Taxi - (78)
Kabla Shamila hajajua ajibu nini Spoiler alikishika kitasa cha mlango na kukinyonga huku akiusukuma mlango kwa nguvu, kumbe haukuwa umefungwa na ufunguo. Ulifunguka na Spoiler akajitoma ndani haraka huku akimwashiria Dulla Mcomoro amfuate.
Dulla Mcomoro alimshika Shamila na kumtanguliza, wakaingia ndani. Kilikuwa chumba kikubwa na chenye nafasi ya kutosha kikiwa na madirisha mawili mapana ya vioo yaliyokuwa yamefunikwa kwa mapazia mepesi marefu.
Katikati ya chumba kulikuwa na kitanda kikubwa cha samadari cha futi sita kwa sita chenye nakshi nzuri za kupendeza, upande wa kulia wa chumba kulikuwa na meza kubwa ya vipodozi yenye vioo viwili virefu vya kujitizama. Upande wa kushoto kulikuwa na mlango wa kuingia katika chumba kidogo cha maliwato.
Dk. Marina alishtushwa sana kwa kitendo cha kuwaona wanaume wawili asiowafahamu wakiingia chumbani kwake bila ruhusa, aliinuka haraka kutoka pale kitandani alipolala huku akitaka kupiga kelele kwa hofu lakini Spoiler alimwahi, akakitoa kisu chake na kumwonesha akiwa amemkazia macho ya ghadhabu.
Dk. Marina, daktari bingwa wa watoto wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, iliyopo eneo la Upanga Magharibi jijini Dar es Salaam, alikuwa mwanamke mwenye umri wa miaka arobaini na nane, alikuwa mrefu wa wastani mwenye mwili mkubwa na rangi ya maji ya kunde. Alipokiona kisu kikubwa cha springi kikimetameta mbele yake akanywea.
“Mnafanya nini ndani kwangu? Kwanza ninyi ni akina?” Dk. Marina aliuliza kwa hofu huku akijikunyata pale kitandani na kuwatazama akina Spoiler na Dulla Mcomoro kwa zamu.
“Mama, hatuko hapa kwa ajili ya kukudhuru, tunahitaji taarifa fulani toka kwako kisha tutaondoka zetu na kuwaacha salama,” Spoiler alisema kwa sauti tulivu huku akimkazia macho.
“Who are you guys?” Dk. Marina aliuliza na kushusha pumzi.
“Huna haja ya kutufahamu, sisi ni watu wazuri sana na tumekuja hapa kuzungumza nawe mambo kadhaa, ila kama utataka kuleta ujanja ujanja sisi ni wabaya sana hata shetani anatuogopa, we can destroy you in a second,” Spoiler alisema kwa sauti ya kufoka kidogo.
“Taarifa gani mnaitaka toka kwangu?” Dk. Marina aliuliza tena huku hofu ikiwa imemtawala.
Spoiler alimgeukia Dulla Mcomoro aliyekuwa bado kamshika Shamila na kumpa ishara ya kumfungia bafuni. Dulla Mcomoro alimkokota Shamila akampeleka katika bafu lililokuwa ndani ya chumba cha Dk. Marina, akamfungia huko baada ya kumpekua ili kuhakikisha hakuwa na simu wala kifaa chochote cha mawasiliano.
“Tunazo taarifa kuwa miaka mitatu iliyopita, mwezi Oktoba mumeo aliuziwa gari aina ya Cadillac DeVille la muundo wa kizamani, tupo hapa kwa kuwa tunalitaka gari hilo,” Spoiler alisema huku akiwa makini kumtazama Dk. Marina.
“Cadillac DeVille?” Dk. Marina alishtuka kidogo na kumtazama Spoiler kwa mshangao, kisha akaendelea, “Ni kweli tuliwahi kununua gari la aina hiyo miaka mitatu iliyopita lakini kwa sasa hatunalo, tumeliuza.”
“Mmeliuza lini na nani aliyelinunua?”
“Limeuzwa mwezi uliopita ila mimi simjui aliyelinunua kwani ni Frank ndiye aliyeliuza…” Dk. Marina alijaribu kujitetea.
“Frank ndiyo nani?”
“Mwanangu mkubwa, yeye anafanya biashara ya kuuza magari.”
“Tutampataje?”
“Nani?”
“Frank. Tunahitaji kujua ni nani aliyelinunua hilo gari.”
“Alikuja hapa muda mfupi uliopita, ameondoka na mkewe kwenda ofisini kwao, show room ya Magomeni Mikumi,” Dk. Marina alijibu huku akijiuliza wale watu ni kina nani waliomvamia kwa sababu ya kuulizia gari la kizamani!
“Magomeni Mikumi ipi?”
"Barabara ya Kawawa, karibu na kituo cha daladala cha Magomeni Mikumi kama unaelekea Ilala,” Dk. Marina alisema na kuwatajia jina la yadi hiyo ya kuuza magari.
“Mmeliuza mwezi uliopita, eeh! Kipindi chote lilikuwa wapi?” Spoiler aliuliza baada ya kufikiria kwa kitambo.
Dk. Marina alitaka kusema akasita na kumeza funda kubwa la mate kutowesha koo lake lililokauka, kisha akashusha pumzi. “Kwani shida yenu ni nini hasa, mbona sielewi?”
“Okay, nipe simu yako,” Spoiler alimwambia Dk. Marina huku akinyoosha mkono wake.
“Mmetaka taarifa nimewapa lakini bado mnataka na simu yangu, ya nini?” Dk. Marina alisema kwa huzuni.
“We mama, umeambiwa toa simu yako, hatuhitaji maswali,” Dulla Mcomoro alisema kwa ukali huku kinyanyua shati lake kumwonesha bastola iliyotuama kiunoni kwake na kumfanya Dk. Marina kuingiwa woga kwa namna Dulla Mcomoro alivyokuwa anamwangalia, akanyoosha mkono wake kumpatia simu Spoiler.
Spoiler aliipokea ile simu na kuizima kisha akatoa betri. Alimpa ishara Dulla Mcomoro kumleta Shamila kutoka bafuni kisha wakawafunga wote wawili kwa kamba na kuwaziba mdomo yao ili wasiweze kupiga kelele.
“Utatusamehe, mama, hatuna namna nyingine ya kufanya, mtabaki hivi kwa muda, tukishamalizana na Frank atakuja kuwafungulia,” Spoiler alimwambia Dk. Marina, wakatoka na kuufunga mlango wa chumba kwa funguo.
Walipofika nje waliingia ndani ya gari lao, wakaondoka kuelekea Magomeni Mikumi.
* * * * *
Saa kumi na mbili jioni jua lilikuwa limekwisha anza kuzama jijini Dar es Salaam na kwa mbali kiza kikianza kuchukua nafasi yake, anga la rangi nyekundu lilikuwa likinywea katika ukungu upande wa magharibi.
Tunu alishuka kutoka kwenye teksi, akatazama kushoto na kulia kwake halafu akavuka barabara akielekea upande ule wa magharibi, alipiga hatua taratibu kwa madaha kuelekea kwenye jengo moja lenye kuta safi za vioo na juu yake kukiwa na bango kubwa jeupe lenye maandishi makubwa mekundu yakisomeka MILAN CLUB & SPA. Chini ya bango lile kulikuwa na maandishi madogo yanayosomeka ‘Just enjoy every moment.’
Inaendelea...