ILIPOISHIA:
Lakini hali yako si bado kwa nini usisubiri upone kabisa.
Mage, mimi sijambo sasa hivi naweza kufanya lolote, lakini afya ya mpenzi wangu siijui. Mpaka leo bado yupo hospitali huenda yupo kwenye hali mbaya lazima niende nikajue hali yake.
SASA ENDELEA...
Mmh! Sawa, Mage aliogopa kutia neno kwa kuhofia kukorofishana na Colin ambaye alionekana bado ana mapenzi mazito na Cecy. Alijua msimamo wake ni kwa vile hajamwona lakini akimwona hali yake aliamini lazima angebadili mawazo na nafasi ile kumpa yeye.
Wakiwa katikati ya mazungumzo walishtuliwa na hodi, waliponyanyua macho Colin hakuamini kumwona mama Cecy aliyejua yupo India na mpenzi wake, lakini afya yake ilionekana imedhoofu sana.
Ha! Mama ni wewe? Colin alisema huku akinyanyuka na kwenda kumpokea mama mkwe.
Ni mimi mwanangu, unaendeleaje na wewe?
Namshukuru Mungu, hali yangu sijambo. Sasa hivi nilikuwa nasema wiki ijayo nakuja India kumwona mchumba wangu. Ha..ha..lafu mbona uko huku Cecy umemwacha na nani hospitali?
Kwani mama yako hajakwambia?
Kuhusu nini?
Kurudi kwetu, nimemuulizia ameniambia hali yako bado si nzuri, hivyo nikaona nije nikujulie hali baba yangu na kumwacha mchumba wako na msichana wa kazi.
Mama unataka kuniambia Cecy yupo Tanzania? Colin alishtuka huku macho yamemtoka pima.
Colin unauliza ukweli au unatania?
Mama mimi na wewe hutujawahi kutaniana, hata muulize Mage muda si mrefu nilikuwa namwambia lazima nije India kumjulia mchumba wangu hali yake baada ya mimi kuamini nimepona.
Siamini unachokisema najua unaumwa hivyo hukuwa na uwezo wa kuja kumpokea mchumba wako, lakini sikubali kauli yako kuwa huna taarifa yoyote kuwa mimi na Cecy tupo nchini kwa wiki sasa.
Wiki!? Colin alishtuka.
Colin hebu acha kujitoa akili, ina maana mama yako hajakwambia?
Hajaniambia, ina maana mama anajua?
Mbona ndiye aliyetupokea na kila siku lazima afike kumuona mgonjwa kasoro leo.
Mmh! Unamaanisha mama yangu, mama Colin?
Ndiye huyohuyo, inamaana hajakwambia?
Haki ya Mungu sijui kitu, sikuwa mgonjwa wa kushindwa kuja kumpokea mpenzi wangu, kwa nini mama kanificha hivi, Cecy mpenzi wangu atanielewa vipi? Colin alisema kwa uchungu.
Sijui, labda muda wake wa kukueleza bado, lakini namshukuru sana amejitolea kwa hali na mali ili kuhakikisha afya ya mpenzi wako inatengemaa.
Vipi hali ya mpenzi wangu?
Bado, lakini ana afadhali kwa mbali.
Colin alinyanyuka na kumwomba mama Cecy aende akamwone mpenzi wake.
Mama naomba nikamwone mpenzi wangu.
Colin pumzika kwanza hujapona vizuri, nilikuja kukuona tu.
Hapana...kama Cecy ana wiki hapa mama kanitendea unyama mkubwa sana, Colin alisema huku akionekana kuchanganywa na taarifa zile ambazo hakutegemea kusikia kwa kuamini Cecy bado yupo India.
Colin hakusema kitu alikwenda ndani na kuchukua ufunguo wa gari na kutoka.
Mama naomba twende, Colin alipagawa na kusahau muda mfupi alikuwa na Mage alitoka bila hata kumuaga na kumfanya Mage aumie moyoni kuona ana kazi kubwa ya kuubadili moyo wa Colin. Lakini aliamini kifo cha Cecy ndiyo tiketi yake ya kuwa na Colin, aliendeleza dua za kuomba kifo cha Cecy.
Colin japo alikuwa hajaruhusiwa kuendesha gari, alikwenda kuchukua gari na kumwomba mama Cecy waondoke. Waliongozana hadi kwenye gari na kuondoka kuelekea kwa Cecy. Wakiwa ndani ya gari, Colin alimdodosa mama Cecy.
Mama kwanza vipi hali ya mchumba wangu?
Hajambo, lakini bado.Bado nini kinamsumbua?
Siwezi kukueleza kwa vile unakwenda mwenyewe kila kitu utakiona.
Mmh! Sawa.
Colin aliendesha gari huku akiwa na mawazo mengi juu ya mama yake kukaa kimya huku kila siku anakwenda kumwona mgonjwa bila kumwambia alijiuliza alikuwa na maana gani na mchumba wake angemwelewa vipi kama amerudi bila kwenda kumwona.
Walipofika walikwenda hadi ndani, Colin alionekana mwenye kimuhemuhe cha kumwona mpenzi wake. Kwa vile alikuwa akikijua chumba cha Cecy, aliingia moja kwa moja. Lakini chumbani kwake hakuwemo alitoka na kukutana na mama Cecy.
Mama mpenzi wangu yupo wapi? Colin aliuliza macho yamemtoka pima na presha juu.
Colin taratibu umefika utamuona, subiri, mama Colin alisema huku akielekea chumba alicholazwa Cecy.
Alipogusa mlango alishtuka kusikia Cecy akimwita sauti ambayo ilipotea toka alipopata ajali.
Mama...mama.
Alisogea haraka kitandani na kuitikia.
Abee mwanangu.Nigeuze nimechoka kulala hivi?
Nini kilitokea? Usikose wiki ijayo.