Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (135)

ILIPOISHIA

“Sawa! lakini hebu kumbuka vizuri ulipoihifadhi memory card, naamini kabisa kuwa itakuwa pamoja na simu yako. Je, simu ipo wapi, au nayo uliiacha kule kule nyumbani?” Tunu aimuuliza Winifrida kwa sauti tulivu ya kubembeleza huku moyoni akijyapima maneno yake kama yalikuwa na ukweli wowote.

“Kwa kweli sikumbuki,” Winifrida alijibu na kumfanya Tunu asitishe mohojiano, alibaki akimtazama kwa makini ingawa Winifrida aliendelea kuyakwepesha macho yake pembeni yasikutane na ya Tunu, na kwa hali ile Tunu akajua kuwa Winifrida alikuwa akimficha jambo fulani ambalo asingeweza kumlazimisha aliweke bayana kwa wakati ule.

“Sawa kama hujisikii kuniambia, inawezekana pengine huniamini au ni kweli hujui. Lakini elewa kuwa mimi pia nimeumizwa sana na matukio haya ya kaka yako na wifi yako, nisingeweza kustahimili kuacha kazi zangu zote na kufuatilia suala hili moja tu,” Tunu alisema huku akijinyoosha.

“Basi niitie wifi yako nimuage niondoke zangu, nitaendelea kuwepo hapa jijini kwa muda wa siku kadhaa, hivyo siku ukijisikia kuniambia chochote namba zangu hizi hapa, wewe nibip tu,” Tunu alimwambia Winifrida huku akisimama na kunyoosha mkono wake kumpa business card yenye namba zake za simu.

Winifrida alionekana kusita kidogo, aliitazama ile kadi kwa wasiwasi kisha macho yake yakahamia kwenye uso wa Tunu, “Basi kaa, n’takwambia ukweli...” alisema huku akimeza mate kutowesha koo lake lililokauka. Tunu alimtazama kwa makini na kuketi tena juu ya sofa.

ENDELEA...

Winifrida alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu kisha akabaki kimya huku akiminyaminya viganja vyake huku akivitazama. Tunu alimtazama kwa tabasamu kwa kitambo fulani.

“Niambie basi, shoga’angu!” Tunu alisema kwa sauti ya chini ya kubembeleza huku akitabasamu.

Winifrida alitaka kuongea neno lakini akasita, aibu ilimwingia, akajifunika uso wake kwa viganja. Tunu aliendelea kumtazama kwa makini huku akitabasamu.

“Naomba kwanza uniambie ukweli, umejuana vipi na kaka Sammy?” hatimaye Winifrida aliuliza huku aibu ikijionesha waziwazi usoni kwake

“Na wewe niambie, una boyfriend?” Tunu naye alimuuliza Winifrida huku akiendelea kutabasamu.

Winifrida alionekana kushtuka sana lakini hakuonesha moja kwa moja. Alimtazama Tunu moja kwa moja machoni huku akijitahidi kuifukuza aibu. Kisha akatingisha kichwa chake juu na chini, kushoto na kulia, alikuwa amekubali na kukataa kwa wakati mmoja, halafu akafunika uso wake kwa viganja tena na kuficha uso kwenye mapaja. Safari hii Tunu hakutabasamu. Alimtazama kwa kina. Winifrida aliinuka huku akimtazama Tunu kwa aibu kisha akajaribu kujiweka sawa kwenye sofa. Alionekana kuwa na hofu iliyochanganyika na aibu.

Okay, kama hutaki kuniambi ngoja mimi nikwambie...” Tunu alisema kwa sauti tulivu huku akijiweka sawa kwenye sofa, “Sammy alikuwa boyfriend wangu… ndiye alikuwa mwanamume wangu wa kwanza, wakati huo alikuwa hajaoa bado. Sasa hebu fikiria, utajisikiaje pale mtu unayempenda sana anapopata matatizo kama haya!”

Winifrida alibaki kimya akionekana kumsikiliza Tunu kwa makini sana. Maneno yale yalionekana kumwingia vilivyo. Akavuta pumzi ndefu huku hofu yake ikionekana kupungua. “Niahidi kwamba hutamwambia kabisa kaka Sammy wala mtu mwingine,” alisema kwa aibu.

“Nilikuahidi na ninakuahidi tena, yote haya yatabaki kuwa siri yetu wawili,” Tunu alisema kwa msisitizo.

“Basi subiri nikuoneshe,” Winifrida alisema na kuinuka, akaelekea chumbani kwao akimwacha Tunu akimsindikiza kwa macho nyuma yake, kisha akatingisha kichwa chake huku akiachia tabasamu.

* * * * *

Katika ofisi ya Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alikuwa hatulii kwenye kiti chake. Kiti chake kilikuwa kama chenye moto. Hakikukalika kabisa. Mara aliinuka mara aliketi kana kwamba alikuwa amekalia makaa ya moto ambayo yalimuunguza kila alipojaribu kuketi. Alikuwa amemezwa na fikra na hakuwa na furaha wala amani kabisa.

Mkono wake wa kulia alikuwa ameshika redio ya upepo akionekana mwenye wasiwasi. Mara kwa mara aliinua mkono wake wa kushoto na kutazama saa yake ya mkononi kisha alitingisha kichwa chake. Alikuwa akiwasubiri askari wake wamletee taarifa ya kiuchunguzi ambayo ilitakiwa iwasilishwe saa kumi na mbili jioni ya siku hiyo, kwenye kikao kati ya wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama na Mawaziri wa Mambo ya Ndani na Waziri wa Ulinzi.

Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alitamani aipate taarifa hiyo mapema ili aipitie na kurekebisha kasoro kabla hajaenda kwenye kikao hicho. Ni muda mfupi tu uliopita alikuwa amepigiwa simu na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Solomon Zirro akitakiwa kuwasilisha taarifa ya uchunguzi wa kile kilichokuwa kimetokea ili kijadiliwe kwenye kikao hicho.

Kabla ya simu hiyo macho yake yalikuwa yakiitazama chati yake ya taarifa za uhalifu katika Kanda Maalumu ya Dar es Salaam huku akijipongeza kwa jinsi ilivyoonesha kuwa tangu akabidhiwe jukumu hilo idadi ya vitendo vya uhalifu ilikuwa imeshuka kwa kasi. Uhalifu mkubwa ulipungua sana na kubakia udokozi mdogomdogo, wizi wa kuaminiana na ufisadi wa mali za umma. Ingekuwa ni amri yake, alitamani sana jiji la Dar es Salaam liwe jiji la kwanza duniani lisilo na uhalifu.

Lakini shambulio la bomu kwenye nyumba ya Sammy liliashiria kuwa mambo hayakuwa shwari kama alivyodhani. Sasa kichwa chake kiliwaka moto, alikuwa mtu wa kwanza aliyestahili kuwa na wasiwasi na hali hiyo kwani ndiye aliyekabidhiwa jukumu la kusimamia usalama wa raia na mali zao katika Kanda Maalumu ya Dar es Salaam. Alikuwa akiumiza kichwa chake na kukesha usiku na mchana kuhakikisha hakuna tukio lolote la kutishia usalama ndani ya jiji hilo linalotokea.

Aliishukuru sana falsafa ya ulinzi shirikishi kwani ilikuwa imesaidia sana kulifanya jiji la Dar es Salaam nan chi kwa ujumla kuwa na hali ya utulivu. Hata hivyo, alijikuta akiingiwa na simanzi mara baada ya kukumbuka kwamba, kama ilikuwa imefikia hatua raia wenyewe walishirikishwa kukesha nje wakijilinda, jukumu lililopaswa kufanywa na vyombo vya usalama, basi hilo ni jambo ambalo hakulipenda kabisa ingawa hakuwa na namna nyingine ya kufanya.

Alijiuliza, kama raia walikuwa wakijilinda wenyewe, je, vyombo hivyo vya ulinzi na usalama vilikuwa vinafanya nini? Inamaana haviwezi? Havifai? Au haviaminiki? Na kama hivyo ndivyo, je, kulikuwa na umuhimu gani wa kuwa na vyombo hivyo na kuvitengea bajeti kila mwaka? Maswali hayo yalimfikirisha sana Naibu Kamishna Ramon Mamboleo, aliamua kuja na mpango kabambe wa kuhakikisha hali hiyo inakoma, kwani alikuwa askari mwaminifu aliyeipenda na kuiamini kazi yake. Alitamani kuona raia wote ndani ya jiji la Dar es Salaam wakilala usingizi wao kwa amani.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus mtugani wa wapi huyo chiqutitta ndukulusudicho

NB: Litro 👩
 
Taxi - (136)

Akiwa bado amezama kwenye lindi la fikra nzito alishtushwa toka kwenye mawazo yake baada ya mlango wa ofisi yake kugongwa mara moja na kisha kufunguliwa, askari wake wawili machachari wakaingia. Hawa walikuwa Inspekta Abel na Sajenti Mapunda ambao walipoingia walisimama mbele ya meza yake kwa ukakamavu na kupiga saluti.

“Vipi, umepata kitu?” Naibu Kamishna Ramon Mamboleo aliuliza mara baada ya kujibu ile salamu huku akiwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wa Inspekta Abel. Muda huo alikuwa amesimama kandokando ya meza yake akiwa ameshika kiuno. Uso wake ulikuwa bado umemezwa na fikra na sononeko.

“Ndiyo, afande!” Inspekta Abel aliitikia kwa ukakamavu huku akinyoosha mkono wake kumkabidhi Naibu Kamishna Ramon Mamboleo faili dogo lenye taarifa za uchunguzi alilokuwa amelishika mkononi.

Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alilipokea lile faili kisha akaketi kwenye kiti chake huku akiwaashiria wale askari waketi. Wote wakaketi kwenye viti vilivyokuwa vinatazamana vikiwa mbele ya meza ya Naibu Kamishna Ramon Mamboleo.

Mamboleo alilifungua lile faili, akajiegemeza kwenye kiti chake na kupitia harakaharaka lakini kwa umakini mkubwa ile taarifa kisha akaziangalia nyaraka zingine kutoka kampuni ya mawasiliano iliyoonesha namba zote za simu alizopigiwa Sammy na ujumbe mfupi aliotumiwa, kisha akaziangalia picha kadhaa zilizokuwa zimeambatanishwa na taarifa ile na kuachia tabasamu. Ingalau sasa alikuwa amepata cha kuelezea, na pia mahali pazuri pa kuanzia. Ilikuwa ni kheri kwake, askari ambao aliwapa kazi ya kufanya uchunguzi wa matukio hayo walipata kitu cha ziada ndani ya muda mfupi.

Baada ya kuipitia taarifa ile kwa takriban dakika ishirini, Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alitulia kwa dakika zipatazo mbili, akavuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu.

“Ingalau tumepata pa kuanzia, hata hivyo, bado nawahitaji sasa mchimbue zaidi, hawa wote waliohusishwa humu nataka wahojiwe na wale mtakaohisi kuhusika muwatie ndani,” Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alisema huku akilifunga lile faili.

“Sawa, afande!” Inspekta Abel aliitikia kwa sauti ya ukakamavu.

Naibu Kamishna Ramon Mamboleo aliinuka na hapo hapo Inspekta Abel na Sajenti Mapunda nao wakainuka na kusimama kwa ukakamavu. Wakapeana mikono na kuagana.

* * * * *

“Vyote ni shilingi laki moja na elfu thetathini na tano tu,” mhudumu mmoja wa kike alisema akimtazama Tom kwa makini. Hayo yalitokea ndani ya ‘supermarket’ kubwa iliyopo kwenye majengo ya Mlimani City eneo la Mwenge jijini Dar es Salaam, ambapo Tom alikwenda kujipatia mahitaji muhimu kwa ajili yake na Tunu.

Baada ya kutajiwa kiasi, Tom alizama mfukoni na kutoa wallet yake, akahesabu kiasi hicho cha fedha na kumkabidhi yule mhudumu na kupewa risiti yake, akaaga na kuanza kupiga hatua kutoka huku akisukuma torori dogo lililojaa bidhaa mbalimbali ambazo zilikuwa zimefungashwa ndani ya mifuko yenye chapa ya jina la ‘supermarket’ hiyo. Tom alikuwa bado amevalia suti nyeusi, kofia na miwani myeusi ya jua.

Wakati akitoka kulifuata gari lake lililokuwa limeegeshwa katika viunga vya maegesho ya magari ndani ya uzio wenye ulinzi wa Mlimani City, aliyazungusha macho yake kutazama pande zote kabla hajajivuta taratibu kuelekea kilipo chombo chake cha usafiri. Muda huohuo simu yake ya mkononi ikaanza kuita, Tom aliiangalia kwa makini na kuliona jina la Tunu, akashusha pumzi na kuipokea.

“Hello!”

“Tom, usije tena, nimewasiliana na Bob Chopa na tumekubaliana kuwa kwa sababu za kiusalama yeye ndiye atanifuata huku, halafu wewe tutakutana Kinyerezi. Sijui wewe umefikia wapi?” Tunu aliuliza kwa sauti iliyoonesha furaha isiyo kifani.

“Nimefanikiwa, sasa ndo natoka hapa Mlimani City,” Tom alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Una uhakika kila kitu kiko sawa? Hakuna shaka yoyote?” Tunu aliuliza kwa shauku.

Yeah, hali ni shwari ila kama kitatokea chochote nitakujulisha,” Tom alisema huku akiyazungusha macho yake pembe zote kuangalia kama kulikuwa na mtu yeyote aliyemtilia shaka.

“Basi nitakukuta huko kuanzia saa mbili usiku, itanibidi kwanza nipitie nyumbani kwangu Sinza nika...” Tunu alijibu.

“Kuwa makini sana, kuna watu wamewekwa huko kukusubiria,” Tom alimuasa Tunu.

“Usihofu, Tom, ninajua... huu ni mchezo mdogo sana kwangu, wenyewe watashangaa na roho zao,” Tunu alisema huku akiangua kicheko hafifu.

“Na vipi kuhusu gari?”

“Wacha likae palepale Elli’s, lipo mahali salama.”

Okay, see you later,” Tom alisema huku akilifikia gari lake aina ya Toyota Rav4 L jeupe, akazungusha tena macho yake pembe zote kuangalia kama kulikuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia, hakumwona.

See you,” Tunu alisema na kukata simu.

Tom akafungua kwanza mlango wa nyuma wa gari na kutia mizigo yake huko kisha akaelekea kwenye mlango wa dereva na kuufungua akaingia na kuketi halafu akatia gari moto. Alitokea kwenye geti la upande wa kaskazini kwenye barabara ya Survey, kisha akaingia upande wa kulia akiifuata barabara ya Survey. Ikapita kama sekunde tano tu, gari lingine aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya bluu lililokuwa na namba bandia ambalo pia lilikuwapo kwenye viunga vya maegesho ya Mlimani City, nalo likatoka kumfuata.

Tom pasipo kujua akaendelea na safari yake, aliufikia mzunguko wa barabara za Sam Nujoma na ile ya Survey na kuingia kulia akiifuata barabara ya Sam Nujoma. Alipoifikia barabara ya Igesa iliyokuwa inakwenda kutokea Sinza akaburini, Tom akaamua kupima upepo ili aone kama kulikuwa na gari lolote lililokuwa limemuungia mkia nyuma, hivyo akakunja kushoto kuifuata barabara ile.

Lile gari aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya bluu lililokuwa nyuma yake likiyaacha magari matatu katikati yao nalo likakunja kuelekea barabara ile, Tom akaanza kupata shaka kwamba huenda alikuwa anafuatiliwa. Kwa kutazama vioo saidizi vya pembeni vya gari lake alipata kuliona gari lile vizuri, akakumbuka kuwa alikuwa ameliona pale kwenye viunga vya maegesho ya Mlimani City.

Akaamua kuongeza kasi ya gari lake ili kuona kama na wao wangeweza kuongeza mwendo. Alipotazama tena kwenye vioo saidizi vya pembeni akaliona lile gari nalo likiongeza mwendo huku likijaribu kuyapita magari yaliyokuwa mbele yake. Sasa Tom hakuwa na shaka kuwa alikuwa anafatwa. Akaona afanye jambo ili kuwapoteza.

Inaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (137)

Alizidisha mwendo na alipofika Kanana Car Garage, kabla hajalifikia duka moja la kuuza keki, maarufu kama Happiness House of Cakes akakunja kushoto akiufuata mtaa mmoja fupi hadi alipokutana na mtaa mwingine wa Social uliokuwa unatokea barabara ya Shekilango na kuishia katika mtaa wa Mjiasali. Hapo akakunja kuingia kushoto kuufuata ule mtaa wa Social, sasa alikuwa anarudi alikotoka.

Kwa kuwa mtaa ule haukuwa na magari mengi aliamua kuendesha gari lake kwa mwendo wa kasi hadi alipoupata mtaa wa Mjiasali akakunja kuingia upande wake wa kulia, kisha akaingia tena kushoto akiifuata barabara ya Igesa na kwenda kutokea barabara ya Sam Nujoma. Hapo akavuka taa za kuongozea magari barabarani bila kujali kama taa nyekundu ilikuwa imewashwa kumtaka asubiri, kidogo asababishe ajali lakini hakujali, akakunja kuingia kulia akionekana kurudi eneo la Mlimani City.

Aliendesha kwa fujo aliyapita magari mengine hadi alipoufikia tena mzunguko wa barabara za Sam Nujoma na ile ya Survey, akakunja kuingia kushoto akiifuata barabara ya Survey. Ndani ya muda mchache, akawa amelipoteza kabisa lile gari lililokuwa linamfuatilia. Sasa aliazimia kupitia barabara ya Makongo kisha akatokee Mbezi Mwisho ili kwenda Kinyerezi.

Alipohakikisha kuwa amefanikiwa kuwapoteza akaona ni vyema amtaarifu Tunu juu ya jambo hilo. Akampigia simu na kumweleza yote yaliyotokea na jinsi alivyofanikiwa kuwapoteza, kisha wakaonyana kuendelea kuwa waangalifu ili wasije wakaharibu mambo wakati wapo katika hatua za mwisho kukamilisha uchunguzi wao.

* * * * *

Saa moja na nusu usiku, gari aina ya Nissan Patrol la rangi ya bluu lilimshusha Tunu katika mtaa wa pili toka barabara ya Mori, katika eneo la Sinza Mori. Eneo alilorushwa lilikuwa umbali wa takriban mita mia tano toka ilipo nyumba ya Tunu, jirani na Kanisa la Reality of Christ. Tunu hakutaka wamfikishe hadi nje ya nyumba yake kwa sababu moja kubwa ya kutotaka kushtukiwa na mtu yeyote ambaye angekuwa ameweka mtego wa kumnasa.

Aliposhuka akaamua kuingia kwenye uchochoro wenye kiza hafifu uliomchukua hadi kwenye mtaa ule wenye nyumba yake kisha akazunguka kuelekea nyuma ya nyumba yake, lakini kabla ya kufanya chochote akaamua kufanya uchunguzi ili kujiridhisha kuhusu usalama wa eneo lote.

Japo hakuweza kumwona mtu yeyote nje ya nyumba ile iliyokuwa na giza kutokana na kutowashwa taa lakini aliamua kuchukua tahadhari zote, alitumia mbinu yake ya kijasusi kuupanda ukuta na kurukia ndani pasipo kutoa kishindo, kisha akaingia ndani ya nyumba kupitia dirisha dogo la jikoni huku akiwa amechukua tahadhari zote za kukwepa kumshtua kiumbe yeyote ambaye angekuwa ameweka mtego mle ndani.

Akiwa anaifahamu vizuri ramani ya nyumba yake, mara tu alipokiacha chumba cha jiko akaingia upande wake wa kulia akiifuata korido ndogo pembeni ya sebule ili aelekee vyumbani, mkono wake wa kuume ulikuwa umeshika bastola yake ndogo ya kijasusi aina ya Glock 19M, macho yalikuwa yamemtoka kukodoa na masikio yake yamesimama kusikiliza.

Hapo akasita kwanza kusikilizia kama yu salama. Alipoona kimya, akapiga moyo konde na kuanza kusonga zaidi. Kisha akahisi kusikia sauti hafifu ya mtu akisogea, alipogeuka kutazama nyuma alikuwa tayari amechelewa kwani mtu mmoja alikuwa amemfikia karibu yake! Kabla hajajua afanye nini akasikia sauti ya kilimi cha bastola kilichovutwa ikipenya masikioni mwake kumwonya asifanye chochote. Ikabidi asitishe kile alichokuwa akitaka kukifanya na hakuwa na namna nyingine ya kufanya zaidi ya kuanzisha mapambano ya ana kwa ana katikati ya giza lile.

Upesi akanyoosha mkono wake wenye bastola lakini kwa kasi ya ajabu ule mkono ukapigwa teke na bastola ile ikadondoka chini! Moyo wake ulikuwa kama uliosimama ghafla kabla ya kurudia mapigo yake na kuanza kwenda mbio huku jasho jepesi likianza kutoka. Hata hivyo alijiweka sawa kwa jili ya pambano.

“Nilikuwa natarajia ujio wako, Tunu,” Victor alisema huku akimwelekezea bastola yake aina ya 45 Colt. Victor alikuwa amevalia mavazi meusi yaliyomfanya aonekane kama kivuli, shati linalobana mwili pamoja na suruali nyepesi mithili ya ‘traki’.

Tunu hakutia neno. Akili yake ilikuwa inafanya kazi haraka sana baada ya kugundua kuwa alikuwa anapambana na Victor. Wakati Victor akijiandaa kufyatua risasi alishtukia akipigwa pigo ambalo hakuweza kulielewa kwa haraka lilipigwa kwa mtindo gani kiasi cha kuweza kuipokonya bastola yake mkononi. Ile bastola ikaangukia sehemu fulani sakafuni ndani ya ile nyumba na kutokana na kiza kilichokuwemo mle ndani hakuweza kuiona.

Kabla hajajua afanye nini, Tunu alizunguka kwa kasi ya ajabu akitupa pigo la ngumi usawa wa shingo ya Victor lakini ilikuwa kazi bure kwani Victor alikuwa mwepesi kuishtukia hila yake hivyo pigo la Tunu lilikata upepo bila kutoa majibu na kumfanya apepesuke kwa kupoteza mhimili na wakati huohuo akajikuta akipokea kipigo cha ngumi mbili kavu za chapuchapu mbavuni mwake.

Victor alikuwa mwepesi sana kiasi cha kumshangaza sana Tunu, alirusha ngumi nyepesi na za haraka. Alikuwa mwepesi sana lakini mashambulizi yake hayakuwa na madhara kwa Tunu. Mara kwa mara Tunu alitabiri mwenendo wake na hivyo basi ikawa rahisi kumkabili adui yake. Alipopiga pigo jingine la teke Tunu aliwahi kulikwepa kwa kuruka hewani kwa mtindo wa samasoti na alipokuwa akitua chini alibinuka na kuachia teke farasi. Lilikuwa pigo zuri lililomfanya Victor kugugumia kwa maumivu.

Tunu hakutaka kumkawiza, akamfuata katika mtindo wa kujiviringisha sakafuni kama gurudumu na alipomfikia akajizungusha na kumchota mtama wa chini lakini Victor aliwahi kumshtukia, akamtandika teke la kifuani lililomrusha nyuma. Jambo ambalo Tunu hakuwa akilifahamu ni kwamba, Victor alikuwa ana silaha nyingine kwenye mwili wake, alikuwa na visu na alikuwa mzuri zaidi kwenye matumizi ya silaha kuliko mapigano ya kawaida.

Basi waliendelea kupimana ubavu, Tunu alikuwa anajipindua na kurusha mateke kwa haraka sana, kisha alimgeuzia mgongo Victor na kupaa juu na kujigeuza huku akiwa ametanua miguu yake na kuutanguliza mguu wake wa kulia kwa nguvu huku ukifuatiwa na mguu wa kushoto. Victor akafanya jitihada za kujikinga na shambulizi hilo huku akiwa tayari amechomoa kisu toka kwenye mguu wake na kukishika vyema mkononi.

Tunu alipotua chini akatahamaki kisu kikipita na kuuchana mguu wake wa kulia, damu ikaanza kumtoka. Tunu hakujali, akaruka hewani na kuganda ukutani huku mguu mmoja ukiwa umegota upande mmoja wa ukuta na mguu wake mwingine upande mwingine wa ukuta wa korido ile, kisha akajibetua na kuruka hewani huku akitua mbele ya Victor, na wakati huohuo akimtupia pigo moja matata la teke kifuani kwake lililomfanya apepesuke na kugugumia kwa maumivu,
Kuona hivyo, Victor akarusha kisu, lakini Tunu alikikwepa na kuruka hewani kisha akamshindilia Victor ngumi tatu mfululizo za mbavuni na kuzivunja. Victor akashika mbavu zake akiugulia huku akitema damu. Alikuwa anahisi maumivu makali sana. Hakuweza tena kuhimili kwani ngumi zile zilimfanya kuwa mdhaifu sana katika kupambana na Tunu.

Tunu aliruka tena hewani na alipotua aliachia teke mauti lililopoteza kabisa fahamu za Victor, teke jingine lilipotua Victor hakujua maumivu yake kwani tayari alikuwa amezirai.

Mambo ni 🔥🔥🔥 kwelikweli! Je, nini kitaendelea? Usichoke kufuatilia simulizi hii ya kusisimua...

NB: Litro 👩
 
Wakuu, kwanza niombe radhi kwa ukimya wangu, ni kwa vile sipo buheri. Nimeshauriwa kupumzika kwa siku kadhaa baada ya kupatwa na uchovu mkali uliosababisha nipoteze fahamu juzi jioni... Hata hivyo tupo pamoja...

NB: Litro 👩
Pole sana Bishop Hiluka, Mungu akufanyie wepesi katika ugonjwa upone Haraka
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom