Simulizi: Roho yake inadai

Simulizi: Roho yake inadai

Daah utamu umekatikia njiani Isee.
Bigup Steve wonder
 
*ROHO YAKE INADAI ---- 47*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Nani huyo?”

“Rafiki yangu.”

“We ni mwongo,” Olivia akasema akimtazama Brian machoni. Uso wake haukuonyesha masikhara hata kidogo. Brian kidogo akapata shaka.

ENDELEA

“Unadhani ni wa nani?” Brian akauliza. Olivia hakumjibu, akabaki akimtazama kwa macho yake ya ukali. Brian akajitengenezea vema kwenye kiti na kuuliza, “Olivia, upo sawa?” Bado Olivia hakujibu, aliendelea kumtazama Brian akikaza macho.

“Olivia,” Brian akaita. “Olivia! … hey, msichana!” akamchezeachezea Olivia mashavu. Olivia asijibu lolote, akaachana na Brian na kuketi kitini akitazama runinga. Brian akabakia na maswali kichwani kwamba nini shida.

Akanyanyuka na kwenda chumbani kuuhifadhi mkufu ule mahali salama tena, alipoufungia na kupaficha, kisha akarudi sebuleni. Hakumkuta Olivia. Runinga ilikuwa inawaka yenyewe sebule ikiwa pweke.

Akatazama jikoni, hakukuwa na mtu. Akaketi na kutazama kidogo runinga kabla hajamezwa na mawazo lukuki aliyokuwa nayo kichwani. Aliwaza siku yake nzima, namna alivyokutana na Wayde na kuona vitu ambavyo hakuwa anavitarajia. Pia alivyoongozana na Wisconsin kwenda kule kwa Dkt Hamill kuchimba kaburi.

Alioona ilikuwa ni siku ndefu, ila zaidi ya hapo, ni siku muhimu sana kwenye zoezi lao la kuhitimisha yale yanayotukia pale Boston. Lakini kama kuna kitu kilimshangaza na kumtia huruma, ni yale mahusiano ya mke wa Dkt Hamill. Aliwaza ni namna gani Dkt Hamill alivyokuwa anajisikia mpaka kumuua mkewe. Hakika lilimuumiza sana. Alijikuta akitikisa kichwa chake na kusonya.

Muda ukazidi kwenda akiwa hapo. Ikiwa inaelekea kuwa majira ya saa saba usiku, akaona ni kheri akapumzike sasa kitandani kwakuwa kesho yampasa kuamka asubuhi na mapema.

Akazima kila kitu na kuendea chumba chake kujilaza. Ila hakuwa amechoka kabisa, alishangazwa kwanini. Bado alijihisi mwenye nguvu na macho yake ni makavu. Hakuwa anahisi usingizi hata kidogo. Alifumba macho yake akigeukia huku na huko lakini hakulala. Alibaki akimtazama Wisconsin akiwa amesombwa na usingizi, anaunguruma kwa utamu.

Akajigeuza kutazama dari, pia dirisha na mara mlangoni, bado usingizi haukuja. Nao muda ukaendelea kusonga mpaka kufikia saa tisa, kimya, alikuwa ameshageukia kila pande anayoijua, akaweka kila mtindo anaoujua, usingizi haukuja.

Akiwa sasa amechoka kujaribu, na anawaza aidha aamke na kutumikia udadisi wake kusoma kitabu cha Wisconsin, akasikia sauti ya kitu huko nje. Alihofia kwanza kisha alipotulia ndipo akajua ya kwamba ni sauti ya mlango. Hapa akili yake ikampeleka moja kwa moja kwenye tukio la usiku wa kuamkia jana. Ina maana lile jaribio la kuuawa kwa Karen litakuwa linajirudia?

Haraka akatoka kitandani na kuufuata mlango. Aakafungua taratibu na kuchungulia koridoni. Macho yake yakaona mlango wa chumba cha Olivia ukiwa wazi, kabla hajajiuliza, akaona tena mlango wa chumba alalacho Karen ukiwa unafunguka na kuwa wazi.

Akabaki akishangaa. Nani anafungua milango hiyo? Macho yalimtoka akiwa anatazama kwa umakini nini kinaelekea kutokea. Kukawa kimya. Hakuona kitu wala mtu. Zikapita kama sekunde sita.

Kidogo, milango ile iliyofunguka ikaanza kucheza, ikaenda mbele na kurudi nyuma. Ilianza kucheza taratibu lakini kadiri na muda ulivyokuwa unaenda kasi yake ikawa inaongezeka. Brian akashagaa ni nani anayeisukuma milango hiyo.

Kidogo tena, kule sebuleni mapazia ya dirishani yakaanza kupepea. Hakukuwa na upepo wowote ule. Lilikuwa ni jambo la kushangaza kwa Brian. Alikunja sura yake akijiuliza ni nini kinachotokea. Ghafla vitu vyote vikakoma ndani ya sekunde kana kwamba vimekatazwa mara moja! Brian akaendelea kushangaa.

Kwa macho yake akauona mkono wa mtoto ukichomoza toka mlangoni ukiwa umebebelea kisu. Ukatokea pia na mkono mwingine, wa pili, ambao ulinyooshea kidole kwenye mlango wa chumba cha Karen. Mara kidole hicho kikafanya ishara ya kukataza kwa kwenda kushoto na kulia alafu kikamnyookea Brian!

Brian akatahamaki. Kufumba na kufumbua, akatoka Olivia akiwa aonekana kama kivuli. Macho yake yalikuwa yanawaka kama gololi iliyomulikwa kurunzi. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea kisu na ule wa kushoto ukiwa mtupu.

Akamnyooshea kidole Brian, alafu akatikisa kichwa chake mara tatu kisha akaanza kusonga taratibu kumfuata kijana huyo. Brian akarejea upesi ndani ya chumba chake na kufunga mlango kwa komeo, alafu akatulia hapo kusikiza nini kitatukia.

Kukawa kimya. Hakusikia sauti ya kitu chochote isipokuwa moyo wake uliokuwa unapiga kwa kasi. Alimtazama Wisconcosin akamwona bado amelala, hana habari, akaona ni kheri akamwamsha na kumjuza yanayoendelea.

“Bwana Wisconsin!” Brian akaita. “Amka uone kinachojiri!”

Hola! Wisconsin alikuwa amelewa usingizi. Hakuwa anasikia lolote isipokuwa utamu wa usingizi. Brian akamsukuma na kumvutavuta. “Amka!” akapaza sauti. “Amka, Wisconsin!” Alistaajabu ni usingizi wa aina gani uliokumba bwana huyo. Hakuwa anasikia wala kuelewa.

Kidogo, Brian akaanza kusikia mlango ukigongwa - tih!-tih!-tih! - na sauti ya kike ikaimba kwa kutetema, “Brian, toka tucheze. Hakika utafurahi. Brian … Brian, toka tucheze.”

Brian akaendelea kumshtua Wisconsin pasipo mafanikio. Akatazama kushoto na kulia kwake kama atapata dhana ya kujitetea. Akanyanyuka na kufuata mahali aliporundika nguo zake, akafukua na kutoa gongo la bati, akalishika vema kujihami.

Kimya. Hakusikia tena ile nyimbo ikiimbwa wala mlango kugongwa. Kulikuwa ni kimya, akisikia pumzi yake ikihema kwa upesi.

Akasonga taratibu kuufuata mlango wake na kutulia hapo kidogo. Akaweka sikio lake mlangoni kuskiza. Hakusikia kitu. Kidogo kabla hajatoa sikio hapo, akasikia sauti ikimnong’oneza, “toka tucheze, Brian. Au niende kucheza na Karen, na kisha mama yako?” baada ya kusema hivyo sauti hiyo ikachekea kooni.

Haraka Brian akafungua mlango na kutazama nje kwa tahadhari ya gongo lake. Alitazama kushoto na kulia. Mikono yake yote ilikuwa imeshikilia gongo lake kwanguvu. Hakuona kitu. Akiwa anasonga kuelekea kwenye milango ile miwili ambayo ipo wazi, akawa anatupa macho yake aliyoyakodoa.

Kumbe Olivia alikuwa darini. Alikuwa amejishikiza katika namna ya ajabu akimtazama Brian anayetembea kwa hatua za pole. Brian aliposonga akiwa amebakiza hatua chache kuufikia mlango wa Karen, Olivia akaanguka toka darini na kumvamia, akamdondosha chini!

Akamchoma Brian kisu cha ubavuni. Brian akapiga kelele kali za maumivu. Akatupa kiwiko chake kwanguvu kikamkita Olivia usoni, Olivia akadondokea kando. Brian akajivuta mbali na Olivia kisha akatazama jeraha lake. Lilikuwa linamwaga damu. Alikuwa anasikia maumivu makali sana.

Olivia akalamba damu kwenye kisu kisha akatabasamu na kusema kwa sauti yake ya ajabu, “ni tamu mno, Brian. Nataka tena!” akanyanyuka na kuanza kumfuata Brian kwa kasi. Akaruka juu akitaka kumkita, upesi Brian akamzaba kichwa kwa gongo lake. Alimzaba kwanguvu mno mpaka damu kuruka. Olivia akatupiwa ukutani na kudondoka chini akiwa amelala kifudifudi, akatulia tuli.

Brian akamtazama kwa mashaka. Akanyanyuka akiwa ameuweka mkono wake wa kushoto kwenye jeraha kuzuia damu zisitoke zaidi. Akahema akimtazama kile kiumbe. Amekufa ama amezirai? Akajiuliza.

Kidogo, akasikia sauti ya Olivia akigugumia, mara akaanza kulia. Alikuwa akilia akivuta makamasi na kubanwa na kwikwi. Sauti yake ya kulia ilikuwa ndogo ila kwakuwa usiku sauti husafiri kiwepesi, Brian aliisikia vema.

Olivia akalia kwa takribani sekunde tano kisha sauti yake iliyobanwa na kilio ikauliza, “Nimekukosea nini Brian kuniadhibu kiasi hiki?” Mara hii sauti ilikuwa ni ya Olivia tunayemjua. Sauti ndogo ya kike ya msichana asiye na makosa. Sauti inayotia huruma.

Basi Brian akashikwa na kigugumizi, akaita na kuuliza, “Olivia, ni wewe?” Olivia akaendelea kulia asijibu. “Olivia, tafadhali niambie, ni wewe?”

“Nimeumia sana, Brian!” Olivia akalalamika kwa sauti yake ya kike. “Siuhisi uso wangu kabisa. Wote umejawa damu.”

“Nisamehe, Olivia,” Brian akasema akisonga. “Sikudhamiria kukuumiza, nilidhani ni mtu mwingine amekuingia.”

Olivia akaendelea kulia na kugugumia, akivuta makamasi na kuguna.

“Nisamehe, Olivia,” Brian akaendelea kuomba akisonga karibu. Moyo wake ulikuwa wa baridi kwa majuto. Alipomkaribia Olivia, akainama na kumshika bega. Upesi Olivia akaamka na kumzaba Brian kofi kali, Brian akadondokea chini! Kabla hajaamka, Olivia akawa tayari amekaa juu yake, akacheka na kusema kwa sauti yake ya awali, sauti ya ajabu, “We ni mpumbavu, Brian!” kisha akanyanyua mkono wake wenye kisu kumkita, ila ghafla akaganda. Akatazama kushoto na kulia kwake akinusanusa. Mara akanyanyuka na kwenda zake chumbani mwa Brian.

Brian akamtazama akiishilia humo. Macho yake yalikuwa hayaoni vizuri kwasababu ya kofi alilozabwa. Nacho kichwa kilikuwa kinamgonga haswa upande wa kulia alipoadhibiwa.

Olivia alielekea mahali ambapo Brian alikuwa amerundika nguo zake. Hapo kwa chini kulikuwa kuna kaki ‘container’ kadogo ka chuma kalichondoka na kukaa wazi. Kumbe Brian wakati anachukua lile gongo lake, alidondosha kifaa hicho pasipo kujua.

Olivia akainama na kutwaa mkufu ule alafu akaubania kiganjani mwake na kusema, “Mama.”



**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 48*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Olivia alielekea mahali ambapo Brian alikuwa amerundika nguo zake. Hapo kwa chini kulikuwa kuna kaki ‘container’ kadogo ka chuma kalichondoka na kukaa wazi. Kumbe Brian wakati anachukua lile gongo lake, alidondosha kifaa hicho pasipo kujua.

Olivia akainama na kutwaa mkufu ule alafu akaubania kiganjani mwake na kusema, “Mama.”

ENDELEA

Akaubusu mkufu ule na kisha akarejea kule koridoni. Hakumkuta Brian. Kugeuka nyuma, akapigwa kwanguvu na gongo, akadondoka chini akiwa amepoteza fahamu. Brian akatokea nyuma yake na kumtazama. Akampokonya kisu na kumgeuza akimkagua.

Akamwona mkononi akiwa na ule mkufu. Akauchukua na kuuweka ndani ya mfuko wake kisha akambeba na kumrejesha chumbani. Akamfunga kamba mikono na miguu kisha akamlaza kitandani. Alipomaliza, akaendea ‘first aid kit’ na kujipa huduma ya kwanza. Akajimiminia dawa ya kukata damu na kuua wadudu alafu akajifunga bandeji.

Akarudi chumbani na kujaribu kumwamsha Wisconsin. Bwana huyo akaamka. Brian akamweleza yaliyotokea. Wisconsin akastaajabu. Alah! Yote yametokea akiwa amelala! Akaamka na kwenda kumtazama Olivia kisha akarejea kwa Brian.

“Utakuwa upo sawa kweli?” akamuuliza.

“Ndio,” Brian akamtoa shaka. “Nipo sawa, asubuhi nitaenda hospitali.”


**


Asubuhi ya saa mbili, Brian akiwa kitandani mwa hospitali.

Mama aliongea kidogo na daktari kisha akaja kukutana na Brian. Akatabasamu na kusema, “Pole sana, mwanangu.” akamshika Brian nywele akitabasamu.

“Daktari amesemaje?” Brian akauliza.

“Amesema tunaweza kwenda. Jeraha halijasababisha maafa makubwa. Kuna dawa za kutumia … na pia amehasa upumzike ili urudi upesi kwenye hali yako.”

Brian akaigiza kutabasamu alafu akauliza, “Wisconsin bado yupo?” Mama akatikisa kichwa. “Hapana, ametoka kidogo. Ila alisema atarejea muda si mrefu.”

Alipomalizia hiyo kauli yake, Brian akamwona Wisconsin akiwa amesimama dirishani. Alikuwa tayari amesharejea. Mama akaenda kuongea naye na muda mfupi, Wisconsin akaingia ndani kukutana na Brian.

“Unaendeleaje, mshindi?”

“Niko sawa. Nadhani nastahili tu kurudi nyumbani.” Wisconsin akatabasamu. “Mama yako anaona uendelee kubaki hapa mpaka upone kabisa.”

“Haitawezekana,” Brian akatikisa kichwa, Wisconsin akaangua kicheko. “Mimi siwezi kulala humu hospitali, unajua Wisconsin. Tuna mambo mengi ya kufanya. Inabidi umwambie Mama hilo.”

“Usijali,” Wisconsin akamtoa hofu. “Kila kitu kitakuwa sawa, Brian. Unajua nini?”

Brian akamtazama Wisconsin kwa kuitikia.

“Kama ingekuwa ni kufa, basi ungeshakufa Brian. Tena muda sana. Mungu yupo upande wako.” akamshika Brian mkono na kumtazama machoni. “Utashinda hata na hili.”

Brian naye akamshika mkono na kumwambia, “Tutashinda wote.” Wisconsin akatabasamu pasipo kutia neno. Brian akamuuliza, “Kuna lolote ambalo umegundua?”

Wisconsin akakuna pua yake na kushusha pumzi ndefu kisha akajitengenezea pale kitandani alipokuwa amekaa. Akaita, “Brian.” Brian akaitikia kwa kuguna. “Olivia ndiye yule mtoto wa mwisho wa Dkt Hamill.”

Habari hizi hazikumshangaza sana Brian. Ni kama vile alikuwa anazitarajia. Matukio ya Olivia, na zaidi juu ya ule mkufu yalimtia mashaka. Akauliza, “Sasa tunafanyaje? Kutakuwa na shida yoyote?”

“Ndio, shida ipo tena kubwa,” Wisconsin akajibu na kuongeza, “Olivia, Brewster pamoja na Alfonso, wote ni mali ya Helo. Wote walitolewa sadaka kumtumikia mdhalimu huyo. Nadhani utakuwa ushajua ni shida kiasi gani.”

“Hatuwezi kulibadili hilo?” Brian akauliza. Wisconsin akabinua mdomo wake na kusema, “Haiwezekani, Brian. Pumzi yake, maisha yake ni mali ya Helo. Wapo hapa duniani kutimiza maagizo hayo. Laiti Helo angelikuwa hajaamka, basi wangelikuwa sawa. Wangeweza kuendelea na maisha yao pasipo bughudhi ya watu.”

Brian akatazama pembeni kwa mafikirio, alafu akaurudisha uso wake kwa Wisconsin na kuuliza, “Ina maana hamna kabisa namna?” kabla hajajibiwa, akaongeza, “Olivia ni msichana mzuri sana. Natamani angelikuwa kwenye ulimwengu wetu.”

Wisconsin akamshika mkono na kumminya kidogo. “Najua, Brian. Hata mimi natamani ikawa hivyo … ila tutafanya kadiri ya uwezo wetu.” Brian akanyamaza. Kuna jambo alikuwa anawaza kichwani. Wisconsin akamtazama na kumwambia, “Inabidi unyanyuke hapa tukaonane na yule binti. Sawa?”


**


Saa nane mchana, nje ya uzio wa shule …

Wanafunzi walikuwa wanatoka kwenda majumbani. Kandokando ya geti, alikuwa amesimama Brian pamoja na Wisconsin. Walikuwa wanatazamia wanafunzi wapungue ili wazame ndani.

Baada ya muda kidogo, wakaingia na kabla hawajaenda mbali wakaliona gari la Wayde likiwa linasonga kwenda zake. Brian akalipungia mkono na kwenda moja kwa moja kulifuata.

Wakaingia ndani ya gari, Wayde akaendesha kuacha nyuma shule. Alipotembea kwa dakika kadhaa, akaegesha gari kando na kumtaka Brian amwelezee kinachoendelea.

“Huyu ni Wisconsin, yeye ni mtaalamu wa yale mambo tuliyokuwa tunayazungumzia. Anahitaji kuona vile vitu ulivyonionyesha jana.”

Wayde akamtazama Wisconsin na kumsalimu, kisha akarejesha uso wake kwa Brian na kumwambia, “sidhani kama itawezekana, Brian.”

“Kwanini?”

“Leo baba anarejea tokea Carolina. Hapa tuongeapo, yupo safarini kurudi. Ni hatari!” Wayde alizungumza akiwa amekodoa macho. Wisconsin akaingilia maongezi,

“Kama kuna nafasi, basi ni hii! Yatupasa kufanya kila jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wetu. Tukishindwa leo, basi tutakuwa tumeshindwa milele. Kitakuwa ni kiama cha Boston.”

Brian akamtazama Wayde. Wakatazamana kwa kama sekunde tatu kisha Wayde akashusha pumzi ndefu na kutazama mbele akiwa ameshika usukani. Akakuna kichwa chake kwanguvu. Akatulia kwa muda kidogo na kusema, “Sawa.”

Alafu akawatazama wageni wake na kuwaambia, “ila sitaweza kwenda nanyi wote.”

“Sawa,” Wisconsin akaitikia. “Nenda na Brian!” bado Wayde akawa anasita. Alilaza kichwa chake kwenye kiti akiwaza, mwisho wa siku akasema yampasa aende mwenyewe.

“Ni hatari kwenda na yeyote. Mama yu nyumbani pamoja na wageni wengine. Endapo nikirudi na yeyote, basi italeta shida. Naomba niende mwenyewe.”

Brian akamtazama Wisconsin.

“Sawa,” Wisconsin akajibu na kuongeza, “Basi itabidi twende kwanza nyumbani.”

Wakaelekea nyumbani kwa wakina Brian, Wisconsin akampatia Wayde kitabu chake cha maarifa na kumwelekeza cha kufanya pindi atakapokuwa karibu na maiti zile zilizotiwa komeoni. Alipomaliza na Wayde kujiridhisha kuwa ameyashika maelekezo hayo, akaenda zake.

Wakamtazama msichana huyo akiishia.

“Unadhani ataweza?” Brian akauliza wakiwa wanatazama barabara.

“Ataweza,” Wisconsin akamjibu. “Anaonekana ni msichana mwerevu sana, pia mwenye kujiamini … nadhani ataweza.”

Brian hakuongeza neno. Aliendelea kuangalia barabara. Wisconsin akamtazama na kumwambia, “inaonekana anakupenda sana.”

“Kwanini?” Brian akamuuliza akimtazama. Wisconsin akatabasamu na kumshika bega, “Ameyafanya haya kwakuwa anakupenda. Si kingine.”


**


Saa kumi jioni …


Baada ya kutazama mazingira na kuyaona yapo salama, Wayde alizama ndani ya chumba cha wazazi wake na kuiba ufunguo, kisha akanyata kutoka, na upesi akakimbia kupandisha kule juu ilipo maktaba. Akafungua mlango wa kwanza, akazama ukumbini, akaufungua tena ule wa pili, wa siri, akazama ndani, kisha akaelekea ile miili ya wafu.

Hapo akaitazama, akavuta na kushusha pumzi ndefu kisha akayafumba macho yake na kunyamaza kwa sekunde tano. Akivuta hewa na kushusha. Kabla hajafungua mdomo wake kunena, akasikia honi huko nje! Akashtuka na kukurupuka.

Akatoka ndani ya chumba kile upesi na kurudi kule maktaba kutazama kupitia dirishani. Akaona gari la baba yake likiingia ndani. Kwa uhakiki zaidi, akangoja mpaka amwone akishuka. Kweli akamwona. Baba yake alikuwa amerudi.

Sasa afanyaje? Aache kufanya ile kazi arejee chumbani ama? Akahisi kichwa kinamuuma. Alipotaka kuondoka, akakumbuka yale maneno ya Wisconsin, ni leo ama milele! Hapo akajihisi kukanganyikiwa. Kwa muda akawa amesimama kana kwamba kuku mwenye homa.

Haraka akakurupuka na kwenda kule kwenye kile chumba, akajifungia ndani na kuendea ile miili iliyokufa. Hapo akafumba macho yake na kutulia. Akazivuta pumzi ndefu na kuzishusha, kisha baada ya muda akaanza kunena maneno kwa kunong’oneza.

Alipoyasema maneno hayo, akaweka kiganja chake kwenye kioo. Kabla hajaendelea kusema tena, akasikia sauti ya mlango wa maktaba ukifunguliwa. Moyo ukampasuka. Akasikia vishindo vya miguu, na mara mlango wa chumba alimo ukafunguliwa. Uso kwa uso na baba yake!


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 49*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Alipoyasema maneno hayo, akaweka kiganja chake kwenye kioo. Kabla hajaendelea kusema tena, akasikia sauti ya mlango wa maktaba ukifunguliwa. Moyo ukampasuka. Akasikia vishindo vya miguu, na mara mlango wa chumba alimo ukafunguliwa. Uso kwa uso na baba yake!

ENDELEA

"Wayde," baba akaita akiwa ametoa macho. Akatazama kushoto na kulia ndani ya chumba alafu akarejesha macho yake kwa Wayde. Sasa yakiwa yamejawa na hasira. Akauliza, "unafanya nini huku, Wayde?"

Wayde angejibu nini? Hakuwa na cha kusema. Alijihisi mdhaivu. Mwili unamtetemeka haswa. Alihofu ni nini ambacho baba yake atamfanya. Akasema kwa kutia huruma, "nisamehe, baba. Sitarudia tena kutazama vitu vyako!"

Kabla baba hajasema jambo, akakagua kwanza chumba chake. Kwa macho yake kana kwamba kamera akabaini ya kuwa Wayde alikuwa amepachika kiganja chake kwenye kioo kilichokuwa kimehifadhi zile maiti.

"Wayde, umeanza lini kuja huku?" Akauliza.

"Ni leo tu," Wayde akajitetea akiapa. "Sijawahi kuja humu siku nyingine isipokuwa hii!"

Baba akamtazama, kisha akaufunga mlango kwa funguo.

"Kuna yeyote ambaye umemwambia kilichomo humu?" Baba akauliza. Wayde akatikisa kichwa upesi, "hapana! Hamna anayejua. Hata mama hajui!"

"Una uhakika?" Baba akauliza. Ungemtazama vema kwenye paji lake la uso alikuwa anachuruzwa na jasho.

"Ndio, nina uhakika, baba! Sijamwambia mtu!"

"Niambie ukweli mwanangu, nani aliyekutuma?" Baba akauliza akimsongea Wayde karibu. Wayde akaogopa maradufu. Akaanza kusonga kurudi nyuma akihofia uhai wake. Hakuwahi kumwogopa baba yake hata siku moja, ila siku hii ilikuwa tofauti. Kila kitu kilikuwa tofauti. Kila baba yake alipokuwa anamtazama, alihisi mapigo yake ya moyo yameamia masikioni kwa namna yanavyokita.

Na zaidi alipokuwa anamsogelea ndiyo akahisi kabisa anaelekea kufa. Kama angeliweza kupotea kimazingara hapo, basi angelishapotea.

Baba akamdaka koo. Akamtazama kwa macho yanayoogofya akisema, "Umeenda mbali ya mipaka, Wayde. Sina budi kukumaliza!" Akamminya koo kwanguvu, Wayde akiwa anapapatika, akapapasa meza aloegemea, mara mkono wake wa kuume ukadaka 'vase' nzito rangi ya zambarau.

Hakujiuliza mara mbili akampachika nayo baba yake kichwani, paah!! Baba akalalamika akimimina damu. Akatazama kiganja chake, kilikuwa kimelowa damu. Akamtazama Wayde kwa hasira pomoni, ila hakukaa vema, akabamizwa tena na vase ya pili. Sasa akawa mlegevu, mtepetevu, akadondoka chini na kutulia tuli.

Wayde akashika mdomo wake na kukodoa macho. "Mungu wangu, nimefanya nini hiki?" Alihisi ameua. Aliinama na kumgeuza baba yake, kisha akaweka mkono wake kifuani kuhisi mapigo ya moyo. Alipohisi yapo sawa, angalau akahema.

"Ahsante, Mungu!"

Baba alikuwa anahema kwa mbali. Kichwa chake kilikuwa kinavuja damu taratibu toka kwenye majeraha. Macho yake hakuwa ameyafumba, bali yanayorembua. Alikuwa anamtazama Wayde akimwona kwa mbali, akimwona kimaruweruwe.

Mwili wake haukuwa na nguvu ya kupambana tena. Kichwa kilikuwa kinamgonga akijihisi mzigo.

"Samahani, baba. Inabidi nifanye hivi kwa ajili ya Boston!"

Jicho la kulia la baba yake likadondosha chozi. Akamfuta kwa kiganja chake na kisha akakiendea kile kioo kinachotunza wafu. Kabla hajaanza kunena, akamtazama baba yake alafu akanong'ona, "Samahani, baba."

**

Saa kumi na mbili na robo ...

Wisconsin alitazama saa yake ya mkononi alafu akaminya lips zake. Brian akamtazama na kumuuliza, "ni muda mrefu, sio?" Wisconsin akashusha pumzi ndefu na kusema, "kutakuwa kuna kitu, si bure. Si zoezi la kuchukua muda wote huo!"

Brian akashika tama, "ilinipasa niende naye, tumempa mzigo mku--" akakatishwa na sauti ya gari huko nje. Upesi wakatoka kuelekea huko. Alikuwa ni Wayde!

Alishuka kwenye gari upesi na kumkimbilia Brian akiwa analia. "Pole, Wayde." Brian akambembeleza. "Usijali, yatakuwa sawa."

Wayde akalia kwa kama sekunde sita, alipojibandua toka kwenye bega la Brian akajifuta machozi kwa kutumia mikono ya sweta alilovaa, kisha akasema, "nimefanikisha!"

"Kweli?" Brian akatahamaki. Wayde akatikisa kichwa, "kweli Brian."

"Hongera sana!" Wisconsin akampongeza, "sasa twende ndani haraka!" Wakazama ndani na upesi wakaelekea chumbani kwa Brian kuchukua kile kitabu cha Wisconsin. Ajabu walipofika, hawakukiona!

"Kilikuwa hapa!" Alisema Wisconsin akiangaza kwenye kabati dogo linalopakana na kitanda. Akafungua droo zote, hamna kitabu!

"Atakuwa kachuku--" Wisconsin alisema na kusita. Haraka akanyanyuka na kwenda chumba cha Olivia, huko wakakuta kamba zikiwa kitandani, hamna mtu.

"Tumtafute Olivia!" Wisconsin akasihi akiwa aliyechanganyikiwa. Kidogo, wakasikia mlango ukibamizwa. Wakatazamana. Upesi wakatoka chumbani kuelekea huko. Walipofika, wakamwona Olivia kwa mbali akiwa anakimbia! Mkononi alikuwa amebebelea kitabu.

"Yule kule!" Wisconsin akapayuka. Basi haraka Brian akaanza kutupa miguu yake kwa fujo kumkimbiza Olivia. Kasi ya Wisconsin na Wayde ilikuwa hafifu kwake. Alikuwa anakimbia mno karibia visigino viguse kisogoni!

Akawa anamkaribia Olivia zaidi na zaidi, na huku akiwa amewaacha wenziwe huko nyuma wasionekane kabisa. Kidogo, Olivia akazama msituni na kuanza kupotelea humo. Naye Brian alipopiga kwanja, akazama mitini. Huyo! Huyo! Akimkimbiza Olivia anayepepea kama kishada.

Akaruka viunzi, matawi na vichaka, akaendelea kukimbia! Akazidi kumsogelea Olivia zaidi na zaidi ya zaidi. Kwa makadirio isingepita sekunde nne angekuwa ameshamtia Olivia mkononi, ila ghafla, mguu wake ukadakwa na mzizi wa mti, akachumpa na kudondoka chini kama kifurushi!

Akaguguma kwa maumivu akishika tumbo. Kutazama mbele, Olivia akasimama na kumcheka, alafu akaendelea kukimbia akiyoyomea msituni! Brian akapoteza matumaini.

Olivia akakimbia kwa takribani dakika moja, akatokezea barabarani, upesi akivuka, aendelee kuzama msituni, akasombwa na gari kwanguvu! Tiih!! Akarushwa na kudondokea mbali, puh! Kisha akatulia tuli kama kiroba cha mchanga. Kitabu kilirushwa mbali kabisa na yeye. Kikiwa huko kikawa kimejifungua kwa shurba.

Kwenye gari akashuka Wayde na Wisconsin.

"Yu wapi, Brian?" Wayde akaangaza. Haraka Wisconsin akafuata kitabu chake na kukitia kwapani. Wakatazama kushoto na kulia kumtafuta Brian, punde Wisconsin akamwona akiwa anajikongoja.

"Yule kule!" Akajikuta akiropoka. Wayde akamkimbilia na kumkumbatia kwanguvu. "Upo sawa?" Brian akatikisa kichwa kuitikia.

"Mmepata kitabu?" Akauliza.

"Ndiyo, tumekipata!" Wayde akamjibu kwa tabasamu. Wakajikongoja kufuata gari waondoke zao, lakini kabla hawajaingia, Brian akatumbua macho na kusema, "Ona, anaamka!"

Wisconsin na Wayde walipotazama wakamwona Olivia akisimama. Viungo vyake vilikuwa vimevunjikavunjika, amejawa na damu mwili mzima. Hata sijui aliwezaje kusimama katika namna ile. Ilikuwa ni ajabu. Akiwa amegeukia mbele, akageuza shingo yake nyuma kuwatazama wakina Brian, alafu akapunga mkono wake na kutabasamu.

"Ingia ndani ya gari!" Wisconsin akahadharisha. "Fanya upesi! Upesi!" Wakazama garini na kufunga milango. Wayde akawasha gari na kulirejesha nyuma kwa kasi, Olivia akaanza kulikimbiza!

Alikimbia akipindapinda ila mwendo wake ukiwa ni wa kasi mno! Wayde kutengenezea gari wageukie walipotokea, Olivia akawa ameshafika, akarukia darini mwa gari na kung'ang'ania huko.

Wisconsin akamsihi dereva, "Endesha! Endesha!" Gari likatimuliwa kwa fujo. Likashika lami na kukaa humo vema, likaenda kwa kasi, kwa mrama!

Wayde alilipeleka kushoto na kulia, kushoto na kulia. Bado Olivia alikuwa darini. Akalichochea kwa usawa, kisha akaminya breki kali, hapo Olivia akatupiwa kwa mbele kama mzigo, ila ajabu mikono yake ikawa imebaki imeng'ang'ania dari!

Wayde hakupoa, akaminya mafuta na kumsigina kiumbe huyo. Kama haitoshi, akarudisha tena gari nyuma na kumkanyaga, kisha akapeleka tena mbele na kumkanyaga. Olivia akawa chapati!

Wakatoka zao msituni.

**

"Ni lazima usiku huu uwe wetu!" Alisema Wisconsin. Alifungua kitabu upesi Brian na Wayde wakiwa kando, na mara kidogo Mama Brian akaungana nao akitokea chumbani.

"Karen yupo wapi?" Brian akauliza.

"Hajarudi tokea kazini," Mama akamjibu akiketi. Wisconsin akawaagiza walete mshuma na wafunge madirisha na milango yote. Maagizo yake yakatiiwa upesi basi akaanza kusoma kile alichokuwa anakitazama kwenye kitabu.

**

Bado kulikuwa kimya ndani ya chumba. Hakuwa amepata msaada wowote tangu mwanaye, Wayde, amwache hapo chini. Macho yake yaliyokuwa yanarembua yalikuwa yanatazama kile kioo kilichohodhi miili ya wafu. Hakuwa anayatoa macho hapo. Hata alipoyafumba, akayafumbulia papo hapo

Ni kana kwamba kuna kitu alikuwa anangoja.

Akiwa anaendelea kutazama, mara akaanza kuona kioo hicho kikichipua ufa! Akakoroma akitaka kusema jambo lakini hakuwa anaweza. Kioo kikaendelea kuchipua ufa zaidi na zaidi. Na mmoja wa mwili uliokuwemo ndani ukaanza kujigusa. Ukachezesha kidole!

Ukafuatiwa na mwingine, ukachezesha jicho!

**
 
*ROHO YAKE INADAI -- 50*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Akiwa anaendelea kutazama, mara akaanza kuona kioo hicho kikichipua ufa! Akakoroma akitaka kusema jambo lakini hakuwa anaweza. Kioo kikaendelea kuchipua ufa zaidi na zaidi. Na mmoja wa mwili uliokuwemo ndani ukaanza kujigusa. Ukachezesha kidole!

Ukafuatiwa na mwingine, ukachezesha jicho!

ENDELEA

Baba yake Wayde akatamani kunyanyuka azuie anachokiona, ila hakuwa anaweza. Hata kusogeza tu mwili wake ulikuwa ni mtihani, angewezaje kunyanyuka? Akabaki akigugumia, macho yakimtoka machozi zaidi na zaidi kutengeneza mto. Ni punde, kioo kikavunjika na wale walio wafu wakawa wazima!

Wakasimama kwa miguu yao. Wakatazama kwa macho yao! Ajabu ni kwamba viumbe hivi havikuwa vikipumua, wala mapigo yao ya moyo hayakuwa yanaita. Miili yao ilikuwa ya baridi na macho yao yalitingwa na mboni zenye rangi ya maziwa yaliyoharibika.

Wakamtazama yule mzee pale chini, wasiwe na habari naye, wakajiendea isijulikane wapi wanaelekea.

**
Wakiwa wameshikana mikono, kwa pamoja wakamalizia kusoma kifungu cha mwisho ambacho Wisconsin alielekezea. Wakiwa wanasoma kifungu hicho, mshumaa ukaanza kufifia, mapazia yakapeperuka kwa upepo, na milango ikaanza kucheza yenyewe.

Hawakukoma, wakamaliza kusoma kabisa, kisha Wisconsin akamchanja Brian kidole gumba na kuchuruzia damu kwenye ukurasa ule waliokuwa wameusoma. Ajabu pakaanza kufuka moshi mweusi karatasi likijifinya kuwa jivu.

Moshi huo Brian alipoutazama kwa sekunde kadhaa, akahisi anapoteza akili yake. Akahisi anapotelea moshini. Hata mwili wake ukaanza kupungukiwa nguvu. Alijishangaa kichwa chake kikidondoka kwa uzito na kujikuta chini!

Akiwa anapata fahamu, akasikia sauti za wadudu, na ngozi yake ikahisi kukalia majani. Akafungua kope zake nzito na kuangaza. Alikuwa kizani, na zaidi alikuwa msituni!

Akanyanyuka upesi na kutupa macho yake huku na kule. Akavuta pumzi ndefu na kujikuna kwa kuwashwa na majani, kisha akaanza kusonga kufuata mwanga anaouona kwa mbali.

Alipotembea kwa dakika tatu, akahisi kuna mtu nyuma yake, upesi akageuka kuangaza. Hakuona mtu! Ni miti ilikuwa imesimama tuli, miti meusi!

Akavuta pumzi ndefu na kusonga na safari. Akatembea tena kwa takribani dakika mbili, akahisi mtu akikatiza kwa mara nyingine! Alipogeuka na kuangaza, hakuona mtu. Akaokota gongo la kuminyia mkononi kwa tahadhari.

Kisha akaendelea kutembea.

**

"Atakuwa sawa?" Mama aliuliza akimtazama Wisconsin. Mikono yake ilikuwa imemshika Brian ambaye alikuwa amelazwa kwenye kochi akiwa hana fahamu.

"Usijali," Wisconsin akamtoa mashaka. "Atakuwa sawa tu. Yeye ni mpambanaji, najua atashinda vita hii."

Mama akamtazama mwanaye na kutikisa kichwa kwa huruma. Alitamani amwamshe na kumkumbatia, ila alikuwa ulimwengu mwingine. Alikuwa yupo kwenye ulimwengu wa wafu.

Mama Brian akauliza, "na vipi kama akiuawa huko?" Wisconsin akamtazama kwa imani na kumwambia, "Halitatokea hilo."

"Vipi kama likitokea?" Mama akasisitiza. "Kama akiuawa huko na huku itakuwaje? ... atakufa pia?"

Wisconsin akatikisa kichwa kuafiki, "ndio, atakufa pia. Hatoamka katika usingizi wake huu."

Mama akajawa na hofu. Akaketi na kumlaza mwanaye mapajani mwake. Mwanaye wa pekee. Naye Wayde akaweka kiganja chake kwenye paji la uso la Brian na kusema, "Tafadhali, kuwa salama."

Kidogo mshumaa ukazimika na ndani kukawa totoro.

"Nini kinatokea?" Mama akapaza sauti. Wisconsin akafanya jitihada za kuwasha mshumaa, ulipowaka, wakamwona mtu akiwa amesimama mlangoni. Mtu mpana mweusi. Wote wakashtuka!

Wasipate muda wa kujiuliza, mtu huyo akamvamia Wisconsin, akamkaba na kumnyanyua juu, kisha akamtupia kwanguvu ukutani!! Alafu, kwa kasi kali ya shingo yake, akamgeukia Mama yake Brian na kumnyooshea kidole chake kirefu. Akasema, "Wewe na mwanao, wote mtakufa!"

Akamnyaka Mama Brian, ila kabla hajafanya kitu, Wayde akamrukia mgongoni na kujaribu kumng'ata shingoni. Haraka akamdaka binti huyo na kumtupia kwenye meza ya runinga. Meza na runinga yake vikavunjikavunjika! Wayde akalalama sana kwa maumivu.

Bwana yule, mweusi kwa rangi, uso wake ukiwa haujulikani ni wa nani, akamgeukia sana Mama Brian aliyekuwa amemkumbatia mwanaye, akamtazama kwa kupindisha shingo, kisha akayarudia maneno yake, "wewe na mwanao, wote mtakufa" akamnyaka Mama Brian na kumnyanyua juu kama unyoya, alafu naye akamtupia mbali, akajibamiza na kudondoka chini akiwa hoi bin taabani.

Sasa dubwana likawa limebaki na mwili wa Brian pekee. Brian ambaye yupo hapo kimwili tu. Akamtazama na kumnyanyua juu akiwa amemkaba, akasema, "sasa na mwisho wako umefika!"

Akanyanyua mkono wake wa kushoto juu, ukachomoza kucha ndefu kama koleo, akamzamishia nazo Brian tumboni, Mama akapiga kelele kwa maumivu ya mwanaye! Mwili wa Brian ukaanza kumimina damu lukuki na yule Dubwana akafurahi haswa.

Akautupia mwili huo kochini alafu akanyonya vidole vyake vyenye makombo ya damu kisha akajilamba kana kwamba ametoka kula chakula kitamu.

"Tafadhali, mwache mwanangu!" Mama akalia. "Kaa mbali na mwanangu wewe shetani!"

Dubwana lile likaangua kicheko na kusema, "nishamwacha ajifie. Bado wewe!"

Likaanza kupiga hatua zake nzito kumfuata Mama Brian, alipomkaribia akamdaka shingo yake na kumnyanyua juu alafu akamkandamizia ukutani. Mama Brian akapapatika kutetea uhai wake. Miguu yake ikaogelea hewani akiwa anaelekea kufa.

Ila kheri, na ni ghafla tu, hilo dubwana likaanza kupoteza nguvu zake kwa upesi! Likastajaabu. Likamwachia Mama Brian akadondoka chini na yeye akaangaza huku na huko akitafuta kinachomtafuna.

Kule kingoni, dirishani, akamwona Wisconsin akiwa amefungua pazia sehemu ndogo na mkononi mwake ameshikilia kitabu anasoma. Basi dubwana hilo likakasirika likinguruma, haraka likaanza kusonga kumfuata Wisconsin akammalize mara moja!

Akiwa amebakiza hatua moja kumkabili mtu wake, Wayde akamrukia na kumganda mgongoni. Kabla hajamwondoa binti huyo, akastaajabu akichomwa na vioo usoni, tena mara nyingi asizoweza kuhesabu. Kumbe Wayde alikuwa ameteka baadhi ya vipande vya runinga. Na japo naye vilikuwa vinamkata kiganjani, hakuwa anajali!

Alimtofoatofoa yule dubwana na kumfanya alalamike kwa kunguruma. Macho yake ambayo hayakuwa yanaonekana, yakavuja damu akihangaika huku na kule kumtoa Wayde mgongoni. Mithili ya chombo kilichokumbwa na dhoruba, akawa anapepesuka, anajigonga na kutaka kuanguka.

Alipofanikiwa kumtia Wayde mkononi, akamvuta kwanguvu kisha akamminya shingo yake akitaka kumvunja na kummaliza moja kwa moja, ila hakuwa na nguvu hizo tena. Sasa alijihisi mdhaifu kuliko hata mara ya kwanza. Magoti yalishindwa kumbeba kabisa akaangukia chini kama mtu anayesujudu.

Mikono yake ikamwachia Wayde, ambaye naye alidondoka akiwa amechoka, amejeruhiwa. Haraka Wisconsin akaenda kumjulia hali binti huyo, na asipoteze muda, akamwagiza aweke presha kwenye jeraha la Brian ingali yeye akienda kutafuta huduma ya kwanza.

Kidogo akarejea akiwa na mkoba wa huduma hiyo, akatoa bandeji na dawa, upesi akamtia dawa Brian na kumfunga kisha akamwendea Mama. "Upo sawa?"

Mama akatikisa kichwa kuafiki. Wisconsin akamnyanyua ampeleke kumlaza kochini, lakini kabla hajasonga, akamwona dubwana lile likiwa limeamka! Tayari alishakusanya nguvu zake kama hapo awali!

"Mungu wangu!" Mama Brian akanong'ona. Upesi Wisconsin akapaza sauti, "Wayde, zima mshumaa!" Haraka Wayde akapuliza mshumaa na kuzimika.

Kidogo Wisconsin, akauwasha tena, na mara hii ulipowaka, mlangoni wakawa wamesimama watu watatu! Kutokana na mwanga hafifu, hawakuwa wanaonekana vema ila Wisconsim aliwatambua. Ni wale watoto wafu wa Helo.

Basi akasema maneno ya ajabu, na mara wale wafu wakamvamia dubwana yule na kumteketeza wakihodhi haki yao kama watoto wa Hernandez Lorenzo. Haki ambayo watoto hawa wa kuasili; Alfonso, Brewster na Olivia waliiteka kwa muda!

**

"Brian, amka! Brian, Brian, amka!" Sauti hiyo ya kike ilikuwa inanong'ona kwenye masikio ya Brian. Hakuwa anajitambua yupo wapi. Alikuwa gizani. Tangu, dubwana lile lilipomkita tumboni kule kwenye ulimwengu wa waliohai, alipoteza nguvu na fahamu.

Sasa anaanza kurejea kwenye hali yake. Bado akiwa kwenye ulimwengu wa kiza! Ule wa waliokufa. Na mtu yule aliyekuwa anamhisi yupo nyuma yake, ameshamteka! Mguu wake wa kuume umedakwa na anaburuzwa.

Akafungua macho yake na kuangaza, alikuwa hajui anapelekwa wapi. Alichokiona ni mwanaume jabali akimburuza kana kwamba kiroba.

Akaangaza kushoto na kulia kwake, bahati akajigongoa kwenye jiwe. Akalibeba jiwe hilo pasipo kulalamika kwa maumivu. Alivumilia. Alipoweka vema mkononi akalirusha kumbamiza yule aliyemshika, naye akageuka na kumtazama.

Alikuwa ni Helo!

Alimdaka Brian kwanguvu, na mara kule kwenye ulimwengu wa waliohai, mwili wa Brian ukaanza kuchuruza damu puani!

Puh! Brian akatupwa chini. Kabla hajakaa sawa, akazabwa teke kali la kichwa. Akahisi kupoteza fahamu. Akiwa ameshajua ameshakwisha, hajui tena alipo, akasikia tena sauti ya kike ikimwambia, "amka! Brian, amka!"

Akafungua macho yake kuangaza, akaona akiwa ameshakaribia kwenye makazi yale yaliyokuwa na mwanga hafifu aliouona kwa mbali. Akajikakamua. Kidogo, bwana yule akamshtukia. Akamwapua na kumbeba kuzama naye ndani. Akiwa amebebwa, Brian akasikia sauti za funguo mfukoni mwa Helo.

Walipofika kwenye chumba fulani, Brian akatupiwa humo na kisha Helo akasimama akimuuliza ni nini amekuja kufanya huko kwenye ardhi ya wafu.

"Kwanini waja huku na hutaki kusikia?" Na akahitimisha, ".. yanipasa nikuue ile uje kutuama huku kabisa maana unapapenda!"

Akamsogelea Brian amnyake, ila ghafla akasikia sauti za watu wakiwa wanagongagonga mlango. Akanguruma kuguna na kutoka humo ndani kwenda huko aliposikia sauti. Ilikuwa ni kwenye chumba ambacho amewafungia mateka wake. Mateka wa kiroho anaowatumikisha. Humo ndani alikuwapo pia na Kecie.

Akafoka, "mnataka nini? Kufa mara ya pili!"

Wote wakatulia. Akajipapasa mfukoni, hakuhisi ufunguo. Akastaajabu! Upesi akakimbilia kule alipomwacha Brian, kufika hakukuta mtu. Akaangaza akishangaa.

Kidogo, akahisi vishindo vya watu. Alipotoka ndani, koridoni akakuta roho zile ambazo alikuwa amezifungia. Zilikuwa tayari huru!

Akafoka, "kabla sijawaangamiza, rejeeni zizini!" Uso wake ulikuwa umeghafirika kwa hasira. Kecie akamjongea na kumwambia, "hauwezi kutufanya chochote hivi sasa, Helo. Hauna nguvu hiyo tena!"

Helo akatazama mikono yake akiwa amekodoa. Akajaribu kumkamata Kecie, akashindwa, mkono ulivuka kama kivuli. Akastaajabu na kuhofia.

Kecie akamwambia, "muda wako umekwisha, Helo. Ni wakati wako wa kuangamia."

Mara, "hapana!" Sauti ya kiume ikasikika. Kutoka nyuma ya wakina Kecie akatokea Brian aliyesonga mbele kabisa. Mkononi alikuwa ameshikilia funguo, ni yeye ndiye aliyewafungua huru wakina Kecie.

Akamtazama Helo na kumwambia, "familia yako iko hapa. Nadhani hauna haja tena ya kuusumbua ulimwengu wa walio hai."

Helo alipotazama nyuma akawaona watoto wake watatu. Akawakimbilia na kuwakumbatia kwanguvu macho yake yakiwa yanalenga machozi.

Kecie naye akamshukuru Brian kisha akamuaga kwa kumfumba macho na kumwambia"rudi sasa duniani. Umemaliza kazi yako Brian."

**

Brian akakohoa.

"Ameamka!" Mama akalipuka kwa furaha. Akamkumbatia mwanaye kwanguvu na kumbusu kwenye paji la uso. Wayde naye akamkumbatia na kisha Wisconsin. Walikuwa wamemaliza na kufaulu mtihani!

Walijawa na furaha tele. Punde Karen akajiunga nao, wakafanya tafrija fupi. Kesho yake Wayde akarejea kwao na kupewa taarifa kuwa baba yake alikuwa hospitalini akiendelea vema
.
Alipomweleza baba yake kilichotukia akiwa kitandani amelazwa, baba yake akamshika mkono kwanguvu na kumwambia, "umefanya kile ambacho sisi tulishindwa." Kisha akatabasamu na kumbusu, "hauna haja ya kuomba msamaha. Najivunia kuwa nawe."

**
.
.
MWISHO
 
duuh finally mzigo umekwisha,ilikuwa burrdaani ya aina yake.asante steve kwa kushare nasi huu utamu tena buree kabisa.Mungu ajazie pale ulipopunguza kwaajili yetu.Natumai hii si story ya mwisho,utaendelea kutupa vitu vizuri na nya uhakika bila arosto pale utakapopata chance.barikiwa mkuu.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom