TEMBO KICHAKA
Senior Member
- Aug 3, 2014
- 137
- 89
safi sana mkuu story imesimama......!
Mkuu hebu endelea kidogo hadithi hii ina muda haijaendelezwa.
Wakili wa Moyo-36
ILIPOISHIA:
Colin nasema hivi, kila usemalo ni kweli tupu na una haki yoyote ya kufanya lakini kumbuka penzi halilazimishwi, nina imani umenielewa, kuwa mstaarabu tuachane kwa usalama.
SASA ENDELEA
Mage alinyanyuka na kumsogelea Colin aliyekuwa ameinama akilia na kumpigapiga mgongoni.
Sweet naomba usilie mwanaume kaumbwa kukabiliana na matatizo, hili ni moja wapo.
Colin alinyanyuka kama mbogo na kumsukuma Mage aliyeanguka chini huku akibwata.
Muongo mkubwa, mnafiki unanipaka mafuta kwa mgongo wa chupa, eti sweet.
Huwezi amini Colin nakupenda sana japo Hans nampenda zaidi, nipo tayari kulipa gharama zote za maandalizi ya harusi yetu pia hata kulipa gharama zozote ili kuhakikisha nawe unakuwa na mke atakayeziba pengo langu.
Mage pamoja na kusukumwa, hakukasirika akaamka pale chini, Colin hakumjibu neno lolote zaidi ya kuinama huku akilia.
Mage alimshika mkono na kumnyanyua, alimtazama kwa macho yaliyojaa machozi na kusema kwa sauti ya chini.
Colin nisamehe sana siwezi kuwa mnafiki mapenzi nayajua, nipe ruksa mpenzi wangu. Nilikuja huku ili tupate muda wa kulizumgumza hili, sikutaka tulizungumze juujuu. Nakupenda lakini sitaki nikutese kwa kukunyanyasa kimapenzi kwa vile mapenzi nayajua yanavyoumiza.
Colin alitulia huku akimtazama Mage aliyekuwa akitia huruma, alijiona mjinga kulazimisha mapenzi. Alikohoa kidogo na kusema:
Sawa nimekuelewa.
Nashukuru.
Kuna la zaidi? Colin alimuuliza Mage.
Hakuna.
Tunaweza kuondoka.
Walichukua vitu vyao na kuelekea nje kwenye gari ili warudi mjini.
***
Cecy baada ya kutoka twisheni, alisimama chini ya mti kuagana na shoga yake huku wakijikumbusha baadhi ya mada walizopewa wakasome nyumbani. Alikuwa amepiga hatua kubwa katika kusoma na kuandika hata kuzungumza lugha ya Kingereza baada ya kusoma kwa uchungu mkubwa.
Siku zote aliamini kumkosa Colin kulitokana na kukosa elimu, kwake umaskini hakuuona sababu kama angekuwa na elimu yake ambayo hata mama Colin angeiheshimu.
Toka aanze kusoma alionekana ndiye mwanafunzi aliyetaka kujua lugha, kuisoma, kuiandika na kuizungumza.
Japokuwa hakukijua sana Kiingereza lakini aliweza kumsikia mtu na kumuelewa hata kumjibu mawili matatu, ile ilimpa kiburi cha kuzungumza muda wote hata alipokosea hakujisikia vibaya kwa vile alielekezwa. Baada ya kujadiliana na shoga yake, alisogea mbele kuelekea njia ya kwao japo palikuwa mbali kidogo lakini hakujali umbali ule kutembea kwa miguu kwa vile alikuwa akitafuta kitu.
Siku zote aliingia darasa la mchana kwa vile asubuhi alikuwa akienda kwenye biashara zake.
Ada ya mwanzo alitumia fedha aliyoachiwa na Colin siku aliyompeleka kwao na kuwaacha kwenye mataa kwa ahadi tamu ya kuyabadili maisha yao. Alikumbatia daftari lake na kutembea taratibu kukifuata kichochoro cha kuingilia njia ya mkato. Aliangalia saa yake, ilimuonesha ni saa kumi na moja na nusu jioni.
Alishtushwa na sauti ya gari aina ya Nisan Patrol New Model jeupe lililosimama nyuma yake, alipogeuka aliona msichana akiteremka kwenye gari huku akibwata kwa sauti kuonesha anazozana na mtu ndani aliye ndani ya gari.
Alipomuangalia aligundua ni Mage, mwanamke aliyezima ndoto zake za kuwa mke wa Colin. Alisimama nyuma ya mti kumuangalia, alimsikia akisema kwa sauti:
Wewe mtu gani unayelazimisha mapenzi, nimekueleza ninaye ninayempenda hutaki kunielewa. Naomba uteremke kwenye gari langu, siwezi kutembea na mtu asiyeelewa. Sasa hiyo elimu uliyosoma inakusaidia nini ikiwa hutambui nini maana ya upendo?
Nasema teremka la sivyo nitakuachia gari niondoke zangu.
Baada ya muda, Cecy alishtuka kumuona mwanaume aliyekuwa akiambiwa vile ni Colin, baada ya kuteremka kwenye gari kinyonge, alisogea pembeni na kusimama bila kujua nyuma yake yupo Cecy.
Cecy roho ilimuuma kuona mtu ampendaye anadhalilishwa vile. Colin alitokwa na machozi kitu kilichozidi kumuumiza moyo Cecy na kushangaa watu ambao muda si mrefu walitegemea kufunga ndoa lakini ajabu mwanamke anatoa maneno makali kama yale ya kumdhalilisha mumewe mtarajiwa.
Alitulia aione sinema ile inaishaje kwa kujificha nyuma ya mti ili wasimjue, baada ya muda alisikia sauti ya Colin.
Mage pamoja na hayo lakini kumbuka ...
Itaendelea............