Wakili wa Moyo-35
ILIPOISHIA:
Mage alimvamia Colin na kuendelea kustarehe bila kuliweka wazi lililokuwa likimliza, alijitahidi kurudi katika hali yake ya kawaida ya uchangamfu na kumfanya Colin asahau kitendawili chake.
SASA ENDELEA...
Walikaa kwenye hoteli ile kwa siku mbili huku wakiongozana kama kumbikumbi, kila mmoja alijua wawili hao wanapenda mapenzi ya dhati.
Siku moja mchana baada ya kupata chakula, walipumzika kwa muda kabla ya kujiandaa kurudi mjini.
Mage akiwa amejilaza pembeni ya Colin, alimnyanyua na kumgeukia mpenzi wake na kumwita.
"Colin."
"Naam mpenzi."
"Hivi unajua kwa nini toka juzi sijakuita mpenzi?"
"Sijajua."
Mage alitulia kwa muda akimtazama Colin usoni mara machozi yalianza kumtoka, Colin alizidi kumshangaa mpenzi wake kwani toka wamefika Bagamoyo ameshindwa kumuelewa.
"Colin," alimwita tena.
"Naam."
"Najua unanipenda."
"Sana."
"Najua kabisa nitakachokueleza kitakushtua na kukumiza moyo wako, sawa na kuupasua bila ganzi kwa kisu butu. Lakini ukweli utabakia palepale sina jinsi, nina imani penzi la kweli huwa halitengenezwi na mtu bali mhusika mwenyewe."
"Ni kweli."
"Unajua penzi letu halikuwa la sisi kupendana bali kutengenezwa na wazazi wetu?"
"Najua lakini tulipoonana kila mtu alimpenda mwenzake."
"Unajua hiyari yashinda utumwa?"
"Najua."
"Nina imani nilikueleza jinsi mapenzi yalivyoniumiza."
"Ndiyo."
"Na aliyesababisha nilikueleza."
"Ndiyo."
"Basi napenda kukueleza hili ambalo moyo wangu unavuja damu kwa maumivu kwa vile sikupenda liwe kwani hiyari yashindwa utumwa, lazima niseme ukweli wa moyo wangu kuwa Colin nilikupenda lakini Hans nilimpenda zaidi. Hans baada ya kufiwa na mkewe amerudi kwangu na yupo tayari kutimiza ndoto yetu tuliyoiweka muda mrefu,"
Mage alimeza mate huku akiendelea kutokwa na machozi kisha aliendelea kuzungumza kwa sauti ya chini yenye mchanganyiko na kilio.
"Najua kauli yangu itakuumiza lakini ndiyo ukweli wenyewe, Colin nimeamua kwa hiyari na mapenzi yangu kuuvunja uchumba wetu kwa hiyo harusi yetu haitakuwepo tena, penzi tamu tulilopeana ndilo la mwisho. Tukitoka hapa kila mtu ashike hamsini zake."
"Mage," Colin alimwita kwa sauti ya chini.
"Abee."
"Unasema kweli au unatania?"
"Nasema kweli," Mage alijibu huku akikaza macho.
"Hapana, acha utani Mage unaweza kuniua kwa presha."
"Huwezi Colin, wewe ni mwanaume umeumbwa kukabiliana na matatizo, kumbuka amenikuta tayari nimeshaanza uhusiano na mtu ambaye ndiye aliyenionjesha dunia ya mapenzi na aliniahidi kunioa. Toka niachane naye sikuwahi kuwa na mwanaume mwingine zaidi yako, kilichotokea ni kutoelewana lakini sasa hivi tumeelewana na mipango yetu lazima itimie."
"Mage japo Hans ndiye aliyekuonjesha dunia ya mahaba lakini alikutenda, Mage nimekukosea nini mpaka uchukue uamuzi mzito na wa kikatili kama huo?" Colin aliuliza huku machozi yakimtoka.
"Hujanikosea kitu, hata mimi nilikupenda sana, lakini siwezi kuishi na wewe kwa kujilazimisha au kukufanya kama bodi lakini injini awe Hans. Colin, Hans nampenda sana aliniudhi na kuumiza moyo wangu lakini siku aliponiomba msamaha moyo wangu uliyeyuka kama bonge la mafuta kwenye kikaango cha moto. Siwezi kuwa nawe kimwili wakati mawazo yangu yote yapo kwa mwanaume mwingine.
"Narudia, naomba ukubaliane na uamuzi wangu wa kuvunja uchumba tukiwa na mioyo safi, kuachana kwetu kusijenge uadui. Tuendelee kuwa marafiki kwenye harusi yangu uje, ya kwako nije."
"Mage uamuzi uliochukua ni kuupasua moyo wangu bila ganzi, naomba urudishe moyo nyuma, mpenzi wangu bora ungeninyang'anya kila kitu katika mwili wangu na kuniachia moyo wako kwani ni muhimu kuliko chochote duniani japo nipo nawe kwa muda mfupi lakini nimekuzoea sana."
"Siwezi kuishi mapenzi ya kuigiza niache nimpende aliyechaguliwa na moyo wangu."
"Mage siwezi kukubali kirahisi namna hiyo, nasema sikubali, lolote na liwe nasema huondoki kama sivyo, nitamwaga damu ya mtu," Colin alisema huku akisimama.
"Colin mapenzi si kulazimishana, usisababishe nikakasirika na kutoa maamuzi yatakayokuumiza mara mbili."
"Nasema sikubali...toa uamuzi wowote kumbuka nimekutoa kwenye mateso ya kutendwa, leo nikuache uondoke hivihivi? Sikubali," Colin alikuwa mkali.
"Colin nasema hivi, kila usemalo ni kweli tupu na una haki yoyote ya kufanya lakini kumbuka penzi halilazimishwi, nina imani umenielewa, kuwa mstaarabu tuachane kwa usalama."
Itaendelea baadaye leo