Dunia haina usawa

Dunia haina usawa

SEHEMU YA 60

Hiyo ilikuwa ni amri, hakukuwa na mtu wa kuipinga, kila alichokitaka Rais Boksa ndicho ambacho kilitakiwa kufanywa mahali hapo. Polisi wakajipanga, nao wananchi wakaingia mitaani katika siku hiyo ambayo mwandishi huyo alikuwa akipelekwa mahakamani, hawakutaka kuona wakionewa, kila mtu alitaka haki na waliamini hakukuwa na haki bila kupambana, ili upate kile unachokihitaji ilikuwa ni lazima kupambana.

“Waziri mkuu amesema tupambane nao. Ikiwezekana tuue pale kunapotakiwa kufanya hivyo,” alisema IGP, alikuwa akiwaambia wenzake.
“Unasemaje?”
“Nadhani umenisikia. Waambie polisi wajipange asubuhi hiihii. Yeyote atakayeonekana na silaha yoyote karibu na uwanja wa mahakama, huyo halali yetu,” alisema IGP.

“Sawa mkuu!” wakaitikia kwa pamoja. Japokuwa mikwara ilitangazwa kila kona na polisi hao lakini wananchi hawakusikia, walichokitaka ni kuona mwandishi huyo akiachiwa huru. Hivyo wakaingia mitaani.
*** Polisi walikuwa wakitoa tangazo kwamba wananchi wote waliokuwa karibu na viunga vya mahakama walitakiwa kuondoka haraka iwezekanavyo lakini hakukuwa na mtu aliyeelewa.

Hakukuwa na mtu aliyeonekana kuogopa kitu chochote kile, walichokuwa wakikitaka mahali hapo ni kumuona mwandishi nguri wa habari za siasa nchini, Matamshi akiachiwa huru au hata kwa dhamana kwani kesi iliyokuwa ikimkabili haikuwa ya kweli bali kulikuwa na watu waliotaka kumuweka kifungoni kwa maslahi yao na si kwamba alisafirisha mzigo wa madawa ya kulevya kutoka nchini Marekani.

Polisi waliendelea kutangaza zaidi na zaidi lakini hakukuwa na mwananchi aliyeelewa, kwao, waliamini zaidi katika maandamano, walijua kabisa kwamba serikali isingeweza kuwakubalia kitu chochote kile kama tu wasingeandamana.
Magari ya polisi yaliyokuwa na maji ya kuwasha yakafika mahali hapo, polisi wakaongezeka huku wakiwa na bunduki zao zilizokuwa na mabomu ya machozi, walisimama imara huku wakisubiri kupewa ruhusa ya kufanya kile walichotakiwa kufanya mahali hapo.

Wakati tangazo la kuondoka mahali hapo likiendelea kutolewa, basi kubwa la gerezani likaanza kuingia katika viunga vya mahakama hiyo na liliposimama, washtakiwa wakaanza kuteremka kutoka ndani ya basi lile.
 
SEHEMU YA 61

Kitendo cha watu kumuona Matamshi, wakaanza kupiga kelele za shangwe huku wakiwataka polisi kumuachia mtu huyo, msafi ambaye hakuonekana kuwa na kosa lolote lile. Matamshi alikuwa kimya, alipowaona watu hao wakipiga kelele huku wakilitaja jina lake, akawaangalia, akatoa tabasamu pana kisha kuwapungia mikono.

“Mbona mnaonea sana, si mmuache na kama hamna kazi za kufanya mkalale,” alisikika mwananchi mmoja kwa sauti kubwa.
“Mwachieniiiiiiiiiii……mwachieniiiiiiii huyooooo,” walisikika watu kadhaa wakipiga kelele za kumtaka mtu huyo aachiwe huru.

Wananchi waigoma kabisa kuondoka mahali hapo mpaka pale Matamshi alipoingizwa mahakamani kwa ajili ya kujibu tuhuma zilizokuwa zikimkabili. Polisi hawakuchoka, waliendelea kuwahimiza watu hao waondoke mahali hapo lakini hakukuwa na mtu yeyote aliyeelewa, walitaka kushuhudia mtu huyo akiachiwa huru kwa kile kilichokuwa kimetokea.

Waandishi wa habari waliendelea kubaki mahali hapo, waliwajua polisi, waliona kabisa kukitokea fujo mahali hapo, walitaka kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Hawakutaka kuishia kupiga picha, walipata nafasi ya kuwahoji baadhi ya waandamanaji ambao hawakuficha hisia zao, walisema wazi kile walichokuwa wakiikiona juu ya mwanaume huyo ambaye alikuwa akipambana usiku na mchana kwa ajili ya kufichua uovu wa serikali.

“Hapa hatuondoki. Huu uonevu umezidi! Za chinichini zinasema kwamba walimtumia yule mzee kwa ajili ya kumkamatisha Matamshi kuhusu uuzaji wa madawa ya kulevya, hii siyo fea,” alisema mwanaume mmoja.

“Kwa hiyo hamuondoki!”
“Hata kama wewe mwandishi! Unaanzaje kuondoka?”
Baada ya kukaa kwa dadkika thetahini, polisi wakaanza kupiga mabomu ya machozi mahali hapo huku wakiwamwagia maji ya kuwasha.

Hakukuwa na mtu aliyebaki mahali hapo, wakaanza kukimbia kurudi katika Barabara ya Kawawa kwani kadiri mabomu yalivyozidi kupigwa mahali hapo, kila mmoja alihisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake.
 
SEHEMU YA 62

Rais Bokasa alikuwa kimya katika kiti chake, akili yake haikuwa sawa hata kidogo, hatua alizopitia katika uongozi wake zilimnyima raha, muda mwingi alionekana kuwa na mawazo tele.

Aliona kulikuwa na mambo mengi ya kufanya mbele yake, hakujua ni mahali gani alitakiwa kuanzia na kuishia. Wakati mwingine aliwaona watu wakiwa wamemzunguka, wakimzomea kwa kila kitu alichokuwa akikifanya.

Serikali ikaanza kukosa fedha, kodi zilizokuwa zikikusanywa kwa kiasi kikubwa zikapungua, akashikwa na hofu na wafanyabiashara kwa kuhisi kwamba walikuwa wakimzunguka, hawakuwa wakilipa kodi kama ilivyotakiwa kuwa.
Aliandaa mikutano na wafanyabishara mbalimbali na kuwaambia umuhimu wa kulipa kodi lakini hawakutaka kuelewa kwani kama wao wangeendelea kulipa kodi kama ilivyotakiwa basi kusingekuwa na shida yoyote ile.

Nchi ikaanza kuyumba kiuchumi, pesa ikakosekana mitaani, kila mtu aliyekuwa akiulizwa kuhusu pesa, alisema kwamba hakuwa nayo. Aliwalalamikia wafanyabiashara wengi, bado hofu yake ilikuwa ni kuhusu ulipaji wa kodi, aliamini kuwa wafanyabishara walikuwa wakikwepa ulipaji wa kodi hiyo.

Mahospitalini, watu walikosa dawa, vyuoni, idadi ya wanavyuo waliokuwa wakipelekwa ilipunguzwa na mikopo ikafungwa. Nchi ilikuwa kwenye hali ya hatari lakini alifanya hivyo kwa kuwa tu alitaka serikali ibaki na fedha, abane matumizi yaliyokuwa makubwa kwa ajili ya nchi yake.

Baada ya kufikiria sana, akagundua kwamba hata mabalozi waliokuwa katika nchi za nje ambao walikuwa wakiwasomesha watoto wao huko kwa kutumia pesa za serikali, walitakiwa kuwarudisha nchini na kusoma katika shule za hapahapa Tanzania.

Hakutaka kupokea ushauri juu ya jambo hilo, akawaita waandishi wa habari ikulu na kuwaambia kile kitu ambacho alikifikiria kwamba watoto wa mabalozi ambao walikuwa wakisoma nje ya nchi walitakiwa kurudishwa nchini Tanzania kwa kuwa tu nchi haikuwa na pesa ya kutosha.

“Warudi Tanzania?” aliuliza Mapoto, alikuwa akipewa taarifa na mkewe.
“Ndivyo alivyosema.”
“Daah! Kweli?”
“Ndiyo!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom