Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (9)

ILIPOISHIA

Kuona hivyo Spoiler alikunja ngumi ya mkono wake wa kulia na kutengeneza alama ya dole gumba, kisha akapeleka lile dole gumba na kuminya pua yake kwa dharau huku akikunja sura yake kana kwamba alikuwa amenusa harufu mbaya.

Alifunua jaketi lake ili kumuonesha kitu Sammy, na hapo macho ya Sammy yakatua kwenye kisu kikubwa cha springi kilichokuwa kimewekwa ndani ya ala na kutuna kiunoni kwa Spoiler.

Sammy alijikuta akisisimkwa mwili wake na damu ikaanza kumchemka na kukimbia kwenye mishipa yake ya damu, vinyweleo mwilini na nywele kichwani zilimsisimka kwa hasira. Hali ile ilisababisha mapigo ya moyo yaende mbio huku jasho jepesi lianze kumtoka sehemu mbalimbali za mwili wake!

Spoiler alitaka kukichomoa kile kisu lakini alisita na kugeuza shingo yake kuwatazama watu walioanza kusogea eneo lile huku wakishangaa. Miongoni mwao alikuwemo askari mmoja wa ulinzi wa kampuni ya Spark K7 aliyekuwa ameshika bunduki akilinda eneo la uzio wa hoteli.

SASA TUENDELEE...

Spoiler aligwaya na wakati akitafakari kipi cha kufanya gari dogo aina ya Toyota Crown la rangi nyeusi lililokuwa na vioo vyeusi visivyoonesha watu waliomo ndani lilifunga breki karibu yake. Spoiler aligeuza shingo yake na kuliona kisha alimtazama Sammy kwa tabasamu la dharau.

“Una bahati sana… Nakuacha uondoke lakini ukithubutu kufumbua mdomo wako na kusema chochote, nakuhakikishia kwamba haitatuchukua dakika thelathini familia yako yote itakuwa mikononi mwangu, nitawakata kiungo kimoja kimoja na watakufa taratibu lakini kwa maumivu makubwa,” Spoiler alimwambia Sammy kwa sauti ya chini.

“Ukiigusa familia yangu nitakuua, naapa,” Sammy alisema kwa hasira huku akipitisha kidole cha shahada shingoni kwake na kukinyooshea juu kisha akakikung’uta hewani kuapia. Spoiler aliachia tabasamu la dharau.

Okay, tutaonana hivi karibuni,” Spoiler alisema kwa dharau huku akianza kupiga hatua kuondoka.

You go to hell!” (Nenda kuzimu!) Sammy alimwambia Spoiler kabla hajapanda kwenye gari huku akimtazama kwa chuki.

You’ll see how hell looks like, very soon…” (Utaiona kuzimu inavyofanana, hivi karibuni…) Spoiler alisema huku akifungua haraka mlango wa lile gari, akaingia na lile gari liliondoka haraka kutoka eneo lile na kupotelea mtaani.

Sammy aliachwa akiwa na mshangao mkubwa, damu ilizidi kumchemka mwilini. Tai shingoni kwake ilikuwa imelegezwa kutokana na purukshani zile na vifungo vya juu vya shati lake vilikuwa vimefunguka na kuachwa wazi.

Aligeuza shingo yake akayatembeza haraka macho yake kuwatazama watu walioanza kumsogelea karibu na kumzunguka huku wengine wakimpa pole na wengine wakimtazama kwa huzuni bila kusema neno. Alishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Vipi, Bosi, kuna tatizo lolote?” yule askari wa ulinzi wa kampuni ya Spark K7 aliyekuwa akilinda eneo lile alimwuliza Sammy huku akimtazama kwa wasiwasi.

“Hakuna tatizo bali tulipishana tu kauli,” Sammy alijibu huku akijifuta vumbi. Kwa kuwa hakupenda kutazamwa na kugeuka kivutio, aliamua aondoke eneo lile haraka kabla mvua ya maswali haijaanza.

“Kwani yule jamaa ni nani na alikuwa anataka nini, mbona anaonekana mtata mtata hivi?” yule askari wa ulinzi alizidi kumdadisi Sammy huku akionesha kuwa na shaka na jibu lake.

“Ni muhuni fulani, wala usijali, hakuna kibaya kilichotokea,” Sammy alisema huku akiwatazama wale watu waliokuwa wameanza kumzunguka ili waweze kusikia anasema nini. Sammy aliwashukuru kwa kuonesha kujali, kisha akaanza kupiga hatua zake kuondoka eneo lile.

Aliisimamisha Bajaj moja iliyokuwa ikipita eneo lile na kupanda haraka, kisha alimtaka dereva ampeleke Kinondoni Studio, ambako angeweza kupata usafiri wa kuelekea Tabata Chang’ombe.

Dereva aliiondoa Bajaj kwa mwendo wa kasi na kuiacha barabara ile ya Ufukweni, akaingia barabara ya Kenyatta. Sammy alishusha pumzi na kujiegemeza kwenye siti huku akizama kwenye mawazo yake binafsi yasiyomhusu yule dereva wa Bajaj.

Alihisi kuwa yule dereva wa Bajaj alikwishatambua kuwa abiria wake alikuwa na mawazo fulani. Hata hivyo, asingeweza kujua ni mawazo gani. Kulikuwa na mengi yangeweza kumsumbua mwanamume mwenye majukumu kama Sammy.

Bila hata kutegemea alianza kuzama kwenye bahari ya mawazo, mawazo yaliyomrudisha hadi usiku wa kuamkia siku ile, hasa alipokumbuka ile kauli ya Spoiler kuwa asifungue mdomo kumweleza yeyote alichosikia ofisini kwa Dk. Masanja, alijikuta akiyakumbuka yote yaliyotukia usiku ule.

Sasa Sammy alitambua kabisa kuwa matatizo yote ya kusimamishwa kazi kwa kisingizio cha utovu wa nidhani na kuihujumu kampuni yalitokana na kile alichokuwa amekisikia usiku wa kuamkia siku ile.

Alikumbuka kuwa siku iliyotangulia alifanya kazi nyingi mno na aliondoka ofisini kwake mnamo saa 3 usiku, lakini alipokuwa njiani kuelekea nyumbani kwake alikumbuka kuwa hakuwa na simu yake ya mkononi aina ya Iphone X, alihisi kuiacha kwenye vyoo vya jumuia vya ofisini alipokwenda kujisaidia haja ndogo.

Sammy aliamua kurudi haraka kabla mtu mwingine hajaiona na kuichukua. Alipofika hotelini alielekea moja kwa moja kwenye kile choo cha ofisini alichohisi ameiacha na bahati nzuri aliikuta simu ikiwa juu ya sinki la kunawia maji.

Alishusha pumzi na kuichukua simu yake akiwa mwenye furaha, akaiweka mfukoni na kuanza kutoka nje, alishuka ngazi haraka haraka lakini akahisi kuwa huenda bosi wake Dk. Masanja alikuwepo ofisini kwake, kwani alikuwa ameliona gari lake pale kwenye viunga vya maegesho ya magari.

Aliamua kuelekea moja kwa moja kwenye mlango wa ofisi ya Dk. Masanja ili amsalimie, akaufungua taratibu mlango na kutokea kwenye ofisi ya sekretari wa Dk. Masanja, ambaye wakati huo alikuwa amekwisha ondoka.

Sammy alitaka kupiga hatua kuelekea kwenye mlango wa ofisi ya Dk. Masanja lakini alisita baada ya kusikia sauti zaidi ya moja za watu wakiongea kwa sauti ya chini yenye kila aina ya tahadhari. Alisimama akasikiliza kwa makini, huku macho yake yakizunguka kulichunguza eneo lile.

“…najua umestuka sana kuona kwamba ninafahamu mambo mengi, nisikilize kwa makini sana… kuanzia sasa unatakiwa kukubaliana nami,” Sammy alisikia sauti nzito yenye mamlaka ya mwanamume mmoja ikiongea kutokea mle ndani.

Inaendelea...
 
Taxi - (10)

“Nimekufuata kwa sababu sitaki ukurupuke, najua umefuatwa na wapinzani wangu ili umuunge mkono mheshimiwa Mrisho Tumbo kwenye Urais… lakini kumbuka mimi nina sapoti kubwa ya kikundi cha mabilionea wakubwa ambao ni wanachama wa Paradise Club na wapo tayari kufadhili kampeni zangu nchi nzima…” ile sauti iliongeza.

“Sikujua kama mwaka huu umeamua kujitosa na uko tayari kwa mapambano!” sauti ya Dk. Masanja ilisikika.

“Wewe unazifahamu siasa za nchi hii, kila kitu kinahitaji mipango madhubuti na bila kuwatumia hawa watu wenye nguvu ya kufanya jambo lolote katika nchi hii ni vigumu sana kufanikiwa. Hawa mabilionea ndio huamua nani awe rais ajaye,” sauti ile iliongeza.

Kisha kikapita kitambo kifupi cha ukimya kabla haijasikika sauti ya Dk. Masanja, “Nakuhakikishia, Mr. Oduya, mimi nipo upande wako. Sasa unataka nikufanyie nini?”

“Kuna mambo mawili makubwa nayataka toka kwako, moja ni hili la kukushirikisha katika mpango wangu wa kugombea Urais wa nchi hii…”

“Hii ni habari nzuri,” sauti ya Dk. Masanja ilidakia.

“Lakini tuko vitani, mheshimiwa Tumbo ni kikwazo kikubwa kwangu kwa kuwa alikuwa upande wangu na anazifahamu siri zangu nyingi, ikiwemo kifo cha Jaji Mkuu, Sylvester Lutego…” sauti ambayo sasa Sammy aliitambua kuwa ni ya Mr. Oduya ilisikika.

“Mungu wangu! Kumbe Jaji Lutego aliuawa!” Sammy aliwaza huku akiwa ameshtuka sana. “Si walitangaza kuwa ametoweka na hajulikani aliko!”

Alianza kuhisi ubaridi fulani wa woga ukimtambaa mwilini mwake huku mapigo ya moyo yakianza kwenda mbio isivyo kawaida! Koo lake lilimkauka ghafla na vinyweleo mwilini vikamsimama kwa hofu.

“Hii si vita rahisi kwani wapinzani wetu wana nguvu sana…” sauti ya Mr. Oduya ilisisitiza na kuendelea, “kuna mambo makubwa sana yanaendelea hivi sasa upande wa wapinzani wetu, nikipata muda nitakufahamisha vizuri.”

“Kwa hiyo mimi nikusaidieje? Au unataka nikusaidie kummaliza mheshimiwa Tumbo… maana mimi ni mzuri kwenye mambo haya!” Dk. Masanja alisikika.

“Usijali, kwenye suala la mheshimiwa Tumbo ninaye mtu makini kabisa ninayemuamini, kijana wangu Spoiler, huyu ndiye atakayeifanya kazi hiyo kwa uangalifu mkubwa, kwani hajawahi hata mara moja kuharibu kazi yangu yoyote,” Mr. Oduya alisikika akijigamba.

Sammy aliogopa sana, aliona kuendelea kuwepo eneo lile lingekuwa jambo la hatari sana kwake, hivyo aliazimia kuondoka haraka kabla hajagundulika. Alianza kunyata taratibu na kwa tahadhari mno akaufuata mlango wa kutokea.

Okay, kwa hiyo unahitaji nikufanyie nini?” sauti ya Dk. Masanja ilisikika tena ikiuliza.

“Kwako nimekuja kwa masuala mawili makubwa, kwanza nina mgeni wangu binafsi muhimu sana ataingia jioni ya keshokutwa kutoka nchini Canada, lakini hii ni siri kubwa sana…” Mr. Oduya alisema lakini ghafla alionekana kusita.

“Kuna nini?” Dk. Masanja alimwuliza kwa wasiwasi.

“Nahisi kuna mtu humu ndani anasikiliza maongezi yetu…” Mr. Oduya alisema kwa wasiwasi na mara wote waliinuka haraka, wakafungua mlango kuchungulia nje. Hawakuona mtu wakaamua kutoka haraka na kutazama kwenye korido.

Muda huo Sammy alikuwa amekimbia na kushika uelekeo wa nyuma ya jengo, akaifuata korido pana iliyokwenda kutokea kwenye jengo la nyuma baada ya kuhisi kuwa kupita mbele isingekuwa jambo la busara kwani angeonekana na watu wa mapokezi.

Alipokuwa akikimbia aligeuka kutazama nyuma, akaona vivuli vya watu wawili vikiwa vimesimama mlangoni. Alizidi kuifuata ile korido pana akiivuka milango minne na upande wake wa kushoto kulikuwa na mlango mkubwa uliokuwa wazi.

Sammy aliufuata ule mlango na kutokea kwenye korido nyingine pana, akauvuka ukumbi wa kisasa wa burudani uliokuwa na kila aina ya starehe, na kila kionjo cha daraja la kimataifa.

Ndani ya ukumbi ule kulikuwa na wahudumu warembo wa kike, waliokuwa wakihudumia wateja wachache waliokuwemo ukumbini mle muda huo wakiwa wameketi kwenye meza nzuri za mbao ya mninga na viti vifupi vyenye foronya laini.

Sammy hakusimama wala kushangaa aliongeza mwendo wake na kulivuka eneo lile kisha akaupita mlango mwingine mbele yake uliokuwa na maandishi juu yake yaliyoandikwa: ‘Sauna’, au ‘Bafu la mvuke’ kwa Kiswahili.

Sauna kilikuwa chumba maalumu kilichobuniwa kama sehemu ya kupata joto la mvuke ambalo huipa hewa ya chumba hicho joto na kisha hewa kusambaa katika chumba na kuipasha ngozi ya mtu aliyeingia humo. Joto lake huwa linategemea mtumiaji alihitaji liwe la kiasi gani na lilitumika zaidi kwenye nchi zenye baridi.

Alivuka na kuufikia mlango wa nyuma kabisa wa lile jengo, kisha alizunguka na kuelekea kwenye jengo la nyuma ya ile hoteli lililokuwa limezungukwa na miti mirefu na mikubwa ya kivuli na bustani nzuri ya nyasi laini aina ya ‘Citronella’ zilizokuwa zimekatwa vizuri na kupendeza.

Eneo lile kulikuwa na mandhari iliyopambwa na aina mbili za maua mazuri: ‘Magnolia grandiflora’ ya rangi ya maziwa na maua aina ya ‘lotus’ yenye mchanganyiko wa rangi nyeupe, pinki na zambarau.

Sammy alikunja, akaelekea kushoto akiifuata barabara nzuri ya kutembea kwa miguu iliyojengwa kwa vitofali vidogo vilivyovutia ikiwa imepita katikati ya ile bustani nzuri ya nyasi laini aina ya ‘Citronella’ ikielekea Paradise Club.

Barabara ile ilikuwa imezungukwa na taa nzuri za rangi mbalimbali na kulifanya eneo lile kufanana na bustani ya Eden. Sammy aliongeza mwendo na kuzipita sehemu za kupumzika zenye viti na meza chini ya miamvuli mikubwa yenye rangi za kupendeza na mabwawa makubwa ya kuogelea.

Inaendelea...
 
Taxi - (11)

Akazipita sehemu zenye viti maalumu vya kupumzikia chini ya miti mizuri aina ya coconut palms pamoja na vibanda vidogo vya faragha. Alitaka ajifiche pale lakini akasita na kuendelea mbele.

Mbele kidogo alipunguza mwendo wake baada ya kufika kwenye kizuizi cha kuelekea Paradise Club, klabu ya mabilionea na vigogo wa serikalini. Kwenye eneo lile kulikuwa na askari watano wa ulinzi wa kampuni ya Spark K7 na wote walikuwa na silaha.

Walipomuona Sammy walimtambua na kumruhusu, alivuka na kuendelea mbele, baada ya mwendo mfupi alikutana tena na kizuizi kingine.

Alijitambulisha tena na kuruhusiwa kupita. Hatua kadhaa mbele yake alikutana na kizuizi cha tatu. Kama kawaida alijitambulisha na kuvuka, kisha aliivuka sehemu nzuri yenye mandhari ya kuvutia sana ya kuegesha magari ya mabilionea na vigogo wa serikali waliofika pale kustarehe.

Hata hivyo, hakuingia ndani ya Paradise Club, alipitiliza hadi kwenye geti la nyuma la kutokea magari ya mabilionea na vigogo wa serikalini, ambako aliwakuta askari wengine wa ulinzi wa kampuni ya Spark K7 wakiwa wameshika bunduki zao tayari kwa lolote. Walimuona wakamtambua…

______

“Mmh… sasa nimeelewa kwa nini Dk. Masanja amenichukia ghafla na kunisimamisha kazi, nadhani waligundua ni mimi niliyeingia ofisini kwake na kuyasikia maongezi yao… waliniona kupitia kamera za usalama mle ndani!” Sammy aliwaza.

Akiwa ameituliza akili yake alijiuliza kama alikuwa anafahamu nini juu ya nguvu alizonazo Mr. Oduya kiasi cha kujiamini na kumtuma kijana wake mchana kweupe ili kumtishia maisha! Hakuna! Aliwaza kwa uchungu kuwa alikuwa hajui chochote zaidi ya ukweli kuwa alikuwa ameingia katika anga za mtu mwenye nguvu zote: kisiasa, kiuchumi, kiulinzi na kiukatili.

Ni hilo lililomfanya ajikute akihisi hofu kubwa na asielewe kama Bajaj iliyomchukua ilikuwa imekwishafika eneo la Kinondoni Studio na muda ule dereva wa ile Bajaj alikuwa ameegesha kando ya barabara akimtazama kwa mshangao.

Na kwa mara ya kwanza maishani mwake, Sammy alianza kujutia uamuzi wake wa kusikiliza mambo yasiyomhusu, ni kitu gani kilimtuma kwenda ofisini kwa Dk. Masanja usiku ule hadi kusikia kilichokuwa kikizungumzwa mle ndani? Alijiuliza na kukosa jibu. Hadi kufikia hapo hakujua afanye nini…

“Bosi wangu, unawaza nini? Tayari tumefika Kinondoni Studio,” sauti ya dereva wa Bajaj ilimzindua Sammy kutoka kwenye lindi la mawazo.

Sammy alishtuka na kuangali nje, aliyaona mazingira ya Kinondoni Studio na kushusha pumzi za ndani kwa ndani, kisha alimlipa dereva wa Bajaj fedha yake na kushuka. Aliwaza vipi kama yule dereva wa Bajaj asingemshtua pengine angeendelea kuwaza hadi jua linakuchwa!

Wakati akianza kupiga hatua kuelekea kilipo kituo cha daladala cha Kinondoni Studio mvua kubwa yenye kuambatana na upepo mkali ilianza kunyesha ghafla na kumfanya akimbilie kwenye korido za jengo moja la ghorofa lenye fremu nyingi za maduka ya mavazi na vipodozi.

Alipoingia katika lile jengo alijibanza upenuni akijumuika na watu wengine ili kujificha mvua ile.

* * * * *

BAMMMM! Spoiler alimkwida mwanamume mmoja aliyekuwa amefungwa mikono na miguu na kumbamiza juu ya meza kubwa ya chuma iliyokuwa katikati ya chumba kikubwa cha siri chenye kuta imara na kisichokuwa na dirisha.

Chumba chote kilikuwa kimetapakaa damu na yule mwanamume hakuwa anatazamika, uso wake na mwili kwa ujumla ulikuwa umetapakaa damu baada ya mateso makali.

Kile chumba kilikuwa na kioo kipana ukutani kilichomfanya mtu aliyekuwemo mle ndani asiweze kumuona mtu aliyekuwa nje ya chumba, lakini mtu wa nje aliweza kumuona vizuri aliyekuwa mle ndani.

Yule mwanamume aliyekuwa akiteswa aliitwa Abbas Dalali, alikuwa mfupi mnene na rangi ya ngozi yake ilikuwa ni ya maji ya kunde, akiwa na umri wa miaka kati ya hamsini na hamsini na tano, alikuwa na misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu na kumfanya aonekane kama bondia mkongwe.

Abbas alikuwa mume wa mke mmoja, watoto wanne na wajukuu wawili, alikuwa mwandishi mkongwe wa habari wa gazeti la kila siku la MamboLeo aliyejizolea umaarufu mkubwa kwa kuandika habari za kisiasa na kijamii zilizofanyiwa uchunguzi wa kina, kwa kuzingatia zaidi uzalendo kwa nchi yake na maslahi ya taifa pasipo kumuogopa yeyote.

Hakusita kufichua uovu uliofanyika wakati wowote na sehemu yoyote bila kujali ulifanywa na mtu au kikundi gani cha watu, ilimradi tu maslahi ya taifa yalionekana kuchezewa. Alikuwa amejitolea maisha yake kwa ajili ya nchi yake kwa hali na mali bila kujali kama kazi hiyo ingeyagharimu maisha yake au la.

Kile chumba kilipewa jina la “Hell” yaani kuzimu, kutokana na yaliyokuwa yakifanyika chumbani humo. Katikati ya kile chumba kulikuwa na viti viwili na meza kubwa ya chuma, kilikuwa na bomba refu la chuma lililokatiza katikati ya chumba kutoka upande mmoja wa chumba hadi mwingine ukutani.

Juu ya meza kulikuwa na balbu ya umeme ya mwanga usiokuwa mkali sana kutoka katika dari ya chumba kile ikiwa imening’inizwa kwa waya mwembamba na mrefu kutoka darini. Na juu ya dari kulining’inizwa vyuma vifupi vilivyokunjwa na kuchongwa mbele yake mfano wa vyuma vya kuning’inizia nyama buchani.

Upande mmoja wa chumba kulikuwa na kitanda chembamba cha chuma chenye mikanda imara, mnyororo mfupi na pingu za miguuni na mikononi za chuma, na kando yake kulikuwa na meza ya kioo iliyowekwa sinia lenye kisu, waya mwembamba lakini imara, koleo, nyundo na misumali, na bomba la sindano lililokuwa na dawa maalumu ambayo mtu akichomwa huufanya ubongo na akili yake iwaze kusema ukweli tu.

Hiki kilikuwa chumba cha siri cha mateso na mahojiano ya kumlazimisha mtu aongee ukweli kwa kubanwa na silaha mbalimbali, vitu vyenye ncha kali, mtungi mdogo wa gesi na vifaa vya kunyongea na kuchania ngozi, kilichotumiwa na Mr. Oduya dhidi ya wapinzani wake kisiasa na kibiashara.

Itaendelea...
 
Taxi - (12)

Chumba hiki kilikuwa ndani ya jumba kubwa la kifahari la ghorofa moja, mali ya Mr. Oduya, lililojengwa katika eneo la Kinondoni Makaburini. Lilikuwa jumba la vyumba vitano vya kulala vilivyosheheni samani zote muhimu, sebule mbili kubwa chini na juu, ukumbi wa chakula, ofisi na maktaba ya siri, na chumba cha siri cha mateso.

Kwa nje jumba lile lilionekana ni nyumba ya kistaarabu sana iliyokaliwa na mtu mwenye ukwasi, lakini ukweli ni kwamba halikuwa jumba lililokaliwa na mtu na kilichokuwa kikifanyika mle ndani kilidhihirisha kila aina ya unyama.

Akiwa bado kamkwida Abbas, Spoiler alikuwa amekunja sura yake huku akimtazama kwa ghadhabu.

“Sipendi tuumizane, hebu nitazame vizuri… I’m a monster. Kama hutanipa majibu sahihi ya nilichokuuliza naapa utakufa kwa maumivu makali sana!” Spoiler alimwambia Abbas kwa ukali huku akimwachia.

One last chance, Mr. Reporter… ni kipi chanzo chako cha habari ulizoandika kwenye gazeti lenu?” Spoiler alifoka huku macho yake yakiwaka kama moto kwa ghadhabu.

Abbas alibaki kimya akimtazama Spoiler bila kusema chochote, alikuwa anavuja damu maeneo ya usoni. Walibaki wanaangaliana kwa kitambo huku kila mmoja akiwa na hasira.

Kitendo cha haraka sana kikatokea, Spoiler alimrukia Abbas na kumpiga ngumi tatu mfululizo za tumbo. Abbas aliguna kwa maumivu makali na kupepesuka, alijaribu kujiweka sawa lakini akapigwa tena ngumi zingine za mfululizo. Kisha Spoiler alimkwida tena na kumbamiza kwenye ukuta.

Spoiler alikuwa amepandwa na ghadhabu, alimkodolea macho Abbas na kuchomoa kisu kutoka kwenye ala yake huku akimtazama kwa ghadhabu, kisha akakielekeza kwenye koo lake.

“Subiri… nadhani sasa yupo tayari kuzungumza,” sauti nzito ya Mr. Oduya ilisikika kutoka kwenye spika zilizokuwa zimefungwa mle chumbani.

Mr. Oduya na mwanamume mmoja aliyeitwa Adam Mafuru walikuwa wamesimama nje ya kile chumba lakini waliweza kuona na kusikia kila kitu kilichoendelea mle chumbani kupitia kioo kikubwa kilichokuwa ukutani.

Mafuru alikuwa mrefu na mweusi mwenye umbo kakamavu la kimichezo. Alikuwa na miaka isiyopungua arobaini na alivalia shati jeupe la mistari ya rangi ya bluu la mikono mirefu, suruali ya jeans ya rangi nyeusi na raba nyeusi.

Macho yake yalikuwa makubwa na mekundu na muda wote yalikuwa makini. Alikuwa msomi wa shahada ya pili ya sheria aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mafuru ndiye alikuwa mwanasheria wa kampuni na familia ya Mr. Oduya kwa miaka zaidi ya kumi.

“Abbas, nadhani umeona kinachoweza kukutokea endapo hutaonesha ushirikiano, tambua hatupo hapa kukuumiza. Ni rahisi tu… tuambie ni kipi chanzo chako cha taarifa kisha tutakuacha uende zako!” sauti nzito ya Mr. Oduya ilivuma ndani ya kile chumba kupitia spika.

Abbas aliendelea kukaa kimya pasipo kujibu chochote. Spoiler alimwachia na kuchukua koleo ndogo mbili kisha akakibana kidole kimoja cha Abbas kwa koleo na kuanza kung’oa kucha.

Aarrgghh! Fu** you… motherfu***r!” Abbas alipiga kelele kubwa iiliyofuatana na matusi mazito kutokana na maumivu makali.

“Kama hutaki tuumizane sema ukweli ili nisiendelee kung’oa na hizi kucha zingine,” Spoiler alisema kwa ukali lakini Abbas aliendelea kuporomosha matusi mazito, akitukana ukoo wote wa Spoiler.

Spoiler alimchapa kofi kali usoni lililomsababisha kuona vimulimuli, hakuishia hapo, aliachia tabasamu la kinyama na kuanza kumshushia kipigo kikali. Ndani ya dakika tano tu chumba chote kilitapakaa damu na Abbas alikuwa hatazamiki.

“Sasa tueleze tunachotakiwa kujua…” Spoiler alisema huku akishusha pumzi ndefu.

Pamoja na yale mateso makali lakini Abbas aliendelea kuwa kimya, alikuwa ameazimia kutosema chochote, hata ikibidi kuuawa. Uso wake haukuwa na chembe ya mashaka wala uoga. Ni kama alikwisha kata shauri la kufa na siri yake moyoni.

Spoiler alimtazama kwa kitambo kisha alichukua kibubu kidogo cha gesi na kukiwasha, akarekebisha moto kwenye kile kibubu na kumfuata Abbas.

“Tunazo njia nyingi za kukulazimisha uongee ukweli usitake tufike huko, sasa sema ukweli vinginevyo nitakuharibu usiweze kutambulika,” Spoiler alimwambia Abbas huku akiupeleka ule moto wa gesi na kuupitisha kwenye kifua chake.

“Unanitishia kuniua? Wewe ni mpumbavu. Kwa taarifa yako siogopi kifo… hutapata chochote toka kwangu, bora mniue tu kuliko kuendelea kupoteza muda wenu,” hatimaye Abbas alifoka na kumtemea mate Spoiler.

“Naona umejitolea kufa peke yako huku wanaokutuma wakiendelea kustarehe huko waliko,” Spoiler alisema na bila kusita aliujaribu ule moto wa gesi hewani kisha aliupeleka kwenye maeneo nyeti ya Abbas, akaupulizia na kuanza kumuunguza. Abbas alitoa sauti kali ya maumivu.

“Sema ukweli ili nimwambie aache hili zoezi, sipendi tuumizane,” sauti ya Mr. Oduya ilisikika kutoka kwenye spika.

“Hamtopata chochote toka kwangu, wala msihangaike,” Abbas alisema kwa ukali huku akiendelea kugugumia kwa maumivu.

“Unaonekana shujaa, eh! Sijawahi kumuona mtu mpumbavu kama wewe, unadhani kwa hiki unachokifanya utaandikwa kwenye vitabu vya kumbukumbu za mashujaa wa nchi hii? Kwa taarifa yako, hata famlia yako hawawezi kukusifia kwa upuuzi huu!” sauti ya Mr. Oduya ilisikika ikiongea kwa hasira kutoka kwenye spika.

“Naona anatuchezea akili zetu, mpe kubwa kama hataki kutapika taarifa muhimu anazozifahamu,” Mr. Oduya alisema kwa hasira.

“Hawezi kuhimili na anaweza kupoteza maisha…” Spoiler alisema huku akiminya midomo yake.

“Nani anajali!” Mr. Oduya alijibu huku sauti yake ikionesha ghadhabu.

Sasa Mr. Oduya alimtaka Mafuru kwenda kusaidia, na bila kuchelewa Mafuru aliingia kwenye kile chumba. Kufumba na kufumbua Abbas alivuliwa nguo zake na kubaki mtupu kama alivyozaliwa kisha alibebwa na kutundikwa kwenye vile vyuma mfano wa vyuma vya kuning’inizia nyama buchani, kichwa chini miguu juu.

Dakika mbili baadaye Spoiler alikuwa ameshika visu viwili maalumu vilivyokuwa kwenye sinia juu ya meza, akavikamata na kuanza kuvinoa kwa kuvisugulisha vyenyewe kwa vyenyewe huku akitembea mbele ya Abbas.

Nini kitaendelea? Usikose kufuatilia mkasa huu wa kusisimua...
 
Aseee kitu matata Sana hiki
Shukran mkubwa!
 
Mr abbas nimempenda maana kama ni kuumia kisha umizwa sasa ya nn kuwaambia
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom