Taxi - (16)
Ilipoishia
Nguo zake zilikuwa zimelowa chepechepe na muda huo alikuwa anahema kwa nguvu akionekana kukosa kabisa nguvu, alitulia kidogo na kusikilizia akiwa bado ameshikilia ile chupa tupu ya pombe.
Muda ule ule simu yake ya mkononi iliyokuwa imedondoka kando kidogo ya lile dimbwi la maji, kwenye eneo kavu kiasi lenye nyasi ilianza kuita.
Ilikuwa ni simu kutoka kwa mkewe Joyce, na Sammy alikuwa amemhifadhi kwenye kumbukumbu ya majina ndani ya simu yake kama “
Wife”. Sammy alianza kutawanya mikono yake huku na huko kupapasa akiitafuta ile simu.
Simu iliita hadi ikakatika, Sammy akakusanya tena nguvu zake zote na kufanikiwa kuinuka, alisimama huku akionekana kuanza kupata nguvu kutokana na kuoga yale maji baridi ya mvua yaliyotuama kwenye dimbwi. Hata hivyo alikuwa hatamaniki kwa jinsi alivyolowa chapachapa.
Muda ule ule walionekana vijana wawili wakora walioelekea kule alikokuwa, mmoja alikuwa ameshika panga na mwingine alikuwa na nondo mkononi.
Sammy aliwaona wakati wakimsogelea na kupatwa na hofu, hata hivyo hakuondoka eneo lile bali alisimama huku akipepesuka tayari kwa kukabiliana nao, wale vijana wakora walimfikia na kumzingira, mmoja mbele yake na mwingine nyuma.
Sasa endelea...
Yule aliyeshika panga alimtazama Sammy kwa makini kisha alinyanyua lile panga lake kutaka kumpiga na ubapa mgongoni lakini kabla hajapata fursa hiyo Sammy aliwahi kulikwepa kirahisi na kusababisha lile panga likate upepo.
Pigo hilo lilikuwa kama la kumzindua tu kwani wakati huo huo alifyatuliwa miguu kwa namna ambayo hakuitegemea na kujikuta akiviringika chini kwenye maji machafu. Mara tu alipotaka kuinuka alifyatuliwa tena, na hapo kengere ya hatari ikalia kichwani kwake.
Sammy hakutaka kujilegeza, akiwa amekwisha jiandaa alianguka hali huku akiachia teke lililompata mmoja wao tumboni na kumfanya apepesuke. Kisha alianza kuwarushia ngumi na mateke huku akikwepa lile panga na nondo vilivyomkosakosa kichwani.
Lakini kutokana na pombe alizokuwa amekunywa alikuwa anayumba na hatimaye alianguka chini, alipotaka kuinuka mkora mmoja alimuwahi kwa teke kali la kwenye mbavu na kumfanya aachie yowe hafifu la maumivu huku akijikunja pale chini.
Wale wakora walizidi kumshambulia Sammy kwa vipigo ili kumlegeza, yeye alijitetea huku akipangua mateke, ngumi, ubapa wa lile panga na nondo. Wakati akiendelea kupangua alifanikiwa kusimama lakini ghafla alipigwa pigo moja bila kutegemea lililompata barabara usoni na kumpa kisulisuli, akadondoka huku akitoa yowe kali, nguvu zikaanza kumuishia.
Muda ule ule zikasikika sauti za watu waliokuwa wanakimbilia eneo lile ili kutoa msaada. Wale wakora walimsachi haraka haraka na kuchukua pochi yake, wakachukua fedha na kuitupa kando, mmoja alimvua viatu vyake kisha wakakimbia kutoka eneo lile wakimwacha anatokwa na damu sehemu mbalimbali za mwili wake.
* * * * *
Palishakucha muda mrefu na ilishatimu saa nne za asubuhi. Sammy alikuwa bado chakari akiwa amelala fofofo na asubuhi ile kwake ilikuwa bado liamba. Alikuwa amelala kifudifudi akiwa ana uchovu mkubwa uliotokana na pombe mchanganyiko za usiku uliotangulia, ‘
hangover’.
Chumba chake kilikuwa kikubwa chenye maliwato ya ndani kwa ndani (
master bedroom) na hakikuwa na vitu vingi sana isipokuwa kitanda kikubwa cha samadari cha futi sita kwa sita, cha mbao ngumu za mkongo, chenye droo mbili kila upande zilizokuwa na taa za rangi ya bluu.
Pia kulikuwa na kabati kubwa la nguo la ukutani na meza nzuri ya vipodozi maarufu kama ‘
dressing table’ iliyokuwa na kioo kirefu cha kujitazama mwili mzima.
Sakafuni kulikuwa na zulia pana la bluu lililokuwa na maua ya rangi nyekundu na manjano. Chumba kilikuwa na madirisha mawili mapana yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu yenye nakshi za michoro ya maua yaliyodariziwa vizuri.
Sammy akiwa bado yupo chakari akiuchapa usingizi, kichwa chake kilikuwa kizito mithili ya mtu aliyekuwa ametwishwa kiroba cha mchanga.
Ghafla, watoto walioanza kupiga kelele nje ya nyumba walimtoa katika usingizi na kumkera, tena walimkera hasa! Sammy aliinua shingo yake, akakigeuzia kichwa chake upande mwingine huku akiziba masikio na kuendelea kulala, hata hivyo zile kelele zilizidi kumkera masikioni. Akasonya kwa hasira.
Alijaribu kuinua kichwa chake lakini aliuhisi ule uzito wa kichwa na alikuwa bado ana mawenge ya usingizi, ukichanganya na uvivu uliomjaa, vilimpa hali ya kutaka kuendelea kuuchapa usingizi, licha ya jua la asubuhi kuhanikiza nuru ya kutosha mle chumbani mwake.
Miale ya jua la saa nne asubuhi ilikuwa imepenya dirishani na kutuama ikienea hadi pale kitandani alipokuwa amelala tangu kulipopambazuka. Joto la miale ile ya jua lilikuwa limeamsha homa hafifu mwilini mwake, homa iliyotokana na pombe mchanganyiko alizokunywa usiku ulioitangulia siku ile.
Sammy alikuwa mnywaji wa kawaida wa bia mbili au tatu tu basi na hakuzoea kunywa pombe kali, hivyo aliutaka utulivu kwa gharama yoyote ile, japo aweze kumalizia n’gwe ile ya usingizi, hakujua uchovu ule ungekwisha saa ngapi. Alichojua yeye ni kulala tu hadi pale mwili wake ungemruhusu kufarakana na kitanda. Watoto walizidi kumkera kwa kelele zao.
Walikuwa watoto wa pale mtaani, eneo la Tabata Chang’ombe, waliokuwa wanacheza asubuhi ile baada ya kushiba chai ya asubuhi. Hawakuwa na kingine cha kufanya isipokuwa kucheza tu, kwani ilikuwa ni siku ya Jumamosi na hapakuwa na shule.
Hao watoto ndio waliomgutua Sammy toka usingizini, kwa kuwa walikuwa wanacheza karibu na dirisha la chumba chake. Japo nyumba yake ilikuwa imezungukwa na ukuta lakini umbali kutoka ule ukuta hadi pale dirishani kwake ulikuwa mdogo sana, isitoshe kulikuwa na uwanja mpana ulioruhusu watoto kucheza.
Kelele za watoto zilimfanya Sammy ajihisi kama mtu aliyekuwa anapigiwa zumari sikioni, alisonya huku akiminya sura yake kana kwamba alikuwa anahisi maumivu makali ya kichwa. Alikuwa amechefukwa kweli kweli!
Aliwavumilia kidogo wale watoto huku akiinua shingo yake na kuzisikiliza sauti zao kwa makini, akazitambua kwani mojawapo ilikuwa sauti ya mtoto wake wa miaka 8 aliyeitwa Pendo, na nyingine ilikuwa ya dada yake mdogo wa miaka 17 aliyeitwa Winifrida.
“Winnie! We Winnie!” Sammy aliita kwa sauti kali ya kukaripia.
“Abee!” Winifrida aliitikia kwa sauti ya juu huku akisogea zaidi pale dirishani.
“Naomba niondosheeni hizo kelele zenu hapo dirishani kwangu. Alaa!” Sammy alitoa amri yake kwa sauti ya kufoka kidogo huku akihisi kizunguzungu na mate kumjaa kinywani, alikunja ndita usoni.
Winifrida aliwaondosha wale watoto kutoka eneo lile, na muda ule ule Sammy alisikia mlango wa chumba chake ukifunguliwa, aligeuza haraka shingo yake kumtazama aliyekuwa akiingia mle chumbani, macho yake yalikutana na macho ya mkewe, Joyce Jengo.
Inaendelea...
Cc
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel