Hadithi: Mikataba ya kishetani

Hadithi: Mikataba ya kishetani

5

Afande Chaku alipotoka katika eneo la maafa alirejea moja kwa moja ofisini kwake. Simu za mara kwa mara toka hapa na pale zilimpa tabu katika kuhimiza usukani wa gari. Hata hivyo, alifika salama. Robo tatu ya wasaidizi wake walikuwa tayari wamerejea wakimsubiri kwaajili ya kutoa taarifa na kusubiri maelezo zaidi.

Muda mfupi baadaye, kikao kilifunguliwa. Kilianza kwa kupokea taarifa toka kwa wasaidizi hao.

Aliyekuwa akifuatilia mwenendo wa pesa alitoa taarifa ambazo zilimshangaza kila mmoja; wingi na idadi ya pesa ambazo zilikuwa zikipaa au kutua ndani ya nchi kila baada ya dakika chache. “Nani anasema Tanzania ni masikini? Ni masikini kwetu tuliokaa hapa na wakulima wa vijijini. Kwa wenzetu mabilioni ya fedha yanatembea huko na kule kama kumbikumbi. Kwa kweli, ni vigumu sana kupata jibu la haraka juu ya fedha ambazo zinastahili kutiliwa shaka,” alisema na kuongeza, “Hata hivyo ninayo orodha ya watu kama ishirini hivi ambayo bado naifanyia kazi. Naendelea kuipunguza kila baada ya uchunguzi wa kina.”

Afisa huyo alipiga hatua kubwa zaidi ambayo ilimsisimua Afande Chaku. Alichunguza pia akaunti za marehemu na kuona kama zingeweza kuwa na kitu cha kutilia wasiwasi. “Anazo shilingi milioni tatu tu, zilizotokana na mshahara wake. Hiyo ni akaunti yake ya CRDB. Akaunti yake nyingine CBA, ina elfu arobaini na haijatumika kwa miaka miwili.’

“Mshahara wake shilingi ngapi?” Afande Chaku aliuliza. “Laki tatu na themanini. Analipwa na Ikulu kupitia hazina.”

Chaku alinukuu mambo kadhaa katika daftari lake dogo. Kisha alimgeukia yule aliyetumwa kupata orodha ya watu waliokuwepo hotelini hapo. Chaku hakuitazama orodha hiyo iliyoandikwa vizuri kwa mwandiko wa mkono.

“Muuaji hakuwa ndani ya hoteli, alikuwa nje. Hilo halina mjadala. Lakini kuna mtu aliyeondoka na briefcase ya marehemu. Hatuna hakika kama alikuwa na uhusiano na tukio hili ama la. Lakini tunamtaka. Na tunaitaka briefcase irudi ndani ya masaa ishirini na nne. Ondoka, rudi hotelini pale. Tazama tena na tena chochote kilichopatikana katika zile kamera zao za ulinzi. Fanya mahojiano na kila mtu anayeweza kukusaidia. Zaidi tumia uwezo wako wa ziada, ikibidi muamshe bibi yako au babu yako aliyekufa akuwezeshe kurudi hapa ama na briefcase hiyo, ama kichwa cha aliyeichukua.”

Wawili watatu walicheka. Havikuwa vicheko vya anasa, kwani haukuwa mzaha.

Taarifa ziliendelea kumiminika. Uwanja wa ndege uchambuzi uliendelea, na kadhalika na kadhalika.

Mtu mmoja akamletea Afande Chaku chai na keki mbili. Ndio kwanza Afande Chaku akakumbuka kuwa alikuwa hajatia chochote kinywani kwa takribani masaa kumi na mbili, akaitazama saa yake. Ilikuwa saa nne na robo usiku. Aliinywa chai hiyo na kuteketeza keki kilafi. Akaagiza maji ambayo alikunywa glasi mbili haraka haraka na ya tatu taratibu.

Afande Chaku akakumbuka jambo jingine. Siku hiyo alikuwa hajanywa! Akatabasamu. Akaamua kurudi nyumbani kwake na kupata usingizi ili kesho yake aendelee na shughuli hizo.

Simu ya Inspekta Matata ambayo hakuitegemea iliingia ghafla. “Unaendeleaje?” Mzee huyo aliuliza bila salamu za kawaida.

“Tunaendelea. Bado tupo katika hatua za awali. Sijaona jambo la maana la kuripoti,” Afande Chaku alijibu kisha alikumbuka kuongeza neno, ‘Afande.’

“Nataka kujua kila hatua uliyopiga. Nataka kujua hata kila mnachofikiria. Unajua huku kuna sokomoko?”

“Najua, afande.”

“Basi utakuwa unajua pia kuwa umekalia kuti kavu,” simu ikakatwa.

Chaku alitafakari kwa muda kabla ya kuvuta kompyuta yake na kuanza kuandaa taarifa ambayo hakuwa tayari kuiandika. Ilikuwa kazi ngumu kuliko hata ile ya kumtafuta muuaji.

***

Frank Mwaipula hakupata usingizi. Toka alipofika nyumbani kwake jana, akiwa na briefcase ya watu mkononi, alihisi akilizake zikiwa hazifanyi kazi vizuri. Hakujua kwanini aliondoka na begi hilo. Hakujua kwanini haondoki kwenda kulirudisha. Zaidi ya yote hakujua kwanini alilifungua!

Mwaipula alikuwa akiishi peke yake, katika nyumba yake binafsi ambayo alianza kuijenga miaka minne iliyopita.

Pato lake lilitokana na ‘Kuzima’ habari moja nzito ya tajiri aliyekuwa akiingiza chakula kichafu isivifikie vyombo vya habari lilimwezesha kununua kiwanja kidogo, Sharif Shamba. Alikusudia kujenga nyumba ya vyumba sita, lakini kwaajili ya ulevi wa kupindukia aliishia vyumba viwili. Kwa jitihada za mke wake, waliweza kupata umeme na bomba la maji. Halafu, pesa zikakatika na ulevi ukaongezeka maradufu. Halikuwa jambo la ajabu kwa Mwaipula kutofika nyumbani kwa siku mbili na alipofika alikuwa taabani kwa ulevi, mfukoni akiwa hana hata senti moja. Hali hiyo ilisababisha kutoweka kwa amani nyumbani humo hata yakamshinda mkewe. Usiku mmoja Mwaipula hakumkuta mkewe wala mtoto wao wa miaka mitatu. Hakumtafuta. Kwa namna moja aliona kama faraja kutokuwa na mtu wa kumsumbua kwa maswali na mahubiri.

Hivyo, Mwaipula alikuwa na faragha ya kutosha kuhangaika na briefcase hiyo hadi alipofanikiwa kuifungua. Lilikuwa begi la kisasa, lililofunguliwa kwa namba. Alicheza na namba zile kwa muda mrefu kabla ya kuipata ile iliyokusudiwa.

Kama alitarajia fedha katika begi hilo, hazikuwemo. Lakini kilichokuwemo kilimsisimua zaidi ya fedha. Zilikuwemo hotuba za Rais zenye sahihi yakechini. Aidha zilikuwemo nyaraka mbalimbali za Ikulu zilizoandikwa ‘Top Secret’ ambazo bila shaka zilikusudiwa kwaajili ya macho ya Rais pekee na wateule wake wachache. Kama mwandishi, ilimsisimua sana kujiona akiwa sambamba na Ikulu kwa mambo ambayo si kila mtu angepata kuyajua.

Hata hivyo, kengele za hatari zilikuwa zikisikika masikioni mwake. Hisia zilimwambia kuwa kwa kuifungua briefcase ile alikuwa akijiweka matatani bila sababu za msingi. Gereza linakuita Mwaipula… funga begi la watu lipeleke polisi mara moja… Alihisi nafsi ikimwambia.

Nafsi ya pili, ilikuwa na mamlaka zaidi, ilimshurutisha kuendelea na udadisi. Alitoa barua zile chini na kuanza kulipekua begi hilo kwa umakini Zaidi. Lilikuwa na mifuko mbalimbali ya pembeni. Mwaipula aliikagua yote, mmoja baada ya mwingine. Alipata nyaraka zaidi, daftari la kumbukumbu za kila siku na namba kadhaa za simu. Wakati akianza kufunga mfuko huo iliaendelee kusoma nyaraka ndipo alipobaini kuwepo kwa mfuko mwingine, wa siri zaidi, nyuma ya kabrasha lililofunika funiko juu ya begi hilo. Alipapasa, akahisi kitu. Akapeleka vidole vyake na kupekenyua kitu hicho.

Ilikuwa flash! Yenye ukubwa wa kidole chake cha shahada.

Flash, katika dunia ya leo ya maendeleo makubwa katika sayansi na teknolojia hakikuwa kitu kigeni. Watumiaji wote wa kompyuta walijua kuwa flash ni teknolojia ya kisasa zaidi ya kuhifadhi nyaraka na kumbukumbu, badala ya kuitegemea kompyuta yenyewe, disketi au CD ambavyo ni vikubwa na uwezo mdogo wa kuhifadhi mambo. Flash na udogo wake ina uwezo wa kubeba majalada ya vitabu vingi vyenye ukurasa miatatu au nne, hata elfu moja, kila kimoja.

Lakini si hilo lililomsisimua Mwaipula. Kilichomsisimua zaidi ni jinsi flash hiyo ilivyofichwa vilivyo, katika hali ambayo haikukusudiwa ionekane kwa urahisi. Maandishi juu ya flash hiyo pia yalimvutia.

Top Secret: Mikataba ya Kishetani,’ yalisomeka. Aliishika flash hiyo kwa mkono unaotetemeka na kuikodolea macho kama anayejaribu kutabiri kilichomo ndani yake.

Ni hilo lililomnyima usingizi na kumwacha akigalagala kitandani usiku kucha. Alfajiri, wakati jogoo wa majirani wakianza kuwika, mlango wake uligongwa. Mwaipula alishituka sana. Hisia za hatari, alizokuwa nazo usiku mzima zilimrejea kwa nguvu zaidi. Hakupata kugongewa alfajiri kama hiyo kwa miaka.

Mlango uligongwa tena, kwa nguvu kuliko awali. Mwaipula alichupa toka kitandani na kusukumia briefcase ile uvunguni. Aliduwaa na flash mkononi akitafakari wapi aifiche.

Mara mlango ulipigwa teke, kwa nguvu zaidi, ukafunguka. Watu wawili waliofunika nyuso zao kwa matambara meusi waliingia, kila mmoja akiwa na bastola mkononi.

“Wewe ndiye Frank Mwaipula…, Mwandishi?”

“Ndi… ndiyo. Kuna nini?”

“Mjinga huyo,” mwenzie alimjibu. Akamgeukia Mwaipula, aliuliza, “kwanini leo hukukesha kwenye mabaa na vilabu vya usiku kama kawaida yako? Unajua umekwisha tuharibia siku yetu? Haya toa!”

“Nini?”

Kofi kali lililotua usoni mwake lilimfanya Mwaipula apepesuke na kuanguka chini. Teke lililofuata hapo, lilimwingia barabara tumboni.

“Toa,” aliamriwa

“Nitoe…nini?”

“Hujui sio? Haya subiri tukuonyeshe” alijibiwa.

***

Nilishusha pumzi ya ghafla mara baada ya kurudi hotelini na kujifungia. Nikajitupa kitandani kujipumzisha na kutuliza akili yangu. Haikutulia. Kengele za kuashiria hatari zilikuwa zikigonga katikati ya ubongo wangu kila nilipojiuliza nini ninachokifanya, kama kazi yangu nilishaifanya, tena kwa ufanisi mkubwa kabisa. Kama malipo niliyapokea, tena makubwa kuliko nilivyotegemea. Ya nini basi kujitia katika hatari ati kwaajili ya shahuku tu ya kumfahamu mwajiri wangu? Ya nini kusumbua kichwa changu kujua ilikuwaje nikapewa maelezo yasiyo na shaka juu ya mhanga wangu?

“Nahitaji kuondoka mara moja.” Nilijikumbusha. Haikuwa kuondoka pekee. Nilihitaji kuhama hoteli hiyo pamoja na kuhama katika sura ya umbile la kike. Watu walioniona pale msibani si wachache. Bila shaka, tayari watakuwa wakiulizana maswali mengi yasiyo na majibu juu ya mwandishi huyu wa kike aliyejitanda baibui gubigubi.

Nahitaji kubadilika pia. Inapendeza kuwa kijana wa kiume mwenye mvuto zaidi ya msichana mrembo. Kazi ya kujibadili haikuwa rahisi, inahitaji muda, umakini na usiri wa hali ya juu. Sikuwa na budi kuifanya. Sudi ya maisha yangu ilikwisha nitupa katika mkondo huo.

Nililala pale siku nzima, mchana na usiku wake, kando ya maiti zote zile, bunduki ikiwa bado mkononi mwangu. Ilikuwa kama ndoto, asubuhi ya siku ya pili mlango ulipofunguliwa ghafla na wazungu waliovalia kijeshi kuingia ndani. Walishangazwa na wingi wa miili iliyolaliana huku ikiwa imegandiana damu. Walishangazwa Zaidi kuniona mtoto mdogo nikiwa hai, bunduki ikiwa imemwelekea maiti mwingine aliyefunika tambara usoni.

“Ni wewe uliyemuua huyu?”

Nilitikisa kichwa kukubali. Wakatazamana kwa mshangao. Mmoja wao alinitazama kwa makini zaidi, jicho kwa jicho kwa dakika nzima kabla hajatikisa kichwa chake kwa namna ya kujiridhisha kwa jambo fulani kichwani mwake.

Pilikapilika zikaanza. Watu wengine waliovaa majoho meupe, yenye nembo za ‘Red Cross’ waliingia na kuanza kubeba maiti za wazazi na ndugu zangu, moja baada ya nyingine. Hadi leo, sijui zilipelekwa wapi, pengine katika makaburi ya halaiki kwaajili ya wingi wa vifo vilivyokuwa vikitokea katika kipindi kifupi.

Mimi nilipelekwa hospitali. Kutembea kwa miguu yangu ilikuwa kazi ngumu.Yule mshenzi alikuwa ameniumiza. Nilipata matibabu kwa siku kadhaa kabla ya kutolewa hospitalini hapo. Nilitegemea kupelekwa katika kambi zilizofunguliwa kwaajili ya mamia ya yatima walioibuka ghafla kufuatia mauaji haya ya kimbari. Lakini nilishangaa nilipotengwa na wenzangu kwa maelezo ya yule askari aliyenitazama sana kwamba “huyu si wa kawaida.”

Ulikuwa mwanzo wa safari yangu mpya ya kimaisha, safari ambayo ilianza kwa kuhamishiwa katika eneo ambalo sikulijua, ambamo nilipatiwa chakula pamoja na malazi mazuri sana kwa takribani mwezi mmoja. Wakati wote huo nilikuwa nikiiitwa ofisini ambako niliulizwa maswali mengi kwa muda mrefu. Baadhi ya maswali yalikuwa ya kipuuzi, baadhi yakirudiwa mara kwa mara, niliyajibu yote bila kujali hili tayari limeulizwa au la. Baadaye nilibaini kuwa maswali hayo yalilenga kupima ujasiri, upeo wangu wa fikra na ustahimilivu.

Kisha nilihamishwa. Nilipelekwa katika nchi nyingine ambayo pia sikuhifahamu na kuanza kupewa mafunzo ya nguvu. Nilifundishwa kutumia silaha mbalimbali, kutega na kutegua mabomu, kubuni silaha n.k. Kwa mfano, nilionyeshwa jinsi chupa ndogo ya mafuta ya taa au kibiriti inavyoweza kuwa bomu kubwa ambalo lingeweza kubomoa jumba la ghorofa kumi.

Zaidi nilifundishwa shabaha.

Kila silaha ina namna yake ya kupata shabaha. Kisu cha mkononi kina namna yake ya kukishika na jinsi ya kukirusha. Bastola ina njia zake na bunduki kubwa pia. Yote hayo niliyapokea kwa furaha, nikifurahia kila somo. Zoezi la kutumia mikono na miguu hata kuua mtu kwa vidole tu nililifurahia zaidi. Nilijiona kama mfalme au Mungu mtu kila nilipojumuika na watu wengine ambao ningeweza kuwaua kana kwamba namuua mende.

Pia nilijifunza lugha mbalimbali; Kiswahili, Kiingereza, Kiarabu, Kifaransa, Kichina, Kijerumani na lugha zingine nyingi. Lugha zote hizi nilizisoma kwa bidii.nikijitahidi kufanya vizuri katika kila lugha tulizofundishwa.
 
6

Askari aliyepewa jukumu la kumtafuta aliyeondoka na briefcase, alifanikiwa kumfahamu mtu huyo baada ya kufanya kazi kubwa; alisoma tena utafiti wake wa watu waliokuwepo hotelini hapo siku ya tukio kwa makini zaidi. Hakuweza kukisia kwa kusoma majina yale tu. Yalikuwa majina mengi, hivyo, aliomba kutazama tukio lote lililorekodiwa kwenye kamera za hotelini humo.

Hapo ndipo alipoweza kumbaini mtu aliyemtaka.

Frank Mwaipula.

Akatoa simu yake ya mkononi na kupigia watu mbalimbali kuhusu mtu huyo. Aliuliza hiki na kile juu ya mtu mwenye jina hilo. Haukupita muda kuwa na taarifa iliyojitosheleza; Wapi anaishi na anajishughulisha na nini.

Kabla ya kurudisha simu yake mfukoni,alibonyeza vitufe kadhaa kabla kumpata Afande Chaku upande wa pili.

“Afande, nimempata.”

“Nani?” Upande wa pili uliuliza kwa mshangao na kisha ukaongeza, “Ongea kama askari mwenye uzoefu, unadhani jeshi la polisi linamtafuta mtu mmoja tu!”

“Samahani Afande,” aliomba msamaha na kuendelea, “Nimempata mtu aliyeondoka na briefcase ya marehemu, anaitwa Frank Mwaipula, anaishi Kinondoni.” Akanyamza kusubiri maelekezo mengine toka kwa Afande Chaku.

Good,sasa fanya hivi, tangulia Kinondoni, tunakuja hapo, make sure mtu wetu hagundui kama anafuatwa wala hatoroki eneo hilo kabla hatujafika.

Simu ikakatwa.




Kwa wakazi wa Mwanzawanaohitaji kitabu hiki,piga simu namba 0763886672 na wale wa Dar na maeneo mengine piga simu namba 0712504985 au 0763044459 kwaajili ya kujipatika kitabu hiki na vingine vingi vya Joram Kiango.
 
***

Afande Chaku akiongoza jeshi lake, walifika Kinondoni muda mfupi baada ya kupokea taarifa za mtu aliyeitwa Frank Mwaipula. Waliizingira nyumba yake mara moja. Afande Chaku alienda mpaka mlangoni na kugonga mlango. Nyumba ilikuwa kimya, kana kwamba hakukuwa na mtu ndani. Afande Chaku aligonga tena huku akisikiliza kwa makini vishindo vyovyote ndani ya nyumba hiyo. Bado ilikuwa kimya. Akaamua kuingia ndani. Akajaribu kufungua mlango ambao ulikuwa wazi kana kwamba ulikuwa unamsuburi yeye.

‘Mtego!’ Aliwaza.

Akaingia ndani taratibu, bastola yake, mkononi tayari kwa lolote. Polisi watatu wakimfuata nyuma yake. Hakuamini alichokiona. Matone ya damu yalikuwa yemetapakaa chini. Afande Chaku alivuta hatua taratibu, macho yake yakifuata matone hayo mpaka yalipoangukia juu ya kitanda ilipokuwa maiti.

Maiti ya Frank Mwaipula.

Maiti hiyo ilikuwa imelala kitandani huku mwili mzima na kitanda vikiwa vimetapakaa damu. Baadhi ya vidole vikiwa vimeondolewa, jicho lake likiwa limeumizwa vibaya kama lililotaka kunyofoka. Vitu vya chumbani humo vikiwa vimetupwa hovyo, nguo zilitupwa huku na kule, makaratasi yalimwagwa hovyohovyo, maiti yenyewe ikiwa juu ya kitanda huku godoro likiwa nusu limebinuliwa, nusu likiwa limebaki kitandani.

‘Nani ambaye atakuwa amefanya kazi hii’ Afande Chaku alijiuliza akiitazama maiti. Kama angekuwa si mzoefu wa mauaji hayo, asingekuwa na uwezo hata wa kuyatupia macho maiti hiyo.

‘Cleopatra, alafu Frank Mwaipula, alafu?’

Alijiuliza bila kupata majibu. ‘Ni lazima mauaji haya yakome, muuaji anaweza kuwa yuleyule aliyemuua Cleopatra! Ila sidhani.’

“Afande, tufanye nini sasa?”

Polisi aliyekuwa nyuma yake alimshitua Afande Chaku toka katika lindi la mawazo. Akageuka kumtazama, macho yake yakionyesha wazi hasira kali dhidi ya mtu yeyote aliyefanya kitendo kile.

“Fanyeni utaratibu wa maiti hii kupelekwa hospitali, iwe chini ya ulinzi, wengine wabaki hapa wakilinda nyumba hii kwa zamu, hakikisheni hakuna anayeingia wala kutoka humu,” Chaku alimtazama polisi huyo kuona kama anachoongea kinamwingia barabara, kisha akaendelea, “Kwa yeyote aliyefanya mauaji haya, anaweza kuwa hajapata kile anachokitafuta hivyo anaweza kurudi hapa ama pengine yupo akitutazama na kusubiri tuondoke ili atimize azma yake.” Alimaliza.

Akazunguka hapa na pale ndani ya chumba hicho, akitazama hiki na kugusa kile kwa uangalifu bila kuharibu ushahidi unaoweza kupatikana. Akachungulia hapa na pale.

Hakukuwa na dalili ba briefcase yoyote.

Akatoa daftari lake dogo na kunukuu kitu Fulani. Kisha akarirudisha ndani ya mfuko wake koti alilokuwa amevaa.

Aliporidhika na msako wake, alitoka nje ya chumba hicho, mikono mfukoni, ndipo alipogusa tena ile bahasha aliyopewa Muhimbili alipoenda kuiona maiti ya Cleopatra.

Wauaji wengine huwa na tabia ya kuuzulia msiba na wengine hudiriki hata kwenda kuzika mtu waliyemuua.

Ndivyo Afande Chaku alivyo amini. Akaingia ndani ya gari lake na kuliwasha kisha kulielekeza Mikocheni.
 
***

Nyumba ya Dkt. Twalib Khalfan ilimlaki kwa vilio vya kwikwi vya kina mama waliokuwa wamekaa ndani wakiomboleza, huku nyimbo za dini zikiimba kwa mbali. Afande Chaku alipitiliza moja kwa moja mpaka chini ya muembe alipokuwa amekaa mfiwa akiomboleza pamoja na wanaume wachache.

Chaku hakusumbuliwa na macho ya waombolezaji, walimchukulia kama mmoja wao kutokana na nguo za kiraia alizokuwa amevaa. Aliwasalimu wote na kuwapa pole. Kisha alijikaribisha katika kiti kimojawapo kilichokuwa kitupu. Akaomba kuongea na Dkt. Khalfan faragha. Khalfan hakuwa na hiyana, alinyanyuka toka alipokuwa amekaa na kumuelekeza mgeni kuingia ndani ya nyumba yake ambapo walikaa kwenye ukumbi wa chumba kikubwa kilichokuwa na utulivu ambao Afande Chaku aliufurahia kimoyomoyo.

Wakakaa kwenye viti vilivyokuwa ndani humo.

“Dkt. Khalfan Twalib, pole sana kwa msiba uliokupata.”

“Asante sana.” Twalib aliitikia kwa sauti ndogo lakini iliyomfikia vema Afande Chaku.

“Mimi ni afisa wa Polisi,” Chaku aliongea akitoa kitambulisho chake na kumkabidhi Dkt. Twalib ambaye alikitazama kwa muda kabla ya kukirudisha kwa Afande Chaku.

“Nimebeba jukumu hili la kumpata muuaji, hivyo ningeomba ushirikiano wako.” Afande Chaku alisema. Dkt. Twalib Khalfan aliitikia kwa kichwa bila kusema lolote.

“Dokta, kuna lolote ambalo umeliona si la kawaida hapa msibani?” Chaku alianza kuuliza.

Dkt. Twalib Khalfan alisita kabla ya kujibu, pengine alikuwa akijaribu kuvuta picha. “Ndiyo,” alijibu huku amemkazia Afande Chaku macho.

“Lipi?” Chaku aliuliza kwa shahuku kubwa iliyojionyesha dhairi machoni mwake.

“Mwandishi wa habari mwenye baibui jipya.”

“Baibui?” Afande Chaku alishangaa, akatoa daftari na kalamu, tayari kwa kunukuu chochote alichoona kinafaa.

“Ndiyo, alikuja mwanana mama akidai ni mwandishi wa habari akiwa amevalia baibui lililoficha sehemu kubwa ya mwili na sura yake.”

Afande Chaku alinukuu kitu fulani. Kisha akamtazama tena mwenyeji wake, “Alisema anaandika gazeti gani?”

This Day.”

Afande Chaku alinukuu tena.

“Kwanini unamuhisi kuwa si wa kawaida?” Afande Chaku aliuliza.

“Kwasababu mhariri wa This Day, ni rafiki yangu. Alinipigia jana kunipa pole. Nikamdokeza juu ya mwandishi wake huyo. Mhariri alishangaa, kwani kwa mujibu wa maelezo yake hajapata kumtuma mwandishi kwangu na hana jina hilo katika orodha ya waandishi wake,” Khalfan alifafanua.

Kalamu ya Afande Chaku ilicheza katika kurasa za daftari lake. “Hakuna kitu kingine ambacho si cha kawaida kwa mwandishi huyu?” aliuliza.

“Kipo”

“Kitu gani?”

“Ni kitu kidogo tu. Lafudhi yake. Pamoja na ukweli kuwa anazungumza Kiswahili, si lugha yake ya kwanza. Ama ni mgeni ama amekulia ugenini.”

Afande Chaku alitafakari hilo kabla ya kuendelea na swali lake la pili. “Dkt. Khalfan kitu fulani kimekua kikisumbua sana akili yangu na ya kila mtu anayehusika kwa namna moja ama nyingine na swala hili. Ni namna ya jinsi marehemu alivyokutwa na maafa. Alikuwa kati ya Rais ambaye kwa kawaida anakuwa na maadui wengi kama alivyo na marafiki. Upande wa pili alikuwepo tajiri mkubwa ambaye pia ana maadui lukuki kama alivyo na marafiki. Tunahitaji maoni yako. Unadhani muuaji alimkusudia yeyote kati ya hao wawili akakosea shabaha na kumuua yeye?”

Lilikuwa swali ambalo tayari lilikuwa limemsumbua sana Khalfan. Hakuweza kuamini kama kuna mtu duniani aliyepata kumchukia Cleopatra kiasi cha kumuua, tena hadharani. Hata hivyo, kwa yale aliyoyasoma gazetini na kutazama eneo la maafa katika televisheni alishindwa kujizuia kushuku kuwa muuaji alikuwa mtu anayeijua kazi yake, hivyo asingekuwa na namna yoyote ya kupoteza shabaha kwa kiwango kile.

Alimweleza hayo Afande Chaku.

“Nakumbuka kusoma mahala kwamba marehemu alikutwa na kifo wakati mkiwa mmetengana?” Afande Chaku aliongeza swali lingine.

“Ni kweli.”

“Mlitengana kwa muda gani?”

“Kama miezi sita hivi.”

“Kitu gani kiliwatenganisha?”

“Sijui.”

Afande Chaku aliinua uso na kumtazama Khalfan kwa mshangao. “Sikuelewi. Mkeo wa ndoa, mliyeishi naye miaka nenda rudi atakuachaje na usijue sababu?”

“Hata mimi nimekuwa nikijiuliza swali hilo hilo kila siku,” lilikuwa jibu la Khalfan, ambalo lilizidi kumchanganya Chaku.

“Mligombana?”

“Hatujapata kugombana”

Chaku alitafakari kwa muda. Akakumbuka kile kijikaratasi alichokipata kwa daktari wa Muhimbili. I love you King Suleiman. Penzi lao liliingiliwa kati. Ama mume hajui ama anajisikia kiburi kukiri hilo hadharani. Akaamua kubadili mkondo wa maswali yake.

“Mna watoto?”

“Mmoja tu.”

“Yuko wapi?”

“Yuko masomoni Arusha, kidato cha tano. Kesho atakua hapa. Nimemtumia tiketi ya ndege.”

“Unaweza kukumbuka siku za mwisho kabla ya marehemu kuondoka alikuwa na mwenendo gani?”

Khalfan alitafakari swali hilo kwa muda kabla hajajibu kwa neno moja tu, “Alibadilika.”

“Kwa vipi?”

“Hakuwa Cleopatra yuleyule ambaye nilimfahamu. Alikuwa mtu mwingine. Alikuwa mkimya mara kwa mara, huku akionekana kutafakari jambo kwa muda mrefu. Simu yake ya mkononi ilipoita, aliipokea bila uhuru huku akihakikisha siyasikii maongezi yake. Halafu akaanza tabia ya kuchelewa nyumbani. Nilipomuuliza alidai shughuli nyingi. Siku moja alipata kulala nje, mwenyewe akidai kuwa anakesha kazini.” Khalfan alieleza.

King Suleiman huyo! Chaku aliwaza akichekea tumboni, wazo ambalo alijikuta akilitilia mashaka pale Khalfan alipoongeza, “Kama angekuwa mtu mwingine ningeweza kumshuku kuwa amerubuniwa huko makazini. Nadhani unajua ofisi kubwa zilivyo na mambo ya kishenzi. Lakini si Cleopatra. Nilimwamini, aliniamini. Nilimkuta bikira, alinikuta bikira.

Wanaume tunavopenda kudanganywa! Chaku aliwaza tena huku akibadili mkondo wa maswali yake. Aliuliza hili na lile, hata yale ambayo hakuyahitaji mradi Khalfan aendelee kuzungumza. Baada ya muda aliitazama saa yake. Muda ulikuwa umekwenda. Akainuka na kuaga kwa kumshukuru Khalfan kwa ukarimu na ushirikiano wake.

“Wewe pia nakushukuru sana, afisa. Umenitoa upweke.”

Khalfan alimjibu, akainuka na kumfungulia mgeni wake mlango.

Ghafla, kama aliyekumbuka jambo, Chaku aligeuka na kuutia mkono wake mfukoni. Aliutoa ukiwa na kile kipande cha karatasi alichopatiwa na Daktari. “Samahani,” alimwambia Khalfan. “Kuna karatasi hii imekutwa katika mfukon wa marehemu. Unaweza kumfahamu mtu huyu aliyeachiiwa ujumbe huu?”

Khalfan aliusoma, kwanza harakaharaka, kisha taratibu. Mara akainua macho yake kumtazama Chaku. Alikuwa amebadilika sura na sauti.

“Unasema mliupata wapi?” aliuliza.

“Marehemu alikuwa nao mfukoni,” Chaku alimjibu.

Khalfan alizidi kubadilika. Alitetemeka mikono na midomo. Akashindwa kuhimili machozi ambayo yalimtoka bila kutarajia.

“Unamfahamu huyu King Suleiman?”

“Namfahamu sana.”

Moyo wa Chaku ukajawa na shahuku.

“Ni nani?”

“King Suleiman ni mimi.”

“Wewe! Yakoje mambo haya?”

Khalfan alimtazama Chaku. Kwa namna fulani alimhurumia, kwani asingeweza kuelewa. King Suleiman lilikuwa jina ambalo mwanzo wa penzi lao lilitumiwa kama siri miongoni mwao. Baadaye, baada ya ndoa, liligeuka kuwa jina pekee lililotumika kuthibitishha penzi na kukoleza mahaba yao. Lilianza kama mzaha, wakiwa shule ya msingi.

“Mwalimu: Cleopatra!”

“Cleopatra: Abee!”

“Mwalimu: Simama mbele ya darasa uniambie nani hapa anafaa kuwa mfalme Suleiman.”

“Cleopatra: Yule pale!”

Darasa zima lilipiga makofi.

“Mwalimu: Darasa hili litaongozwa na Mfalme Suleiman kama kiranja na Cleopatra msaidizi wake. Sawa?”

Ndivyo ilivyokuwa. Miaka ya shule ya msingi ilipoteketea walipotezana kwa muda. Walionana wakiwa sekondari. Ni Cleopatra aliyemwona kwanza Khalfan, “King Suleiman!” aliita. Dkt. Khalfan aligeuka na kushangazwa na msichana anayevutia kwa sura na umbile, kasimama pale akitabasamu. Alikuwa malaika!

“Malaika!” Khalfan aliita akimkimbilia na kumkumbatia.

“Malaika wangu! Ulipotelea wapi?” alimuuliza akimkumbatia kwa nguvu zaidi. Walipotengana kimwili, kiroho hawakupata kutengana tena. Kila mmoja aliishi kwaajili ya mwingine, alisoma kwaajili ya mwingine. Moyoni mwa Khalfan, Cleopatra alikuwa malkia halisi wa ‘Mfalme Suleiman.’
 
Namsaidia kujibu kila kimoja sh 10000 tu pia wale walioko mwanza mwaweza piga 0763886672//0788453209//0715120496 utapata nakala yako kwa being lhiyo hiyo
Nipe majina ya vitabu ulivyonavyo tafadhali....
 
Back
Top Bottom