Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Hahaa, wapo, utakutana nao huko mbele. Lakini wewe huna sura ngumu, hebu geuka nione...
Daaah toka tumeanza ni wadada wazuri wazuri tu, nkasema hakuna mwenye sura ya baba,yangu bwana hata Marehem Remmy hanifikii
 
Wakuu, ni siku nyingine tena... baada ya mlinzi kuonesha kuwashtukia akina Spoiler. Je, watafanikiwa kuingia ndani na kupata taarifa kuhusu mmiliki wa sasa wa gari wanalolitafuta? Vipi kuhusu Sammy na mkewe Joyce, moto wao utapoa au ndiyo mwanzo wa mwisho wa ndoa yao iliyodumu miaka minane? Na Tunu je, nini mission yake? Karibuni tuendelee...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple
 
Taxi - (77)

ILIPOISHIA

“Hii ni nyumba ya Dk. Mloka lakini mbona yeye amefariki dunia miaka miwili iliyopita!” yule mlinzi alisema huku akiwa bado anawatazama kwa makini.

“Kwa hiyo hapa anaishi nani kwa sasa?” Spoiler akamwahi kabla hajafanya chochote.

“Anaishi mkewe, Dk. Marina na watoto wake.”

“Hivi sasa kuna nani ndani?” Spoiler aliuliza huku akijaribu kuchungulia ndani kupitia upenyo mdogo ulio wazi wa mlango wa lile geti.

“Kwani ninyi mnamtaka nani hasa?” yule mlinzi akawauliza baada ya kufikiria kwa kitambo huku akionesha wasiwasi.

“Basi tunaomba tuonane na mama, mke wa Dk. Mloka, maana sisi ni jamaa zake marehemu Dk. Mloka,” Spoiler alisema huku akisogea karibu na yule mlinzi.

“Jamaa zake Dk. Mloka halafu hamjui kama alishakufa! Itabidi msubiri hapa ili nikaulize ndani kwanza, maana siwafahamu na wala sikutaarifiwa kama kuna wageni wa aina yenu watakuja hapa leo!” yule mlinzi alisema huku akijiandaa kuufunga ule mlango wa geti.

SASA ENDELEA...

Spoiler na Dulla Mcomoro wakaihisi hatari iliyotaka kutokea, bila kusubiri na kwa kasi ya umeme Spoiler akampiga pigo moja la haraka yule mlinzi kabla hajafunga ule mlango wa geti, pigo hilo lilimpeleka chini, kisha akaruka bila kishindo kama paka na kumkaba kabali matata pale chini iliyomfanya apoteze fahamu.

Wakati hayo yakitendeka Dulla Mcomoro alikuwa makini kuchunguza eneo lile kama kulikuwa na mtu yeyote aliyeona tukio lile, aliwaona watu wachache wakiwa na hamsini zao na hakuna aliyejishughulisha kuwatazama. Haraka akachungulia ndani lakini hakuona mtu mwingine yeyote.

“Shwari!” Dulla Mcomoro alimwambia Spoiler ambaye muda huo alikuwa amemvuta haraka yule mlinzi na kumficha kwenye maua, wakasaidiana kumwingiza kwenye kibanda maalumu cha mlinzi kilichojengwa kando ya lile geti kubwa la nyumba hiyo kisha wakaufunga ule mlango wa geti kwa ndani kumzuia mtu aliyeko nje asiweze kuingia ndani.

Dula Mcomoro alikuwa makini kuhakikisha hakuna aliyeona tukio lile wakati Spoiler akimpekua haraka haraka yule mlinzi na kuchukua simu yake ya mkononi kisha wakamfungia kwenye kile kibanda na kuelekea katika mlango mkubwa wa barazani wa kuingilia sebuleni.

Ilikuwa ni nyumba kubwa ya kisasa iliyokuwa na madirisha makubwa ya vioo na baraza kubwa mbele yake. Nje ya nyumba ile upande wa kulia kulikuwa na banda la wazi la kuegeshea magari na kulikuwa na gari moja la kifahari aina ya Toyota Landcruiser GX V8 jeusi lililokuwa na milango sita.

Sehemu nyingine ya mandhari ya nyumba ile ilizungukwa na miti miwili mirefu na mikubwa ya kivuli ambayo matawi yake yalikuwa makubwa na yalitengeneza vichaka vilivyosababisha kivuli kizito na kiza wakati wa usiku.

Sehemu ya mbele ya ile nyumba ilikuwa imezungukwa na bustani nzuri ya maua ya kupendeza yaliyotoa harufu nzuri na katikati ya bustani ile kulitengenezwa njia nzuri ya kutembea kwa miguu kwa vitofali vidogo vilivyokuwa vinavutia.

Wakiwa hapo barazani Spoiler akagonga mlango lakini hakuna mtu aliyejibu wala kufungua mlango. Akagonga tena, safari hii aligonga kwa nguvu, wakasikia nyayo za mtu zikija na mara mlango ukafunguliwa, msichana mmoja aliyeonekana wazi kuwa ni mfanyakazi za ndani akachungulia nje.

Yule msichana alikuwa mfupi na maji ya kunde, alikuwa na mwili mkubwa kiasi na kifua kipana kilichobeba maziwa makubwa ya mviringo, sura yake ilikuwa ya kitoto tofauti na mwili wake na alionekana hakuzidi miaka ishirini na tano.

Alikuwa na nywele ndefu alizozisuka mtindo wa twende kilioni, alivaa dela refu na apron nyeupe juu yake, ikionesha kuwa kabla mlango haujagongwa alikuwa jikoni akiandaa maakuli. Alisimama akiwatazama akina Spoiler mara moja na kutupa macho yake kutazama getini, hakumwona mlinzi na kuonekana kushtuka kidogo, akawasalimu akina Spoiler kwa woga.

“Mama yupo?” Spoiler alimtupia swali baada ya kujibu salamu yake.

“Yuko chumbani kwake amelala, anaumwa,” yule msichana alijibu baada ya kufikiria kwa sekunde kadhaa huku akiendelea kuwatazama akina Spoiler kwa wasiwasi.

“Nani mwingine yupo ndani?” Spoiler aliuliza kwa sauti tulivu huku akimtazama bila kupepesa macho.

“Yupo peke yake,” yule msichana alijibu huku uso wake ukishindwa kuficha wasiwasi aliokuwa nao. Aliendelea kuwatazama Spoiler na Dulla Mcomoro kwa zamu.

“Kwani humu ndani mnaishi watu wangapi?” Spoiler alimtandika swali jingine na kumfanya aachie mguno wa mshangao uliosikika kwa wote.

“Kwani nyiye ni kina nani?” yule msichana aliuliza kwa mshangao huku uso wake ukishindwa kuficha mshangao wake.

“Jibu swali unaloulizwa, we msichana,” Dulla Mcomoro alisema kwa ukali kidogo huku akifunua shati lake kumwonesha bastola yake iliyofichwa kiunoni.

Yule msichana aliiona ile bastola na kuingiwa na hofu, alimeza funda kubwa la mate kutowesha koo lake lililokauka ghafla na kushusha pumzi.

“Tunaishi wanne…” yule msichana alijibu kwa hofu.

“Watu wengine wamekwenda wapi?”

“Kaka Frank na mkewe wametoka muda si mrefu, wameenda kazini.”

“Okay, tupeleke chumbani kwa mama, tunahitaji kuongea naye,” Spoiler alimwambia yule msichana kwa sauti tulivu lakini iliyoamuru huku akimkazia macho yaliyowaka kwa ghadhabu.

Yule msichana alishusha pumzi, akaonekana kama aliyekuwa akijishauri, lakini alipokumbuka kuhusu ile bastola kiunino kwa Dulla Mcomoro akaogopa sana na kuwaongoza ndani. Waliingia na kuivuka sebule kubwa yenye samani zote muhimu za kisasa, ilikuwa imepambwa kwa seti mbili za makochi ya sofa ya kifahari yaliyokuwa yamepangwa katika mtindo wa kuizunguka.

Pia ilikuwa na zulia zuri la rangi nyekundu sakafuni na katikati kulikuwa na meza nzuri ya kioo iliyokuwa na umbo la yai ikizungukwa na stuli ndogo nne za sofa. Spoiler aliitupia jicho la haraka ile subule akijaribu kuyasoma mazingira ya nyumba ile.

Walielekea upande wa kushoto wakaifuata korido moja fupi na pana iliyokuwa na milango mitatu, milango miwili ilikuwa upande wa kushoto na mmoja ulikuwa upande kulia, mwisho kabisa wa ile korido. Yule msichana akawaongoza hadi kwenye ule mlango wa mwisho na kusimama mbele ya ule mlango huku akiwaangalia kwa hofu.

“Mlango wa chumba chake ni huu hapa,” yule msichana alisema kwa sauti ya kutetemeka huku akiwaonesha mlango.

“We Shamila, unaongea na kina nani?” sauti kali ya mwanamke ilisikika ikitokea ndani.

Yule msichana alishtuka, akawafanyia ishara akina Spoiler kwamba sauti ile waliyoisikia ndiyo sauti ya mama.

“Mama, ni wageni wako wanataka kukuona,” yule msichana alisema kwa wasiwasi huku akijikunyata.

“Nani aliyekuruhusu uwalete huku, kama ni wageni wangu kwa nini wasinisubiri sebuleni? Sauti ya Dk. Marina iliuliza kwa ukali toka chumbani.

Inaendelea...
 
Taxi - (78)

Kabla Shamila hajajua ajibu nini Spoiler alikishika kitasa cha mlango na kukinyonga huku akiusukuma mlango kwa nguvu, kumbe haukuwa umefungwa na ufunguo. Ulifunguka na Spoiler akajitoma ndani haraka huku akimwashiria Dulla Mcomoro amfuate.

Dulla Mcomoro alimshika Shamila na kumtanguliza, wakaingia ndani. Kilikuwa chumba kikubwa na chenye nafasi ya kutosha kikiwa na madirisha mawili mapana ya vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia mepesi marefu.

Katikati ya chumba kulikuwa na kitanda kikubwa cha samadari cha futi sita kwa sita chenye nakshi nzuri za kupendeza, upande wa kulia wa chumba kulikuwa na meza kubwa ya vipodozi yenye vioo viwili virefu vya kujitizama. Upande wa kushoto kulikuwa na mlango wa kuingia katika chumba kidogo cha maliwato.

Dk. Marina alishtushwa sana kwa kitendo cha kuwaona wanaume wawili asiowafahamu wakiingia chumbani kwake bila ruhusa, aliinuka haraka kutoka pale kitandani alipolala huku akitaka kupiga kelele kwa hofu lakini Spoiler alimwahi, akakitoa kisu chake na kumwonesha akiwa amemkazia macho ya ghadhabu.

Dk. Marina, daktari bingwa wa watoto wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, iliyopo eneo la Upanga Magharibi jijini Dar es Salaam, alikuwa mwanamke mwenye umri wa miaka arobaini na nane, alikuwa mrefu wa wastani mwenye mwili mkubwa na rangi ya maji ya kunde. Alipokiona kisu kikubwa cha springi kikimetameta mbele yake akanywea.

“Mnafanya nini ndani kwangu? Kwanza ninyi ni akina?” Dk. Marina aliuliza kwa hofu huku akijikunyata pale kitandani na kuwatazama akina Spoiler na Dulla Mcomoro kwa zamu.

“Mama, hatuko hapa kwa ajili ya kukudhuru, tunahitaji taarifa fulani toka kwako kisha tutaondoka zetu na kuwaacha salama,” Spoiler alisema kwa sauti tulivu huku akimkazia macho.

Who are you guys?” Dk. Marina aliuliza na kushusha pumzi.

“Huna haja ya kutufahamu, sisi ni watu wazuri sana na tumekuja hapa kuzungumza nawe mambo kadhaa, ila kama utataka kuleta ujanja ujanja sisi ni wabaya sana hata shetani anatuogopa, we can destroy you in a second,” Spoiler alisema kwa sauti ya kufoka kidogo.

“Taarifa gani mnaitaka toka kwangu?” Dk. Marina aliuliza tena huku hofu ikiwa imemtawala.

Spoiler alimgeukia Dulla Mcomoro aliyekuwa bado kamshika Shamila na kumpa ishara ya kumfungia bafuni. Dulla Mcomoro alimkokota Shamila akampeleka katika bafu lililokuwa ndani ya chumba cha Dk. Marina, akamfungia huko baada ya kumpekua ili kuhakikisha hakuwa na simu wala kifaa chochote cha mawasiliano.

“Tunazo taarifa kuwa miaka mitatu iliyopita, mwezi Oktoba mumeo aliuziwa gari aina ya Cadillac DeVille la muundo wa kizamani, tupo hapa kwa kuwa tunalitaka gari hilo,” Spoiler alisema huku akiwa makini kumtazama Dk. Marina.

“Cadillac DeVille?” Dk. Marina alishtuka kidogo na kumtazama Spoiler kwa mshangao, kisha akaendelea, “Ni kweli tuliwahi kununua gari la aina hiyo miaka mitatu iliyopita lakini kwa sasa hatunalo, tumeliuza.”

“Mmeliuza lini na nani aliyelinunua?”

“Limeuzwa mwezi uliopita ila mimi simjui aliyelinunua kwani ni Frank ndiye aliyeliuza…” Dk. Marina alijaribu kujitetea.

“Frank ndiyo nani?”

“Mwanangu mkubwa, yeye anafanya biashara ya kuuza magari.”

“Tutampataje?”

“Nani?”

“Frank. Tunahitaji kujua ni nani aliyelinunua hilo gari.”

“Alikuja hapa muda mfupi uliopita, ameondoka na mkewe kwenda ofisini kwao, show room ya Magomeni Mikumi,” Dk. Marina alijibu huku akijiuliza wale watu ni kina nani waliomvamia kwa sababu ya kuulizia gari la kizamani!

“Magomeni Mikumi ipi?”

"Barabara ya Kawawa, karibu na kituo cha daladala cha Magomeni Mikumi kama unaelekea Ilala,” Dk. Marina alisema na kuwatajia jina la yadi hiyo ya kuuza magari.

“Mmeliuza mwezi uliopita, eeh! Kipindi chote lilikuwa wapi?” Spoiler aliuliza baada ya kufikiria kwa kitambo.

Dk. Marina alitaka kusema akasita na kumeza funda kubwa la mate kutowesha koo lake lililokauka, kisha akashusha pumzi. “Kwani shida yenu ni nini hasa, mbona sielewi?”

Okay, nipe simu yako,” Spoiler alimwambia Dk. Marina huku akinyoosha mkono wake.

“Mmetaka taarifa nimewapa lakini bado mnataka na simu yangu, ya nini?” Dk. Marina alisema kwa huzuni.

“We mama, umeambiwa toa simu yako, hatuhitaji maswali,” Dulla Mcomoro alisema kwa ukali huku kinyanyua shati lake kumwonesha bastola iliyotuama kiunoni kwake na kumfanya Dk. Marina kuingiwa woga kwa namna Dulla Mcomoro alivyokuwa anamwangalia, akanyoosha mkono wake kumpatia simu Spoiler.

Spoiler aliipokea ile simu na kuizima kisha akatoa betri. Alimpa ishara Dulla Mcomoro kumleta Shamila kutoka bafuni kisha wakawafunga wote wawili kwa kamba na kuwaziba mdomo yao ili wasiweze kupiga kelele.

“Utatusamehe, mama, hatuna namna nyingine ya kufanya, mtabaki hivi kwa muda, tukishamalizana na Frank atakuja kuwafungulia,” Spoiler alimwambia Dk. Marina, wakatoka na kuufunga mlango wa chumba kwa funguo.

Walipofika nje waliingia ndani ya gari lao, wakaondoka kuelekea Magomeni Mikumi.

* * * * *

Saa kumi na mbili jioni jua lilikuwa limekwisha anza kuzama jijini Dar es Salaam na kwa mbali kiza kikianza kuchukua nafasi yake, anga la rangi nyekundu lilikuwa likinywea katika ukungu upande wa magharibi.

Tunu alishuka kutoka kwenye teksi, akatazama kushoto na kulia kwake halafu akavuka barabara akielekea upande ule wa magharibi, alipiga hatua taratibu kwa madaha kuelekea kwenye jengo moja lenye kuta safi za vioo na juu yake kukiwa na bango kubwa jeupe lenye maandishi makubwa mekundu yakisomeka MILAN CLUB & SPA. Chini ya bango lile kulikuwa na maandishi madogo yanayosomeka ‘Just enjoy every moment.’

Inaendelea...
 
Taxi - (79)

Tunu alikuwa amevalia gauni zuri la kitenge cha wax lililoshonwa kwa mtindo wa ‘Ankara midi tube dress’ likiishia juu kidogo ya magoti yake, likaushika vyema mwili wake na kulichora umbo lake maridhawa. Nywele zake fupi na laini alizozitia rangi ya dhahabu alikuwa amezichana vizuri na macho yake aliyafunika kwa miwani mikubwa ya jua. Miguuni alivaa viatu vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio na begani alining’iniza mkoba mzuri wa kike.

Katika eneo lile la MILAN CLUB & SPA kulikuwa na magari machache yaliyokuwa yameegeshwa kwenye eneo la maegesho ya magari na watu wachache waliokuwa wamesimama nje ya Club ile wakiendelea na mazungumzo yao. Watu wale waligeuza shingo zao kumtazama Tunu kwa matamanio na wengine walimsemesha wakati alipokuwa akikatiza eneo lile kuelekea kwenye mlango mkubwa wa mbele wa kuingilia ndani ya ile Club, hata hivyo hakuwatilia maanani badala yake aliendelea na hamsini zake.

Wakati akiukaribia ule mlango mkubwa wa mbele wa Club ile alizamisha mkono wake ndani ya mkoba wake na kutoa simu yake ya kisasa aina ya Iphone X iliyokuwa inaita. Akapokea na kuiweka kwenye sikio lake, “Hello, yeah ndiyo kwanza nafika… kwani wewe uko wapi?” Akasikiliza kidogo na kubetua kichwa chake, “Okay!”

Alikata simu kisha akairudisha ndani ya mkoba wake na kuzama ndani ya Club bila kujishughulisha na wanaume walioendelea kumtazama kwa matamanio na wengine wakimwita, kwani hali kama ile alikwishaizoea. Alipoingia ndani alikwenda moja kwa moja kukaa mwishoni kabisa mwa ukumbi wa baa.

Punde kidogo akatokea mwanamume mmoja mfupi kiumbo lakini mkakamavu akiwa na mwili uliojengeka kwa mazoezi na sura yake ilionesha unyenyekevu mkubwa tofauti na tabia yake halisi ya ubabe, unyama na wendawazimu. Alikuwa amevalia sweta jepesi lililoungana na kofia iliyofunika kichwa chake, suruali ya kadeti na buti ngumu nyeusi miguuni na usoni alivaa miwani myeusi ya jua.

Mwanamume huyo alitazama huku na kule kabla hajaelekea sehemu aliyoketi Tunu. Kabla hawajasalimiana, kila mtu akatazama kushoto na kulia kwake kabla ya kuendelea na mengine.

“Umenishtua sana uliponipigia simu kuniambia unanihitaji haraka,” yule mwanamume alisema na kushusha pumzi. Uso wake ulionesha wasiwasi kidogo.

“Kinachokushtua nini! Una soo gani hadi ushtuke baada ya kuona simu yangu?” Tunu alimuuliza yule mwanamume huku akiachia kicheko hafifu. Kabla yule mwanamume hajajibu, alitazama tena huku na kule kana kwamba alikuwa hapaamini mahala pale.

“Usihofu, Bob,” Tunu alimwambia kwa sauti ya chini. “Hapa hamna kamera, pia unadili na mtu makini kuliko maelezo.”

Yule mwanamume alishusha pumzi za ahueni lakini kabla hajasema lolote mhudumu wa Club ile akafika na kuwasalimia kwa tabasamu bashasha la kibiashara kisha akawataka radhi kwa kuchelewa kuwahudumia.

Yule mhudumu alikuwa msichana mwenye umbo kubwa lililofichwa ndani ya sare na miguu minene. Nywele zake ndefu zilikuwa zimefunikwa na kofia maalumu ya Club ili kuzuia kuharibu vinavyotiwa mdomoni.

“Naomba tuletee chupa kubwa ya Dompo na glasi mbili,” Tunu aliagiza na kutoa fedha, akampa yule mhudumu ambaye alipokea na kuondoka haraka.

Alipotoka wakaendelea kuteta wakipanga hiki na kile, baada ya dakika chache yule mhudumu alirudi na kuweka ile chupa ya dompo na bilauri mbili kwenye meza, alipotaka kurudisha chenji Tunu akamwambia abaki nayo. Alishukuru kisha akaenda zake huku akitabasamu.

Tunu na yule mwanamume wakaendelea kuteta huku sasa wakiwa wanalainisha makoo yao kwa kinywaji kile, mzao wa mzabibu kutoka Dodoma. Baada ya dakika ishirini tangu walipokutana pale yule mwanamume aliinuka, akajiondokea taratibu akimwacha Tunu bado kaketi ananywa kinywaji chake taratibu.

Tunu alikuwa ametulia tuli akiendela kunywa taratibu huku akitafakari kuhusu kazi iliyo mbele yake kwa kitambo kirefu kidogo, muda wote alizungusha macho yake kutazama huku na kule kulichunguza eneo lile. Alipomaliza kinywaji chake aliitupia jicho saa yake ya mkononi na kushtuka, ilionesha kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa mbili ya usiku.

Alichukua simu yake kutoka kwenye mkoba wake na kuandika ujumbe mfupi kisha akautuma na kuinuka, akatoka nje ya jengo la MILAN CLUB & SPA, alisimama pale akishangaa kuona eneo lile kulikuwa na wasichana wengi waliokuwa wakirandaranda nje. Walikuwa wa kila sampuli: wembamba kwa vibonge, warefu kwa wafupi, wenye sura mbovu na warembo, wote walikuwa wamevalia mavazi yaliyowaacha nusu utupu.

Tunu alishusha pumzi, akaanza kupiga hatua taratibu kuelekea kando ya eneo lile sehemu kulipokuwa na maegesho ya teksi, mara akasita baada ya kumwona mwanamume mmoja mrefu aliyekuwa amemwegemeza msichana mmoja kibonge ukutani wakiongea. Yule msichana alikuwa na kiuno chembamba na makalio makubwa na alivaa sketi fupi sana iliyoacha sehemu kubwa ya mapaja yake wazi na juu alivaa kitopu chepesi kilichoacha wazi sehemu kubwa ya kifua, matiti na tumbo lake.

Yule mwanamume alizungusha macho yake kuangalia huku na huko kisha akamwinamia yule msichana kibonge na kunong’ona jambo kwenye sikio lake. Yule msichana alishtuka sana, akamwangalia yule mwanamume kwa mshangao mkubwa na kuachia tabasamu huku akijiziba mdomo wake kwa viganja kuzuia kicheko.

Yule mwanamume alimtazama yule msichana kwa tabasamu na kumkumbatia kwenye kiuno lakini akashtuka na kugeuka nyuma, alimwona Tunu akiwa amesimama akiwaangalia kwa makini. Alimwachia yule msichana akitaka kujificha lakini alikuwa amechelewa.

Tunu aliendelea kumtazama, tazama yake ilikuwa ya dharau akimshusha na kumpandisha kuanzia juu hadi chini na chini hadi juu, kisha akabinua midomo yake na kusonya. Yule mwanamume alimtazama Tunu huku uso wake ukipambwa na aibu, hata hivyo alilazimisha tabasamu.

Itaendelea...
 
Taxi - (80)

“Mambo, Tunu!” yule mwanamume alimsalimia Tunu huku akijichekesha. Tunu hakumjibu bali alimwangalia kwa makini kwa kitambo. “Kuna mtu namuulizia hapa, nimeambiwa siku hizi anafanya kazi hapa!” alisema bila kuulizwa.

“Malaya wa kiume!” Tunu alisema kwa dharau na kuachia msonyo, kisha alibana pua yake na kuyarudia maneno ya yule mwanamume, “Kuna mtu namuulizia hapa, nimeambiwa siku hizi anafanya kazi hapa!…” kisha aliachia pua yake, akatema mate chini na kutingisha kichwa chake kwa huzuni, “Bora hata nilivyokupiga chini.”

“Mimi Malaya! Haya wewe usiye malaya unatafuta nini hapa?” yule mwanamume aliuliza huku akimkodolea macho Tunu.

“Mimi sipo hapa kujiuza. Natafuta mwanamume bora kuliko wewe usiyejielewa.”

“Sasa ndiyo natambua kuwa nilifanya uamuzi sahihi kuachana na wewe. Kahaba mkubwa!” yule mwanamume alisema huku akisonya kwa dharau.

“Nyoo! Hayo ni maneno ya mkosaji!” Tunu alisema na kubinua midomo yake kwa dharau, “Eti ulifanya uamuzi sahihi kuachana na mimi! Uamuzi upi sahihi wakati ulikuwa unanibembeleza usiku na mchana nisikuache!”

Yule mwanamume alitaka kusema neno lakini hatia ikamkaba kooni, akabaki akimtumbulia macho Tunu bila kusema neno. Tunu aliachia kicheko cha dharau na kuanza kupiga hatua za madaha kuelekea kwenye maegesho ya teksi akimwacha yule mwanamume anashangaa.

Dereva mmoja wa teksi, kijana mwenye sura yenye bashasha zote za kirafiki akawahi kumfungulia mlango wa mbele wa teksi yake wakati alipokuwa mbioni kuyafikia yale maegesho ya teksi nje ya MILAN CLUB & SPA.

Hata hivyo, Tunu hakutaka kukaa mbele badala yake alizunguka na kufungua mlango wa nyuma wa teksi ile, akaingia ndani na kuketi. Yule dereva wa teksi kuona vile haraka akaufunga ule mlango aliomfungulia Tunu kisha haraka akazunguka na kufungua mlango wa dereva na kuingia.

“Nikupeleke wapi, bibie?” yule dereva alimuuliza Tunu huku akimtazama kwa macho ya matamanio.

“Leo nitaenda kwako,” Tunu alimwambia yule dereva huku akimtazama kwa tabasamu.

“Kwangu?” yule dereva alishtuka sana na kumkodolea macho Tunu kwa mshangao mkubwa kana kwamba alikuwa ameona kiumbe cha ajabu kutoka sayari ya mbali.

“Kwani haiwezekani kwenda kwako? Naona umeshtuka sana!” Tunu alisema huku akiachia kicheko hafifu.

“Nimeshangazwa maana mimi nina mke, tena ndoa yangu bado changa. Sitaki kuletewa songombingo na waifu!”

“Hahaa, nilikuwa nakutania mwaya! Naomba nipeleke ELLI’S,” Tunu alimwambia yule dereva wa teksi huku akijiegemeza kwenye siti.

Yule dereva wa teksi akamtazama kidogo Tunu na kutikisa kichwa chake katika namna ya kuashiria kuwa alikuwa amemwelewa. Aliwasha gari na muda uleule ile teksi ikaanza kuyaacha yale maegesho.

* * * * *

Saa moja na ushee usiku katika ofisi za Mr. Oduya zilizo ghorofa ya sita ya jengo lake la ghorofa kumi na mbili lililopo katika barabara ya Bagamoyo eneo la Kijitonyama jijini Dar es Salaam, Mr. Oduya alikuwa yupo ofisini kwake.

Alikuwa ameketi nyuma ya meza yake kubwa ya ofisini mwisho wa ofisi ile upande wa kuume akiwa katika uso wa kusawajika huku akiwa ameegemea kiti chake cha ofisi na kuweka miguu yake juu ya meza. Kama kawaida alikuwa amevalia suti nadhifu na viatu vya ngozi halisi ya mamba. Aliketi huku mche wa sigara ukiteketea taratibu kwenye pembe ya mdomo wake. Sura yake ilionesha wazi kuwa mambo hayakuwa salama kabisa.

Wakati huo Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa wanaingia baada ya mizunguko mingi ya hapa na pale ili kuhakikisha wanakamilisha kazi waliyotumwa kuifanya. Ukimya ulikuwa umetawala ndani ya ofisi ile ukawafanya Spoiler na Dulla Mcomoro watembee taratibu kama waliokuwa wananyata huku wakisikia sauti hafifu ya hatua zao wakati walipokuwa wakikatisha kuelekea kwenye viti ili kuketi.

Spoiler alikwenda moja kwa moja kwenye meza ya Mr. Oduya huku akimtazama kwa utulivu na kumkabidhi bahasha kubwa ya khaki aliyokuwa ameishika mkononi ikiwa na karatasi ndani yake. Mr. Oduya alinyoosha mkono wake kuipokea ile bahasha kisha akajiegemeza vizuri kwenye kiti chake cha ofisini.

Aliifungua na kutoa nyaraka za manunuzi ya gari aina ya Cadillac DeVille lililokuwa limenunuliwa na Sammy katika yadi ya kuuza magari ya Magomeni Mikumi. Mr. Oduya alizitazama kwa makini huku mche wa sigara ukiendelea kuteketea taratibu kwenye pembe ya mdomo wake na macho yake yakizipitia mstari kwa mstari zile nyaraka.

Kabla hata hajamaliza kusoma nyaraka zile moyo wake ukapoteza utulivu na kijasho chepesi kikaanza kumtoka sehemu mbalimbali za mwili wake.

“Samuel John Kambona!” alilitamka jina hilo kwa sauti ya chini kama aliyekuwa ananong’ona. Jina lilijiumba na kujirudia akilini kwake likiacha mwangwi. Alihisi kulisikia jina hilo mara kadhaa, si hivyo tu bali alimfahamu hata mmiliki wa jina lenyewe ambaye kwa mujibu wa nyaraka zile, ndiye mnunuzi wa gari lile.

Mr. Oduya alichukua simu yake na kutafuta namba za Dk. Masanja, meneja mkuu wa hoteli ya Udzungwa Beach Resort na kupiga ili kupata uhakika. Majibu aliyopewa yalimfanya ajihisi kukanganyikiwa, akili yake ilijaribu kukataa kabisa kukubaliana na taarifa ile na kile alichokishuhudia kwenye katika nyaraka zile za ununuzi wa gari.

Alijitahidi kuwa makini zaidi na akiishirikisha akili yake kikamilifu katika kumletea taarifa za kuaminika, kwani mambo yale hayakuwa yanamwingia kichwani kabisa! Ni vipi Sammy ameendelea kujitokeza katika harakati zake za kuusaka urais wa Tanzania na kugeuka kuwa kitisho?

Aliinua uso wake na kutazama juu akionekana kuwaza mbali. Wakati huo Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa kimya kabisa wakimtazama kwa wasiwasi. Akiwa katika hali ile mara hisia mbaya zikamjia na hapo mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda kasi isivyo kawaida, hasa alipowaza kuwa huwenda wapinzani wake kisiasa walikuwa na fununu fulani kuhusiana na lile gari na wangeweza kulitumia kummaliza.

Dah! Mambo yanazidi kunoga. Nini kitaendelea? Usikose kuwa nami kwenye safari hii ya kusisimua...
 
Sipati picha huko alipo Dr Malina Njelekela Kama ameshafunguliwa kamba au bado anakula msoto
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom