SEHEMU YA 67
Bado Watanzania walihitaji mabadiliko, kila mtu alijiandikisha kwa ajili ya kupiga kura kwani kitendo cha kuwa na kadi ya kupiga kura ilimaanisha kwamba ungepiga kura na kumchagua kiongozi uliyekuwa ukimtaka, na wengi waliaidi kumwangusha Bokasa na kumchagua kiongozi wa chama pinzani.
“Mwaka ujao tunashinda, cha msingi ni kuziba mianya yote ya wizi wa kura na kuwataarifu watu juu ya upigaji kura ili tusije kuchezewa mchezo kama mwaka ule,” alisema Edward.
Alifanya kazi zake kama kawaida, ilipofika mchana, muda wa kurudi nyumbani akaingia ndani ya gari lake na kuanza kurudi nyumbani. Wakati gari likiwa linaingia katika barabara kubwa ya Lansdowne, ghafla wakakutana uso kwa uso na gari moja kubwa ambalo lililigonga gari lao, na kwa sababu lilikuwa kwenye mwendokasi, gari la balozi Mapoto likaharibiwa vibaya kiasi kwamba ilikuwa ni vigumu kuamini kama ndani ya gari hilo kungekuwa na mtu ambaye angetoka salama.
“Mungu wangu!” alisema mwanaume mmoja aliyekuwa kwenye gari jingine.
Kila mtu alishtuka, ajali iliyokuwa imetokea ilikuwa mbaya mno, gari la balozi Mapoto liliharibika vibaya na watu waliposogea kuangalia, kulitapakaa damu na hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akitingishika kuonyesha kwamba alikuwa hai.
Ulikuwa ni uzembe mkubwa mno kwani gari la balozi Mapoto lilikuwa katika njia yake lakini gari kubwa ambalo liliwagonga halikuwa kwenye njia yake, lilihama kutoka kati magari yanayoelekea upande wa Mashariki na kuhamia katika upande wa magari yanayokwenda upande wa Magharibi.
Ilikuwa ni ajali mbaya mno, kila mmoja aliyeiona, aliogopa, alitetemeka kwani katika histori ya ajali za barabarani hasa katika Jiji la New York, hakukuwa na ajali mbaya ya magari kugongana ambayo iliwahi kutokea kama ilivyokuwa ajali hiyo.