ITAKUWA ni makosa kuitathmini Awamu ya Nne bila kutanabahisha kuwa serikali hiyo ilianza kazi kwa ahadi kubwa kubwa bila kuangalia hali halisi ya wakati na mazingira yaliyokuwepo wakati wa kuingia madarakani.
Kama tunavyojua ahadi nyingi hadi wa leo zimekuwa ni nyimbo kiasi cha kusababisha uongozi wa awamu hiyo kuitwa viongozi wasanii.
Usanii huu ulifikia kilele katika sakata la EPA na kuhusishwa kwa jamaa za Rais na kashfa hiyo hadi kufungiwa kwa gazeti la Mwanahalisi bila kufuata katiba, taratibu na sheria za nchi.
Laiti kama uongozi wa awamu ya nne ungelichukua muda kupata picha halisi ya nchi kama ilivyoachwa na Rais aliyetangulia kuna mambo kadhaa yaliyohitaji kurekebishwa kabla ya kuingilia masuala ya utekelezaji.
Hadi Rais wa awamu ya tatu anaondoka madarakani nyufa kadhaa za kisiasa na kijamii zilikwishaonekana:
. Awamu ya tatu ilikwishawagawa Wazanzibari na Watanganyika kwa siasa zake za kibabe;
. Awamu ya tatu ilifanya kosa kubwa la kukataa Kuwepo kwa Katiba Mpya wakati mazingira ya ksiasa, kiuchumi na kijamii yalikuwa yakililia jambo hilo;
. Awamu ya tatu ilikwishawagawa Wakiristo na Waislamu kwa kushughulikia chapuchapu mambo ya Wakiristo na kulalia au kuyapuuza masuala ya Waislamu;
. Awamu ya tatu iliuza mashirika ya umma kwa watu wachache, wa nje na wa ndani, na waliowekeza katika mashirika ya umma, yaani wananchi, hawakununafaika chochote na ubianfsishaji isipokuwa kwa vigogo, vizito na wanjanya wachache. Hii ilichangia kwa kiasi kikubwa kugawa nchi kati ya walionacho na wasionacho;
. Awamu ya tatu haikuimarisha demokrasia kwa kushindwa kuunda Tume Huru ya Uchaguzi na kuendelea kukubali vipengele vya katiba na sheria vilivyokiuka haki za msingi za raia;
. Kwa kutumia jeshi la polisi vibaya awamu ya tatu iligawa polisi na wananchi, jambo ambalo bado linaendelea kudhihirika mahakamani;
. Katika siasa za nje, awamu ya tatu ilifanikiwa sana kuwagawa wafadhili kati ya washirika wateuliwa na washirika wanaojipendekeza, kwa maana Uingereza (ambayo ilibariki rushwa kati ya makampuni ya Uingereza na serikali ya Tanzania) ilionekana ndio baba na mama wa kila kitu na nchi zilizokuwa na nia ya kweli kuitoa Tanzania kutoka kwenye umasikini kama vile nchi za Kiarabu, Japan, Scandinavia, China, India, Brazil na kadhalika zilionekana hazina umuhimu wala maana kwa nchi hii;
. Awamu ya tatu iliwagawa wanasiasa kati ya wale wasio na mahusiano na matajiri na wale waliokuwa na fedha za matajiri nyuma yao. Jambo ambalo kwa kiasi kikubwa limechangia tabia, hulka na majibu ya uongozi wa sasa katika kashfa mbalimbali zilizoikumbuka nchi na serikali;
. Awamu ya tatu iliingia madarakani ikijua fika kuwa Tanzania imekuwa ikitumia muda na rasilimali zake ndogo katika masuala ya kimataifa na hususan Afrika bila faida wala manufaa yoyote kwa Watanzania;
. Awamu ya tatu ilikwishaanzisha 'apartheid' ya afya na tiba kwa kuwa na Watananzia wanaotibiwa nje na wale wasiotibiwa nje;
. Awamu ya tatu pia ndio iliyoanzisha 'apartheid' kati ya watoto wa viongozi, mangimeza wa serikali na watoto wa wananchi wa kawaida. Kikundi cha kwanza, kilisomeshwa nje kwa fedha za serikali, na kikundi cha pili kinasomeshwa kwa mikopo toka serikalini katika hali ya kusimbuliwa na kudhalilishwa mara kwa mara;
. Awamu ya tatu iliwafanya Watanzania kuwa hawana thamani kama mitambo na fedha za makampuni ya nje na hivyo kuuza au kukodi migodi ya dhahabu na madini mengine kwa bei sawa na bure;
. Awamu ya tatu haikukaa na kutathmini kwa makini yale yanyoweza kuendeshwa na serikali na yale ya kuwaachia watu binafsi na hivyo kuingiza nchi katika matatizo ya maji, usafiri wa reli, simu, mabenki na kadhalika;
. Awamu ya tatu iliachia askari wa kukodiwa kuendesha kampeni za CCM kwa namna ambayo wote leo tunaikumbuka na bila shaka kuna uhusiano mkubwa kati ya waendesha kampeni hizo na BOT, Hazina, EPA, migodi ya dhahabu na matatizo yanayoikumba nchi kwa sasa;
. Awamu ya tatu haikuzipa WIzara wala mikoa visheni na misheni stetimenti na awamu ya nne ikapokea serikali vivyo hivyo na imeendelea vivyo hivyo, yaani kama vile nchi wala sehemu za nchi hazina mipango wala ramani kuu ya kule tunakostahili kuelekea;
. Awamu ya tatu ilizungukwa na watu wenye ubinafsi wa hali ya juu na ni wachache sana waliokuwa na uchungu wa nchi na watu wake. Hawa wachache wengi wao walifukuzwa au kwa namna moja au nyingine kuondolewa serikalini;
. Awamu ya tatu imechangia sana mikoa kadhaa nchi kubaki nyuma au kurudi nyuma kimaendeleo kutokana na sera mbovu za kijamii na kiuchumi na uwezo duni wa serikali kuwafikia na kutafutia ufumbuzi matatizo ya wananchi mikoani;
. Awamu ya tatu ilikifanya chama tawala kuwa chama yatima kwa kukosa uongozi na dira ya kuwatumikia wananchi waliokiweka chama hicho madarakani na kuishia kuwafanya viongozi wa chama wa mikoa, wilaya na matawini kukitumia chama kwa faida yao binafsi na wala sio huduma kwa wananchi;
. Kubwa zaidi ni kuwa awamu ya tatu ilishindwa kudhibiti vitabu, mapato na matumizi ya serikali kwani ilijali wakubwa tu kulipwa na kilichofanyika BOT, Hazina na mawizarani hakuna aliyekijua.
Ukiyazingatia yote haya utaona kwamba kuna mambo kadhaa yalistahili kushughulikiwa kwanza kabla ya serikali ya awamu ya nne kuwa na nafasi ya kuweza kutekeleza ahadi zake njema kwa wananchi wa Tanzania.
Kwa kuwa haya hayakufanyika matokeo yake ni kuwa Kikwete, kwa kifupi, hapa nyumbani anaonekana kuishindwa kazi ya Urais na imani na matumaini wananchi waliyokuwa nayo kwake kwa kiasi kikubwa vimeshuka.
Huko nje kabla ya BOT na EPA alianza kupanda chati. Hata hivyo, matokeo ya ufisadi na udhaifu wake katika maamuzi na uwezo wa kuleta marekebisho muhimu kunaanza kuwafanya wengi kuuliza maswali juu ya uwezo wake kama kiongozi anayewafaa Watanzania.
MAENEO YA TATHMINI
Katika kuifanya tathmini hii tunaweza kutumia maeneo haya:
. HARAKATI
kuingia Ikulu
. UONGOZI
. UCHUMI
. JAMII
. UTAMADUNI
. TEKNOLOJIA
. SIASA NA SIASA ZA NJE
Harakati za kuelekea Ikulu
Dalili za mashaka zilianza kuonekana pale ambapo timu ya kampeni ya rais aliyeko madarakani ilipoanza kuvinunua vyombo vya habari, kupaka matope wagombea wengine na kuweka mkakati wa kisasi kwa kila aliyesimama dhidi yao na kile walichokitaka.
Hatuna haja ya kuingia ndani sana, lakini ujumbe muhimu hapa ilikuwa ni kuwa ama mgombea au waliokuwa wanamtaka mgombea huyu waliutaka urais kwa udi na uvumba kwa sababu walizozijua wao zaidi kuliko maslahi ya nchi na Watanzania.
Hakukuwa na mkakati wala malengo yakinifu kiuchumi na kimaendeleo wakati huo kama ilivyo sasa. Nchi, kwa wengi, inaonekana inakwenda kwa kudra za Mungu, na kwamba yeyote yule angeliweza kuwepo madarakani na bado nchi isingelikuwa na jipya.
Fundisho kubwa hapa ni kwamba kuutaka Urais, sio kuweza na kumudu kikamilifu kazi za urais.
UONGOZI
Kiongozi hapimwi kwa uwezo wake binafsi au kwa kazi anayoifanya yeye mwenyewe.
Aghalabu, kiongozi mzuri hutambulika kutokana na uwezo na kazi za wale walioko chini yake.
Rais kama mtendaji mkuu anafaulu pale anapokuwa na mawaziri, makatibu wakuu, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na watumishi wa umma wanaojituma na wanaochukulia kazi zao kama wito wa kubadilisha maisha ya wananchi wote na sio tu maisha yao, wake na familia zao.
Hili halionekani kuwa ndio hali halisi ya uongozi ulioko madarakani. Ndio kuna timu, lakini kama zilivyo timu za mpira wa miguu Tanzania sio timu zenye wachezaji wanaocheza kama timu moja na kuonesha matumaini kwamba wanaweza wakashinda mechi yoyote ya kimataifa!
Guru wa menejimenti wanasema kwamba mwanzo wa mafanikio katika oganaizesheni yoyote ni kuwa na timu inayocheza kama timu. Kinyume cha hivyo, ni bure kutegemea sio tu maajabu bali hata utendaji kazi mzuri wa kawaida.
Uongozi ni kuonesha njia. Hapa tunatarajira kuwa kiongozi alikuwa tayari anajua njia. Kama na yeye alikuwa akioneshwa njia sasa inakuwa ni mtihani mkubwa. Kama kiongozi mwenyewe keshapotea njia ni vigumu kuona ni jinsi gani anaweza kuwaongoza wanaomfuata. Na huu ndio msiba wa Watanzania hivi leo.
Pamoja na kuzungukwa na wapiga-debe, marafiki, watu wa kulipwa au kulipiwa fadhila na kama hao ni vyema pia kuzungukwa na asilimia kidogo ya watu ambao hawakuogopi na ambao watakupa hata habari na maelezo ambayo hupendi kuyasikia na yatakayokuharibia siku yako. Lakini habari ambazo zitawaonesha watu uko juu ya mambo na unajua unachokifanya na unachokisema saa zote na wakati wote.
UCHUMI
Yapo madai kwamba nchi imepiga hatua hii au ile, lakini kipimo halisi kama nchi inaendelea au haiendelei ni kile cha GPD per capita. Hadi wa leo GDP per capita ya Mtanzania ni ndogo kuliko ya Rwanda, Uganda na Kenya. Hata Algeria, Burundi, Sudan, Ethiopia,Mozambique, Malawi, Zambia na kadhalika zimetuzidi pamoja na matatizo yao ya uchumi au kukosa amani. Ni vigumu kwa hiyo kuona maendeleo hayo yanatoka wapi.
Nchi haijawa na mpango wowote wa kutumia tathmini kama zile za Human Development Index wala ile ya karibuni ya Mo Ibrahim Index of African Development kujiangalia na kujipanga upya ili kufanya kwanza yale yanayowezekana kufanyika bila msaada toka nje. Hakuna anayekubali tena kisingizio kwamba uchumi wa Tanzania kwa kiasi kikubwa hauko kwenye rekodi au vitabu kwa sababu hizo ni porojo tu na kuwa nchi nyingi za Kiafrika zina hulka hiyo hiyo na sisi hatupimwi na nchi za nje bali wenzetu hapa Afrika.
Kwa kifupi, katika miaka minne ya Kikwete Watanzania wana hali mbaya ya kiuchumi na kimaisha kuliko alivyowakuta pamoja na ahadi za chama chake kuwa kinakuja na kasi zaidi, nguvu mpya na ari mpya.
Kasi mpya iliyopo na ile ya kuendelea kuacha matatizo kuendelea kuwa matatizo; nguvu mpya ni ile ya kukwaza uhuru wa vyombo vya habari na kubwekea kufuata kwa sheria zilizopitwa na wakati au zilizowekwa kulinda ubovu wa serikali na wanasiasa walioko madarakani; na ari mpya ni ile ya kuwalinda wanaohujumu haki za wananchi na uchumi wa nchi hii.
JAMII
Jamii ya Tanzania iliahidiwa mengi na Chama tawala wakati rais wake anaingia madarakani. Lakini mojawapo kubwa ni lile la kuahidi kwamba:
'Maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana!'
Hilo halijawa na haiwezekani kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja uliobakia kufikia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Dalili zote zilizopo ni kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kuwa na maisha duni kwa kila Mtanzania tunapoingia mwaka 2009 hasa ukizingatia migomo mbalimbali na kuzorota kwa utawala wa kisheria mambo yanayokithiri lwa sasa. Pamoja na kushuka kwa bei ya mafuta duniani ni dhahiri serikali iliyoko madarakani ni dhaifu na haiwezi kufanya lolote la kufikisha nafuu inayotokea kwenye soko la dunia kwa Mtanzania wa kawaida.
Wakati wake na watoto wa vizito na vigogo wananufaika na kabala ya walaji mali za nchi kiharamu watoto na vijana wa walalahoi wanaendelea kuadhirika katika masuala ya elimu, tiba na ajira kama vile hawana mzazi wala mlezi katika nchi hii. Kazi iliyotakiwa kufanywa na serikali yenye viongozi waadilifu na wenye mapenzi na uchungu wa maendeleo ya nchi na watu wake.
Pamoja na kuwa na tatizo la ukimwi lakini jinsi linavyochukuliwa na serikali kwa msaada wa Wamarekani ni kichekesho kitupu. Imekuwa kama vile Tanzania haina matatizo mengine makubwa kuliko ukimwi, ikiwemo maradhi yanayoua maelfu ya watu wetu kila siku. Na hata ukiangalia misaada inayomiminika kusaidia ukimwi utagundua kuwa misaada hiyo inawasaidia zaidi wasio na ugonjwa huo kuliko wenye ugonjwa huo.
UTAMADUNI
BADALA ya kulinda utamaduni wa nchi hii serikali ya awamu ya pili imekuwa mwanasesere wa Wamarekani na Waingereza.
Inaelekea sio tu viongozi wetu wanawapenda jamaa hawa bali wanawaabudu kama Miungu yao ya dunia.
Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC) ndio liko mstari wa mbele katika kupotosha watoto na watu wazima kwa kutangaza vipindi vyenye kusambaza utamaduni na maadili ya kigeni hapa nchini.
Badala ya kuendeleza mpira wetu, sasa tunajiandaa kuwa koloni la Waingereza kimpira, kisaikolojia.
TBC kwa kupewa meno na makucha na serikali imeingia kwenye soko la habari na kuanza kuwararua walipa kodi wazuri wa nchi hii katika ushindani uanogemea upande mmoja.
Pamoja na nia nzuri ya kuwa na vyombo vya habari vya umma kilichopo hivi sasa ni vyombo vya habari vya chama tawala na wala sio vya serikali. Hakuna jipya lolote lililoneshwa zaidi ya mbwembwe za kisanii katika sauti na kitaswira ambazo hazijamwongezea Mtanzania lolote jipya kihabari, kielimu na kiburudani.
Shirika hilo limeshindwa kabisa kuandaa vipindi vinavyoenzi utamaduni wetu na kuwalea watoto na vijana wetu katika maadili ya kitanzania pengine kwa sababu nchi yenyewe chini yc CCM kimeshindwa kuwa na maadili ya Kitaifa. Ni vigumu hivi leo kumtofautisha Mtanznia na mtu wa nchi nyingine maana tumeishia kumfanya Mtanzania kinyago tu hapa duniani. Hili ni pamoja na kutambua au kutotambua kwamba utamaduni ni roho ya taifa. Bila utamaduni nchi hii haina tofauti na mfu! Kubwa zaidi, hakuna nchi inayoweza kuwa na maendeleo ya kweli yasiyojengwa juu ya msingi wa utamaduni, jadi, desturi na mila zake.
TEKNOLOJIA
Wale waliopewa dhamana ya uongozi katika nchi hii wametumia upatikanaji na ununuaji teknolojia mpya kama njia ya kujitajirisha kwa kuinunulia nchi hii mitambo mibovu kuanzia rada hadi jenereta za umeme na kadhalika. Haya, yamechangia kwa kiasi kikubwa umasikini zaidi wa Mtanzania.
Isitoshe, kwa kushinda kufanya utafiti makini kuhusiana na gharama za mashine na mitambo ya aina mbalimbali ikiwemo ile ya kuchimba madini tumekodisha migodi yetu kwa mapato sawa na hamna. Kiasi ambacho kinaonesha kuwa uongozi unaona mitambo na mashine za wawekezaji kuwa na thamani zaidi kuliko Watanzania wote wakiwekwa pamoja.
Pale walipotokea Watanzania wenye kipaji cha kutengeneza teknolojia moja au ya aina nyingine utawala umeendelea kuwakwaza badala ya kuwasaidia na hivyo kuisadia nchi na watu wake.
Hata mapokeo ya teknolojia mpya yamekuwa legelege kiasi ya kwamba hivi leo Rwanda iliyokuwa nyuma yetu kimaendeleo imeanza kutuwashia indiketa na bila shaka hautopita muda kabla ya kushindwa kuona taa hizo za indiketa.
SIASA ZA NJE NA SIASA ZA NDANI.
HILI wala halina mjadala. Kwa siasa za ndani Tanzania chini ya Bw. Kikwete imepata F, wakati katika siasa za nje imepata B+.
Mamilioni ya fedha yametumika kugharamia masuala ya siasa za nje huku baadhi ya mikoa na wilaya ikisahaulika kama ni sehemu ya Tanzania kiuchumi na kijamii. Hali za maisha katika mikoa ya Tanga, Tabora, Mbeya, Rukwa, Singida, Kigoma kwa kweli inakatisha tama na haionekani kama kuna nafuu inakuja njiani hivi karibuni.
Suala hapa ni je, miaka 47 baada ya Uhuru Watanzania wataendelea kuridhika kuona akili na rasilimali za nchi yao vinaendelea kuwanufaisha watu wa nje na sio wao wenyewe? Hasa ukizingatia kwamba hivi sasa Watanzania hawatakiwi na wanauawa katika nchi kama Afrika Kusini, Msumbiji, Zimbabwe, Angola na kadhalika?