Taxi - (81)
ILIPOISHIA
Mr. Oduya alichukua simu yake na kutafuta namba za Dk. Masanja, meneja mkuu wa hoteli ya
Udzungwa Beach Resort na kupiga ili kupata uhakika. Majibu aliyopewa yalimfanya ajihisi kukanganyikiwa, akili yake ilijaribu kukataa kabisa kukubaliana na taarifa ile na kile alichokishuhudia kwenye katika nyaraka zile za ununuzi wa gari.
Alijitahidi kuwa makini zaidi na akiishirikisha akili yake kikamilifu katika kumletea taarifa za kuaminika, kwani mambo yale hayakuwa yanamwingia kichwani kabisa! Ni vipi Sammy ameendelea kujitokeza katika harakati zake za kuusaka urais wa Tanzania na kugeuka kuwa kitisho?
Aliinua uso wake na kutazama juu akionekana kuwaza mbali. Wakati huo Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa kimya kabisa wakimtazama kwa wasiwasi. Akiwa katika hali ile mara hisia mbaya zikamjia na hapo mapigo ya moyo wake yakaanza kwenda kasi isivyo kawaida, hasa alipowaza kuwa huwenda wapinzani wake kisiasa walikuwa na fununu fulani kuhusiana na lile gari na wangeweza kulitumia kummaliza.
SASA ENDELEA...
Akiwa amezama kwenye tafakuri ile, akili yake ikaenda mbele zaidi katika kuunda hoja kichwani. Akaanza kuwaorodhesha washindani wake wakuu wa kisiasa bila kujali vyama walivyotokea, akianzia na wapinzani wake wakuu ndani ya Chama Cha Ukombozi, Benard Tumbo, Dk. Hussein Abbas na Anuary Kamba. Kisha akawafikiria wa kutoka vyama vingine walioonekana kukubalika zaidi, Zingo Kabwela na Tindua Luis.
Alipomaliza akaanza kutathmini vizuri nguvu na hali ya mahusiano yake kisiasa na viongozi wa nchi ikiwemo wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama. Tathmini yake ikamweleza kuwa mahusiano ya nyanja zote baina yake na viongozi wa nchi na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama bado yalikuwa mazuri ingawa kulikuwa na misuguano ya kawaida ya hapa na pale kati yake na baadhi ya viongozi hao kutokana na tofauti za kimitazamo.
Alipotafakari kwa kina juu ya misuguano hiyo akajaribu kuwaza kama kulikuwepo mmojawapo wa wapinzani wake kisiasa au kiongozi ambaye angeweza kuwa na ukaribu na Sammy, bado haikuweza kumridhisha kuwa hata kama kusingekuwa na yeyote kati yao mwenye ukaribu na Sammy bado isingeweza kuwa sababu toshelevu ya kumfanya asichukue tahadhari.
Baada ya kimya cha kitambo fulani Mr. Oduya aliinua uso wake uliosawajika na kumtazama Spoiler. “Unamfahamu Samuel John Kambona?” alumuuliza kwa sauti tulivu.
“Sina hakika, lakini nadhani ni yule bwege aliyekuwa anafanya kazi hoteli ya
Udzungwa Beach Resort,” Spoiler alisema baada ya kitambo kifupi cha kuvuta kumbukumbu. Mr. Oduya alibetua kichwa chake kukubali.
“Bado ni kizungumkuti kwani sina hakika kama hadi wakati huu hakuna yeyote kati ya wapinzani wangu kisiasa anayefahamu kuhusu hilo gari. Nimeshtuka sana kuona kuwa ni Sammy huyu huyu ndiye mmiliki wa gari ambalo siku zote nilidhani lilishateketezwa. Kwa kweli hizi ni taarifa za kustaajabisha na kuogofya sana,” Mr. Oduya alisema katika hali ya kukanganyikiwa huku taratibu akiviminyaminya vidole vyake vya mikononi katika hali ya kuupisha utulivu kichwani mwamke.
Kilipita tena kitambo fulani cha ukimya kila mmoja akijaribu kutafakari, kisha Mr. Oduya alishtuka akionekana kukumbuka jambo.
“Katika kufuatilia taarifa hizi mmehakikisha hamjaacha kielelezo?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler huku akimkazia macho.
“Hapana, hatujaacha kitu, tulichukua tahadhari zote, tulihakikisha tumebadili muonekano wetu, tukitumia gari lenye namba bandia na kuvaa glavu laini mikononi ambazo haikuwa rahisi mtu kutushtukia,” Spoiler alisema kwa uhakika.
“Silas, usichukulie kirahisi hivyo, kumbukeni kuwa hii ni vita. Mkifanya chochote hakikisheni hamuachi kitu tusije tukavuruga na kujipa kesi nyingine. Sawa?”
“Usijali, mkuu,” Spoiler na Dulla Mcomoro wakasema kwa pamoja.
“Okay, sasa mna kazi nyingine. Hakikisheni usiku huu huu huyu mtu anayeitwa Samuel John Kambona anapatikana kisha mpelekeni kwenye nyumba ya Kinondoni Makaburini na gari lake liteketezwe kabisa. Amenitafuta muda mrefu na sasa amenipata,
I think he derseves to die,” Mr. Oduya alisema kwa sauti ya kitetemeshi kutokana na ghadhabu aliyokuwa nayo.
Spoiler na Dulla Mcomoro walikubali kwa kubetua kichwa, kisha wakanyanyuka na kuanza kuondoka wakifahamu kuwa kauli ile iliashiria kuwa maongezi kati yao mle ndani na Mr. Oduya yalikuwa yamefika tamati. Spoiler ndiye alikuwa wa kwanza kusimama sekunde chache kabla Dulla Mcomoro hajafanya hivyo.
“Tambueni kuwa nimewapa jukumu hili kwa sababu bado nawaamini sana, hivyo hakikisheni hamfanyi makosa,” Mr. Oduya aliongea kwa sauti tulivu ya kusihi na katika sauti yake kulikuwa na hali ya hofu iliyokuwa imejificha nafsini mwake. Alilazimisha tabasamu usoni mwake ingawa tabasamu hilo lilikataa kabisa kuumbika.
Spoiler na Dulla Mcomoro walibetua vichwa huku wakisimama kwa ukakamavu kama wanajeshi kisha wakaanza kuzitupa hatua zao taratibu kuondoka kwenye ofisi ile na kuufikia mlango, Spoiler aliufungua huku akiwa na hakika kuwa macho ya Mr. Oduya yalikuwa nyuma yao yakiwasindikiza.
Alipoufungua ule mlango akageuka na kumtazama tena Mr. Oduya aliyekuwa ameketi kwa utulivu kwenye kiti chake, alichokiona usoni kwa Mr. Oduya lilikuwa ni tabasamu lililohanikiza kila aina ya unyama. Bila kupoteza muda Spoiler akamtupia tabasamu la kuonesha kuwa alikuwa tayari kwa lolote, kisha wakatoka nje ya ofisi ile na kufunga mlango.
* * * * *
Saa mbili kasorobo usiku nyumbani kwa Sammy, Winifrida alikuwa anakatakata nyanya za kachumbari huku akimtupia jicho la wizi Joyce, ambaye muda huo alikuwa kafungua milango ya jokofu kubwa lililokuwa katika ukumbi wa chakula ila alionekana kuzama kwenye lindi la mawazo wala asichukue kitu alichokusudia.
Joyce alikuwa amesimama huku aking’ong’ona kucha zake, alikuwa amezama katika lindi la mawazo yaliyomfanya kuiona dunia yote ikiwa imemwelemea na kumkalia kichwani. Alijaribu kuwaza hili na lile katika namna ya kutafuta ni jinsi gani angeweza kuirejesha faraja na furaha iliyotoweka ghafla kwenye ndoa yake.
Donge la uchungu lilikuwa limemkaba kooni, alishindwa kuuzuia uchungu aliouhisi ukipenya moyoni mwake kutokana na mzozo uliokuwa umezuka kati yake na Sammy mchana wa siku ile. Tangu Sammy aliporudi nyumbani saa tano na ushee asubuhi hadi alipoondoka saa kumi na mbili jioni hawakuwa katika hali ya maelewano.
Siku nzima Sammy alikuwa akimpiga vijembe Joyce. Joyce hakuamini, alizoea utani wa mumewe lakini kila alipomtazama machoni hakuona dalili yoyote ya utani. Hakutaka kuamini kuwa ingetokea siku mumewe angemkasirikia kiasi kile. Ilifikia hatua alijiuliza kama yote hayo yalitokana na yeye kumweleza ukweli kuhusu kilichojitokeza kati yake na mwanamuziki Dynamo Plus au kulikuwa na jambo jingine lililojificha katikati.
Inaendelea...
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple