SEHEMU YA 78
“Imekuwaje?”
“Mama! Hali ni ngumu sana!”
“Lakini si huwa kitu kama hiki kunakuwa na mwanasheria. Ningependa nionane na huyo mwanasheria ambaye alimsimamia katika hili,” alisema Rosemary huku akionekana kuchanganyikiwa hasa.
Hilo halikuwa tatizo, kwa sababu katika karatasi zile aliandikwa mwanasheria aliyemsimamia katika hilo, akatafutwa na alipoulizwa, alimwambia Rosemary kwamba kweli alikuwepo siku hiyo na yeye ndiye aliyemsimamia Mapoto kupata pesa hizo, na uzuri ni kwamba walikwenda kuandikisha mpaka mahakamani.
“Mpaka mahakamani?”
“Ndiyo!”
Rosemary hakutaka kukubali, alitaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea, akaelekea mahakamani, kweli, alipofika akaonyeshewa nyaraka zote alizosaini mume wake kama kukamilisha kuuchukua mkopo huo mkubwa.
Miguu yake ikakosa nguvu, palepale mahakamani alipokuwa, akapiga magoti na kuuficha uso wake, akaanza kulia kama mtoto mdogo kwani alihisi akiwa amebeba dunia nzima, alijiona kuwa mtu mwenye mikosi kuliko watu wote duniani.
Hakujua angekimbilia wapi, hakujua angefanya nini kuzilipa fedha hizo, kilikuwa kiasi kikubwa sana ambacho asingeweza kulipa, na kama angeshindwa kulipa, inamaana kuwa angepokonywa nyumba aliyokuwa akiishi.
“Haiwezekani! Mungu! Mume wangu hawezi kufanya ujinga huu! Hapa kuna kitu, ninamuamini mume wangu, ni mtu makini, tulishirikiana kwa kila kitu, hawezi kufanya hivi,” alisema Rosemary huku akiwa amekiinamisha kichwa chake, alikuwa akilia kama mtoto.
Watu wote waliokuwa mahali hapo walimshangaa, walimfahamu, alikuwa mke wa mtu aliyekuwa na nguvu sana nchini Tanzania, hawakujua ni kitu gani kilitokea mpaka kumwaga machozi namna ile hapo mahakamani. Hawakukubali, wakawapigia simu waandishi wa habari na kuwapa taarifa kile kilichokuwa kinaendelea mahali hapo.
Ni kama Rosemary alijua, hakutaka kukaa sana mahakamani hapo, akaingia ndani ya gari lake na kuondoka huku akiendelea kulia kama kawaida. Baada ya dakika kadhaa, waandishi wakafika mahali hapo wakiwa na kamera zao, walitaka kuhakikisha kile walichokuwa wameambiwa.
“Yupo wapi?” aliuliza mwandishi mmoja.
“Ameondoka!”
“Mna uhakika kwamba ni yeye?”
“Sasa sisi tutakupa taarifa ya uongo bwana! Kwani hatumjui?” aliuliza jamaa mmoja.