Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (127)

ILIPOISHIA

Wakati wakikaribia kwenye fremu za maduka yanayozunguka Kanisa la Anglikana, Tunu alitoa noti tatu za shilingi elfu kumi kumi na kuzirushia mbele kwa dereva, “Ukifika mtaa wa Moshi kunja kulia na kuufuata mtaa huo, kisha punguza kidogo mwendo, nishuke halafu wewe ongeza mwendo ili kuwapoteza, sawa?”

Yule dereva aliitikia kwa kichwa huku akilitupia jicho lile gari lililokuwa nyuma yao. Akakunja kuingia kulia akiufuata mtaa wa Moshi huku akimkwepa mtoto mmoja aliyekuwa anakatiza barabara. Muda ule ule Tunu aliufungua mlango akashuka haraka na kuusukuma ule mlango, ukajibamiza. Akachepuka na kujibanza nyuma ya mti mmoja mkubwa wa kivuli jirani ya nyumba moja ya wageni.

Lile gari lililokuwa nyuma yao pia liliingia barabara ile lakini kwa kuchelewa kidogo likaongeza mwendo kuifuata ile taxi. Dereva wa taxi aliufikia mtaa wa Arusha na kuuvuka, akaendelea mbele akiifuata barabara ile ya vumbi. Sasa alikusudia kuwafanya wale watu waamini kuwa yule dada alikuwa bado yumo ndani ya ile taxi.

* * * * *

Kwa mara ya kwanza tangu alipoanza harakati zake za kutaka kuingia ikulu, Mr. Oduya alijikuta katika hali ya wasiwasi na mashaka makubwa. Kwa mbali hofu ilikuwa ikitishia kuutawala moyo wake, hasa kwa hisia zilizokuwa zikimnong’oneza kuwa mambo yameanza kumwendea mrama. Alikuwa amekanganyikiwa akiwa ameketi kwenye kiti chake cha kuzunguka ofisini kwake.

ENDELEA...

Mambo hayo hayakuwa yakimwingia kichwani kwake kabisa, alikuwa anajiuliza ni vipi Tunu akafanikiwa kuwatoroka watu wote waliowekwa kumfuatilia? Tena watu wenye ufanisi mkubwa katika kazi hiyo na wenye silaha? Kidogo akawa amejifunza ni mtu wa aina gani alikuwa anasumbuka naye ndiyo maana baadaye aliamua kuwatuma watu maalumu kwa kazi moja tu, kuua. Watu hao walitakiwa kumuua Tunu popote ambapo wangemwona.

Mr. Oduya aliamini kuwa Tunu hakuwa mtu wa kawaida kama alivyokuwa anamchukulia mwanzo, mbaya zaidi, hata yule dereva teksi Tom ambaye walimtegemea kwa shughuli za kuchukua watu wake na kuwakimbiza huku na kule pia alikuwa amejiunga na Tunu!

Sasa Mr. Oduya alianza kujiuliza iwapo aachane na ndoto ile ya urais kisha atoroke nchi na kukimbilia nchini Canada ambako alikuwa amewekeza kwa kiasi kikubwa, akaishi kwa raha mustarehe na mpenzi wake Zainabu, akitumia utajiri wake mkubwa. Hata hivyo, wazo hilo alilipinga kwa kuona kuwa hiyo ilikuwa dalili ya mtu mwoga. Yeye hakuwa mwoga, hivyo alipaswa kupambana hadi dakika ya mwisho.

Kichwa chake kilikuwa kimechemka utadhani ubongo wake uligeuka kuwa volcano iliyotishia kulipuka wakati wowote, aliuhisi ubongo wake ukiwaka moto na muda wowote kichwa kingelipuka na kusambaratika. Hadi muda huo hakuwa ameambua japo lepe la usingizi, kwa siku mbili mfululizo tangu alipogundua kuwa lile gari aina ya Cadillac DeVille lenye muundo wa kizamani lilionekana Mzizima TV na sasa lilikuwa linamilikiwa na mtu mwingine.

Kwa kuiamini timu yake iliyoongozwa na Spoiler, Mr. Oduya alitegemea suala la kumpata mmiliki mpya wa lile gari na kuliteketeza lile gari lingekuwa rahisi na kuchukua muda mfupi, lakini tangu kuibuka kwa yule binti, Tunu, ambaye alionekana waziwazi kuanzisha vita ili kumkwamisha, mambo yakaanza kwenda mrama.

Timu yote aliyoitegemea kuifanya kazi hiyo ilionekana kuzidiwa akili na yule binti. Mr. Oduya hakujua Tunu alikuwa ana nini hasa? Ni mara ngapi amejaribu kwa uwezo wake wote kutaka kumtia mkononi lakini binti huyo amekuwa akiikwepa mitego yote na kuwapotea katika mazingira ya utata?

Alikuwa ameketi pale kwenye kiti chake kwa takriban dakika arobaini na tano akiwa hajui afanye nini, hiyo ilikuwa ni baada ya kuongea na vijana wake aliowafokea sana kuhusiana na kitendo cha wao kuendelea kuzidiwa akili na Tunu.

“Ninaomba maelezo mafupi sasa hivi, kwa nini mmeshindwa kumnasa huyo binti?” Mr. Oduya aliwauliza Spoiler, Victor na Job waliokuwa wameketi mbele yake huku wamejiinamia.

Spoiler, Victor na Job waliinua nyuso zao, wakatazamana na Spoiler akawa wa kwanza kusema. “Nadhani, bosi hatutakuwa na maelezo ya kukuridhisha kwa nini hatujafanikiwa kumtia mbaroni hadi sasa, kwa sababu…”

“Ni wazembe tu!” Mr. Oduya alimkatiza Spoiler kwa kufoka, uso kaukunja na kutengeneza ndita usoni. “Au mna sababu nyingine?”

Spoiler aliwatupia jicho Victor na Job mara moja kisha akaketi vema kitini. Alishaanza kuingiwa na hofu iliyochanganyika na woga. Alikuwa na kila sababu ya kujisikia vile. Mr. Oduya alikuwa mtu katili sana asiyeruhusu makosa ya kipumbavu yaliyoashiria uzembe yatokee kwenye kazi zake, ingawa machoni kwa watu alionekana mnyenyekevu na mwenye kusaidia jamii lakini ukweli ni kwamba alikuwa hana tofauti na mnyama yeyote wa porini.

“Siyo wazembe bosi,” Spoiler alisema kwa sauti ya chini.

“Kumbe nini?” Mr. Oduya aliuliza huku akimtolea macho. “Mlishajua kuwa Tunu tayari amekutana na Sammy na kisha akagundua kuwa gari lake limewekwa GPS device. Hakukuwa tena na sababu ya kuendelea kumwacha akiwa hai, mlikuwa mnasubiri nini, pingu? Sasa amefanikiwa kuwatoroka, mnataka kusema nini? Ni uzembe tu!” Mr. Oduya alifoka.

Victor alishusha pumzi, akawageukia akina Spoiler na Job waliokuwa wanamtumbulia macho Mr. Oduya kwa wasiwasi.

“Inawezekana kweli kuwa ni uzembe wetu, mzee,” Victor alijikakamua na kusema, “lakini hapa tunamzungumzia Tunu Michael, shushushu mbobezi aliyepata mafunzo maalumu ya kijeshi na mwenye shahada ya umahiri ya ujasusi wa mambo ya usalama na mapambano dhidi ya ugaidi, isitoshe ni ninja na kama ilivyo kwa maninja wote ni kama wanatumia nguvu za mizimu…”

“Upumbavu!” Mr. Oduya alisema huku akishusha ngumi nzito mezani iliyowashtua watu wote. “Hatuzungumzii nguvu ya mizimu katika kazi kama hizi, Victor… wewe na Job pia ni mashushushu. Wewe umekaa miaka mitatu nchini Cuba ukijifunza upelelezi wa kisasa na bado unazungumzia nguvu ya mizimu…” Mr. Oduya alikuwa amefura kwelikweli, sasa alikuwa anaongea kama anayetaka kupiga kelele. “Au mlitakaje? Tuwachanje kwanza chale mwilini ndipo mumkamate Tunu?”

Victor alimlaani sana Mr. Oduya kimoyomoyo, alitamani kumtukana kisha ainuke na kuondoka zake lakini akaogopa, kwani yule mzee hakuwa tajiri tu wa kawaida, alikuwa na nguvu kubwa sana serikalini na ndani ya vyombo vya usalama akiaminiwa na watu wengi kama bilionea anayesaidia jamii.

“Hatuhitaji kuchanjwa chale, mzee, hilo tunalijua. Lakini Tunu, si kama unavyomjua… huyu ni shushushu hatari sana aliyepata mafunzo ambayo katika nchi hii wapo wawili tu, mafunzo hayo ndiyo humsaidia kung’amua jambo lolote hatari kabla halijatokea. Sisi si wazembe, kama unavyotutuhumu. Tumefanya kazi ngapi kubwa na za hatari, mzee?” Victor alisema kwa sauti kakamavu iliyoficha hasira ndani yake.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus

NB: Litro 👩
 
Taxi - (128)

Mr. Oduya alishusha pumzi, akajiegemeza kitini. Ni kweli kabisa Victor na Job walikuwa mashushushu shupavu ambao serikali ilikuwa ikijivunia kuwa nao. Walikubali kukiuka misingi ya kazi yao ya usalama wa taifa ili kumtumikia katika uhalifu wake, wakifanya kazi kwa kujituma bila ya kuhitaji kusimamiwa au kuhimizwa. Mr. Oduya mwenyewe aliwategemea katika kazi zake na aliwaahidi kuwapa nafasi nyeti ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa pindi akishika madaraka ya nchi.

Sasa walikuwa wameondoka kwenda kusaidiana kumtafuta Tunu, alikuwa amewataka wasirudi hapo bila taarifa ya kifo au kichwa cha Tunu, haijalishi kama Tunu ni ninja au anatumia nguvu ya mizimu. Ni kweli Tunu alikuwa shushushu hatari, mbobezi, ninja au vyovyote ambavyo angeitwa, lakini Mr. Oduya alikuwa na uhakika kuwa pamoja na sifa zote hizo bado alikuwa na mwili wa nyama, na risasi haichagui raia, shushushu au ninja.

Jambo lililompa ahueni kidogo Mr. Oduya ni kwamba, aliamini kuwa Tunu bado alikuwa hayajui mambo mengi yaliyokuwa yanaendelea kwenye harakati zake ingawa kitendo chake cha kufanikiwa kukwepa mitego yote aliyowekewa kilitosha kumpa salamu Mr. Oduya kuwa alikuwa anadili na mtu wa aina gani. Shushushu hatari, mbobezi na ninja, kama alivyosema Victor.

Hilo lilizidi kumtisha Mr. Oduya kwani pamoja na kuweka watu wake karibu maeneo yote ya mji na yale aliyodhani Tunu angeweza kufika ikiwemo hospitali ya Amana na Muhimbili, bado hawakufua dafu. Aliona kuwa anatakiwa kutafuta njia mbadala za kumpata Tunu, lakini sasa angempataje? Aliona kichwa chake kinakaribia kupasuka kwani bila kumpata Tunu mambo yake yote yangeharibika. Njia mbadala ya kumpata ilikuwa ni kwa kupitia Victor, lakini sasa wameshaitifua.

Akiwa bado amezama kwenye lindi la fikra alishtuliwa na mtu aliyegonga mlango wa ofisi yake mara moja kisha mlango huo ukafunguliwa. Aliingia mtu aliyevaa suti maridadi ya kijivu mmoja na Mr. Oduya alipomtazama akamtambua mara moja na kushusha pumzi. Alikuwa Dk. Masanja.

Mr. Oduya alishangaa maana hakuwa na miadi yoyote na Dk. Masanja siku hiyo, tangu kikao chao cha kupanga mikakati kilipovunjika usiku ule baada ya taarifa za kuonekana kwa lile gari aina ya Cadillac DeVille lenye muundo wa kizamani, hawakuweza kuongea tena. Dk. Masanja hakuwa na kawaida ya kumtembelea ofisini kwake na hata kama angefika pale ilikuwa ni mpaka wakubaliane. Dk. Masanja alijikaribisha mwenyewe kwenye kiti kisha wakasalimiana.

“Kwani ni kipi kilichotokea, naona hadi leo bado haupo katika hali yako ya kawaida!” Dk. Masanja alimuuliza Mr. Oduya huku akimtazama usoni kwa makini.

“Ni mambo ya kifamilia tu, nisingependa kuyaongelea,” Mr. Oduya alisema huku sura yake ikishindwa kuficha wasiwasi aliokuwa nao, “ni kwamba ninahitaji siku mbili zaidi ili kuyaweka sawa kabla hatujaendelea na mipango yetu.”

Okay!” Dk. Masanja alisema kisha akajiweka sawa kwenye kiti, “Maana hatujawasiliana wala hujatokea pale Paradise Club jambo ambalo si kawaida yako, imenipa wasiwasi kidogo.”

“Uihofu juu yangu, hata hivyo nimeshangaa kidogo kwa ujio wako maana ungeweza kunipigia simu tu badala ya kusumbuka kuja huku.”

“Ni kweli, ila sikutaka kufanya hivyo maana mambo mengine hayafai kuzungumzwa kwenye simu, si unajua tena tupo kwenye ulimwengu wa teknolojia, watu wanaweza kudukua mawasiliano…” Dk. Masanja alisema na kuendelea, “Nilihitaji kujua kuhusu suala la huyu bwana mdogo Sammy!” Dk. Masanja aliuliza huku akimkazia macho Mr. oduya.

“Kuhusu nini?” Mr. Oduya aliuliza huku akionesha mshtuko usoni kwake.

“Naamini unafahamu kilichompata. Nilitaka kujua kama unahusika!” Dk. Masanja aliongea huku kamkazia macho Mr. Oduya.

“Nimesikia yaliyompata lakini si mimi niliyehusika,” Mr. Oduya alisema huku akitingisha kichwa chake kushoto na kulia kukataa.

Dk. Masanja akamtazama kwa sekunde kadhaa kabla hajashusha pumzi na kutia neno, “Mr. Oduya, mimi sipo hapa kukuhukumu ama kukutuhumu. Nipo hapa kuona namna gani tunaweza kufanya ili polisi wasiweze kugundua lolote. Labda nikwambie, nimefuatwa ofisini na maofisa wa polisi wakitaka maelezo yangu kama bosi wa Sammy.”

Mr. Oduya akashtuka kidogo, “Kwani hujawaambia kama alikwisha acha kazi katika hoteli yenu?”

“Sijawaambia lakini wanajua kuwa aliacha kazi, walitaka kujua aliacha lini na kwa nini! Hapa nipo njia panda kwa kuwa inaonekana wanazo taarifa nyingi kuliko tunavyodhani, ndiyo maana nimekuja kwako,” Dk. Masanja alisema na kumeza funda la mate kutowesha koo lake lililokauka.

Mr. Oduya alibaki kimya, alikuwa ametahayari sana. Uso wake haukuweza kuficha hofu aliyokuwa nayo.

* * * * *

Tangu aliposhuka toka ndani ya ile taxi iliyomchukua toka katika mgahawa wa Elli’s, Tunu alitembea kwa tahadhari kubwa huku akiwa na wasiwasi mkubwa. Kubwa lililomsumbua ni jinsi watu wa Mr. Oduya walivyoonekana kupania kumpata kwa gharama yoyote. Alijiuliza, ilikuwaje huko nyuma baada ya kuachana na yule dereva wa teksi? Je, walifanikiwa kumpata? Na kama walimpata walimuhoji? Aliwajibu nini?

Tunu alikuwa na wasiwasi na yule dereva kwani alishaanza kuonesha dalili za hofu na wasiwasi. Kama alihojiwa, akaudhihirisha wasiwasi wake, yawezekana waliamua kumtumia kama chambo ili kuja kumnasa Tunu, au pengine walimpeleka nyumba ya mateso. Yawezekana muda huo alikuwa anapokea mateso wakiamini kuwa alikuwa anayajua mengi.

Mawazo yalikuwa yakipita kichwani kwa Tunu wakati akiambaa na ukuta kuelekea kwenye jengo la wadi ya wagonjwa mahututi wenye kuhitaji uangalizi maalumu katika hospitali ya Amana. Muda wote alikuwa makini sana akizungusha macho yake kila pembe ili kubaini mtego wowote uliokuwa umewekwa dhidi yake. Mawazo hayo yaliufanya moyo wake uongeze kasi ya mapigo yake. Alivuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu.

Inaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (129)

Alikuwa ameingia ndani ya eneo la hospitali ya Amana baada ya kuruka ukuta, pasipo kuambiwa alitambua kuwa watu wa Mr. Oduya wangekuwepo pale hospitali kumsubiri, hivyo ilimbidi kuwakwepa na kuzunguka nyuma ya hospitali ambako alifanikiwa kuingia ndani.

Haikuwa rahisi kuingia ndani ya uzio wa hospitali ile, kwani alipotoka mtaa wa Moshi, alitembea haraka huku akiwa makini kuangalia pande zote na kuvuka barabara ya Uhuru, akaelekea kwenye vibanda vya wasusi wa Kimasai ambapo alipita, akashika njia kama anakwenda kwenye maghorofa ya Ilala. Alipofika eneo lile aliyazungusha macho yake pande zote kutazama kama kulikuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia, hata hivyo hakumwona mtu yeyote hivyo aliendelea na safari yake akiyapita maghorofa ya Ilala na kuambaa ambaa na ukuta wa hospitali.

Aliporidhika kuwa hakuna aliyekuwa akimtazama alichepuka chini ya miti mikubwa iliyokuwa imepandwa kandokando ya ukuta wa Hospitali ya Amana na kwenda kwenye ule ukuta wa hospitali. Akafanikiwa kuufikia ukuta ule ambapo kwa mbinu zake za kijasusi alifanikiwa kuupanda kama anayeruka mtaro mdogo wa maji machafu. Muda mfupi baadaye akatua upande wa pili ndani ya ukuta.

Mara tu alipotua mle ndani alisimama akachunguza vizuri mazingira ya eneo lile. Kulikuwa na miti miwili mikubwa eneo lile na hakukuwapo mtu karibu, na hapo akaanza kutembea kwa tahadhari akiambaa na ukuta huo kuelekea ilipo wadi maalumu ya wagonjwa mahututi wenye kuhitaji uangalizi maalumu.

Alisimama ghafla baada ya kuona eneo lile la nje ya wadi ya wagonjwa mahututi likiwa linalindwa na askari watatu wenye silaha. Askari wale walikuwa makini sana wakizungusha macho yao pembe zote kuhakikisha usalama unakuwepo. Tunu alipochunguza kwa makini akagundua kuwa kila aliyepita eneo lile alisimamishwa na kuhojiwa, na pengine alikamatwa au alizuiwa na kutakiwa kurudi alikotoka.

Alitweta, akajiuliza iwapo alitakiwa aendelee na safari yake au arudi. Katikati ya mawazo hayo, mlio hafifu wa simu yake ya mkononi ukamshtua! Tunu aliiangalia ile simu kwa makini, akaliona jina la Tom. Alijibanza sehemu akaipokea na kuongea, “Hallo!”

“Uko wapi?” Tom aliongea kwa sauti iliyoonesha wasiwasi kidogo.

“Nipo sehemu fulani kuna kitu nafuatilia. Wewe upo wapi?” Tunu alisema huku akizungusha macho yake pembe zote kuhakikisha usalama wake.

“Pia nipo sehemu fulani nimetulia, nilitaka kukwambia kwamba, kuwa makini sana na kila mtu unayepishana naye wakiwemo baadhi ya askari polisi, kuna wauaji wawili wa kukodiwa wamepewa kazi ya kukufuatilia kokote uliko na kukuua, hawatakiwi kufanya kitu kingine isipokuwa kukuua tu,” Tom alisema kwa wasiwasi.

“Usijali kuhusu mimi, watakufa wao kabla hawajafanikiwa kuniua,” Tunu alijibu kwa sauti tulivu ingawa mapigo ya moyo wake yalikuwa yanakwenda mbio isivyo kawaida.

“Vipi umesikia kuhusu kilichompata Sammy?” Tom aliuliza kwa wasiwasi.

“Hapana, amepatwa na nini?” Tunu aliuliza huku akihisi ubaridi mwepesi ukimtambaa mwilini mwake na kuzifanya nywele zake kusisimka.

“Walimtegesha bomu kwenye gari lake, likalipuka wakati ameliegesha na kuingia ndani. Hivi sasa yupo hospitali akiwa mahututi…”

What?” Tunu aling’aka kwa mshtuko mkubwa. Alihisi kama vile moyo wake uliyasahau mapigo yake kwa muda, na yaliporejea yalianza kwenda mbio isivyo kawaida. “Dah! Yupo hospitali gani?” Tunu aliuliza baada ya kitambo.

“Walimpeleka Amana, hali ikaonekana ni mbaya zaidi, wakamhamishia Muhimbili.”

Okay! Vipi kuhusu wewe, bado hawajakushtukia?”

“Dah, sijui nikwambie nini! Ninasakwa kwa udi na uvumba. Nimekutana na rafiki yangu mmoja huwa tunapaki wote pale Elli’s, akanitonya kuwa natafutwa kama gaidi na watu fulani ambao wamemwaga fedha kwa siri pale kijiweni ili nikionekana tu wapewe taarifa. Ila usijali niko poa,” Tom alisema na kushusha pumzi.

“Basi nitakupigia baadaye ili tujue cha kufanya,” Tunu alisema na kukata simu baada ya kuhisi kulikuwa na watu waliokuwa wanaelekea kule alikokuwa. Hakuona sababu ya kuendelea kuwepo pale, akaondoka haraka na kurudi alikotoka akitumia mbinu ile ile ya kijasusi kuupanda ukuta na kurukia nje. Sasa alihisi kuwa eneo lile lilikuwa halifai tena, alipaswa aende sehemu akajipange kwanza kabla ya kuendelea na harakati zake.

* * * * *

Habari za kuvamiwa nyumba ya Sammy, kupigwa risasi mkewe na yeye kujeruhiwa kwa bomu lililotegwa kwenye gari na kuharibu nyumba yao zilitapakaa nchi nzima na nje ya mipaka ya nchi. Hofu ilitanda kila mahali watu wakijiuliza, huyu Sammy alikuwa na nini kiasi cha kuandamwa na watu hao walioonesha wazi kuwa nia yao ilikuwa kumteketeza.

Wakazi wa jiji la Dar es Salaam walikuwa wamezipokea habari zile kwa kitu zaidi ya mshangao, hofu kubwa. Hofu ilipenya katika fikra zao kwa kule kusikia kwamba haikuwepo fununu yoyote juu ya kupatikana kwa watu waliofanya tukio lile ambalo lilionekana ni zaidi ya uhalifu wa kawaida, lilikuwa limefikia kiwango cha kuitwa ugaidi. Kila mtu alimtazama mwenziwe kwa macho yaliyoitangaza hofu iliyojificha moyoni mwake.

Siku hiyo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alikuwa na hasira kali na alikuwa katika uso wa kusawajika kidogo. Hakuna kitu kilichomkasirisha kama wahalifu. Mhalifu alimchukulia kama shetani mwenyewe na alikuwa tayari kumsaka kwa ari zote ili ampate na kumpeleka gerezani alikokuita jehanamu.

Ilikuwa saa tisa alasiri alipowasili kituo kikuu cha polisi akitokea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kukuta watu wa habari: waandishi wa magazeti, redio na televisheni wakimsubiri. Muda wote alikuwa akipokea ujumbe mfupi wa simu na kupigiwa simu toka kwa wakuu wake wa kazi na watu wengine waliotaka kujua jeshi la polisi lilikuwa limefikia wapi katika uchunguzi wake ili kuwabaini waliofanya uhalifu huo.

Safari bado inaendelea. Taxi imezua mambo na sasa wenzi wawili wanapigania uhai vitandani, mmoja yupo Amana na mwingine Muhimbili! Tunu naye anasakwa kama gaidi, popote atakapoonekana anatakiwa auawe. Je, nini kitaendelea? Endelea kufuatilia stori hii ya kusisismua hapa hapa JamiiForums ili kuujua mwisho wake. Ciao...

NB: Litro 👩
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom