Taxi - (134)
Tunu alihisi mwili wake ukizizima kwa hofu na kuishiwa nguvu. Kikatokea kitambo fulani cha ukimya, alipotaka kusema neno akasita baada ya kumwona Winifrida akirudi akiwa amebeba trei ndogo yenye chupa kubwa ya mvinyo aina ya
Pinot Noir na bilauri ndefu, aliiweka ile trei mezani. “Karibu,” alimkaribisha Tunu kwa heshima zote huku akishusha pumzi.
“Ahsante, mdogo wangu,” Tunu alimshukuru Winifrida, akaifungua ile chupa na kumimina mvinyo kwenye bilauri kisha akanyanyua ile bilauri na kupiga funda moja kubwa kisha akairudisha bilauri ile mezani, na hapo wakabaki wakitazamana kwa kitambo. Winifrida alikuwa ameketi kwenye sofa akiwa jirani kabisa na Tunu huku akimtazama kwa namna ambayo hakuna aliyeelewa nini kilikuwa moyoni mwake.
Victoria alimwangalia Winifrida kwa makini kisha akayahamishia macho yake kwa Tunu, wakaangaliana. Macho yao yaliweza kuongea mengi. Victoria akashusha pumzi na kuinuka.
“Utanisamehe kidogo, Tunu, ninakuacha na Winnie, kuna kitu nakwenda kufanya na nitarejea baada ya kama dakika kumi hivi. Jisikie huru,” Victoria alimwambia Tunu na kusimama huku akimtazama kwa makini akionekana kusubiri ruhusa yake.
“Usihofu, dada, maadam nipo na Winnie basi unaruhusiwa kiroho safi,” Tunu alimwambia Victoria huku akiachia kicheko hafifu. Victoria akaondoka akiwaacha Tunu na Winifrida.
* * * * *
“Tunu amefanikiwa kuwatoroka tena!” Mr. Oduya alimaka kwa mshangao uliochanganyika na hasira kwenye simu huku akiyakodoa macho yake mbele kwa hasira kana kwamba kulikuwa na mtu mbele yake aliyekuwa akiongea naye.
Alikuwa akiitazama picha yake mwenyewe iliyokuwa imetundikwa ukutani. Ilikuwa picha kubwa iliyotundikwa jirani na picha ya Rais wa Tanzania, Dk. Yohana Funguo. Mr. Oduya alibaki akiwa kimya ameyakodoa macho yake kwenye ile picha huku akiwa hajui aseme nini. Kwa kadiri alivyomfahamu Tunu, alijua kuwa bila ya kumdhibiti mapema basi angesababisha matatizo makubwa.
Kwa mara nyingine tena katika harakati zake Tunu alikuwa amesababisha hofu katika moyo wake, akahisi jasho jembamba likimtoka usoni. Hakujua afanye nini, kwani aliamini kuwa Tunu alipenda sana kufanya harakati za kimya kimya kwa hadhari na uangalifu zaidi.
Hata hivyo, alifarijika kiasi fulani alipojikumbusha kuwa pamoja na ujanja wote wa Tunu lakini asingeweza kuwakwepa watu wote aliowaweka kumfuatilia, Mr. Oduya aliwaamini sana watu wake aliowaweka sehemu mbalimbali za mji walizoamini kuwa Tunu angeweza kufika au kupita, watu hao walikuwa kikazi na hawakuwa na mzaha kabisa.
Kama Tunu angethubutu kurudi tena hospitali au kulifuata gari lake aliloliacha kule kwenye mgahawa wa Elli’s angekufa kama kuku. Na kama angekuwa mpumbavu kiasi cha kujitokeza ili kupambana na watu wake angekufa pia. Mr. Oduya alitamani kumpata Tunu akiwa hai ili amfundishe adabu, alitamani yeye mwenyewe aitumie bastola yake, kwa dhamira moja tu, kumuua.
Mawazo yakiwa bado yanapita kichwani kwake, alikumbuka kuwa simu ilikuwa bado ipo hewani na upande wa pili wa simu kulikuwa na watu waliokuwa wanasubiri kusikia neno lake. “Tunu ametoroka!” Mr. Oduya aliongea tena, safari hii aliongea kwa sauti ya kunong’ona kana kwamba alikuwa akimnong’oneza mtu aliyekuwa ameketi jirani yake.
“Sikieni, hakikisheni anapatikana haraka kwa gharama yoyote ile, akiwa hai au maiti. Jipangeni maeneo yote kama tulivyokubaliana na msisahau kufuatilia Sinza nyumbani kwake na Sharif Shamba, nyumbani kwa Tom. Ila kuweni makini sana maana ana hila nyingi, msikubali awababaishe,” alisema na kukata simu.
Aliketi kwenye kiti chake kikubwa cha kuzunguka kilichokuwa na magurudumu yaliyokiwezesha kusogea kisha akashusha pumzi za ndani kwa ndani huku akimhurumia Tunu kwa kuwa alikuwa anajihangaisha, kwani asingeweza kufika mbali wala kupata ushahidi wowote wa kumtia Oduya hatiani kuhusiana na suala la Sammy na mkewe.
* * * * *
Baada ya Victoria kuondoka na kuwaacha Tunu na Winifrida wakiwa peke yao, kilizuka tena kitambo kirefu cha ukimya. Katika kipindi kile cha ukimya Tunu alikuwa anatafakari sana kuhusu kazi iliyo mbele yake na jinsi ya kupata ushahidi wa kumtia hatiani Mr. Oduya na genge lake, kama si kwa suala la Sammy na familia yake basi kwa kile alichokifanya hapo kabla.
Alinyakua tena bilauri ya mvinyo aina ya
Pinot Noir na kupiga mafunda mawili na kuirudisha bilauri ile mezani, akamtazama Winifrida kwa makini akijaribu kuyasoma mawazo yake. Kuna jambo alikuwa ameligundua usoni kwa Winifrida, jambo hilo likamfanya aachie tabasamu pana. Winifrida alikuwa ametahayari sana na hakujua aseme nini.
“Pole sana, Winnie, nafahamu ni majonzi kiasi gani uliyo nayo baada
ya mkasa huu uliowakumba kaka’ako na wifi yako. Mimi pia nimesikitika sana ndiyo maana unaniona narudi hapa mara mbilimbili,” Tunu alimwambia Winifrida huku huzuni ikiwa imemshika.
Winifrida alikuwa ameinamisha uso wake akitazama sakafuni huku anamsikiliza Tunu kwa makini halafu akashusha pumzi kwa mkupuo huku akiwa kama anayefikiria jambo fulani, kisha akainua uso wake kumwangalia Tunu huku machozi yakimlenga lenga machoni, akayafuta na kuinamisha tena uso wake kutazama chini.
“Ninaamini kuwa vyombo vya dola vinafanya kazi kikamilifu kuwasaka watu wote waliohusika, hata hivyo sina hakika sana kama watafanikiwa kwani waliofanya hivyo ni watu makini waliojipanga na wanaozifahamu vyema nyendo za maafisa wa usalama wa serikali hii, hali inayowapa mwanya rahisi wa kutopatikana. Mimi na wewe tunawafahamu wahusika, na kwa kupitia ile
memory card tungeweza kuwafanya waozee gerezani lakini tatizo ndiyo imespotea baada ya nyumba kulipuliwa na bomu...” Tunu alisema kwa huzuni huku akimkazia macho Winifrida.
“Nimerudi tena kwako nikitaka kujua, pengine uliamua kunificha au sasa unakumbuka uliiweka sehemu gani. Kama uliiacha kule kule nijue sehemu, naweza kuwatumia watu wangu wa karibu wajaribu kupekua kama wataweza kuiona,” Tunu alimaliza kuongea kisha akainyakua tena ile bilauri ya mvinyo iliyokuwa mezani na kuvuta funda moja kubwa na kuirudisha tena mezani huku akiendelea kumtazama Winifrida.
“Da, Tunu, hata sijui nisemeje sasa!” Winifrida alisema kwa sauti ya chini ya kukata tamaa kama ambaye hakutaka watu wengine zaidi ya Tunu wasikie maongezi yao. Mara hii Tunu aliweza kuhisi kuwa Winifrida alikuwa mwingi wa wasiwasi na alikuwa akiongea kwa woga. Hali hiyo ikamshtua ingawaje alijitahidi sana kuuzuia mshtuko wake.
“Nafahamu kuwa pengine ikawa si rahisi sana kwako kufahamu kaka yako yupo kwenye hatari kwa kiwango gani, ila naamini kuwa ukitulia vizuri na kufikiria unaweza kuwa na hisia ya jambo fulani ambalo huenda likawa msaada mkubwa wa kuniwezesha kuwanasa wote waliohusika,” Tunu alizungumza kwa sauti ya chini huku pia akikwepa maongezi yao yasisikike na watu wengine.
Tunu alifikiria sana na kushusha pumzi, alikuwa anatazama kule alikokuwa ameelekea Victoria katika namna ya kuibia ibia, ingawa alijitahidi sana kuificha hali ile. Tunu aliona, hali hiyo ilikuwa ni ishara nyingine muhimu aliyoweza kuishtukia haraka, hivyo hakuwa na mashaka tena kuwa Winifrida alikuwa na jambo ambalo alitamani sana kulisema ila hakutaka mtu mwingine asikie.
“Ni kweli kuwa nilikuwemo ndani wakati wale majambazi wanaingia lakini hiyo haiwezi kuwa sababu ya mimi kufahamu yaliyokuwa yanaendelea kwa kuwa nilikuwa nimejificha ndani ya kabati,” Winifrida alimjibu Tunu kwa msisitizo.
“Sawa! lakini hebu kumbuka vizuri ulipoihifadhi memory card, naamini kabisa kuwa itakuwa pamoja na simu yako. Je, simu ipo wapi, au nayo uliiacha kule kule nyumbani?” Tunu aimuuliza Winifrida kwa sauti tulivu ya kubembeleza huku moyoni akijyapima maneno yake kama yalikuwa na ukweli wowote.
“Kwa kweli sikumbuki,” Winifrida alijibu na kumfanya Tunu asitishe mohojiano, alibaki akimtazama kwa makini ingawa Winifrida aliendelea kuyakwepesha macho yake pembeni yasikutane na ya Tunu, na kwa hali ile Tunu akajua kuwa Winifrida alikuwa akimficha jambo fulani ambalo asingeweza kumlazimisha aliweke bayana kwa wakati ule.
“Sawa kama hujisikii kuniambia, inawezekana pengine huniamini au ni kweli hujui. Lakini elewa kuwa mimi pia nimeumizwa sana na matukio haya ya kaka yako na wifi yako, nisingeweza kustahimili kuacha kazi zangu zote na kufuatilia suala hili moja tu,” Tunu alisema huku akijinyoosha.
“Basi niitie wifi yako nimuage niondoke zangu, nitaendelea kuwepo hapa jijini kwa muda wa siku kadhaa, hivyo siku ukijisikia kuniambia chochote namba zangu hizi hapa, wewe nibip tu,” Tunu alimwambia Winifrida huku akisimama na kunyoosha mkono wake kumpa
business card yenye namba zake za simu.
Winifrida alionekana kusita kidogo, aliitazama ile kadi kwa wasiwasi kisha macho yake yakahamia kwenye uso wa Tunu, “Basi kaa, n’takwambia ukweli...” alisema huku akimeza mate kutowesha koo lake lililokauka. Tunu alimtazama kwa makini na kuketi tena juu ya sofa.
Mambo yanazidi kunoga. Je, Winifrida anataka kumwambia nini Tunu? Usikose kufuatilia mkasa huu wa kusisimua...
NB:
Litro 👩