Bishop Hiluka
JF-Expert Member
- Aug 12, 2011
- 7,147
- 14,711
- Thread starter
- #81
Taxi - (27)
Joyce alimsindikiza Sammy kwa macho na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha aligeuka kumtazama Winifrida huku akiwa amekunja sura yake, alitaka kusema neno lakini akasita.
* * * * *
Saa 2:30 usiku ilimkuta Mr. Oduya akiwa amesimama chumbani kwake mbele ya meza nzuri ya kisasa ya vipodozi maarufu kama ‘dressing table’ iliyokuwa na vioo virefu vitatu vilivyowekwa kuizunguka ile meza na kumfanya mtu ajione mara tatu, alionekana yupo katika harakati za kujiandaa ili atoke.
Mr. Oduya alikuwa amevaa suti ya bei ghali nyeusi aina ya Kenzo, shati jeupe la mikono mirefu na viatu vyeusi vya ngozi, alikuwa anachana nywele zake taratibu huku akijitazama kwenye vile vioo, kisha mikono yake ilianza kurekebisha tai yake ya rangi nyekundu shingoni.
Alionekana kuwa mtulivu sana huku akiwa amezama katika lindi la fikra, hata hivyo, alikuwa makini akimtupia jicho la wizi mkewe, Dk. Salma Oduya aliyekuwa amesimama kando yake akimtazama kwa makini huku amekunja sura yake.
Dk. Oduya alikuwa mwanamke mnene wa wastani, hakuwa mfupi wala mrefu bali alikuwa na kimo cha wastani na rangi ya maji ya kunde iliyokuwa ina mng’aro wa aina yake.
Akiwa na umri wa miaka hamsini na tano, alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mama wa watoto wawili: Omari Oduya aliyekuwa na miaka 30 na kwa wakati huo alikuwa anaishi nchini Marekani, na Zuhura Oduya aliyekuwa na miaka 26 na wakati huo alikuwa anachukua Shahada ya Umahili ya Maendeleo ya Uchumi wa Kimataifa nchini Uingereza.
Usiku ule Dk. Oduya alikuwa amevaa nguo nyepesi ya kulalia maarufu kama ‘night dress’ ya rangi ya samawati na alijifunga kitenge kiunoni, juu alivaa sweta la mikono mirefu na kichwani alikuwa amevaa kofia laini maalumu kwa kukinga nywele.
Muda ule wa saa mbili na nusu usiku upepo ulikuwa unavuma na kutengeneza sauti ya mvumo wa kustaajabisha kwenye matawi ya miti mikubwa ya kivuli iliyozunguka jumba la kifahari la Mr. Oduya, kadiri matawi ya miti yalivyocheza huku na kule kwa utulivu ndivyo mvumo ule ulivyosikika na kutengeneza sauti kama ya chatu mkali aliyehisi hatari kichakani.
Upepo ulivuma ukayasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha mawili makubwa mle chumbani.
Jumba la Mr. Oduya ambalo lilistahili kuitwa kasri, lilikuwa katika eneo la ufukweni mwa Bahari ya Hindi, Mbezi Beach, eneo lililokuwa na makazi ya watu wenye ukwasi mkubwa au viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Tanzania. Katika eneo lile tulivu yalionekana majumba kadhaa ya kifahari yaliyozungukwa na kuta ndefu na mageti makubwa mbele yake.
Lilikuwa jumba kubwa la ghorofa mbili lenye vyumba saba vya kulala kila kimoja kikiwa na maliwato yake, sebule tatu kubwa, kumbi mbili za chakula, majiko mawili ya kisasa, kaunta ya baa iliyokuwa katika sehemu ya chini ya jengo na sehemu mbili za ghorofani za kubarizi zenye kochi safi za sofa.
Eneo lile lilikuwa na barabara pana ya lami yenye usafi wa hali ya juu, iliyopandwa miti mizuri ya kivuli kando ya barabara. Muda ule wa usiku eneo lile lilikuwa na utulivu mkubwa sana huku likimulikwa na taa nzuri zenye mwanga mkali. Ni sauti kali za mbwa waliokuwa wakibweka eneo lile bila sababu za msingi ndizo zilizokuwa zinasikika kwa mbali na magari machache sana yalipita barabarani.
Ndani ya lile jumba waliishi watu kumi, watu wazima wanane na watoto wawili: Mr. Oduya mwenyewe na mkewe Dk. Oduya, ndugu watatu wa familia ya mkewe na watoto wao wawili, wahudumu wawili wa kike wa ndani na mhudumu mmoja wa kiume aliyesaidia shughuli za mifugo na shamba. Pia kulikuwa na walinzi watatu waliolinda kwa kupokezana, lakini hawakuwa wakiishi pale.
Hata hivyo, lile jumba lilikuwa na ulinzi madhubuti kwa kujengewa ukuta mrefu uliofungwa mfumo maalumu wa umeme wa kuzuia wezi juu yake na usiomwezesha mtu yeyote kuona mle ndani.
“Hivi wewe mwanamume, unajua mimi sikuelewi kabisa!” sauti ya Dk. Oduya ilimgutusha Mr. Oduya kutoka kwenye lindi la mawazo.
Muda wote Dk. Oduya alikuwa anamwangalia mumewe akionesha wazi kuwa alikuwa na hasira na sura yake alikuwa kaikunja na kutengeneza matuta madogo usoni.
“Kwa nini hunielewi?” Mr. Oduya alimwuliza mkewe bila kugeuka ingawa alikuwa akimtazama kupitia vioo vya kwenye meza ya vipodozi.
“Eti eeh! Unajifanya huelewi ninachomaanisha!” Dk. Oduya aliongea kwa hasira huku sasa akiwa ameshika kiuno chake kwa mikono yote miwili na kumkazia macho mumewe.
“Hapana naelewa,” Mr. Oduya alimjibu huku akigeuza shingo yake kumtazama kwa makini.
“Unaelewa nini?” Dk. Oduya alihoji huku macho yake yakiwa hayabanduki usoni kwa mumewe.
“Naelewa kwamba hunielewi kabisa!” Mr. Oduya alijibu huku hasira zikianza kuchipua ndani yake.
“Haya wewe endelea tu… huo umalaya wako wa uzeeni utakugharimu siku moja… ila usisahau kutumia condom usije ukaniletea maradhi,” Dk. Oduya alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.
“Naomba tusianze kuharibiana siku, unaropoka tu wala hujui naenda kukutana na kina nani saa hizi, hivi kwa mwendo huu nitaweza kweli kushinda uchaguzi wa urais kama hata kwenda kukutana na washirika muhimu wa kisiasa inakuwa nongwa!” Mr. Oduya alianza kulalamika.
“Wadau gani wa kisiasa? Hivi unaniona mimi mtoto mdogo siyo! Wewe si umetoka huko huko muda huu! Hata hujapumzika vizuri unataka kuondoka tena, eti kuwaona wadau wa kisiasa, ni wadau gani wasiokupa hata muda wa kupumzika na familia yako?” Dk. Oduya alizidi kuhoji,
Mr. Oduya alimtazama kwa makini, akataka kumjibu lakini alisita na kuamua kumpuuza, ni mwanamke aliyeishi naye katika ndoa kwa miaka therathini na moja. Alimchukulia kama mwanamke wa kawaida tu ambaye hakuwa na jipya zaidi ya maneno mengi mithili ya chiriku kila uchao.
Badala yake Mr. Oduya alichukua mkoba wake wa kiofisi na kugeuka, akaanza kupiga hatua za taratibu kuondoka, aliazimia kwenda kuumaliza usiku wa siku ile akiwa na Zainab, mwanadada mtundu mno na aliyekuwa amemuonesha ulimwengu mpya wa mapenzi, pamoja na umri wake mkubwa, alikiri kuwa hakuwa mjuzi kabisa.
Inaendelea...
Joyce alimsindikiza Sammy kwa macho na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha aligeuka kumtazama Winifrida huku akiwa amekunja sura yake, alitaka kusema neno lakini akasita.
* * * * *
Saa 2:30 usiku ilimkuta Mr. Oduya akiwa amesimama chumbani kwake mbele ya meza nzuri ya kisasa ya vipodozi maarufu kama ‘dressing table’ iliyokuwa na vioo virefu vitatu vilivyowekwa kuizunguka ile meza na kumfanya mtu ajione mara tatu, alionekana yupo katika harakati za kujiandaa ili atoke.
Mr. Oduya alikuwa amevaa suti ya bei ghali nyeusi aina ya Kenzo, shati jeupe la mikono mirefu na viatu vyeusi vya ngozi, alikuwa anachana nywele zake taratibu huku akijitazama kwenye vile vioo, kisha mikono yake ilianza kurekebisha tai yake ya rangi nyekundu shingoni.
Alionekana kuwa mtulivu sana huku akiwa amezama katika lindi la fikra, hata hivyo, alikuwa makini akimtupia jicho la wizi mkewe, Dk. Salma Oduya aliyekuwa amesimama kando yake akimtazama kwa makini huku amekunja sura yake.
Dk. Oduya alikuwa mwanamke mnene wa wastani, hakuwa mfupi wala mrefu bali alikuwa na kimo cha wastani na rangi ya maji ya kunde iliyokuwa ina mng’aro wa aina yake.
Akiwa na umri wa miaka hamsini na tano, alikuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Sheria katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mama wa watoto wawili: Omari Oduya aliyekuwa na miaka 30 na kwa wakati huo alikuwa anaishi nchini Marekani, na Zuhura Oduya aliyekuwa na miaka 26 na wakati huo alikuwa anachukua Shahada ya Umahili ya Maendeleo ya Uchumi wa Kimataifa nchini Uingereza.
Usiku ule Dk. Oduya alikuwa amevaa nguo nyepesi ya kulalia maarufu kama ‘night dress’ ya rangi ya samawati na alijifunga kitenge kiunoni, juu alivaa sweta la mikono mirefu na kichwani alikuwa amevaa kofia laini maalumu kwa kukinga nywele.
Muda ule wa saa mbili na nusu usiku upepo ulikuwa unavuma na kutengeneza sauti ya mvumo wa kustaajabisha kwenye matawi ya miti mikubwa ya kivuli iliyozunguka jumba la kifahari la Mr. Oduya, kadiri matawi ya miti yalivyocheza huku na kule kwa utulivu ndivyo mvumo ule ulivyosikika na kutengeneza sauti kama ya chatu mkali aliyehisi hatari kichakani.
Upepo ulivuma ukayasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha mawili makubwa mle chumbani.
Jumba la Mr. Oduya ambalo lilistahili kuitwa kasri, lilikuwa katika eneo la ufukweni mwa Bahari ya Hindi, Mbezi Beach, eneo lililokuwa na makazi ya watu wenye ukwasi mkubwa au viongozi wa ngazi za juu wa serikali ya Tanzania. Katika eneo lile tulivu yalionekana majumba kadhaa ya kifahari yaliyozungukwa na kuta ndefu na mageti makubwa mbele yake.
Lilikuwa jumba kubwa la ghorofa mbili lenye vyumba saba vya kulala kila kimoja kikiwa na maliwato yake, sebule tatu kubwa, kumbi mbili za chakula, majiko mawili ya kisasa, kaunta ya baa iliyokuwa katika sehemu ya chini ya jengo na sehemu mbili za ghorofani za kubarizi zenye kochi safi za sofa.
Eneo lile lilikuwa na barabara pana ya lami yenye usafi wa hali ya juu, iliyopandwa miti mizuri ya kivuli kando ya barabara. Muda ule wa usiku eneo lile lilikuwa na utulivu mkubwa sana huku likimulikwa na taa nzuri zenye mwanga mkali. Ni sauti kali za mbwa waliokuwa wakibweka eneo lile bila sababu za msingi ndizo zilizokuwa zinasikika kwa mbali na magari machache sana yalipita barabarani.
Ndani ya lile jumba waliishi watu kumi, watu wazima wanane na watoto wawili: Mr. Oduya mwenyewe na mkewe Dk. Oduya, ndugu watatu wa familia ya mkewe na watoto wao wawili, wahudumu wawili wa kike wa ndani na mhudumu mmoja wa kiume aliyesaidia shughuli za mifugo na shamba. Pia kulikuwa na walinzi watatu waliolinda kwa kupokezana, lakini hawakuwa wakiishi pale.
Hata hivyo, lile jumba lilikuwa na ulinzi madhubuti kwa kujengewa ukuta mrefu uliofungwa mfumo maalumu wa umeme wa kuzuia wezi juu yake na usiomwezesha mtu yeyote kuona mle ndani.
“Hivi wewe mwanamume, unajua mimi sikuelewi kabisa!” sauti ya Dk. Oduya ilimgutusha Mr. Oduya kutoka kwenye lindi la mawazo.
Muda wote Dk. Oduya alikuwa anamwangalia mumewe akionesha wazi kuwa alikuwa na hasira na sura yake alikuwa kaikunja na kutengeneza matuta madogo usoni.
“Kwa nini hunielewi?” Mr. Oduya alimwuliza mkewe bila kugeuka ingawa alikuwa akimtazama kupitia vioo vya kwenye meza ya vipodozi.
“Eti eeh! Unajifanya huelewi ninachomaanisha!” Dk. Oduya aliongea kwa hasira huku sasa akiwa ameshika kiuno chake kwa mikono yote miwili na kumkazia macho mumewe.
“Hapana naelewa,” Mr. Oduya alimjibu huku akigeuza shingo yake kumtazama kwa makini.
“Unaelewa nini?” Dk. Oduya alihoji huku macho yake yakiwa hayabanduki usoni kwa mumewe.
“Naelewa kwamba hunielewi kabisa!” Mr. Oduya alijibu huku hasira zikianza kuchipua ndani yake.
“Haya wewe endelea tu… huo umalaya wako wa uzeeni utakugharimu siku moja… ila usisahau kutumia condom usije ukaniletea maradhi,” Dk. Oduya alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.
“Naomba tusianze kuharibiana siku, unaropoka tu wala hujui naenda kukutana na kina nani saa hizi, hivi kwa mwendo huu nitaweza kweli kushinda uchaguzi wa urais kama hata kwenda kukutana na washirika muhimu wa kisiasa inakuwa nongwa!” Mr. Oduya alianza kulalamika.
“Wadau gani wa kisiasa? Hivi unaniona mimi mtoto mdogo siyo! Wewe si umetoka huko huko muda huu! Hata hujapumzika vizuri unataka kuondoka tena, eti kuwaona wadau wa kisiasa, ni wadau gani wasiokupa hata muda wa kupumzika na familia yako?” Dk. Oduya alizidi kuhoji,
Mr. Oduya alimtazama kwa makini, akataka kumjibu lakini alisita na kuamua kumpuuza, ni mwanamke aliyeishi naye katika ndoa kwa miaka therathini na moja. Alimchukulia kama mwanamke wa kawaida tu ambaye hakuwa na jipya zaidi ya maneno mengi mithili ya chiriku kila uchao.
Badala yake Mr. Oduya alichukua mkoba wake wa kiofisi na kugeuka, akaanza kupiga hatua za taratibu kuondoka, aliazimia kwenda kuumaliza usiku wa siku ile akiwa na Zainab, mwanadada mtundu mno na aliyekuwa amemuonesha ulimwengu mpya wa mapenzi, pamoja na umri wake mkubwa, alikiri kuwa hakuwa mjuzi kabisa.
Inaendelea...
