Nimefika Mkuu...Taxi - (5)
ILIPOISHIA
Dk. Masanja hakuitikia ile salamu ya Sammy wala hakumtazama usoni, aliendelea kulikodolea macho lile gazeti aliloshika mkononi huku uso wake ukiwa umesawajika na mawazo yake yakiwa mbali sana.
“Boss mbona leo unaonekana hauko sawa, kuna tatizo lolote?” Sammy aliuliza huku akiwa na mshangao mkubwa.
“Sina shida na salamu yako,” Dk. Masanja alisema huku akivuta mtoto wa meza na kuchukua bahasha ndogo ya khaki iliyokuwa na barua ndani yake, akanyoosha mkono wake kumpa Sammy bila hata kumtazama usoni. Uso wake ulikuwa bado umekunja ndita.
Sammy alishtuka sana na kuitazama ile bahasha kwa mshangao mkubwa, alishusha pumzi za ndani kwa ndani na macho yake yakatulia kwenye uso wa Dk. Masanja. Alimkazia macho huku akionesha wasiwasi mkubwa.
SASA ENDELEA...
“Kwani kuna tatizo gani, Boss?” Sammy aliuliza kwa wasiwasi huku akionekana kuchanganyikiwa kidogo.
“Unashtuka nini, kwani hujawahi kupewa barua?” Dk. Masanja alimuuliza Sammy huku akimtazama kwa mara ya kwanza tangu aingie ofisini kwake.
“Nimeshawahi kupewa, tena nyingi tu…” Sammy alisema huku akihisi jasho jepesi likianza kumtoka na ubaridi wa woga wa aina yake ukimtambaa mwilini.
“Sasa! Kinachokushtua ni nini?” Dk. Masanja aliuliza tena huku akiwa amemkazia macho Sammy.
“Hakuna tatizo, ila…” Sammy alitaka kusema lakini Dk. Masanja alimkata kauli.
“Kama hakuna tatizo basi chukua barua yako na usinipotezee muda wangu hapa,” Dk. Masanja alisema kwa sauti iliyovuma kwa ghadhabu huku akimkazia macho Sammy.
Sammy alimtazama yule mzee kwa makini, alitaka kunyoosha mkono wake kuichukua ile barua lakini akasita. Dk. Masanja alimkazia macho huku akimsisitiza kuichukua ile barua.
Sammy aliipokea na kuichana pale pale, akaifungua na kutoa karatasi iliyokuwa ndani yake, na hapo akakutana na na kichwa acha habari kilicoaandikwa: “Yahusu kusimamishwa kazi kwa utovu wa nidhamu na kuihujumu kampuni”
Sammy alipigwa butwaa na kuiachia ile barua ikadondoka sakafuni. Alishusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani huku akihisi mapigo ya moyo wake yakibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida!
“I can’t believe this! Unawezaje kunifanyia hivi?” Sammy aliuliza huku akikihisi joto kali sana likimtambaa mwilini! Alionekana kupatwa na mshtuko mkubwa sana kutokana na barua ile.
Dk. Masanja hakujibu bali alibaki kimya akimtazama Sammy kwa hasira. Kikapita kitambo kifupi cha ukimya huku wakitazamana kama majogoo waliotaka kupigana.
“Nimehukumiwa bila makosa! Sijawahi hata kupewa barua ya onyo, iweje leo naandikiwa kuwa mimi mtovu wa nidhamu na naihujumu kampuni! Lazima kuna kitu kinaendelea hapa, si bure,” Sammy alisema kwa uchungu.
“Kama unadhani hujatendewa haki unaweza kukata rufaa kwenye ngazi husika, ila kwa sasa hutakiwi kuwepo hapa na kampuni haitahusika na jambo lolote linalokuhusu,” Dk. Masanja alisisitiza.
Sammy alionekana kunywea sana utadhani kifaranga cha kuku kilichonyeshewa na mvua. Alifungua mdomo wake kutaka kusema lakini maneno hayakutoka, akabaki mdomo wazi huku akimkodolea macho Dk. Masanja. Donge la fadhaa lilikuwa limemkaba kooni.
Dk. Masanja alionekana kumpuuza Sammy na kuyahamishia macho yake kwenye lile gazeti alilokuwa ameshika mkononi, japo ilionekana wazi kuwa akili yake haikuwa pale.
Sammy aliinamisha uso wake chini na kuanza kutafakari, fikra zikamjia kwamba huenda alikuwa ndotoni, hata hivyo, hisia zake zilimtanabaisha kuwa ile haikuwa ndoto bali ni kitu halisi kilikuwa kinatokea.
Hakujua ni utovu upi wa nidhamu aliowahi kumfanyia mkuu wake wa kazi, kiasi cha kusimamishwa kazi. Hakukumbuka ni lini aliwahi kuihujumu kampuni! Kilichomjia akilini ni jinsi alikuwa akijitoa kwa moyo wake wote kuitumika kampuni ile na alivyomuheshimu mkuu wake wa kazi. Hakutaka kabisa kuamini kwamba kitu kama hicho kingeweza kutokea.
“I’m totaly confused! Au pengine huyu boss ana hofu ya kupokonywa cheo? Kwani tangu nimepata tuzo ya kimataifa kutoka taasisi ya Institute of Hospitality ya Uingereza naona kama amebadilika sana!” Sammy aliwaza.
Hata hivyo, aliyafuta mawazo hayo haraka kichwani kwake, kwani alikuwa na uhakika kuwa Dk. Masanja hakuwa na shida yoyote ya kung’ang’ania kile cheo, ingawa naye alikuwa kaajiriwa hapo New Udzungwa Beach Resort lakini alikuwa amejitosheleza kwa vitu vingi.
Mara mbili alitaka kuacha kazi ili akasimamie biashara zake lakini kampuni ilimuomba na hata kumuongezea mshahara mara dufu ili asiache kazi.
Si hivyo tu, alikuwa anamiliki migahawa miwili ya kisasa, mmoja ukiwa jijini Dar es Salaam na mwingine jijini Mwanza, alikuwa na ranchi ya ng'ombe wa kisasa wasiopungua therathini, shamba kubwa la matunda na mazao mbalimbali eneo la Ruvu mkoani Pwani, na nyumba kadhaa za kisasa alizozipangisha katika majiji ya Dar es Salaam na Mwanza.
Mkewe pia alikuwa anamiliki maduka makubwa mawili ya vipodozi na nguo za kike, maarufu kama boutique, yalikuwa katika majiji ya Dar es Salaam na Mwanza, na alikuwa mbioni kufungua duka jingine jijini Arusha. Pia mara kwa mara alikuwa akisafiri nje ya nchi kwenda kununua bidhaa.
Sasa Sammy alijiuliza, kama haikuwa hofu ya kunyang’anywa cheo kulikuwa na tatizo gani kubwa? “I need to find out,” aliwaza na kuzidi kutweta.
Pamoja na uwepo wa kiyoyozi mle ofisini kilichotoa ubaridi mkali lakini alianza kutokwa jasho. Mara kikohozi kidogo kikamtoka, na nyuma yake wimbi la machozi lilikuja mbio. Alijaribu kuyazuia machozi yasimtoke bila mafanikio, aliyafuta kwa kutumia viganja vyake vya mikono.
“Boss, unaweza kuniambia kwa nini unanifanyia hivi?” hatimaye Sammy alimudu kuuliza huku akiwa amefadhaika sana.
“Umefanya jambo la kipumbavu sana lililonifedhehesha mno… sasa toka ofisini kwangu kabla sijasahau kuwa sisi ni marafiki!” Dk. Masanja alimwambia Sammy huku akimtazama kwa macho makali yaliyokuwa yakiwaka kwa ghadhabu.
Sammy alijikuta akihamaki sana, alitaka kusema neno lakini akashindwa kutokana na donge la hasira kumkaba kooni, na mara alishangaa kuona ukungu mwepesi ukianza kutanda mbele ya macho yake. Alianza kupumua kwa nguvu huku miguu yake ikianza kuishiwa nguvu…
_____
Hakujua ni muda gani alikuwa ameutumia akiwa kasimama ofisini kwa Dk. Masanja na hakuamini kama ni kweli mambo yale yalikuwa yamemtokea.
Itaendelea...
Cc the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali
Naam! Nimeshatupia mzigo mwingine...Bishop..
asante mkuuNaam! Nimeshatupia mzigo mwingine...