Wabunge wamfunga mdomo Hosea
na Happiness Katabazi
Tanzania daima
UAMUZI wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kuamua kwa kauli moja, kuunda kamati teule ya Bunge kuchunguza utata katika mkataba wa kuzalisha umeme wa dharura wa Kampuni ya Richmond umemfunga mdomo Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU), Edward Hosea.
Ukweli kuhusu hali hiyo ulidhihirika jana, wakati gazeti hili lilipofanya juhudi za makusudi kupata kauli ya mkurugenzi huyo ambaye Mei mwaka huu, alilitangazia taifa kuwa, taaasisi anayoiongza ilikuwa imebaini kutokuwapo kwa dalili zozote za rushwa katika mkataba huo wa Richmond.
I have no comment, alisema Hosea na kukata simu mara tu mwandishi wa gazeti hili alipomuuliza maoni yake kuhusu uamuzi wa Bunge kuunda kamati teule ikiwa ni miezi sita tangu taasisi yake iisafishe Richmond, uamuzi ambao ulizusha manunguniko mengi kutoka kwa wananchi mbalimbali.
Wakati Hosea akikataa kutoa maoni yake kuhusu suala hilo, baadhi ya wasomi, viongozi wa vyama vya upinzani na wananchi wa kawaida wamepokea kwa hisia tofauti uamuzi huo wa Bunge kuunda kamati ya kuchunguza mkataba wa Richmond.
Mwenyekiti wa taifa wa TLP, Augustine Mrema, alisema Takukuru ni chombo kinacholinda wakubwa, kwa sababu wakati wapinzani na wananchi wakilalamika kuhusu mkataba huo, wao waliwaona wazushi.
Muhadhiri Mwandamizi kutoka Kitivo cha Sayansi ya Jamii na Siasa cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Mwesiga Baregu, alisema, uamuzi wa kuunda kamati ya kuchunguza mkataba wa Richmond umechelewa na kwamba umeonyesha wazi udhaifu wa serikali kutokana na ukinzani unaoonyeshwa na taasisi zake.
Profesa Baregu alisema mapema mwaka huu Takukuru ilitoa ripoti yake ya uchunguzi ambayo ilisema mkataba huo haukuwa na chembe wala harufu ya rushwa, hatua ambayo ilipingwa na Watanzania wengi.
Naye Muhadhiri Mwandamizi katika Kitivo cha Sheria Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Sengondo Mvungi, alihoji ni kwanini Bunge halikuchunguza mkataba wa Richmond wakati kashfa ya mkataba huo ilipoibuliwa mapema mwaka jana.
Binafsi uamuzi wa kuunda kamati ya kuchunguza mkataba huo, umetoa nafasi kwa wahusika wakuu wa kashfa hiyo kupika makabrasha ya kujitetea na sasa serikali imeona makabrasha hayo yametimia, ndiyo maana juzi wakaamua kuunda kamati ya kuchunguza
hii ni danganya toto, alisema Dk. Mvungi.
Dk. Mvungi alisema ripoti ya Takukuru haikuaminika kwa raia, ndiyo maana serikali na Bunge vimeamua kuunda kamati ya Bunge ili waweze kujisafisha vizuri.
Mimi ninahoji, kipindi chote hiki cha mwaka mmoja sasa kimepita, Bunge lilikuwa wapi? Na kama lilikuwa na nia njema na taifa hili, kwanini halikuunda kamati tangu mwaka jana? Ningependa jambo linapotokea lichunguzwe kwa wakati ule ule na si kutoa nafasi kwa wahusika kupika makabrasha ambayo yakija kuchunguzwa na kamati hizo tunaambiwa hakukuwa na rushwa, alisema Dk. Mvungi.
Mei mwaka huu Takukuru ilitoa taarifa ikionyesha kuwapo kwa uzembe katika kuingia kwa mkataba kati ya Kampuni ya Richmond kwa upande mmoja na Shirika la Ugavi wa Umeme (Tanesco) kwa upande mwingine.
Hata baada ya kukiri kwamba, kulikuwa na kile ilichokielezea kuwa uzembe katika kuipa mkataba kampuni hiyo, Takukuru wakati huo ikijulikana kama Takuru ilieleza bayana kwamba, kampuni hiyo haikuwa na uwezo wa kukidhi matakwa ya mkataba huo.
Ripoti hiyo ya Takukuru kwa upande mwingine ilibainisha kwamba, Richmond ilikwama katika mchakato wa kwanza wa kutafuta kampuni ya kuipa mkataba wa kuzalisha umeme wa dharura baada ya kuonekana kutokuwa na sifa.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baada ya kuona hivyo, Richmond ilitangaza kushirikiana na kampuni maarufu ya utengenezaji wa vifaa ya umeme ya Pratt & Whitney, ushirikiano ambao unadaiwa kuwa ndiyo uliowafanya wajumbe wa kamati maalumu iliyoundwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa, waipe mkataba kabla ya kubaini kuwa maamuzi hayo yalikuwa na makosa pia.
Pamoja na kukiri kuwapo kwa kile kilichoitwa uzembe na Takuru, ripoti hiyo ya maandishi ya kurasa 12 iliyosomwa na Hosea mwenyewe mbele ya wanahabari, iliwasafisha viongozi wa serikali kuwa hawakuhusika katika vitendo vya rushwa wakati wa mchakato mzima wa kutafuta kampuni ya kuzalisha umeme wa dharura.
Hata hivyo pamoja na ripoti hiyo kukiri kuwa Waziri Mkuu Lowassa ndiye aliyeamua kubatilisha uamuzi wa kutafuta kampuni kwa njia ya kutangaza zabuni kimataifa, bado ilishindwa kutoa tathmini iwapo uamuzi huo ulikuwa wa manufaa kwa taifa au la.
Uzembe pekee uliotajwa katika ripoti hiyo ni madai kwamba, serikali haikufanya juhudi za kutosha kuchunguza uwezo wa kampuni hiyo ambayo ilishindwa kukidhi matakwa ya kuzalisha umeme kwa wakati, kabla ya kuuza mkataba wake kwa Kampuni nyingine ya Dowans.
Hata hivyo, katika mazingira ambayo hakuweka wazi, aliutetea uzembe huo na kusema kuwa hauwezi kuhesabika kuwa ni kosa, kwa sababu haukusababisha hasara.