SEHEMU YA 52
“Don’t dare to lie to someone who knows the truth,” (usijaribu kumdanganya mtu anayejua ukweli) nilimwambia, akashtuka.
“Unamaanisha nini?”
“Ni msemo ulioandikwa na mtu fulani hivi, unamjua Boniphace Ngumije?” nilimjibu na kumuuliza.
“Yule mwandishi wa vitabu? Rafiki yako?”
“Ndiyo!”
“Ila maana yako nini?”
“Ni maneno tu! Naomba nikaoge kwanza,” nilimwambia, nikapotezea mambo hayo kwani tayari niliona alianza kubadilika na kuwa na hofu.
Nikavua nguo zangu, nikachukua taulo na kuelekea bafuni kuoga. Sikufichi, hakuna siku ambayo nilimuona Scaila akiwa amebadilika kama siku hiyo.
Alinywea, alikuwa akiniangalia huku akiwa na maswali mengi mno. Scaila ameniumiza sana, nadhani umeyasoma mambo yote ambayo yalitokea kati yangu na yeye, hivyo na mimi nikataka nianze kumuumiza nafsi yake, awe na maumivu, ateseke kila siku kwa kujiuliza juu ya nilichokuwa nikimwambia.
Nilichukua dakika kadhaa bafuni, nikatoka na kumfuata kitandani, alionekana kuwa mpole sana, wakati mwingine alikuwa akitoa tabasamu lakini nilijua kabisa halikuwa kutoka moyoni, lilikuwa tabasamu lenye maswali mengi nyuma yake.
“Unaifahamu muvi ya Acrimony?” nilimuuliza.
“Hapana! Inahusu nini?”
“Ni filamu ya maisha tu. Kulikuwa na jamaa alimpenda sana msichana, akamuahidi mambo mengi atakayoyafanya baada ya kumuoa, bahati mbaya wakaachana kwa talaka kabla mwanaume hajafikia ndoto zake za kuwa tajiri, hivyo yale yote aliyokuwa ameahidiwa, akapewa mwanamke mwingine,” nilimwambia, maneno hayo yakazidi kumtia hofu.
“Unanitia hofu!”
Nikatabasamu.
“Usijali! Ni muvi tu. Wakati mwingine unapopata nafasi ya kuaminika, kuahidiwa mambo mengi baada ya kuoana, usijali kuyaacha mambo hayo akafanyiwa mwanamke mwingine,” niliendelea kumwambia huku nikijifuta maji.
“Mh!”
“Scaila! Kuna wanawake wengi wanatamani kuolewa, wengine wanasaka ndoa mpaka kwa waganda, wanajichubua kwa kuamini wanaume wanapenda wanawake weupe, wengine wanatumia mpaka dawa za kichina kuongeza makalio....wanafanya hivyo kwa sababu wanahitaji ndoa. Unapofanikiwa kupata mwanaume anayekuahidi kukuoa, anakufanyia mambo mengi, achana na watu wengine,” nilimwambia, niliamua kumpa kadarasa kidogo.