ULE mpango wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa kuwatuma viongozi wake waandamizi mikoani kwenda kukabili hali ya mambo baada ya ziara ya vyama vinne vya upinzani, unaanza rasmi leo.
Katika kukabili mapigo, CCM imeamua kuitumia bendi yake ya muziki wa dansi ya Tanzania One Theatre (TOT), ili kuvuta wananchi wengi mikoani kuhudhuria mikutano, ili waweze kupewa somo mbadala juu ya hoja zilizotolewa hivi karibuni na viongozi wa vyama vinne vya upinzani.
Kundi la makada waandamizi wa CCM, likiongozana na kundi la TOT, chini ya uongozi wa Muumini Mwinjuma, linatarajia kuondoka jijini kesho kuelekea Mbeya, kuanza kujibu hoja za wapinzani.
Makada wa CCM waliopewa jukumu la kujibu hoja za wapinzani ni pamoja na Katibu Mkuu wa CCM, Yusuph Makamba, Katibu Mwenezi na Itikadi wa CCM, Agrey Mwanri, Richard Tambwe Hizza, Salum Msabaha na Shaibu Akwilombe, ambao wanatarajia kuanza kuyeyusha sumu ya upinzani kuanzia kesho mkoani Mbeya, Songea na baadaye katika mikoa mingine ambayo muungano wa vyama vinne vya upinzani walipita kwa kutumia helkopta, wakimwaga sumu ambayo hadi leo inaisumbua CCM na serikali yake.
Vyanzo vyetu vya habari vilisema kuwa, mbali ya kutumia TOT ili kukusanya watu, CCM imepanga kutumia vizuri vyombo vya habari ili kuujulisha umma kile ambacho makada wake watakizungumza na kukifanya katika ziara hizo.
Kesho tunaondoka na TOT, tunaanzia Mbeya, kuna timu maalum kabisa iliyoteuliwa na CCM chini ya Makamba kuanza kujibu hoja ya Zitto (Kabwe, Mbunge wa Kigoma Kaskazini - CHADEMA) na zingine, na tunaanzia Mbeya, Songea na katika mikoa yote ambayo wapinzani wamepita kumwaga sumu ya Zitto, kilisema chanzo chetu cha habari kutoka ndani ya CCM.
Makamba, Tambwe na Akwilombe, wamemaliza ziara ya wiki nzima mkoani Shinyanga kujaribu kujibu pamoja na mambo mengine hoja ya Zitto katika mikutano ya hadhara, ambayo inadaiwa kuwa na idadi ndogo ya wananchi, hivyo kulazimika kuitumia TOT ambayo inamilikiwa na CCM.
Wakati CCM ikijipanga kukabiliana na hoja hiyo, serikali kwa upande wake imebuni mpango kama huo, kama sehemu ya kuweka rekodi sawa, baada ya viongozi wa upinzani, kuzunguka katika mikoa kadhaa nchini kuelezea udhaifu wa serikali.
Chini ya mpango huo, mawaziri watapangwa katika mikoa kadhaa, wakizunguka na kuzungumza na wananchi na viongozi wa CCM, kuelezea kile ambacho serikali imeshakifanya hadi hivi sasa katika kutekeleza ilani ya uchaguzi iliyokiweka chama hicho madarakani kupitia uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.
Habari zilizopatikana jana zilieleza kuwa, katika utekelezaji wa mpango huo, timu ya mawaziri wawili na naibu waziri mmoja, leo inaanza ziara ya siku saba mkoani Arusha, kwa madhumuni hayo.
Habari zilizopatikana kutoka mkoani humo zinaeleza kuwa, timu hiyo itaongozwa na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma), Hawa Ghasia.
Ghasia atawaongoza Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernad Membe pamoja na Naibu Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Dk. Emmanuel Nchimbi.
Habari za uhakika zinaeleza kuwa, pamoja na kuzungumza na wananchi na kuwaelezea mafanikio ya serikali ya awamu ya nne, pia watasikiliza na kupokea hoja, maoni na ushauri kutoka kwa viongozi wa chama na watendaji wa serikali kuhusu utekelezaji wa bajeti ya 2007/08.
Ziara hiyo inakuja wakati nchi ikiwa imetawaliwa na hoja mbili kuu, zilizotolewa na wapinzani kuhusu undeshaji wa nchi.
Hoja zote mbili ziliibuliwa bungeni na kusambaa kwa wananchi baada ya wapinzani kutoridhishwa na yaliyotokea bungeni.
Hoja moja iliibuliwa na Zitto kupitisa hoja yake binafsi, akihoji hatua ya Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, kusaini mkataba wa mradi wa mgodi wa Buzwagi akiwa nje ya nchi na kukiuka taratibu.
Zitto alihoji kwa nini waziri alifikia hatua hiyo licha ya kuwepo kwa agizo la Rais Jakaya Kikwete, lililotaka kutosainiwa kwa mkataba wowote wa madini, hadi hapo serikali itakapokamilisha kazi ya kudurusu mikataba iliyopo pamoja na sheria na sera zinazotawala sekta hiyo.
Hata hivyo, mbunge huyo alisimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge hadi Januari mwakani, kwa tuhuma za kusema uongo bungeni.
Hoja nyingine iliibuliwa na Dk. Willibrod Slaa (Karatu-CHADEMA), ambaye aliwasilisha kwa Spika, Samuel Sitta, nia yake ya kuleta hoja binafsi akihoji madai ya ubadhirifu Benki Kuu (BoT).
Hata hivyo, Dk. Slaa aliiondoa hoja hiyo na baada ya kumalizika kwa kikao cha Bunge la bajeti, vyama vinne vya upinzani; CHADEMA, TLP, NCCR-Mageruzi na CUF, vilifanya ziara katika mikoa kadhaa, kuwaelezea wananchi kuhusu masuala hayo.
Wakati wa kuhitimisha ziara hizo, katika viwanja vya Mwembe Yanga, Dar es Salaam, Dk. Slaa alitaja orodha ya viongzoi kadhaa wa serikali, akiwatuhumu kwa ufisadi na kuzusha mjadala mzito ambao unaendelea hadi hii leo.
Hatua hii ya serikali inakuja wakati viongozi kadhaa, waliotajwa katika orodha ya Dk. Slaa, wakiwa wamekanusha, na wengi wao kuonyesha nia ya kwenda mahakamani kumshtaki mbunge huyo pamoja na wengine wanaomsaidia kusambaza taarifa hizo.
Inaaminika kuwa, katika ziara hizo za mawaziri, hayo ndiyo yatakayotawala ingawa ziara hizo pia zitatoa fursa kwa watendaji wa serikali katika ngazi za chini kufahamu kwa undani mipango ya serikali na utekelezaji wake.
Habari zilizopatikana toka Arusha zinaeleza kuwa, viongozi hao wataanzia ziara hiyo wilayani Longindo na watazungukia wilaya zote za mkoa huo.