Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (20)

Ilipoishia...

Madame Norah mwenye umri wa miaka 50, alikuwa mwanamke mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, alikuwa amejitosheleza kwa vitu vingi. Alimiliki kituo cha redio na cha televisheni, kampuni kubwa ya samani za majumbani na ofisini, mgahawa wa kisasa katikati ya jiji la Dar es Salaam na duka kubwa la vipodozi na nguo za kike.

Alikuwa mrefu na mweupe mwenye umbo kubwa kiasi lililosheheni vema na kunesanesa, likafanya kila jicho la mwanamume lililomuona kumtazama mara mbili mbili. Alikuwa mcheshi na mwenye ushawishi mkubwa asiyependa kuwa chini ya mwanamume, ndiyo maana hakutaka kuolewa.

Ingawa alikuwa na umri mkubwa, lakini ilikuwa vigumu mno kumtofautisha na wasichana wenye umri mdogo kutokana na urembo wake usiochujuka, hakuwa mwanamke wa kumtazama mara moja tu ukamwacha. Watu wengi walijiuliza kuwa endapo aliweza kuonekana mrembo kiasi kile katika umri huo, ilikuwaje enzi za usichana wake?

Joyce, are you there?” sauti ya Madame Norah ilimgutusha Joyce aliyekuwa ameanza kutekwa na mawazo.

“Oh… Madame Norah! Samahani mama’angu, kwa kweli sikutegemea kabisa kupata simu yako…” Joyce alisema huku akibabaika kidogo.

Sasa endelea...

“Ooh… usijali,” Madame Norah alijibu, na papo hapo akauliza, “Kesho Jumapili utakuwa na ratiba gani?”

“Kesho muda gani?” Joyce aliuliza kwa shauku kubwa.

“Jioni.”

“Nitakuwepo tu nyumbani, sina pa kwenda.”

“Naomba uje ofisini kwangu Mikocheni tuongee, japo maongezi yangu yanaweza yasiwe matamu kama ya mumeo! Au wasemaje?” Madame Norah alisema kwa madaha na kuachia kicheko hafifu.

“Sawa tu nitafika muda huo, sijui saa ngapi?” Joyce aliuliza huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Saa kumi na mbili…” Madame Norah alisema na kuongeza, “See you at that time.”

Okay, Madame!” Joyce alisema huku akipitisha ulimi wake kwenye mdomo wake ulioanza kukauka, na hapo simu ikakatwa. Joyce hakuamini, alibaki akiitazama simu yake huku uso wake ukiwa umepambwa na tabasamu bashasha. Alionekana kuwa na furaha isiyo kifani.

Kisha alijiegemeza kwenye sofa huku akiendelea kutabasamu, na kushusha pumzi za ndani kwa ndani. Muda huo kipindi cha “Madame Norah Show” kilichokuwa kinaendeshwa na Madam Norah mwenyewe kilikuwa kinarushwa kwenye runinga, Joyce alichukua rimoti ya runinga akaongeza sauti.

Muda wote tabasamu lake lilikataa kwenda likizo, alimwangalia Madame Norah kwenye runinga kwa makini sana na kuonekana kuvutiwa naye. Pendo alikuwa ameketi kwenye sofa jirani na mama yake akifuatilia kwa makini kila kilichokuwa kinaendelea pale sebuleni. Hakusema neno bali alikuwa anamwangalia mama yake kwa makini.

Winifrida aliingia pale sebuleni akitokea jikoni na kuketi juu ya mkono wa sofa huku akimwangalia Joyce kwa makini, kisha akaguna.

“Wifi, mbona umefurahi sana, inaonekana unampenda sana Madam Norah!” alisema Winifrida.

“Madame Norah ni mfano mzuri wa mwanamke mjasiriamali… natamani sana kufikia mafanikio kama yake,” alisema Joyce huku akishusha pumzi ndefu.

“Mama, kwani na wewe unataka kuwa kama Madam Norah?” Pendo alimwuliza mama yake huku akimkazia macho kwa makini.

“Ndiyo mwanangu, natamani sana na ninaamini Mungu atanisaidia.”

“Kwa hiyo na wewe utamwacha baba yangu?” Pendo alimwuliza tena Joyce na kumfanya amtazame kwa mshangao.

“Kwa nini nimwache baba yako? Kwani haya maneno huwa unayapata wapi we mtoto!” Joyce alimwuliza pendo huku akiendelea kumtazama kwa mshangao.

“Si wanasema Madam Norah hataki wanaume!” Pendo alisema kwa kujiamini na kuwafanya wote wamkodolee macho kwa mshangao. Winifrida aliziba mdomo wake kwa kiganja cha mkono.

“We mtoto wewe… ni nani kakwambia maneno haya?” Joyce aliuliza huku mshangao ukiwa bado haujamtoka usoni kwake. Winifrida aliachia kicheko hafifu na kumfanya Pendo naye acheke.

“Watu wanasema, hata anti Winnie alikuwa anasema…” Pendo alisema huku akinyoosha kidole chake kumuonesha Winifrida.

“Aka! Lini mimi nimekwambia? Utakuja kusutwa we mtoto!” Winifrida alimkata kauli Pendo na kumruka huku akiinuka na kubetua mabega yake juu. Joyce aliguna tu na wala hakujua la kufanya wala kusema.

* * * * *

Sammy alikuwa ameketi kwenye kiti kifupi chenye foronya laini ndani ya mgahawa mkubwa wa kisasa wenye kuta safi za vioo, uliokuwa ukimilikiwa na rafiki yake, Elli Kiango, na juu ya meza ya mbao ya mti wa mpodo kulikuwa na chupa kubwa ya maji baridi ya Kilimanjaro na bilauri ndefu.

Nje ya ule mgahawa kulikuwa na bango kubwa jeupe juu yake lililokuwa na maandishi makubwa ya rangi nyekundu yakisomeka ‘ELLI’S’. Pia kulikuwa na eneo la maegesho ya magari na kulikuwa na takriban sabini yaliyokuwa yameegeshwa kwenye eneo la maegesho ya magari na mengi yalikuwa ya watu wenye vipato vya juu.

Elli’s ulikuwa mgahawa wa kisasa kabisa wenye kila aina ya vionjo vya daraja la kimataifa, ukifananishwa na migahawa mikubwa duniani kama McDonald; Royal Dragon; West Lake ulioko Mji wa Changsha, China; Varsity Downtown wa Atlanta, Georgia; Lundy’s wa Brooklyn, Newyork; Cosmo wa Croydon, Uingereza n.k.

Kutokana na umaarufu wa mgahawa huo, Elli’s ulikuwa na uwezo wa kuhudumia watu zaidi ya 2,000 kwa siku na uliajiri wafanyakazi zaidi ya 200 waliotoa huduma mbalimbali katika mgahawa huo.

Mgahawa huo ulikuwa na mandhari yenye ubora iliyowafanya wageni wengi kuingia kwa wingi na kujionea mandhari yake na vivutio vilivyopo kwenye mgahawa huo.

Pia ukubwa wa majengo yake yaliyotengenezwa kwa ustadi wa hali juu yakiambatana na nakshi zilizochorwa na kutengenezwa kwa ustadi zikiashiria mila na tamaduni za makabila yaliyopo Tanzania ndiyo sababu zilizowafanya watu wengi pamoja na wageni mbalimbali kutembelea mgahawa wa Elli’s.

Ulikuwa na ukumbi maalumu mkubwa wa vyakula mbalimbali (dining hall) vya watu wa mataifa tofauti uliokuwa na utulivu wa kutosha, ukiwa na meza ndefu za kisasa zilizozungukwa na viti vizuri vya sofa vyenye foronya laini. Ukumbi huo ulikuwa na uwezo wa kubeba takriban watu 500, ambapo wateja walikaa kwa vipindi fulani (shifting zone).

Pia kulikuwa na ukumbi mwingine mkubwa wa kisasa uliotumika kwa ajili ya burudani au mikutano mbalimbali, ukumbi ule ulikuwa na jukwaa zuri la kisasa lililokuwa likitazamana na viti vingi vya kisasa na ulikuwa na uwezo wa kuingiza watu wasiopungua 1,000 kwa wakati mmoja bila bugudha yoyote.

Huduma ya mtandao wa intaneti ya WiFi (Wireless Fidelity) haikukosekana ndani ya ukumbi ule, hasa kwa mtu mwenye kifaa kilichoweza kunasa taarifa za kimtandao wa intaneti, kama simu za kisasa za mkononi, kompyuta na kadhalika.

Muda ule wa mchana kulikuwa na sauti ya muziki laini wa taratibu iliyosikika kutoka katika spika zilizokuwa sehemu fulani ndani ya ule mgahawa na kuzikonga vizuri nyoyo za watu waliofika kwa ajili ya chakula, vinywaji au huduma zingine muhimu.

Inaendelea...

Cc the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego
 
Taxi - (21)

Ndani ya ule mgahawa kulikuwa na wahudumu wa kike warembo kwelikweli waliokuwa wakihudumia wateja. Wahudumu wale walikuwa wamevaa sare za kazi, sketi fupi nyeusi zilizoishia juu ya magoti, makoti ya suti ya rangi nyeupe yenye kola nyeusi na kofia nyeusi kichwani, na walikuwa na nyuso zilizopambwa na tabasamu la kirafiki muda wote.

Ukumbi ule wa chakula na vinywaji ulikuwa na meza nyingi ndogo fupi na pana zilizozungukwa na viti vifupi vyenye sofa laini, na muda ule wa mchana kulikuwa na watu wasiopungua mia moja walioketi kwa utulivu kwenye viti vyao huku wakijipatia chakula na vinywaji, wengi wao wakiwa Wazungu na Waasia.

Sammy alikuwa ameketi kwenye kile kiti kifupi chenye foronya laini kwa utulivu mno akionekana kuwa mbali kimawazo, muda ule ule mwanamume mmoja mrefu na mwenye mwili uliojengeka kwa mazoezi, alifika pale na kuketi kwenye kiti kingine kifupi chenye foronya laini kilichokuwa mkabala na kile alichoketi Sammy.

Mwanamume yule mcheshi na mwenye macho ya upole alikuwa amevaa suti nadhifu ya rangi ya kijivu ya ‘single button’ na shati jeusi lililomkaa vyema na kumpendeza. Miguuni alikuwa amevaa viatu vyeusi vya ngozi kutoka Italia na mkononi alivaa saa aina ya Rolex Submariner.

Aliitwa Elli Kiango na alikuwa rika moja na Sammy, huyo ndiye aliyekuwa mmiliki wa ule mgahawa wa kisasa. Yeye na Sammy walifahamiana tangu utoto wao, walikuwa ni zaidi ya marafiki, walikuwa ni ndugu hasa.

Wakati Sammy alikuwa msomi wa ngazi ya Uzamili aliyesomea biashara ya kimataifa na lugha (M.A. in International Business With Languages), Elli pia alikuwa msomi wa ngazi ya Uzamili aliyesomea Uongozi wa Biashara (M.A. in Business Administration).

Tofauti kubwa kati yao ilikuwa katika misimamo, wakati Sammy alikubali kuajiriwa, Elli hakupenda kabisa kuajiriwa na aliona kuwa elimu yake ingemletea mafanikio makubwa akiamini katika falsafa kuwa: ‘huwezi kutimiza ndoto yako kama utakuwa chini ya mtu mwingine, ukimfanyia kazi na yeye akikupangia na kukulipa mshahara’.

Elli alipoketi kwenye kiti aliweka miguu yake juu ya kiti kingine kilichokuwa mbele yake, akashusha pumzi za ndani kwa ndani huku akimtazama Sammy kwa makini kwenye jicho lake la kushoto lililokuwa na jeraha. Sammy alijaribu kuyakwepa macho ya Elli kwa kutazama kando huku akiilamba midomo yake.

“Samahani kuna mambo yalinitinga kidogo nikalazimika kukuacha peke yako, I hope you are not bored,” Elli alisema huku akijiweka vizuri pale kwenye kiti.

I’m not bored at all,” Sammy alisema huku akiachia tabasamu na kutazama kando. Kilipita kitambo fulani cha ukimya kila mmoja akionekana kutafakari.

“Kama ulivyoniambia, bado sioni mantiki ya wewe kusimamishwa kazi kwa utovu wa nidhamu, mbona kama hainiingii akilini! Au kuna kitu wewe na bosi wako mmepishana au kuchukuliana?” Elli alivunja ukimya huku macho yake yakiweka kituo kwenye uso wa Sammy na kumtazama kwa makini.

“Wala hatujapishana au kuchukuliana chochote, yeye tu na roho yake!” Sammy alisema na kushusha pumzi. Usoni wake haukuonesha tashwishwi yoyote na badala yake alikaa kimya akiupisha utulivu kama afikiriaye jambo fulani.

Jibu lile lilimfanya Elli amtazame Sammy kwa mshangao kisha akamuuliza kwa sauti tulivu, “Inaonesha kama kuna jambo fulani unalijua ila hutaki kuniambia, don’t you trust me?”

“Kwani lini nimewahi kukuficha jambo, ndugu yangu?” Sammy naye aliuliza huku akimkazia macho.

“Sikumbuki… lakini niseme tu ukweli nilishtushwa sana pale mkeo aliponipigia simu asubuhi kunieleza kuwa ulirudishwa nyumbani usiku wa saa 7 ukiwa umebebwa kwenye mkokoteni chakari hujitambui,” Elli alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

Sammy hakusema neno, alibaki kimya akiwa ameinamisha uso wake akiangalia chini kwa fadhaa, ni wazi alionekana kuwa na huzuni.

“Anasema ulipoingia ndani ukaiangukia meza ndogo ya kioo na kuivunja, kisha ukatapika kwenye korido na ulipotaka kukimbilia kwenye mlango ukabamiza jicho… mkeo akakuburuza kukupeleka chumba cha kulala, na alipoanza kukuvua nguo ukapiga kelele ‘niache, mi nimeoa’,” Elli alisema na kuangua kicheko hafifu.

Sammy alitamani kucheka lakini alionekana kujizuia na kuangalia kando kwa aibu. Alishusha punzi za ndani kwa ndani na kukunja sura yake akijaribu kukumbuka, hata hivyo hakuonekana kukumbuka chochote.

By the way… sidhani kama kulewa ni suluhisho la matatizo yako, unatakiwa kuyakubali matokeo na uwe tayari kwa chochote, kwa sababu kilichotokea siyo mwisho wa dunia,” Elli alisema na kumwita mhudumu mmoja mrembo sana aliyekuwa akipita eneo lile.

“Hamisa, naomba uniletee juice ya avocado,” Elli alimwambia yule mhudumu ambaye aliitikia kwa kubetua kichwa chake huku akitabasamu, kisha akageuka na kuondoka haraka kutoka eneo lile huku mtikisiko wa mzigo wa makalio yake ukiwafanya wateja kugeuza shingo zao kumtazama kwa matamanio.

Baada ya yule mhudumu kuondoka Sammy alishusha pumzi za ndani kwa ndani. “Kwa kweli nipo njia panda,” alisema kwa huzuni.

“Nadhani sasa utakuwa umepata funzo, usikubali tena kuwafanyia kazi watu wasioona umuhimu wa wengine, bali wanachojali wao ni kutengeneza fedha tu na kutunisha mifuko yao,” Elli alisema kwa msisitizo na kuongeza.

“Kwa nini usifikirie kuanzisha kampuni ya kukodisha magari, a car rental… naamini unao uzoefu wa kutosha kwa kuwa uliwahi kufanya kazi ya kutembeza watalii kabla hujafanya kazi katika hoteli.”

“Ninatamani sana kumiliki kampuni yangu tatizo fedha ninayoitegemea haitatosha.”

“Si lazima kuanza na magari mengi, hata moja au mawili yanatosha na utakuwa unaongeza kadiri biashara inavyochanganya… tafuta gari zuri na lenye utofauti ili kukabili ushindani,” alisema Elli na kumfanya Sammy ashushe pumzi huku akionekana kukosa uthubutu. Alitazama kando akionekana kufikiria jambo kwa kitambo fulani.

Inaendelea...
 
Taxi - (22)

“Itakuwaje iwapo nitatumia akiba yangu yote na mambo yasiende vyema?” Sammy aliuliza.

“Tatizo lako kwa kuwa umesomea biashara ya kimataifa basi unafikiria kimataifa badala ya kufikiria huku chini, wewe amua mimi nipo nitakusaidia kusajili kampuni, unajua inapendeza zaidi kufanya kazi unayoipenda, ambayo wewe mwenyewe ndiye bosi,” Elli alisema huku akimtazama Sammy kwa makini na kutabasamu.

I’m still in dilemma, nahisi nnaweza kupoteza thamani kwa familia yangu pindi ikibainika kuwa nimepoteza kazi, japo nina ndoa thabiti, lakini hali hii inaweza kubadili kila kitu kwenye uhusiano wetu,” Sammy alisema kwa wasiwasi.

“Mwambie Joyce ukweli na umdokeze kuhusu wazo la kuanzisha kampuni,” Elli alimwambia Sammy na kuongeza, “Ila tafuta njia nzuri ya kumweleza na umpe nafasi aongee ili usikie mawazo yake.”

“Mmh!” Sammy aliguna huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani, akaminya midomo yake.

“Kuambiana ukweli ni muhimu sana katika kuijenga familia…”

“Nakubaliana kabisa na wewe, ukweli ni mzuri lakini si kwa mwanamume kumwambia mwanamke kuwa amesimamishwa kazi eti kwa madai ya utovu wa nidhamu!” alidakia Sammy.

“Unadhani utaendelea kumficha hadi lini? Huoni kama siku akigundua mambo yanaweza kuwa mabaya zaidi?” Elli alijaribu kumtahadharisha Sammy.

“Ndiyo hapo sasa! Nadhani natakiwa kukubaliana na wewe na nimweleze tu ukweli, tena nitamweleza leo hii hii.”

“Fanya hivyo, mara nyingi ili kushinda vita ni lazima ukubali ukweli, usahau yaliyopita na uyaishi yaliyopo,” Elli alishauri na kumfanya Sammy kubetua kichwa chake huku akiachia tabasamu.

“Nitazame mimi, nilikataa utumwa wa kuajiriwa na kuamua kufungua biashara yangu mwenyewe kwa sababu sipendi kutumika kumuingizia mtu mwingine fedha nyingi ili anilipe mshahara,” Elli alisema na kuongeza, “Pia ninapenda nifanye kitu ninachokipenda na niwe bosi wa kazi yangu mwenyewe.”

Japo Sammy alikuwa bado ana wasiwasi lakini alianza kupata matumaini kwa mbali, sasa shauku ya kuanzisha biashara yake ilijionesha waziwazi usoni kwake, alinyanyua uso wake kuangalia juu kwa kitambo akitafakari sana kuhusu hatma yake, kisha alishusha pumzi za ndani kwa ndani.

* * * * *

Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) kilikuwa na pilika pilika nyingi sana jioni hiyo, kulikuwa na hali ya mawingu kiasi. Watu mbalimbali walikuwa katika pilika pilika za kusafiri au kupokea wageni wao kutoka ndani na nje ya nchi.

Gari la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi, mali ya Mr. Oduya lililokuwa likiendeshwa na Madjid Chege liliwasili katika kiwanja hicho cha ndege saa 10:30 za jioni, likaelekea katika kituo namba tatu (terminal III) cha kiwanja cha ndege.

Mr. Oduya alikuwa ameketi kwa utulivu ndani ya lile gari na alikuwa amekuja kumpokea mgeni wake binafsi na muhimu sana, mwanadada Zainab Semaya, hiyo ilikuwa nusu saa kabla ya mgeni huyo kuwasili na ndege ya shirika la ndege la Ujerumani la Lufthansa.

Mipango yote ilikuwa imepangwa kwamba mgeni huyo akiwasili tu katika kiwanja cha ndege cha Julius Nyerere apelekwe moja kwa moja Paradise Club alikotakiwa kufikia, kabla wafukunyuku wenye kufuatilia mambo yasiyowahusu hawajamtia machoni.

Madjid Chege, dereva wa Mr. oduya aliyedumu naye kwa miaka kumi na mbili sasa, aliliegesha lile gari kwenye eneo maalumu la maegesho ya magari la kile kituo namba 3 cha JNIA, kituo kilichokuwa na uwezo wa kuruhusu ndege kubwa 24 kwa wakati mmoja na abiria milioni 6 kwa mwaka kikiwa na mandhari ya kupendeza, yaliyomvutia kila aliyefika pale kwa mpangilio wake mzuri.

Mr. Oduya aliangaza macho yake huku na kule akionekana kutafuta kitu kisha alitoa simu yake lakini kabla hajapiga alimuona Mafuru akielekea pale walipoegesha gari lao. Kumbe muda wote Mafuru alikuwa ameliona gari la Mr. Oduya tangu lilipokuwa likiingia pale kiwanjani.

Waliongea kwa dakika chache, kisha Mafuru aliondoka haraka akimwacha Mr. Oduya ndani ya gari, akavuta hatu zake kuelekea ndani ya lile jengo la kituo namba 3, hasa katika eneo la kusubiria wageni. Akajichanganya na watu waliokuwa katika eneo hilo wakisubiri ndugu na jamaa zao.

Muda wote Mr. Oduya alionekana kuwa na wasiwasi, alijiegemeza kwenye siti yake na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha alifumba macho na kuanza kutafakari.

Ingawa hakupenda kabisa Zainab aje Tanzania lakini hakuwa na namna nyingine ya kumzuia, alihofia kuwa endapo wapinzani wake kisiasa wangejua kuhusu uhusiano wake na Zainab na ujio wa Zainab nchini wangeweza kutumia kama silaha ya kumharibia katika harakati zake za kutaka kuwa Rais wa Tanzania, nafasi aliyoitamani kwa miaka mingi.

Zainab alikuwa ameng’ang’ania kuja jijini Dar es Salaam na kama Mr. Oduya angekataa basi angetakiwa yeye aende nchini Canada alikoishi Zainab na watoto wake wawili, Jasmine na Latifah. Ilikuwa imeshapita takriban mwaka mmoja na ushee bila Mr. Oduya kwenda nchini Canada kuwaona, japo walikuwa wanawasiliana kwa simu na njia ya skype takriban kila siku.

Mr. Oduya alishindwa kwenda Canada kwa kuwa alikuwa kwenye harakati za kuweka mambo yake sawa kabla ya pazia la kampeni za uchaguzi halijafunguliwa, hivyo hakuwa na namna nyingine isipokuwa kukubali kwa shingo upande Zainab aje ili asimuudhi, lakini kwa sharti kuwa safari hiyo iwe ya siri sana na asije na watoto, pia asikae muda mrefu arudi Canada.

Zainab na Mr. Oduya wamekuwa na uhusiano wa siri na mapenzi yao waliyafanya kuwa ya siri sana kwa zaidi ya miaka kumi na miwili, Mr. Oduya alikuwa amempora Zainab kutoka kwa mumewe, Hemed Kimaro, aliyekuwa mfanyabiashara wa madini.

Inaendelea...
 
Taxi - (23)

Hemed alikuwa shemeji wa Mr. Oduya, kwani alikuwa ndugu wa tumbo moja na Dk. Salma K. Oduya, mke wa Mr. Oduya. Ilitokea wakati ndoa yao ikiwa katika mgogoro ndipo Mr. Oduya alipopata mwanya huo kumshawishi Zainab kwa kila njia ikiwemo kumpa fedha nyingi ambazo hakuwahi kuota kuzipata. Hatimaye waliingia kwenye uhusiano wa mapenzi.

Kabla, Zainab alikuwa mwanamke mtulivu na mwaminifu sana kwa mumewe licha ya urembo na upole wake, lakini Hemed alikuwa ‘bize’ na biashara zake na muda mwingi aliutumia kusafiri huku na huko au kuwa na washirika wake wa kibiashara, jambo lililosababisha mgogoro wa mara kwa mara kwenye ndoa yake.

Kabla ya uhusiano na Zainab, Mr. Oduya alishakuwa na uhusiano na wanawake kadhaa warembo akitumai kupata faraja aliyoikosa kutoka kwa mkewe Dk. Oduya, ambaye alikuwa ana gubu na alijaa kisirani. Ilifika kipindi Mr. Oduya alijilaumu kwa nini alimwoa.

Kwa Zainab alijikuta akiweka kituo, na wote wawili (Zainab na Oduya) walijikuta wakihitaji faraja nje ya ndoa zao, ndiyo maana mapenzi yao ya siri yalichipua na kumea kama mche kwenye udongo wenye rutuba, japo kulikuwa na tofauti kubwa ya umri kati yao.

Mr. Oduya alikuwa akimpatia Zainab chochote alichokitaka ikiwemo kumnunulia kwa siri jumba la kifahari eneo la Kijitonyama na penzi lao kukua kwa kasi mithili ya moto mkali ulao nyika.

Kwa kuwa Zainab hakuwahi kuwa na uhusiano mwingine wowote wa kimapenzi kabla na hata baada ya ndoa yake, hivyo alijikuta akilivamia penzi la ‘shuga dadi’ kwa miguu yote miwili, alikuwa ni kama aliyepatwa na wazimu wa mapenzi na pepo la uzinzi lilikuwa limeingia kazini.

Hatimaye Hemed alianza kuzishtukia nyendo za mkewe, alianza kuhisi kuwa mkewe alikuwa akiisaliti ndoa yake na mwanamume mwingine, ingawa hakujua ni mwanamume gani. Aliumia sana na kuanza kufuatilia, siku moja alirudi ghafla nyumbani usiku na kumfumania Zainab akiwa na Mr. Oduya kitandani, akaishiwa nguvu na kupoteza fahamu.

Mr. Oduya alihofia mambo hayo kumfikia mkewe, isitoshe Zainab alishakuwa na ujauzito. Kesho yake asubuhi mwili wa Hemed ulikutwa kwenye mtaro wa maji machafu nyuma ya nyumba yake ukiwa umetapakaa damu baada ya kuchakazwa risasi tatu kifuani...

“Naona ndege ndiyo inaingia,” sauti ya Chege ilimzindua Mr. Oduya kutoka kwenye mawazo. Alichungulia dirishani na kuiona ndege kubwa ya shirika la ndege la Lufthansa ikishuka taratibu katika Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere.

Mawazo yalikuwa yamemteka Mr. Oduya, alikwishaanza kuchoka kuishi mbali na Zainab na aliazimia kuwa baada ya kushinda uchaguzi na kuwa Rais wa nchi, asingeendelea kuficha bali angefanya kila njia, hata ikibidi kusababisha kifo cha mkewe ili Zainab awe mkewe rasmi ‘first lady’.

Aliamini kuwa mambo yalikwisha isha kwani miaka mingi ilikwishapita tangu mauaji ya mumewe Hemed Kimaro na baadaye jaji aliyekuwa kimbelembele katika ile kesi kabla hajapandishwa cheo kuwa jaji mkuu, Sylvester Lutego. Hata hivyo alikuwa na uhakika faili la kesi ya mauaji ya Hemed halikuwepo tena, kwani waliliteketeza kwa moto na hakukuwa na kumbukumbu zozote zilizoachwa...

_____

Saa kumi na moja kamili, ndege kubwa ya shirika la ndege la Lufthansa ilikuwa ikikimbia kwa kasi kwenye barabara ndefu ya lami maarufu kama ‘runway’ iliyokuwa imewekwa alama elekezi za kuwaongoza marubani wa ndege, katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere.

Baada ya muda ilipunguza mwendo na kugeuza, kisha ikaingia katika barabara nyingine ya lami ambayo pia ilikuwa imechorwa alama elekezi za kuwaongoza marubani wa ndege kisha aliingia kwenye maegesho tayari kwa kuteremsha abiria waliokuwa wameabiri katika shirika hilo.

Muda mfupi baada ya ile ndege kusimama na abiria kuruhusiwa kufungua mikanda ya siti zao milango ya ndege ikafunguliwa na ngazi zikiwekwa sawa, abiria walikuwa katika foleni ya kushuka. Mmoja wa abiria wale aliitwa Zainab Semaya.

Zainab alikuwa mwanamama mrembo kwelikweli, alikuwa na umri wa miaka therathini na nane, mrefu na mweupe kiasi mwenye umbo la kuvutia, nywele ndefu na laini alizokuwa amezifunika kwa kofia ya kapelo na alivaa miwani mikubwa myeusi iliyoyaficha vyema macho yake makubwa ya kike yenye ulegevu.

Sura yake ilikuwa ndefu kiasi, midomo laini yenye kingo pana kiasi zilizopakwa rangi nzuri ya mdomo ya chocolate, pua yake ilikuwa ndefu na vishimo vidogo mashavuni mwake viliwafanya wanaume wababaike kila walipomtazama.

Alivaa suruali nyeusi ya jeans, iliyoshikiliwa na kiuno chembamba kiasi mithili ya dondola lakini imara kilichoshikilia minofu laini ya mapaja yake yaliyonona, fulana nyepesi nyekundu iliyoyaficha vyema matiti yenye ukubwa wa wastani na juu yake alivaa jaketi jeusi la jeans. Miguuni alivaa raba ngumu za rangi nyekundu.

Baada ya taratibu zote za uhamiaji hatimaye alishika uelekeo wa upande wa kulia akifuatana na abiria wengine, wakaifuata korido ndefu iliyokuwa ikipakana na ofisi mbalimbali za utawala wa kile kituo namba 3, na kutokea eneo maalumu la kuchukulia mizigo yao iliyokuwa ikipita kwenye mikanda maalumu.

Alichukua begi lake kubwa la magurudumu na kuelekea kwenye korido nyingine upande wa kushoto iliyokuwa ikipakana na ofisi mbalimbali za mashirika tofauti ya ndege, migahawa ya kisasa, maduka ya kubadilishia fedha za kigeni, ofisi za mawakala wa kampuni za utalii na kadhalika.

Mwisho wa ile korido wakatokea kwenye eneo pana la mbele sehemu kulipokuwa na watu wengi waliokuja kupokea wageni wao na nyuma yao kulikuwa na maegesho ya magari. Mafuru alikuwa amesimama huku akiangaza macho yake huku na kule kumtazama mgeni aliyepewa maagizo na Mr. Oduya kumpokea.

Mkononi alikuwa ameshika bango dogo jeupe lililoandikwa maandishi makubwa ya: “Welcome Suzanne Ross”.

Zainab alikuwa akijongea eneo lile taratibu huku akitazama huku na kule akiwa anaburuta begi lake kwa mkono mmoja na begani akiwa ametundika mkoba mdogo mzuri wa kike wa rangi nyekundu. Mara alimuona mwanamume mmoja aliyekuwa ameshika bango dogo lililoandikwa jina la Suzanne Ross.

Inaendelea...
 
Taxi - (24)

Alishtuka kidogo na kumtazama kwa makini yule mwanamume huku akijiuliza kama kulikuwa na mtu mwingine aliyeitwa Suzanne Ross aliyekuwa akiwasili katika kiwanja kile cha ndege. Hili lilikuwa jina lake alilobadilisha ili kukwepa utambulisho wake baada ya kuhamia Canada.

Alimtazama yule mwanamume kwa makini, akakumbuka kuwa alikuwa ameambiwa na Mr. Oduya kuwa mwanasheria wake aliyeitwa Adam Mafuru angempokea pale kiwanjani na kumpeleka sehemu salama, hivyo akaamua kumkabili.

I’m Suzanne Ross,” Zainab alijitambulisha kwa Mafuru huku akinyoosha mkono wake kumsalimia. Mafuru alionekana kubabaika sana na uzuri wa Zainab.

I’m Adam Mafuru,” Mafuru naye alijitambulisha huku akimpa mkono wake. Kisha kwa unyenyekevu Mafuru alimwambia Zainab kuwa Mr. Oduya alikuwepo pale kiwanjani ila kwa sababu maalumu asingeweza kujitokeza kumpokea, na kumtaka amfuate.

Walianza kutoka huku Mafuru akiliburuta lile begi la Zainab kuelekea kwenye gari aina ya Toyota Lexus RX la rangi nyeupe lililokuwa na vioo vya ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani, ambalo lilikuwa likitumiwa na Spoiler.

Spoiler aliwaona na kufungua sehemu ya nyuma ya gari, akaweka lile begi la Zainab na kwa heshima zote na tabasamu la kirafiki Mafuru alimfungulia Zainab mlango wa nyuma wa gari na kumkaribisha aingie.

Muda wote Mr. Oduya alikuwa ametulia kwenye gari akishuhudia kila kitu, hakutaka kabisa kushuka kwa kuwa hakupenda watu waliomfahamu wamuone au wajue nini kilikuwa kinaendelea kati yake na Zainab.

I see! Nimeimisi sana nchi yangu, ni bahati iliyoje kurudi tena baada ya miaka mingi ya kuishi uhamishoni,” Zainab alijiambia nafsi mwake huku akishangaa kuona kulikuwa na maendeleo makubwa tofauti na wakati alipokuwa akiondoka.

Gari lilianza kuondoka kutoka eneo lile na safari ya kuelekea mjini ikaanza. Aligeuza shingo yake kuyatazama mandhari ya kupendeza ya Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere yaliyomvutia sana kwa mpangilio wake mzuri wa majengo.

* * * * *

Saa 12:30 jioni gari dogo la kifahari aina ya BMW X6 xDrive 50i la rangi nyeupe likiwa na vioo vilivyowekwa ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani, lilikuwa kwenye foleni likizivuka taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni Shell.

Gari lile lilikuwa linatokea katika barabara ya Uhuru na lilipozivuka taa za kuongozea magari barabarani liliingia barabara ya Mandela likielekea eneo la Tazara.

Ndani ya lile gari kulikuwa na watu watatu, Elli, aliyekuwa akiendesha lile gari na mwanadada mrembo sana alikuwa ameketi pembeni yake kwenye siti ya abiria. Kwenye siti ya nyuma aliketi Sammy akionekana mtulivu sana. Lile gari lilipokivuka kituo cha daladala cha Buguruni Chama likasimama kando ya ile barabara ya Mandela.

Sammy alishuka huku akimshukuru Elli, wakaagana kisha alianza kutembea taratibu kando ya ile barabara na kukivuka kituo cha daladala cha Buguruni Chama akielekea ziliko taa za barabarani za kuongozea magari.

Pale kwenye kituo cha daladala abiria walikuwa wengi wakiwa wanakimbilia kupanda magari ya Gongolamboto na Mbagala yaliyokuwa yamejaza abiria. Sammy aliendelea kutembea taratibu na kuwapita vijana waliokuwa wanauza maji na wengine wakiwa wamebeba madeli ya barafu (ice cream) za Ukwaju.

Yeye alitembeaa taratibu pasipo kujishughulisha na mambo ya watu wengine, alionekana kuwa na mawazo. Muda huo jua lilikwishaanza kuzama na kiza kuanza kuchukua nafasi ya mchana, hivyo magari yalianza kuwasha taa.

Sammy aliangalia huku na huko na kuvuka barabara ya Mandela iliyokuwa na magari yanayoelekea Tazara kisha akapanda juu ya ukuta wa katikati uliotenganisha magari ya kuelekea Tazara na yale yaliyokuwa yakielekea Ubungo, akitaka kuelekea upande wa pili wa barabara.

Wakati akianza kuvuka barabara upande wa pili sauti ya breki kali za gari ilisikika na kumshtua sana, alijikunja na kuruka huku akiongeza mwendo. Dereva wa lile gari alijitahidi kumkwepa kisha gari lilisimama katikati ya barabara. Sammy aligeuka kutazama kule kwenye gari huku mwili wake ukitetemeka kwa hofu.

Aliliona gari la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi likiwa limesimama huku dereva akimtazama kwa hasira, kisha macho ya Sammy yakatua moja kwa moja kwenye uso wa Mr. Oduya aliyekuwa ameketi kwenye siti ya nyuma akiangalia nje kupitia kioo cha dirisha.

Japokuwa Mr. Oduya alionekana kutafakari jambo fulani kwa kina lakini alikuwa makini sana kumtazama Sammy. Waliangaliana kwa kitambo na Mr. Oduya akaachia tabasamu.

Sammy alionekana kushtuka sana na kukimbilia kwenye baa ya Kimboka lakini akaona haitoshi, akajichanganya na watu wengine akiwapita wauzaji wa biashara ndogo waliopanga biashara zao kando ya barabara ya waenda kwa miguu na kuifuata njia nyembamba iliyokuwa ikielekea kwenye hoteli ya New Popex.

Mr. Oduya alibaki akiwa mtulivu huku akitazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy huku akiendelea kutabasamu, muda huo huo magari mengine yaliyokuwa nyuma ya lile gari la Mr. Oduya yalianza kupiga honi ya kumtaka dereva aondoe gari.

Dereva wa Mr. Oduya aliangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha katikati na kuyaona yale magari yaliyokuwa nyuma yake yakimuwashia taa kumuashiria aondoe gari, alitii na kukanyaga pedeli ya mafuta, magurudumu ya gari yakaserereka kwenye lami huku gari likiondoka kwa kasi.

Wakati lile gari likiondoka kwa kasi eneo lile Mr. Oduya aligeuza shingo yake kutazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy, lakini hakumuona.

Itaendelea...
 
Taxi - (25)

Ilipoishia

Mr. Oduya alibaki akiwa mtulivu huku akitazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy huku akiendelea kutabasamu, muda huo huo magari mengine yaliyokuwa nyuma ya lile gari la Mr. Oduya yalianza kupiga honi ya kumtaka dereva aondoe gari.

Dereva wa Mr. Oduya aliangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha katikati na kuyaona yale magari yaliyokuwa nyuma yake yakimuwashia taa kumuashiria aondoe gari, alitii na kukanyaga pedeli ya mafuta, magurudumu ya gari yakaserereka kwenye lami huku gari likiondoka kwa kasi.

Wakati lile gari likiondoka kwa kasi eneo lile Mr. Oduya aligeuza shingo yake kutazama kule alikokuwa amekimbilia Sammy, lakini hakumuona.

Sasa endelea...

* * * * *

Saa 1:00 jioni gari aina ya Toyota Lexus RX la rangi nyeupe lililokuwa na vioo vya ‘tinted’ nyeusi isiyomruhusu mtu kuona waliokuwemo ndani lilikuwa linaukaribia uzio wa hoteli ya Udzungwa Beach Resort katika barabara ya Ufukweni, eneo la Oysterbay.

Lilikata na kuingia kulia likishika barabara iliyoelekea nyuma ya majengo ya hoteli ya Udzungwa Beach Resort, kisha liliingia kushoto na kuishika barabara maalumu iliyoelekea Paradise Club.

Eneo lile lilikuwa na ulinzi mkali nje na ndani ya uzio, na walioruhusiwa kuingia ndani ya Paradise Club ni wanachama waliosajiliwa tu au wageni wao maalumu, lakini kwa utambulisho maalumu.

Barabara ile ilipambwa na maua mazuri ya ‘Magnolia grandiflora’ yaliyokuwa na rangi ya maziwa na maua mengine aina ya ‘lotus’ yaliyokuwa na rangi mchanganyiko nyeupe, pinki na zambarau, pia ilikuwa imezungukwa na taa nzuri za rangi mbalimbali na maua ya kupendeza.

Lile gari lililokuwa likiendeshwa na Spoiler lilikaribia kwenye kizuizi cha barabarani kilichokuwa na maandishi makubwa yaliyoandikwa kwa lugha ya Kiingereza: ‘Security Check Point’, na kwenye kizuizi hicho kulikuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7, watatu kati yao walikuwa na silaha.

Spoiler alikanyaga breki na kupunguza mwendo na hatimaye kusimamisha gari lake umbali wa mita kumi kutoka kilipokuwa kizuizi huku walinzi wenye silaha wakiwa wamenyoosha silaha zao kumuelekea. Walinzi wawili kati yao walianza kupiga hatua zao kulisogelea lile gari huku wakiwa wameshika vyema bunduki zao wakizielekeza kwenye lile gari.

Mlinzi mmoja alielekea kwenye dirisha la Mafuru, akamsalimia kwa adabu sana na kumuomba kadi yake. Wakati huo huo mlinzi mwingine alizunguka akaelekea upande wa nyuma wa lile gari huku akiwa analichunguza kwa jicho la hadhari.

“Mgeni wa PC.008.19, nadhani taarifa zote mnazo!” Mafuru alimwambia yule mlinzi huku akionesha kadi maalumu ambayo walipewa wageni, kisha aliachia tabasamu.

Yule mlinzi aliwapa ishara walinzi wengine waliokuwa wamesimama kwenye kile kizuizi kuondoa kile kizuizi, wale walinzi walitii na kuondoa kizuizi wakimruhusu Spoiler kupita.

Madame, hivi sasa Tanzania imeendelea sana tofauti na ulivyoiacha, unaona kama hapa kuna ulinzi mkali sana, kwa kuwa wanaokuja hapa ni mabilionea na watu wenye nyadhifa kubwa serikalini,” Mafuru alimwambia Zainab aliyekuwa kimya muda wote akionekana kushangaa sana.

Baada ya mita hamsini walikutana na kizuizi kingine kilichokuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7 huku wawili wakiwa na silaha. Spoiler alisimamisha gari lake na Mafuru akatoa kichwa chake nje.

Alitaja tena namba ya utambulisho huku akiwaonesha ile kadi na wale walinzi walimruhusu kupita, walikwenda mita therathini tu mbele wakakutana na kizuizi cha tatu, ambacho pia kulikuwa na askari maalumu watano wa kampuni ya ulinzi ya Spark K7 huku watatu wakiwa na silaha.

Mafuru alitaja tena namba ya utambulisho huku akionesha ile kadi na mara mlinzi mmoja alibonyeza kitufe fulani, geti kubwa likajifungua na kuwaruhusu kuingia ndani. Walijikuta wametokea katika eneo zuri mno lenye bustani nzuri ya nyasi laini aina ya ‘Citronella’ na mandhari ya kuvutia sana yaliyopambwa na mazuri aina ya ‘Magnolia grandiflora’ na ‘lotus’.

Waliegesha gari lao kwenye maegesho maalumu ya magari, na kulikuwa na magari mengine kadhaa ya kifahari yaliyokuwa yamejipanga.

Madame, tumefika,” Mafuru alimwambia Zainab huku akishuka na kumfungulia mlango wa gari kisha alishusha begi lake.

Zainab alishuka na mara moja akatokea mwanadada mmoja mrembo sana aliyekuwa amevaa gauni zuri lililochanganywa kitenge cha fabric na kitambaa cha rangi ya pinki ndani ya kitenge, lenye mshono mzuri wa kisasa. Nywele zake ndefu nyeusi alikuwa amezisuka mtindo wa mkia wa pweza.

Midomo yake alikuwa ameipaka rangi ya pinki na macho yake alikuwa ameyatia wanja mzito na kumfanya aonekane kama malkia wa uzuri katika njozi ya alfajiri.

“Naitwa Lilian Japhet, sina shaka ni Madame Suzanne Ross wa PC.008.19…” yule mrembo alijitambulisha kwa kina Mafuru huku akiachia tabasamu pana na kusalimia kwa adabu.

“Yeah, ni mgeni wa PC.008.19,” Mafuru alisema huku akimtambulisha Zainab kwa Lilian. Mara moja Lilian aliachia tabasamu na kupokea begi la Zainab.

“Karibu sana Madame, mimi ndiye nitakayekuhudumia muda wote utakaokuwepo hapa, naomba nifuate,” Lilian alisema na kupiga hatua zake taratibu na kwa madaha akitangulia mbele huku akiburuta begi.

Zainab alimfuata nyuma taratibu hadi kwenye mlango mkubwa wa mbele wa Paradise Club, Lilian akausukuma taratibu na kumruhusu Zainab aingie ndani. Lilian akaurudisha ule mlango nyuma yake kisha taratibu akaanza kupiga hatua zake kwa utulivu huku akifuatwa na Zainab, wakakatisha katikati ya ukumbi.

Zainabu alitembea huku akiyatembeza macho yake taratibu kutazama huku na huko, mazingira aliyoyaona yalimuashiria kuwa eneo lile lilikuwa ni klabu ya kisasa kabisa yenye vionjo vyote vya burudani kwa watu wenye ukwasi wa daraja la kimataifa, walikuwa wakipishana na sura zilizoonekana za watu wenye ukwasi mkubwa na kulikuwa na burudani ya kila aina.

Kisha walikatisha kwenye korido pana iliyopita kwenye ukumbi mkubwa wa baa ya kisasa uliokuwa na viti vizuri vya sofa vyenye foronya laini pamoja na meza fupi na pana zenye umbo duara. Zainab aliyatembeza macho yake taratibu kuwatazama mabilionea wachache, wengi wakiwa wageni wa kutoka nje ya nchi ya Tanzania, na zaidi kabisa nje ya bara la Afrika, waliokuwa mle ndani na wenzi wao.

Kisha waliufikia mlango mwingine mkubwa uliokuwa na maandishi makubwa ya ‘VVIP’, nje ya ule mlango kulikuwa na walinzi watatu wa kampuni ya Spark K7 waliokuwa nje ya ule mlango, wawili kati yao walikuwa wameshika silaha.

Inaendelea...

Cc the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego esiankiki
 
Taxi - (26)

Lilian alimtambulisha mgeni wake. Wale walinzi walimsalimia Zainab kwa adabu na mmoja wao alichukua kifaa cha kukagulia na kuwakagua Zainab na Lilian kuona kama yeyote kati yao alikuwa na silaha yoyote. Kisha walilichukua lile begi lake na kulipitisha kwenye mtambo maalumu na walipohakikisha kwamba hana silaha yoyote, waliufungua mlango na kuwaruhusu waingie.

Lilian na Zainab wakaingia na kutokea kwenye korido pana iliyokuwa ikielekea kwenye vyumba vya VVIP, wao waliifuata korido nyingine fupi kushoto kwao na kukuta vyumba viwili vya lifti upande wa kushoto na upande wao wa kulia kulikuwa na ngazi za kuelekea juu.

Lilian alibonyeza kitufe chenye alama za mshale unaotazama juu na mwingine ukitazama chini kilichokuwa pembeni ya milango ya lifti na mara milango ya kile chumba cha lifti ikafunguka na kuwaruhusu kuingia ndani.

Walipoingia Lilian akabonyeza nambari mbili kwenye kitufe fulani kilichokuwa humo ndani kikiwa na namba kadhaa pembeni ya mlango, milango ya kile chumba cha lifti ikajifunga kisha lifti ikaanza kupanda juu taratibu na ilipofika katika ghorofa ya pili ikasimama na milango ikajifungua yenyewe.

Walipotoka tu wakakuta korido nyingine pana na mlango mkubwa wenye maandishi ya ‘Presidential Suites’. Hapo waliwakuta walinzi wengine watatu wa kampuni ya Spark K7 waliokuwa nje ya ule mlango, wawili kati yao walikuwa wameshika silaha.

Lilian alimtambulisha tena mgeni wa PC.008.19. Wale walinzi walimsalimia Zainab kwa adabu na kuwafanyia ukaguzi. Waliporidhika kuwa hawakuwa na silaha waliwaruhusu kuingia ndani

Lilian alimuongoza Zainab, wakafuata korido nyingine pana iliyopita katikati ya vyumba kadhaa, mbele yao wakaingia kushoto wakiifuata korido nyingine fupi iliyowapeleka hadi mbele ya mlango madhubuti wa mbao uliokuwa na maandishi: PC.19.

Lilian aliufungua ule mlango kwa kadi maalumu ya kielektroniki aliyoigusisha juu ya kitasa cha mlango kisha wakaingia na kutokea kwenye sebule pana. Lilian alibonyeza swichi zilizokuwa ukutani na kuwasha taa na kiyoyozi kilichokuwa sehemu fulani kwenye kona ya kile chumba, na hapo hewa safi ya ubaridi ilianza kusambaa mle ndani.

Sakafuni kulikuwa na zulia nene la rangi nyekundu na upande wa kushoto kulikuwa na runinga pana aina ya Sony iliyofungwa ukutani na chini yake kulikuwa na meza fupi nyeusi yenye kisimbusi chenye chaneli nyingi za kimataifa.

Upande wa kulia kwenye kona kulikuwa na meza fupi ya mapambo na jokofu na ukumbi mdogo wa chakula wenye meza ya umbo duara ya chakula iliyokuwa imezungukwa na viti vinne nadhifu vyenye foronya laini.

Jirani na ule ukumbi wa chakula kulikuwa na mlango ulioelekea kwenye chumba cha kulala. Lilian alimwelekeza Zainab ule mlango huku akiufungua, wakatokea kwenye chumba kikubwa cha kifahari chenye nafasi ya kutosha na kilichokuwa na kitanda kikubwa cha samadari katikati.

Mbele ya kitanda kulikuwa na seti nzuri ya runinga pana aina ya Sony na chini ya ile runinga kulikuwa na meza fupi nyeusi ya kioo, na juu ya meza kulikuwa na simu ya mezani na kitabu chenye orodha ya majina ya watu na kampuni zilizotumia huduma ya simu hiyo ya mezani.

Pia kulikuwa na kabati kubwa la kisasa la nguo lililokuwa ukutani, kando yake kulikuwa na meza ya vipodozi yenye kioo kirefu cha kujitazama na kochi moja kubwa la sofa.

Kulikuwa na madirisha mawili mapana ya vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia mazito na marefu yenye nakshi za kupendeza. Kwa kutokea kwenye lile dirisha mtu angeweza kuona mandhari nzuri ya kuvutia, na kwenye kona ya chumba kile upande wa kushoto kulikuwa na mlango wa kuelekea kwenye maliwato.

* * * * *

Sammy alifika nyumbani kwake muda wa saa moja na ushee za jioni akiwa amebeba mkoba wake mdogo wa kiofisi aina ya Pad & Quill wa rangi ya hudhurungi aliokuwa ameusahau pub ya Barakuda usiku wa siku iliyokuwa imetangulia.

Aliupitia baada ya kukumbuka, na alipoingia ndani ya nyumba yake alimkuta Joyce akiwa mwenye furaha mno, Sammy alimtazama kwa makini huku mshangao wa wazi ukijitokeza usoni kwake, kisha aliwatupia macho watu wengine waliokuwepo pale sebuleni.

Pale sebuleni walikuwepo Joyce, Pendo na Winifrida waliokuwa wanafuatilia marudio ya mchezo maarufu wa kuigiza wa runinga ulioitwa ‘Gereza la Kifo’ kutoka kwa mtunzi mahiri wa michezo ya kuigiza, Hamisi Kibari.

Hata hivyo, mawazo ya Joyce hayakuwa kwenye ule mchezo wa kuigiza bali alikuwa anawaza kuhusu ahadi yake ya kwenda kuonana na Madame Norah, huku akianza kuiona njia ya kuelekea kwenye mafanikio makubwa kimataifa. Muda ule alikuwa amejiegemeza kwenye sofa huku uso wake ukiwa umepambwa na tabasamu muda wote.

Joyce alimuona Sammy na kuinuka, akamkaribisha huku akiupokea mkoba wake, hata hivyo tabasamu pana usoni kwake lilishindwa kabisa kwenda likizo. Sammy aliguna huku akimkazia macho Joyce kwa umakini zaidi.

“Mwenzetu vipi, mbona naona leo una furaha kupita maelezo, au umeshinda jackpot?” Sammy aliuliza kwa shauku huku akimkazia macho Joyce.

“Kapigiwa simu, kipindi chake cha mitindo kimekubaliwa,” Winifrida alidakia huku akiachia tabasamu.

“Kapigiwa simu na nani?” Sammy aliuliza huku akiwa bado ana mshangao, alimkodolea macho Joyce huku akiwa na maswali lukuki kichwani kwake. Joyce alibaki kimya, lakini sasa hakuwa anatabasamu tena!

“Kapigiwa na Madam Norah…” Winifrida alisema bila wasiwasi wowote huku akionesha kufurahishwa sana na hatua ya Madam Norah kumpigia simu Joyce.

Sammy alishtuka kidogo, alibana taya za midomo yake akionekana kuzuia hasira huku akimkazia macho Joyce. Hakuonesha kufurahishwa kabisa na zile taarifa.

“Madam Norah ndiyo habari ya mjini… anamiliki vituo vya radio na televisheni na ana kipindi cha “Madame Norah Show” cha kuhamasisha harakati za wanawake,” Winifrida alizidi kuongea kama ametiwa ufunguo na kumfanya Sammy akunje sura yake, kisha aliondoka taratibu na kuelekea chumbani kwake bila kusema neno.

Joyce alimsindikiza Sammy kwa macho na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha aligeuka kumtazama Winifrida huku akiwa amekunja sura yake, alitaka kusema neno lakini akasita.

Inaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom