***
Msichana aliyekuwa mapokezi Hollyday Inn alishangaa kidogo alipomwona kijana mrefu wa kiume akivuta begi lake kutoka nje ya hoteli. Hakukumbuka aliingia lini wala hakujua alitokea chumba kipi. Alimtazama toka aliposhuka kutoka katika lifti na kisha kutembea taratibu kuelekea lango kuu.
Mgeni huyo alipomfikia alimsalimu na kumuaga kwa alama ya dole huku akitabasamu. Alipita hadi nje ambako alionekana akiita gari mojawapo la teksi za hotelini hapo, akaingia. Gari ikatiwa moto na kutokomea.
Mara msichana huyo akamkumbuka Mfaume. Alitazama eneo la kadi wanayoita ‘malaya’ ambayo aliichukua. Ilikuwa haijarudishwa. Hilo lilimtia wasiwasi. Kwa kawaida, kadi hiyo hutumika kwa amri ya Meneja wa hoteli tu, pale mgeni anaposahau na kuifungia yake chumbani au kuondoka nayo. Alikuwa amemwamini Mfaume kwa kujua kuwa ingemchukua dakika chache tu kuirejesha.
Kisha, msichana huyo akabaini kitu gani kilimfanya amkumbuke Tenga Mfaume. Ni shati alilovaa yule mgeni aliyetoka punde. Lilifanana sana na shati alilovaa Tenga Mfaume siku hiyo, shati ambalo siku zote amekuwa akijitapa hotelini hapo kwamba ni yeye pekee aliyekuwa nalo nchini. Lilikuwa moja ya zawadi zake nyingi ambazo alizipokea toka kwa rafiki zake mbalimbali wa ughaibuni waliopata kulala hotelini humo.
“Shati la milionea.” Mara kwa mara Tenga Mfaume alitamka.
9
Moto ulilipuka upya kufuatia kifo cha Afande Chaku. Vigogo wa kamati maalumu iliyokuwa ikitafuta ufumbuzi wa kifo cha kutatanisha cha Bi. Cleopatra walikuwa bado hawajajinasua katika jinamizi la mwandishi wa habari ambaye walimtegemea kuwa ufunguo la sakata zima kwa kiwango fulani. Wakiwa bado wanalitafakari hilo mara yameibuka mengine. Mpelelezi mahiri, aliyetwishwa mzigo wa kuongoza timu mahususi ya kutafuta ufumbuzi naye ameuawa kinyama muda mfupi uliopita!
Taarifa za kifo chake ziliwasilishwa na Inspekta Matata katika kikao cha dharura kilichoitishwa usiku huo. Kwa mujibu wa maelezo yake kikaoni hapo maiti ya Chaku iligunduliwa katika hoteli ya Sunlight ya ufukwe wa bahari maeneo ya Msasani. Mmoja wa wahudumu wa hotelini hapo, ambaye alimuhudumia marehemu aliuarifu uongozi wa hoteli mara alipobaini kuwa alikuwa akizungumza na maiti wakati akijaribu kumwamsha ili amlipe pesa za vinywaji alivyotumia. Alihisi mteja wake huyo alikuwa marehemu pale alipomgusa kifuani na kushangazwa na jinsi alivyopoa. Baadae aliona damu iliyoganda kwenye kifua chake, ambayo marehemu aliilalia. Kijana huyo alikuwa jasiri wa kutozungumza hadharani tukio hilo hadi alipompeleka chemba meneja wake ambaye baada ya kuthibitisha aliitarifu polisi.
“Maiti amechukuliwa bila ya wateja wala wafanyakazi wengine kujua.kwao walidhani ni mlevi mmoja aliyezidiwa anabebwa kupelekwa nyumbani kwake.” Matata alikitaarifu kikao.
Wenzake, waliopigwa butwaa walimtazama kwa macho yaliyojaa maelfu ya maswali. Mkuu wa majeshi alikuwa wa kwanza kuyaweka maswali yake hadharani. “Kwasasa kinachoendelea ni kipi?” Alimuuliza.
“Kwanza tulichokifanya ni kumuhifadhi meneja wa hoteli na msaidizi wake. Tunaamini watatusaidia sana.” Alijibu.
“Kuwahifadhi kwa maana ya kuwatia ndani, sio?” Mkuu huyo wa majeshi aliuliza.
Inspekta Matata alikubali kwa kichwa kabla hajaongeza, “Wako ndani, lakini katika mazingira tofauti. Wako chumba cha peke yao, wanakula na kunywa wanachotaka.”
“Kwanini umewaweka ndani?” Kigogo mwingine aliingilia kati.
“Kwa usalama wao na wetu pia.” Matata alimjibu kwa sauti ambayo ilimwonyesha kila mtu katika meza hiyo ya mviringo ahisi anavyojisikia; mtaalamu anayezungumza na makinda katika taaluma hiyo.
“Fafanua…” Kigogo yule alisisitiza.
“Nini?”
“Hayo madai ya usalama wao na wetu. Sijakuelewa.
Matata alitabasamu kidogo kabla hajaeleza, “Hakuna anayejua Afande ameuawa na nani. Ni wao peke yao pamoja na muuaji wanaojua kuwa afisa muhimu kama yule ameuawa. Hivyo, tuliona ni hatari kuwaacha mitaani kabla upepo haujatulia.” Alikohoa kidogo. Akaendelea, “Hali kadhalika, wanao mwelekeo wa kutusaidia sana. Yule mhudumu anadhani kuwa alimuona muuaji na kuzungumza naye na kuwa anaweza kumtambua wakati wowote. Kwamba ni mtu mrefu na mtulivu aliyekwenda hotelini humo na kumuomba huduma ya kinywaji ambayo aliitaka ipelekwe ufukweni ambako marehemu aliketi peke yake. Kisha, alienda akaketi meza moja na merehemu. Wakati anampelekea oda yake mhudumu anadai alipishana na mteja huyo akiwa na haraka. Awali, alidhani kuwa anaelekea maliwatoni lakini alipoona kimya ndipo alipoiendea meza ile na kutoa vinywaji ambavyo havikutumika na kumdai Afande Chaku.”
Wenzake walimkazia macho. Alikuwa akisema ukweli lakini ukweli huo haukuweza kuwaridhisha. Mjumbe mmoja alishindwa kustahimili, “Nikuambie kitu Inspekta?” hata kabla ya kusubiri jibu la Matata aliendelea. “Maelezo yako ni matamu sana lakini vitendo hatuvioni. Sidhani kama kuna yeyote kati yetu aliyekutarajia kuwa mtoa habari za matukio badala ya ufumbuzi. Mtu kauawa mbele ya Rais, tunataka kujua kama muuaji alimkusudia Rais au la. Aidha, tunamtaka muuaji huyo akamatwe. Tulichoambulia kwako ni taarifa ya kifo kingine, ambacho kinahusiana sana na cha Cleopatra. Haya, hata kabla hilo pia kupatiwa ufumbuzi leo unatuletea taarifa nyingine ya kutisha zaidi; kuuawa kwa mpelelezi wako mkuu katika sakata hili. Mimi binafsi nasikitika kuwa naanza kupoteza imani na uwezo wako.”
Matata alijaribu kutabasamu kuficha hasira kali iliyompanda ghafla na kumpanda kooni. Tabasamu lilikataa. Akaishia kumkazia macho mjumbe huyo. Alikasirika zaidi alipowatazama wajumbe wengine na kuona wakitikisa vichwa kumuunga mwenzao mkono.
“Nadhani huu ni wakati wa kufikiria kung’atuka,” alinong’ona kwa sauti dhaifu.
***
Masudi Kipanya, Patrick Mgata, David Chikoko na wengineo walikuwa miongoni mwa wachoraji mashuhuri sita walioshangazwa na kitendo cha polisi kuwataka msaada. Kwa utamaduni wa Tanzania kuwasaidia polisi kuna maana moja tu, kukamatwa, kuwekwa rumande na kuanza kumiminiwa maswali na vitisho. Hivyo ilimshangaza kila mmoja wao, alfajiri hiyo walipotembelewa na polisi waliovaa kiraia.
“Kipanya?”
“Masoud Kipanya anaishi kwenye kurasa za magazeti.” Aliwajibu.
Polisi walicheka. Mmoja wao alitoa kitambulisho chake.
“Tunahitaji msaada wako. Unaweza kuvaa mara moja tutoke?” alieleza.
Moyo wake ulipoteza mapigo. Hata hivyo, sauti yake haikupotezan usanii pale alipowauliza, “Mbona hamna pingu?”
“Za nini”
Alioga upesiupesi, akabadili nguo toka katika mavazi ya kulalia na kisha kuongozwa kwenye gari lililokuwa na namba za kiraia. Ni humo alimowakuta wakina Chikoko na Mgatta. Tofauti na alivyotegemea, badala ya kupelekwa Kituo cha Kati, gari ilielekezwa nje ya mji likifuata njia ya Bagamoyo. Lilichepuka na kuelekea kulia hadi katika Hoteli ya Kunduchi ambako lilisimama. Walielekezwa katika moja wapo ya vyumba vya mikutano ambako waliombwa kujisikia huru.
“Tunahitaji msaada wenu katika suala nyeti la kitaifa.” Mmoja wa maafisa waliowaleta alieleza. “Jana kama saa kumi hivi zilizopita mtu mmoja muhimu sana ameuawa.Hapa tunaye mtu mmoja ambaye anaamini alimwona muuaji. Tumempa mamia ya picha za watuhumiwa sugu wa mauaji, ndani na nje ya nchi, hakuweza kumtambua. Hivyo, nyie kama wachoraji, tunadhani mkikaa naye na kumsikiliza huku mkifanya uchawi wenu kwenye makaratasi au kompyuta bila shaka tutaipata sura yake halisi.”
Kwa mara ya kwanza wachoraji hao walitabasamu kwa dhati. Kwa gharama za jeshi la polisi walipatiwa kifungua kinywa cha haja. “Ambaye hachori bila kutia vitu vikali tumboni anaruhusiwa kunywa chochote anachotaka.” Mwenyeji wao alizidi kuwakarimu.
Saa moja baadaye, mhudumu ambaye alikuwa akiwasaidia polisi kumpata mtuhumiwa alitambulishwa kwao. Kwa kila hali alikuwa taabani, kukesha, maswali elfu moja na moja aliyoulizwa na tukio la kuona maiti ya mtu bila kutegemea vilikuwa vimemmaliza. Hata hivyo, baada ya nusu saa ya mizaha ya wachoraji hao, chai ya nguvu na kushushia bia mbili baridi, alichangamka.
Aina nyingine ya maswali ikaanza.
“Pua pana kama hii?”
“Hapana, imechongoka kidogo.”
“Miwani?”
“Hakuwa nayo.”
“Nywele?”
“Fupi tu za kawaida.”
Na kadhalika na kadhalika. Ilitayarishwa michoro aina aina. Mhudumu huyo, ambaye baadaye alifahamika kuwa aliitwa Mwanakatwe, alitoa ushirikiano kwa kila mchoraji. Alitazama kila mchoro wa awali na kukanusha hapa na kuelekeza pale.
Siku ilipita bila mafanikio.
Siku ya pili matumaini yalianza kuonekana. Mwanakatwe alianza kutoa maelezo madogomadogo. “Urefu huu una tofauti kidogo… viatu vilikuwa vyeusi… na kadhalika. Wachoraji wawili walimtia matumaini zaidi. Alitazama picha zao kwa makini, nuru ya utambuzi ikizidi kuchanua katika macho yake.
Michoro hiyo ilipowekwa katika kompyuta na utaalamu wa Coral drawing na graphic designing kutumika baada ya marekebisho mawili matatu, Mwanakatwe aliangua kicheko.
“Ni huyu hapa,” alisema
Kipanya na Mgatta walitazamana kwa mshangao.
Maafisa wa upelelezi walipoitwa kutazama michoro hiyo miwili ambayo Mwanakatwe aliafikiana nao, wao pia walitazamana kwa mshangao. Walichukuana chemba ambapo mmoja alimuuliza mwenzake, “Nadhani unamfahamu mtuhumiwa wetu.”
“Bila shaka. Si mwingine zaidi ya Joram Kiango.”
“Inawezekana?”
“Nani anajua?” alimjibu.
***
“Joram Kiango!” ilinguruma sauti ya kigogo mwingine. “Ni Joram Kiango! Na bado mmekubali kumwacha hai katika swala nyeti kama hili! Mnajua mmefanya kosa ambalo tutalijutia maisha yetu yote?”
Inspekta Matata alimjua fika Joram Kiango. Kwa kiasi fulani, alimchukia kama ilivyokuwa kwa vigogo wenzake wengi wenye mengi ya kuficha. Ushoga wa siri ulioanza baina ya Inspekta mstaafu, Kombora ni moja ya mambo yaliyofanya mzee yule ajikute akistaafishwa mapema wakati alikuwa bado na nguvu na akili zake timamu. Moja ya ajenda alizopewa Matata ni kufuta kabisa Ujoram Kiango katika Jhamuhuri ya Tanzania. Hivyo yeye pia angeshusha pumzi kama bastola iliyomwondoa Chaku ingefanya hivyo kwa Joram Kiango pia. Kwa bahati mbaya, haikufahamika mapema kuwa mgeni ambaye alikuwa akitarajiwa na Afande Chaku angekuwa Joram Kiango. Kamwe asingeondoka akiwa hai.
Kwa sauti, Matata alisema, “Haikufahamika mapema. Lakini maadamu hili limetokea, tayari amejiweka katika mstari wa shabaha. Toka kesho soma magazeti, tazama televisheni uone. Hata kama atajifanya panya ajichimbie ardhini kama Saddam Hussein tutamchoropoa na kumfunga mdomo kabla hajaufungua.
Msikilizaji wake alimtazama kwa macho yenye mashaka. Akasema, “Inspekta, nadhani unamfahamu Joram Kiango. Kamwe si mtu wa kubeza na wala hatabiriki.”
“Namjua sana,” Matata alisema akitabasamu. “Ni play boy tu mwenye bahati. Naona bahati yake imefika ukingoni. Tulia uone.”
Kimya kifupi kilitawala kati yao. Mmoja akaitazama saa yake, wa pili akiwa amejiinamia. Aliyeinama aliinuka na kutazama huko na huko. Yeye pia aliitazama saa yake kabla hajasema, “Nadhani sina budi kuondoka.” Kisha, kama aliyekumbuka jambo aliketi tena na kumkazia macho Inspekta Matata. “Sidhani kama nina haki ya kukufundisha wajibu wako. Lakini kuna swala hili la huyu mtu ambaye tayari tumemtumia mara mbili, kumwondoa yule mwandishi na sasa afisa wa upelelezi. Unadhani tuko salama kuwa na mtu anayefahamu yote hayo miongoni mwetu?”
Matata aliangua kicheko, “Yule niachie mimi. Tutampa ujira wake wa mwisho kati ya leo na kesho. Ataupokea lakini hatautumia. Tayari amejichimbia kaburi lake mwenyewe.
“Nani ataifanya kazi hiyo?”
“Niachie mimi.”
Mgeni aliinuka tena, kisha akakumbuka jambo jingine na kumkazia macho Matata, “Hili ni kati ya mimi na wewe. Niambie tafadhali. Nani aliyemuua Cleopatra?
Inspekta Matata alicheka kidogo kabla ya kumjibu, “Sijui.”
“Una uhakika?” Kigogo alisisitiza.
“Kwanini nikudanganye?” alimjibu kwa swali jingine.
Kigogo alimtazama kwa macho ya kumsoma rohoni. Chochote alichokitafuta katika uso huo hakukipata. Akageuka na kuanza kuondoka. Matata akabonyeza tufe chini ya meza yake, sehemu ya ukuta ikafunguka na kuruhusu mlango wa lifti kufunguka, mgeni akaingia na kupaa toka katika chumba hicho cha siri hadi ghorofa ya pili ambako ilifunguka naye kutoka. Akatumia ngazi kushuka hadi chini ambako mlango wa kioo ulifunguka wenyewe mara alipoukaribia. Alipita ndani ya bustani kubwa yenye miti na maua mbalimbali hadi alipoliacha gari lake. Akalitia moto. Geti la lango kuu lilifunguka lenyewe vilevile kwa harufu au uzito wa gari lake, ingawa mlinzi mwenye sare za kampuni moja ya ulinzi aliketi pale akisoma gazeti.
Kigogo aliingia mitaani na kutokomea.
Matata alimtazama mgeni wake katika screen maalumu hadi alipotokomea mitaani. Screen hiyo ni moja ya vitu ambavyo vilikuwa siri hata kwa mkewe katika jumba hilo. Siri nyingine ilikuwa chumba hicho cha chini ya ardhi. Ni watu wachache sana waliofahamu uwepo wake. Na wachache zaidi walioweza kukifungua. Mhandisi aliyeongoza ujenzi huo alikufa kitambo kwa ajali ya gari. Msaidizi wake aliuawa na majambazi nyumbani kwake.
Machoni mwa wapiti njia, nyumba hii ilikuwa ya kawaida tu, yenye ghorofa mbili, ambayo kama nyumba nyingine nyingi jijini Dar es Salaam iliota na kupaa kama uyoga. Hakuna aliyefahamu fika jinsi ilivyokuwa ndani.
Kama ilivyokuwa kwa mwenye nyumba, machoni mwa watu wengi alikuwa Afisa wa juu wa ama jeshi la polisi ama usalama aliyekuwa akiongoza kitengo nyeti ambacho haakikutofautiana sana na kile cha polisi wa kimataifa INTERPOL. Kwa sura alikuwa mtu makini, mzalendo halisi, aliyekuwa tayari kupoteza maisha yake kulinda maslahi ya nchi yake. Lakini, kwa sura yake ya pili, ambayo daima ilifichwa katika kinyago cha umakini na uzito wa majukumu, alikuwa mtu wa kuogopwa. Toka miaka ya themanini, fisadi alipogeuka shujaa, uongozi ulipoanza kununuliwa kwa pesa, huku aibu ya kufanya madhambi ikizidi kuyoyoma; Matata alijikuta katikati ya dimba hilo. Alifanya chochote kilichomwongezea chochote, mradi mfuko wake wa mafichoni ulizidi kutuna. Wakorofi wengi waliokwenda kinyume cha matakwa ya watu wake ama walifutika duniani ama waliozea gerezani; wawili watatu walipata kuponyoka na kukimbilia nje ya nchi ambako hawakupata hali ya kutia tena miguu yao katika ardhi ya nchi yao. Mmoja kati yao tayari amefia huko ugenini kwa ajali yenye utata.
Zamani kidogo tatizo la Matata lilikuwa fedha, namna ya kuzipata. Sasa tatizo lake halikuwa fedha isipokuwa namna ya kuzitumia. Ingawa siku hizi haikuwa tena aibu kutangaza utajiri wake japo mchafu kiasi gani, bado kwa nafasi yake fursa hiyo hakuwa nayo. Kwa majina ya ndugu zake na watoto wake tayari alijenga hoteli nne za kitalii. Alikuwa na hisa nzito katika kampuni mbili za uwindaji, ikiwa ni pamoja na kumiliki hekta elfu kumi za ardhi ya kitalii. Nchini Kenya na Afrika Kusini alikuwa na majengo ya ghorofa kumi na tano yaliyotumika kibiashara. Pamoja na miradi yote hiyo kutumia fedha bado lilikuwa tatizo. Swala la mfuko wa madeni ya nje, EPA, swala la Richmond, mikataba tata ya madini na uwindaji kharamu ni miongoni mwa maswala ambayo yalikuwa yamemmwagia neema zaidi na zaidi. Dola za marekani bilioni mbili alizopokea katika harakati za kuziba na kuzibua mambo zilikuwa na miezi tele chumbani humu zikisumbua kichwa chake.
Katikakati ya fanaka zote hizo yule mwanamke wa Ikulu akafumuliwa kichwa. Halafu, toka kusikojulikana anaibuka huyu mtu anayejiita Joram Kiango.
“Atanitambua,” Inspekta Matata aliapa kimyakimya.
***
Mara nyingi Joram Kiango aliwapuuza polisi,lakini kamwe hakupata kuwadharau, hasa pale inapotokea mmoja wao kuuawa kinyama huku akiwa katikati ya suala nyeti, polisi, kama nzige au nyuki waliolala, huamka na kuanza mashambulizi makali kushoto na kulia.
Joram Kiango alilitegemea sana hilokwa kifo cha Afande Chaku. Ni kwa kuamini hivyo ndipo mara tu alipoiacha maiti ya Chaku alifanya haraka kurudi nyumbani kwake ambako alitumia dakika zisizozidi ishirini tu kuchukua vifaa alivyovihitaji; kompyuta yake ya mapajani, bastola, mabomu mawili ya machozi, suitcase yenye mavazi yake ya kazi ainaaina na nyaraka zake nyeti. Kisha alitegesha alarm yake ambayo humwarifu mara chumba chake kinapotembelewa na mtu ambaye hakumtegemea. Muda mfupi baadaye alifungia gari yake katika gereji na kwa kupitia mlango wa uani aliingia mitaani.
Dar es Salaam ina hoteli bubu nyingi sana. Baadhi zikiwa katika maeneo duni ambayo hayafikiki kwa gari isipokuwa vichochoro vya njia ya miguu. Moja ya hoteli hizo iliitwa Darajani Inn. Iko katika mtaa wa Manda, Magomeni, katikati ya uchochoro maarufu unaoiunganisha Magomeni na Kigogo, Mburahati hadi Luanga. Akiwa amefunika kichwa chake kwa kofia pana ya wachunga ng’ombe na sehemu kubwa ya uso wake kwa miwani mieusi, hakuna aliyeweza kumtambua mara moja. Alipatiwa chumba cha uani ambamo alishangaa kubaini kuwa kulikuwa na bafu na choo cha kujitegemea huku maji yakitoka katika mabomba kama kawaida. Aidha, kulikuwa na televisheni ndogo ambayo mwenyeji wake aliiwasha kumtia matumaini zaidi.
“Tukuletee nini, mzee?” tuna bia kila aina na kuku wa kukaanga.” Mhudumu huyo, mvulana wa miaka ishirini na mitano, aliuliza.
Joram Kiango alikuwa na njaa. Alikuwa na kiu vilevile. Lakini njaa na kiu yake kubwa zaidi ilikua kuijua hatma yake katika mkasa huu. Hivyo, alimruhusu kijana huyo kwa kumwambia kuwa pindi atakapohitaji chochote atamwarifu.
Mara kijana huyo alipotoka, Joram Kiango aliufunga mlango wake kwa komeo na kisha kuketi kwenye kiti pekee chumbani humo, daftari dogo la Afande Chaku likiwa mikononi mwake. Akijua kuwa atake asitake tayari amelazimishwa kuingia katika sakata la Cleopatra alijikuta akilazimika kulisoma daftari hilo kwa makini na utulivu mkubwa, kwani lilikuwa kiungo pekee baina yake na marehemu.
Afande Chaku alikuwa mwandishi wa aina yake. Kuna maeneo ambayo aliyaandika mambo mengi kwa ufupi sana, mara nyingine neno moja tu kama, ‘vurumai.’ Maeneo mengine, hasa pale alipohojiana na wahusika ana kwa ana alinukuu kila kauli kwa uzito wake. Jina la bosi wake Afande Chaku, Inspekta Matata, lilitajwa mara mbili tatu huku mara kwa mara likifuatiwa na alama ya kuuliza (?) au ya mshangao (!) ambazo Afande Chaku aliziandika kila baada ya nukuu mbili tatu. Haikumchukua muda Joram Kiango kushuku kuwa Afande Chaku alikuwa katika shinikizo zito ambalo halikutoka popote isipokuwa kwa Matata.
Tathmini ya Afande Chaku juu ya mauaji ya Cleopatra pia yalimfumbua macho Joram Kiangon kwa kiwango fulani. Maelezo hayo mafupi yalimthibitishia kile alichokuwa akikifikiria muda mrefu kwamba ili kumuua ama Rais ama mtu karibu na Rais, mbele ya halaiki kama ile na muuaji atoke salama salimini, kwa vyovyote alikuwa mbali na alitumia silaha kubwa. Afande Chaku alimtajia aina ya silaha, jumba na chumba ambacho aliamini muuaji alikitumia. Joram aliafikiana naye mara moja.
Mazingira ya kifo cha yule mwandishi koko pia yalimsisimua Joram. Mateso ya kishetani aliyoyapata na purukushani za chumbanihumo,vitu vyote hadi magodoro yakiwa yametupwa ovyo ilifanya Joram akubaliane na hisia za Afande Chaku kuwa chochote ambacho wauaji walikuwa wakitafuta ama walikipata kwa shida ama hawakukipata kabisa.
Mtu anayeitwa ‘King Suleiman’ katika kimemo alichokuwa nacho Afande Chaku ndani ya daftari lake nalokilimvutia Joram, hasa baada ya maelezo mafupi kuwa kilikuwa katika mfuko wa nguo alizovaa wakati mauti yanamkuta. Hata hivyo, yeye pia kama Afande Chaku, alivunjika nguvu baada ya kukuta nukuu za Afande Chaku katika mahojianao yake na mume wa marehemu zikifafanua kuwa ‘King Suleiman’ alikuwa yeye.
Nukuu ndogo ya Afande Chaku juu ya mtumishi wa hoteli, ‘anayehitajika kuzungumza naye,’ ikiwa pamoja na namba yake ya simu ilimvuta Joram. Baaada ya kuona alama ya nyota ambayo Afande Chaku aliichora juu kwa namna ya msisitizo. Joram Kiango alinukuu katika simu yake na kuamua kumuona yeye kwa niaba ya merehemu.
Baada ya kusoma nukuu zake kwa makini, ikiwa pamoja na zile ambazo hazikuhusiana na suala hilo, Joram Kiango alijikuta katika hali ile ile aliyomshuku Afande Chaku kuwa nayo; maswali mengi pasipo majibu. Swali la msingi likiwa lile lile ambalo lilimsumbua kila mtu; nani alimuua Cleopatra na kwasababu gani? Maswali mengine kama uhusiano uliopo baina ya kifo cha Cleopatra na yule mwandishi au kifo cha Afande Chaku na Cleopatra yalimsumbua pia. Hata hivyo, aliamini jibu la swali moja likimwelekeza kwa jingine. Alilihitaji jibu hilo, kwa udi na uvumba,akizingatia ukweli kuwa upatikanaji wake kwa namna moja hadi nyingine ulikuwa wake. Hakujisikia kama alikuwa na mtu mwenye uwezo wa kuishi hai mapangoni kama Osama walau kwa wiki mbili tu.
Tatizo lilikuwa aanzie wapi naswali lipi.
Alifikiri kwa muda wa dakika mbili tatu kabla hajakumbuka jambo. Akalichukua tena daftari la hayati Chaku na kulifunua taratibu hadi alipofikia ukurasa uliotaja aina ya silaha inayoshukiwa kumuua Cleopatra. AK 47 bunduki maarufu duniani hasa kwa wapigania uhuru wa misituni na wadunguaji katika nchi mbalimbali duniani. Bunduki hiyo,iliyogunduliwa na Mrusi, Avtmat Kalashnikova mwaka 1947 na baadaye kuboreshwa tena na tena na wataalamu mbalimbali, ilikuwa kipenzi cha wadunguaji wengi duniani. Ikiwa nyepesi, inayokubali mabadiliko katika maumbile yake ilikuwa imetumiwa mara nyingi katika shughuli hizo. Hivyo Joram hakusita kuafikiana na Afande Chaku katika hisia zake, kwamba ilitumika kumuua Cleopatra.
Baada ya kulitafakari hilo, Joram aliifungua suitcase yake na kuichomoa kompyuta yake. Akachomeka nyaya kwenye umeme kisha kuiwasha. Alifungua mtandao pepe na kutafuta mtandao wa Google ambako alipata kurasa zilizomweleza mengi zaidi kuhusu AK 47, majeshi ya nchi, ya waasi, vikundi na matukio mbalimbali yaliyoihusisha silaha hiyo. Alipotosheka na mtandao huo alihamia katika mitandao mingine, kama Yahoo, Gmail, Hotmail na mengineyo, na kupokea majibu ambayo aliyachambua kwa makini. Kwa mfano, alitaka kujua mauaji ya kigaidi ambayo AK 47 ilitumika toka miaka kumi iliyopita. Majibu yalikuwa lukuki, ya kusisimua.
Akiwa mdau katika ufuatiliaji wa maswala ya aina hii alitumia namba yake ya siri kuingia katika mitandao nyeti zaidi iliyoelezea matukio ya silaha hiyo kwa undani zaidi. Matukio yapatayo arobaini na nne yaliripotiwa kwa uwazi, majina au aina ya watuhumiwa yakitajwa au kupendekezwa na wahanga waliopata kupoteza maisha yao kwa silaha hiyo.
Carlos Ramirez, yule mtuhumiwa mashuhuri anayetumikia kifungo, alitajwa mara mbili tatu kuhusika na matukio yapatayo matatu ya udunguaji kwa AK 47. Katika tukio moja, mwanasiasa mmoja wa Amerika Kusini aliuawa. Tukio la pili, Marekani, Washington DC Gavana wa jimbo alijeruhiwa vibaya na kuponea chupuchupu. Tukio la tatu lililomhusu Carlos na kufanya ashukiwe lilitokea katika nchi za Kiarabu dhidi ya Rais mmoja ambaye alionekana kibaraka kwa utawala wa Israel. Huyu, alifia hospitalini, lakiniilikuwa baada ya kueleza jinsi mtu anayejiita mkono wa Zibril alivyomtumia ujumbe wa vitisho mara tatu kabla ya jaribio hilo.
Joram hakuona kama huyu alikuwa mtu wake, kwani tayari alikuwa gerezani, pia mara nyingi alitoa onyo kabla ya kutekeleza kusudio lake. Aidha Carlos alikuwa mwanasiasa zaidi.
Joram aliendelea kuchimbua. Watuhumiwa wengine kadhaa hawakumvutia kabisa. Matukio yao hayakuonyesha kuwa na uwiano wala malengo maalumu isipokuwa ama wazimu wa mtu aliyekuwa nyuma ya silaha hiyo ama uroho wa pesa.
Wakati akikaribia kuvunjika moyo Joram alikutana na tukio moja lililomfanya asite kuzima kompyuta na kutafuta usingizi. Ilikuwa baada ya kukutana tena na taarifa ya mauaji ambayo yamekuwa yakiwasisismua sana wanahabari na wachunguzi wa masuala ya ugaidi wa kimataifa, mauaji ambayo mtafiti mmoja alipata kuyaita ‘Mkono wa Jibril,’ jina ambalo liliwavutia wana habari hata wakaanza kulitumia kulitumia katika taarifa zao kila yalipotokea mauaji ya aina ile. Mauaji ambayo muuaji hakupata kuonekana wala kutuhumiwa kwa vigezo vya dhati na mpelelezi yeyote yule duniani. Ilikuwa kama mkono wa Jibril ulipita mahala kama upepo, akaua kwa namna ile ile na silaha ile ile, kabla ya kuibuka upya, miaka kadhaa baadaye katika nchi tofauti, kwa kazi tofauti.
Joram Kiango, kama tu yeyote yule aliyevutwa na habari yoyote iliyohusishwa na ‘Mkono wa Jibril’ alizisoma habari hizo kwa makini na tafakuri. Katika miaka mitano iliyopita zaidi ya matukio tisa yalihusishwa na mkono wa Jibril. Aina ya silaha iliyotumiwa, uhakika wa shabaha na kutoweka kwa muuaji bila kuacha chembe chembe yoyote ya kasoro ambayo ingeweza kumfanya apatikane. Hata hivyo mauaji matano kati ya hayo yalitibuliwa toka mikononi mwa ‘Mkono wa Jibril’ baada ya watuhumiwa kadhaa kupatikana na ushahidi kudhihirisha kuwa waliyafanya au kushiriki.
Mauaji matatu kati ya hayo yaliendelea kuwa kitendawili, moja likiwa kifo cha yule mrithi wa tajiri wa kiarabu, Abdul Karim. Kifo cha pili kilikuwa cha yule kadinali aliyetarajiwa kuwa papa kufuatia muda wa papa aliyekuwa madarakani kukaribia ukingoni. Cha tatu kilikuwa kifo cha Rais mmoja aliyefunguliwa. Vifo hivi vilikuwa vikimshawishi Joram Kiango kuwa vilitokea kwa mkono wa mtu mmoja, mkono wa Jibril.Joram aliamini kuwa matukio hayohayo yalifanyika kwa mkono mmoja hasa ikizingatiwa kuwa risasi ilikuwa ileile, ilifumua paji la uso vilevile na muuaji kutoweka kama tone la maji katika bahari.
Hivyo, aliposoma tena habari zilizokusanywa na watayarishaji wa mtandao huo juu ya ‘Mkono wa Jibril’ akili yake ilizinduka ghafla alipoyalinganisha na tukio la kifo cha Cleopatra. Kwa kusoma daftari la Chaku na aina ya risasi iliyotumika,ukamilifu wa shabaha na kutoweka kwa muuaji, hakuwa na shaka kuwa mkono uliotumika ulikuwa ‘Mkono wa Jibril,’
Kwa namna fulani, Joram alijisikia faraja kwa kulibaini hilo. Aliamini kuwa ilikua hatua moja mbele. Hata aliichukulia kuwa ilikuwa hatua fupi sana, kwani bado ilizua maswali mengi zaidi ya majibu. Mkono wa Jibril ni moja ya makusudi ya watu? Kwa uzoefu wake Joram alishuku kwa kuwepo kundi la magaidi kuliko mmoja mmoja kwani ndani ya kundi, kuna mmoja, siku moja atatapika ukweli, ama katika ulevi ama kwa matumizi ya fujo ama hata usaliti tu. Gaidi mmoja mmoja ni yeye na roho yake. Hatatoa siri zake kwa gharama zozote hata kwa kumwuza mama yake mzazi.