VIPEPEO WEUSI
SEASON 2 – FROM ZURICH WITH RULES
EPISODE 27
Majengo ya chuo kikuu cha Zurich yalikuwa yanapendeza haswa. Yalikuwa yanaakisi kwa uzuri kabisa umahiri wa stadi za uhandisi wa majengo wa karne ya kumi na tisa. Muda mchache uliopita nilikuwa nimemtumia Winnie ujumbe mfupi wa maandishi kumfahamisha kwamba nimeshafika hapo chuoni na alinijibu kwamba nimsubiri kwenye eneo la kuingilia kwenye Campus ya chuo ambayo lina sanamu maarufu sana la kutambulisha chuo hiki. Ilikuwa ni sanamu ya mwanamke aliyekaa juu ya jiwe huku akiwa amejitanda kwa shuka upande mmoja huku upande mwingine wa kifua ukiwa wazi titi moja likionekana. Mkono wa kulia kulikuwa na sanamu nyingine ya mwanaume ambaye naye pia alikuwa amekaa juu ya jiwe akiwa kifua wazi na huku amejifunika na shuka kuanzia kiunoni. Sanamu hizi zilikuwa zina umaridadi wa kuvutia mno kwa macho kutokana na kudhihirisha ustadi wa sanaa ya ufinyanzi ambayo ilitamalaki mno kwenye nchi za ulaya kwenye karne ya kumi na saba, kumi na nane na karne ya kumi na tisa.
Chini ya viambaza vyenye kushikilia sanamu hizi kulikuwa na maneno yaliyoandikwa kwa herufi kubwa katika lugha ya kijerumni, “UNIVERSITAT ZURICH ZENTRIUM” yakimaanisha “Zurich University Center” kwa umombo.
Nilisogea mpaka kwenye benchi dogo la kumpumzika ambalo lilikuwa karibu na sanamu hizi. Nilikuwa nimeomba kuonana na Winnie ili nimuhoji maswali kadhaa ambayo nilihisi kuwa yanaweza kunisaidia. Kwa siku mbili zilizopita nilikuwa nimekesha kuchambua nyaraka nilizonazo nikijaribu kutafuta uhusiano kati ya zile nyaraka nilizonazo na namba ya akaunti ya benki ambayo Winnie alikuwa amenipa. Mwanzoni nilihisi ingekuwa kazi rahisi tu lakini kwamuda wa siku mbili nilikuwa kama nazunguka mbuyu tu hivi. Waliondaa nyaraka zile walikuwa wamefanya kazi ya umaridadi sana kuficha uhalisia wa wahusika wake. Ni kama ambavyo nilikuwa nimemueleza Jimmy kuhusu ‘shell companies’. Kampuni moja ilifichwa ndani ya kampuni nyingine kivuli na nyingine ndani ya nyingine vivyo hivyo tena na tena.
“where is your bodyguard?”
Nilisikia mtu akinisemesha, nikainua shingo kutazama.Nilitabasamu, alikuwa ni Winnie akinitazama kwa kutabasamu na kisha kukaa pembeni yangu pale kwenye benchi.
“bodyguard?” nilimuuliza huku nikijifanya kana kwamba sikuelewa anaumuongelea nani.
“yes, your bodyguard... that serious guy!”
Nilimuelewa kabisa kwamba alikuwa anamuongelea Jiimy na alikuwa anaongea kwa utani tu.
“he is not my bodyguard… he is a friend!” nilimjibu huku natabasamu.