Mbako.
"Njiani hamkufanya chochote?"
"Hatukufanya chochote, tumekwenda na kurudi."
"Mmh! Sawa, lakini kwa nini hukuaga?"
"Niliogopa mnaweza kunikatalia nami sitaki kumuudhi mpenzi wangu, nina imani dawa niliyompaka itafanya kazi. Nimefurahi wazazi wangu kuupigania moyo wangu. Maana nilikuwa najiuliza uso wangu nitauweka wapi."
"Usiwe na wasi kila kitu kitaenda vizuri."
Baada ya kula alijipumzisha kumsubiri mpenzi wake kwa vile alikuwa amechoka sana kwa ajili ya kuendesha baiskeli masafa marefu huku amempakia mtu.
***
Usiku wa saa tatu, kama kawaida Ambakisye alitoka nyumbani kwao kumfuata mpenzi wake. Kabla hajatoka, alikumbuka dawa aliyopewa na wazazi wake ya kwenda kuitega mlangoni kwa mpenzi wake ambayo jana yake aliisahau akiamini kufanya vile ni kuzuia ujauzito ambao wazazi wake walitaka kuutoa.
Baada ya kuichukua dawa, alikwenda mpaka kwenye chumba anacholala mpenzi wake, kabla ya kumgongea aliinyunyizia kukata mlango ili akitoka airuke.
Aliifanya kwa umakini mkubwa huku akiangalia nyumba ya wazazi wake waliokuwa wamelala, baada ya kulifanya zoezi aligonga dirisha la mpenzi wake ambaye muda huo alikuwa amepitiwa na usingizi kutoka na uchovu wa safari.
"Atu..Atu," alimwita kwa sauti ya juu kidogo.
"Mmh!"
"Mi Amba."
"Ooh! Mpenzi."
"Eeh! Nimefika."
"Nakuja."
Atuganile aliamka na kujifunga upande wa kanga kwa vile alilala na gauni akimsumbiri mpenzi wake na kutoka nje. Kutoka na maelezo aliyopewa Ambakisye na wazazi wake kuwa lazima aruke ile dawa, alisimama mbele kidogo ya mlango.
Baada ya Atuganile kufungua mlango, alimfuata mpenzi wake aliposimama na kuruka dawa aliyotegewa bila kujua huku Ambakisye akifurahi kumuokoa mwanaye aliye tumboni bila kujua alikuwa akimuua.
Baada ya kutoka ndani kabla hajamkumbatia mpenzi wake alisikia kitu kikimkata ghafla chini ya kitovu na kupiga kelele ya maumivu.
"Mama nakufa," alisema huku akiinama akiwa ameshika tumbo.
"Nini mpenzi wangu?" Ambakisye alishtuka.
"Nimesikia kitu kikinikata chini ya kitovu," alisema kwa sauti ya maumivu.
"Mmh! Nini tena?" Ambakisye alimshika mpenzi wake aliyekuwa ameinama bado ameshika tumbo.
"Usiwe na wasi mpenzi ni mshtuko tu," Atuganile alisema huku akinyanyuka baada ya maumivu kukata ghafla.
"Vipi?"
"Nipo sawa, tunaweza kwenda."
Waliurudisha mlango na kuondoka kuelekea kwa mpenzi wake, walipofika kama kawaida waliingia chumbani kwao. Baada ya mazunguzo walijiandaa kwa ajili ya kustarehe.
Kila Atuganile alivyomuandaa mwenzake kama kawaida alishangaa mpenzi wake kuwa baridi.
"Mmh! Amba vipi leo?"
"Hata mimi nashangaa."
Atuganile hakukata tamaa, aliendelea kumuandaa mpenzi wake mpaka jasho likamtoka japokuwa kulikuwa na hali ya baridi. Lakini ilikuwa hali ileile maiki kuendelea kutotoa sauti na sinyaa kitu kilichowashtua wote.
"Amba umekuwaje leo mpenzi?"
"Yaani leo nashangaa toka nizaliwe sijawahi kutokewa na hali hii."
"Sasa hii ni nini?"
"Labda uchovu wa safari," Ambakisye alijitetea.
"Si kweli mbona uliniambia kuna siku ulikwenda na baba yako Isaki na wewe ndiye uliendesha kwenda na kurudi lakini jioni tulipokutana ulikuwa kwenye hali ya kawaida?"


Itaendelea kesho jioni....
 
Mhh kitoto kshakufa..mzee wa kazii kagoma kusimama dede...uchaw kweli siyo dilii
 
Mtumeeeeeeeeeeeee hii Kali, mtoto kafa bwana harus ndio hivyo tena na kule bibi harus tumeambiwa tusubir siku mbili tutasikia tu ,mmmh sipat picha
 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-9

ILIPOISHIA:
Atuganile hakukata tamaa, aliendelea kumuandaa mpenzi wake mpaka jasho likamtoka japokuwa kulikuwa na hali ya baridi. Lakini
ilikuwa hali ileile sehemu kuendelea kusinyaa badala ya kunyanyuka kitu kilichowashtua wote.
“Amba umekuwaje leo mpenzi?”
“Yaani leo nashangaa toka nizaliwe sijawahi kutokewa na hali hii.”
“Sasa hii ni nini?”
“Labda uchovu wa Safari,” Ambakisye alijitetea.
“Si kweli mbona uliniambia kuna siku ulikwenda na baba yako Isaki na wewe ndiye uliendesha kwenda na kurudi lakini jioni
tulipokutana ulikuwa kwenye hali ya kawaida.”
SASA ENDELEA…


“
Sasa hii sijui nini?” Ambakisye alishangaa.
“Kwanza mbona sehemu zako zimezidi kusinyaa.”
“Mmh! Hili litakuwa tatizo,” Ambakisye aliingiwa wasiwasi.
“Sasa tutafanyaje?”
“Acha nikusindikize kwenu ili niangalie hali hii mpaka kesho.”
“Mmh! Sawa,” Atuganile alikubali kwa shingo upande.
Walikubaliana kusindikizana baada ya kila mmoja kuvaa nguo zake, walikwenda hadi nyumbani kwa Atuganile na kuagana kwa shingo
upande. Ambakisye alirudi nyumbani na kuingia chumbani kwake, hakuamini hali iliyomtokea, alisogeza taa kujiangalia.
Maumbile yake yalikuwa madogo tofauti na umbile lake halisi la kuzaliwa.
Hakutaka kuwa na haraka, alilala ili kesho ajitazame hali yake, kama itaendelea kuwa vile basi angemueleza baba yake. Upande
wa pili, Atuganile alishtushwa sana na hali ya mpenzi wake Ambakisye, akawa na wasiwasi na dawa aliyopewa na wazazi wake
ampake sehemu za siri huenda ndiyo iliyokuwa imemfanya awe vile.
Alipanga asubuhi kumuuliza mama yake hali iliyomtokea mpenzi wake, ili amsaidie kwani aliogopa kama ile hali itaendelea
lazima mapenzi yao yataingia dosari. Baada ya kuwaza sana alipitiwa na usingizi. Usiku wa manane tumbo lilianza kumsokota na
kufanya asikie maumivu makali.
Baada ya kuvumilia labda ile hali itapoa lakini kila dakika maumivu yalizidi, ilibidi anyanyuke ili akafie kwa wazazi wake.
Aliponyanyuka damu nzito nyeusi zilianza kutoka sehemu za siri. Alitembea kwa kupepesuka huku akijitahidi kuwaita wazazi wake
kwa sauti ya juu.
“Mamaaa nakufa….Nakufa mie jamani.”
Sauti ile iliwaamsha wazazi wake ambao walitoka mbio nje walishtuka kumuona Atuganile ameanguka karibu na mlango wao.
“Mungu wangu mwanangu,” mama Atuganile alisema kwa sauti huku akimkimbilia mwanaye aliyekuwa amekata kauli wakati huo.
Walimnyanyua na kumuingiza ndani na kumlaza kwenye mkeka, walishangaa kuona amejaa damu nyeusi miguuni. Wakati huo Atuganile
alikuwa amepoteza fahamu kitu kilichoongeza taharuki kwa wazazi wake.
“Mmh! Hii nini?” Mzee Andendekisye alichanganyikiwa.
“Mume wangu tuwe makini la sivyo tutampoteza mtoto hivihivi .”
Walianza kazi ya kuhakikisha wanaokoa uhai wa Atuganile aliyekuwa bado amepoteza fahamu huku akionesha amepoteza damu nyingi.
Walijitahidi kumrudisha katika hali yake ya kawaida, ilionekana kama inashindikana kwani hakukuwa na dalili zozote za
Atuganile kuamka.
“Mume wangu hii hali inatisha.”
“Tufanyeje?” mzee Andendekisye alichanganyikiwa kwa hali ya mwanaye.
“Hebu kimbia haraka kwa bibi Tumwambilile,” ilibidi atafute msaada baada ya wao kuchemsha.
Mzee Andendekisye alitoka mbio kwenda kwa bibi Tumwambilile japokuwa usiku ulikuwa mzito uliokuwa na kiza cha kutisha kutokana na kutokuwa na mwezi angani. Alipofika aligonga mlango wa bibi Tumwambilile.
“Nani tena usiku huu?” bibi aliuliza.
“Mimi Andendekisye.”
“Baba Atu?”
“Ndiyo bibi.”
“Vipi mbona usiku?”
“Mjukuu wako anakufa huko.”
“Kafanya nini?”
“Tumesikia usiku huu akituita akisema anakufa alipotoka tulimkuta ameanguka chini huku akitoka damu nzito nyeusi katikati ya miguu akiwa tayari kapoteza fahamu.”
“Mmh! Isiwe ametoa mimba?” bibi aliuliza.
“Hatujui kwa vile toka tulipomkuta ameanguka haongei na pumzi zake zipo mbali.”
“Mmh! Hebu subiri.”
Bibi Tumwambilile alirudi ndani na kutoka baada muda na kusema:
“Mmh! Wajanja wamewawahi.”
“Una maana gani? Ina maana Atu ndiyo amekufa?” mzee Andendekisye alishtuka.
“Sina maana hiyo kuna kitu mtoto wenu alitegewa na kuruka ndicho kilichosababisha tatizo lile.”
“Tatizo gani?”
“Ujauzito umetoka?”
“Kautoa nani?”
“Kwanza twende tukamhudumie mtoto.”
Waliongozana usiku ule kuelekea nyumbani, uani kwake bibi Tumwambilile alichuma majani mabichi na kwenda nayo. Walipofika walimkuta mama Atuganile bado amemuinamia mwanaye huku akilia.
Bibi Tumwambilile alipofika pale alimkemea kwa kitendo cha kumlilia mwanaye aliye hai.
“Unalia nini wakati wewe ndiye bingwa wa kuwalipua watu, leo umewahiwa badala ya kupambana unalia, kweli vita ikitokea utaiweza?” bibi Tumwambilile alimuuliza akiwa amemkazia macho.
“Hapana Tumwambilile, sijui mwanangu amepatwa na nini, kila tulivyojitahidi kumrudisha katika hali yake ya kawaida ilishindikana,” mama alisema kwa sauti ya kilio.
“Siku zote nilikueleza ukijua kupiga ujue na kupigwa, hivyo ujue kukwepa na kujikinga. Umewahiwa unatakiwa kujua utafanyaje kumuokoa mtoto na si kulia.”
“Mpaka nalia uwezo wangu umefikia mwisho.”
“Basi tuache maneno tumsaidie mtoto, lete maji kwenye beseni.”
Walifanya vile mara moja na kumletea maji kwenye beseni , bibi Tumwambilile alimuomba mzee Andendekisye aondoke kwa vile ilitakiwa kufanyika kazi ya wanawake.
Baada ya kuondoka walimvua Atuganile nguo zote na kumlaza chali kwenye mkeka.
Walichukua majani mabichi na kuyaweka kwenye maji na kuyachikicha mpaka maji yote yakabadilika rangi na kuwa ya kijani.
“Msugue sehemu zake mpaka ndani,” bibi Tumwambilile alimuelekeza mama Atuganile. Naye alifanya kama alivyoelekezwa baada ya zoezi lile, alielezwa aendelee kumsugua mwili wote na kufanya hivyo kisha walimwosha maji yaliyobakia. Pamoja na zoezi lile
kufanyika hakukuwa na mabadiliko yoyote kwa Atuganile alikuwa amelala vilevile hali iliyozidi kumtisha mama yake.
“Tumwambilile mbona hakuna mabadiliko yoyote?”
“Kwani nimemaliza kazi yangu, mama Atu unataka kuniudhi,” bibi Tumwambilile alikuja juu.
“Basi bibi nisamehe nimechanganyikiwa mwenzio.”
“Wewe ulipotoa uhai wa mtoto wa mwenzio hukuchanganyikiwa lakini ugonjwa wa mwanao ukuchanganye.”
“Bibi eeh! Si nimekubali nimekosa.”
Bibi Tumwambilile hakusema kitu alichukua kichupa kidogo alichokuja nacho na kukiweka puani kwa Atuganile kwa muda kisha alikitoa. Walitulia kwa muda ghafla Atuganile alipiga chafya mfululizo na kutulia akiwa bado amejilaza chini.
“Atu,” bibi Tumwambilile alimwita.
“Abee,” aliitikia.
“Vipi?”
“Mmh!”
Alifumbua macho na kushtuka kumuona bibi Tumwambilile na mama yake wakiwa wamesimama pembeni yake kingine kilichomshtua ubaridi wa usiku ule.
“Jamani kwani vipi?” alisema huku akikaa na kujishangaa kukaa kwenye mkeka akiwa hana nguo mwilini huku sehemu ya mwili wake zikiwa na vipande vya majani mabichi.
“Unajisikiaje?” bibi Tumwambilile alimuuliza huku mama yake akiwa kimya kuogopa kumuudhi bibi.
“Kwani kuna nini?” bado Atuganilie hakuelewa kumemtokea nini.
“Kwani nini kimekutokea?”
Atuganile alitulia na kukumbuka kilichomtokea wakati amelala, alikumbuka tatizo lilivyoanza wakati alipofuatwa na Ambakisye.
Lakini hakutaka kusema chanzo bali tatizo lilivyompata usiku kwa kuhofia kuingiza imani za kishirikina kutoka kwa wazazi wa mpenzi wake na kuleta mzozo wa familia mbili wakati wazazi wake waliisha mhakikishia Ambakisye hawezi kuoa mwanamke mwingine.


Itaendelea Kesho wakati kama huu.
 
HADITHI YA KUSISIMUWA VITA YA WACHAWI-10

ILIPOISHIA
Atuganile alitulia na kukumbuka kilichomtokea wakati amelala, alikumbuka tatizo lilivyoanza wakati alipofuatwa na Ambakisye. Lakini hakutaka kusema chanzo bali tatizo lilivyompata usiku kwa kuhofia kuingiza imani za kishirikina kutoka kwa wazazi wa mpenzi wake na kuleta mzozo wa familia mbili wakati wazazi wake waliisha mhakikishia Ambakisye hawezi kuoa mwanamke mwingine.
SASA ENDELEA…

Baada ya kumsikiliza walimpa dawa ya kunywa ya majani mabichi yaliyofikichwa kwenye maji. Yalikuwa mengi ambayo alielezwa anywe ili kuondoa sumu iliyoingia mwilini na kusafishwa sehemu zake ambazo zilikuwa na sumu.
Baada ya kunywa maji ya dawa jagi zima, Atuganile alianza kutapika na kuharisha kwa wakati mmoja.
Walimsaidia kumshika mpaka alipomaliza walimuongeza na kufanya aende haja ndogo kwa muda mrefu kisha alipewa dawa ya unga na kunywa kwenye maji ya moto na kupumzishwa ili wajue kesho wafanye nini na kuangalia afya yake japo bibi Tumwambilile alisema ataamka hajambo kabisa.
Baada ya zoezi lile kwenda vizuri walimshukuru bibi Tumwambilile kisha mzee Andendekisye alimsindikiza mpaka kwake kisha alirudi nyumbani salama. Alimkuta mkewe akimsubiri, baada ya kuingia ndani na kufunga mlango mkewe alimwambia:
“Mume wangu hii vita, siwezi kukubali mtu amchezee mwanangu nitaununua uchawi kwa gharama yoyote nitaufuata hata Ulaya ikiwezekana.
Najua hii ni familia ya Amangise ndiyo waliofanya kazi hii ili wapate cha kusema baada ya kumharibu mwanetu. Nakwambia atakufa mtu nitahakikisha nawashikisha adabu,” alisema kwa hasira.
“Lakini mbona Tumwambilile amekataa kumtaja aliyefanya vile.”
“Hata asipomtaja waliofanya vile ni familia ya Amangise tu,” Mama Atuganile alisema.
“Inawezekana wamelipiza kisasi baada ya kumuumiza mtoto wao.”
“Walitakiwa kuja tuzungumze ili tulimalize kwa sharti la kumuoa Atu na siyo kuniulia mjukuu wangu.”
“Na kweli, mtoto wao anaweza kupona lakini hawezi kumrudisha mtoto tumboni.”
“Yaani sikubali damu ya mjukuu wangu ipotee bure nitaipigania kwa gharama yoyote, tena kuna dawa nitampa Atu akampake yule mshenzi ili sehemu zake za siri zioze kabisa asiweze kutibika popote,” mama Atuganile alisema kwa hasira.
“Kama ni hivyo basi tukio hili tufanye siri yetu Atu asijue kitu ili tuwatie adabu.”
“Hilo ndilo umesema neno.”
Baada ya makubaliano walipanda kitandani kulala.


KATIKA KIJIJI CHA KILASILO
Bupe mchumba wa Ambakisye aliyechaguliwa na wazazi wake, akiwa nyumbani peke yake baada ya wazazi wake kwenda shambani, alijikuta akiwa na hamu ya kwenda mtoni kuchota maji kitu alichokatazwa na wazazi wake.
Toka alipochumbiwa na kulipiwa mahari, wazazi wake walimkataza kutoka eneo la nyumbani kwa muda wote mpaka siku ya harusi ambayo haikuwa muda mrefu.
Siku hiyo alijikuta moyo wake ukimsukasuka kutaka kwenda kuchota maji, alisubiri wazazi wake wamekwenda shamba, alitoka hadi nyumba ya pili na kumwambia shoga yake Pendo, mtoto wa mzee Mwakasanga kuwa waende mtoni wakachote maji.
Walikubaliana na kuchukua ndoo kuelekea mtoni, walipofika waliwakuta wanawake wengi, kinamama na wasichana waliokuwa wakifua na wengine wakichota maji.
Bupe na Pendo walikunja nguo zao na kuingia ndani ya maji kuchota maji. Wakiwa wanachota maji ghafla watu wakapiga kelele baada ya kumuona mamba akielea juu ya maji akielekea walipokuwa wakichota maji.
“Jamani mambaaa!” mtu mmoja alipaza sauti.
Walipogeuka walimuona na kila aliyekuwa ndani ya maji alitaharuki kwa kutupa ndoo na kutoka mbio nje japokuwa maji yalikuwa mazito.
Ajabu yule mamba aliwaacha watu wote waliokuwa karibu na kumfuata Bupe aliyekuwa akikimbilia nje na kumpiga na mkia uliomfanya aanguke ndani ya maji.
Alimfuata na kumlalia juu na kumzamisha chini kisha aliondoka naye, hali ile iliacha taharuki kwa watu wote waliokuwa pale mtoni na kushangaa ujaji wa mamba yule ambaye alionesha kumchagua mtu na kuwaacha wote waliokuwa nyuma yake.
“Jamani hivi hali hii itaisha lini mnataka tuishi wapi? Porini wanyama wakali mjini watu wenye roho mbaya!” alisema mwanamke mmoja aliyekuwa ameshikilia mikono kichwani kwa sauti ya kilio.
“Huyu mamba si bure mkono wa mtu tokea lini eneo hili likatokea mamba?” mwanamke mwingine alihoji.
“Jamani watu wana roho mbaya yaani Bupe kutaka kuolewa watu hawajafurahi mpaka wanamtumia mamba?” mwingine aliyekuwa akimfahamu alisema huku amejishika kifuani kwa hofu ya tukio.
“Lakini jamani huu uchawi si wa maeneo yetu lazima mfanyaji amesafiri,” mwingine alichangia.
“Huu uchawi wa Malawi tu ndiyo wenye tabia ya kutumiana mamba,” mwingine aliunga mkono kauli ya mwenzake.
Wakati huo Pendo shoga yake alikuwa ameangua kilio kwa sauti ya juu kumlilia shoga yake mpaka akapoteza fahamu, kwa vile ndiye aliyefuatana naye mtoni. Baada ya kupatiwa huduma ya kwanza alielezea alivyofuatwa na Bupe kwenda naye mtoni.
“Wazazi wake wapo wapi?” mama mmoja aliuliza.
“Wameenda shamba.”
“Si nilisikia anataka kuolewa?” mmoja aliuliza.
“Ndiyo,” alijibu dada aliyemfahamu Bupe.
“Sasa ilikuwaje aje kuchota maji badala ya kukaa ndani?”
“Alikatazwa na wazazi wake asiende kuchota maji wala kutoka eneo la kwao, lakini leo nilishangaa kanifuata na kuniomba nije naye kisimani ndiyo yakatokea haya,” Pendo alipofikia hapo aliangua kilio upya kwa kujitupa chini na kuwapa watu kazi ya kumbembeleza.
Kila mmoja alisema lake, mwenye jicho la tatu alijua ule ni mchezo umechezwa kwa kutumia uchawi wa mamba ambao ulitumika sana Malawi. Ilibidi taarifa zipelekwe kwa wazazi wa Bupe waliokuwa shamba. Mama Bupe alipatwa na mshtuko uliofanya apoteze fahamu baada ya kuzipata taarifa za mwanaye Bupe na kufanya watu waliopeleka taarifa wapate kazi ya kumbeba kumkimbiza hospitali.
Taarifa za Bupe kukamatwa na mamba zilizagaa kijijini haraka kama moto kwenye majani makavu. Kwa vile upoteaji wake ulikuwa wa utata...

....Itaendelea Kesho
 
Nakukubali sana #Mzizi mkavu !
Huwa sizikosi story zako but jitahidi ifike mwisho basi na hii isiwe kama ile ya nyanyo za kuzimu (666).
 
Back
Top Bottom