Wajumbe wa mkutano wa UNEA-6 waipongeza China kwa kupeleka nishati safi katika nchi zinazoendelea na kulinda mazingira ya dunia

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
1710916811488.png

Baada ya maandalizi ya miezi kadhaa na mikutano rasmi iliyofanyika kwa siku tano, kikao cha sita cha Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEA-6) kilichofanyika mjini Nairobi, Kenya, hatimaye kimefikia tamati. Kikao hicho kilichoanza tarehe 26 Februari hadi Machi 1, kilipitisha maazimio 15 yenye lengo la kushughulikia changamoto kubwa kadhaa za kimazingira duniani, ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa hewa na kuenea kwa jangwa.

Juu ya yote hayo, mkutano huo uliokuwa na kaulimbiu "hatua madhubuti, shirikishi na endelevu za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa viumbe hai na uchafuzi wa mazingira", ulionesha kuwa licha ya mgawanyiko mkubwa wa kijiografia, nchi bado zinaweza kufanya kazi pamoja linapokuja suala la mazingira.

Ikiwa mwanzilishi wa sera za uhifadhi wa rasilimali na ulinzi wa mazingira, China kwa sasa imepiga hatua kubwa katika maendeleo ya kijani yanayojikita katika kulinda mazingira. Na pia ikizingatiwa kuwa hili ni taifa kubwa zaidi linaloendelea duniani, lina kila sababu ya kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa ifikapo mwaka 2030.

Katika miaka ya hivi karibuni, China imekuwa kinara wa kutunza mazingira huku ikitoa mchango mkubwa katika masuala ya mabadiliko ya tabianchi, kuendeleza teknolojia ya nishati safi, wakati huohuo ikiwekeza pakubwa katika teknolojia na uzalishaji wa kisasa. Ikumbukwe kuwa katika mkutano wa kilele wa Umoja wa Mataifa wa COP28 uliofanyika mwezi Disemba mwaka 2023, China na zaidi ya nchi 120 zilitangaza lengo lao la kuongeza mara tatu uwezo wao wa uzalishaji wa nishati mbadala. Hatua hii inatarajiwa kuimarisha juhudi zaidi za kuendeleza na kufadhili miradi ya nishati safi ndani na nje ya China, na kuleta matokeo chanya kwa binadamu na dunia kwa ujumla.

Tukitolea mfano mwaka jana, nishati safi nchini China ilichangia asilimia 40 ya ukuaji wa uchumi wa nchi. Pia pato la taifa la China liliingiza yuan trilioni 11.4 (dola trilioni 1.6) zilizotokana na uchumi wa kijani, ikiashiria ongezeko la asilimia 30 kutoka mwaka wa nyuma yake. Ukuaji na uwekezaji huo ulichangiwa zaidi na nishati ya jua, utengenezaji wa paneli, magari ya umeme, na betri.

Juhudi hizi za kuhakikisha dunia inakuwa mahali salama pa kuishi, zimeifanya China kupongezwa sana na wataalamu mbalimbali waliohudhuria mkutano wa UNEA-6. Wataalamu hao wamesema mageuzi ya kuhamia kwenye magari yanayotumia nishati ya kijani, ambayo yanahimiza mfumo wa ikolojia na afya ya binadamu katika vituo vya mijini, yameharakishwa kutokana na upatikanaji mkubwa wa magari mapya ya nishati mpya yaliyotengenezwa na China. Pia imechukua nafasi kubwa katika kusaidia nchi zinazoendelea, ambazo nyingi zipo barani Afrika, kutumia magari ya umeme mijini na kupunguza kiwango cha hewa ya kaboni.

Mjumbe maalum wa hali ya hewa wa Kenya katika Ofisi ya Rais, Ali Mohamed alisema China ndio chanzo cha takriban magari yote ya umeme yanayosafiri katika barabara za Kenya, ikiisaidia Kenya katika harakati zake za mpito wa kuingia kwenye matumizi ya magari yasiyo na uchafuzi sambamba na kuongeza ubora wa hewa. Amesmea kwa kuwa China imejitokeza kama mshirika muhimu, sasa wanaagiza magari mapya ya nishati safi kutoka China na vipuri muhimu kama vile kuchaji betri.

Takwimu kutoka Shirikisho la Watengenezaji Magari wa China zinaonesha kuwa mwaka 2023 mauzo ya nje ya magari ya nishati safi ya China, yakiwemo yale yanayotumia umeme pekee na yale ya nishati mseto, yalipanda kwa asilimia 77.6 hadi zaidi ya milioni 1.2. Wataalamu wanaona teknolojia za China na ustadi wa hali ya juu wa uzalishaji wa vipuri muhimu kama vile betri, injini na kabini za teknolojia ya kisasa utadumu katika utengenezaji na usafirishaji wa magari ya umeme.
 
Back
Top Bottom