Bibianna
JF-Expert Member
- Jun 6, 2025
- 400
- 135
Akiongea mbele ya wanahabari mkuu wa mkoa wa Tanga amesea, Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi Afrika Mashariki (East African Crude Oil Pipeline – EACOP) kutoka Hoima, Uganda hadi Bandari ya Chongoleani, Tanga, ni moja ya miradi mikubwa ya kimkakati inayotekelezwa kwa ushirikiano wa kimataifa kati ya Tanzania, Uganda, na wawekezaji binafsi. Mradi huu una urefu wa kilomita 1,443, ambapo kilomita 205.91 ziko ndani ya Mkoa wa Tanga. Utekelezaji wa mradi kwa ujumla unagharimu takribani dola za Marekani bilioni 5 (sawa na takriban TZS trilioni 12.5), na Tanzania inanufaika kwa kuwa mwenyeji wa zaidi ya km 1,147 za bomba hilo. Mafuta yanayosafirishwa kupitia bomba hili ni wastani wa mapipa 216,000 kwa siku kutoka Uganda kuelekea soko la kimataifa kupitia Bandari ya Tanga.
Taarifa zaidi, Kwa sasa, utekelezaji wa mradi huu upande wa Tanzania umefikia asilimia 53, ukiambatana na ujenzi wa kituo cha kupokelea mafuta, matangi 4 makubwa ya kuhifadhi mafuta, miundombinu ya usimamizi, kambi za wafanyakazi, na barabara za kiutawala. Katika Mkoa wa Tanga, Serikali imetoa fidia kwa asilimia 98.7 ya wananchi waliopisha mradi, ambapo kati ya wananchi 1,580, tayari 1,560 wamelipwa jumla ya TZS bilioni 9.38. Zaidi ya hayo, nyumba 43 za makazi mbadala zimejengwa na kukabidhiwa kwa wananchi 40, ikiwa ni hatua ya kuhakikisha ustawi na haki za wakazi waliopisha mkuza wa bomba. Kwa ujumla, Tanzania imepata takriban TZS bilioni 181 kupitia ada, kodi na ushuru mbalimbali katika hatua za mwanzo tu za utekelezaji wa mradi huu.
Mradi huu unatarajiwa kutoa ajira zaidi ya 10,000 kwa Watanzania katika ngazi mbalimbali ajira za moja kwa moja kwenye ujenzi, huduma za usaidizi, usafirishaji, usambazaji wa vifaa, chakula, na usalama. Katika Mkoa wa Tanga pekee, ajira 810 zimetolewa kwenye eneo la Chongoleani, huku biashara ndogo ndogo zikiendelea kunawiri zikiwemo mama/baba lishe, bodaboda, wauzaji wa bidhaa ndogo, na huduma za kifedha. Mradi umeongeza mzunguko wa fedha katika jamii, kuimarisha vipato vya kaya, na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki za ardhi, uhifadhi wa mazingira na usalama wa kazi.
Faida kubwa ya mradi huu kwa Watanzania ni pamoja na mapato ya kitaifa, kupitia kodi, ushuru wa forodha, na tozo za usafirishaji, pamoja na uimarishaji wa miundombinu ya kitaifa ya mafuta kwa siku zijazo. Bandari ya Tanga inanufaika kwa kuwa lango kuu la mafuta ghafi kwa Afrika Mashariki, jambo linaloongeza hadhi ya kiuchumi ya mkoa huo. Uwepo wa bomba hili pia umefungua fursa za muda mrefu za uwekezaji, viwanda vya kuhifadhi mafuta, vituo vya usambazaji, na huduma za kiufundi kwa mafuta. Kwa ujumla, mradi huu ni kichocheo kikubwa cha uchumi wa Tanzania, ukiiweka nchi katika nafasi nzuri ya kuwa kitovu cha nishati na biashara ukanda wa Afrika Mashariki.