Huyo kwenu Ndiye Allaah, Rabb wenu. Hapana mwabudiwa wa haki ila Yeye Muumbaji wa kila kitu, basi mwabuduni Yeye Pekee. Naye Ni Mtegemewa wa kila kitu.
Kwa yakini zimekujieni hoja, ishara na dalili wazi kutoka kwa Rabb wenu. Atakayeona na kuzitambua, basi ni kwa faida yake mwenyewe, na atakayepofuka asizione basi hasara itamrudia mwenyewe, (sema) nami si msimamizi.
Na hivyo ndivyo Tunavyosarifu namna kwa namna Aayaat ili (makafiri) waseme: Umedurusu (kutoka kwa Watu wa Kitabu), na ili pia Tuibainishe kwa watu wenye kujua.
Na wala msiwatukane wale wanaowaomba asiyekuwa Allaah, wasije nao kumtukana Allaah kwa uadui bila ya ujuzi. Hivyo ndivyo Tumewapambia kila ummah amali zao, kisha kwa Rabb wao Pekee yatakuwa marejeo yao, Atawajulisha yale waliyokuwa wakiyatenda.
Na wakaapa kwa Allaah, viapo vyao thabiti vya nguvu, kwamba ikiwafikia Aayah (Muujiza) bila shaka wataiamini. Sema: Hakika Aayaat (Miujiza, Ishara) ziko kwa Allaah. Na kitu gani kitakutambulisheni kwamba zitakapokuja hawatoamini?
Na Tunazigeuza nyoyo zao na macho yao kama wasivyoiamini mara ya kwanza. Na Tunawaacha katika upindukaji mipaka ya kuasi kwao, wanatangatanga kwa upofu.
Na lau kama Sisi Tungeliwateremshia Malaika, na wao wakasemeshwa na wafu, na Tukawakusanyia kila kitu mbele yao, basi bado wasingeliamini ila Allaah Atake, lakini wengi wamo katika ujahili.
Na hivyo ndivyo Tulivyojaalia kwa kila Nabiy maadui mashaytwaan wa kibinaadam na kijini, wanadokezana wenyewe kwa wenyewe maneno ya kupambapamba na ya ghururi. Na lau Angetaka Rabb wako wasingeliyafanya hayo. Basi waachilie mbali na wanayoyatunga (ya uongo).
(Sema): Je, nitafute hakimu ghairi ya Allaah na hali Yeye Ndiye Aliyekuteremshieni Kitabu kilichofasiliwa waziwazi? Na wale Tuliowapa Kitabu (kabla) wanajua kwamba kimeteremshwa kutoka kwa Rabb wako kwa haki. Basi usijekuwa miongoni mwa wanaotia shaka.
JamiiForums uses cookies to help personalise content, tailor your experience and to keep you logged in if you register.
By continuing to use this site, you are consenting to our use of cookies.