HEKAHEKA! 24
Na Bishop Hiluka
“Chochote atakachowaleleza ni uongo, simjui huyu mtu na wala sijawahi kukutana naye,” nikasema kwa hasira kabla Trésor hajajibu lakini nikashtukia nikizabwa kofi la nguvu usoni lililonifanya kuona vimulimuli mbele ya macho yangu.
“Shut up! Hujaulizwa wewe, unakimbilia kujibu!” Komandoo aliyenichapa kibao akafoka.
Nikasonya kwa hasira huku nikigeuza shingo yangu kumtazama yule komandoo, nikamtemea mate, kutahamaki nikazabwa kofi la pili lililonifanya kuyahisi maumivu makali sana yaliyosambaa haraka hadi shingoni hadi mgongoni.
“Trésor, tueleze ni wapi mmeficha silaha!” Madame Pamela akamwambia Trésor kwa ukali kidogo.
Endelea...
“Ukweli japo mimi ni mshirika wa karibu wa Brown lakini naapa sijui mahali zilikofichwa kwani mkakati wote anaujua yeye na watu wengine wasiozidi watatu ambao mimi siwafahamu, mimi nilikuwa mtu wa kusubiri kupewa amri tu,” alisisitiza Trésor na kuniacha na mshangao usioelezeka.
“Na kuhusu washirika unaowafahamu?” aliuliza Madame Pamela.
“Wote ninaowafahamu ndio wale niliowataja, siwajui wengine labda muulizeni mwenyewe,” alisema Trésor huku akiyakwepa macho yangu na kuinamisha uso wake chini kwa hofu.
“Wapi mmezificha silaha, au unataka tukurudishe tena chumba cha mahojiano ndipo useme ukweli, siyo?” Madame Pamela alimuuliza Trésor kwa ukali.
“Nimewaambia Brown ndiye anayejua kila kitu, mimi ningekuwa najua zilipo ningewaambia, mbona haya mengine nimesema! Najua hata nikificha bado adhabu inayonikabili ni kifo tu,” alisema Trésor.
“Mimi naona mmeamua kupandikiza watu wenu ili mnikomoe, huu ni uongo mkubwa na ninaapa kuwa lazima niwashtaki kwenye mahakama ya haki za binadamu,” niling’aka kwa hasira.
“Kama unadhani kuwa Trésor ni muongo kwanini usijiulize tuliipata wapi ile picha mliyopiga wote mkiwa na Jasmine, au hujiulizi zile nyaraka zako zikiwemo zile pasipoti na kijitabu chenye mipango yako haramu tulivipataje kama siyo yeye aliyetusaidia kuvipata?” Madame Pamela akaniuliza huku akinitazama kwa udadisi.
“Nimekwishawaambia mimi siitwi Brown. Sijui mmewatoa wapi hawa watu wanaotoa ushahidi wa uongo dhidi yangu, na mkakubali kudanganywa kiasi hiki! Muulizeni kila kitu yeye ndiye atakuwa anafahamu kuhusu hiyo mipango na ugaidi mnaonituhumu nao,” nilijitetea lakini haikuonekana kusaidia.
Madame Pamela alimpa ishara yule komandoo ya kumwondoa Trésor na kumrudisha alikomtoa. Wakati Trésor akiondolewa Madame Pamela alinigeukia akanitazama kwa uyakinifu huku akiachia tabasamu la ushindi.
“Sasa niambie, washirika wenzako wako wapi na silaha mmezificha wapi?” aliniuliza kwa sauti tulivu.
Sikumjibu bali niliendelea kubaki kimya huku nikimkodolea macho kwani nilionesha kuchoshwa na maswali yake.
Alishusha pumzi ndefu huku akiendelea kutabasamu na baadaye tabasamu lake liligeuka kuwa kicheko, kisha nikamuona yule komandoo aliyetoka na Trésor akirudi na muda huo huo Madame Pamela akawapa ishara fulani wale makomandoo ambayo sikufahamu maana yake.
Mara nikawaona wale makomandoo wakinisogelea kwa ukakamavu mkubwa, na kwa haraka sana wakanifungua zile pingu zilizokuwa zimefungwa kwenye mikono na miguu yangu pale kwenye kile kiti cha umeme kilichokuwa kikitumika kunisulubu.
Nikiwa bado nashangaa ghafla wale makomandoo wakanishika miguu yangu na kunivuta wakinishusha kwa nguvu kutoka pale kwenye kile kiti hali iliyonifanya nitue pale chini sakafuni kwa matako na kunifanya nisikie maumivu makali sana yaliyosambaa mwili mzima.
Nilijaribu kujitetea lakini ilikuwa kazi bure kwani walianza kunishushia kipigo cha mateke mwilini mwangu na kujikuta nikiishiwa na nguvu na kulala sakafuni kama mfu.
Wale makomandoo waliporidhika kuwa kile kipigo kilikuwa kimenilegeza kiasi cha kutosha, wakaanza kuniburuza kibabe kuelekea kule kwenye lile tangi kubwa lililokuwa limejengwa kwa vioo ambalo ndani yake lilikuwa limejazwa maji.
Walinibwaga pale chini jirani na lile tangi la maji. Nikiwa pale chini nikihema kwa nguvu kutokana na kile kipigo nilimuona Madame Pamela akinisogelea taratibu huku wale makomandoo wakinizunguka na hapo nikafungwa kamba mikononi.
“Tuambie wenzako wako wapi na silaha mmezificha wapi?” aliniuliza Madame Pamela kwa hasira.
“Wenzangu akina nani?” nilimuuliza kwa hasira.
“Unaoshirikiana nao kufanya ugaidi”
“Sifahamu chochote kuhusu ugaidi unaouzungumzia…”
Nilikatishwa na kipigo cha mateke ya mgongoni, kabla sijajua niseme nini mara nikabebwa mzobe mzobe na wale makomandoo kisha nikarushwa na kuangukia ndani ya lile tangi la maji. Matukio yote yale yalifanyika kwa haraka sana.
Nikajua sasa walikuwa wamedhamiria kunitesa kwa kunizamisha ndani ya lile tangi la maji kwa kufungulia umeme ulioungwa ndani ya lile tangi la maji ili kunipiga shoti mbaya na ikiwezekana kuniua kabisa.
Nikakumbuka kuwa niliwahi kusoma habari kuhusu matumizi ya mbinu za ukatili na utesaji kwa kuwaweka watuhumiwa kwenye maji, kuwakosesha usingizi, kuwapiga shoti ya umeme na kila aina ya utesaji ili kupata siri kutoka kwa magaidi.
Nilisimama na yale maji ndani ya lile tangi yaliishia usawa wa kifua changu. Nikiwa sijui kilichokuwa kinaendelea ghafla nikapigwa shoti kali ya umeme iliyonitetemesha mwili mzima huku nikihisi ngozi yangu ikiunguzwa na moto wa umeme uliokuwa ukisambaa haraka sana mwilini mwangu.
Nikajikuta nikiwa katikati ya maumivu makali sana yasiyoelezeka, nikaanza kutetemeka kama niliyekumbwa na ugonjwa mbaya wa degedege.
Nilifumbua mdomo wangu kupiga kelele za kumuomba Madame Pamela asitishe yale mateso lakini sauti yangu haikuweza kutoka, kila nilipopiga kelele niliisikia sauti yangu ikiishia ndani ya akili yangu.
Kwa mbali nikasikia mlango wa kile chumba ukigongwa kwa nguvu kisha ukafunguliwa na hapo nikasikia sauti ya vishindo vya watu waliokuwa wakija mbio kule kwenye lile tangi huku wakipiga kelele kumtaka Madame Pamela asitishe yale mateso.
Muda ule ule nikaanza kujiona nikipaa angani kwa kasi ya ajabu sana, na nilipofika juu zaidi nikajikuta nikianza kushuka chini kwa kasi ile ile na kisha nikatumbukia kwenye shimo refu sana lililokuwa na kiza kilichotisha.
Na mara giza zito likatanda kwenye mboni zangu za macho huku taratibu nguvu zikianza kuniishia na mwili wangu ukilegea, mapigo yangu ya moyo nayo yakaanza kudorora, mwishowe nikahisi roho yangu ikifika njia panda…
* * * * *
Nilizinduka nikajikuta nipo kwenye chumba kikubwa nikiwa nimelala kwenye kitanda kikubwa cha chuma cha futi nne na nusu kwa sita, nikiwa nimelalia foronya laini na mto wa kuegemeza kichwa.
Ndani ya chumba kile kulikuwa na hewa safi iliyokuwa ikisambazwa taratibu na kiyoyozi kilichokuwa juu ya dari ya kile chumba iliyokuwa imetengenezwa kwa gypsum nzuri ya rangi nyeupe na katika sehemu za dari ile kulining’inizwa taa nzuri.
Nilikuwa nimerudiwa na fahamu zangu na sikujua nilipoteza fahamu kwa muda gani, hisia zangu zilinitanabaisha kuwa nilikuwa nimerudiwa na fahamu huku nikikumbuka vizuri masaibu yote yaliyonitokea kule kwenye chumba cha mateso makali.
Sikuwa na uhakika kama nililetwa pale kwa gari, mkokoteni, machela au niliburuzwa kama ilivyotokea kule kwenye chumba cha mateso, kwa kuwa sikuwa na fahamu yoyote nilipokuwa nikiletwa pale.
Hata hivyo, jambo hilo halikuwa la muhimu sana kwangu. Jambo lililokuwa la muhimu ni kwamba nilikuwa bado nipo hai, na hivyo nikataka kujua nilikuwa wapi.
Mambo sasa yananoga, ni nini kitaendelea? Fuatilia kuujua mwisho wa Hekaheka...