Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (140)

Don’t try to do anything stupid,” Spoiler alifoka huku akichomoa haraka kisu chake cha springi toka kwenye ala yake, akakielekeza kwenye shingo ya Tunu. Alikuwa ameghadhabika sana.

Tunu aliuma meno yake kwa hasira na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, ujanja wake ulikuwa umegundulika. Sasa alihisi kuwa huenda huo ulikuwa mwisho wa maisha yake. Wakati gari likikata kona kuingia barabara ya Mori, Tunu akaliona gari fulani likija nyuma yao kwa kasi na kulitambua, akaachia tabasamu huku akijiegemeza kwenye siti yake. Lilikuwa ni lile gari aina ya Nissan Patrol la rangi ya bluu. Mara akahisi kuchomwa na kitu fulani ubavuni kwake mfano wa sindano na mara usingizi mzito ukaanza kumnyemelea.

Hakutaka kulala, alijaribu kufumbua macho yake lakini hakuweza na mara usingizi mzito ukammeza kabisa. Kama ndoto alianza kusikia mabishano kati ya wale watu wawili, mmoja alisema, “Tumuue kabisa maana haaminiki huyu.”

“Hapana, hana tena ujanja. Hii dawa itamlaza hadi keshokutwa hivyo ngoja tumfikishe kwa mzee, ndiye ataamua cha kumfanya!” mwingine alisema na mara akasikia kishindo kikubwa na kuanza kuyumba huku na kule.

Lile gari aina ya Nissan Patrol la rangi ya bluu lilikuwa limeifikia ile taxi na kuipiga kumbo ubavuni kiasi cha kufanikiwa kuihamisha kabisa barabarani na kuisogeza hadi kando ya barabara kwenye mfereji wa maji machafu. Tukio lile likaifanya ile taxi ianze kupoteza uelekeo huku ikiyumbayumba ovyo barabarani. Kilikuwa kitendo cha ghafla kilichowatokea kina Spoiler wakati wakiwa hawajajiandaa.

Yule mwanamume mwenye mwili ulioshiba aliyeketi kule mbele kushoto kwa dereva aliielekeza bastola yake kwenye lile Nissan Patrol na alipokuwa akijiandaa kufyatua risasi, Bob aliyekuwa akiendesha lile Nissan Patrol akawa mwerevu wa kushtukia mapema hila yake na hivyo akaliwahi lile taxi na kuligonga tena ubavuni. Mtikisiko uliotokea ukafanya bastola ya yule mtu imponyoke mkononi na kuangukia chini siti.

Lakini kabla hawajapata ufumbuzi Dumba, aliyekuwa pamoja na Bob aliachia risasi moja iliyokisambaratisha kichwa cha dereva wa ile taxi na muda huohuo uhai ukawa mbali na mwili wake. Wote ndani ya taxi walifahamu kuwa ule ungekuwa mwisho wao kwani kilichokuwa kinafuata baada ya hapo kingekuwa hatari zaidi kwao. Kwa haraka yule mwanamume mwenye mwili ulioshiba aliyekuwa ameketi mbele akawahi kuudaka usukani ili kuiongoza ile taxi.

Muda uleule ile taxi ikaparamia ukuta wa nyumba moja iliyokuwa kwenye kona kuelekea barabara ya Kwa Mwarabu na hapo yowe la hofu kutoka kwa watu waliokuwa kando kando ya ile barabara wakishuhudia kilichokuwa kinatokea likasikika wakati lile gari likiuparamia ule ukuta na kubomoa kabisa kisha likazama ndani ya nyumba.

Lile gari aina ya Nissan Patrol lililoendeshwa na Bob lilifunga breki na kusimama kando ya barabara ya Kwa Mwarabu, na kwa haraka sana Bob na mwenzake Dumba wakashuka na kuelekea kule ndani ilikokuwa ile taxi pasipo kujali macho ya watu walioanza kukusanyika eneo lile kushuhudia ajali ile ya kutisha.

Walipoifikia ile taxi wakawakuta watu watatu tu ndani ya gari. Dereva ambaye alikuwa amekufa, yule mwanamume mwenye mwili ulioshiba alikuwa amebanwa katikati ya lile gari na ukuta pale alipojaribu kuruka ili ajiokoe na damu zilikuwa zikimtoka mdomoni, na Tunu aliyekuwa amelala kwenye siti akiwa amepoteza fahamu. Spoiler alikuwa ametoweka.

Haikujulikana kama yule mwanamume mwenye mwili ulioshiba alikuwa mzima au mfu na wala hakuna kati yao aliyejihangaisha naye. Kina Bob walihitaji kumuokoa Tunu, na walipomwona amelala akiwa hana fahamu huku akitokwa damu mdomoni na sehemu ya kichwani, begi lake lenye laptop likiwa kando yake.

Walimchomoa haraka toka kwenye siti yake. Bob akambeba na wakati huohuo Dumba alilichukuwa lile begin a kuiona bastola ya Tunu, akaichukua na kutoka haraka kumfuata Bob kwenye gari lao.

Muda mfupi baadaye lile gari aina ya Nissan Patrol liliondoka toka eneo lile kwa mwendo wa kasi huku watu waliokuwa wameanza kujaa eneo lile wakiwa wamepigwa na butwaa.

* * * * *

Gari dogo aina ya Land-Rover 110 jeupe la POLISI lilifika katika eneo ilipotokea ajali nusu saa baada ya gari la kina Bob aina ya Nissan Patrol kuondoka. Polisi walikuwa wametaarifia uwepo wa ajali ile na mmiliki wa nyumba iliyogongwa na kubomoka. Ndani ya gari lile la polisi kulikuwa na watu wane. Mbele ya gari kulikuwa na watu wawili, dereva wa gari aliyekuwa amevaa sare ya kazi ikiwa na cheo cha koplo na mtu mwingine aliyekuwa amevaa suti ya kijivu na shati jeusi akiwa ameketi upande wa kushoto.

Nyuma ya gari lile kulikuwa na askari wawili wengine waliokuwa wamebebelea bunduki na vifua vyao vimekingwa na mavazi maalumu yanayozuia risasi maarufu kama ‘bullet proof’. Askari wote walikuwa na sura ya kazi.

Wale askari wawili walioketi nyuma pamoja na yule kiongozi wao mwenye suti ya kijivu ambaye kimwonekano alikuwa mweusi wa miaka arobaini wakashuka haraka na kuuliza kilichotokea, baada ya kuelezwa kwa ufupi wakaanza kupenya kuelekea kule ndani ilipokuwa ile taxi wakipita kwenye makundi ya watu waliokuwa wamekusanyika pale wakishangaa.

Walipozama ndani wakakutana na mmiliki wa ile nyumba ambaye alijitambulisha kwao na kuwaeleza kilichotokea: tangu aliposikia mshindo mkubwa wakati yeye na familia yake wakiwa mezani wanakula kisha wakaona ukuta wa nyumba yao ukianguka na gari kupenya ndani, kisha alivyoweza kumwona mtu mmoja akitoka ndani ya lile gari akiwa ameshika kisu na kupotelea kizani, na mwisho alivyowashuhudia wanaume wengine wawili wakiingia pale na kumbeba msichana mmoja aliyekuwa ndani ya ile taxi akiwa amezirai na kuondoka naye.

inaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (141)

Baada ya hapo yule askari mwenye suti ya kijivu ambaye alikuwa na cheo cha Inspekta akapata kuuona mwili wa dereva wa ile taxi ukiwa umelalia usukani ukivuja damu, kichwa chake kilikuwa kimechakazwa kwa risasi, na akamwona mtu mwingine mwenye mwili uliojazia aliyekuwa amebanwa katikati ya gari na ukuta huku akiugulia kutokana na maumivu aliyokuwa akiyapata.

Inspekta akamtazama kwa makini yule mtu mwenye mwili uliojazia aliyekuwa akiugulia na kuwataka watu wenye ujasiri waliokuwepo pale wasaidiane na askari wake kumtoa pale alipokuwa amenasa, wakafanikiwa kumtoa na kumlaza kando wakati yule Inspekta akipiga simu ofisini kuomba magari mawili, moja la wagonjwa na gari jingine kwa ajili ya kuuchukua ule mwili wa dereva wa taxi.

Alipokata simu akaanza kukagua eneo zima ambapo tukio lilitokea na kupiga picha kwa kutumia kamera yake ndogo maalumu kwa kazi hiyo. Alipomaliza kufanya ukaguzi wake ikiwa ni pamoja na kupiga picha akaanza kuwauliza maswali watu aliowakuta pale ambao walikiri kushuhudia kila kitu tangu magari yale yalipokuwa yakigongana hadi ajali kutokea na kisha watu wawili kutoka ndani ya gari aina ya Nissan Patrol na kumbeba yule msichana aliyekuwa ndani ya taxi na kuondoka naye.

Baada ya mahojiano ya kutosha kwa takribani dakika therathini na tano, yule Inspekta akawa amebaini mambo kadhaa kuhusiana na tukio lile, mambo hayo aliyahusisha na matukio ya kutekwa kwa Sammy na kisha kulipuliwa kwa nyumba yake.
Wakati akitafakari mara magari mawili yakawasili eneo lile, moja likiwa gari la wagonjwa na gari la pili lilikuja kwa ajili ya kuuchukua ule mwili wa dereva. Wakashuka watu waliokuwa wamevaa glavu mikononi na kusaidiana kumchukua yule mtu mwenye mwili uliojazia na kisha kumpakia kwenye lile gari la wagonjwa na wakati huo huo wengine wakiupakia mwili wa yule dereva, kisha magari hayo yakaondoka haraka kuelekea hospitali ya Mwananyamala.

Yule Inspekta hakuonekana kuridhika, aliendelea kuuliza maswali mengine machache ambayo kwa kiasi fulani yalikuwa yamemsaidia kupata picha halisi, kisha akaaga na kuondoka huku akiwaacha wale askari wawili wenye silaha wakilinda eneo lile wakati wakisubiri gari maalumu kuja kuivuta ile taxi.

* * * * *

Saa kumi na mbili na nusu ya asubuhi ilimkuta Mr. Oduya akiwa ameketi ofisini kwake kwenye jengo lake la ghorofa kumi na mbili lililopo barabara ya Bagamoyo, eneo la Kijitonyama, jijini Dar es Salaam. Hakuwa ameambua japo lepe la usingizi na muda huo alikuwa amekwisha pata taarifa juu ya kile kilichokuwa kimewatokea vijana wake watatu.

Ajali ya ile taxi ilikuwa imesababisha kifo cha dereva wa taxi huku yule muuaji wake wa kukodiwa mwenye mwili uliojazia ambaye alikuwa akiitwa Casmir akiwa ameumia sana eneo la kifuani na mbavuni na kukimbizwa katika hospitali ya Mwananyamala, baada ya kutokea mapambano na lile gari aina ya Nissan Patrol lililokuwa limewachukua watu wa Tunu.

Mr. Oduya pia alikuwa amepokea taarifa hizo za kusikitisha sana kwa mshtuko mkubwa na zilizidi kumnyima raha. Kilichomzidishia uchungu ni taarifa za kwamba Victor alikuwa amechakazwa vibaya na hali yake ilikuwa mbaya sana kiasi cha kukimbizwa hosipitali akiwa mahututi baada ya kuvunjwa mbavu kwenye mapambano kati yake na Tunu.

Kwa ujumla taarifa zote mbili zilimtisha sana Mr. Oduya. Alihofia kuwa sasa ingeweza kugundulika kuwa yeye ndiye alikuwa mhusika mkuu baada ya majanga mfululizo yaliyokuwa yakiwaandama watu wake wa karibu na endapo taarifa zile zingewafikia watu wa magazeti basi zingeweza kumharibia kwenye harakati zake.

Muda wote alikuwa akivuta sigara kwa fujo kama mtu asiye na akili sawasawa. Kutokana na maelezo aliyokuwa ameyapata toka kwa Spoiler kuhusu lile gari aina ya Nissan Patrol na aina ya watu waliokuwa ndani ya lile gari ilimaanisha kuwa sasa matumaini ya kumpata Tunu yalikuwa yamekufa kabisa, kwani Tunu alikuwa tayari anacho kikosi kabambe kilichojiandaa kwa ajili ya mapambano dhidi yake.

Muda mfupi tu uliokuwa umepita Mr. Oduya alikuwa amewapigia simu baadhi ya washirika wake muhimu na kuwaomba wakutane hapo ofisini kwake ili awaeleze ukweli wa kile ambacho mwanzoni hakuwa ametaka kukiweka wazi kwao, nia yake ilikuwa kuwataka wamsaidie jinsi ya kujikwamua kutoka kwenye balaa hilo baada ya maji kumfika shingoni.

Kati ya washirika muhimu sana wa Mr. Oduya ambao aliamua kuwaita walikuwemo Balozi Mageuzi na Dk. Masanja. Mr. Oduya alikuwa amefikia uamuzi huo baada ya kuona kuwa timu yake ya mauaji aliyokuwa ameiandaa kummaliza Tunu ikizidiwa ujanja kwa kila hali na Tunu.

Baada ya hapo Mr. Oduya aliendelea kuketi kwa utulivu kwenye kiti chake cha ofisini huku sigara zikipishana mdomoni. Baada ya kitambo fulani alionekana kushtuka, akaitazama saa yake ya mkononi na kushusha pumzi. Alikuwa anahofia sana muda huo wa kusubiri kwa kudhani lolote baya lingeweza kutokea. Kwa mara nyingine tena wazo la kutaka kutoroka nchini lilimjia, sasa hakuwa na uhakika kama alistahili kuendelea na harakati zake za kuuwania urais wa nchi ya Tanzania au atoroke nchini mara moja na kukimbilia Canada akaanze maisha mapya.

C’mon! Urais hauji kwa starehe, ni mapambano ya kufa au kupona,” Mr. Oduya alijikumbusha maneno hayo na hapo hapo yakamtia moyo hata kicheko hafifu kikamtoka. Kilikuwa kicheko halisi cha faraja kilichoujaza moyo wake furaha na kumsahaulisha kwa muda mashaka yote aliyokuwa nayo, akaapa kupambana hadi dakika ya mwisho ili atimize ndoto yake.

* * * * *

Saa moja ya asubuhi Tunu aliyatega masikio yake kwa makini huku akijaribu kutafakari kuwa pale alikuwa wapi. Hakusikia sauti ya kitu chochote na utulivu wa eneo lile ulikuwa ni wa hali ya juu kiasi kwamba nafsi yake ilianza kuingiwa na hofu. Muda huo alikuwa amerudiwa na fahamu, na kumbukumbu juu ya yote yaliyomtokea kule Sinza alipotekwa na kina Spoiler zikamjia.

Itaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (142)

Hakuweza kukumbuka nini kilichokuwa kimemtokea baada ya kuchomwa na kitu mfano wa sindano na kisha fahamu zake kuanza kupotea huku akichukuliwa na usingizi mzito. Kitu pekee alichoambulia ni kuhisi maumivu kwenye mguu wake wa kulia na kichwa chake kilichoelemewa na uzito. Aliuinua mkono wake wa kulia na kuanza kujipapasa kichwani taratibu na hapo akagundua kuwa alikuwa amefungwa bendeji kukizunguka kichwa chake.

Hata hivyo, alipiga moyo konde na kumshukuru Mungu kwa kumweka hai hadi wakati ule kwani aliamini kuwa mambo mengine angeyafahamu baadaye.

Alikuwa na maswali kadhaa kichwani kwake lakini alijua kuwa asingeweza kupata majibu katika tafakari yake na badala yake aliyatembeza kwa siri macho yake kuyapeleleza mazingira ya mle ndani. Alikuwa amelala kitandani kwenye foronya laini na mto wa kuegemeza kichwa. Alikuwa na kila hakika kuwa alikuwa ndani ya nyumba ila hakujua nyumba ile ilikuwa ya nani na alifikaje hapo!

Alikuwa bado amevaa suruali ya blue ya jeans na t-shirt nyeusi, na alipotazama mbele ya kile kitanda alicholazwa akaliona dirisha kubwa la kioo na akaweza kubaini kuwa muda ule ulikuwa ni asubuhi kwani miale hafifu ya jua la asubuhi ilikuwa inapenya na kuingia mle chumbani dirisha hilo.

Hakutaka kuendelea kulala, alinyanyuka taratibu toka pale kitandani na kuketi kitako, na wakati akifanya hivyo alihisi maumivu makali yakipenya kwenye mguu wake wa kulia. Kichwa chake nacho kilikuwa kizito na hakikuonesha utulivu hata kidogo kutokana na kizunguzungu kilichokuwa kimemshika, hata hivyo alijitahidi akaketi na kuanza kuyazungusha macho yake taratibu kuyatazama mazingira ya chumba kile.

Lakini alisitisha uchunguzi wake baada ya kuona kitasa cha mlango wa kile chumba kikizungushwa taratibu. Tukio lile likayavuta macho yake kuutazama ule mlango huku moyo wake ukipoteza utulivu katika kiwango fulani. Mlango ulipofunguka Tunu akamwona Tom akiingia mle ndani. Wakatazamana kwa sekunde kadhaa na Tom alipomwona Tunu ameamka na kuketi kitako akaachia tabasamu.

Tom alikuwa amevaa mavazi ya michezo, tracksuit nyekundu na raba nyepesi nyeusi aina ya Kung Fu na alionekana kuwa alikuwa ametoka kufanya mazoezi ya karate, kwani alikuwa amening’iniza chain shingoni na taulo dogo la kufutia jasho begani kwake huku jasho jepesi likiwa linamtiririka taratibu mwilini.

“Tom!” Tunu aliita kwa mshangao uliochanganyika na furaha baada ya kumwona akiwa amesimama mbele yake akimtazama kwa tabasamu.

“Tunu!” Tom naye akaita kwa furaha huku akiharakisha kuelekea pale kitandani alipoketi Tunu na kumkumbatia kwa furaha. “Thanks Lord!” Tom alisema kwa sauti ya chini huku akizidi kumkumbatia Tunu.

Walikumbatiana kwa kitambo fulani huku kila mmoja wao akionesha hisia za furaha kwa mwenzake. Tom alipomwachia Tunu na kumtazama usoni alikuwa amelengwa na machozi ya furaha. Tunu alimtazama kwa Tom makini.

“Hivi nimefikaje hapa?” Tunu alimuuliza Tom kwa shauku kubwa ya kutaka kufahamu kile kilichokuwa kimetokea huku wakitazamana kwa furaha.

“Uliokolewa na kina Bob baada ya kutekwa na watu wa Mr. Oduya na kuletwa hapa baada ya Bob kuwasiliana na mimi,” Tom alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

Mara Tunu akakumbuka kuwa kabla hajapoteza fahamu na kulala usingizi mzito akiwa ndani ya ile taxi alikuwa ameliona gari la Bob, aina ya Nissan Patrol.

“Bob yuko wapi?” Tunu aliuliza kwa shauku huku furaha yake ikizidi kuongezeka.

“Ametoka sasa hivi, amempeleka daktari mmoja rafiki yangu aliyekuja kukuhudumia, lakini yule mwenzake yupo sebuleni amepumzika…” Tom alisema huku akimtazama Tunu kwa makini. “Vipi unajisiaje kwa sasa?”

“Nahisi maumivu kwenye mguu wangu wa kulia, kichwa nacho kinauma kidogo na kizunguzungu. Kwani nini kilinitokea?” Tunu alisema huku akifinya macho yake.

“Ulichomwa sindano fulani yenye dawa ya kuupumbaza ubongo wako ili usiweze kuwaletea matata na kama ungeachwa hivyo hivyo bila kupatiwa antidote basi ingekuchukua saa arobaini na nane kuweza kuzinduka na kurudia hali yako ya kawaida,” Tom alisema maneno yaliyomfanya Tunu asisimkwe mwili wake.

“Na begi langu la laptop liko wapi?” Tunu akauliza tena kwa wasiwasi baada ya kutokuliona begi lake la laptop sehemu yoyote mle chumbani.

“Usihofu, lipo mahala salama, begi pamoja na vitu vyako vyote ikiwemo bastola na simu,” Tom alisema huku akimpetipeti Tunu mgongoni katika namna ya kumtoa hofu.

“Basi fanyafanya mpango unitafutie msosi, nina njaa ya kufa,” Tunu aliongea kwa utulivu huku akipiga mwayo hafifu.
“Usijali, tayari chakula kimeshaandaliwa. Kuna mchemsho wa ndizi nyama, mchemsho wa kuku, maziwa fresh na vitafunwa. Chaguo ni lako!” Tom alisema na kumtazama Tunu kwa utulivu huku akitabasamu.

Tunu naye aliachia tabasamu lake jepesi huku akijiinua toka pale kitandani lakini akaketi tena juu ya kitanda baada ya kuhisi kizunguzungu. Akayafumba macho yake huku akivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu.

Tom alimtazama kwa makini, “Pumzika kwanza, Tunu, nitakwenda kukuchukulia chakula na ukila kila kitu kitakuwa sawa,” Tom alisema na kumuaga Tunu kisha akaondoka kuelekea kule jikoni akimwacha pale kitandani.

Mara tu Tom alipoondoka mle chumbani ile hali ya upweke ikamrudia tena Tunu pale kitandani huku akiupisha utulivu kichwani mwake. Alipoitazama saa yake ya mkononi akagundua kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa moja na robo ya asubuhi, hapo fikra zake zikahamia kutafakari juu ya kazi iliyokuwa mbele yake. Alitamani sana aangalie kilichomo kwenye ile memory card kabla ya mambo mengine yote na alikuwa akimuomba Mungu kusiwe na chochote kilichofutwa.

Mambo bado ni 🔥🔥🔥 kwelikweli. Ili kujua kitakachoendelea, endelea kufuatana nami katika safari hii ya kusisimua ndani ya 🚖...

NB: Litro 👩
 
askofu asante sana leo kama yote kuna vitu viananiuzi kama kwann Tunu hakumuua Victor kabisa au kwann kina bob hawakumuua Casmir au kwanini walivomteka tu Tunu wasimuue hapo hapo
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom