Taxi (146)
ILIPOISHIA
“Tumegundua kuwa kwa siku za karibuni yamekuwepo mawasiliano ya simu kati ya Casmir Njoroge na wafanyakazi wako wawili, Silas Potela na dereva wako Madjid Chege, ambaye pia ana asili ya Kenya! Mawasiliano hayo yamemhusisha pia mtu mwingine kutoka Kenya, Robert Kamau, na tunadhani pia yumo humu nchini,” Inspekta Abel aliongeza huku akimtazama Mr. Oduya kwa makini.
“Inspekta, naona sasa unaanza kuvuka mipaka! Nimeshakwambia sihusiki na chochote kuhusu maisha binafsi ya wafanyakazi wangu lakini hutaki kunielewa!” Mr. Oduya alisema kwa kufoka. Kama sauti yake ilivyobadilika, sura yake pia ilikuwa imebadilika.
Kitambo cha sekunde kadhaa za ukimya kilipita, walibaki wakitumbuliana macho kwa namna ya kusomana mawazo yao. Kisha, taratibu tabasamu jipya lilianza kuchanua usoni kwa Mr. Oduya. Halikuwa tabasamu lile ambalo Inspekta Abel alilizoea. Hili lilikuwa tabasamu jembamba, lisilopendeza hata kidogo, tabasamu ambalo lilifuatiwa na swali, “Bado tu unataka maelezo zaidi, bwana inspekta?”
“Vifo vya watu watatu wanaokuhusu vimetokea, mmoja wao ametambuliwa kuhusika na uvamizi kwenye nyumba ya Sammy. Mwingine tena anayehusishwa na watu wako anapata ajali ya kutatanisha, pia amehusishwa kulipua nyumba ya Sammy. Kama unadhani utaweza kuwa na jambo la kuniambia, basi utanitafuta,” Inspekta Abel alisema na kunyanyuka.
Alisimama akamtazama Mr. Oduya kwa kitambo na kuachia tabasamu, “Natumai kupata msaada toka kwako, mzee wangu.” Akasema na kuanza kupiga hatua kuondoka huku akimwacha Mr. Oduya ameketi kimya akimsindikiza kwa macho makali wakati akitoka nje ya ofisi yake.
ENDELEA...
Baada ya yule inspekta wa polisi kutoka, Mr. Oduya alijiegemeza kwenye kiti chake na kushusha pumzi ndefu. Sasa aliona kuwa mambo yalianza kwenda mrama na maji kumfika kooni. Vifo vya Dulla, Uledi na Lisa vilianza kumgeuka.
Kama hiyo haitoshi, kushtukiwa kwa Casmir Njoroge na hata Robert Kamau ambaye alikuwa hajatiwa nguvuni kulianza kumweka Mr. Oduya matatani. Sasa akili yake ilianza kufanya kazi mara mbili, aliwaza jinsi ya kujinasua toka kwenye sakata hilo huku akihisi mwili wake ukipata joto zaidi.
Alifikiria kidogo kisha akachukua simu yake ya mkononi na kutafuta namba fulani za mshirika wake muhimu aliyepo ndani ya jeshi la polisi. Alipozipata namba hizo alitaka kupiga simu lakini akashtuka na kuirudisha ile simu, kisha akachukua simu nyingine ambayo hakuwa akiitumia kwa kila mtu, bali kwa watu wachache sana na kwa mawasiliano nyeti kama yale.
Alizinakiri zile namba kisha akapiga na kuiweka sikioni. Simu ikaita mara mbili na kupokelewa. “Hallo, nahitaji sana kukuona, mkuu…” Mr. Oduya aliongea mara ile simu ilipopokelewa.
“Vipi, kuna tatizo lolote?” sauti nzito ilisikika ikiuliza toka upande wa pili wa ile simu.
“Tatizo lipo, ni kuhusu mmoja wa vijana wako, Inspekta Abel… ningeomba tuonane hata sasa hivi kama inawezekana!” Mr. Oduya alisema na kusikiliza kidogo kisha asiongeze kitu, akakata simu na kuinuka lakini kabla hajatoka akakumbuka jambo. Akatafuta namba za Spoiler na kupiga kisha akaiweka ile simu sikioni.
“Silas, ni nini sasa umefanya?” Mr. Oduya alimdaka Spoiler juu kwa juu, aliongea kwa sauti iliyoashiria hasira. Spoiler hakujibu, alibaki kimya.
“Hivi umekuwaje? Mbona umeanza kuwa mzembe kiasi hicho?” Mr. Oduya aliuliza kwa hasira.
“Usijali, mkuu, mambo yatakuwa sawa tu,” Spoiler aliongea kwa wasiwasi.
“Ninahitaji
actions na siyo hizo soga zako!” Mr. Oduya alifoka. “Hivi unajua imenigharimu kiasi gani tangu uliposhindwa kutii agizo langu la kuliteketeza lile gari lililonunuliwa na Sammy?”
“Nisamehe, mkuu, naahidi kurekebisha makosa yote na kufuta kabisa ushahidi wote,” Spoiler alisema kwa kujitetea.
“Una uhakika?” Mr. Oduya aliuliza kwa sauti ya kufoka kidogo.
“Ninaamini hilo, mkuu. Kuanzia sasa nalishughulikia kwa umakini zaidi na wala jua halitakuchwa kabla sijafuta ushahidi wote,” Spoiler aliongea kwa msisitizo.
“Omba Mungu mpango huo utimie, vinginevyo hatutaelewana…” Mr. Oduya alisema kwa hasira na kukata simu kisha akaanza kupiga hatua kutoka nje, akaelekea kwenye chumba cha lifti na kushuka hadi chini. Sura yake ilionesha wazi hasira alizokuwa nazo.
Aliposhuka chini ya lile jengo alitembea taratibu huku mawazo yakiwa yamemtawala. Kitendo cha Spoiler kushindwa kizembe kukamilisha misheni aliyotumwa kilimuumiza kichwa, alianza kupoteza imani. Alielekea kwenye gari lake la kifahari aina ya
Range Rover Velar la rangi nyeupe, akamkuta dereva wake Chege akimsubiri. Dakika mbili baadaye lile gari lilikuwa linayaacha maegesho yake na kuelekea mjini.
* * * * *
Baada ya kutoka katika jengo la makao makuu ya ofisi za
The Splendid Group lililopo barabara ya Bagamoyo, eneo la Kijitonyama, jijini Dar es Salaam, Inspekta Abel alielekea moja kwa moja katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kinondoni, ya Mwananyamala.
Ilimchukua takriban dakika arobaini na tano kutoka ofisini kwa Mr. Oduya hadi Hospitali ya Mwananyamala, hali ambayo ilisababishwa na msongamano wa magari na ubovu wa barabara. Aliingia kwenye geti la kuingilia la hospitali hiyo na kwenda hadi katika viunga vya maegesho vya hospitali hiyo, akaliegesha gari lake jirani na gari nyingine aina ya
Toyota Alphard jeusi lenye vioo vyenye
tinted nyeusi.
Alishuka na kuanza kupiga hatua taratibu kuelekea katika jengo maalumu la wagonjwa mahututi alikolazwa Casmir Njoroge. Nje ya kile chumba maalumu cha wagonjwa wenye kuhitaji uangalizi maalumu alicholazwa Casmir, alimkuta askari wake Koplo Rashid, kijana mwembamba, mrefu, aliyevalia sare rasmi za polisi, akimsubiri.
Wakati Inspekta Abel anapokewa na Koplo Rashid pale nje ya kile chumba alicholazwa Casmir, Spoiler alikuwa analifikia gari lake aina ya
Toyota Alphard jeusi na kujipakia kisha akaliondoa taratibu kutoka eneo lile na kutokomea mtaani.
Mara Inspekta Abel akashangaa kumwona muuguzi wa kile chumba alicholazwa Casmir akitoka mle chumbani huku akiwa na uso uliojaa wasiwasi na kukimbilia kwenye ofisi ya daktari wa jengo lile. Kabla hajajua akamwona tena yule muuguzi akiwa ameongozana na daktari wakikimbilia kuelekea kwenye chumba alicholazwa Casmir.
“Nini kimetokea?” Inspekta Abel aliwauliza kwa wasiwasi huku akitaka kuzama ndani lakini lakini akazuiwa kwa kuwa mtu yeyote hakuruhusiwa kuingia humo muda huo. Inspekta Abel alitii na kusubiri pale nje huku akiwa na wasiwasi, alijaribu kuchungulia mle ndani kupitia kioo kidogo cha mlangoni lakini hakuweza kuona kitu
Baada ya dakika zisizopungua tano, yule daktari alitoka nje huku uso wake ukiwa umesawajika na jasho jepesi lilikuwa linamtoka usoni.
“Nini kimetokea, daktari?” Inspekta Abel aliuliza tena kwa wasiwasi. Alikuwa amepigwa na butwaa, mikono yake ilikuwa imeshika kiuno huku akimtazama yule daktari kwa makini. “Ni nini kimetokea?” akauliza tena baada ya kuona hajibiwi.
“Nashangaa, hali ya mgonjwa ilikuwa inaanza kuimarika vizuri na muda mfupi tu uliopita nilimwona, lakini imebadilika ghafla na mapigo ya moyo wake kushuka isivyo kawaida...” yule daktari alisema kwa huzuni na kunyamaza kidogo.
Inaendelea...
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus mtugani wa wapi huyo chiqutitta ndukulusudicho ADK aggyd BAHARI J
NB:
Litro 👩