Usife kwanza mpenzi wangu

Usife kwanza mpenzi wangu

USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE.5.

"Samahani Deo, naweza kupata namba zako za simu?" Levina akamwuliza.
"Simu?"
"Ndiyo!"
"Mimi sina, labda nikupe namba za nyumbani!"

"Hapana, nataka namba zako mwenyewe!"
"Sina."
"Kwanini?"
"Maisha Levina!"

"Ok! basi chukua zangu...ukimaliza kazi zako nipigie kwenye kibanda cha simu, nahitaji kuzungumza na wewe!" Levina akasema akiandika namba na kumkabidhi Deo akiambatanisha na noti ya elfu tano.
"Ahsante sana Levina, nitakupigia!"
"Usiache tafadhali, ni muhimu sana!"
"Sawa."
ANZA SASA KUISOMA....

DEO alibaki na maswali mengi sana kichwani mwake bila kuwa na majibu, bado kitu kikubwa kilichokuwa kinamsumbua ni kwamba, ni kweli hisia zake zilikuwa sawa kwamba Levina alikuwa anampenda au zilikuwa hisia zake mwenyewe?

Hakujua hakika!
Lilikuwa suala gumu sana kichwani mwake kupitishwa moja kwa moja kuwa Levina alikuwa anampenda, hata hivyo ndani ya moyo wake alijua wazi kuwa kabisa yeye alimpenda sana Levina.
"Nitampataje jamani huyu msichana? Nahisi kabisa moyo wangu unaniambia kuna kitu fulani, ni kweli nampenda sana Levina," akawaza Deo.

Siku nzima alishinda akiwa na mawazo, alitamani sana kumpigia simu Levina ili amsikilize alichokuwa akitaka kumwambia, lakini kwa sababu alikuwa na wateja wengi alishindwa kufanya hivyo, lakini kubwa zaidi kelele za pale sokoni zilimfanya ashindwe kumpigia kwakuwa alifahamu kwamba hawataweza kuelewana vyema!

Jioni alifunga biashara yake na kuanza kurudi zake nyumbani, kwakuwa alipewa pesa na Levina na pia alikuwa na haraka ya kuwahi kumpigia simu, akaona bora apande daladala.

Akachepuka kutoka sokoni Tandale hadi Manzese ya Agerntina, pale akapanda daladala iliyompeleka mpaka Magomeni ya Mwembechai, akashuka na kutafuta kibanda cha simu.
"Habari yako dada?" Deo akamsalimia mhudumu wa kibanda cha simu.
"Salama, karibu kaka'ngu!"

"Nahitaji kupiga simu."
"Sawa, naomba namba."
Deo akamtajia.

Yule dada akabonyeza zile namba kwenye simu, kisha akaweka saa yake ya kuhesabu muda tayari na kumpatia Deo simu.
"Hallow," sauti laini ya kike ilisikika upande wa pili, baada ya kupokelewa.

"Hallow, habari yako?"
"Nzuri, bila shaka ni Deo?"
"Umejuaje?"
"Kwanza sauti yako, lakini pia wengi wanaonipigia simu namba zao nimezi-save!"
"Niambie Levina."

"Poa!"
"Nimekupigia kama ulivyoniambia."
"Hujakosea kitu Deo, tena umefanya vizuri sana, maana nilikuwa nawaza namna ya kukupata kama usingenipigia."
"Sawa...sawa...nini kipya?" Deo akauliza.

Kimsingi hakuonekana kuwa na jambo lolote la kuzungumza zaidi ya kusubiri kumsikiliza Levina.
"Sikia Deo, kuna kitu cha muhimu sana nilitaka kuzungumza na wewe, lakini naona kama mazingira hayafanani kabisa."
"Kivipi?"

"Nahisi upo kwenye kelele sana, kiasi kwamba hata hutakuwa na usikilizaji na uelewa mzuri wa nitakayokuambia."
"Kwani unataka kuniambia nini?"

"Subiri Deo, usiwe na haraka kiasi hicho, huwezi kupata muda nikazungumza na wewe nje ya kazini kwako?"
"Kama lini?"
"Wewe off yako ni lini?"

"Jumapili, ingawa si mapumziko ya moja kwa moja!"
"Kivipi?"
"Huwa siendi sokoni, lakini kazi nyingine za nyumbani zinaendelea kama kawaida."
"Sasa?"

"Naweza kujaribu kutoka mara moja, lini unataka tuonane?"
"Itakuwa Jumapili, lakini kesho nitakuja tena kuzungumza na wewe zaidi!"
"Sawa."
"Haya usiku mwema mwaya Deo!"

"Ahsante,nawe pia ulale salama."
Wakakata simu zao.
Deo akalipa na kuanza kutembea kwa miguu akienda Mburahati, nyumbani kwa bosi wake. Ndani ya moyo wake alijihakikishia kumpenda Levina, lakini ufukara wake ulimfanya ashindwe kuelewa namna ambavyo angeweza kumfanya Levina awe wake.

Alifika nyumbani nusu baadaye, kwanza alikabidhi mahesabu, akaingia bafuni kuoga. Aliporudi alifikia mezani kupata chakula cha usiku, kabla ya kwenda jikoni kuanza kazi ya kufunga mifuko ya barafu kama ilivyo kawaida yake.

***
Kama ni mateka, alikuwa mateka asiye na hali, ambaye pamoja na kutekwa kwenyewe, alikuwa tayari kufanywa mateka. Levina alijishangaa sana jinsi alivyotokea kumpenda Deo.

Hakika hakuwa hadhi ya mwanaume wa kuwa naye, uwezo wao kifamilia, heshima waliyonayo wazazi wake ni kati ya mambo ambayo yalimchanganya sana na kumfanya ashindwe kuwa na maamuzi ya moja kwa moja ya nini cha kufanya kwa ajili ya Deo.

Pamoja na yote hayo, moyo wake ulikuwa na kitu kimoja tu...
Mapenzi!
Alimpenda sana Deo, lakini alikuwa na changamoto nyingi sana kichwani mwake. Kwanza aliwaza juu ya wazazi wake...hakujua kama wangekubaliana na wazo lake la kuolewa na Deo, kijana fukara ambaye hana mbele wala nyuma.

Hilo lilimchanganya sana kichwa chake, lakini alijipa moyo kwamba siku moja lazima Deo angekuwa mikononi mwake, yeye akiwa mama na Deo akiwa baba.

"Hilo nitahakikisha nalitimiza, maadamu nimempenda, hayo mengine nitajua baadaye!" Akawaza Levina.

***
"Mambo Deo," alikuwa ni Levina akimsalimia Deo, asubuhi ya siku iliyofuata alipokwenda sokoni.
"Poa, za nyumbani?"
"Salama."
"Kilo ngapi?"

"Hapana, leo sihitaji mchele, nimekuletea zawadi yako," akasema Levina akimkabidhi bahasha ya khaki.
Deo akapokea...
"Hiyo ni simu Deo, imebidi nikununulie ili kurahisha mawasiliano yetu."

"Mh! Ahsante sana jamani, lakini kwanini umeamua kufanya hivi?"
"Kwa sababu sisi ni marafiki, unajua tunatakiwa kudumisha urafiki wetu kwa kuwasiliana mara kwa mara, au wewe hupendi tukiwa marafiki?"
"Napenda sana, nashukuru sana!"

"Usijali, line imo humo humo ndani, tayari nimeshakuwekea vocha za elfu ishirini, zikiisha nijulishe nikuongeze nyingine."
"Ahsante sana," Deo akashukuru tena.

Haikuwa rahisi kuamini jambo hilo, zawadi ile kwa Deo ilikuwa zaidi ya zawadi,ule ulikuwa uthibitisho tosha kwamba Levina alikuwa anampenda.
Levina hakukaa muda mrefu sana, akaaga na kuondoka.

***
Siku zilivyozidi kwenda na kuwasiliana, mapenzi kati ya wawili hawa yalizidi kuchipuka kwa kasi, lakini si Deo wala Levina aliyekuwa tayari kueleza hisia zilizokuwa ndani ya moyo wake.

Wote waliishi na siri nzito za mapenzi ndani ya nafsi zao, lakini leo Levina amepata wazo la kufanya ili aweze kumnasa Deo. Alitumia kila njia kumuonesha kwamba anampenda na alichokuwa akikisubiri siku zote ni Deo kumtamkia kwamba anampenda, lakini hilo halikutokea.

Deo naye alishangazwa na jinsi Levina alivyopenda kuwa naye karibu na kumsaidia mambo mbalimbali, lakini aliogopa kumwambia kwamba anampenda, akihofia kupoteza urafiki wao ambao kwake ulikuwa na manufaa makubwa sana.

Levina ameshapata njia za kumsogeza karibu Deo ili iwe rahisi kwake kutamka kwamba anampenda. Alipanga mpango hatari, haukuwa mwingine zaidi ya kufanya jitihada mfanyakazi wao wa kiume wa nyumbani atimuliwe ili amfanyie Deo mipango ya kupata kazi nyumbani kwao.

Hapo ndipo angempata Deo kwa urahisi zaidi, maana angekuwa anammiliki. Hilo alijihakikishia kulifanya.

Je, nini kitatokea? Levina atafanikiwa kumpata Deo? Usikose kufuatilia ..........





USIFE KWANZA MPENZI WANGU.....EPISODE.6.-7

Levina ametekwa kimapenzi na Deo. Kilichopo akilini mwake ni kumfukuzisha kazi kijana wao wa nyumbani ili nafasi hiyo ichukuliwe na Deo, hapo angempata kirahisi zaidi.
Je, itawezekana? Endelea...

LEVINA alikuwa mateka wa mapenzi, alimpenda sana Deo na alitaka kuhakikikisha anakuwa wake wa maisha yake yote. Kitu pekee kilichokuwa kichwani mwake ilikuwa ni namna gani angeweza kumwondoa Rashid nyumbani kwao na kufanya jitihada za kumwingiza haraka sana Deo nyumbani, hapo lengo lake lingeweza kutimia bila mushkeli kabisa.

"Mimi ndiye ninayejua thamani ya penzi langu kwa Deo, najua kama nikimwambia ghafla anaweza kunichukia na kuniona malaya, lakini nikimsogeza kwanza nyumbani, naamini itakuwa vyema zaidi maana hataweza kupindua," akawaza kichwani mwake Levina.

"Lazima atakuwa wangu, lazima..." akazidi kujihakikishia ushindi.
Tayari alishakuwa na mbinu zake, mipango ilikuwa tayari kabisa, kilichobaki ilikuwa ni utekelezeji tu.

"Rashid hana ujanja wowote kwangu, mimi ndiye Levina na nitahakikisha namtoa nyumbani," akazidi kupanga mipango ya kummaliza.

****
Ilikuwa Jumapili asubuhi, nyumba ikiwa kimya kabisa, wazazi wa Levina, mdogo wao mdogo pamoja na house girl wote walikuwa wamekwenda kanisani, nyumbani wakiwa wamebaki Levina na Rashid, kijana wa kazi.

"Rashidiiiiiii...." Levina akaita akiwa amekaa sebuleni akiangalia runinga.
"Naam dada..."
"Njoo!"
"Nakuja."

Rashid akakimbia haraka hadi sebuleni alipokuwa akiitwa na Levina. Akamkuta akiwa ametulia kwenye sofa.
"Mambo kaka?" Rashid akasalimia.
"Poa,mzima?"
"Nipo poa, nina shida moja muhimu nataka unisaidie."
"Nini?"

"Naomba uniazime simu yako mara moja, maana yangu imekufa display!"
"Haina pesa lakini."
"Usijali, ninayo nitaongeza, kuna mtu nataka kuchat naye kidogo!"
"Hii hapa."

"Poa basi, nikimaliza nitakushtua, unafanya nini nje?"
"Nakatia fensi, si unajua tena dingi akija akikuta sijakamilisha anaweza kuniletea muziki?"
"Poa bwana endelea."

Levina akachukua ile simu na kuiangalia kwa dharau...
"Nakumaliza na simu yako hii hii," akawaza kichwani mwake Levina.

Zoezi kubwa lililokuwa likiendelea ni kutuma meseji kutoka kwenye simu ya Rashid kwenda kwenye simu yake, huku akijibizana naye. Alipomaliza, akafuta meseji zote zilizoingia na kutoka kwenye simu ya Rashid, ili kuondoa ushahidi.

Baadaye akamrudishia Rashid simu yake.
"Umefanikiwa kuwasiliana naye?" Rashid akamwuliza Levina.
"Siyo kuwasiliana naye, ni kuwasiliana nao?"
"Kwani walikuwa wangapi?"
"Nilikuwa nachat na marafiki zangu kibao, si mmoja kama unavyodhani."

"Poa, mi nipo nje."
"Sawa kaka Rashid."
Kwa alivyokuwa akizungumza, ni kama muungwana mwenye roho nzuri na upendo, lakini kikubwa alikuwa amepanga kumfukuzisha kazi Rashid.

Ni kijana aliyefanya kazi kwao kwa muda mrefu sana, akiaminiwa sana na wazazi wake, isingekuwa rahisi kumtoa nyumbani kwao kienyeji kutokana na utendaji wake kuwa bora kwa miaka mitatu aliyoishi kwa uaminifu mkubwa katika nyumba ile.

****
"Samahani kwa kukusumbua Deo, naamini wewe ni rafiki yangu, ni kweli?" Levina alimwambia Deo, jioni moja alipomsubiri Magomeni Mwembechai, ambapo Deo alikuwa anarudi nyumbani Mburahati.
"Naamini hivyo, sisi ni marafiki."

"Kweli?"
"Naamini hivyo au?"
"Hata mimi pia, lakini nilitaka kupata uhakika kutoka kwako."
"Sisi ni marafiki Levina."
"Bila shaka huwezi kunificha chochote katika maisha yako."
"Hilo halina ubishi."

"Ulisema unaitwa Deo, ukoo wako ni nani na wewe ni kabila gani?"
"Mh! Jamani, kwanini?"
"Nataka tu, kujua."
"Niite Deogratius Mgana, ni mwenyeji wa Kiomboi, Singida, nikimaanisha kwamba mimi ni Mnyiramba."

"Ok! nimefurahi sana kukufahamu kwa uzuri Deo, mimi ni Levina Masamu, ni Mchaga wa Old Moshi."
"Oh! Ahsante sana kukufahamu zaidi, lakini kwanini umeniuliza yote hayo?"

"Nina maana yangu, utaijua baadaye kidogo. Samahani, mshahara wako ni shilingi ngapi kwa mwezi?"
"Nalipwa elfu arobaini na tano."
"Jamani zinakutosha kweli?"
"Nitafanyaje Levina, maisha..."
"Elimu yako ikoje?"

"Mimi?"
"Ndiyo!"
"Darasa la saba tu, nilifaulu lakini wazazi wangu wakakosa fedha za kuniendeleza."

"Usijali, vipi utakuwa tayari nikikutafutia mahali pengine utakapolipwa fedha nyingi zaidi?"
"Ndiyo, hata sasa hivi."

"Kweli?"
"Ndiyo!"
Levina akafurahi sana, mpango wake ulikuwa unanukia kukamilika.

Itaendelea.......



 
USIFE KWANZA MPENZI WANGU.....EPISODE.8.

Mpango wa kumtoa Rashid nyumbani kwao unaendelea, nia hasa ya Levina ni kumwingiza Deo nyumbani kwao.
Lakini moyoni aliumia sana, maana machozi ya Rashid yalikuwa yanamuuma sana!
Ni kweli alimsingizia. Nini kitatokea? Endelea kuisoma...

LEVINA aliumia ndani kwa ndani, alikiri kabisa kwamba Rashid hakuwa anahusika na chochote katika mchezo ule. Kitu pekee kilichomsukuma kufanya vile ni mapenzi yake ya dhati pekee, hakuwa na kitu kingine ndani yake zaidi ya hivyo.

Tangu Rashid alipoondoka kwenda chumbani kwake kukusanya mizigo yake, alijisikia mkosaji sana.
Mwenye roho mbaya sana!
Alijihisi kama si binadamu kabisa!
Sifa zote mbaya akajipa yeye!

Mama yake aliweza kugundua tofauti aliyokuwa nayo mwanaye, akaona njia pekee ya kugundua kilichokuwa kikimtatiza mwanaye ni kumuuliza tu!
"Nini tatizo tena mwanangu?"
Levina akabaki kimya!
"Levina..." mama yake akaita.

"Abee..." Levina akaitikia kwa kushtuka kidogo.
Ni kama alikuwa amegutuka kutoka katika usingizi mzito, lakini ukweli haukuwa huo. Levina alikuwa na mawazo ya usaliti. Kusema uongo na kumnyanyasa Rashid kwa sababu ya mapenzi.
"Una nini mama?!!"

"Inaniuma sana mama..." Levina akasema machozi yakidondoka machoni mwake, ni kama alikuwa akiumizwa na meseji za Rashid, lakini ukweli halisi haukuwa huo.
Ndani ya nafsi yake alikuwa akiumizwa na kitendo cha kumsingizia na si kufanyiwa kama ambavyo alitaka kutengeneza.

"Lakini ndiyo nimemtimua hivyo."
"Amekosa adabu kabisa, yaani siku zote hizo naishi naye kama kaka yangu halafu anakuja kuniambia maneno machafu kiasi hicho? Hana adabu kabisa..." akasema Levina lakini kichwani mwake kukiwa na kitu kingine.

Moyoni mwake alihifadhi kitu tofauti kabisa, alikuwa na siri nzito sana, ambayo hakutakiwa kumwambia mtu yeyote, ilikuwa ni siri ambayo alitakiwa kuijua yeye na moyo wake pekee.

"Potelea mbali, kama ni kazi anaweza kupata mahali pengine, lakini nitapata wapi mwanaume kama Deo, lazima nifanye hivi, sina namna!" Akazidi kuwaza kichani mwake.

"Usijali mwanangu, nimeshamtimua huyu mwanaharamu. Hutakiwi kuwa na mawazo mwanangu na mimi mama yako nipo. Tena subiri...wewe Rashid, unasubiri nini? Kwani una mizigo gani mingi ya kuchukua muda mrefu kiasi hicho?" Akasema mama Levina akisimama kumfuata chumbani kwake.

Mama Levina alikuwa amevimba kwa hasira, akafika chumbani kwa Rashid na kumwita kwa sauti kubwa...
"Si naongea na wewe, hebu toka haraka nyumbani kwangu."

"Natoka mama,lakini siku moja utakuja kugundua ukweli, siwezi kufanya mambo ya ujinga kiasi hicho mama, lakini kwakuwa wewe umeamua kumuamini Levina sawa!"

"Tena funga domo lako kabisa wewe mwanaharamu, inaonekana unataka kunigombanisha na mwanangu, unataka kuniambia mwanangu anaongopa?"
"Ndiyo mama!"
"Kwa lipi hasa?"

"Sijui mama, lakini ukichunguza utagundua ukweli."
"Tena ishia hapo hapo kuniita mama, anayeruhusiwa kuniita mama ni yule anayeheshimu wanangu na kuwachukulia kama dada zake, si wewe mpumbavu!"
"Hapana mama!"

"We' mwendawazimu, sina muda wa kubishana zaidi na wewe. Paki vitu vyako, nakwenda kukuchukulia pesa zako uondoke!"
Rashid akabaki kimya.
Mama Levina akaenda ndani haraka na kuchukua fedha alizokuwa akidaiwa na Rashid kisha akarudi na kumkuta tayari ameshajiandaa.

"Chukua pesa zako, tena nimekuongezea na elfu thelathini zikusaidie, ondoka kwangu!"
"Ahsante mama, lakini Mungu mwenyewe ndiye anayejua ukweli wa haya yote!"

"Hayo mahubiri yako huwa nakutana nayo kanisani, sasa sioni kama hata hapa nyumbani kwangu panafaa kuhubiriwa!"
"Siyo mahubiri mama, ni ukweli kabisa kutoka ndani ya moyo wangu!"
"Ukweli wa nini?"

"Sijamtumia zile meseji mimi mama."
"Hivi wewe una akili? Zile namba ni zako au za nani?"
"Zangu."

"Sasa kama ni zako, kwanini unaruka?"
"Unajua mama...juzi..." mama Levina hakumpa nafasi ya kumalizia utetezi wake.

"Hebu toka kwangu haraka tafadhali, sidhani kama bado nina nafasi ya kuendelea kuusikiliza utumbo wako, ondoka tafadhali!"
Rashid alikuwa anataka kumweleza mama Levina kwamba kuna siku alimuazima simu yake, lakini hakupewa nafasi hiyo.

Rashid akaondoka analia, mama Levina akiendelea kufoka huku akirusha mikono. Alikuwa amekasirika sana. Pamoja na utendaji kazi wake kuwa mzuri kwa muda mrefu aliokuwa akikaa naye, lakini siku aliyasahau yote hayo kwa meseji iliyoonekana kutumiwa mwanaye.

****
Mto wote ulikuwa umelowana kwa machozi, Levina alikuwa na uchungu sana ndani ya moyo wake. Usiku huo ulikuwa mgumu sana kwake, aliteswa na watu mawili; DEO NA RASHID!

Alifanya dhambi ya kumsingizia Rashid kwamba amemtongoza na akafukuzwa kazi. Hilo lilimuuma, lakini lingepoa kama kweli Deo angekubali kuwa naye. Lakini aliteseka sana, akiwa hana uhakika kama kweli Deo atamkubalia.

Tabu yote ya nini? Usiku ule ule, akachukua simu na kumpigia Deo.
Je, nini kitatokea?





USIFE KWANZA MPENZI WANGU.......EPISODE.9.

Zoezi la kwanza la Rashid kuondoka nyumbani kwao, linakamilika. Zoezi lililokuwa linafuata kwa Levina ilikuwa ni kuhakikisha Deo anaingia nyumbani kwao. Pamoja na mafanikio yale makubwa, moyo wake haukuwa na amani kabisa kutokana na fitna alizomfanyia Rashid.

Hata hivyo, kikubwa zaidi kwake ilikuwa ni Deo kukubali kwenda nyumbani kwao na baadaye alitamani sana Deo mpenzi wake wa maisha yake yote. Hiyo ndiyo ilikuwa ndoto yake kubwa. Akiwa katika lindi la mawazo, akaamua kumpigia simu Deo.
Je, nini kitaendelea? Endelea kuisoma...

LEVINA aliumia sana ndani ya moyo wake, akaona ni vyema kama angenyanyua simu yake na kumpigia Deo. Alitaka kujua hisia zake zina nini juu yake. Hakutaka kufanya mambo kwa hasara!

Akachukua simu na kwenda moja kwa moja kwenye Menu, akabonyeza Contacts kisha akaanza kutafuta jina la Deo, alipolipata akabonyeza kwenye kitufe cha kijani ili kuruhusu upigwaji simu.

Punde tu, sauti ya Deo ikasikika...
"Vipi Levina mbona usiku sana?"
"Nina matatizo Deo!"
"Matatizo gani?"
"Naomba nikuulize kwanza maswali yangu!"

"Uliza."
"Mimi ni rafiki yako?"
"Ndiyo!"
"Unaniamini?"
"Ndiyo!"

"Unanipenda?" Levina akauliza kwa sauti ya taratibu, lakini iliyochanganyikana na kilio cha kwikwi kwa mbali.
Deo hakupata shida sana kugundua kwamba Levina alikuwa analia. Pengine hilo si neno sana, lakini kwanini amemuuliza kama anampenda? Hata kama anampenda, ndiyo alie?
Kwanini analia?

Hakujua!
Kimya cha muda mfupi kikapita, Deo akiwa ametulia kwenye simu na Levina akiendeleza kilio chake cha chini chini huku kwikwi zikisikika kwa mbali.
"Levina," baadaye Deo akaita.
"Bee!"
"Nini tatizo?"

"Si tatizo, napenda kusikia ukinijibu!"
"Uliuliza nini?"
"Nilikuuliza kama unanipenda?"
"Ni kweli nakupenda Levina, wewe ni rafiki yangu na umekuwa msaada kwangu kwa kila kitu, lazima nieleze ukweli, nakupenda, kwani wewe hunipendi?"
"Swali gani hilo Deo?"

"Samahani kama nimekuudhi, lakini ndani ya moyo wangu natambua kwamba tunapendana, mimi nafahamu hilo, naamini hata wewe ni kama mimi."
"Kweli."
"Lakini ni kwanini unalia?"
"Silii ila sauti yangu leo haipo vizuri sana."
"Unakohoa?"

"Ndiyo!"
"Pole sana."
"Ahsante."
"Nina swali lingine kwako Deo!"
"Uliza."

"Lakini kabla sijauliza, nataka unihakikishie kwamba utajibu ukweli wako wote na hutanidanganya jambo lolote."
"Hilo kabla hujauliza, naamini unatambua kabisa jinsi nilivyo mkweli."
"Umewahi kuona mtu akilia?"

"Mara nyingi sana, hata leo kuna mtoto nimemuona akilia."
"Siyo mtoto, nazungumzia mtu mzima."
"Ndiyo, kwenye misiba huwa wanalia sana, nimeshaona mara nyingi, kwani kuna nini, mbona unaniacha na maswali?"
"Lakini vipi kama ukiona mtu mzima analia?"
"Nitajisikia vibaya sana."

"Umeshawahi kumuona mtu akilia kwa ajili yako?"
"Hapana."
"Utapenda siku moja hilo likitokea?"
"Hapana."
"Basi usiku mwema."

"Kwanini?"
"Nimekutakia usiku mwema Deo."
"Lakini sijakuelewa kabisa. Mbona leo maneno yako yamekuwa magumu sana kuingia kichwani mwangu? Kwani kuna nini kimetokea?"
"Hakuna...nilitaka kujua tu unachowaza kichwani mwako!"
"Nikuambie kitu Levina?"

"Nakusikiliza."
"Nitalala nikiwa na mawazo sana leo. Maneno yako yananiacha na maswali mengi yasiyo na majibu kabisa. Mpaka sasa sijajua maana ya kauli yako."
"Siku moja utajua...."
"Usiku mwema."

"Na wewe pia!"
Wakakata simu zao.
Deo akapata wakati mgumu sana wa kuwaza mambo kichwani mwake bila kupata majibu. Alikuwa katika wakati mgumu sana wa kujaribu kuwaza kilicho kichwani mwa Levina kitu ambacho kwa hakika kisingekuwa rahisi kuelewa.

"Sijajua anamaanisha nini? Anyway itajulikana baadaye!" Akawaza na kujifunika shuka kisha akaishilia usingizini.

****
Siku nzima ilikuwa kama wiki kwa Levina, kichwa kilikuwa kinamuuma mawazo mengi yakimsumbua. Hakuwa na kitu kingine kilichomtesa zaidi ya Deo, aliendelea kuwaza namna ya kumsogeza karibu yake.

"Nampenda sana Deo, ni kweli kwamba nampenda sana, lazima nitumie kila njia, nihakikishe anakuwa wangu. Hilo lazima nitalifanya," akawaza Levina akiwa kazini kwake Posta.

Levina baada ya kumaliza kidato cha sita, wazazi wake walimkabidhi moja ya maduka yao yaliyopo mjini, Levina alipewa duka la simu lililopo Posta Mpya jijini Dar es Salaam.
Alichojua yeye ni kwamba alikuwa msimamizi wa duka lile kubwa, lakini wazazi wake walipanga kumwachia moja kwa moja kama lake. Walimfanya msimamizi mkuu, akishughulikia kila kitu, mpaka mishahara ya wafanyakazi, walichokifanya wao ni kukagua mahesabu ya fedha zinazoingia na kutoka benki.

Mali ikipungua dukani, ilikuwa ni kazi ya Levina kuagiza au kwenda nje ya nchi kununua mzigo mwingine wa dukani.
Akionekana mwenye mawazo tele kichwani mwake, simu yake ikatoa mlio wa ujumbe mfupi wa maneno, mara moja akaufungua na kusoma.

Ilikuwa meseji kutoka kwa mama yake, alijikuta anarudia kusoma zaidi ya mara mbili ile meseji akiwa haamini kabisa alichokiona.
Ujumbe ule ulisomeka; "Levina ni wiki moja sasa tangu Rashid ameondoka, hatuna house boy, sasa kama unaweza ni vizuri ukashughulikia hilo, tukapata mtu mwingine haraka."
Levina akatabasamu.

Ilikuwa nafasi nzuri kwake ya kumwingiza Deo nyumbani kwao.
"Yes, mambo yanakwenda kama nilivyopanga, afadhali," akasema kwa sauti ya taratibu akiachia tabasamu.

***
Jioni Levina aliwahi sana kurudi nyumbani, akamkuta mama yake sebuleni, baada ya kumsalimia akamwambia...
"Mama nilipata sms yako ya mchana, nimeanza kuifanyia kazi, ndani ya siku tatu tutapata mtu mwingine."

"Oh! Usijali binti yangu, ameshapatikana kijana mwingine kutoka Bagamoyo, atakuja kuanza kazi kesho."
Uso wa Levina ukasawagika kwa huzuni.

Itaendelea,..........







USIFE KWANZA MPENZI WANGU,.....EPISODE.10.

Jioni Levina aliwahi sana kurudi nyumbani, akamkuta mama yake sebuleni, baada ya kumsalimia akamwambia...
"Mama nilipata sms yako ya mchana, nimeanza kuifanyia kazi, ndani ya siku tatu tutapata mtu mwingine."

"Oh! Usijali binti yangu, ameshapatikana kijana mwingine kutoka Bagamoyo, atakuja kuanza kazi kesho."
Uso wa Levina ukasawagika kwa huzuni.
Sasa endelea...

KWA sekunde kumi na tano, Levina alikuwa ameganda akimwangalia mama yake, ni kama hakusikia vyema maneno yale, hata kama aliyasikia vizuri lakini yalionekana kuwa magumu sana kupenyeza kwenye ngoma za masikio yake.

Anamwangalia mama yake kwa macho yanayozungumza jambo fulani, ingawa haijulikani moja kwa moja kuwa anazungumza nini. Mama yake aliweza kugundua tofauti aliyonayo mwanaye haraka sana.

"Vipi Levina mwanangu, mbona kama hujafurahia?"
"Siyo hivyo mama?"
"Bali nini tena?"
"Nimeshangaa, maana tayari nilishaanza taratibu za kumpata huyo mtu."

"Kwani umeshampata?"
"Kuna dada mmoja ameniambia kwamba jioni ya leo atakwenda kuzungumza naye. Yupo kaka mmoja amesema anaishi Mburahati, kwahiyo akionana naye atajaribu kumweleza."
"Ni mfanyakazi au yupo tu, nyumbani?"

"Anafanya kazi!"
"Sasa atawezaje kutoka?"
"Kasema atamshawishi, maana hata pale halipwi mshahara mkubwa, lakini pia atamwambia mazingira ya kazi ni mazuri."
"Sawa, ngoja tuone."

"Na huyo mwingine uliyesema?"
"Huyo kila kitu kipo tayari, nimeshafanya naye mawasiliano na tumekubaliana aje kesho!"
"Sasa itakuwaje? Maana sitaki kuonekana mwongo kwa rafiki yangu."

"Kesho tutapata majibu kamili, kama akija huyo wa Bagamoyo sawa, asipokuja basi utanijulisha makubaliano ya huyo kijana mwingine atakayezungumza na rafiki yako leo usiku."
"Sawa mama, mimi nipo ndani," akasema Levina.
"Sawa mama."

Levina akajikongoja mpaka ndani akionekana kuwa na uchangamfu kidogo, bado alikuwa akiomba sana huyo kijana wa Bagamoyo asitokee ili Deo apate nafasi ya kuingia kwao.
"Itawezekana tu, maadamu moyo wangu umempenda, naamini itakuwa hivyo," akawaza Levina.

Baada ya kubadili nguo, aliingia bafuni kuoga, alipotoka alionekana kuwa na nguvu kidogo, akachukua simu na kumpigia Deo.
"Uko wapi?"
"Nipo njiani naelekea nyumbani."

"Umefika wapi sasa hivi?"
"Ndiyo nakaribia kushuka Mwembechai!"
"Ok! ukishuka naomba unisubiri!"
"Kwani wewe uko wapi?"
"Nipo home, lakini natoka sasa hivi nachukua taxi nakuja."

"Basi jitahidi ufanye haraka!"
"Usijali, sina muda mrefu sana nitakuwa hapo."
"Poa."
Levina akabadili nguo haraka na kutoka. Alipopita sebuleni alimkuta mama yake akiwa amekaa pale pale!

"Haya wapi tena?"
"Natoka kidogo mama!"
"Ila saa hizi ni usiku na baba yako hapendi kabisa utoke usiku."
"Mama siendi mbali, nakwenda hapo Mwembechai mara moja."
"Unatoka na gari?"

"Hapana, sitaki baba ajue nimeenda mbali kama akirudi mapema, ni bora alione gari atajua nipo jirani!"
"Kumbe hutakuwa jirani siyo?"
"Mama...!!! Mwembechai si mbali, lakini ni mbali pia mama. Kwa baba kule ni mbali!"

Mama Levina akacheka.
"Uwahi kurudi," akasema mama Levina akiendelea kutabasamu.
"Nakuahidi mama."
Levina akaondoka zake.

***
Levina alifurahi sana kukutana na Deo, moyo wake ulikuwa ukisisimka sana kila alipokutanisha macho yake na Deogratius.
Alikuwa mwanaume pekee ambaye aliweza kuutetemesha moyo wake.
"Nina habari njema Deo!"
"Juu ya nini?"

"Unakumbuka mara ya mwisho nilizungumza nini na wewe?"
"Ndiyo, nakumbuka vizuri sana."
"Ilikuwa ni nini?"
"Kuhusu kazi nyingine!"
"Halafu?"
"Kusoma."

"Safi sana, kumbe unakumbuka vizuri sana, sasa tunaanza na kimoja baada ya kingine. Kama nilivyokuambia sisi ni marafiki na nitakuwa tayari kutumia kila njia nihakikishe nakufurahisha!"
"Nimefurahi kusikia hivyo."
"Nimekupatia kazi, tena nyumbani kwetu kabisa."

"Unasema kweli?" Deo akauliza akiwa haamini kabisa alichoambiwa na Levina.
"Kwanini isiwe kweli?" Levina akauliza akitabasamu.

Tabasamu lililomchoma Deo moyoni, kwa mara ya kwanza alikiri kumuona Levina akiwa ameachia tabasamu zuri zaidi kuliko siku zote!
Uzuri wa Levina ukawa hadharani!
Je, nini kitaendelea......





USIFE KWANZA MPENZI WANGU .....EPISODE..11

Pamoja na taarifa kutoka kwa mama yake kwamba alishapata kijana mwingine wa kazi, bado Levina hakukata tamaa kuhusu Deo. Usiku ule ule akatoka na kwenda kukutana naye Mwembechai.

Levina akamweleza kwamba amempatia kazi nyumbani kwao, Deo akafurahi sana. Furaha iliyosababisha Levina aachie tabasamu mwanana! Uzuri wake ukawa hadharani!
Nini kitatokea? Endelea kuisoma...

DEOGRATIUS akagundua kitu kipya kabisa kutoka kwa Levina, aligundua kwamba alikuwa msichana mzuri kupindukia! Tabasamu lake lililoacha sehemu kubwa ya meno yake nje, lilisababisha aone vijishimo vidogo mashavuni mwake na hivyo kuzidisha urembo wake.

Alihisi moyo wake kama umepigwa na shoti ya umeme, alikuwa amesimama mbele ya mwanamke mrembo sana tofauti na matarajio yake. Levina alikuwa mzuri zaidi ya alivyofikiria.
Kwanini anamsaidia sana?

Kwanini anakuwa naye karibu sana? Hayo yaliendelea kuwa maswali ambayo hayakuwa na majibu ya moja kwa moja kichwani mwake. Alibaki ameganda akimwangalia Levina ambaye sasa aliamua kucheka kabisa. Furaha ya Levina ilikuwa ni kuona jinsi Deo anavyomkubali yeye.

Hakujali umasikini wake, alichojua yeye ni mapenzi tu. Moyo wake ulianguka kwake, alitamani sana awe mpenzi wake wa dhati ndani ya moyo wake.

"Deo!" Levina akaita kwa sauti tamu sana.
"Naam!"
"Vipi?"
"Poa."

Levina akacheka.
"Mbona unanicheka?"
"Sijakucheka Deo!"
"Bali!"

"Nimecheka. Unajua kuna tofauti kubwa sana kati ya kucheka na kumcheka mtu. Mimi nimecheka, sijakucheka. Umeona tofauti hiyo?"
"Haya mama wa Kiswahili, siwezi kushindana na wewe, hapo umenishinda."
"Enhee stori nyingine?"

"Sina!"
"Basi poa, acha mimi nirudi zangu home, si unajua tena dingi hajaingia, sasa akija na kunikuta sijafika nyumbani mpaka saa hizi haitakuwa sawa!"

"Sawa basi. Enhee niambie, naanza lini kazi?"
"Una hamu eeh!"

"Sasa kumbe ningefanyaje?"
"Subiri kidogo, mpaka kesho nitakupa jibu kamili la lini utaanza kazi rasmi."

"Sawa."
"Usiku mwema."
"Nawe pia!"

Deo akaondoka, Levina akaendelea kumkazia macho mpaka alipoondoka. Baada ya hapo akavuka upande wa pili, akachukua taxi nyingine na kurudi zake nyumbani. Kwa bahati nzuri, baba yake alikuwa bado hajafika nyumbani.
"Una bahati, baba yako hajafika!"

"Acha tu mama!"
"Enhee vipi, mambo yanaendaje?"
"Huyo kijana yupo mama, hata kesho anaweza kuja!"

"Sawa basi, lakini naomba tusubiri hadi kesho, kama yule wa Bagamoyo hatakuja basi atakuja huyo, unajua tayari nilishamuahidi na huyo mtu alimuhangaikia sana!"
"Sawa mama," Levina akasema kwa sauti ya chini lakini ndani ya moyo wake akiumia sana.

Alitamani sana huyo kijana asitokee ili Deo wake aweze kwenda nyumbani kwao. Hiyo ilikuwa dua yake kubwa.
"Mimi naingia chumbani mama."

"Sawa, bado nipo hapa naendelea kuangalia taarifa ya habari."
Muda mfupi baada ya Levina kuingia chumbani kwake, simu ya Mama yake ikaita. Namba hakuzijua, lakini mara moja akapokea!
"Nani mwenzangu?" Ndiyo neno la kwanza mama Levina kutamka mara baada ya kupokea simu.

"Mama Happy wa Bagamoyo...samahani mama Levina, nimekupigia na namba ya kibandani, simu yangu haina chaji!"
"Usijali, vipi za huko?"
"Bwana wangu, si salama."

"Kuna nini tena?"
"Yule kijana amefiwa na mama yake, kwahiyo anatakiwa kwenda kwao Morogoro kesho, kurudi ni baada ya wiki mbili!"
"Duh!"

"Ndiyo mwenzangu, matatizo yamemfika kijana wa watu, kwa jinsi alivyokuwa na hamu na hiyo kazi, yaani amechanganyikiwa kabisa!"
"Poleni mwaya, umpe pole na yeye, hakuna jinsi, maana nilikuwa na shida ya haraka sana na kijana wa kazi, sasa nalazimika kutafuta mwingine."

"Hakuna shida, haikuwa riziki yake!"
Wakakata simu zao. Muda ule ule mama Levina akamwita binti yake, ambaye alifika baada ya muda mfupi sana.

"Levina nimepigiwa simu na Happy sasa hivi, yule kijana amepatwa na matatizo. Amefiwa na mama yake, kwahiyo hataweza tena kuja labda mpaka baada ya wiki mbili, nimemwambia mama Happy kwakuwa nina haraka, nalazimika kutafuta mwingine kwahiyo basi zungumza na huyo rafiki yako, yule kijana aje kesho aanze kazi mara moja!"

"Sawa," Levina akajibu kwa sauti ya chini sana, akionekana kuwa na huzuni lakini ndani ya moyo wake alikuwa akishangilia kwamba Deo wake alikuwa anakwenda kuwa karibu naye.

****
Levina alivyoingia tu chumbani kwake, kitu cha kwanza ilikuwa kuchukua simu yake na kumpigia Deo haraka sana.
"Vipi?"

"Habari njema zaidi ya zile za saa ile!"
"Zipi tena Levina?"
"Unatakiwa kuanza kazi kesho, vipi utaweza?"
"Nitaweza!"
"Kweli?"

"Kweli kabisa."
"Basi fanya juu chini, kesho tukutane saa 3:00 asubuhi!"
"Sawa."
Wakaagana.

****
Kama walivyokubaliana, siku iliyofuata walikutana Mwembechai, Deo akiwa na begi lake, tayari alikuwa ameshaacha kazi alipokuwa akifanya mwanzoni na akawa tayari kwenda kuanza kazi kwa akina Levina.

Wakaingia sebuleni na kukutana na mama yake Levina akiwa anamsubiria kwa hamu...

"Karibu mwanangu!" Mama Levina akamwambia Deo.
"Ahsante mama!"
"Jisikie uko nyumbani!"

"Ahsante mama."
"Nina imani maelekezo yote umeshapewa na Levina, kama bado atakupa. Acha mimi niwahi kazini, nawatakieni siku njema," akasema mama Levina akisimama na kupiga hatua za kuondoka.

"Ahsante!" Deo akajibu akiona haya.
Mama Levina akaondoka zake, akawaacha Deo na Levina tu nyumbani. Levina aliposikia muungurumo wa gari la mama yake nje, akajua tayari ameshaondoka. Akamkazia macho Deo, aliyekuwa amesimama kama mlingoti!

Mara ghafla akamsogelea na kumkumbatia kwa nguvu! Kilikuwa kitendo cha haraka na ghafla sana, kilichomshtua sana Deo. Akabaki ameduwaa akimwangalia bila majibu!
Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia




 
USIFE KWANZA MPENZI WANGU.....EPISODE.12

Levina anafanikiwa kumsogeza Deo karibu yake, baada ya kumtafutia kazi ndani mwao. Nini kitaendelea? Songa nayo...

Levina alimshangaa Deo kwa kutoonesha furaha kwa kupata kazi.
“Jamani Deo mbona huoneshi furaha?”
“Levina mbona nipo happy.”
“Muongo, au hukupenda kuja kufanya kazi hizi?”
“Kwa nini nisipende.”

“Basi Deo nakwambia achana na mshahara utakao lipwa nitahakikisha nakuongezea pesa zaidi ya mshahara wako.”
“Nitashukuru Levina.”
“Basi twende nikakuoneshe chumba chako.”

Levina alichukua begi la Deo na kumpeleka kwenye banda la uani kulikokuwa na chumba kimoja. Baada ya kuingia chumbani alitoka na kurudi na ufagio na shuka za kumtandikia. Deo alishangaa mtoto wa tajiri yake kumuhangaikia vile, baada ya usafi wa chumba alimtandikia kisha alimkaribisha.

“Deo karibu hiki ndicho chumba chako.”
“Asante.”
“Vipi umekipenda?’
”Nimekipenda.”

Baada ya kumuonesha kile chumba alimuelekeza kazi zote alizotakiwa kuzifanya kisha alimuacha aendelee na majuku ya siku ile. Levina alirudi hadi sebuleni kutaka kujiandaa kwenda mjini kwenye duka.

Lakini roho haikumpa alisogea hadi dirishani kumtazama Deo aliyekuwa katika vazi la bukta na singland, alijikuta akitabasamu mwenyewe jinsi moyo wake ulivyofurahi kuwa na Deo mwanaume aliyeutesa moyo wake.

Kuwa mbali na Deo aliona kama kuinyima uhuru nafsi yake, aliamini muda ule ambao wazazi wake hawapo ni muda mzuri wa kujisogeza karibu na Deo. Alitoka hadi uani ambako Deo alikuwa ameanza kazi ya kupunguza majani, alisogea karibu yake huku kidole kikiwa mdomoni kujipa ujasiri.

“Deo,” alimwita huku akiachia tabasamu pana.
“Levina si umesema unawahi kazini?”
“Ndiyo Deo lakini bado nina muda, Deo,” Levina alimwita Deo huku akimtoa majani kichwani.
“Unasemaje Levina?”
“Kazi unaionaje?”

”Ndiyo naianza lakini siyo mbaya.”
“Leo kuna kitu nataka kukueleza.”
“Kipi hicho?” Deo aliuliza bila kumuangalia.
“Deo acha kwanza kukata majani nisikilize.”

“Levina hii ndiyo kazi iliyonileta acha niifanye, we wahi kazini jioni tutazungumza nitakuwa nimepunguza kazi si unajua leo ndiyo siku ya kwanza nitaonesha picha mbaya.”
“Deo ufanye kazi usifanye kazi mimi ndiye mwenye mamlaka, na kukuleta hapa si kufanya kazi hii.”

“Si kazi hii, kwa kazi gani?”
“Ili uwe karibu na mimi”.
“Kivipi?”
“Deo lazima usome alama za nyakati kila ninachokifanya lazima ujiulize kina maana gani.”

“Levina mimi na wewe tumefahamiana kitambo umekuwa msichana ambaye umeonesha kunijali, nimekuwa nikivunia upendo wako na kujikuta nikikosa cha kukulipa.”
“Deo cha kunipa unacho hakihitaji pesa wala nguvu.”
“Kipi hicho?”

“Deo lazima leo nikueleze ukweli...na..na..ku...,” Levina hakumalizia aliweka kidole mdomoni huku mkono ukitetemeka baada ya kupoteza ujasiri wa kulitamka neno toka moyoni mwake.
“Levina unasemaa!”

Levina aliona aibu na kukimbilia ndani huku akimwacha Deo akijiuliza maswali yasiyo na majibu, alijiuliza Levina alimaanisha anampenda. Kama ni kweli ulikuwa mtihani ambao aliamini kabisa mapenzi ni kikohozi kamwe wasingeyaficha. Kwa muonekano wa haraka ilionekana familia yake ilikuwa ikimpenda sana na kumjali.

Aliamini kama wazazi wake wakigundua lazima wangemfukuza kazi, alijua lazima atataabika kutokana na kuacha kazi iliyokuwa ikimuingizia riziki. Pia alikuwa na mtihani mwingine kama atamkatalia Levina lazima atamfukuzisha kazi, lakini hakutaka kuingilia sana mawazo ya Levina.

Levina alikimbia hadi chumbani kwake na kuanza kulia kutokana na kukosa ujasiri kuwasilisha uju mbe wake. Alichukua kitambaa cha mkononi na kufuta machozi. Mara simu ya mama yake iliingia, aliipokea na kuzungumza.
“Haloo Mamy.”

“Levina upo wapi?” Alimuuliza kwa ukali kidogo.
“Mbona hivyo mama?”
“Hujanijibu upo wapi?”
“Mamy nipo njiani nakwenda mjini.”

“Jitahidi uwahi kuna mteja wa jana mlikubaliana afuate simu dukani amefika muda, bado duka halijafunguliwa.”
“Namjulisha sasa hivi.”

Alikata simu na kukimbia bafuni kuoga kisha alibadili nguo haraka haraka kuwahi dukani, alitoka hadi uani alipokuwa Deo akikata majani alitembea kwa mwendo wa kunyata alipomkaribia alimgusa begani, Deo alipogeuka alikutana na busu la mdomoni.
“Deo bai, nawahi kazini kazi njema.”
“Na wewe pia.”

Levina alitembea kwa haraka kuelekea kwenye gari lake ili awahi kwenye mihangaiko yake. Nyuma alimuacha Deo na maswali mengi juu ya vitendo vya kimahaba vya Levina, Levina alibadilika kwa muda mfupi hakuwa yule mpole na mnyenyekevu muda wote, alikuwa ni mtu aliyeonekana kuchizika kimahaba.

Kauli ya Levina ilimfumbulia fumbo zito moyoni mwake la muda mrefu la huduma zote zilizoelekezwa kwake na Levina haikuwa bure na ukweli wake ulikuwa umedhihirika muda mfupi uliopita. Deo alicheka na kuendelea kupunguza majani huku umbile la Levina msichana mrembo tena anayetoka katika familia tajiri lilitawala katika ubongo wake.

Nini Kitaendelea?





USIFE KWANZA MPENZI WANGU ......EPISODE .13.


ILIPOISHIA:
Kauli ya Levina ilimfumbulia fumbo zito moyoni mwake la muda mrefu la huduma zote zilizoelekezwa kwake na Levina haikuwa bure na ukweli wake ulikuwa umedhihirika muda mfupi uliopita. Deo alicheka na kuendelea kupunguza majani huku umbile la Levina msichana mrembo tena anayetoka katika familia tajiri likiwa limetawala katika ubongo wake.
SASA ENDELEA...

Mbinu za Levina kumuingiza ndani ya jumba lao lilimfanya Deo acheke peke yake kwa kicheko cha chini chini huku akitikisa kichwa, kama alikuwa akizungumza na mtu alisema kwa sauti ya chini.

“Kweli Levina kiboko, mbinu zake mwenyewe sina hamu.”
Baada ya kumaliza kukata majani aliyakusanya na kuyapeleka kwenye shimo la takataka lililokuwa nyuma ya banda la ng’ombe.
***
Levina akiwa ndani ya gari lake akielekea kwenye duka lao la simu, macho yake yalikuwa yametazama mbele huku akikanyaga mafuta taratibu kutokana na foleni ya jijini. Pembeni ya barabara alimuona mvulana mmoja na msichana wakitaniana katika hali ya mapenzi.

Aliwakazia macho mpaka alipowapita, alitabasamu na kuchukua simu yake iliyokuwa kwenye dash boad na kuifungua upande wa picha. Aliifungua na kuijaza picha ya Deo kwenye kioo cha simu, picha ambayo alipiga kwa siri bila yeye kujijua.

Aliibusu simu na kusema kwa sauti ya chini.
“Lazima Deo atanielewa si mtoto mdogo.”
Kutokana na foleni ya barabarani kila gari liliposimama aliiangalia picha ya Deo na kutabasamu. Aliikumbatia simu kifuani katika mahaba mazito na kufumba macho huku akisindikizwa na muziki mtamu wa kizazi kipya wa Suma Usemao Mapenzi ni sumu.

Alirudia maneno ya kiitikio kimoyomoyo, kumbe wakati huo foleni ilikuwa imeshasogea lakini Levina alikuwa amejisahau na mahaba mazito ya picha ya Deo kwenye simu yake. Hata kelele za honi hakuzisikia kutokana na kujifungia ndani ya gari huku akipulizwa na kiyoyozi. Sauti ya kugongwa dirisha ndiyo iliyomshtua alipofumbua macho aligundua foleni imefika mbele ambapo alibadili gia na kukanyaga mafuta akiwaacha watu wakimsindikiza na matusi mazito ya nguoni lakini hakuyasikia.

Hata alipofika dukani muda wateja walipopungua alitumia muda huo kuzungumza na Deo huku akimpigia simu mfanyakazi wa ndani ampatie Deo chakula kizuri na kila kitu ambacho baba yake alikitumia wakati wa chakula. Kingine alimuonya mfanyakazi wa ndani kuwa mbali na Deo bila kufanya utani wowote.

“Haloo Deo.”
“Ooh, Levina za kazi?”
“Zimezidi kuwa nzuri baada ya kusikia sauti yako.”
“Nashukuru kusikia hivyo.”

“Vipi unafanya nini sasa hivi?”
“Mmh, nimepumzika ndiyo nimemaliza kula.”
“Umekula nini Deo?”
“Chakula.”

“Chakula gani?”
“Ndizi na nyama.”
“Matunda je?”
“Nimepata.”

“Juisi?”
“Nimepata.”
“Umeshiba?”
“Nimeshiba.”

“Muongo, usione aibu wewe kwa sasa ni zaidi ya baba yangu mzazi.”
“Kivipi?”
“Umekuwa mtu muhimu sana maishani mwangu, kuwa nawe karibu nimefarijika. Nilijihisi ufahari siku uliyonikubalia kuja kufanya kazi kwetu.”

“Mh!”
“Usigune Deo, lazima niseme ukweli, Deo nakupenda sana.”
Maneno yale yalimfanya Deo anyamaze kwa muda kitu kilichomnyima raha Levina na kuona mbegu yake huenda hakuipanda muda muafaka. Lakini kwa upande mwingine alijiona yupo sawa kutokana na moyo wa kupenda ulivyo.

Siku zote macho yakiona moyo unapenda na moyo ukipenda subira hakuna tena na subira ikitoweka aibu hukimbia. Aliamini mchuzi wa mbwa ulitakiwa kunywewa ungali moto.

Hakujutia kauli yake kumueleza ukweli Deo kuwa anampenda, ulikuwa ujumbe sahihi toka moyoni mwake ambao aliamini kupitia njia ya simu kidogo ujasiri ulikuwepo. Lakini kimya cha Deo kilimfanya akose raha moyoni kwake aliamini kama Deo hataafiki ombi lake lilikuwa sawa na kutwanga maji kwenye kinu.

“Deo,” Levina alimwita baada ya kupita ukimya mfupi.
“Levina.”
“Mbona hunijibu, kujivua nguo mbele yako si umalaya Deo, usinihukumu kwa jinsia yangu bali kwa upendo wangu mzito moyoni mwangu. Deo sikuwa na njia yoyote ya kukueleza kuwa nakupenda, naomba uheshimu hisia zangu.”
“Levina,” Deo alimwita Levina kisha alishusha pumzi nzito.

“Deo,” Levina aliitikia upande wa pili na sauti yenye dalili za kilio.
“Levina naogopa sana mimi kuwa sehemu ya matatizo yako katika furaha zako za kila siku.”
“Deo kunikubalia ni kuniingiza kwenye matatizo?”

“Sina maana hiyo!”
“Muongo Deo, unataka kuongopa nini?”
“Levina wewe ni mtu muhimu sana kwangu, nilikuwa na maana kutokana na kujitoa kwangu na mimi kuniona ni sehemu ya furaha yako. Nami najitoa kwako kwa nguvu zote ili kukuhakikishia zile raha ulizokuwa ukizitafuta kwangu unazipata.”
“Kweli Deo?”

“Siwezi kukudanganya.”
“Waooo, I can’t beleave my dear, Thanks God thanks Deo I love you soooo much.”
Levina alishangilia kukubaliwa ombi lake na kujisahau kama yupo dukani na kuwashangaza wateja waliokuwa dukani wakisubiri amalize kuzungumza kwa simu.
Nini kitaendelea?




USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE .14.na 15.

ILIPOISHIA
“Waooo, I can’t beleave my dear, Thanks God thanks Deo I love you soooo much.”
Levina alishangilia kukubaliwa ombi lake na kujisahau kama yupo dukani na kuwashangaza wateja waliokuwa dukani wakisubiri amalize kuzungumza kwa simu.
SASA ENDELEA...

Hata baada ya kumaliza kuzungumza na simu, uso wa Levina ulionesha dhahiri kuwa amezama ndani ya dimbwi la huba. Aliendelea kuchekacheka mwenyewe kama mwendawazimu bila kujali idadi kubwa ya wateja ambao walikuwa wakisubiri kuhudumiwa. Akili yake ilijawa na taswira ya Deo kiasi cha kusahau kazi.

“Oya sista vipi? Tumesimama muda mwingi kusubiri huduma we uko bize na simu tu! Tuhudumie tafadhali!”
Kauli ya mmoja wa wateja waliokuwa wamesimama kusubiri huduma kwenye duka la simu la kina Levina ilimzindua kutoka kwenye mawazo yaliyoiteka akili yake.

Oops! Im sorry, samahani wateja, hii simu imetoka kwa mtu muhimu sana, enhe, ulisema unataka Nokia toleo gani?”
“Nokia 5130c-2!”
“Mimi nakudai chenji yangu, naona simu imekupagawisha kabisa, shemeji nini?”

Levina aliendelea kuwahudumia wateja waliokuwa wakiingia na kutoka kwenye duka lao la simu. Wakati akiendelea na kazi, majibu ya Deo yalikuwa yakiendelea kuzunguka kichwani mwake kama filamu nzuri ya kusisimua.

Wateja walipopungua, alichukua simu yake na kuendelea kuitazama picha ya Deo aliyompiga bila mwenyewe kujijua, akawa anaitazama huku usoni akiwa na bonge la tabasamu! Moto wa penzi la Deo ulikuwa umewaka kikweli ndani ya moyo wake, akawa anasubiri kwa hamu muda wa kufunga duka ufike haraka ili akaonane na Deo, kipenzi cha moyo wake.

***
Kuchanganya mapenzi na kazi ni suala ambalo Deo alikuwa akiliogopa sana. Mara kwa mara alikuwa akijiambia mwenyewe kuwa safari ya kutoka nyumbani kwao Shinyanga hadi Dar es Salaam ilikuwa ni kutafuta maisha, hivyo hakuwa tayari kuona anashindwa kutimiza ndoto zake kwa sababu ya kuchanganya mapenzi na kazi.

Alipofikiria kitakachotokea endapo uhusiano wake na Levina ungegunduliwa na wazazi wa Levina, alijikuta akibatilisha majibu aliyompa Levina siku ile. Alichokiamua ni kutojihusisha kwenye uhusiano wa kimapenzi na Levina, aliamua kuelekeza nguvu na akili zake kwenye kazi.

Saa zilizidi kuyoyoma na hatimaye muda wa Levina kurudi nyumbani ukawa umewadia. Akilini mwake, Levina alikuwa akiwaza namna atakavyomkumbatia na kumkiss Deo mara atakapowasili nyumbani kwao. Alipanga kufanya kila linalowezekana ili kumfanya Deo ampende kama yeye anavyompenda.

Baada ya kufunguliwa geti na kwenda kuegesha gari lake, Levina alishuka akiwa na hamu kubwa ya kuoanana na Deo. Nyumbani kwao hakukuwa na mtu mwingine yeyote zaidi ya mfanyakazi wao na Deo kwani wazazi wake walikuwa bado hawajarejea kutoka kwenye mihangaiko yao.

‘Jamani Deo! Nilikukumbuka sana sweetie, yaani nilikuwa naona saa haziendi,’ aliongea Levina kwa sauti ya kudeka na kumkumbatia Deo kimahaba. Katika hali ambayo hakuitegemea, Levina alishangaa kumuona Deo akikunja sura na kumsukuma pembeni, kisha akaondoka na kuelekea chumbani kwake na kumuacha Levina akiwa bado haamini kile kilichotokea.

“Kwa nini unanitesa Deo, nifanye nini ili uamini kuwa ni kweli nakupenda?” Aliongea Levina huku akimfuata Deo.
“Tafadhali sana Levina, sina maana ya kukutesa lakini naona kama najihatarisha sana pamoja na kukuweka wewe kwenye matatizo.”

“Kivipi Deo, mi sikuelewi mwenzio?”
“Namaanisha hivi, nakupenda sana Levina lakini sitaki kuwaudhi wazazi wako! Naamini wakigundua watakasirika sana na watanitimua hapa kwenu, nimetoka mbali sana Levina kuja mjini kutafuta maisha, sitaki mapenzi yaniharibie maisha yangu ya baadaye…”

Wakati Deo akiendelea kujitetea mbele ya Levina, walisikia geti la nje likifunguliwa na gari la wazazi wa Levina likaingia ndani. Kwa haraka Deo alitoka nje na Levina naye akaelekea chumbani kwake huku wakiahidiana kuzungumza vizuri baadaye wakiwa peke yao.

***
Deo alijitahidi kuficha hisia zake mbele ya wazazi wa Levina. Bado hofu ilikuwa imeupamba mtima wake. Muda wa chakula cha jioni ulipowadia, kama kawaida familia nzima ilijumuika Dinning room kwa ajili ya maakuli. Kwa makusudi kabisa, Levina alijisogeza na kukaa jirani na Deo, akamsaidia kumpakulia chakula na kumkaribisha kwa heshima.

Wakati wakiendelea kula huku wakibadilishana mawazo hapa na pale, Levina alikuwa akimtazama Deo usoni kwa kuibia na kuishia kutabasamu mwenyewe. Mchezo ule ulishtukiwa na mama yake Levina, ambaye hata hivyo alijikausha ili awanase vizuri.

Kwa aibu alizokuwa nazo Deo, alijikuta akishindwa hata kula kwa uhuru kwani mamcho ya Levina yalikuwa hayabanduki kwake. Kaamua kujikaza kiume na kumtaza na yeye usoni bila kujali kuwa wamekaa na baba na mama. Macho yao yalipogongana, wote walitabasamu kimahaba, hali iliyomfanyampaka baba Levina kushtuka.



Nisiwachoshe kwa kusoma sana Itaendelea leo jioni nawaacha hapo....
 
“Mama Deo amepigwa risasi, yupo hospitalini,” akasema Cleopatra akiwa tayari ameshaingia kwenye gari.
Akapiga honi kwa nguvu, mlinzi akafungua haraka. Cleopatra akaondoa gari kwa kasi sana. Alikuwa anakwenda Muhimbili, huku nyuma akiwa amemuacha mama yake akiwa mwenye mawazo.

MziziMkavu simulizi zenye risasi kidogo zinanipunguzia uhondo........................napenda happy endings because we rarely get them in rel life......
 
USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE.16-17


Penzi linachipuka kutoka ndani mwa Levina kwenda kwa Deo, kijana anayefanya kazi nyumbani kwao kwa kasi ya ajabu sana. Anashindwa kufanya kazi vyema kutoka na hisia hizo kali za mapenzi. Anajaribu kumweleza Deo, ambaye alimkubalia kwa shangwe!

Hili lilimfanya afunge duka lake haraka na kurejea nyumbani ili aweze kupata wasaa wa kuzungumza na Deo, lakini jambo la ajabu, alipofika akakuta Deo akiwa na maamuzi mengine mapya! Hakuwa tayari kuwa naye kimapenzi, kiasi cha kumsukuma mbali!

Baadaye wakiwa kwenye meza ya chakula, Levina alionesha alama zote kuwa anampenda Deo au walikuwa katika uhusiano, jambo ambalo baba yake, aliligundua! Akahisi kuwepo kwa jambo linaloendelea kimya kimya! Je, nini kitatokea? Endelea kufuatilia...

MZEE Masamu aligundua kitu kupitia macho ya mwanaye aliyekuwa akimwangalia Deo kwa macho yaliyojaa ubembe wa mahaba. Ni kitu ambacho hakukipenda hakika, hakutaka kabisa mwanaye awe na uhusiano na kijana yule. Hakuwa na hadhi ya familia yao.

Mara ghafla, akasogeza pembeni sahani yake ya chakula na kunawa mikono yake, jambo hilo lilimshangaza sana mke wake.
“Vipi baba Levina?!”
“I’m okay!”

“No dady, you are not okay, vipi chakula hujakipenda?” Mama Levina akasema kwa sauti ya taratibu sana.
“Nimeshiba mama Levina,” akasema mzee Masamu akimwangalia Levina kwa macho yenye kiashiria kibaya.

Mama Levina aliweza kugundua kwamba kuna jambo ambalo si la kawaida lilikuwa likiendelea. Anamfahamu vizuri sana mume wake, hakuwa na kawaida ya kushiba haraka kiasi kile, lazima kulikuwa na kitu. Naye akasogeza sahani yake pembeni na kunawa mikono.
“Mom, kwanini mnasusa chakula?” Levina akauliza kwa mashaka kidogo.

“Shiiiiii...” mama Levina akamnyamazisha mwanaye.
Deo akagundua kwamba mchezo wa Levina ulikuwa umegundulika, mara moja akanawa mikono na kukimbilia chumbani kwake. Bwana na Bibi Masamu wote kwa pamoja wakaongozana kwenda chumbani kwako kulala.

“Mume wangu mpenzi, nini tatizo? Nini kimetokea mpenzi wangu, maana naona haupo sawa kabisa!” Mama Deo akamwuliza mumewe walipoingia chumbani kwao.
“Unataka kusema hujaona chochote?” Mzee Masamu akasema kwa hasira.
“Nini tena dear?”

“Hivi unakumbuka kwanini tulimwondoa Rashid hapa nyumbani?”
“Ndiyo!”
“Unaona anayofanya mwanao?”
“Nani Levina?”

“Kwani nani mwingine?”
“Kivipi basi mume wangu?”
“Hujaona anavyomwangalia yule kijana?”
“Kwakweli sijawa makini kuwaangalia mume wangu!”

“Sasa wewe kuwa makini au usiwe makini, lakini nataka kukuambia kwamba, sitaki matatizo katika familia yangu! Deo hana hadhi ya kuwa na mwanangu!”
“Kwani amesema anataka hivyo?”
“Hapana, lakini dalili zipo wazi.”
“Nitazungumza na Levina!”

“Siyo utazungumza naye, nenda ukaongee naye sasa hivi, sihitaji matatizo katika familia yangu. Narudia tena sihitaji matatizo katika familia yangu, nenda kazungumze naye tafadhali.”

“Nimekuelewa mume wangu, ngoja niende nikaongee naye.”
Mama Levina akatoka haraka na kumuacha mumewe chumbani akiwa amefura kwa hasira. Alipofika sebuleni, alimkuta Levina akiwa anamalizia kuondoa vyombo mezani.
“Levina nahitaji kuongea na wewe!”

“Natoa vyombo mama!”
“Achana navyo isitoshe si kazi yako, kwani Helena yupo wapi? Hiyo ni kazi yake, haikuhusu wewe hata kidogo.”
“Najua mama, lakini...” Levina akaendelea kujitetea.
“Wewe tusikilizane!”

“I’m coming mom!”
“Hurry up!”
“Ok mom!”
Levina akaacha kila kitu na kujisogeza kwa mama yake, aliyekuwa amekaa kwenye sofa kubwa pale sebuleni.

“Hebu niambie, nini kinaendelea kati yako na Deo?!” Mama yake akamwuliza mara baada ya kukaa sofani.
“Unamaanisha nini mama?”
“Macho yako yanaonesha jinsi unavyofahamu ninachomaanisha!”
“Sijui kitu mama, kwani vipi?”

“Sasa mimi sina kitu cha kuzungumza zaidi au kubembelezana na wewe, lakini nataka kukuambia kwa kifupi sana, kama una wazo la kuanzisha uhusiano na Deo, futa kabisa wazo hilo!”
“Uhusiano?”
“Ndiyo nimekuambia sasa, ondoa wazo hilo kichwani mwako na kama mmeshaanza tafadhali acha mara moja!”

“Maamaaa...mimi na Deo wapi na wapi mama?”
“Hili agizo limetoka kwa baba yako!” Mama Deo akaongeza kusema.
“Mungu wangu, kweli mama?” Levina akashtuka sana.
“Nadhani unamfahamu vizuri sana mzee Masamu, unajua hasira zake, sasa endelea na upuuzi wako ndiyo utajua kitakachotokea!” Mama yake akasema na kusimama kisha akaondoka zake.

Levina akabaki pale subuleni akiwa mwenye mawazo mengi sana kichwani mwake. Alimfahamu vizuri sana baba yake, kama ni kweli yeye ndiye alikuwa ameagiza aachane na Deo, basi hali ilikuwa mbaya kuliko alivyofikiria.

Jambo hilo lilimtisha sana, lakini halikusababisha penzi lake dhidi ya Deo lishuke, bado alihisi penzi zito sana moyoni mwake, alimpenda sana Deo na hakuwa tayari kumpoteza.
Je, Levina atatii kauli ya mama yake?






USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE.18-19-20

Tayari mambo yamekuwa mabaya kwa upande wa Deo, ambaye Levina anaonekana kumpenda sana, lakini kitu cha ajabu ni kwamba, Levina anashindwa kuficha hisia zake na hivyo kusababisha baba mzazi wa Levina mzee Massamu kuhisi kitu!

Jambo hilo lilimtisha sana Deo, ambaye aliingia chumbani kwake akiwa na mawazo tele akianza kuhofia kupoteza ajira yake. Akiwa bado ana mawazo, usingizi ukiwa umekataa kabisa kumchukua, akasikia mtu akigonga mlango. Akashtuka sana.

Alipouliza aliyekuwa akigonga ni nani, hakujibu! Je, nini kitatokea? Endelea kuisoma...

DEO alishtuka kuliko kawaida, mawazo tele kichwani mwake yakamuandama, kitu kilichoingia kwa kasi sana akilini mwake ni kwamba aliyekuwa akigonga mlango ule alikuwa ni mzee Massamu.

Hapo hakika ungekuwa mwisho wa ajira yake. Jambo ambalo hakutaka kabisa litokee. Akasogea mpaka kwenye kitasa cha mlango wa chumbani kwake, akasogeza mdomo wake kwenye tundu la funguo, akauliza kwa sauti ya chini kabisa...
“Nani?”

“Fungua!” Sasa akajibiwa na sauti ya kike, ambayo haikuwa ngeni sana masikioni mwake.
Alikuwa ni Levina.
“We’ Levina, acha ujinga bwana, rudi chumbani kwako.”
“Fungua kwanza, kuna kitu nataka kukuambia.”
“Nini?”

“Fungua.”
Deo akatumia muda wa dakika mbili tatu kuwaza, kisha akaamua kwenda kufungua ili kuepuka kelele za levina ambazo zingeweza kusababisha matatizo zaidi.
“Haya unasemaje?” Akamwuliza baada ya kufungua mlango.
“Kabla hata sijakaa?” Akauliza Levina kwa sauti ya chini, ambayo Deo alishtuka sana kuisikia, akihisi kama ni kubwa.

“Ongea taratibu bwana...” Deo akasema kwa woga.
“Niongee taratibu nini? Unamuogopa nani?”
“Wazazi wako.”
“Wameshalala bwana.”

“Kwani unasemaje?”
“Acha utoto, inamaana hujui kwamba mimi nakupenda?”
“Najua.”
“Sasa?”
“Sitaki tena.”

“Unasemaje?”
“Sitaki tena.”
“Utataka Deo, lazima utake, hujui ni kwa kiasi gani nimehangaika kukupata. Hujui nimefanya mambo mangapi na wakati mwingine kuwakosea watu kwa sababu yako.”
“Lakini Levina ukumbuke kwamba ulisema unanileta kazini.”

“Ndiyo nakumbuka.”
“Sasa?”
“Lakini si nilikuambia kwamba nakupenda? Unadhani ningeweza kufanya mambo yote hayo hivi hivi tu!”

“Hivi unajua kwamba haya mambo ni ya hatari sana? Kwanza baba yako anaonekana ameshaanza kuhisi kwamba kuna kitu kinaendelea, huoni kwamba ni tatizo kwangu? Hivi nikipoteza kazi, unadhani nitakuwa mgeni wa nani mimi?”

“Acha kuwaza mambo ya kijinga...” akasema Levina akivua gauni lake jepesi la kulalia.
“Acha kufanya hivyo Levina.”

Levina hakusikia kitu, akalitupa mbali baada ya kumaliza kulivua na kumsogelea Deo, kisha akamsukuma kitandani. Kama mzigo Deo akaanguka kitandani na mara Levina akamzidi ujanja, dakika chache baadaye wakajikuta wakiwa kwenye kiota cha huba ya mapenzi, wakiwa wamesahau shida zote za ulimwengu.

***
“Umeongea naye?” Mzee Massamu akamwuliza mkewe.
“Ndiyo.”
“Anasemaje?”
“Aseme nini?”
“Kwahiyo hajasema chochote?”

“Simaanishi hivyo...kifupi amekataa.”
“Amekataa?”
“Ndiyo amekataa.”
“Sasa kuanzia leo anza kuwafuatilia utapata majibu, tena nahisi huenda huwa wanalala pamoja usiku. Ngoja muda uende kidogo, nataka kwenda kuhakikisha mwenyewe leo.”

“Sawa mume wangu, unajua kama itakuwa ni kweli, utakuwa mchezo mbaya sana.”
“Siyo mchezo mbaya tu, sitaki mwanangu ajiingize kwenye matatizo. Unajua kuolewa na lofa, ni sawa na kukaribisha ulofa katika familia. Hilo siwezi kuliruhusu likatokea katika familia yangu. Siwezi kabisa.”
“Ni kweli kabisa baba Levina...itakuwa aibu kwa familia,” akasema mama Levina akiunga mkono kauli ya mumewe.

***
Saa nane na dakika zake za usiku, Mzee Massamu aliamka kitandani na kutoka nje taratibu kabisa. Akaenda moja kwa moja hadi kwenye mlango wa chumba cha Levina. Akatega sikio kusikia kama Levina alikuwa akihema ndani, lakini hakusikia kitu. Kwakuwa taa ilikuwa haijazimwa, akaamua kuchungulia kupitia kwenye tundu la ufunguo kuangalia kama alikuwemo mle ndani.

Hakuwepo!
Akashtuka sana.
Akashika kitasa cha mlango na kukizungusha taratibu, mlango ukafunguka wenyewe. Mzee Massamu akaingia mpaka ndani na kuangalia kila kona, hakuona mtu! Ni kweli Levina hakuwemo ndani.
“Shiiiti, huyu mtoto amekwenda wapi?” Akawaza.

Papo hapo likaja wazo lingine, akahisi huenda alikuwa ameingia msalani, kwa bahati nzuri choo kilikuwa mle mle ndani. Kwahiyo akaamua kuita kwa sauti ya chini...
“Levina...Levina...we Levina...” lakini Levina hakuitika.
Hapo akaamua kuusogelea mlango wa chooni, akajaribu kuusukuma kwa nguvu! Ukafunguka!
Levina hakuwepo!

“Lazima atakuwa chumbani kwa Deo,” akawaza na kutoka chumbani kwa Levina haraka.
Akapiga hatua za taratibu hadi kufikia mlango wa Deo. Korido nzima ilikuwa kimya kabisa. Alipoufikia mlango wa Deo alitarajia kusikia kelele za mahaba chumbani, lakini hakusikia.

Chumba kilikuwa kimya kabisa. Hakujiuliza mara mbili, akajaribu kuusukuma ule mlango ambapo ulifunguka mara moja kwakuwa haukufungwa!
Alihisi kuchangikiwa!
Akahisi kuzimia!

Alichokiona mle chumbani, ilikuwa vigumu sana kuamini. Macho yake yaliona gauni la kulalia la mwanaye likiwa chini, huku nguo yake ya ndani ikiwa juu ya kiti! Deo alikuwa amelala na mwanaye wakiwa kama walivyozaliwa!
Alihisia harufu ya damu!
Akatamani kuua!

Lakini akajipa moyo!
“Deo unamfanya mwanangu hivi?” akajisemea moyoni mwake.
Haikuwa na maana kwao maana wote walikuwa wameishilia kwenye usingizi mzito, wakiwa kama walivyozaliwa. Busara ya Mzee Massamu ikatumika, akaamua kutoka mle chumbani taratibu na kurudi chumbani kwake. Akamkuta mkewe akiwa macho. Kwa hali aliyoingia nayo, mkewe akajua lazima kulikuwa na kitu kibaya kimetokea.

“Vipi mume wangu?”
“Nenda mwenyewe chumbani kwa Deo ukajionee.”
“Kuna nini?”
“Nenda mke wangu,” akasema Mzee Massamu akitoka jasho mwili mzima.
Je, nini kitatokea?






USIFE KWANZA MPENZI WANGU ....EPISODE.21.


Mzee Massamu ametoka chumbani kwa Deo na kushuhudia akiwa amelala na mwanaye Levina, akamwamsha mkewe na kumwambia aende akajionee mwenyewe chumbani kwa Deo. Nini kitatokea? Endelea...

MAMA Levina ni kama alikuwa haelewi kabisa anachoambiwa na mumewe. Alimwangalia bila kupata majibu ya moja kwa moja. Kwanini anamwambia aende akajionee mwenyewe chumbani kwa Deo.

“Mume wangu, niambie tafadhali, kuna nini?”
“Nenda mama, nenda ukaoane mwenyewe!”
Mama Levina hakutaka kuuliza swali lingine zaidi, akatoka na kunyata hadi kwenye mlango wa Deo, kwa haraka za mzee Massamu, hakuufunga ule mlango, kwa hiyo mama Levina alivyotokeza tu akaona kila kitu!
Nusu azimie!

Akajikaza sana, lakini akashindwa, macho yake yakaanza kumwaga machozi. Hakutaka haraka, akaufunga ule mlango na kuwaacha waendelee na usingizi wao. akatoka haraka hadi chumbani kwao.

Huko akamkuta mumewe akiwa amejiinamia kwa mawazo tele. Mama Levina naye akaungana naye, yeye akaenda kujitupa kwenye sofa kubwa na kuyatupa macho yake juu ya dari.
Akawaza alichowaza!

Majibu hayakupatikana!
Lakini akiwa katikati ya mawazo hayo, kumbukumbu za zamani zikaanza kurejea kama sinema ya kusisimua! Akakumbuka jinsi Levina alivyomweleza kuhusu kijana wao wa kazi aliyepita, ambaye alifukuzwa baada ya kumuonesha meseji za mapenzi akimtongoza!

Ni Levina yule yule!
Iweje leo alale na kijana wa aina ile ile? Mama wa watu akawaza lakini hakupata majibu.
“Hii ni laana, huu ni upuuzi mtupu,” akajisemea moyoni mwake.

Lakini ghafla kuna kitu kilianza kuingia kichwani mwake kwa kasi ya ajabu, kwamba kuna uwezekano mkubwa Levina alimsingizia yule kijana wa mwanzoni ili aweze kupata nafasi ya kumuingiza yule kijana nyumbani kwao.

Hilo lilikuja kichwani mwake hasa kutokana na kukumbuka tukio la kumweleza Levina kwamba alikuwa amepata kijana mwingine kutoka Bagamoyo, akalipokea bila furaha. Lakini baadaye aliposikia kwamba kijana huyo amefiwa na alitakiwa kusafiri kwenda kwenye msiba, zikawa taarifa njema kwake na kumleta Deo!

Kila kitu kikafunguka kama sinema ya kusisimua. Akagundua uchafu wote alioufanya Levina.
“Shiiit! Kumbe ndiyo maana alikuwa anafanya yote yale ili aweze kuja kufanya uchafu wake na huyu mpuuzi siyo?” akawaza kichwani mwake mama Levina.

Baba Levina alikuwa kimya kabisa, hakuelewa kilichokuwa kikiendelea. Alimpenda sana mwanaye, siku zote aliamini bado alikuwa kigori, lakini kitendo cha kushuhudia uchafu wake, tena mbele ya macho yake kabisa kilimchoma sana moyo wake.
“Mama Levina...” baba Levina akaita.

“Abee mume wangu!”
“Umeona?”
“Acha tu!”
“Sasa?”
“Sasa nini tena, zaidi ya kumtimua huyo mpumbavu hapa nyumbani?”

“Sawa, tulale, hili nitalimaliza mwenyewe asubuhi!”
“Sawa mume wangu, lakini ukweli ni kwamba sijaamini kabisa kama Levina angeweza kutuabisha kiasi hiki!”

“Hata mimi pia, sina amani kabisa. Nahisi kama dunia nzima inaniangalia mimi. Huyu mtoto ametuvua nguo kabisa!”
Wakaamua kulala, lakini wakiwa na majonzi tele mioyoni mwao.

***
Mzee Massamu aliamka mapema sana siku hiyo, lakini kila alipokuwa akitaka kutoka nje, alijikuta miguu yake ikikataa kabisa. Alihisi alikuwa na hasira kali ambayo ingeweza kusababisha madhara makubwa.
Baada ya kujishauri kwa muda mrefu, akatoka hadi sebuleni huku akiendelea kufunga tai yake shingoni.

Akiwa sebuleni, akafungua pazia kuangalia nje, akamuona Deo akikatia majani ya fensi, akahisi moyo wake kwenda mbio sana.
Akaketi kwenye kiti, akachukua viatu vyake, akafunga kamba na kutoka nje. Alipofika mlangoni, akajikuta anasita kuinua mguu wake kupiga hatua nyingine.

“Deo,” akajikuta ameita.
“Naam baba,” Deo akaitika haraka na kukimbia alipokuwa amesimama mzee Massamu.
“Shikamoo baba!” akasalimia Deo.
“Mar-haba bwana, mzima?”
“Sijambo!”

“Hata mimi naona hujambo!” Mzee Massamu akamjibu.
Kwa mara ya kwanza alimuona mzee huyo akiongea naye kwa muda mrefu, tena maneno ambayo yalionekana kuwa na mafumbo ndani yake. Moyo wake ukapiga kambi!...Puuu!
“Mchezo umeshtukiwa nini?” akawaza.

“Hivi hapa ndani una mke?” swali hili likazidisha utata kichwani mwake.
“Mke?”
“Kwani umekuja kuoa au kufanya kazi?” Lilikuwa swali gumu kidogo kujibu. Akabaki anababaika akikosa cha kuongea.

“Hivi, unajua huyu Levina nimeteseka naye kwa kiasi gani?” akamwuliza tena.
Deo akanyamaza kimya.
“I’m talking to you!” akasema kwa Kiingereza, hapo ndipo Deo hakuelewa chochote kabisa.
Deo bado aliendelea kubaki kimya.

“Sikia kijana...huwa nina roho nzuri sana, lakini pia nina roho mbaya sana. Naweza kukutwanga risasi kufumba na kufumbua...naomba ndani ya dakika tano, uwe umeshaondoka hapa kwangu...haraka sana naomba ufutike!”
“Sawa mzee.”

“Ingia ndani uchukue kila kilicho chako, uondoe nuksi nyumbani kwangu!” akasema Mzee Massamu akionekana kuzidiwa na hasira.
Deo akabaki anatetemeka, hakuwa na neno lolote la kuongea, kwa hali aliyoonekana kuwa nayo Mzee Massamu, kama angeongea neno lolote, angeweza kuishia kupigwa risasi na kufa pale pale. Mzee Massamu akaondoka na kuingia kwenye gari lake, hapo Deo akaingia ndani na kuchukua nguo zake, akaondoka.

Hakumuaga Levina wala mama yake. Alijua ni kiasi gani angepata matatizo kama angefanya hivyo! Akatokomea mitaani akiwa anajuta. Usiku mmoja tu, ndiyo chanzo cha matatizo yale. Alikuwa anarudi kwenye dhiki ambayo tayari alishaisahau. Anarudi kwenye maisha yake ya mitaani!
Akaikumbuka Singida!
Alitakiwa kurudi kwao Singida!

***
Alikuwa amezama kwenye kumbukumbu ambazo zilibaki kuwa historia, Deo anaumwa, risasi zimepenyeza kwenye bega lake. Hana matumaini tena ya kufunga ndoa na mpenzi wake Cleopatra. Akiwa ameyatoa macho yake pale kitandani, sasa ameweza kumkumbuka vizuri mwanamke yule mrembo aliyekuwa amesimama.

Yes, alikuwa ni Levina!
Levina Massamu!
“Pole na kuumwa!” Levina akatamka akimkazia macho.
Deo hakujibu!
“Pole sana mwaya, kwahiyo ndoa itaahirishwa?” akauliza tena Levina.

Uso wa mwanamke huyu, ulikuwa wa upole, lakini aliachia tabasamu mwanana wakati wote alipokuwa akizungumza. Tabasamu ni kitu cha ajabu sana kwa wakati huu ambao Deo anaugulia maumivu kitandani.

Anatabasamu na wakati yeye yupo kitandani? Tena na tundu la risasi begani! Moyo wa Deo ukaingiwa ubaridi, mara akajihisi kuumia sana, machozi kama maji yakaanza kumiminika machoni mwake. Punde, akamuona mpenzi wake akija uelekeo ule. Mpenzi wake mpya ambaye alikuwa bibi harusi mtarajiwa!
Cleopatra!!!

Msomaji wangu mpenzi, kama kuna mahali nimekuacha kidogo, piga simu namba 0656 819552 nikuelekeze. Hii ni simulizi tamu ambayo itakuacha na mafunzo makubwa. Usikose kuendelea nayo







USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE.22.

Deo amefukuzwa nyumbani kwa mzee Massamu alipokuwa anafanya kazi, haijulikani alipoelekea, lakini upande wa pili anaonekana akiwa amelezwa hospitalini Muhimbili. Mbele yake amesimama mwanamke ambaye sasa amemkumbuka vizuri, ni Levina aliyekutana naye sokoni Tandale akiwa anauza mchele.

Je, baada ya Deo kufukuzwa nyumbani kwa mzee Massamu alikwenda wapi? Ilikuwaje akakutana na Cleopatra na kuamua kuachana na Levina? Kwanini waliachana na nani aliyempiga Deo risasi? Endelea kufuatilia...

DEOGRATIUS aliyakodoa macho yake akiwa hajui la kufanya, akamwangalia Levina kwa umakani, lakini akiwa na maswali mengi sana kichwani mwake. Mosi, Levina alijuaje kwamba yeye anaumwa? Nani alimpa taarifa hizo?

Hata hivyo, hayo hayakuwa maswali magumu sana, swali gumu zaidi ambalo lilimchanganya kichwa chake ni akina nani wale waliompiga risasi na kwanini walifanya hivyo?
Akiwa katika maswali hayo, anamuona mwanamke mwingine akija uelekeo wa kitanda chake akitokea mlango mkubwa wa kuingilia pale wodini. Alimfahamu vizuri sana.

Ni Cleopatra!
Macho ya Cleopatra yalikuwa na wasiwasi mwingi, lakini alipokaribia yakaonesha ukali kidogo. Ukali uliosababishwa na kiumbe kilichokuwa mbele ya kitanda cha Deo.

Levina!!!
“We’ malaya unafanya nini hapa?” Cleopatra akauliza kwa sauti ya chini lakini iliyojaa ukali.
“Umeniita nani?”
“Malaya!”
“Nani?”

“Malaya!!! Kwani hujasikia au hutaki? Au hufahamu kwamba wewe ni malaya?”
“Cleopatra mimi ni malaya?”
“Tena mchafu!”

“Ok! Ahsante sana, ahsante sana mama, sikuja kwa ugomvi, nilikuja kwa ajili ya kumsalimia mgonjwa!”
“Mgonjwa?”
“Ndiyo Deo!”
“Anakuhusu nini Deo?”

“Ni boyfriend wangu wa zamani, kwahiyo sina tatizo kuja kumsalimia akipata matatizo!”
“Kwanza aliyekupa taarifa za Deo kuumwa ni nani? Tena haraka kiasi hicho?”
“Unataka kumjua?”
“Ndiyo!”

“Ipo siku utamjua, lakini kwa leo hupaswi kumjua...kwaheri...kwa mara nyingine tena Deo pole sana mwaya, najua unaumia na una maumivu mawili! Ya kuugua, lakini pia una maumivu ya kusogeza ndoa yako mbele, pole sana...” akasema Levina na kuanza kupiga hatua kuondoka pale kwenye kitanda cha Deo.

Deo hakuzungumza chochote, Cleopatra naye hakuwa na la kuzungumza zaidi ya kumsindikiza kwa macho mpaka alipopotea mbele ya macho yake. Akamgeukia Deo aliyekuwa ameyatoa macho yake kwa kukata tamaa kabisa. Akapiga magoti pale na kumbusu usoni mwake.

“Pole mwaya Deo wangu!”
“Ahsante...” akaitikia Deo kwa taabu kidogo.
“Unajisikiaje sasa?”
“Nina nafuu!”

“Utapona mpenzi wangu, naamini hadi siku ya ndoa yetu utakuwa umeshapona kabisa na utaweza kwenda kanisani kutimiza ahadi yetu ya muda mrefu!”
“Siamini Cleopatra!”
“Kwanini?”
“Nakufa Patra, nakufa mpenzi wangu!”

“Hapana baby, usife kwanza mpenzi wangu kabla hatujafunga ndoa yetu...subiri kidogo mpenzi wangu, unioe kwanza...” akasema Cleopatra akilengwa na machozi machoni mwake.

“Siamini kama nitapona mpenzi, moyo wangu una maumivu makali sana, lakini hata mwili wangu naona unauma, sioni tumaini kabisa, nakufa mpenzi wangu!”
“Hufi baba!”
“Nakufa!”

“Usife kwanza mpenzi wangu, nakupenda Deo!”
Deo hakujibu kitu, alikuwa na mambo mengi sana kichwani mwake. Alikuwa na maumivu ya kupigwa risasi, lakini pia alikuwa na maumivu na ndoa yake na Cleopatra!

Alimkumbuka sana Levina, kila alipojaribu kukumbuka sababu ya kuachana kwao, hakuona kama alistahili!
Akazidi kulia.
“Unalia nini mpenzi wangu?” Cleopatra akauliza.
“Maumivu mpenzi!”

“Pole sana!”
“Ahsante!”
“Hivi dokta ameshakuja kukuona?”
“Sijajua!”
“Namaanisha baada ya kuzinduka!”
“Hapana.”

“Ngoja niende kumwita mara moja,” Cleopatra akasema na kusimama mara moja kisha kwenda ofisini kwa daktari.
Muda mfupi baadaye daktari alikuwa ameshafika kitandani kwa Deo na kuanza kumpima na kumjulia hali yake.
“Pole sana Deo, unajisikiaje sasa?” Dokta akamwuliza.
“Kidogo nina nafuu.”

“Usijali, kilichotokea ni mshtuko tu, hujaumia sana, utakuwa sawa wala usiwe na hofu!”
“Lakini dokta kama nilivyokuambia, wiki tatu zijazo tunafunga ndoa, anaweza kuwa ameshapona kabisa?”

“Bila shaka, tutajitahidi kadri ya uwezo wetu, maadamu yupo chini yetu, kila kitu kitakuwa sawa, kikubwa ni kumuomba Mungu tu!”
“Ahsante sana, naweza kumpa chakula kwa sasa?”
“Umemletea nini?”
“Ndizi nyama!”

“Sawa, lakini hakikisha anakula chakula laini na chenye kumpa hamu ya kula. Unaweza kumpa.”
“Ahsante Dokta.”
Dokta Pallangyo akaondoka zake na kumuacha Cleopatra akiwa na mgonjwa wake. Akatayarisha chakula na kuanza kumlisha kwa upendo.

“Nakupenda sana Deo wangu, sipo tayari kukupoteza katika maisha yangu, usijali utapona!”
“Ahsante mpenzi wangu kwa kunipa moyo!”

Muda wa kuwaona wagonjwa ulipoisha, Cleopatra alitakiwa kuondoka na kumuacha Deo peke yake, jambo ambalo lilimuhuzunisha sana. Moyo wake uliumizwa sana na jambo hilo, lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kuondoka!
“Nitakuja kukuona mpenzi wangu, ugua pole na ulale salama.”

“Ahsante, msalimie mama!”
“Sawa, nitamsalimia.”
Akaondoka.

***
Macho yake yalikuwa yanagoma kufumbuka kabisa, alihisi kama yanauma kwa mbali, hata hivyo hakuwa na tatizo la macho, alikuwa na tatizo la bega, lakini macho yake yalikuwa yakipambana na nuru ya asubuhi baada ya kuzoea giza kwa usiku mzima.

Akajilazimisha kuyafumbua, akayafumbua kwa tabu kidogo. Alipofumbua tu, akakutanisha macho yake na sura ambayo haikuwa ngeni kwake hata kidogo. Alimfahamu vizuri sana msichana aliyekuwa amesimama mbele yake.
Alikuwa ni Levina!

“Habari za asubuhi Deo? Samahani nimekuja kukusalimia, nimefika mapema sana hapa, lakini sikuona sababu ya kukusumbua katika usingizi, ndipo nikaamua kukusubiri uamke mwenyewe...pole sana,” akasema Levina akiweka uaridi jekundu mezani kwa Deo.

“Ahsante Levina!”
“Unajua kwanini nimekuja mapema yote hii?”
Deo hakujibu kitu, alitingisha kichwa kuashiria kwamba hakujua sababu.

“Nilitaka kuwa wa kwanza kuijua hali yako baada ya kuamka leo, lakini pia nilitaka kukuthibitishia kwamba huyo Cleopatra wako hakupendi kama anavyokudanganya, kama angekuwa anakupenda asingeweza kulala usingizi ukiwa wewe unaumwa, alipaswa awahi kukuona...upo hapo?” Akasema Levina akimwangalia Deo usoni.

Deo hakujibu kitu!
Akabaki anashangaa, akiwa katika hali ya mshangao huo, akamuona Cleopatra akiwa anaingia wodini. Sekunde chache baadaye alikuwa amesimama mbele yake.

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia
 
USIFE KWANZA MPENZI WANGU....... EPISODE..23.

Levina amekuwa wa kwanza kufika hospitalini kumwona Deo akiwa na uaridi mkononi mwake. Anaeleza hisia zake jinsi alivyokuwa akimpenda. Akiwa amesimama pale Cleopatra akaingia wodini akitembea kwa kunyata, baadaye anafika na kusimama mbele ya kitanda chake! Sasa endelea...

ALIONEKANA kabisa kuchukizwa na kitendo cha Levina kufika hospitalini kumuona Deo, tena kabla yake. Akamwangalia Levina kwa macho yaliyojaa hasira sana, akabenua midomo na kurudisha macho yake kwa Deo aliyekuwa pale kitandani. Akamwonea imani.

"Lakini Levina unatafuta nini kwangu?" Cleopatra akamwuliza.
"Kivipi?'
"Hujui?"

"Nimekuuliza kivipi? Mtu anayeuliza maana yake ni kwamba hajui; mimi sijui ndiyo maana nakuuliza. Haya niambie kivipi?"
"Kwanini unakuja kumwangalia mpenzi wangu?"
"Kuna ubaya gani?"
"Ubaya upo?"

"Upi?"
Cleopatra akakaa kimya!
Ni wazi kwamba hakuwa na jibu la haraka na la moja kwa moja. Maana ni kweli hakukuwa na ubaya katika kumjulia hali mgonjwa.

"…najua unaogopa kusalitiwa? Ni kweli?" Levina akamwuliza akimwangalia usoni.
Cleopatra akaendelea kubaki kimya.
"Mbona kimya? Unaogopa nitakuibia Deo wako siyo?"
"Ndiyo!"

"Lazima uwe na woga huo….lazima…tena ni kawaida kabisa. Maana siku zote mwizi huwa na hofu sana ya kuibiwa…kwasababu wewe ni mwizi wa waume za watu, ndiyo maana unahofia nitakuibia, mwanamke huna haya kabisa…hivi unajua nilimtoa wapi Deo? Alikuwaje na nilifanya nini hadi ukamkuta akiwa katika hali hii?

"Unajua? Leo unajifanya unampenda, unajua alikuwaje kabla hajaanza kukuvutia? Unajua hali aliyokuwanayo kabla ya kuwa handsome na kupata kazi nzuri? Wewe ni mpumbavu sana mtoto wa kike.

Kwa taarifa yako sina haja na Deo tena, ninachokifanya hapa ni ustaarabu tu wa kuja kumjulia hali kama binadamu mwingine, si zaidi ya hapo. Mwone alivyo na sura ya huruma? Utadhani ni mkarimu kumbe muuaji mkubwa!" Akasema Levina kisha akashika njia ya kutokea nje.

Cleopatra akabakia akimwangalia Levina anavyoishia.
"Amekuambia nini?" Cleopatra akamwuliza Deo aliyekuwa amelala kimya kitandani.
"Amenipa pole!"
"Kingine?"

"Kaniletea ua!"
"Amesema kuwa anakupenda?"
"Hapana."
"Wewe unahisi nini?"

"Kwakweli siwezi kujua, lakini naona kikubwa hapa ni mimi na moyo wangu. Sidhani kama nitabadilisha uamuzi wangu. Bado wewe ni wangu, nitafunga ndoa na wewe. Nakupenda sana Cleopatra, usiwe na wasiwasi na hilo mama, nakupenda sana."
"Kweli?"

"Niamini."
Cleopatra akainama pale kitandani kisha akamwangushia busu mwanana shavuni mwake, machozi yakaanza kumiminika kama maji.

"Naomba asikudanganye kwa lolote, nakupenda mpenzi, lazima tutimize dhamira yetu."
"Usijali mpenzi wangu."
Akamnywesha uji na kumpa matunda akala. Muda wa kuwaona wagonjwa ulivyoisha, akaaga na kuondoka zake.

***
Ilikuwa asubuhi mbaya zaidi kwa Deo, zaidi ya jana yake. Alikuwa akimuwaza sana Levina. Tena safari hii alikuwa akimuwaza kama mwanamke asiye na hatia. Ni kweli hakuwa na sababu za kumuacha na kutaka kuoana na Cleopatra. Kulikuwa hakuna njia yoyote ya kubadilisha kilichokuwa mbele yake, ni kweli alikuwa anakwenda kufunga ndoa na Cleopatra.

Tena wiki mbili na siku chache baadaye. Tayari ndoa ilikuwa imeshatangazwa kanisani, kwahiyo isingekuwa rahisi hata kidogo kughairi. Akayatupa macho yake juu ya dari, mawazo tele yakamjaa. Kwa hakika alimkumbuka sana Levina. Mawazo yake yakarudi asubuhi ile ya fumanizi.

Siku ambayo alifukuzwa na mzee Massamu nyumbani kwao na Levina. Akaikumbuka siku hiyo na mtiririko wa matukio mengine mengi yaliyoonesha mapenzi ya dhati kutoka kwa Levina. Matukio yale yakashuka kama sinema ya kusisimua…
Akakumbuka vizuri…

***
Kitu cha kwanza Deo kufanya alipofika Magomeni kwenye mataa, ilikuwa ni kumpigia simu Levina, lakini simu yake ilikuwa haipatikani. Akarudia tena na tena, lakini jibu liliendelea kuwa lile lile, haipatikani! Akachanganyikiwa.

Hapo akajua alitakiwa kuanza maisha yake mapya, ambayo kwa vyovyote yangekuwa ya tabu na shida nyingi! Hakuwa na jinsi ndivyo hali halisi ilivyokuwa…na alitakiwa kukabiliana nayo!

Hakuwa na kitu kingine chochote zaidi ya begi lake dogo mgongoni lililokuwa limehifadhi nguo zake. Ndani ya begi hilo, pia alikuwa na kiasi cha shilingi laki mbili na arobaini elfu, alizokuwa amezihifadhi wakati akifanya kazi ya kuuza mchele sokoni Tandale! Alikuwa na mawazo tele kichwani, huku akikosa uamuzi wa muelekeo.

Alisimama pembeni mwa sheli, karibu kabisa na geti la kuingia katika Hoteli ya Travertine. Akaangalia barabara nne, moja ya Kawawa ikitokea Ilala kwenda Kinondoni, nyingine ya Morogoro ikitokea Ubungo kuelekea Posta.

Akaanza kuwaza atumie ipi? Aende wapi? Kwa nani?
Hakuwa na majibu ya haraka ya wapi aelekee, lakini kikubwa zaidi ni kwamba, aliumizwa sana na kitendo cha kuingia kwenye mateso kwa sababu ya starehe ya usiku mmoja. Hilo lilimchoma sana moyo wake.

"Lakini nilimwambia Levina hakusikia…sasa ona sasa sina kazi, nabaki nahangaika," akawaza Deo, lakini hilo haikuwa dawa.

Alitakiwa kujua anaelekea wapi baada ya tukio hilo. Wazo lililoingia haraka kichwani mwake ni kwenda kutafuta kwanza gesti kwa ajili ya kujibanza kwa siku kadhaa wakati akitafuta kazi. Sehemu pekee ambayo aliamini angepata chumba cha bei nafuu ni Manzese.

Akaingia kwenye gari la Ubungo, akashukia Manzese – Tip Top na kukata mitaa, akakodisha gesti ya elfu mbili kwa siku!
"Utakaa siku ngapi?" Mhudumu akamwuliza.

"Kwasasa nitakulipa elfu kumi kwa ajili ya siku tano, kama nitaendelea nitakuongeza pesa nyingine."
"Sawa, nenda namba sita."
"Ahsante sana."

Deo akaondoka na kwenda kufungua mlango wa chumba namba sita kama alivyoelekezwa, akaingia na kujitupa kitandani. Mawazo tele kichwani mwake. Akiwa bado hajatulia vizuri, simu yake ikaanza kuita, akaichukua haraka, jina lilioonekana kwenye kioo, lilikuwa la Levina.
Akapokea.

"Umeridhika sasa siyo? Naamini roho yako ipo kwatu sasa…" akasema Deo kwa sauti iliyojaa hasira kwenye simu.
"Niridhike na nini Deo?"
"Kunisababisha nifukuzwe kazi? Sasa maisha yangu yameharibika kama ulivyokuwa unataka siyo?"

"Sina maana hiyo Deo, kumbuka kwamba mimi nakupenda na sipo tayari kuona maisha yako yanaharibika. Ndiyo maana nimekupigia simu, kwanza uko wapi? Nataka kukutana na wewe!"

"Kukutana na mimi?"
"Ndiyo!"
"Unataka nini kwangu?"
"Ni juu ya maisha yako. Nia yangu ilikuwa kukusaidia, bado nahitaji kukusaidia."
Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia





USIFE KWANZA MPENZI WANGU.....EPISODE .24.

Licha ya Levina kumsababishia afukuzwe kazi, bado Deo hakati tamaa ya maisha na anaendelea kujipa moyo kuwa ipo siku mambo yake yatatulia.

Levina analazimika kufanya kazi ya ziada ili kubadili fikra za Deo anayemchukulia kama mtu aliyepania kumharibia maisha yake. Baada ya kumshawishi kwa muda mrefu, Deo anakubali kukutana tena na Levina na wanajikuta wakifungua ukurasa mpya katika maisha yao. Endelea mwenyewe…

Kitendo cha kupoteza kazi kwa sababu ya mapenzi kilikuwa ni pigo lililomgharimu Deo kwa kiasi kikubwa. Kumbukumbu za yote aliyofanya na Levina ilikuwa ikipita kichwani mwake mithili ya mkanda wa sinema ya kusisimua, hakuamini kuwa kila kitu kimeharibika na kufikia mwisho kwa sababu ya mapenzi.

Wakati hayo yakiendelea kupita kichwani mwake, alikuwa akifikiria juu ya ombi la Levina kutaka kukutana naye tena.
"Unataka nini kwangu? Deo alirudia kuuliza swali lile, na majibu ya Levina yakawa ni yaleyale, kwamba alikuwa akimpenda na alikuwa tayari kumsaidia.

"Siwezi kukuruhusu unione tena, najua lengo lako ni kuniharibia maisha yangu, niache nife peke yangu ili ufurahi."

"Usiseme hivyo Deo, lengo langu ni kukusaidia na sitokata tamaa mpaka hapo nitakapofanikiwa," alijibu Levina kwa sauti iliyoonesha kuwa alikuwa akilia kwa uchungu. Mazungumzo kwa njia ya simu yaliendelea lakini msimamo wa Deo ukawa ule ule, hakutaka kuonana tena na Levina.

Deo akiwa amejilaza pale kitandani, aliendelea kusanifu mandhari ya chumba kile cha kulala wageni alichofikia. Kwa hakika hakuwa na hadhi ya kukaa kwenye chumba kama kile, ila kutokana na yaliyomsibu aliamua kuvumilia na kuyaacha yote yapite.

Usiku wa siku ile aliuona kama mwaka mzima kwani mpaka kunapambazuka alikuwa hajapata hata tone la usingizi. Kulipopambazuka tu, Deo aliinuka pale kitandani na kwenda kupiga mswaki, lakini kabla hajatoka, simu yake iliita tena na alipoitazama aligundua kuwa ni Levina ndiye aliyekuwa akipiga. Aliitazama simu ile bila kuipokea kwa dakika kadhaa hadi ilipokatika.

"Anataka nini kwangu? Sihitaji tena kuwa na mpenzi, bora peke yangu," alijisemea Deo kimoyomoyo. Akiwa bado anatafakari, simu ya Levina iliingia tena, akaipokea kwa jazba…

"Si nilishakwambia uniache Levina? Sitaki uendelee kunifuatilia tafadhali," kabla Deo hajamaliza Levina alimkata kauli…

"Najua unanichukia sana Deo kwa yaliyotokea, lakini amini nakuambia ipo siku utaelewa kuwa nina lengo zuri sana na wewe. Naomba unielekeze mahali ulipo, nina jambo muhimu sana la kukuambia ambalo ni lazima nikuambie leo," aliongea Levina kwa hisia, jambo lililomfanya Deo arudishe moyo nyuma.

"Njoo mpaka Manzese, mwambie konda akushushe Tiptop."
"Nakuja na usafiri binafsi, wala usihofu na nitakuwa hapo baada ya muda mfupi," alijibu Levina kwa furaha na akaanza kujiandaa.

"Jamani Deo, nisamehe kwa yote yaliyotokea, nakupenda na niko tayari kukufanyia lolote, amini kuwa sina lengo la kukuharibia maisha yako," alianza kujitetea Levina mara baada ya kufika Manzese alikoelekezwa na Deo.

Kitendo cha kumkuta akiwa amepanga chumba katika gesti chafu, yenye mashuka machafu na kitanda kibovu huku dari na kuta zikiwa katika hali mbaya kilimuumiza sana Levina, akashindwa kuificha huzuni yake.

"Siridhishwi na wewe kuishi mahali hapa, kuonesha kuwa kweli nimepania kukusaidia nataka nikutafutie nyumba nzuri ili tupange vizuri malengo ya maisha yetu ya baadaye," aliongea Levina huku akiwa amemkumbatia Deo.

Baada ya mazungumzo ya kina yaliyochukua muda mrefu, Deo alikubali msaada wa Levina na wakatoka kwa ajili ya kwenda kutafuta nyumba ya kupanga.

Kwa msaada wa madalali aliokuwa akifahamiana nao, walifanikiwa kupata nyumba nzuri ya kuishi maeneo ya Sinza Bwawani, wakakamilisha malipo ya kodi ya mwaka mzima iliyotolewa na Levina ‘cash', kisha mipango ya kuhamia makazi mapya ikaanza kufanywa mara moja.

"Mimi nafikiri tukitoka hapa tukanunue kitanda na godoro zuri, kisha vitu vingine vidogo vidogo vitafuata," alisema Levina.

"Sawa mama, mimi nakusikiliza wewe."
Mpaka jioni ya siku ile inafika, tayari Deo alishanunuliwa vitu vyote muhimu vya kuanzia maisha vikiwemo kitanda kizuri na godoro, meza, zulia na viti. Deo akaanza maisha mapya. Angalau sasa alianza kuamini kuwa Levina alikuwa na mapenzi ya dhati kwake.

Maisha yakawa yanasonga mbele huku mapenzi kati ya Deo na Levina yakizidi kuchanua siku baada ya siku. Ikafika mahali Deo akayasahau machungu yote aliyopitia maishani mwake, akawa anazifukuzia ndoto zake zilizoonekana kupotea kwa kipindi kirefu.

"Uliwahi kuniambia kuwa una malengo ya kujiendeleza kimasomo, huoni kuwa huu ni muda muafaka," Levina alimuuliza Deo wakiwa faragha.

"Ni kweli baby, lakini naona kama nitakuwa nakupa mzigo mkubwa sana, natamani kuja kuwa mhasibu lakini kila nikitazama naona kama kuna kazi nzito mbele yangu."

"Wala usihofu Deo, nilishakwambia kuwa nataka kuyabadili maisha yako, amini nakwambia kuwa nitashughulikia masuala yote ya wewe kuanza masomo, cha msingi jiweke tayari.
"Hamna shida sweet, sitakuangusha."

Siku chache baadaye Deo akaandikishwa kuanza rasmi masomo ya muda mfupi (Qualifying Test) ili kujiweka tayari kabla ya kujiunga na chuo cha Uhasibu kwani ndoto zake zilikuwa ni kuja kuwa mhasibu.

Deo akayaanza maisha mapya ya uanafunzi. Licha ya kwamba umri wake ulikuwa mkubwa, hakuona aibu kujichanganya na vijana wadogo katika masomo ya elimu ya sekondari kwa muda mfupi (QT).

Hiyo ilimpa nguvu kubwa kwani hatimaye alikuwa akielekea kutimiza ndoto zake za siku nyingi kwa msaada mkubwa wa Levina. Aliahidi kumpenda na kumfanyia mema Levina kwani aliyoyafanya kwa ajili yake hayakuwa na kifani.









USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE..25.

Deo na Levina wameanza ukurasa mpya wa maisha yao ya kimapenzi kiasi cha kusahau yote yaliyowahi kuwasibu. Kwa msaada mkubwa wa Levina, Deo anaanza maisha mapya akiwa katika makazi mapya na anajitahidi kuzifukuzia ndoto zake, hasa ya kusoma na kupata kazi, lakini ghafla mambo yanaanza kubadilika. Shuka nayo…

Deo aliendelea na masomo ya kujiendeleza na akawa anaonesha juhudi kubwa katika kila anachokifanya. Alijiapiza kuwa ataendelea kumpenda na kumheshimu Levina kwa maisha yake yote kwani alimbadilisha kabisa.

Kutokana na juhudi alizozionesha kwenye masomo, haikumchukua muda Deo akawa na uwezo wa kufanya vizuri mitihani na kujibu maswali kwa ufasaha mkubwa, hali iliyomfanya awe kivutio kikubwa kwa wanafunzi wenzake.

Wasichana wengi walianza kumshobokea na kujifanya wanataka awafundishe. Kwa kuwa alishajiwekea nadhiri ya kutomsaliti Levina, alikaa nao mbali.

Maisha yalizidi kusonga na hatimaye Deo akamaliza masomo yake kwa mafanikio makubwa. Alifaulu vizuri mtihani wake na kupata vyeti vilivyomuwezesha kujiunga na Chuo cha Uhasibu cha Planet Link Accountancy ambako alisomea stashahada ya uhasibu.

Kwa kipindi chote hiki maisha ya kimapenzi kati yake na Levina yalikuwa yakizidi kupamba moto siku baada ya siku.

"Deo malengo yako si yanakaribia kutimia? Bila shaka haitakuwa vibaya tukianza kufikiria kujenga familia yetu, au unasemaje?"
"Ni kweli sweet, lakini kwanini tusisubiri nimalize kabisa halafu nikishapata kazi ndiyo tuanze kufikiria hayo?"

"Unajua mimi ni mwanamke niliyekamilika, siwezi kuendelea kukaa hivihivi, wenzangu wataanza kunicheka kwamba sizai, mi nataka nikuzalie mtoto wakati wewe unaendelea na masomo yako," alisema Levina kwa sauti ya mahaba akiwa amejilaza kifuani kwa Deo.

Licha ya Deo kukwepakwepa, lakini hatimaye aliukubali ushauri wa Levina, wa kutafuta mtoto wa kuupamba uhusiano wao.
"Lakini huoni kwamba litakuwa tatizo kuzaa kabla hatujafunga pingu za maisha," alihoji Deo huku akizichezea nywele za Levina wakiwa kitandani.

"Sidhani kama hili litakuwa tatizo, nimehiyari mwenyewe na hakuna wa kunizuia. Nakupenda sana Deo."

***

MIAKA MITATU BAADAYE
Deo alifanikiwa kumaliza salama masomo yake na kupata kazi kama mhasibu wa Kampuni ya Usafirishaji Mizigo ya Snox Carries LTD ya jijini Dar es Salaam. Kwa upande wa Levina tayari alishajifungua mtoto wa kike aliyekuwa na umri wa mwaka mmoja na miezi kadhaa, waliyempa jina la Precious wakiwa na maana ya kitu cha thamani.

Baada ya kupata mtoto, maisha yalibadilika sana na sasa wakawa wanatumia muda mwingi kumuhudumia na kumfikiria mtoto wao kuliko wanavyojijali wao.

Deo alikuwa akirudi nyumbani kutoka kazini anamsaidia mkewe malezi ya mtoto wao Precious. Pesa walizopata walizitumia pamoja kufanya mambo mbalimbali ya kimaendeleo. Maisha yao kwa ujumla yalibadilika na usingeweza kudhani kuwa huyu ndiye Deo wa miaka ile.

"Levina! Nadhani sasa wewe ni mke wangu na nina mamlaka yote juu yako na wewe una mamlaka juu yangu," aliongea Deo jioni moja wakiwa wanapunga upepo kwenye bustani ya maua nje ya nyumba wanayoishi.

"Ni kweli mume wangu!"
"Lakini mbona siku hizi hutaki mimi niguse simu yako kama zamani, unapigiwa simu usiku halafu unaenda kupokelea nje na wakati mwingine unaikata mbele ya macho yangu, tatizo nini?"

"Wewe nawe kwa wivuu! Hakuna anayekuzidi mume wangu kwa kila kitu, siwezi kutoka nje na kukusaliti, amini nakwambia Deo, mimi ni wako peke yako…" alisema Levina huku akimsugua sugua mumewe mgongoni kimahaba.

Licha ya kujibiwa hivyo, Deo alibaki na dukuduku moyoni kwani mabadiliko ya mkewe yalishaanza kumtia hofu. Tangu mkewe aache kunyonyesha miezi michache iliyopita, alianza tabia za ajabu ambazo zilimfanya ahisi anaibiwa mali zake. Mkewe alikuwa akichelewa kurudi nyumbani bila sababu za kueleweka, na alipokuwa akimuuliza kisingizio kikubwa kilikuwa ni ubize wa kazi.

Siku nyingine alikuwa akirudi nyumbani ananukia pombe, hali iliyotoa ishara kuwa tayari mwenzake anamsaliti. Shughuli zote za kumlea mtoto zikabaki kwa Deo na msichana wa kazi aliyetafutwa kwa lazima baada ya kuona Levina ameanza kubadilika. Ilifika mahali hata suala la kufurahishana faragha likaanza kupungua taratibu.

"Najua umenisaidia sana maishani Levina, Bila wewe nisingekuwa hapa nilipo leo, lakini kaa ukitambua kuwa mabadiliko yako ya tabia unayonionesha kwa sasa yanauumiza sana mtima wangu.

"Kama kuna kosa nililokuudhi niambie na naahidi nitajirekebisha kwani bado nakuhitaji Levina wangu." Uzalendo ulishaanza kumshinda Deo, ikafika mahali akawa anamwaga machozi mbele ya mkewe akimsihi ajirudi kama alivyokuwa hapo mwanzo.

Jibu la Levina siku zote lilikuwa ni kwamba anampenda Deo na kamwe hawezi kumsaliti, lakini kumbe nyuma ya pazia alikuwa akimfanyia mambo ya kusikitisha sana.

Usiku mmoja, Deo akiwa na mwanae mdogo Precious sebuleni, mkewe alichelewa kurudi, na hata aliporudi saa tano usiku alikuwa akipepesuka na kunuka pombe. Alipoingia ndani, aliweka simu yake mezani na kupitiliza bafuni kwenda kuoga.

Akiwa bafuni, ujumbe mfupi wa simu uliingia kwenye simu yake, Deo akaiwahi na kuichukua kutaka kujua ni nani aliyemtumia meseji mkewe usiku wote ule.

Alipoifungua na kuisoma, hakuamini macho yake…akarudia kuisoma tena… akajikuta mwili wote ukiishiwa nguvu. Wakati anaisoma kwa mara ya tatu, mkewe akawa anatoka bafuni. Macho yao yakagongana.


USIFE KWANZA MPENZI WANGU....EPISODE.26.

Baada ya Deo kufukuzwa nyumbani kwa akina mzee Massamu Magomeni, ameamua kwenda kuanza maisha mapya katika gesti moja iliyopo Manzese Tip Top. Levina amewasiliana naye na amefika hadi kwenye gesti hiyo ambapo ameonesha nia yake ya kumsaidia.

Tayari ameshampangia nyumba yenye vyumba viwili, Sinza. Deo amesoma elimu ya sekondari kwa miaka miwili na baada ya hapo akasomea masomo ya Uhasibu katika chuo kimoja jijini Dar.

Akiwa anaendelea na masomo, Levina anamweleza Deo nia yake ya kuzaa mtoto, lakini jambo hilo Deo anapingana nalo. Je, nini kitatokea? Endelea...

SUALA la kuzaa na Levina lilikataa kabisa kupenya kwenye ubongo wa Deo, alijaribu kuvuta picha ya miaka mitatu ijayo akaona hatari kubwa kuzaa na Levina. Hakujua ilikuwaje, lakini akahisi kwamba Levina angeweza kubadilika na kumsababishia jakamoyo la mapenzi moyoni mwake.

Aliona kuzaa naye, ingekuwa tiketi ya kuingia kwenye matatizo, lakini pia aliona wazi vita iliyokuwa mbele yake ikimuhusisha yeye na wazazi wa Levina. Hilo hakutaka kabisa litokee.

"Levina haiwezekani, kama nilivyokuambia siwezi kuzaa na wewe!"
"Kwanini unanifikiria vibaya lakini?"
"Vipi?"

"Kwamba nitakusaliti?"
"Ni kweli, lazima baadaye utanigeuka na kuninyanyasa."
"Kwanini unahisi hivyo?"

"Lakini kwani ni vibaya kukueleza hisia zangu? Nilichokifanya ni kukueleza nilichokuwa nahisi kichwani mwangu. Sijui kwanini sina amani na wewe, nahisi matatizo tupu kuendelea na wewe katika uhusiano huu tena na kuzaa."

"Mh! Siamini kama huniamini kwa kiwango hicho?"
"Siyo hivyo Levina, nawajua wanawake mimi, tena wale wanaotoka kwenye familia za kitajiri."
"Unajua nini sasa?"

"Sikiliza nikuambie Levina, wewe mpaka sasa hivi unaishi kwenu na unatambua kabisa kwamba nilifukuzwa kwenu baada ya kugundulika nina uhusiano na wewe, unadhani baba yako akigundua kwamba una mimba yangu itakuwaje?"

"Lakini atakayekuwa amebeba mimba ni mimi au yeye?"
"Ni wewe ndiyo, lakini atakayepata matatizo ni mimi!"
"Basi tuachane na hayo mpenzi wangu, tatizo si kuhusu mtoto tu siyo?"
"Ndivyo!"

"Basi huo mjadala tuukatishe kwasasa tusiharibu penzi letu kwa jambo dogo, mambo mengine tutajua baadaye!"
"Sawa."
"Enhee lini sasa utakuja kulala kwangu?"
"Kwahiyo ndiyo unanifukuza au?"

"Sina maana hiyo, muda utakaoondoka, si vibaya lakini hata nikikuambia muda huu. Hapa ni kwako mama."
"Ahsante sana mpenzi kwa maneno yako matamu!"
"Nakupenda sana Levina wangu!"

"Nakupenda pia Deo!"
"Lakini bado hujaniambia ni lini utakuja kulala kabisa hapa?"
"Mh! Mpaka nipange safari ya uongo...acha nifikirie kwanza nitakujulisha mpenzi wangu!"

"Sawa mama!"
Waliendelea na mazungumzo hadi saa mbili za usiku, ndipo Levina alipoondoka Sinza kuelekea nyumbani kwao Magomeni.

***
Usiku mzima Deo aliendelea kufikiria kuhusu Levina, alishindwa kuelewa ni kwanini mawazo yake yalienda mbali kiasi kile. Hakujua ni kwanini aliwaza kusalitiwa na mwanamke ambaye amekuwa chachu ya mafanikio yake.
Hata hivyo, alijitahidi kuubembeleza usingizi hadi alipofanikiwa kulala.

***
Levina aliendelea kuwa msada mkubwa sana katika maisha ya Deo. Alimsaidia kwa kila kitu kwa siri, alifanya uhusiano wao kuwa siri kubwa, kwani wazazi wake wasingekubali awe katika uhusiano naye wakati hali ya maisha yake ikiwa chini sana.

Alihakikisha anaendelea kufanya kazi kwa bidii, mtaji wake haushuki na badala yake faida inazidi kuongezeka. Jambo hilo lilizidi kuwafurahisha wazazi wake, kwani alionekana msichana mwenye bidii kubwa katika kazi zake.

Siku moja aliamua kuvunja ukimya kwa kuamua kumshirikisha mama yake kuhusu uhusiano wake na Deo. Ilikuwa kazi ngumu sana lakini ilikuwa lazima amweleza ukweli ili kujua kama mama yake angemuunga mkono. Ilikuwa Jumamosi, ambapo mzee Massamu alikuwa kazini.

"Mama kuna kitu nataka kukuambia muda mrefu sana lakini nashindwa, ila naona leo ni muda muafaka wa kukuambia."
"Ni nini mwanangu?"
"Mama nina mpenzi ambaye nataka kumtambulisha hapa nyumbani."
"Umeanza lini tena hayo mambo mwanangu?"

"Lakini muda umefika mama, umri wangu unaniruhusu!"
"Sawa, ni nani huyo mwanaume mwenyewe!"
"Unamaanisha nini?"
"Ni wa hapa mtaani kwetu?"
"Hapana!"

"Ni wa wapi?"
"Kwasasa anaishi Sinza."
"Sawa, kama ni kijana mwenye heshima zake na mmependana, mwambie atume ujumbe wa wazee tutawasikiliza, lakini chunga asije kuwa ni mzururaji asiye na mpango mzuri na maisha yako ya baadaye!"

"Hapana si mzururaji, lakini sidhani kama mtamkubali!"
"Kwanini?"
"Ni Deo mama!"
"Deo?"
"Ndiyo!"

"Deo gani?"
"Yule aliyekuwa akifanya kazi hapa nyumbani?"
"Wewe una kichaa kabisa, baba yako hawezi kukubaliana na hilo jambo, yaani unataka kuolewa na houseboy?"
"Hapana si houseboy tena, sasa anamalizia masomo yake ya Uhasibu!"
"Lini alianza kusoma?"

"Tangu kipindi kile, nilikutana naye akasema kwamba kuna mfadhili amejitolea kumsaidia, ndiyo huyo anayemlipia mpaka sasa hivi!"
"Kwa ninavyomjua baba yako, sijui kama atakubaliana na wewe."
"Ndiyo maana nimeoomba msaada wako mama, nampenda sana Deo!"

"Nitajaribu kuongea naye, ingawa sina uhakika kabisa kama atakubaliana na jambo hili!"
"Nisaidie mama!"
"Nitajaribu!"

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua baadae ...............





 
[h=1]Usife kwanza mpenzi wangu (27).....[/h]Penzi la Levina na Deo linazidi kunoga kiasi cha Levina kuamua kumweleza mama yake na kumwomba amuweke sawa baba yake mzee Massamu. Inakuwa vigumu mama yake kumwelewa, lakini anaahidi kujitahidi kuzungumza naye, mtihani ambao ni mgumu zaidi. Je, atakubaliwa? Endelea...

JIONI baada ya chakula cha usiku Levina aliingia chumbani kwake kulala na kuwaacha wazazi wake sebuleni wakiendelea kuangalia runinga. Mama Levina alionekana kuwa na jambo alilotaka kumwambia mumewe lakini alikuwa anasita.

Mzee Massamu aliweza kugundua hilo kupitia macho yake. Kila kitu kilionekana wazi kwamba ana jambo alilotaka kusema, lakini alikuwa akisita sana.
"Mama Levina mke wangu, uko sawa?"

"Kwanini?"
"Nahisi kama kuna kitu unataka kuniambia!"
"Ni kweli!"
"Sema basi, kwanini unakaa na jambo wakati wa kuniambia nipo hapa?"

"Ni kuhusu binti yetu Levina."
"Amefanyaje tena?"
"Mh! Eti amepata mchumba!"
"Amepata mchumba?"

"Ndiyo!"
"Sasa si amlete hapa nyumbani tuzungumze naye?"
"Tatizo siyo hilo!"
"Bali?"

"Tatizo ni huyo mtu mwenyewe."
"Kwani ana nini? Unafahamu?"
"Ndiyo namfahamu... hata wewe unamfahamu!"

"Kwa hiyo unataka kuniambia anaishi hapa hapa mtaani kwetu?"
"Sina maana hiyo... namaanisha Deo!"
"Deo?"
"Ndiyo!"

"Yule kijana aliyekuwa akifanya kazi hapa nikamtimua?"
"Ndiyo!"
"Bado wanaendelea na upumbavu wao? Hivi kwanini mwanao anataka kuniletea balaa katika familia yangu? Yaani yeye ni wa kuolewa na ‘Shamba Boy', mpuuzi asiye na mbele wala nyuma?"

"Lakini mwenyewe anasema eti alivyoondoka hapa alipata mfadhili, akamsomesha na sasa anamalizia Stashahada yake ya Uhasibu na Biashara!"

"Hata kama, mimi sitaki kumsikia kabisa yule kijana. Kwanza hana adabu, hawezi kufanya upumbavu ndani ya nyumba yangu.
Kwanza nenda kamwite Levina haraka sana!"

Mama Levina akasimama na kwenda chumbani kwa Levina, akamgongea na muda mfupi baadaye Levina alitoka.
"Baba yako anakuita!"
"Nakuja mama!"

Levina akatoka na kwenda sebuleni, alipokutana na uso wenye hasira kali wa baba yake akaanza kutetemeka. Kabla hata hajafungua kinywa chake kuongea chochote, tayari alikuwa na majibu kwamba ombi lake la kuolewa na Deo lilikuwa limekataliwa.

"Levina binti yangu, kwanini unataka kuniletea nuksi katika familia yangu? Kwanini unataka kuniabisha? Kwanini lakini?!" Mzee Massamu akauliza mfululizo.
"Kivipi baba?"

"Sitaki kuvuta maneno mengi, lakini ninachotaka kukuambia ni kwamba sitaki kusikia unaendelea na yule mpuuzi wako. Kama kweli mimi ni baba yako basi fahamu kwamba sitaki uwe na uhusiano na yule Deo, nimemaliza!"

"Lakini baba..." akasema Levina.
"Hakuna cha lakini... nenda kalale ‘please'!"
Levina hakuweza kubishana na baba yake, mara moja akainuka na kuelekea chumbani kwake. Baba yake alikuwa amekasirika sana na hakutaka kuendelea kumuudhi.

Alikuwa na maumivu makali sana moyoni mwake, kwani Deo alikuwa mwanaume ambaye alimpenda sana kwa moyo wake wote na hakutegemea kuolewa na mwanaume mwingine yeyote zaidi yake.

Aliingia ndani kwake kwa unyonge huku mawazo tele kichwani mwake yakimuandama. Muda mfupi baada ya yeye kuingia chumbani kwake, wazazi wake nao wakainuka na kuingia chumbani kwao.

***
Mzee Massamu hakufurahishwa kabisa na ujumbe wa mwanaye, hakutarajia kama bado angekuwa anaendelea na uhusiano na Deo, kijana ambaye kwake hakuwa na thamani kabisa.

"Mke wangu, zungumza na mwanao. Wewe ni mwanamke mwenzake kwa hiyo ni rahisi kukuelewa. Kifupi sitaki kusikia habari za huyo Deo!"

"Nimekuelewa mume wangu, nitajitahidi kuhakikisha anaelewa."
"Najua lipo ndani ya uwezo wako, naomba ufanye hivyo."
"Sawa."

***
Levina alipuuza maamuzi ya wazazi wake, pamoja na kwamba mama yake aliendelea kumsisitiza akatishe uhusiano wake na Deo, lakini alikaidi. Aliwahakikishia kwamba ameachana naye, lakini ukweli ni kwamba bado alikuwa na Deo.

Alikuwa akienda nyumbani kwake mara kwa mara na mwisho wa wiki alikuwa akitoka naye kwenda sehemu mbalimbali za burudani. Hata hivyo siri ya kwamba wazazi wake hawakutaka aendelee na uhusiano naye, iliendelea kuwa yake peke yake. Hakutaka kabisa kumshirikisha Deo.

Deo hakujua chochote kinachoendelea, lakini pia hakujua kama Levina alizungumza na wazazi wake kuhusu yeye. Aliendelea na masomo vizuri mpaka alipohitimu na kupata Stashahada yake. Hapo sasa ndipo alipotakiwa kutafuta kazi.

"Usihangaike mpenzi wangu, nitakutafutia. Kuna rafiki yangu mmoja anakaa Mbezi, hebu twende jioni tukazungumze naye, tuone uwezekano wa kupata kazi kwenye kampuni ya baba yake ambayo naye pia anafanya kazi hapo, tena ana cheo!"
"Sawa mpenzi."

Kama walivyokubaliana, jioni wakaenda Mbezi Beach nyumbani kwa huyo rafiki yake. Walipofika walipokelewa vizuri sana. Wakaamua kukaa nje kwenye bustani nzuri ya maua.
"Karibuni!"

"Ahsante sana!"
"Deo, kutana na rafiki yangu anaitwa Cleopatra. Nimesoma naye kunzia ‘O- Level' hadi ‘Advance', tumeshibana sana!" alisema Levina huku akimwangalia Cleopatra aliyekuwa akicheka.

"Cleopatra huyu hapa ni boyfriend wangu, anaitwa Deogratius lakini waweza kumuita Deo. Ndiyo huyu niliyekuwa nakuambia kuhusu ile ishu, amemaliza juzi tu, lakini kichwa chake ni mashine, kama akipata kazi kwenye kampuni yenu ataonyesha maajabu!"

"Nice to meet you Deo!" (Nimefurahi kukutana na wewe Deo) Akasema Clepatra wakipeana mikono.
"Me too!" (Hata mimi pia) Akajibu Deo akimwangalia kwa aibu.

Cleopatra akahisi kitu cha ajabu sana mwilini mwake, alihisi kama anaungua na moto mkali wa mahaba. Ghafla alijikuta akiwa mnyonge, Deo alimvutia sana.

Thamani ya urafiki wao haikuwa na maana sana, mawazo mapya yakauvamia ubongo wake.
"No! Lazima nimpate huyu kijana...tena ataanza kazi wiki hii, nitampanga kwenye kitengo changu, hapindui huyu..." akawaza akiendelea kuung'ang'ania mkono wake.

"Vipi shosti, mbona salamu imekuwa ya muda mrefu hivyo? Shemeji yako huyu ujue..." akasema Levina kwa utani, lakini moyoni alikuwa anamaanisha.
"Mwanamke kwa wivu wewe!!!" Akasema Cleopatra akimwachia mkono Deo.


Je, nini kitatokea katika ligi hii ya mapenzi? Usikose kufuatilia
 
[h=1]Usife kwanza mpenzi wangu (28)...[/h]Baada ya kufanikiwa kusoma na kumaliza masomo yake ya Stashahada ya Uhasibu na Biashara, Deo anasaidiwa na mpenzi wake, Levina kutafuta kazi. Harakati hizo zinawakutanisha na Cleopatra, rafiki wa siku nyingi wa Levina ambaye ni bosi kwenye kampuni ya baba yake.

Katika hali isiyo ya kawaida, Cleopatra anajikuta akivutiwa mno kimapenzi na Deo, na anajiwekea nadhiri ya kumpata. Je, nini kitaendelea?

Vipi shosti, mbona salamu imekuwa ya muda mrefu hivyo? Shemeji yako huyu ujue…" akasema Levina kwa utani, lakini moyoni alikuwa akimaanisha. Mwanamke kwa wivu wewe!" Akasema Cleopatra akimwachia mkono Deo.

Ukweli ambao Cleopatra alishindwa kuuficha mbele ya shoga yake wa siku nyingi Levina, ni kwamba alitokea kumzimikia ghafla Deo, na sasa alitamani kumpindua na kulionja penzi la Deo. Moyoni alijiwekea nadhiri kuwa lazima atafanya chochote kinachowezekana ilimradi ampate Deo.

Mazungumzo yaliendelea wakiwa kwenye bustani ya maua, nyumbani kwa akina Cleopatra, Mbezi Beach na kwa moyo mkunjufu akakubali kumpatia Deo kazi katika kampuni ya baba yake ambayo yeye ndiyo alikuwa bosi.

"Shaka ondoa, kazi umepata Deo, Levina ni mtu wangu tangu kitambo, siwezi kumuangusha,"
"Ahsante sana!" Alijibu Deo kwa furaha akiamini sasa maisha yake yatabadilika.

Mazungumzo ya kawaida yakawa yanaendelea kati ya Levina na Cleopatra. Baada ya kukaa pamoja na kuzungumza mengi, hatimaye muda wa Deo na Levina kuondoka ulifika.

Kama ilivyokuwa wakati wa kusalimiana mara ya kwanza, Cleopatra alijikuta akiganda kwa Deo, hali iliyozidi kumtia hofu Levina.
"Hii ni ‘business card' yangu, chukua tafadhali," aliongea Cleopatra wakati akimkabidhi Deo kadi yake ya mawasiliano.

"Namba yako nitachukua kwa Levina kwa ajili ya kukutaarifu siku ya kuja kuripoti kazini."
"Sawa! Nashukuru sana," alijibu Deo huku akionesha wazi jinsi alivyofurahi kupata kazi.

"Hee shosti, utanikwaza sasa hivi! Kuagana tu ndiyo mpaka umgande shemejiyo kama ruba! hebu mwachie huko, na wewe ndiyo utakuwa mlinzi wake kazini, ole wako nisikie unamtaka," alisema kwa utani Levina lakini akionekana kumaanisha kile alichokisema.

Cleopatra alimuachia mkono Deo na wakaanza kuondoka. Akilini mwake, Deo alishahisi kuwa amezimikiwa na bosi wake mtarajiwa, lakini kwa jinsi alivyokuwa anampenda Levina, alijiapiza kuwa kamwe hawezi kumsaliti.

"Deo mpenzi, unaenda kuanza kazi, na sasa kila mtu anakusifia kuwa wewe ni ‘handsome', tafadhali usije ukanisaliti mpenzi wangu," alilalama Levina huku akimkumbatia Deo kimahaba.
"Siwezi honey, amini nakwambia."

***
Siku chache baadaye Deo aliitwa kwa ajili ya kufanyiwa usaili (Interview) ambapo alikidhi vigezo vyote. Kesho yake akaanza kazi akiwa kama mhasibu kwenye kampuni ya baba yake Cleopatra ya Planet-link Enterprises, ambayo Cleopatra ndiyo alikuwa msimamizi wa shughuli zote (bosi).

Kama alivyokuwa amejiapiza tangu siku ya kwanza anakutana na Deo, alimuweka kwenye kitengo cha uhasibu, hali iliyowafanya wawili hao kuwa karibu muda mwingi wawapo kazini.

"Nitakufundisha kazi mpaka utakapozoea vizuri, usisite kuniuliza chochote kinachokusumbua na nitakupa msaada unaouhitaji," alisema Cleopatra wakati akimkaribisha Deo ofisini.

Tofauti na alivyokuwa mwanzo, Deo wa sasa hakuwa tena yule ‘shamba boy'. Alikuwa akionekana ‘smart' muda wote, huku ‘u-handsome' aliojaaliwa na Mungu ukichanua na kuwachanganya wanawake wengi, Cleopatra akiwa mmoja wapo.

Kwa kadri siku zilivyokuwa zinazidi kusonga, Cleopatra alizidisha vituko kwa Deo, akimtega kwa kila namna ili anase kwenye himaya yake.
"Leo naomba tutoke wote nikakupe ‘lunch'!" Cleopatra alimwambia Deo.

"Sawa, hakuna shida! Ngoja nimalizie kazi kidogo ‘then' tutatoka."
Wakiwa kupata ‘lunch', Cleopatra alikuwa akimchombeza Deo kwa maneno ya uchokozi huku akimsisitiza kuwa asije kumwambia Levina kuwa wametoka pamoja.

"Namjua shoga yangu, Levina. Ana wivu sana akimpenda mtu, kwa hiyo tafadhali usije kumwambia kitu."
"Lakini mi naona hakuna tatizo lolote akijua, si tumetoka ‘lunch' ya kawaida, hata mwenyewe angekuwepo tungejumuika pamoja."

"Ni kweli Deo, lakini sitaki kukorofishana na Levina."
"Poa nimekuelewa!"
"Nikwambie kitu Deo, ‘You are soo handsome!' (Wewe ni mzuri sana).
Deo hakujibu kitu zaidi ya kutabasamu kwa haya, hakuzoea kusifiwa maishani mwake.

Baada ya kumaliza kupata chakula cha mchana, walirudi kazini na kuendelea na shughuli za kawaida, kila mtu akiwajibika sehemu yake.
Siku zilizidi kusonga ambapo Deo na Cleopatra wakazidi kuwa jirani.
Ilifika mahali ikawa bila kumuona Deo, Cleopatra hawezi kwenda kupata chakula cha mchana peke yake. Akaanza mazoea ya kumpelekea zawadi ndogondogo. Urafiki wao ukazidi kushamiri.
"Deo!"

"Naam Bosi!"
Aah! Si nilishakukataza kuniita bosi? Niite jina langu bwana."
"Im sorry, naam Cleopatra"
"Leo ukimaliza kazi jioni una ratiba gani?"
"Nitamsindikiza Levina kwa shangazi yake Mabibo."

"Basi kama leo utakuwa taiti, naomba wikiendi hii nikutoe ‘out'."
"Labda nikamuombe kwanza ruhusa Levina, akikubali sawa."
"Acha mambo ya kitoto Deo, we unafikiri Levina atakuruhusu kutoka na mimi? Halafu si nilishakwambia mambo yangu na wewe usimwambie? Usiniangushe bwana."

"Ok basi poa, si Jumamosi eti eeh!"
"Eeh! Nataka nikakupe zawadi nzuri niliyokutunzia kwa siku nyingi," alijibu Cleopatra kwa kudeka huku akimtazama Deo kwa jicho la huba."

Hatimaye Jumamosi ikafika, siku ya miadi ambayo Cleopatra na Deo walikubaliana kutoka ‘out' pamoja.
"Huwa unatumia kinywaji gani? Namaanisha bia gani?"
"Pombe huwa sinywi, labda soda tu."

"Leo kwa kuwa uko na mimi , naomba unywe japo kidogo uchangamshe akili," alisema Cleopatra huku akiendesha gari lake kuelekea Kunduchi Wet and Wild Hotel. Mawazoni mwake, alikuwa akipanga mengine, na aliamini ile ndiyo siku yake ya kumfaidi Deo.


Je, nini kitaendelea? Tukutane baadae.....
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom