SEHEMU YA 79
“Inawezekana mkawa mmemchanganya. Si mnajua duniani wawiliwawili!” alisema mwandishi huyo.
“Mtafuteni. Ila alikuwa akilia kama mtoto!”
“Kweli?”
“Habari ndiyo hiyo!” alijibu mtoa taarifa, waandishi wa habari wakaondoka na kuanza kuelekea nyumbani kwa Rosemary huku wakiwa na kiu ya kutaka kufahamu ukweli juu ya kitu kilichokuwa kikimliza mahakamani?
“Hii ishu inaweza kuwa habari kubwa sana,” alisema mwandishi mmoja.
“Ndiyo hivyo! Halafu siku nyingi hajasikika, kama tukiiandika, inaweza ikawa kiki kubwa ya kutupatia wasomaji wengi,” alisema mwandishi mwingine.
“Kweli kabisa. Hebu tuwahi nyumbani kwake kabla ya waandishi wengine hawajajua kuhusu hii taarifa,” alisema mwandishi mmoja, safari ikaanza.
*** “Ni kweli?” aliuliza mmoja wa waandishi wa habari waliokwenda kuonana naye.
“Kuhusu nini?”
“Kuhusu benki kuitaka nyumba yako kwa deni la milioni mia tano unalodaiwa?”
“Naomba mniache kwanza.”
Rosemary hakutaka kulizungumzia hilo, alitaka kuachwa kwani kwa kipindi hicho akili yake haikuwa sawa kabisa. Alijua fika kwamba mumewe hakuchukua huo mkopo, mumewe hakuwahi kufanya jambo kimyakimya pasipo kumtaarifu lakini hakujua mambo hayo yalisababishwa na nini kwani kama kufariki, alifariki na alichokijua ni kwamba kila kitu kilianza upya.
Akawasiliana na Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania National Party, Elibariki Edward na kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Mwenyekiti huyo hakuamini, alichomwambia ni kwamba angeonana naye na kulizungumza hilo kwani naye kwa jinsi alivyomfahamu Mapoto, asingeweza kufanya jambo kama hilo.
“Nakuja!”
Ndani ya nusu saa, mwanaume huyo alikuwa nyumbani kwa Mapoto kwa ajili ya kuzungumza na Rosemary. Alikuwa mwanamke mjane aliyehitaji msaada kwa hali na mali. Alizungumza naye, akamwambia jinsi alivyoletewa barua ile na mwanasheria wake kufuatilia kila kitu mahakamani na kuambiwa kwamba kile alichokiona ndicho kilivyokuwa.
“Inawezekana vipi?” aliuliza Edward huku akishangaa.
“Sijajua! Nimechanganyikiwa, sijajua ni kitu gani natakiwa kufanya. Huu ni uonevu, kwa nini jambo hili wasingelisema wakati mume wangu akiwa hai? Kwa nini wamesubiri mpaka afe?” aliuliza Rosemary.