Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (130)

ILIPOISHIA

Wakazi wa jiji la Dar es Salaam walikuwa wamezipokea habari zile kwa kitu zaidi ya mshangao, hofu kubwa. Hofu ilipenya katika fikra zao kwa kule kusikia kwamba haikuwepo fununu yoyote juu ya kupatikana kwa watu waliofanya tukio lile ambalo lilionekana ni zaidi ya uhalifu wa kawaida, lilikuwa limefikia kiwango cha kuitwa ugaidi. Kila mtu alimtazama mwenziwe kwa macho yaliyoitangaza hofu iliyojificha moyoni mwake.

Siku hiyo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Naibu Kamishna Ramon Mamboleo alikuwa na hasira kali na alikuwa katika uso wa kusawajika kidogo. Hakuna kitu kilichomkasirisha kama wahalifu. Mhalifu alimchukulia kama shetani mwenyewe na alikuwa tayari kumsaka kwa ari zote ili ampate na kumpeleka gerezani alikokuita jehanamu.

Ilikuwa saa tisa alasiri alipowasili kituo kikuu cha polisi akitokea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kukuta watu wa habari: waandishi wa magazeti, redio na televisheni wakimsubiri. Muda wote alikuwa akipokea ujumbe mfupi wa simu na kupigiwa simu toka kwa wakuu wake wa kazi na watu wengine waliotaka kujua jeshi la polisi lilikuwa limefikia wapi katika uchunguzi wake ili kuwabaini waliofanya uhalifu huo.

ENDELEA...

Hakutaka kuongea na mwanahabari yeyote kwa muda ule, kwani hakuwa amepokea taarifa yoyote toka kwa wasaidizi wake. Aliposhuka garini alielekea moja kwa moja ofisini kwake. Ilikuwa ofisi pana na sakafuni ilifunikwa kwa zulia maridadi jekundu na katikati ya lile zulia likiwa na nembo kubwa ya Jeshi la Polisi la Tanzania.

Ndani ya ofisi ile kulikuwa na meza ndefu ya mikutano iliyozungukwa na viti kumi na mbili. Viti vitano upande wa kushoto, viti vingine vitano upande wa kulia, kiti kimoja mwanzoni mwa ile meza na kiti kimoja kilikuwa mwisho wa meza.

Naibu Kamishna Mamboleo aliketi juu ya kiti chake kikubwa chenye foronya laini cha kuzunguka na chenye magurudumu yaliyokiruhusu kusogea, kiti kile kilikuwa nyuma ya meza kubwa ya ofisini yenye majalada mengi juu yake. Bendera ndogo mbili zilionekana juu ya ile meza, moja ikiwa bendera za Taifa na nyingine ya Jeshi la Polisi. Vitabu kadhaa vikiwemo vya Sheria na Katiba ya Tanzania, kidau cha wino, mhuri na kichupa kidogo chenye wino mweupe wa kufutia maandishi.

Pembeni ya ile meza ya ofisini kulikuwa na mashine ndogo ya kidijitali ya kurudufu, mashine maalumu ya kuchapa barua na nyraka mbalimbali za kiofisi, mashine ya picha na mashine moja ya nukushi. Naibu Kamishna Mamboleo alishusha pumzi ndefu.

“Majaribo mawili ya mauaji katika familia moja ndani ya saa kumi na nne!” Naibu Kamishna Mamboleo alijikuta akiropoka. “Mke kwa risasi na mume kwa bomu! Ni nani hawa waliofanya hivi? Na kwa nini wafanye hivi kwa familia hii? Je, familia hii ina adui yeyote?” Naibu Kamishna Mamboleo alijiuliza.

Hata hivyo, hakutarajia kupata majibu haraka kiasi hicho kwani alikuwa anasubiri uchunguzi uliokuwa ukifanywa na vijana wake machachari wakiongozwa na Inspekta Abel wa mkoa wa kipolisi wa Ilala. Hata hivyo, kama kuna kitu kilikuwa kinamsumbua sana Naibu Kamishna Mamboleo ni kusubiri. Subira ni jambo lililokuwa likimtesa mno kama adhabu. Alihisi kila dakika aliyoendelea kusubiri ilikuwa ikimjeruhi moyo wake na kuutia jeraha. Kiti alichokalia alikihisi kilikuwa kinawaka moto.

Wazo kuu lilikuwa moja tu, awapate vipi wahalifu hao wasio na hata chembe ya huruma, wahalifu wenye kutaka kuichafua amani ya nchi hii na kufurahia kumwaga damu isiyo na hatia? Angepeda sana kuwapata wahalifu hao haraka iwezekanavyo. Tatizo lilikuwa angewapataje haraka kiasi hicho? Jiji la Dar es Salaam lilifurika watu wote: wema kwa waovu, wenye hatia kwa wasio na hatia. Ni vipi awapate watu wachache wenye hatia miongoni mwa mamilioni wasio na hatia kwa muda mfupi?

Kila alivyojiuliza alijikuta akipata jibu moja tu, jibu lililozidi kumjeruhi moyo wake, hakuwa na budi ya kusubiri taarifa ya uchunguzi! Alitakiwa asubiri hadi hapo wasaidizi wake wamalize uchunguzi wao na kukusanya taarifa zote muhimu za kiitelijensia ambazo zingewaongoza hadi mbele ya wahalifu hao.

Taarifa hizo zilitegemea sana kuifahamu mienendo ya Sammy katika siku za karibuni na watu aliokuwa anakutana nao, wapi alikokuwa usiku wa siku ambayo mkewe alipigwa risasi, alikopita kabla ya kufika nyumbani, watu gani waliokutana nao siku hiyo au alioongea nao kwenye simu na mambo gani waliyoongea.

Ni hayo ambayo yangetengeneza njia ya kuwapeleka polisi kwa wahalifu hao, lakini ilihitajika subira. Kusubiri kulimtisha zaidi Naibu Kamishna Mamboleo kuliko hata wahalifu wenyewe. Hakupenda kuketi ofisini akisubiri kwa sababu hakujua wahalifu hao walikuwa wanapanga nini katika kipindi hicho, pengine walikuwa wanajiandaa kushambulia watu wengine wasio na hatia au hata kutoroka nchi!

Sababu nyingine iliyomfanya ashindwe kusubiri ni kwamba raia wema jijini Dar es Salaam walikuwa wamejawa hofu kubwa na usalama wao, ni yeye Naibu Kamishna Mamboleo aliyekabidhiwa jukumu la kuhakikisha raia na mali zao ndani ya jiji la Dar es Salaam wanakuwa salama.

Hakupendezwa kabisa na hali ile, kama mlinzi wa amani katika jiji la Dar es Salaam, aliyepewa dhamana hiyo na taifa, asingeweza kukaa kwa amani ofisini kwake akishuhudia amani hiyo ikitoweka na hata kuwafanya raia wema kuanza kuichukia serikali yao.

Hadi muda huo jeshi la polisi lilikwisha wahoji watu wengi wakiwemo majirani wa Sammy, marafiki, jamaa wa karibu na hata wafanyakazi wa Udzungwa Beach Resort alikokuwa akifanya kazi Sammy kabla hajaacha. Katika mahojiano na msako mkali uliofanywa, wapo wengi waliokamatwa na kushikiliwa na polisi kwa mahojiano zaidi baada ya kushukiwa kuhusika, lakini bado kulikuwapo maswali mengi ya kukanganya yaliyotakiwa kupatiwa majibu ili kuwaongoza polisi mbele ya wahalifu hao.

Hata hivyo, kulikuwa na mtu mmoja tu katika jiji zima la Dar es Salaam ambaye alikuwa na majibu yote ya maswali hayo. Mtu huyo, msichana mrembo, mrefu, maji ya kunde na mwenye umbo matata lenye kuweza kuitaabisha vibaya nafsi ya mwanamume yeyote, alikuwa na sura ya duara, macho malegevu, pua ndefu na midomo yenye kingo pana.

Mtu huyo machoni kwa jamii isiyoelewa kazi yake alionekana binti mrembo aliyepaswa kuolewa na mwanamume mwenye fedha zake akatulia ndani, azae na kumhudumia mume basi. Lakini kwa magaidi na wahalifu wa kimataifa, binti huyo aliogopwa sana kwani alikuwa na uwezo mkubwa na mbinu nyingi za kumfikia adui na oparesheni alizowahi kuzifanya ziliwafanya wengi kuhisi pengine hakuwa binadamu wa kawaida.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple the-sniper MR KUO dan oseko Jackal kuku mweus mtugani wa wapi huyo

NB: Litro 👩
 
Taxi - (131)

Huyu ni mtu aliyeijua vyema njia ya kuelekea mbele ya wahalifu hao walioleta taharuki jijini Dar es Salaam na tayari alikuwa mbele ya wakati akitumia mbinu zake kuifuata njia aijuayo mwenyewe hadi ahakikishe wahalifu hao wanapokea tuzo ya uhalifu wao. Tatizo lilikuwa moja tu, alihitaji ushahidi kamili ili kuwafikisha wahalifu hao mbele ya sharia. Ushahidi huo ulikuwa umefichwa kwenye memory card ambayo sasa ilikuwa imepotelea ndani ya nyumba ya Sammy baada ya kubomolewa na bomu. Mtu huyo aliitwa Tunu Michael.

* * * * *

Elli na Jengo walikuwa wamejiinamia kwa huzuni kwenye mabenchi nje ya chumba maalumu cha wagonjwa mahututi wenye kuhitaji uangalizi maalumu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kila mmoja aliwaza lake na walionekana wamekata tamaa. Sammy alikuwa bado hana fahamu na juhudi za kuyaokoa maisha yake zilikuwa zikiendelea kufanywa na jopo la madaktari bingwa watano wa hospitali hiyo.

Muda wote akina Elli walikuwa wakiwasiliana na akina Madame Norah na Bi. Pamela waliokuwa katika Hospitali ya Amana, ili kujua maendeleo ya kila upande. Hadi muda huo Joyce hakuwa ameambiwa chochote kuhusiana na hali ya Sammy, ingawa alikuwa akisumbua sana kwa maswali ya “Sammy yupo wapi?”; “Mbona haji kuniona?” na kadhalika.

Eneo lote kuzunguka jengo la wadi ya wagonjwa mahututi wenye kuhitaji uangalizi maalumu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili alimokuwa amelazwa Sammy lilikuwa na ulinzi mkali wa polisi wenye silaha, nia ilikuwa ni kuzuia uwezekano wa watu wenye nia ovu ya kutaka kumuua Sammy wasijipenyeze ndani ya kile chumba alimolazwa.

Pia ilikubalika kuwa hata matibabu ya Sammy yafanywe kwa usiri mkubwa kutokana na hali ya wasiwasi iliyokuwa imelikumba jiji zima la Dar es Salaam.

Uchunguzi wa awali kuhusu hali ya Sammy ulionesha kuwa alikuwa amepatwa na tatizo la mtikisiko wa ubongo, tatizo ambalo kitalaamu lilijulikana kama brain concussion. Tatizo hilo liligunduliwa baada ya jopo hilo la madaktari bingwa watano kumfanyia uchunguzi na wasiwasi ulikuwepo miongoni mwao kuwa lingeweza kumfanya Sammy apoteze maisha mara moja au baada ya siku kadhaa.

Hadi muda ule walikuwa wanaendelea na vipimo katika sehemu ya maini yake na majimaji ya machoni kuona kama ubongo wake ulikuwa umevimba na kushuka karibu na uti wa mgongo kwani mfumo wake wa upumuaji ulikuwa umeathirika. Vipimo hivyo vilikuwa vimepelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kubaini endapo kulikuwa na sumu au kitu kingine katika mwili wake.

Hata hivyo, walijiridhisha kwamba mtikisiko huo wa ubongo haukuwa umetokea katika sehemu ya nyuma ya ubongo (cerebrum) kwani ingetokea hivyo asingeweza kuinuka tena, kwa kuwa hali hiyo huua haraka. Kingine kilichogunduliwa ni mapigo ya moyo wake na joto la mwili vilikuwa katika hali ya kukatisha tamaa kabisa, kwa kifupi, daktari bingwa mmoja alisema kuwa “the patient is basically dead” akimaanisha kuwa kimsingi mgonjwa alikuwa amekufa.

Hicho ndicho kilichowafanya Elli na Jengo waonekane kukata tamaa wakiamini kuwa Sammy alikuwa katika hali ambayo ni hatua moja tu kutoka kati yake na kifo, kwani ndicho kilichoonekana mbele ya wale madaktari bingwa.

Kipindi chote Elli alikuwa anajiuliza maswali yasiyo na majibu kuhusu watu waliomshambulia Sammy na hata Joyce. Je, shida yao kubwa ilikuwa nini? Kilichomtokea Sammy kilimaanisha kuwa huenda alikuwa tishio kwa watu fulani, je, ni watu gani hao? Je, kulikuwa na uhusiano wowote kati ya mashambulizi hayo na kusimamishwa kwake kazini?

“Daktari, unadhani upo uwezekano wa Sammy kuinuka tena na kuendelea na maisha yake ya kawaida?” Elli alikuwa amemuuliza daktari bingwa mmoja hapo awali wakati walipoelezwa kuhusu matokeo ya uchunguzi wa awali.

“Hilo linawezekana, tumuombe Mungu.” lilikuwa jibu fupi la daktari huyo ambaye hakutaka kuelezea kiundani zaidi kwa kuwa hakuwa msemaji.

* * * * *

Tunu alipotua nje ya ukuta wa Hospitali ya Amana alitembea haraka haraka akipita chini ya miti mikubwa ya kivuli kando kando ya ule ukuta hadi kwenye vibanda vya wasusi wa Kimasai, alipotaka kuvuka barabara ya Uhuru ili kuelekea upande wa pili alianza kusikia vishindo hafifu vya watu waliokuwa wakija nyuma yake, alipogeuka nyuma kutazama akawaona wanaume wawili wakitimua mbio kumfuata.

Hakuhitaji kueleweshwa kuwa wale watu walikuwa wakimfuata yeye kwa lengo la kumdhuru kwani alikwisha wafahamu ni watu gani na walikuwa na dhamira gani. Bila ya kupoteza muda akaanza kutimua mbio na kuvuka barabara ya Uhuru kisha akaingia katika mtaa wa Kigoma.

Wale wanaume waliongeza mwendo na kuvuka barabara ya Uhuru lakini tayari Tunu alikwisha ufikia mtaa wa Moshi na kuufuata ule mtaa akienda kasi zaidi. Wale watu walikuwa wameishtukia dhamira yake ya kutaka kuwapotea hivyo nao waliongeza mbio kumkaribia na walikuwa na kasi sana. Tunu hakutaka kuwapa nafasi hiyo wakati wao wakiufikia mtaa wa Moshi Tunu alikuwa anaelekea mwishoni mwa mtaa ule, katika mtaa mwingine wenye msongamano mkubwa wa watu, wa Utete.

Mtaa wa utete ulikuwa na wafanyabiashara ndogo wengi waliopanga bidhaa zao chini, Tunu akajichanganya na watu katika namna ya kuwapotezea wale watu waliokuwa wakimfukuza. Akautumia mwanya huo wa kujichanganya kwenye kundi lile la watu na kupotea akishika uelekeo wa upande wa kulia. Alipofika kwenye makutano ya mitaa ya Utete na Nzasa akaingia kushoto kuufuata mtaa wa Nzasa, akizidi kujichanganya kwenye umati wa watu.

Itaendelea...

NB: Litro 👩
 
Taxi - (132)

Hakujua uelekeo ule ungemfikisha wapi ila alichokuwa amepanga ni kutoweka haraka eneo lile. Wakati akiharakisha kutoweka eneo lile kichwa chake kilikuwa kimetawaliwa na mchanganyiko wa mawazo. Moyo wake ulikuwa ukienda mbio sana. Alizidi kujichanganya na watu wengine na mbele kidogo akakutana na mtaa mwingine wa Morogoro uliokatisha mbele yake.

Kabla ya kujua afuate uelekeo wa upande gani; kulia au kushoto akakumbuka kutazama nyuma yake na hapo moyo wake ukapiga kite kwa nguvu. Alimwona mtu mmoja tu, mwanamume aliyekuwa amevaa suti nyeusi, kofia kubwa nyeusi ya pama na miwani myeusi ya jua akimfuatilia kwa nyuma.

Japokuwa kulikuwa na msongamano mkubwa wa watu katika eneo lile la soko lakini uzoefu wa mbinu za kijasusi ulimsaidia Tunu kugundua kuwa yule mtu alikuwa akimfuatilia yeye. Hata hivyo, kuna kitu kilianza kumchanganya, alijiuliza yule mtu alitokea wapi kwani hakuwa mmoja wa wale wawili waliokuwa wakimfuatilia tangu mwanzo.

Tunu aliamua kushika uelekeo wa upande wa kulia akiufuata mtaa wa Morogoro huku mkono wake ukiwa tayari umezama mafichoni kuipapasa bastola yake ya kijasusi. Kwa kweli alikuwa ameanza kuchoshwa sana na hali ya kufuatiliwa, hivyo alipanga kufanya shambulizi la kujihami na la kushtukiza kwa kugeuka na kumshindilia risasi za kutosha mtu yule bila kujali macho ya watu waliokuwa eneo lile kisha angepotea haraka toka eneo lile.

Aligeuka tena nyuma kumtazama yule mtu aliyekuwa akimfuatilia huku akiwa tayari amekwisha jiandaa kumfanyia shambulizi la kushtukiza lakini hakumwona! Akashangaa kidogo lakini mara akawaona tena wale wanaume wawili waliokuwa wakimfuata tangu mwanzo toka kule hospitali. Sasa walikuwa wakitimua mbio kumfuata. Tunu hakutaka kuanza kutimua mbio kwani kwa kufanya hivyo angeweza kuyavuta macho ya watu waliokuwa eneo lile, hivyo aliongeza mwendo huku akipanga namna ya kuwafanyia shambulizi la kushtukiza.

Aliufikia mtaa wa Pangani na kabla hajajua afanye nini au aelekee upande upi alimwona mwendesha bodaboda mmoja aliyekuwa anapita pale akitokea katika msikiti wa Irshaad Salafy na kuelekea upande wa Kariakoo. Tunu alikimbia kisha akarukia juu ya ile bodaboda huku akimtaka yule mwendesha bodaboda amkimbize haraka Machinga Complex, Kariakoo. Lilikuwa ni tukio la ghafla sana na wale watu waliokuwa wakimfukuza Tunu hawakuwa wamelitarajia kabisa.

Yule mwendesha bodaboda hakuwa amemtilia shaka yoyote Tunu ingawa alishangazwa na kitendo chake cha kurukia juu ya pikipiki wakati ikiwa katika mwendo. Pikipiki iliongeza mwendo na kwenda kasi kama alivyotaka Tunu, wakaufuata mtaa ule wa Pangani hadi walipoufikia mtaa wa Tabora, wakaingia upande wa kulia na safari ikaendelea. Wakati wakiingia katika mtaa wa Tabora Tunu aligeuza shingo yake kutazama nyuma, hakuwaona tena wale watu waliokuwa wakimfukuza nyuma yake.

Walipofika eneo la Machinga Complex Tunu alimlipa yule mtu wa bodaboda fedha aliyoitaja, akateremka na kujichanganya na watu wengine, kisha akachukua bodaboda nyingine akimtaka dereva wake ampeleke haraka mtaa wa Kongo. Vivyo hivyo alipofika mtaa wa Kongo na kushuka alichukua bodaboda nyingine hadi Mnazi Mmoja.

Aliendelea na mchezo huo wa kubadilisha pikipiki toka eneo moja hadi jingine na baadaye alichukua taxi katika eneo la Gerezani iliyompeleka Temeke kisha akachukua taxi nyingine, na akiwa ndani ya taxi simu yake ya mkononi ikaanza kuita. Tunu aliitazama na kuliona jina la Tom, hata hivyo aliikata na kumtumia ujumbe kuwa angempigia baadaye kwani hakuwa sehemu nzuri. Tom alimsisitiza kutoacha kumpigia kwani ilikuwa muhimu.

Saa yake ya mkononi ilimwonesha kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa kumi na nusu wakati alipokuwa anasimama mbele ya geti kubwa jeusi la nyumba ya kifahari ya Elli katika eneo la Kurasini, huku akiiacha ile taxi ikitoweka nyuma yake. Kwa kiasi fulani alikuwa amechanganyikiwa kutokana na kuona kuwa harakati zake za upelelezi ziliingia dosari baada ya lile shambulizi la bomu nyumbani kwa Sammy.

Alibonyeza kitufe cha kengele kilichokuwa kando ya lile geti na kushangaa kuona kulikuwa na ulinzi tofauti na alivyokuwa ameacha alipokuja mwanzoni. Geti dogo kando ya lile geti kubwa jeusi likafunguliwa, mlinzi mmoja aliyekuwa wamevaa sare maalumu za kampuni binafsi ya ulinzi na mkononi akiwa ameshika bunduki akachungulia nje na kumuona Tunu.

Alimtazama kwa makini kwa kumkazia macho. Tunu alimsalimia kisha akajieleza kuwa yeye ni rafiki wa familia ya Elli na alifika hapo kuonana na Victoria. Baada ya maswali mawili matatu hatimaye Victoria aliulizwa na kuwataka wale walinzi wamruhusu Tunu aingie.

Tunu aliruhusiwa kuingia ndani ya ule uzio alikowakuta walinzi wengine wawili. Akapokelelwa na Victoria aliyemshangaa baada ya kuona akiwa hana gari. Tunu alimwabia kuwa alilazimika kuliacha kule kwenye mgahawa wa Elli’s kwa sababu za kiusalama, wakaongozana na kuingia sebuleni alikomkuta Winifrida akiwa amejikuyata kwa huzuni huku akilia kilio cha kwikwi. Winifrida alipomwona Tunu akaanza kulia kwa uchungu uchungu mkubwa na kwa sauti ya juu, mwili wote ulikuwa unamtetemeka.

“Winnie!” Tunu aliita huku akimshika Winifrida mikono, akamwinua na kumkumbatia lakini miguu ya Tunu haikuwa na nguvu hata za kusimama. Tunu akamketisha kwenye sofa huku akiketi kando yake na kuanza kumpetipeti mgongoni katika hali ya kumfariji. Tunu alikuwa amepata taarifa za shambulizi lililomlaza kitandani kaka yake Sammy.

Shughuli bado pevu na mambo ni 🔥🔥🔥. Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua...

NB: Litro 👩
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom