Taxi - (124)
Madame Norah alishindwa aseme nini tena, aliweka mikono yake kichwani huku michirizi ya machozi ikianza kuonekana kwenye macho yake. Alibaki kimya kwa kitambo kifupi akionekana kuwa mbali sana kifikra kisha akamwashiria yule daktari amsubiri palepale. Akafuta machozi na kuingia ndani huku akijitahidi kutokuonesha hisia zozote za majonzi ingawa uso wake ulisindwa kuficha ile hali ya kunyong’onyea. Mikono alikuwa ameikunjia kifuani.
“Vipi, dada, kuna nini kimetokea?” Bi. Pamela alimuuliza Madame Norah huku akimtazama kwa makini.
Madame Norah alimtupia jicho Joyce ambaye pia alikuwa anamtazama usoni, akashusha pumzi na kulazimisha tabasamu ingawa bado tabasamu lake halikuweza kuiondoa hisia ya majonzi usoni kwake. Alibaki amesimama akiwa kimya huku akionekana kutafuta neno la kumwambia Bi. Pamela kwani hakutaka kuongea mbele ya Joyce kwa kuhofia kumsababishia matatizo mengine.
“Kuna nini?” Bi. Pamela aliuliza tena.
“Kuna matatizo fulani yametokea ofisini kwangu, nahitajika kwenda mara moja kuyashughulikia. Sasa njoo tuongee mara moja,” Madame Norah alimwambia Bi. Pamela aliinuka na kumfuata, wakatoka nje ambako walimkuta Daktari Mshana akisubiri.
“Sasa sikiliza, naomba uwe jasiri kwa hiki ninachokwenda kukwambia, sawa...” Madame Norah alianza kusema, “Nyumba ya mkweo Sammy imeshambuliwa na watu wasiojulikana wakati wao wakiwamo ndani...” Madame Norah alisema kwa sauti ya kumtetemeka.
“Mungu wangu! Wamesalimika kweli?” Bi. Pamela aliuliza kwa huku akihisi mwili wake ukiishiwa nguvu.
“Nimeambiwa mmoja wao yupo mahututi na mwingine kaumia kidogo tu, sasa sijajua ni nani aliye mahututi na nani hajaumia sana...” Madame Norah alisema huku akishindwa kuzuia machozi. Bi. Pamela naye hakuvumilia, akaanza kulia.
Daktari Mshari aliwataka wamfuate, wakaondoka hadi kwenye chumba kimoja ambako walimkuta Jengo akiwa amepumzishwa, mwili wake ulikuwa umelowa damu na alikuwa amefungwa bandeji kichwani na kwenye jeraha katika mkono wake wa kulia lililokuwa linatoa damu. Mwili wake wote ulikuwa unamteteteka kwa hofu ya kile alichokuwa amekishuhudia siku hiyo.
Madame Norah na Bi. Pamela walimtazama kwa mshangao mkubwa, kisha wakaangalia kwa kitambo pasipo kuongea chochote. Sammy hakuwemo katika chumba hicho. Kisha Madame Norah aliyarudisha macho yake kumwangalia Jengo huku mwili wake ukitetemeka. Machozi yalianza kububujika machoni na midomo yake ilishindwa kutulia, alikuwa anatetemeka japo alijitahidi kubana meno yake lakini bado haikusaidia.
Moyo wake ulikuwa umevunjika, hakutegemea kabisa kama siku ile ingegeuka kuwa ya huzuni kiasi kile badala ya kuwa siku ya furaha, furaha ya kumpata binti yake waliyepotezana kwa miaka therathini na mbili. Moyo wake sasa ulikuwa kama unaovuja damu ndani kwa ndani. Japo amewahi kupita katika mapito magumu sana lakini hakuwahi kuhisi hisia kama hizo hapo nyuma. Hakuwahi kuhisi namna ile tangu kuzaliwa kwake, hisia mchanganyiko wa hasira, uchungu na mfadhaiko kwa pamoja! Alitamani kupiga yowe kali kwa ghadhabu lakini hakuweza.
“Mkwe wangu yuko wapi, mbona simuoni hapa?” Bi. Pamela alimudu kuuliza baada ya kimya kirefu kutamalaki mle ndani.
“Hali yake ni mbaya sana, tulichohitaji ni kuwapa taarifa kuwa anapelekwa moja kwa moja Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, tayari taratibu zingine zote zimeshafanyika,” Daktari Mshana alisema huku akiangalia saa yake ya mkononi.
“Kwa hiyo dokta, huyu mwingine hajaumia mahala kokote?” Bi. Pamela alimuuliza Daktari Mshana huku akimtazama Jengo kwa namna ya kumkagua.
“Hata sijielewi elewi. Najihisi kama mtu niliyekufa,” Jengo alijibu huku akijitazama kwa namna ya kujikagua.
“Usiseme hivyo, hujafa. Bado unaishi...” Bi. Pamela alisema huku machozi yakimlengalenga machoni, kisha akaongeza, “Kwani hakuna sehemu yoyote inauma?”
“Ninasikia maumivu makali hapa katika mkono wa kulia labda kidogo kichwani na chini ya mguu wa kushoto,” Jengo alisema huku akionesha maeneo yenye maumivu.
“Pole sana,” Bi. Pamela alisema kwa upole huku akijifuta machozi.
Wakati hayo yanaendelea Madame Norah alikuwa bado amezama kwenye dunia yake, dunia ya kisasi. Sasa alikuwa anahisi kifua chake kikiwaka moto utadhani alikuwa anataka kulipuka! Aliapa kushughulika na yeyote aliyefanya hivyo. Donge la hasira lilikuwa limemkaba kooni na alikuwa anapumua kwa shida kama mgonjwa anayepigania pumzi ya mwisho.
Alichokumbuka kuongea muda huo ilikuwa kuomba ruhusa ya kumwona Sammy kabla hajapelekwa Muhimbili. Wote waliongozana hadi nje walikolikuta gari la wagonjwa likiwa tayari kuondoka. Sammy alikuwa kalala kwenye kitanda maalumu hajitambui, alikuwa kama mfu akiwa anapumua kwa msaada wa mashine maalumu ya kumsaidia kupumua na alitundikiwa chupa maalumu ya maji aina ya
Normal Saline yaliyowekwa dawa maalumu ndani yake ili kusaidia kuyafanya mapigo ya moyo yasishuke.
Wote walishindwa kuyazuia machozi, walijikuta wakilia kwa uchungu huku wakimwangalia Sammy ambaye alikuwa ametulia, hatingishiki. Madame Norah alimwita Sammy huku akibubujikwa na machozi kana kwamba ni mama aliyempoteza mwanawe wa pekee kwenye shimo refu sana, alimwita huku akilia kilio cha uchungu.
Itaendelea...
NB:
Litro 👩🦱