Simulizi: Soka Lilivyonikutanisha Na Shetani

Simulizi: Soka Lilivyonikutanisha Na Shetani

Sehemu ya 16

Nilikuwa nakwenda katika moja ya jiji kubwa hapa nchini, nilikuwa naikimbilia dunia mpya maishani mwangu. Nilizaliwa kijijini Maji moto, mkoani Mara na kukulia huko, sikuwahi kufika katika sehemu nyingine zaidi ya kijijini kwetu.

Sasa nilikuwa nalikaribia jiji kubwa la Mwanza, jiji lenye sifa za kuogofya. Moyo ulikuwa unanidunda. Nilikuwa na hofu ila kamwe sikuisikiliza sauti ya roho dhaifu ya hofu. Mwalimu Keneth alinifundisha falsafa moja ambayo ilinikaa kichwani.

Aliniambia: “Adui namba moja katika maendelea ya binadamu yeyote duniani, ni HOFU” hivyo sikupenda kabisa kuindekeza sauti iliyonitia wasiwasi na mashaka.

Wakati wote nilikuwa namwomba Mungu kimoyomoyo anisaidie katika safari ile, nilihitaji mafanikio, nilihitaji kuishi katika ndoto zangu, nilihitaji furaha maishani. ***** Saa kumi jioni, tuliingia Mwanza, ilikuwa ni kama paradiso machoni mwangu, ulikuwa ni mji mzuri wa kuvutia, zaidi nilivutiwa na nyumba zilizojengwa katika milima.

Abiria wote tukashushwa katika stendi ya Buzuruga, wakati huo ilikuwa ni kabla ya stendi ya Nyegezi kujengwa.
Kwa kuwa sikuwa na mawasiliano na kocha wa timu ya Igogo Fc, Gideon Nkisi, nilichofanya ni kuulizia daladala za Igogo. Nikaelekezwa. Kupitia maelekezo ya mwalimu Keneth.

Aliniambia nikifika Igogo, huko ningeulizia maskani ya timu ya Igogo Fc, ambapo kama ningeweza kuonyeshwa, ingekuwa rahisi kumpata kocha wa timu hiyo, Gideon Nkisi.

Waswahili husema: Maisha ni fumbo. Laiti kama ningekujua madhila yatakayo nikuta mbeleni basi ningerudi nyumbani haraka sana kuendelea na maisha yangu na mke wangu Pili. Sikujua.

DAKIKA ishirini na tano badaye, nilifika Igogo. Nilishukia karibu na kituo kidogo cha polisi, nikasogea katika kioski cha jamaa aliyekuwa anauza vinywaji baridi.
“Samahani ndugu yangu,” nilimsemesha jamaa aliyeonekana kuwa mwenyeji wa pale.

“Bila samahani.”
“Naulizia maskani ya timu ya Igogo Fc?” nilimuliza.
 
Sehemu ya 17

“Uwanja wa wanaofanyia mazoezi si unaujua?” jamaa naye akaniuliza. Mtanzania ukimuuliza swali naye anakuuliza swali.

“Hapana mimi ni mgeni kabisa hapa. Ila labda ukinielekeza naweza kufika.”
“Unaona hii njia...” alisema huku akisonta kijinjia kilichopandisha kilimani.

“Nenda nayo moja kwa moja. Itakupeleka hadi uwanja ulipo, na ndipo maskani ya timu ya Igogo Fc” alisema.

“Hawana ofisi?”
“Waitoe wapi? Timu za daraja pili zenyewe hapa mjini hazina ofisi, sembuse Igogo Fc, timu ya daraja la nne.” Jamaa alisema. Alionekana kuidharau timu hiyo.

Nilimshukuru yule jamaa, nikafuata ile njia aliyonielekeza. Dakika kumi badaye nilikuwa mbele ya uwanja wa mpira. Uwanja uliokuwa na nyasi zilizokosa utunzwaji mzuri.

Niliachia tabasamu pana baada ya kuona wachezaji ambao walivalia jezi nzuri machoni mwangu. Jamaa walikuwa wakifanya mazoezi ya viungo chini ya makocha kama watatu.

Kocha mmoja mnene wa umbo lakini mwepesi, alikuwa amevalia traksuit na soksi mikononi mwake alikuwa upande wa makipa watatu akitoa mazoezi ya peke yao. mwingine alikuwa jamaa kati ya miaka 40 ama 45 alikuwa na misuli mikakamavu, alivaa bukta na raba alikuwa akiongoza mazoezi mepesi ya viungo.

Na mwingine alikuwa ni mzee wa kati ya miaka 60, naye alikuwa amevaa kimichezo, alisimama kando akingalia namna mazoezi yote kati ya wale makipa na wachezaji wengine namna yalivyokuwa yakifanyika. Mara kadhaa alikuwa akihamasisha wachezaji kujituma mazoezini. Nikaamini ndiye Gideon Nkisi. Kocha mkuu wa timu hiyo. Nikamfuata.

“Shikamoo kocha.” nilimsalimia
“Hujambo.” “Sijambo kocha, bila shaka wewe ndiye Gideon Nkisi?” nilimuliza.
Alibaki ananiangalia kwa jicho loliloashiria nieleze shida yangu, nikaanza kujitambulisha:

“Mimi naitwa Ajibu Maganga, nimetokea Mkoani Mara, kijiji cha maji moto. Bila shaka mwalimu Keneth Edsoni, alikwisha kueleza juu ya ujio wangu.” nilijieleza na kumuuliza.
“Ndio wewe!!” mzee aliniuliza kwa mshangao.
“Naam! ndio mimi kocha.”

“Umefika lini?”
“Leo, kama lisaa limoja limepita,” nilimjibu. Aliniangalia kwa kunisaili, kisha akanimbia:
“Hebu kanisubiri kwenye mti pale, tutaongea badaye,” alisema.
 
Sehemu ya 18

Nilitoka nje ya uwanja na kumsubiri kocha yule kama alivyonieleza, niliketi kivulini huku nikiwaza mambo chungu nzima, kama ni safari yangu kisoka, sasa ndio ilikuwa ikiaanza.

Wakati niko nje nilikuwa nafuatilia mazoezi ya timu, nilivutiwa na aina ya mazoezi waliokuwa wakipata wale wachezaji, shauku ya kuwa miongoni mwao ilikuwa kubwa.

Timu hii ya Mwanza ilikuwa na vipaji vya aina yake, ilikuwa inatofauti fulani na ile ya Home Boys ya Bunda. Kwa kweli hii ilikuwa na vijana wenye vipaji vya kuvutia.

Walipoanza kufanya mazoezi ya mpira, nilifuatilia kwa makini sana. Bado niliona pamoja na jamaa kuwa na vipaji miguuni mwao ila bado nafasi yangu ilikuwa kubwa mbele yao.

Saa moja kasoro, mazoezi yalikwisha, wachezaji na makocha wote wakaja katika mti niliokuwa nimeketi, walikaa kando yangu, miilii yao ikiwa inavuja jasho, makocha walitoa maelekezo mawili matatu juu ya mazoezi ya siku hiyo, kisha wakatakiwa kuondoka na kukutana kesho yake asubuhi.

Yule kocha mtu mzima, alikuwa ni kama amenisahau, tangu aniambie nimngoje chini ya mti. Hakuonekana kama alikuwa na miadi na mimi.

Nilimfuata na kumsemesha.
“Kocha,”nilimwita. Alipogeuka akataharuki.
“Aaaagh! Nilikuwa nimekusahau kijana wangu.” alisema kwa sauti ya wahaka, kisha papo hapo akanimbia.

“Naomba kesho uwahi asubuhi mazoezini nione uwezo wako,” alisema halafu hakusubiri swali wala maoni. Akaondoka.
Nilibaki nimeganda, nilitaka kuongea kitu lakini sikujua ni nini nilitaka kusema, watu walizidi kutawanyika, mimi nikabakia nimesimama pale pale.

Sikuwa na mahali pakuishi. Ukarimu wa watu wa mjini ni tofuati na kijijini kwetu, nilitegemea labda mwalimu yule angeniuliza nimefikia wapi na kwa nani?

Au basi hata anitambulishe kwa timu yake ikiwezekana hata ani karibishe mahali ambapo ningeweza kuishi kwa siku mbili tatu. Ila hakuwa na lolote alilojali juu yangu.

Maisha ni vita. Lazima nipambane hadi nishinde. Niliwaza kimoyomoyo, baada ya kubakia peke yangu pale uwanjani, kinyonge nilishika ile njia iliyonileta mara ya kwanza.

Nikateremka nayo hadi kwenye kioski cha yule aliyenielekeza njia. Aliponiona alitabasamu. “Ulifika?” aliniuliza.
“Ndio, bila tatizo kabisa.”nilimjibu huku nikijibwaga.
 
Sehemu ya 19

nikijibwaga. katika benchi lililokuwa mbele ya kioski chake. “Nipe soda na mandazi, ” niliagiza. Jamaa haraka haraka akanihudumia.
“Jisikie upo Serena hotel, karibu sana,” jamaa yule chakaramu aliniambia. Nikatabasamu.

Nikamuuliza jambo jingine. “Hapa ni wapi nitapata gesti ya bei rahisi?”
“Zimejaa tele.”
“Ziko wapi?”
“Unaona zile ofisi za idara ya maji, pale...”alisonta kunionyesha. Majengo yaliyokuwa mita kama 100 kutokea pale.
“Ndio.”

“Pale kuna gesti moja bei rahisi sana, askari polisi wa hapa, wote huwa wanapeleka wachumba zao pale,” alisema.
Nilicheka, jamaa alikuwa na meneno mengi sana ya kufurahisha. “Nashukuru ndugu yangu, acha nikapumzike sasa.”
“Unakwenda kupiga peku kaka?

Kondomu hununui?”
“ Kwani nimekwambia nina kwenda kulala na mwanamke?”
“Unakwendaje kulala mpweke sehemu kama ile kaka?” “Una maneno mengi sana, kabila gani wewe.”

“Mimi mtu wa Kigoma, ila hapa nafahamika kwa jina la Chado” niliondoka nikimuacha Chado na uchakaramu wake.
*****
Alfajiri na mapema, nilikuwa mtu wa kwanza kuwasili katika uwanja wa mazoezi, nilifanya mazoezi mepesi ya peke yangu, Nusu saa badaye mtu mmoja mmoja wakaanza kujitokeza uwanjani.

Dakika 45 badaye timu nzima na makocha ikawa imetimia. Nilijisogeza kwa kocha, mzee Gideon na kumsalimu ili tu aniaone. Maana kwa muda mfupi tu nilimtambua mzee yule ana ugonjwa wa kusahau mambo.

Kweli mzee yule nadhani umri ulikuwa unamwacha, aliponiona, alishituka tena, akanisalimu kwa ukarimu tu kisha alinitambulisha kwa kocha wa viungo kama mchezaji mgeni ninayetakiwa kufanyiwa majaribio, kama nitafaa basi nijumuishwe kwenye timu yake.
“Jina lako?” Kocha msadizi aliuliza.
“Ajibu maganga.” Nilijibu.

“Karibu.” Alisema
Asubuhi ile tulifanya mazoezi pamoja,ingawa nilikuwa mgeni kwenye baadhi ya mazoezi, lakini nilijituma kiasi cha kuwafurahisha wale walimu.

Tulipogawa timu mbili, na kufanya mazoezi ya kucheza mpira, kocha mkuu aliniuliza namudu zaidi kucheza nafasi gani, nikamwambi kama mshambuliaji, yanii namba tisa.

Wakati huo nilikuwa nimekwisha fahamiana na baadhi ya wachezaji kadhaa, wao pia walionekana kuvutiwa na mimi.
 
Sehemu ya 20

Niliamini kitu pekee kitakachonifikisha mbali katika mchezo wa soka ni nidhamu. Kwa kweli niliweka hilo akilini.

Katika mazoezi ya mpira, nilionyesha uwezo mkubwa kiasi cha kumwacha kila mtu mdomo wazi, nilikuwa na uwezo mkubwa wa kufunga na kutoa pasi za magoli.

Watu kadhaa waliokuwa wakifuatilia mazoezi nje, walionekana kukoshwa na uwezo wangu.
“Anaitwa nani yule?” “Sijui, jamaa ni mgeni huyo.”

“Atakuwa ametokea timu ya ligi kuu, si bure, “Inawezekana kabisa.”
Kwa masikio yangu nilisikia mashabiki wakiongea nje ya uwanja. Sio hao tu hata kocha Gideon Nkisi, kila nilichokuwa nafanya uwanjani, alikuwa akinisifia waziwazi.

Nusu saa baada ya mazoezi, nilikuwa gumzo pale uwanjani, kocha na wachezaji wenzangu walinipongeza kwa uwezo nilio uonesha. Baada ya wachezaji kusambaa makocha aliniambia mimi nisubiri. “Umefikia wapi Ajibu?” waliniuliza.
“Nimefikia gesti ya pele chini. Inaitwa...inaitwa... ipo karibu na ofisi za idara ya maji.” Nilisema.

“Huna ndugu hapa mjini?”
“Sina.” “Kwa hiyo umekuja Mwanza kwa ajili ya mpira tu, au una biashara zako nyingine?”

“Mpira peke yake ndio umenileta huku.” Nilisema. “Kweli!!” waliuliza kwa pamoja.
Niliwasimulia kila kitu kuhusu kuondoka kwangu kijijini na kuja mjini kwa ajili ya mpira, nikailezea kiu yangu ya kufanikiwa kupitia mchezo huo.

Kila aliyenisikiliza alivutiwa na fikra nilizokuwa nazo, hakuna ambaye alitegemea mtu kama mimi kutoka kijiji cha Maji moto, ningeweza kuwa shauku kubwa ya mafanikio kuliko vijana wa mjini.

“Sasa nisikilize Ajibu, walimu wote kwa pamoja tumekubaliana na uwezo wako, jioni njoo mazoezini tutakuwa tumekwisha fahamu namna gani utaishi na pia utapewa maelezo namna ambavyo klabu yetu inavyojiendesha...umesikia?”
“Nimesikia kocha.”

Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nilikuwa nina furaha ambayo sijui kama iliwahi kutokea maishani. Nilimshukuru Mungu kimoyo moyo, niliamini kupitia timu ile ningeweza kucheza katika ligi kuu ya nchi.
 
Sehemu ya 21

Na hiyo ingekuwa ni fursa nzuri ya kuwa mchezaji wa kimataifa.
Niliondoka na kushuka kule kwenye kioski cha Chado, kwa kuwa tangu jioni ya jana nilikuwa nimelalia soda na mandazi hivyo njaa ilikuwa inaniuma.

Chado alinionyesha kwa mama ntilie, nikaenda nikanywa chai kisha nikaelekea katika ile gesti ya bei rahisi, ambayo nilikuwa nimefikia, nikapumzika. Nilikuwa bado na akiba ya kuniweka mjini angalau kwa wiki mbili ama tatu.

Mchana ulipotimu, nilikula kisha nikaenda uwanjani kusubiri muda wa mazoezi. Kila nilipokuwa nikiungalia uwanja wa mpira niliuona kama ndio barabara ya kunifikisha kwenye nchi ya ahadi.

Kama kawaida yangu, ilipotimu saa tisa alasiri, lisaa limoja kabla ya mazoezi ya pamoja, nilianza mazoezi ya peke yangu. Hadi wenzangu wanafika walikuta mwenzao mwili umwekwisha pamba moto.

Nilikuwa tayari nimekwishaanza kujulikana, mbali ya makocha hakuna niliyemwambia jina langu naitwa nani, ajabu kila mtu tayari alikuwa amekwisha nitambua kuwa naitwa Ajibu Maganga.
Nilichokuwa nimekionesha asubuhi ndicho, nilichokiendeleza jioni ile na zaidi.

“Komredi Ajibu nakuonea wivu sana Kop,” mchezaji mmoja anaitwa Edward Anthony aliniambia nikiwa nimefunga ‘hattrick’ mazoezini.

“Kwa nini?”
“Hauna muda mrefu huku mchangani, utachezea primier legue.”
“Kweli.”

“Kabisa nakuambia. Una vitu adimu sana.” Kauli ya mchezaji yule iliujaza moyo wangu. “Ila itabidi ukabiliane na mambo madogo madogo.”
“Mambo madogo kama yapi?”
“Uchawi na kurogana.” Alisema, nikabakia nimeduwaa nimeghafirika.

INGAWA kweli niliwahi kusikia habari za ushirikina katika mpira, lakini sikuwa mtu mwenye kuamini juu ya ukweli huo, kauli ya Edward Anthony ilinitingisha kwa kiasi chake.

Hivi haya mambo kweli yapo? Nilijiuliza kimyomoyo bila majibu.
Hata hivyo, sikutilia manani sana jambo hilo. Nikaendelea na vitu vyangu uwanjani. Mwisho wa mazoezi, makocha waliniita kando, wakaniambia:
“Tutakuwa na kikao na wewe, pamoja na mfadhili na mlezi wa timu yetu,
 
Sehemu ya 22

“Tutakuwa na kikao na wewe, pamoja na mfadhili na mlezi wa timu yetu, nenda upesi ukachukue mizigo yako kisha urudi hapa uwanjani twakungoja.”

Kocha aliniruhusu niondoke muda huohuo, wao wakabakia na wachezaji wengine pale uwanjani kwa ajili ya kuwapa mawaidha ya kimpira.

Kule kuniambia nikachukue vifaa vyangu katika gesti huku wao wakiwa wananingoja kuelekea katika kikao na mlezi wa timu hiyo, nikatambua, sasa nyota njema inanimulikia.

Kivyovyote vile , wale jamaa walivutiwa na kiwango changu, hivyo kuna jambo walikuwa wameliandaa kwa ajili yangu, kwa kweli nilifurahi mno, maisha yangu yalikuwa yanabadilika kwa kasi sana.

Niliteremka kule chini katika kioski cha Chado. Chado alinipungia mkono kunisalimia, wala sikuhaingaika na salamu yake, nilikuwa katika shauku kubwa ya kikao nilichoitiwa.

Nikatembea harakaharaka kuzifuata ofisi za idara ya maji, kisha nikachepuka na kuingia katika kichochoro kirefu kilichotenganishwa na jengo la idara ya maji na gesti hiyo.

Hatimaye nikatokea kwenye geti la kigesti kile, nikapitia funguo za chumba changu mapokezi, nikaelekea mbio mbio chumbani mwangu. Kwa wahaka niliokuwa nao, hata kuoga sikutamani, nilichofanya ni kubadili nguo zile za mazoezi, nikachukua begi, huyoo. Nikatimka zangu.

Niliporudi uwanjani, niliwakuta walimu wale wananingoja. Wachezaji wengine wote walikuwa wamekwisha tawanyika. “Uko tayari?” Kocha Gideon Nkisi aliniuliza

“Ndio.”
“Tuondokeni.”
Tulikwenda katika kituo cha basi, tukapanda daladala. Sikujua safari yetu ilikuwa wapi, ila ninachokumbuka, tulikwenda hadi sehemu moja inaitwa Mabatini, tuliposhuka kituoni, tukaetembea hadi katika hotel moja sio nzuri sana wala sio mbaya. Inaitwa Orange Tree.

Hapo tukachukua nafasi katika moja ya meza. Muda si mrefu akaja mwanaume mmoja mrefu mwembamba uso wake ulionesha ni mtu mkarimu na makini sana. Alionekana ni mtu mwenye fedha na cheo fulani serikalini.

Wale makocha walimlaki kwa heshima na unyeyekevu, alipoketi kitini utambulisho ukaanza.

“Mheshimiwa huyu anaitwa Ajibu Maganga ndiye mchezaji tuliyekueleza habari zake jana usiku. Anatokea mkoani Mara wilaya ya Serengeti.” Kocha alisema.
 
Sehemu ya 23

Kweli” Ntamasambilo aliuliza huku akinitupia jicho mimi, kisha kwa wale makocha.

“Kabisa...Ndio...Yeah..” makocha wote watatu walimuhakikishia maneno aliyoyasema mwenzao.

“Uwezo wake ni mkubwa kwa ngazi ipi?” jamaa akauliza tena.
“Hata ligi kuu, hakuna mchezaji anayeweza kumfikia Ajibu kwa uwezo alionao,” kocha alisema.

Jamaa alionekana kutoamini moja kwa moja maneno yale. Alinyanyua chupa ya wisk na kunywa funda refu, wakati pombe ile inaishia ndani ya tumbo lake, akauliza swali ambalo lilikuwa gumu kujibika kwa wale makocha.

“Sasa kama uwezo wake ni mkubwa kwa nini yupo huku? Kwa nini hayupo katika timu kubwa za ligi kuu? Anafanya nini huku mchangani?” aliuliza.

Wale makocha wakabakia wametoa macho kama mjusi aliyebanwa na mlango. Jamaa kuona wale wazee hawana jibu la kumpa, akanigeukia mimi na akaniuliza swali hilo hilo.

“Mazingira mheshimiwa, nilisema. Nikaendelea kujieleza.
“Nimetokea kwenye mazingira ambayo yalikuwa magumu kuonesha kipaji changu.” Nilimwambia.
Akatafakari kidogo kisha akauliza:

“Kwa hiyo shida kubwa mliyokuwa mnataka ni nini hasa?”
Kama timu itamshikilia huyu kijana, namwona ni mtu anatekaye ipa mafanikio na heshima kubwa klabu yetu, tatizo ni kwamba hapo alipo hana hata sehemu ya kuishi.” Kocha Gideon Nkisi alimwambia yule jamaa mwenye kuitwa Ntamasambilo Kabuye.

Kabla Ntamasambilo hajasema kitu, mara mhudumu akaja kumwita akimwambia kuna simu yake muhimu.. Akatutaka radhi akasimama na kwenda kusikiliza simu hiyo.

“Jamani ni mmiliki wa hii hotel, utapata hifadhi hapa, Ajibu, ondoa hofu,” Kocha Gideon aliniong’oneza.
Dakika tano badaye Ntamasambilo alirudi, safari hii hakuketi kitini alizungumza akiwa amesimama.

Jamani niwieni radhi nimepata simu muhimu hivyo inanapasa niondoke, lakini nimekwisha acha maagizo kwa wahudumu.

Bwana mdogo atapatiwa chumba katika hotel hii, chakula na nauli juu yangu.” Aliongea haraka haraka. Akauliza tena.
“Ligi inaanza lini?”
“Wiki ijayo.”
“Basi nitakuja kumwona kijana.”
 
Sehemu ya 24

Kikao kikaisha.
Basi kuanzia siku hiyo, nikawa naishi katika hotel ya Orange Tree iliyopo Mabatini jijini Mwanza. *****

Nilicheza mpira kwa mafanikio makubwa sana, kwa muda mfupi nilikuwa gumzo katika ligi daraja la nne, nilikuwa ndiye mshambuliaji ninaye ongoza kwa magoli mengi.

Timu yetu iikapanda hadi ligi daraja la tatu, tulipanda tukiwa vinara kwenye kundi letu. Wakati huohuo nikaanza kupata ofa kutoka katika vilabu vya ligi daraja la kwanza.

Mheshimiwa Ntamasambilo, ambaye badaye nilikuja baini alikuwa ni katibu tawala wa mkoa wa Mwanza, alikuwa akinipa posho na marupu rupu ya kutosha, sikuwa na haja na timu nyingine ila Igogo Fc. Katika timu ile mimi ndiye nilikuwa napewa posho ndefu kuliko mchezaji mwingine yeyote.

Niliishi maisha ya furaha jijini Mwanza. mimi na wachezaji wenzangu sambasamba na makocha wa Igogo Fc niliishi nao vizuri tu, kwa kweli nilikuwa mtu mwenye furaha kubwa maishani.
Msimu wa mwisho wa ligi daraja la tatu, timu yetu ikapanda tena Daraja na kuingia ligi daraja la pili. Mimi nikibuka kinara wa kupachika mabao.

Katika kipindi chote, nilikuwa sina habari na jambo lolote la kijijini kwetu Maji moto. Sikumkumbuka mke wangu, Pili, na mimba yake, nilimsahau kabisa mwanamke huyo.

Mwanamke huyo hakuwa chaguo langu, alikuwa ni mwanamke mzuri kwenye macho ya mwanaume mwingine, ila kwangu alipungukiwa sifa moja. Weupe. Nilikuwa sijiwezi mbele ya wanawake weupe.

Kwa bahati nzuri ama mbaya, mke wangu Pili alikuwa mwanamke mwenye sura ya kuvutia, na umbo la kuteka hisia za mwanaume yeyote. Alikuwa na nywele nyingi kichwani, matiti mazuri na miguu ya bia. Ila ngozi yake tu.

ilikuwa mweusi tii. Kutokuwa na hisia na mke wangu huyo, kulinipa kibali cha kutokumbuka lolote juu ya ahadi nilizompa kabla ya kuja mjini Mwanza, nilichokuwa nakihitaji mimi ni kuwa mchezaji mkubwa hapa nchini. Sio kuishi na pili.
 
Sehemu ya 25

Katika nyakati hizohizo za umaarufu wangu, huku nikiwa nimemfuta Pili mawazoni mwangu. Nilikutana na binti mmoja anaitwa Lawalawa, alikuwa ni msichana shombe, aliyechanganya Uafrika na Uarabu, alikuwa ni mkazi wa mjini Tabora, mjini Mwanza alikuja tu kwa ajili ya kusimamia miradi ya baba yake.

Lawalawa akiwa anaishi kwa shangazi yake ambaye nyumba yao ilikuwa mkabala na hotel ya Orange Tree ambayo nilikuwa nikiishi mimi, alikuwa ni moja ya watu waliokuwa wakisikia sifa zangu.
Siku moja wakati natoka katika mechi nikiwa nimekwisha fanya vitu vyangu.

Kumbe siku hiyo msichana huyo alikuwa ameamua kupunga upepo kwenye ile hotel. Wakati natoka chumbani nakwenda katika ukumbi kuangalia bendi iliyokuwa ikitumbuiza siku hiyo ndipo nilipomwona mrembo huyo.

Nilimfuata na kumsalimu, akanichangamkia na kunikaribisha kiti, sura yake ilikuwa ngeni machoni kwangu ila yeye alisema ananifahamu.

Katika maongezi ya hapa na pale tukajikuta mioyo yetu imeridhiana, kufumba na kufumbua tukajikuta tunaishia kitandani kwangu, ndani ya chumba cha hotel ya Orange Tree.

Kuanzia wakati huo moyo wangu ulikuwa haujiwezi kwa Lawalawa. Si Pili wala mpuuuzi mwingine yeyote. Lawalawa ndiye aliyegusa moyo wangu. Mpira na penzi la Lawalawa, likanifanya niwe miongoni mwa Watanzania wachache wenye furaha maishani.

Nakumbuka katika kipindi timu yetu inanatarajia kucheza ligi daraja la pili, Mheshimiwa Ntamasambilo alikwisha ona kwamba naweza kunyakuliwa na timu vigogo muda wowote. Alichofanya ni kunipa mkataba wa miaka miwili na mshahara mnono.

Kwa kweli kupitia mchango wangu, hata Cv ya kocha wangu Gedion Nkisi ilianza kujitengeneza. Walimu wale walivutiwa mno na kazi yangu. Timu yote ya Igogo Fc ilitengenezwa kunizunguka mimi uwanjani.

Nilipachika mabao kila nilipopata nafasi. Timu ikaongeza mashabiki, wakanipenda nikawa maarufu mithili ya moto wa kiangazi nyikani.

Mashabiki walinipachika jina la utani na kuniita Fowler, wakinifananisha na mchezaji wa zamani wa Liverpool aliyeitwa Robert Bernard Fowler.
 
Sehemu ya 26

Katikati ya ligi daraja la pili, mpenzi wangu lawalawa alinieleza kwamba, anataraji kurudi mjini Tabora kwa kuwa baba yake alikuwa amemwita akaongoze miradi yake huko, baada ya yeye kukumbwa na maradhi.

Siku ambayo Lawalawa anapanda treni kurudi Tabora nilikuwa mithili ya mgonjwa pale stesheni, nilimzoe mno mrembo wangu huyo. Ingawa tulikuwa tumekubaliana kwamba ningekwenda Tabora baada ya msimu kuisha, kiasi cha kama miezi mitatu ikiwa imesalia. lakini niliona ni kama mwaka mzima.

Nilibakia naiangalia treni hadi ilipopotelea machoni mwangu. Nikarudi hotelini kuanza maisha ya upweke bila Lawalawa wangu.

Maisha yaliendelea nikicheza mpira kwa ari na mori kubwa, mwisho wa ligi, timu yetu ikafuzu kupanda daraja, tukawa miongoni mwa timu zitakazocheza ligi daraja la kwanza.

Ilikuwa ni furaha kubwa, furaha kwa viongozi, furaha kwa mashabiki, wachezaji na wadau mbalimbali wa Igogo Fc. Zaidi ilikuwa ni furaha kwangu.

Siku mbili zilikuwa zimepita tangu sherehe za timu yetu kupanda ligi daraja za kwanza zimalizike katika ukumbi wa Tripol.

Asubuhi ya siku hiyo nilipanga kwenda kukata tiketi stesheni kwa ajili ya safari ya Tabora. Kwenda kuonana na mpenzi wangu Lawalawa.

Nilikuwa nimemkumbuka mno mrembo huyo
Nikiwa katika maandalizi chumbani kwangu, mara nikasikia mlango wa chumba ukigongwa, nikatambua labada ni wahudumu, mara nyingi asubuhi huwa wanakuja chumbani kwangu kufanya usafi. Bila wasiwasi nikasogelea mlango na kufungua.

Lahaulaaaa!! Sikuamini nilichokiona.
Mke wangu Pili akiwa na Chado, jamaa mwenye kioski kule Igogo, Walikuwa wamesimama wima kama mlingoti wa nguzo ya umeme.

Lilikuwa ni shambulio la ghafla mbele yangu, moyo wangu ulipiga kite baada ya kumwona mke wangu, Pili, alikuwa mbele ya mlango wa chumba changu kifuani akiwa amembeba mtoto mdogo. Nilitambua mtoto yule kivyovyote vile atakuwa ni ile mimba niliyomwacha nayo kijijini Maji moto.
 
Sehemu ya 27

“Pili!!” nilisema kwa mshangao. Mwanamke huyo akapiga tambo kubwa mbele yangu kisha akanikumbatia kwa furaha. Pili alionekana kuwa na furaha ya ajabu baada ya kunipata mume wake, niliona machozi ya furaha kijikusanya machoni mwake.

Niliwakaribisha ndani, moyoni nilikuwa sina raha. Sikupenda ujio wa mwanamke huyo. Amekuja kufanya nini? Ujio wake utavunja safari yangu ya kwenda kwa mpenzi wangu Lawalawa huko mjini Tabora.

Kutokuonana Lawalawa kwa sababu ya mpumbavu Pili, ilinichukiza mno. “Umefikaje hapa?” niliuliza huku nikiwangalia kwa zamu. Uso wangu ulikuwa na tabasamu bandia.

“Shemeji amefika kama ulivyofika wewe Ajibu, ni ajabu ” Chado alianza kueleza.
“Amekuja kwa kuulizia timu ya Igogo Fc, ilikuwa kama bahati tu, katika uliza uliza akaangukia bandani kwangu.

Alipouliza timu hiyo na kutaja jina la mtu amtakaye, ndipo nilipohamasika kumjua zaidi, maana wewe na mimi ni mwaswahiba bwana.

Shemeji alinieleza kwamba wewe ni mume wake na huyu ni mtoto wenu. Maneno hayo yalitosha kabisa kumleta shemeji hadi hapa ulipo” Chado alimaliza kueleza.

Nilimshukuru Chado kwa wema aliomfanyia mke wangu Pili, nikampoza fedha kidogo. Akaondoka. Baada ya Chado kuondoka kabisa, nikarudi kuzungumza na Pili.

“Eeh! Pili kulikoni mbona ghafla? Bila taarifa ” niliuliza. Uso wangu safari hii ukisawijika kwa hasira ya waziwazi.
“Ajibu!!” aliniita kwa taharuki, hakutegemea kama ningekuwa vile ghafla. Akaniuliza.

“Mume wangu, nimefanya makosa kukutafuta!” “Nipe majibu Pili.” Nilifoka.
Pili akazidi kunishangaa, hakuwahi kuniona katika uso wa chuki hata siku moja.

“Mbona umebadilika hivyo Ajibu tumefanya makosa kuja?”
“Kwa nini unakuja bila taarifa?”
“Taarifa ningeitoaje Mume wangu? ulipoondoka kijijini hukuniamba kama unakuja Mwanza, si ulisema unakwenda Bunda wewe.” Alisema.

Nilikosa cha kusema nikabaki nimevimba kama chatu. Kwa sauti ya upole Pili akaniambia:

“Ajibu nimemleta mtoto....” “Sababu ndio hiyo tu?” nilimkatisha. “Ajibu!!!.” Mke wangu alimaka
Nilimwangalia Pili kwa chati, nikaona sio wakati sahihi kulumbana na mwanamke yule. Nilimsogelea mwanangu na kumfunua kanga aliyokuwa amefunikiwa .
 
Khaaaa [emoji1787][emoji1787][emoji1787] toka lini we na story kwahiyo episode zote umeshamaliza
Nimemaliza zote mpenzi, mimi napenda mnooo kusoma tofauti na ulivyofikiri hahahahahahahah
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom