Taxi (100)
Tunu aliviringika na kutambaa kama nyoka akihama kutoka sofa lile dogo na kwenda kwenye sofa kubwa. Akajilaza kimya akijaribu kusikilizia lakini akahisi chuma kikielekezwa kichwani kwake, moja kwa moja akatambua kuwa ulikuwa ni mtutu wa bastola na aliyeshika bastola hiyo alikuwa hatua moja tu toka alipolala. Mwili wake ukaingiwa na baridi.
Tunu hakutikisika wala kuinua mikono yake iliyoshika bastola. Alijua wazi kuwa alikuwa amepatikana. Hakuwa na ujanja na wala hakutakiwa kufanya lolote lile kwa pupa isipokuwa kuutii kila atakachoambiwa na mtu yule.
“Weka bastola zako chini na uinuke taratibu,” sauti ya ukakamavu ya yule mtu ilimwamrisha Tunu. Taratibu akaziweka chini bastola na kusimama akiwa amenyoosha mikono yake juu.
Alihisi kama ameona mzimu, alijikuta akitazamana na mtutu wa bastola aina ya
FNX 45 Tactical yenye kiwambo cha kuzuia sauti. Bastola ile ilikuwa imeshikwa na mwanamume mfupi mwenye umbo lililojengeka kwa misuli kutokana na ratiba nzuri ya mazoezi. Mwanamume yule alikuwa amevaa fulana nyekundu iliyombana na kulionesha vyema umbo lake lililojengeka kwa misuli, suruali ya bluu ya jeans na miguuni alivaa raba nyeusi.
Tunu alimtazama kwa wasiwasi. Macho ya yule mwanamume yalikuwa na dalili zote za ukatili, uwendawazimu na unyama uliokubuhu.
“Uledi!” Tunu alimaka kwa mshangao. Alikuwa akimfahamu vyema Uledi Mkama tangu alipokutana naye katika ofisi ya Mr. Oduya wakati huo yeye Tunu akifanya kazi hapo. Alifahamu kuwa Uledi alikuwa mmoja wa vijana wawili waliokuwa wakitumwa kufanya kazi maalumu na za siri za Mr. Oduya, yeye na Dulla Mcomoro. Alikumbuka kuwa ni hawa wawili wakishirikiana na Spoiler waliohusika kwenye mauaji ya Jaji Lutego.
“Uledi!” Tunu aliita katika namna ya kutaka kumzubaisha lakini Uledi hakutaka maongezi yoyote na Tunu, yeye alidhamiria kuua na kupeleka kichwa kama alivyoagizwa na Mr. Oduya.
Alianza kuvuta ndimi ya bastola, Tunu akafumba macho kwani alijua kile ambacho kingetokea na hakutaka kuona. Mara ukasikika mlio mkubwa wa risasi kutoka kwenye bastola isiyo na kiwambo cha kuzuia sauti, damu zikamrukia Tunu ambaye alianguka sakafuni huku akihisi moyo wake ulikuwa umepoteza mapigo yake, kisha akatulia kama mfu akiwa hajui iwapo alikuwa amekufa au alikuwa ndotoni.
“
Sister! Sister!” Tunu akasikia sauti ya mwanamume ambayo haikuwa ngeni masikioni mwake, alihisi kuitambua vyema. Akajiuliza ameisikia wapi?
“
Sister... ni mimi dereva wako. Inuka tuondoke haraka kuna wenzao wataingia hapa dakika yoyote kuanzia sasa,” ile sauti ilisema tena kwa wasiwasi. Sasa aliikumba vyema. Ni kweli ilikuwa ni sauti ya yule dereva wa teksi aliyoikodi. Hata hivyo hakujitokeza kwa kuogopa kuwa huenda ulikuwa ni mtego.
Tunu aliinua uso wake kwa wasiwasi na kumwona yule dereva akiwa ameshika bastola akiangalia kule kwenye mlango mkubwa wa kuingilia sebuleni kwa wasiwasi na kuanza kutoka haraka. Tunu hakutaka kuwa mbishi, akainuka na kuokota haraka bastola yake na mkoba wake, akautupia jicho mwili wa Uledi na kuona jinsi kichwa chake kilivyokuwa kimefumuliwa kwa risasi, hakutaka kuzubaa akatoka kuanza kumfuata nyuma yule dereva.
Walielekea nyuma ya ile nyumba na wakati huo huo ukasikika muungurumo wa gari lililokuwa linaikaribia ile nyumba na kukomea mbele ya geti kubwa la nyumba ile. Hawakusubiri, wakarukia matawi ya mti yaliyokuwa yameinamia mle ndani na kupanda haraka kisha wakajirusha na kuangukia nje ya ukuta wa ile nyumba. Yule dereva akaanza kutimua mbio kuelekea bondeni. Tunu akamfuata. Baada ya mwendo mfupi wakaanza kuambaa na ule Mto Msimbazi kabla hawajaanza tena kupandisha kama wanarudi juu lakini wakiwa mbali na eneo la ile nyumba waliyotoka.
“
Tunu, are you okay?” yule dereva alimuuliza Tunu wakati wakikimbia. Tunu akashtuka sana kusikia yule dereva akimwita kwa jina lake, muda huo walikuwa wanapita katika vichochoro vya nyumba za eneo lile.
“
I’m okay!” Tunu akamjibu yule dereva kwa ufupi huku akiwa katika tahadhari kubwa. Bastola amezishika mkononi tayari kwa lolote.
“Endelea kunifuata, gari nilikwenda kulificha sehemu huko mbele ili wasinishtukie.” yule dereva alisema huku akiendelea kukimbia.
Pamoja na kuendelea kumfuata yule dereva lakini Tunu bado alikuwa katika mawazo kumuhusu yule dereva. Alikuwa anajiuliza yule nin nani hasa? Kwa nini amemwokoa toka kwa wale watu wakati inasemekana yeye pia ni mmoja wao? Je, katumwa na nani aje amwokoe? Au yeye pia ni
undercover? Tunu alijiambia kuwa alikwisha hisi tangu mwanzo kuwa yule dereva hakuwa wa kawaida kama walivyo madereva wengine, alionekana mwelewa sana wa mambo na mwepesi wa kushika maelekezo.
Waliendelea kukimbia kwa kasi, yule dereva akiwa mbele na Tunu akiwa nyuma ingawa kwa upande fulani alianza kumwogopa sana. Jasho jingi lilikuwa linamtoka kwa kukimbia. Baada ya dakika kadhaa za kukimbia wakatokea kwenye kichochoro kimoja na kuikuta ile taxi ikiwa imeegeshwa hapo. Yule dereva akageuka kumtazama Tunu kwa macho makali.
“Pole sana, huo ndiyo uzalendo kwa nchi yako,” yule dereva alisema lakini Tunu hakumjibu. Alimtazama usoni kwa makini.
Mchezo unazidi kunoga, wamejitokeza wengi na sasa kuna huyu dereva wa taxi! Kuna nini ndani ya Taxi? Endelea kufuatilia hadi mwisho...
Thisi is for you Shunie