HADI SASA EMERY AMESHAIPATA ARSENAL YA MSIMU UJAO
LONDON, England
WIKIENDI iliyopita, timu ya Arsenal ilimaliza ziara yao ya mechi za kirafiki nchini Singapore kwa ushindi mnono wa mabao 5-1 dhidi ya PSG.
Arsenal iliibuka na ushindi huo mnono katika mchezo huo wa michuano ya ICC, siku chache baada ya kucheza mechi ya kwanza ya michuano hiyo dhidi ya Atletico Madrid na kupoteza kwa penalti 3-1.
Katika mechi hizo za kirafiki, Arsenal imetumia asilimia kubwa ya wachezaji wa kikosi chao cha kwanza ambao wameonekana kuzoea haraka mfumo wa kocha wao, Unai Emery.
Aina ya mfumo huo wa Emery umedhihirisha kwamba Arsenal itacheza soka kama ambalo PSG walikuwa wakicheza chini yake misimu kadhaa iliyopita.
Mhispania huyo anapendelea kutumia mfumo wa 4-2-3-1 hasa alipokuwa akifundisha klabu za Hispania na 4-3-3 alipokuwa PSG.
Alipohojiwa kwa mara ya kwanza baada ya kutua Arsenal, Emery alisema kwamba falsafa anayotegemea kuipandikiza katika timu hiyo ni kucheza soka la kukaba na kushambulia kwa kasi, kama inavyoonekana katika timu nyingi kwa sasa.
“Huwa napenda niwe na manufaa katika timu ambayo wachezaji na mashabiki wake wanataka kuona mafanikio,” alisema Emery.
“Wazo langu ni kutaka kuwa shujaa hapa, nimependa kuona kwamba historia ya Arsenal ni kucheza kwa kumiliki mpira.
“Napenda aina hiyo ya soka na kama hatuna mpira nataka timu nzima ikabe sana kuurudisha katika himaya yetu. Kuna vitu viwili muhimu sana, kwanza ni kumiliki mpira na kukaba pale unapoupoteza,” alisema Emery.
Hivi karibuni jijini London, katika mazoezi ya timu hiyo kuelekea msimu ujao, Emery alionekana akiwa ameshikilia nyaraka muhimu za mifumo yake na karatasi iliyokuwa juu ilionyesha aina fulani ya mfumo ambao huenda akautumia msimu ujao.
Akiwa PSG, zaidi ya kuwa alipenda kutumia mfumo wa 4-3-3, mara kadhaa pia alitumia mfumo wa 4-1-4-1 ambao uliiwezesha timu yake kuwa na watu wengi katika mashambulizi.
Lakini pia mfumo huo ulimsaidia kuwa na watu wengi kwenye safu ya kiungo pindi walipokuwa wakikaba.
Hata hivyo, haionekani kama Arsenal wataiga mfumo huo msimu ujao, lakini kuna uwezekano wakacheza katika aina ya mfumo huo; 4-1-2-2-1 au labda mfumo maarufu wa 4-3-3.
Kwenye safu ya ulinzi, Hector Bellerin na Nacho Monreal watacheza pembeni wakiwasaidia Sokratis Papastathopoulos na Shkodran Mustafi mbele ya kipa Bernd Leno.
Kiungo mkabaji aliyesajiliwa katika majira haya ya kiangazi kwa ada ya uhamisho wa pauni milioni 22, Lucas Torreira, atakuwa akivuruga mipango ya wapinzani (kama ilivyo mfumo wa 4-1-4-1).
Mbele ya Torreira, tayari Emery ana idadi nzuri ya wachezaji atakaowatumia hapo, Aaron Ramsey na Granit Xhaka kwa Mesut Ozil, Henrikh Mkhitaryan na hata Emile Smith Rowe pia.
Safu ya ushambuliaji ya Arsenal ambayo lazima itakuwa na watu watatu aidha Ozil au Mkhitaryan upande wa kulia, Pierre-Emerick Aubameyang kushoto na Alexandre Lacazette katikati.
Alipoulizwa kwanini alipenda kutumia mfumo huo akiwa PSG, Emery alisema: “Kwangu mfumo wa 4-1-4-1 una nguvu zaidi katika falsafa ya kukaba na kushambulia kwa kasi.
“4-4-2 mara nyingi ni kwa ajili ya kukaba nafasi, hauna matumizi makubwa ya nguvu lakini ni mgumu sana kupitika. Kama umezitazama timu za Marcelino (ikiwemo Valencia), Quique Sanchez Flores au Saint-Etienne tuliyocheza nayo msimu uliopita (Ligue 1), utanielewa vizuri.
“Sitaki kusema hatutatumia mfumo wa 4-4-2. Siupendelei sana mfumo huo lakini kama utaiongezea nguvu timu yangu, basi nitautumia bila kusita.
“Niliwahi kuutumia mara kadhaa nikiwa Sevilla. Ningemchezesha Ever Banega kama kiungo mchezeshaji na ningemsogeza juu acheze kama straika namba mbili bila mpira.”