SEHEMU YA 74
Ulikuwa ni msiba mzito uliotokea nchini Tanzania, kila mtu alihuzunika, furaha ikatoweka mioyoni mwa Watanzania wengi. Mtu ambaye walimwamini kwamba angeweza kuyabadilisha maisha yao, aliondoka, Mungu alimchukua hata kabla hajapata nafasi hiyo.
Vijana wengi wakakata tamaa, walitamani kuona Tanzania ikiingia katika mabadiliko ya kweli, hawakukipenda Chama cha Labour Party, hawakumpenda Rais Bokasa kwa sababu hakujua kitu chochote kile kuhusu uongozi, aliongoza ilimradi tu kitu kilichowafanya watu wengi kuumia.
Ilikuwa imebaki miezi kadhaa kabla ya kuingia katika uchaguzi mkuu. Kuanzia kipindi hicho maisha yakawa magumu zaidi, serikali ikabana fedha kwa ajili ya kuitumia katika kipindi cha uchaguzi. Wananchi wakakosa pesa, mitaani hakukuwa na pesa tena hali iliyofanya hata matendo ya kikatili, wizi kuongezeka.
“Hakuna hela!” alisema kijana mmoja.
“Ndiyo! Rais amezibana eti kwa sababu ya uchaguzi wa mwaka kesho! Hii siyo haki kabisa,” alisema jamaa mwingine.
“Nyamaza! Ukisikiwa tu, msala. Hutakiwi kumwamini mtu yeyote yule, jikaze kisabuni kwani usalama wamemwagwa kila kona,” alisema jamaa mwingine na kumfanya jamaa aliyeanzisha mazungumzo hayo kunyamaza.
Hakukuwa na unafuu, Watanzania wenyewe waliichukia nchi yao, wengine wakadiriki hata kukimbia na kwenda nje ya nchi, matajiri hawakutaka kukaa nchini humo, walichokifanya wao na familia zao kuondoka na kuelekea Dubai, Oman, Marekani na sehemu nyingine kuendelea na maisha yao.
Kila kitu kikawa shaghalabaghala, ugumu wa maisha ukatawala kila kona, masikini walilia, kwa kile kiasi kidogo walichokuwa nacho ikawa kama wamenyang’anywa, ili upate pesa ilikuwa ni lazima ufanye kazi kwa nguvu, pesa iliyokuwa ikipatikana kwa urahisi, haikupatikana tena.
Maisha ya Rosemary na watoto wake yalibadilika, hakukuwa na furaha tena, kila siku kwao ilikuwa ni majonzi mazito. Kifo cha mapoto kilibadilisha maisha yao yote, kwa watoto wake, Godwin na Irene, nyumbani hawakuwa na furaha tena, hawakuwa kama zamani kwani baba yao ambaye ndiye alikuwa furaha kubwa mioyoni mwao hakuwa nao tena, baba yao ambaye kila siku aliwauliza kuhusu ndoto zao aliondoka maishani mwao.