Hadithi: Wakili wa moyo

Hadithi: Wakili wa moyo

LIPOISHIA :
BAADA ya kutoka gym wakati wa kurudi
nyumbani, Cecy alionekana mtu mwenye
mawazo mengi kitu kilichomfanya apoteze
uchangamfu wake wa kawaida .
SASA ENDELEA .. .
“Bebi. ”
“Abee , Cecy alitikia huku akichukua chupa ya
juisi.
“Vipi mazoezi ya leo yamekuchosha?”
alimuuliza huku akimtazama .
“Hapana kawaida tu,” Cecy alimjibu bila
kumtazama.
“Mbona huna uchangamfu wako wa kawaida.”
“Kuna kitu kinaniumiza kichwa , nafikiria
kubadili uamuzi .”
“He ! Uamuzi tena mpenzi wangu ?” Colin
alishtuka kidogo agongane uso kwa uso na
gari lililokuwa likija kwa mbele yao lakini
alijitahidi kulirudisha sehemu yake ...
“Ndiyo mpenzi kuna jinamizi linataka kuivamia
furaha ya moyo wangu .”
“Jinamizi gani tena mpenzi wangu ?” Colin
aliipaki gari pembeni ya barabara ili amsikilize
vizuri mpenzi wake .
“Colin naomba unisikilize vizuri .”
“Sawa mpenzi . ”
“Nimeamua kuvunja mkataba wa kwenda
kufanya maonyesho nje ya nchi.”
“He ! Kwa nini jamani? Si nimekubali kufunga
nawe ndoa ndipo uondoke, ” Colin alishtuka .
“Hukumu ya Hans imeondoa kabisa amani ya
moyo wangu. ”
“Kivipi mpenzi ?”
“Najua nikiondoka utarudiana na Mage .”
“Siwezi ...siwezi mpenzi , yule ni matapishi
sitayarudisha mdomoni mwangu .”
“Hapana Colin , yule mwanamke nikiondoka
lazima atatumia hila za kike kukurudisha
mikononi mwake na mimi kutoka kapa . Kwa
hiyo mimi siendi popote wapigie simu waeleze
nimevunja mikataba yote .”
“Mpenzi utafungwa , una hela za kuwalipa ili
kuvunja mikataba ?”
“Kwani kazi nimeanza?”
“Hakuna kitu kama hicho , ukitaka fanya hata
mwaka mmoja ndipo uvunje. ”
“Basi kama hivyo tutaondoka wote kwenda
huko nitakapokuwa .”
“Sawa hakuna tatizo lakini usiache kazi .”
“Hapo tutaelewana kidogo na sitaki kumuona
Mage kwenu wala kukupigia simu. ”
“Yote yanatekelezeka mpenzi wangu.”
Kauli ya Colin ilirudisha furaha ya Cecy na
kujikuta akitabasamu na kumnywesha juisi
mpenzi wake aliyekuwa amezima gari kwa
mshtuko. Aliwasha gari na safari ya kurudi
nyumbani iliendelea . Wakiwa njiani simu ya
Colin iliita , Cecy aliichukua na kuangalia na
kukuta haina jina alimpa Colin.
“Mpenzi pokea simu. ”
“Kapiga nani?”
“Haina jina . ”
“Achana naye .”
“Hapana pokea hujui nani anakupigia .”
Colin aliichukua siku na kupokea :
“Haloo.”
“Ooh! Mpenzi wa maisha yangu, za toka jana
mahakamani nina imani unajua kabisa sasa
ndiyo nafasi yetu ya kufunga ndoa na kuwa
mke na mume?”
“We ! Nani ?” Colin pamoja na kujua aliyepiga
simu ni Mage alijifanya hamjui aliyepiga ili
Cecy asijue kitu .
“Colin mpenzi kipi kilichokufanya usahau sauti
ya malkia wa moyo wako au sababu ya hicho
kinyago?”
“Jitambulishe au siyo nakata simu ,” Colin
alijifanya kuja juu .
Cecy alishtuka majibu ya mpenzi wake lakini
alitulia amalize kuzungumza ndipo amuulize .
“Ni mimi Mage mwanamke pekee
uliyeshushiwa na Mungu , amini kufungwa kwa
Hans Mungu ametenda ili ile ndoa yetu ya
ahadi itimie .”
“Umekosea namba ,” Colin alisema huku
akikata simu.
“Nani?” Cecy alimuuliza.
“Kuna mtu anaonekana amekosea namba. ”
“Basi unakuta mtu anapiga simu na kuanza
kutoa maagizo mengi bila kujua anazungumza
na nani, ” Cecy alimuunga mkono mpenzi wake .
“Umeona eeh , mpenzi nawe yamekukuta?”
“Mara chache .”
“Mara nyingi watu huwa wanachanganya
namba badala ya sita wanaandika tisa basi
akipiga inakwenda kwa mwingine,” Colin alizidi
kuficha kilichopita.
Wakiwa katika ya mazungumzo ujumbe uliingia
kwenye simu ya Colin , aliichukua simu haraka
kwa kuamini unatoka kwa Mage . Kabla
hajafungua upande wa ujumbe Cecy alidakia na
kusema:
“Nipo kwa ajili yako nitasoma na kukueleza
kimeandikwa nini .”
Colin alipoangalia namba ya ujumbe ule ilikuwa
iliyopigwa muda mfupi na Mage , alijikuta njia
panda kumuachia simu Cecy asome ujumbe
ule ambao aliamini si mzuri kusomwa naye.
Lakini hakuwa na jinsi huku akiomba usiwe
ujumbe mbaya ambao utamchanganya mpenzi
wake na kulizua jipya pengine kukataa hata
kazi yenyewe ...
Cecy alichukua simu na kufungua upande wa
ujumbe na kuanza kusoma, ghafla macho
yalimtoka pima na mapigo ya moyo yalianza
kwenda mbio huku jasho likitanda kwenye paji
la uso .
Ujumbe ulikuwa umeandikwa :
“Colin wewe ndiye mpenzi wangu wa maisha ,
kumbuka ahadi yetu tuliyoahidiana kuwa mume
na mke ipo palepale. Huu ndiyo wakati wangu
hicho kinyago chako hakina nafasi , mimi na
wewe tunajulikana kwa wazazi wetu na mbele
ya Mungu . Colin nakupenda zaidi ya kupenda,
kufungwa kwa Hans Mungu ametenda ili ahadi
yetu itimie . Mimi ndiye mkeo uliyechangulia na
Mungu. I love you my husband to be Colin
forever and ever mmmmwaaa .”
Colin aliyekuwa akifuatilia uso wa Cecy
alishtuka kuona macho ya Cecy yakikodolewa
pima kisha kuanza kutoka machozi, alijua
kimenuka, kwa mchecheto bila kujielewa kama
yupo barabarani gari lilihama njia na kwenda
kujingonga kwenye nguzo ya umeme na
kufanya utokee mlipuko mkubwa baada ya
waya za umeme kugusana.
Mlipuko ule ulifanya watu wakimbie kuokoa
maisha yao , ghafla gari lilianza kuwaka moto
kabla hawajatoka. Watu walishtuka na
kukimbia kuangalia kuna nini . Waliwakuta watu
wawili wamejilaza mwanamke kwenye dashi
bodi na mwanaume kwenye usukani huku
damu zikiwatoka vichwani .
Haraka waliwatoa kwenye gari na kuwalaza
pembeni huku wengine wakijitahidi kuzima gari
ambalo moto wake ulikuwa mkubwa . Kwa
haraka walisimamisha gari na kuwapakiza
majeruhi waliokuwa hawana ufahamu na
kuwawahisha hospitali.
Kutokana na hali zao ambazo hazikujulikana
kama wapo hai au wamekufa waliwawahisha
Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Gari alilokuwa
akiendesha Colin liliendelea kuteketea na
hatimaye lilishika moto lote kutokana na
miundo mbinu midogo ya kuzimia.
Je, nini kiliendelea? Fuatilia Jumamosi ijayo .
 
Show ya mwanamtindo imepona kweli? Maana ndiyo mtaji wenyewe huo.
 
Mmmmmh majanga haya we mage umezaliwa au ulijikuta tu duniani? Balaa gn kwa my Colin
 
ILIPOISHIA :
Kutokana na hali zao ambazo hazikujulikana
kama wapo hai au wamekufa waliwawahisha
Muhimbili.
Gari alilokuwa akiendesha Colin liliendelea
kuteketea na hatimaye lilishika moto lote
kutokana na miundo mbinu mibovu ya kuzimia
moto.
SASA ENDELEA .. .
Liliteketea na kila kilichokuwepo pamoja na
simu zote za Colin na Cecy .
Msichana mmoja shoga wa Brenda rafiki wa
Mage ambaye alikuwa akimfahamu Colin
kutokana na kuwepo siku Colin alipomvisha
pete Mage , alikuwepo kwenye ajali ile baada ya
kuteremka kwenye daladala na kukuta watu
wakitolewa kwenye gari lililokuwa likiwaka
moto.
Kwa vile hakuijua namba ya simu ya mama
Colin aliamua kumpigia simu Brenda amweleze
Mage ili ampigie mama Colin kumjulisha ajali
ile. Baada ya kupigiwa simu Brenda alipokea
upande wa pili:
“Haloo Loveness, niambie shoga !”
“Aisee kuna tatizo , ” alisema kwa sauti iliyojaa
wasiwasi .
“Mbona unanitisha kuna nini?” Brenda
alishtuka.
“Colin kapata ajali mbaya sana .”
“Colin ! Yupi ?”
Aliyekuwa mchumba wa Mage .”
“Wewe! Ajali ya nini tena Mungu wangu?”
“Gari alililokuwa akiendesha limepata ajali
barabara ya Sam Nujoma jirani na Mlimani City
kwa kugonga nguzo ya umeme .”
“Mungu wangu, vipi hali yake ?”
“Mmh ! Kwa kweli kuna taarifa nyingi japo si
rasmi.”
“Mungu wangu nisaidie mja wako , taarifa gani
tena Love ?”
“Wapo wanaosema wamekufa hapohapo.”
“Jamaniii! Kwani alikuwa na nani ?”
“Na msichana mmoja ambaye anaonekana
alikuwa na nguo za mazoezi. ”
“He ! Yaani nimechoka , siamini kama Colin
amekufa kirahisi namna hiyo.”
“Sasa shoga nina imani Mage ana namba ya
mama yake , mpigie ili awajulishe nina imani
hawana taarifa. ”
“Poa, lakini siamini mpaka niuone mwili wa
Colin kwenye jeneza. ”
Brenda akiwa amechanganyikiwa alimpigia
simu Mage aliyekuwa amekaa kwao huku
akichezea simu yake . Baada ya kumtumia
ujumbe Colin alipiga simu ambayo iliita bila
kupokelewa na mwisho ilizimwa kabisa.
Baada ya kuzimwa alijikuta akijiapiza :
“Lazima nimpate Colin kwa hiyari kwa nguvu,
nitahakikisha nampoteza kinyago wake ili
niipate nafasi yangu bila hiyo sina maisha heri
ninywe sumu .”
Akiwa katikati ya mawazo simu yake iliita ,
wazo lake alijua Colin alikuwa akitafuta sehemu
nzuri ili ampigie. Alipoangalia alikuta inatoka
kwa shoga yake Brenda , aliipokea .
“Niambie shoga.”
“Mage kuna taarifa siyo nzuri .”
“Taarifa gani?”
“Zinamhusu zilipendwa wako .”
“Nani, Hans ?”
“Hapana, Colin. ”
“He ! Colin kakupigia simu ?”
“Siyo kunipigia simu bali kapata ajali mbaya .”
“Acha utani , acha kunirusha roho unione kama
nampenda, sio siri Colin ndiye aliyebeba uhai
wangu.”
“Mage hebu tuliza akili unisilize.”
“Haya niambie mpenzi. ”
“Colin amepata ajali mbaya barabara ya Sam
Nujoma jirani na Mlimani City na haijulikani
kama mzima au amekufa .”
“Brenda sipendi utani wa kujinga , nimetoka
kuzungumza na Colin hata robo saa haijapita.”
“Sasa wewe fanya utani naomba umpigie simu
mama yake sasa hivi , mweleze Colin amepata
ajali na amekimbizwa Muhimbili. Naomba
usiongeze lingine usije muua mama wa watu
kwa mshtuko . Najua anampenda sana
mwanaye ndiye kama mboni ya macho yake .”
“Japo siamini nitampigia tu.”
“Fanya haraka, unaambiwa hata gari alilokuwa
akiendesha limeteketea lote . ”
“Mungu wangu! Brenda unasema kweli ?” Mage
aliuliza kwa sauti ya kilio.
“Kweli , siwezi kukutania kwa jambo zito kama
hili.”
“Mungu wangu hii nuksi gani ? Kama Colin akifa
nitakuwa na faida gani ya kuendelea kuishi,”
Mage alizungumza peke yake huku macho
yamejaa machozi na mikono kumtetemeka
wakati wa kutafuta namba ya mama Colin .
Kila alivyokuwa akilitafuta machozi yalizidi
kuyafunika macho yake hata alipoyafuta kwa
mkono yalijaa tena. Alitoka chumbani na simu
mkononi hadi sebuleni na kumkuta mama yake.
“Mage nini ?” mama yake alishtuka na hali ya
mwanaye.
“Colin mama, ” alisema huku akilia na kumpa
simu mama yake .
“Colin ! Kafanya nini ?”
“Ajali. ”
“He ! Lini ?”
“Sasa hivi .”
“Taarifa umezitoa wapi ?”
“Kanipigia Brenda sasa hivi ?”
“Dah! Vipi hali yake .”
“Na ..na. .sikia a ..a ..meku . .”
“Wewe mtoto ishia hapohapo,” mama Mage
alimkata kauli mwanaye hakutaka kulisikia
neno la mwisho kwa vile aliamini litamuumiza
moyo wake .
“Mama mpigie simu mama yake hana habari.”
“Mmh !”
Mama Mage alichukua simu yake kutafuta
namba ya mama Colin huku naye mikono
ikimtetemeka. Baada ya kuipata alipiga simu
ambayo ilipokelewa upande wa pili .
“Haloo dada vipi ?”
“Kwema , una habari gani?”
“Za nini ?”
“Kuhusu Colin .”
“Mmh ! Sina habari zozote.”
“Kuna taarifa kapata ajali.”
“Ajali!?” mama Colin alishtuka .
“Eeh , ndiyo , kuna mtu kampigia simu Mage na
kutaka tukujulishe kwa vile hakuwa na namba
yako ya simu .”
“Mungu wangu wee, yupo katika hali gani?”
“Hebu subiri ,” alisema na kuziba sehemu ya
kuzungumzia na kumgeukia Mage .
“Eti Mage mwili wa Colin umepelekwa hospitali
gani?”
“Mama sijasema amekufa ila watu wanafikiria
hivyo, ” Mage alimgeuka mama yake .
“Sasa kapelekwa wapi ?”
“Mama mwambie amekimbizwa Muhimbili, ila
usimwambie yupo vipi . .
Itaendelea Jumamosi ijayo .
 
Back
Top Bottom