Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (125)

ILIPOISHIA

Wakati hayo yanaendelea Madame Norah alikuwa bado amezama kwenye dunia yake, dunia ya kisasi. Sasa alikuwa anahisi kifua chake kikiwaka moto utadhani alikuwa anataka kulipuka! Aliapa kushughulika na yeyote aliyefanya hivyo. Donge la hasira lilikuwa limemkaba kooni na alikuwa anapumua kwa shida kama mgonjwa anayepigania pumzi ya mwisho.

Alichokumbuka kuongea muda huo ilikuwa kuomba ruhusa ya kumwona Sammy kabla hajapelekwa Muhimbili. Wote waliongozana hadi nje walikolikuta gari la wagonjwa likiwa tayari kuondoka. Sammy alikuwa kalala kwenye kitanda maalumu hajitambui, alikuwa kama mfu akiwa anapumua kwa msaada wa mashine ya maalumu ya kumsaidia kupumua na alikuwa ametundikiwa chupa maalumu ya maji aina ya Normal Saline yaliyowekwa dawa maalumu ndani yake ili kusaidia kuyafanya mapigo ya moyo wake yasishuke.

Wote walishindwa kuyazuia machozi, walijikuta wakilia kwa uchungu huku wakimwangalia Sammy ambaye alikuwa ametulia, hatingishiki. Madame Norah alimwita Sammy huku akibubujikwa na machozi kana kwamba ni mama aliyempoteza mwanawe wa pekee kwenye shimo refu sana, alimwita huku akilia kilio cha uchungu.

SASA ENDELEA...

Muda huo Madame Norah alikuwa anatiririkwa na jasho jingi hali iliyoanza kuwapa wasiwasi mkubwa walinzi wake na watu wengine waliokuwepo mahali hapo.

* * * * *

Tunu aliufungua mkoba wake, akatoa noti moja ya shilingi elfu kumi na kumpatia mlinzi mmoja kijana aliyekuwa akilinda katika eneo la viunga vya maegesho ya magari la mgahawa maarufu wa Elli’s. alimpa ile fedha kama ‘tip’ akimwomba kumwangalizia gari lake makini ili mtu yeyote asilifikie na kupachika kifaa. Tunu alikuwa ameamua kwenda kuliacha lile gari pale Elli’s kutokana na kuhisi usalama wake ungekuwa shakani endapo angeendelea kulitumia.

Alikuwa amepata wazo la kwenda kuliacha lile gari pale kwenye mgahawa wa Elli’s wakati alipokuwa akitoka Shaurimoyo, japo alikuwa amefanikiwa kung’amua mtego wa adui zake kumwekea kifaa cha GPS lakini aliamini kuwa wangeendelea kumwandama, hasa baada ya kugundua kuwa alikwisha ng’amua mtego huo.

Sasa alikuwa akimtilia shaka kila mtu, hakutaka kumwamini mtu kirahisi hasa kila alipokumbuka kuwa hata Victor, mtu aliyemwamini sana aliweza kumsaliti, hivyo alijiambia kuwa alipaswa kuwa makini zaidi. Ndipo alipofikia hatua ya kupeleka gari lake pale Elli’s akiamini kuwa hiyo ndiyo ilikuwa sehemu pekee kwa wakati huo ingeweza kuwa salama kwa gari lake.

Eneo la viunga vya maegesho ya magari la Elli’s lilikuwa na ulinzi madhubuti likiwa limezungushiwa kamera za ulinzi kila sehemu. Hata hivyo, hakutaka kuzitegemea kamera peke yake, ndipo alipoamua kumtafuta yule kijana mlinzi ambaye kwa macho tu aliweza kutambua kuwa alikuwa mwaminifu. Akamwachia jukumu hilo na kumtaka ampigie simu endapo angehisi jambo lolote lisilo la kawaida kwenye gari lake. Muda huo eneo lile lilikuwa na magari yasiyopungua therathini, mengi yakiwa ya watu wenye vipato vya juu.

Baada ya kuachana na yule mlinzi, Tunu alitoka na kuelekea sehemu zilipokuwa zimeegeshwa taxi, upande wa pili wa barabara. Alitazama pande zote mbili kabla hajavuka barabara na kwenda kuingia kwenye taxi moja, ambayo dereva wake alikuwa mtu mzima, mrefu na mwembamba mwenye sura ya ucheshi muda wote akiwa amevaa kofia aina ya baragashia, shati la mistari ya pundamilia, suruali ya kijivu na makubazi meusi ya ngozi miguuni.

Kwa mtazamo wa haraka haraka Tunu aliona ile taxi ingemfaa sana, alipoifikia alifungua mlango wa nyuma na kuingia haraka, akaketi huku akimtaka dereva ampeleke hospitali ya Amana. Yule dereva aliwasha injini, akaliondoa gari taratibu na kuifuata barabara ya lami iliyokuwa inakwenda kutokea hospitali ya Amana. Zikapita kama sekunde tano tu tangu waondoke eneo la maegesho ya taxi, gari jingine aina ya Toyota Wish la rangi nyeusi ambalo lilikuwepo karibu na maegesho yale ya taxi, nalo likaondoka kuwafuata.

Ile taxi haikwenda mbali kabla Tunu hajakumbuka wajibu wake. Toka katika siti ile ya nyuma aliyoketi alikizungusha kichwa chake taratibu kutazama nyuma bila kumshtua dereva na hapo mwili wake ukajikuta ukiingiwa na ubaridi wa ghafla. Aliliona lile gari aina ya Toyota Wish lenye watu wawili mbele likiwa nyuma yao.

Alikumbuka kuliona lile gari likiwa limeegeshwa karibu na maegesho ya taxi pale nje ya mgahawa wa Elli’s wakati alipofika kutoka Shaurimoyo na kuingiza gari lake ndani ya viunga vya magari vya mgahawa wa Elli’s, hata alipotoka na kuvuka barabara kisha akaingia ndani ya ile taxi alikuwa ameliona tena lile gari likiwa palepale, na sasa lilikuwa nyuma yao. Aligeuka na kumtazama dereva wake kwa udadisi na kugundua kuwa alikuwa hafahamu chochote kilichokuwa kikiendelea. Tunu akageuka tena kutazama kule nyuma.

Lile gari aina ya Toyota Wish lilikuwa nyuma yao kiasi cha umbali wa mita therathini hivi na lilikuwa linakuja kwa mwendo wa kasi likionekana kutaka kuwapita. Kilichozidi kumtia hofu Tunu ni kuwa wale watu sasa walionekana wazi kuwa walikuwa wamedhamiria kumfuatilia pasipo uficho wowote. Akapanga kubadilisha mwelekeo ili kuwapoteza.

“Dereva, ongeza mwendo na uhakikishe gari lolote toka nyuma yetu lisitupite,” Tunu alimwambia yule dereva, na pasipo kuhoji chochote yule dereva aliongeza mwendo.

Kwa kitendo kile cha lile taxi kuongeza mwendo Tunu alikuwa na uhakika kuwa kingetosha kabisa kuwafahamisha wale watu kwenye lile gari lililokuwa nyuma yao kuwa tayari alikuwa ameshawashtukia hila yao, hata hivyo, hilo halikumpa shida. Akili yake sasa ilikuwa makini mno kupanga mikakati ya namna ya kuwapoteza wale watu.

Hakutaka wajue kama alikuwa anakwenda Amana, kwani alihitaji sana kuongea na Sammy ili amweleze ukweli kuwa yeye ni ofisa wa usalama na kwamba alikwisha gundua kuwa adui yake ni Mr. Oduya, hivyo alipaswa achukue tahadhari.

“Dereva, naomba ukifika mwisho wa hii barabara ingia kulia,” Tunu alimwambia yule dereva na kumfanya ashangae kidogo.

“Kwani tunaelekea wapi, bosi wangu? Mimi nilidhani tunaelekea hospitali ya Amana!” yule dereva alihoji kwa mshangao huku akimtupia jicho Tunu kupitia kwenye kioo cha kati cha gari kinachotumika kutazama vitu vilivyoko nyuma.

“Hatuelekei tena Amana kuna mtu nahitaji kuonana naye kwanza kabla ya kuelekea huko,” Tunu alimdanganya yule dereva huku akiwa anafikiria cha kufanya endapo lile gari lililokuwa nyuma yao lingefanikiwa kuwafikia au kuwapita. Alipeleka mkono wake kiunoni, akaigusa bastola yake ndogo aina ya Glock 19M ambayo hutumiwa na wapelelezi wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI), mwili ukamsisimka.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus

NB: Litro 👩
 
Taxi - (126)

“Oh! kumbe umebadili mawazo, ungeniambia ni wapi tunapoelekea sasa badala ya kusema tu ingia kulia!” yule dereva alisema kwa jazba kidogo. Wakati huo ile taxi ilikuwa inafika mwisho wa ile barabara, dereva akaingia kulia.

“Wewe fuata maelekezo yangu, suala la fedha siyo tatizo,” Tunu alimjibu kwa sauti tulivu lakini akionekana kukerwa kidogo.
“Sawa basi usijali bosi wangu, wewe kwangu siyo mfalme tu, hata ukitaka urais nakupa. Wewe sema popote nitakupeleka,” yule dereva alisema huku uso wake ukitengeneza tabasamu la kirafiki.

“Ingia upande wa kulia hapo kama unaifuata barabara ya Uhuru kisha uingie kushoto kuufuata mtaa wa Tukuyu,” Tunu alimwambia yule dereva wakati wakiifikia ile barabara ya Uhuru iliyokuwa na msongamano wa magari muda huo.

Dereva akafanya kama alivyoagizwa. Aliliingiza gari lake katika barabara ya Uhuru kama aliyekuwa anaeleka Buguruni kisha akachepuka na kuufuata ule mtaa wa Tukuyu huku gari likikosakosa kugongana na daladala linalofanya safari zake kati ya Mnazi Mmoja na Banana. Pasipo kujali matusi ya dereva na abiria wa lile daladala, yule dereva aliongeza mwendo wakapita mtaa ule uliokatiza katikati ya makazi ya watu hadi walipoufikia mtaa wa Kasulu.

Walipokuwa mwishoni mwa mtaa ule wa Tukuyu kabla hawajaufikia mtaa wa Kasulu Tunu akageuka tena nyuma kulitazama lile gari lililokuwa limewafungia mkia kwa nyuma. Bado lilikuwa likiwafuatilia na sasa lilikuwa likiufuata mtaa ule wa Tukuyu likiwa katika mwendo wa kasi. Ilionekana wazi kabisa kuwa watu waty hawakuonekana kuwapa mwanya wa kuwatoroka.

Kengele ya hatari ikalia kichwani kwa Tunu, sasa alihisi kuwa wale watu walikuwa wamedhamiria kufanya jambo baya zaidi, pengine walidhamiria kuua. Hakuona tena sababu ya kuendelea kumficha dereva wake, kwani kumficha kungemfanya kuwa na wakati mgumu sana wa kuwapoteza wale watu.

“Naomba nisikilie, sina sababu ya kukuficha kwa sababu nakuamini. Kuna gari nyuma yetu linatufuata tangu tulipotoka kule Elli’s, fanya namna yoyote ya kuhakikisha unawapoteza kwani sitaki kabisa wajue naenda wapi, sawa?” Tunu alimwambia yule dereva kwa sauti ya kuamuru.

Yule dereva akaangalia nyuma na kuliona lile gari aina ya Toyota Wish likizidi kuwasogelea, akaonekana kushtuka sana na kumtupia Tunu jicho huku wasiwasi ukijengeka usoni kwake. “Kwa nini wakufuatilie, kwani umewafanya nini, dada?” yule dereva aliuliza huku akihisi jasho likimtoka mwilini.

“Yule ni mume wangu, nimemtoroka nyumbani. Naomba fanya nilivyokwambia mambo mengine nitakueleza tukishawapoteza,” Tunu alisema huku akigeuza shingo yake kutazama nyuma. Dereva akamwelewa na kuchepuka kuufuata mtaa wa Kasulu upande wa kushoto. Muda huo Tunu aligeuka tena kutazama nyuma akaliona lile gari likizidi kuwasogelea, akatabasamu huku akijisemea moyoni, “Nyie subirini tu, dawa yenu ipo jikoni.”

Sasa dereva wa taxi alianza kuendesha gari kama aliyepandwa na kichaa, alipoufikia mtaa wa Arusha akakunja kushoto akiufuata ule mtaa kisha akakunja kuingia kulia na kuufuata mtaa wa Pangani kisha akakunja tena kuingia kulia akiufuata mtaa wa Mwanza. Mtaa ule ulikuwa mfupi, akakunja kuingia kulia kwake akiufuata mtaa wa Tanga, akawa anarudi nyuma kwenda kutokea tena mtaa wa Arusha.

Walipoingia tena kwenye barabara ya mtaa wa Arusha Tunu akageuka tena kulitazama lile gari kwa nyuma, akafarijika kutoliona likiwa nyuma yao na hapo akageuka tena mbele kumtazama dereva ambaye alikuwa anatabasamu. Katika mtaa ule wa Arusha dereva aliingia kushoto na walipofika Pangan Water, Ilala Depot akaingia kulia kuufuata mtaa mmoja wa barabara ya vumbi hadi alipoufikia tena mtaa Tukuyu.

Walipokuwa wanaingia katika mtaa ule wa Tukuyu Tunu alipogeuka tena kutazama nyuma, na hapo moyo wake ukapiga kite kwa nguvu kama aliyepigwa konde zito la kushtukiza kichwani. Lile gari aina ya Toyota Wish lilikuwepo nyuma yao. Akashtuka sana. Hata yule dereva pia alishtuka sana. Tunu alimwona yule dereva akibabaika kidogo.

“Usijali, wewe nyoosha moja kwa moja, nitakwambia cha kufanya,” Tunu alimwambia yule dereva huku akipeleka mkono wake kiunoni, akaishika bastola yake akiwa tayari kwa lolote. Dereva wa taxi aliongeza mwendo. Wakati huo akili ya Tunu ilikuwa inafanya kazi haraka sana ili aweze kujinasua kutoka kwenye mawindo ya wale watu walioonekana kuwa na uchu wa kuutoa uhai wake.

Wakati wakikaribia kwenye fremu za maduka yanayozunguka Kanisa la Anglikana, Tunu alitoa noti tatu za shilingi elfu kumi kumi na kuzirushia mbele kwa dereva, “Ukifika mtaa wa Moshi kunja kulia na kuufuata mtaa huo, kisha punguza kidogo mwendo, nishuke halafu wewe ongeza mwendo ili kuwapoteza, sawa?”

Yule dereva aliitikia kwa kichwa huku akilitupia jicho lile gari lililokuwa nyuma yao. Akakunja kuingia kulia akiufuata mtaa wa Moshi huku akimkwepa mtoto mmoja aliyekuwa anakatiza barabara. Muda ule ule Tunu aliufungua mlango akashuka haraka na kuusukuma ule mlango, ukajibamiza. Akachepuka na kujibanza nyuma ya mti mmoja mkubwa wa kivuli jirani ya nyumba moja ya wageni.

Lile gari lililokuwa nyuma yao pia liliingia barabara ile lakini kwa kuchelewa kidogo likaongeza mwendo kuifuata ile taxi. Dereva wa taxi aliufikia mtaa wa Arusha na kuuvuka, akaendelea mbele akiifuata barabara ile ya vumbi. Sasa alikusudia kuwafanya wale watu waamini kuwa yule dada alikuwa bado yumo ndani ya ile taxi.

* * * * *

Kwa mara ya kwanza tangu alipoanza harakati zake za kutaka kuingia ikulu, Mr. Oduya alijikuta katika hali ya wasiwasi na mashaka makubwa. Kwa mbali hofu ilikuwa ikitishia kuutawala moyo wake, hasa kwa hisia zilizokuwa zikimnong’oneza kuwa mambo yameanza kumwendea mrama. Alikuwa amekanganyikiwa akiwa ameketi kwenye kiti chake cha kuzunguka ofisini kwake.

Itaendelea...

NB: Litro 👩
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom