Date::10/25/2008
Dowans kurudi kwa mlango wa nyuma
*Waitunishia misuli Tanesco kuhamisha mitambo
Na Waandishi Wetu
Mwananchi
MIEZI miwili baada ya serikali kusitisha malipo kwa kampuni kuzalisha umeme wa dharura kuna taarifa kuwa serikali inapanga kuinunua mitambo hiyo.
Habari zilizolifikia Mwananchi Jumapili zinasema kuwa lengo la kununua mitambo hiyo ni kupunguza upungufu wa nishati ya umeme unaolikabili taifa ambao mara kwa mara umekuwa ukisababisha mgawo wa umeme pale mtambo mmojawapo unapoharibika au kina cha maji kupungua.
Akizungumzia suala hilo jana Ngeleja alisema ni kweli taifa linaweza kuinunua mitambo hiyo endapo watalaamu wake wataridhika nayo.
Alisema hali hiyo inatokana na upungufu wa mitambo ya kuzalishia umeme unaoilazimisha serikali kununua mitambo yake ya kufua umeme.
"Nchi yetu imebarikiwa kwa rasilimali mbalimbali, lakini hatuna mitambo, hivyo serikali iko kwenye mchakato wa kununua mitambo kwa ajili ya umeme wa dharura, si tu ya Dowans hata tukiipata mingine kutoka nje, lakini kama wataalamu wetu wakijiridhisha na mitambo hiyo (ya Dowans) serikali itafanya hivyo," alisema Ngeleja.
Alisema endapo serikali ikinunua mitambo yake itakuwa imepunguza gharama kubwa za uzalishaji wa umeme ukizingatia kuwa matumizi ya nishati hiyo yanaendelea kuongezeka siku hadi siku kutokana na kukua kwa miji.
"Umeme unaozalishwa kwa sasa ni megawati 1,200 tu, ambao umekuwa ukitumika katika maeneo ya mijini, lakini vijijini hakuna huduma hii ingawa nao wanaihitaji, kwa hiyo tunalazimika kununua mitambo mingine ya kusaidiana na hii iliyopo," alisema Waziri Ngeleja.
Wachambuzi wa mambo wanasema kwa kufanya hivyo serikali itakuwa inaendelea kuwawekea mwavuli waliohusika na mkataba wa Richmond ili wasipate hasara ya mitambo yao kubaki bila kazi yoyote
Kauli hiyo ya Ngeleja imekuja siku chache baada ya naibu wake, Adam Malima kukaririwa akisema kwamba endapo mgawo wa umeme ungendelea wangeweza kuruhusu Dowans iuzie Tanesco umeme.
Malima alisema hayo wakati akizungumzia mgawo wa umeme ambao uliikumba nchi baada ya mitambo mitatu ya Kampuni ya Sogas kuharibika.
Wakati huo huo, Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), limepanga kuondoa mitambo ya Dowans kwenye eneo lake Ubungo, jijini Dar es Salaam, huku kampuni hiyo imetunisha msuli ikisema haitafanya hivyo kwa kuwa haina mahali pa kuipeleka.
Hatua hiyo imekuja wakati tayari Tanesco imekwishasitisha malipo kwa Dowans ambayo ilirithi mkataba wa tata wa Richmond.
Meneja Mawasiliano wa Tanesco, Badra Masoud amelieleza gazeti hili kwamba shirika lake litaondoa mitambo hiyo muda wowote kuanzia sasa.
"Tupo mbioni kuondoa mitambo ya umeme ya Dowans,na sasa tunaandaa mikakati hiyo halafu tutatoa taarifa kamili wiki ijayo kuhusiana na uondoshwaji wake,"alisema Masoud.
Lakini tamko hilo limepata upinzani kutoka kwa Dowans wanaosema kuwa hakuna kitu kama hicho kwa kuwa hawana pa kuipeleka mitambo hiyo.
Afisa mwandamizi wa Dowans ambaye aliomba kutotajwa jina lake gazetini, alisema wao hawana pa kuipeleka mitambo hiyo, hivyo wataiacha katika eneo hilo mpaka watakapoamua wao.
"Kwa sasa hatuna mawazo ya kuondoa mitambo hiyo katika eneo la Tanesco, kwa sababu hatuna pa kuiweka wala pa kuipeleka, hivyo itabaki pale pale," alisema afisa huyo.
Akizungumzia suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alisema suala la kuhamisha mitambo hiyo liko mikononi mwa Tanesco.
Kulingana na mkataba huo uliositishwa, Tanesco ilikuwa inatakiwa kulipia gharama za kuhamisha mitambo hiyo kwenda popote atakapotaka mwekezaji baada ya muda wa mkataba huo kumalizika.