Simulizi: Roho yake inadai

*ROHO YAKE INADAI --- 43*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Mbali na hivyo, watu kadhaa, haswa majirani, walikuwa wametoka nje ya makazi yao wakitazama eneo la tukio kwa macho ya maulizo na nyuso za mashaka. Kulikuwa na zogo fulani midomoni mwao.

Muda si mrefu gari ya wagonjwa ikawasili eneoni na kujitengenezea vema. Kutoka ndani ya nyumba, ikatolewa miili mitatu ambayo imefunikwa gubigubi, ikatiwa ndani ya gari la wagonjwa na kisha gari hilo kutimka.

ENDELEA

Baadae ikaja kuwekwa bayana ya kuwa afisa Randall alikuwa amefariki, pia mke na mtoto wake mdogo aitwae Bestie. Na kama haitoshi, baadae taarifa zaidi zikaja juu ya kifo cha afisa Williamson. Alikutwa amekakamaa ndani ya chumba chake mwili wake ukiwa mweusi kabisa kana kwamba mtu aliyekitwa na shoti kubwa ya umeme.

Vifo vikawekwa bayana kwenye vyombo vya habari na karibia Boston nzima ikajuzwa. Misiba miwili iliyotokea ndani ya usiku mmoja. Na yote ikiwa imefanana mtindo, yaani muuaji hakuwa anajulikana.

Ila hakuwa anajulikana kweli?

“Padri Alfonso atakuwa ameshamuua,” alisema Brian aliyekuwa ameketi nyuma ya gari hili liendalo. Kwa mbele alikuwa ameketi Wisconsin na Mama ambaye alikuwa ameshikilia usukani.

Katika majira haya ya asubuhi, walikuwa wanaelekea msibani. Msiba wa Brewster. Siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya mazishi yake kwa mujibu wa taarifa. Jana yake hawakupata muda wa kwenda msibani kutokana na kutingwa na shughuli zile za hapa na pale polisi.

“Mbaya zaidi amewaua wote,” akasema Mama. “Ameona awamalize kabisa kufuta ushahidi.”

Kidogo Wisconsin akasema, “ebu twendee kule kwenye kituo cha habari!” Mama akamtazama na kisha akarejesha uso wake haraka barabarani akiuliza, “kufanya nini huko?”

“Nahisi yule dada atakuwa mashakani,” Wisconsin akaeleza. “Kama wale polisi wameuawa wote, basi huenda pia akamuwinda na yule mwanamke ammalize!”

Basi Mama akaongeza mwendokasi akielekezea chombo kule alipoambiwa, muda mchache, kama dakika kumi na tatu, wakawa wamewasili. Wakashuka na kwenda ndani ya ofisi. Pale kwenye ofisi ya mapokezi wakamkuta mwanamke mwingine mwembamba sana mwenye nywele nyingi nyeusi.

Wakamsalimu na kumweleza shida yao, “Tumemkuta Karen?” Mama Brian akauliza pasipo kuonyesha shaka usoni. Yule mwanamapokezi akawatazama kidogo alafu akatabasamu na kutikisa kichwa. “Hapana, hayupo!”

“Atakuja leo?”

“Yah! Atakuja. Ninyi ni wakina nani?”

“Wageni wake tu, tulikuwa na shida naye. Unaweza kuwasiliana naye kumwambia twamngoja?”

“Nishajaribu hilo, nimeongea naye mara moja, lakini baada ya muda sikumpata,” akasema yule dada na kuongezea, “Nimeshampigia mara tano, hajapokea. Mara ya mwisho simu yake haikupatikana kabisa!”

“Unajua unapokaa?” akauliza Mama Brian sasa akiwa ametoa macho.


**


Gari lilipiga breki kali na kisha kukata kona kwa fujo. Mama Brian alikuwa amechanganyikiwa? Aliendesha gari upesi sana na hata wale abiria aliowabeba hawakumkataza wala kumwonya.

Aliyavuka magari mengine kwa haraka, akiwa anabadilisha gia na kukanyagia pedeli ya mafuta, akaadhibu barabara kwa ustadi. Akatembea mithili ya kishada. Uso wake ulikuwa umetambaliwa na mashaka na mikono yake ilikuwa imeshikilia usukani kwanguvu.

Kitu kimoja walichokiamini ni kuwa mwanamke huyo anaweza kuwa mzima, au basi kama sivyo, atakuwa yupo hatarini kwa muda huo, kwani kwa makadirio ya muda ambao aliongea na mwenzake, ilikuwa ni asubuhi hii hii, muda mchache nyuma.

Lakini kwanini hakuuawa usiku? Sababu wauaji walikuwa wakiwamaliza maafisa wa polisi kama ilivyoonyesha wa mwisho kuuawa, afisa Williamson, kwa mujibu wa makadirio ya maelezo ya daktari, alikata moto majira ya alfajiri.

Punde gari lilipokamta breki, likiwa limetumia dakika nane tu kufika hapo, Wisconsin na Brian wakawa wa kwanza kushuka, nyuma wakifuatiwa na Mama yao. Wakagonga mlango, ulipokawia kufunguliwa, Wisconsin akausukuma kwanguvu akitumia bega lake pana. Mlango ukafunguka wakazama ndani.

Kutazama sebuleni hakukuwa na mtu, ila punde kidogo, Karen akatokea akiwa amefungia taulo lake jeupe kifuani. Mwili wake ulikuwa umejawa na maji na macho yake yakiwa yamebebeba mashaka.

Mama Brian akatahamaki kumwona, akaita, “Karen!” na kisha akamkimbilia na kumjulia hali. Karen akasema yu sawa, hakukumbana na tatizo lolote. Ndipo Mama Brian na wenziwe wakaketi na kumweleza kwanini walikuwa wanahofia mpaka kukimbia kuja hapo.

“Kuwa makini sana,” Wisconsin akamhusia. “Huenda muuaji akakufuata na wewe pia.”

Karen, akiwa aliyejawa na woga na mkanganyiko, akatikisa kichwa chake kupokea taarifa hiyo. Akaenda ndani na kujivesha nguo kisha akawaomba wageni wake hao wa dharura wampeleke kazini kwani hana usafiri.


**


“Madam, tunaomba uegeshe upande wako wa kulia, huko kuna nafasi zaidi!” alisema mwanaume aliyevalia sare ya suti nyeusi na mikononi mwake akiwa amevalia glovu nyeupe. Alikuwa hapa maalum kwa ajili ya kazi ya kuwalekeza wageni, aidha wenye vyombo vya usafiri ama lah, waliofika hapa kwenye mazishi.

“Nashukuru.” Mama Brian akakunja kona kufuata maelekezo. Alipoegesha gari na kulizima, wakashuka na kuelekea kwenye viti kadhaa ambavyo viliwekwa kwenye uwanja wa makaburi. Wakaketi na kuchambua eneo.

Hapo kulikuwa na watu takribani thelathini na tatu na magari kumi. Jeneza la Brewster lilikuwa limeshawekwa karibu kabisa na shimo lake na mbele kabisa, kwenye mpangilio wa viti, walikuwa wameketi watu wa karibu wa Brewster, haswa wafanyakazi wenziwe kwani hakuwa na marafiki.

Miongoni mwao, Padri Alfonso na watumishi wawili wa kike waliovalia sare zao kama ilivyo ada wakati wowote.

“Brian,” Wisconsin akaita kwa kunong’oneza. “Hakikisha macho yako yanamtazama Padri Alfonso muda wote, sawa?” Kabla Brian hajajibu, Padri Alfonso akageuka na kuwatazama kwa kuwakazia macho, na kisha akarejesha uso wake mbele.

Brian akauliza, “Atakuwa amesikia?” Kabla Wisconsin hajajibu, wakamwona Padri Alfonso akitikisa kichwa. Wakashtuka na kutazamana kisha hawakuongea tena.

Basi tangu hapo, Brian akawa anamtazama Padri Alfonso kwa woga. Kweli hakubandua macho yake. Hata alipoyafumba, akayafumbua upesi na kuendelea kukodoa.

Muda kidogo Wisconsin akampatia kikaratasi kidogo chenye ujumbe. Akaikichukua na kukisoma.

“Tutawasiliana kwa maandishi,” ujumbe ulisomeka vivyo. Akamtazama Wisconsin na kumtikisia kichwa kama ishara. Wisconsin akamwandikia pia Mama ujumbe kuwa watakuwa wanasiliana kwa maandishi, naye Mama akaelewa.

Muda ukasonga zaidi. Ilipopita lisaa limoja, shughuli za mazishi zikaanza rasmi baada ya ujio wa mwakilishi mkubwa wa serikali. Jeneza likafunguliwa, na watu wakaanza zoezi la kumuaga Brewster kwa mara ya mwisho kabla hajamezwa na udongo.

‘Utaenda kuaga?’ Wisconsin akaandika ujumbe wake kwa peni na kumpatia Brian.

‘Hapana, sitaenda,’ Brian akajibu na kurejesha karatasi.

‘Kwanini?’

‘Naogopa.’

‘Umekuwa ukimtazama Padri Alfonso?’

Kabla Brian hajaandika kujibu, akarusha tena macho yake kumtafuta Padri Alfonso. Hakumwona. Akaangaza kushoto na kulia, hakumwona. Akastaajabu atakuwa ameenda wapi, mara yake ya mwisho kumwona alikuwa amesimama kandokando na jeneza.

Alipomkosa, akarejesha macho yake kwenye karatasi apate kumwandikia Wisconsin ujumbe. Ajabu alipotazama karatasi hiyo, akaikuta tayari ina maandishi. Haukuwa mwandiko wa Wisconsin!

‘Unanitafuta?’ Maandishi yalisomeka hivyo. Brian akahofia sana. Akarusha tena macho yake kuangaza, hakuona kitu. Aliporejesha tena macho yake kwenye karatasi akaukuta ujumbe mwingine, ‘Nipo nyumbani kwenu.’

Hapa sasa ndiyo akatamani kupiga kelele. Haraka akamrejeshea Wisconsin kile kikaratasi kisha akamshtua Mama yake kumtaka waende nyumbani haraka iwezekanavyo!

“Yupo nyumbani!” Brian alisema akiwa amekunja ndita, macho yamejawa na woga. Nyumbani alikuwa amebakia Olivia pekee.

Basi wakatoka upesi na kwenda kwenye gari. Mama akatia ufunguo na kuwasha chombo, ila kabla hawajaondoka, akamwona Padri Alfonso kwa mbali akiwa amesimama na watu watatu wanateta!

Akauliza akistaajabu, “si yule?” wote wakatazama. Kweli alikuwa ndiye. Wakiwa kwenye buwazo hilo, Padri Alfonso akawapatia mkono watu wawili aliokuwa amesimama nao, kisha akaanza kutembea kulifuata gari walilopo wakina Brian.

“Mama, twende!” Brian akasema akimpigapiga mama yake begani, lakini Wisconsin akasema, “Hapana.” wote wakamtazama kwa nyuso za kushangaa.

“Ngoja tuone atafanya nini mbele za watu!”

Basi punde Padri Alfonso akawafikia na kutabasamu. Akawasalimu na kuwakaribisha kwa ukarimu.

“Kuna tatizo lolote?” akauliza.

Mama Brian akawahi kutikisa kichwa na kusema, “Hamna!”

“Una uhakika?” Padri Alfonso akauliza.

“Ndio, hamna!” Mama akasihi. “Nashukuru, padri.”

Padri akamtazama na kumuuliza kwa mara nyingine, “Una uhakika?” sasa hivi macho yake alikuwa ameyakodoa. Mama Brian akasihi baridi na moyo wake waenda mbio.

Ghafla Padri akatabasamu na kusema, “Msijali.” kisha akaenda zake.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 44*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Una uhakika?” Padri Alfonso akauliza.

“Ndio, hamna!” Mama akasihi. “Nashukuru, padri.”

Padri akamtazama na kumuuliza kwa mara nyingine, “Una uhakika?” sasa hivi macho yake alikuwa ameyakodoa. Mama Brian akahisi baridi na moyo wake waenda mbio.

Ghafla Padri akatabasamu na kusema, “Msijali.” kisha akaenda zake.

ENDELEA

Wakamtazama Padri akiishia na kisha Mama akaondoa chombo hapo msibani kurudi zao nyumbani. Walipomfika wakamkuta Olivia akiwa ameketi sebuleni anatazama runinga akila.

“Uko sawa, Olivia?” Mama akauliza. Olivia akatikisa kichwa chake na kumjibu kiufupi, “Ndio.” kisha akaendelea kutazama runinga kana kwamba hamna mtu.

Baadae , baada ya kupumzika, ikiwa ni majirani ya jioni, Wisconsin akamwita Brian na kumtaka watoke kidogo kwani ana maongezi naye. Wakitumia usafiri wa Mama, wakaenda kwenye moja ya bustani inayopatikana katikati mwa mji wa Boston, hapo wakatulia kwenye mojawapo ya viti vinavyopatikana kwenye maeneo hayo, alafu Wisconsin akasema,

“Niambie machache unayoyajua kuhusu Hamill, Dkt. Hamill.”

Brian akamtazama kwanza Wisconsin kabla hajasema jambo. Kwa kiasi fulani alikuwa ameshangazwa na hilo swali. Aliwatazama watoto waliokuwa wanacheza bustanini alafu baada ya muda kidogo, akasema, “Sina mengi ya kusema juu yake. Alikuwa ni mmoja wa watu wazuri ninaowajua, mwenye upendo na haja ya kusaidia wengine. Japo maisha yake yaligubikwa na upweke.”

Wisconsin akaingiza mkono wake ndani ya mfuko wa koti, humo akatoa kiko chake na kibiriti, akawasha na kuanza kuvuta. Akavuta mapafu manne alafu akasema sasa kwa kinywa chake kikavu, “Hakuna kitu chochote alichowahi kukwambia juu ya familia yake?”

“Kidogo,” Brian akajibu. “Mke na watoto wake walifariki na kumwacha mkiwa.”

“Nini kiliwaua?” Wisconsin akauliza. “Alikwambia nini kimewaua?”

Brian akatikisa kichwa. “Hapana,” akasema. “Hakuwahi kunambia, ila …” Wisconsin akamtazama kwa jicho la udadisi. “Aliniachia nyaraka zake tatu nizipitie. Zilikuwa zinahusu maisha yake, lakini sikupata muda wa kuzimaliza kusoma.”

“Ziko wapi sasa?” Wisconsin akadadisi.

“Zilipeperushwa na upepo wa ajabu tukiwa safarini kuja kule kwako,” Brian akaeleza. Kidogo Wisconsin akatulia, akavuta tena kiko chake akiwaza alafu akamtazama Brian na kumwambia, “pengine ungesoma na kuzimaliza nyaraka hizo ungekuwa umebadilisha mawazo juu ya Dkt Hamill.”

Kauli hiyo ikamtia Brian hamasa ya kutaka kujua zaidi. “Kwanini unasema hivyo?” akauliza.

Wisconsin akakuna kidevu chake na kusema, “Dkt Hamill aliua familia yake. Kwa mkono wake, alimmaliza mkewe na watoto akitumia kisu kirefu chenye ncha kali.”

“Kwanini afanye hivyo?” Brian akastaajabu.

“Labda kabla hatujajua kwanini alifanya hivyo, inabidi kwanza ujue kuwa Dkt Hamill alikuwa na familia ya watoto watatu, wawili walikuwa wa kiume na mmoja akiwa wa kike. Alifanikiwa kuwapata watoto hao akiwa kwenye enzi za ujana wake.

Pengine aliwapenda sana, mimi na wewe hatufahamu maana hatukuwapo. Ila tulilo na uhakika nalo ni kuwa alikuja kuwaua pamoja pia na mkewe. Nililikuta hilo kwenye ‘diary’ yake.”

Wisconsin akazamisha mkono ndani ya koti lake na kutoa kijitabu kidogo chenye jalada gumu jeusi, akampatia Brian.

Brian akakikagua na huku Wisconsin akiendelea kunena. “Sijajua kwanini aliua familia yake, kutakuwa na sababu kubwa nadhani. Lakini kwenye karatasi ambayo alikuwa ameeleza ya kuwa amehusika na kuua familia yake, alikuwa ameweka hapo mkufu wenye kidani cha kito cha kijani, kito cha duara.”

Wisconsin akazamisha tena mkono wake ndani ya koti lake na kutoa mkufu huo. Akautazama kwa muda kidogo alafu akamkabidhi Brian.

“Shida si kwamba amewaua familia yake. Tunaweza tukapuuzia juu ya hilo, ila tatizo ni kwamba, makaburi ya wanawe sikuyaona isipokuwa lile la mkewe tu. Ukifungua kwenye diary yake, utaona ameelekeza juu ya wapi alipomzika mkewe, lakini kuwahusu watoto wake, hamna anayejua. Hajaeleza wapi walipo.”

“Unadhani watakuwa wapi?” Brian akauliza. Mkononi alikuwa amebebelea kijitabu na mkufu.

“Sijajua wapo wapi,” akajibu Wisconsin, “Ila nahisi watakuwa wazima.”

“Kwanini unahisi hivyo?” Brian akauliza. “Dkt Hamill ameandika hilo kwenye diary yake?”

“Hapana, hajaandika. Lakini pia hajaandika watoto hao wapo wapi. Kwanini amzike mkewe ndani ya eneo la nyumba, na watoto wasijulikane kawapeleka wapi?”

Brian hakuwa na majibu. Wisconsin akavuta kiko chake na kutia neno, “Ni ajabu, maana hata hilo amelifanya kuwa siri ndani ya siri. Siri ambayo hata yeye hakutaka kuiandika ikajulikana kwa watu.”

“Sasa tutafanyaje kujua hilo?” Brian akauliza.

“Hatuna namna, Brian!” Wisconsin akatikisa kichwa. “Kwa sasa tuna kazi nyingi za kufanya, visa huwa haviishi ndani ya mji. Nilitaka tu kukuweka bayana juu ya hilo ila hatutadiriki kuhangaika nalo. Tumalize kwanza hili kumi lilipo mikononi mwetu.”

Basi baada ya maongezi hayo, Wisconsin akabadili mada na kumwambia Brian ya kwamba tangu Brewster alipofariki, hakuna mtoto yeyote aliyepotea ndani ya mji wa Boston. Hiyo ni ishara kuwa Helo atakuwa amedhoofu kwa mtu huyo kufa. Na endapo watafanikiwa kummaliza na Padri Alfonso, basi kazi itakuwa imekwisha. Atakachokifanya, yeye Brian, ni kwenda kule kwenye ulimwengu wa wafu, akamkabili na kummaliza Helo.

“Lakini tutammalizaje Alfonso?” Brian akauliza. “Anaonekana ni mwenye nguvu, pengine kumzidi Brewster!”

“Ni kweli,” akajibu Wisconsin, “lakini lazima kutakuwa na njia. Mpaka kufikia kesho nitakuwa nimejua cha kufanya. Twende sasa, tumekaa sana hapa.”


**


“Afadhali mmekuja!” Alisema Mama akiwa amekodoa macho. Akawafungulia mlango Wisconsin na Brian kuingia ndani. Wakamwona Karen, dada wa mapokezi, akiwa amejaa kwenye kiti cha pekee, uso wake umeshikwa na wasiwasi.

“Karen amefika hapa muda si mrefu,” Mama akasema kwa pupa, “ameniletea ujumbe mzito sana. Naomba mumsikize.”

Baada ya kusema hivyo, Karen akaanza kujieleza na hakuchukua muda mrefu macho yake yakaanza kumimina machozi. Sauti yake ilikuwa nyembamba inayotetemeka.

“ … amekuja kunifuata. Nimekuta jumbe zake kwenye dawati la kazini akiniambia ni mimi ndiye nitafuata kufa.” Karen akiwa anatumia mkono wake unaotetemeka, akawapatia Brian na Wisconsin karatasi mbili. Wakazisoma na zote zikiwa na jumbe moja, “ NI WEWE NDIYE UTAFUATA.” karatasi zote zikiwa zimefanana na zile zile ambazo yule mtangazaji wa awali alikuwa anazipata.

Lakini,

“Msichana yule aliyefanyiwa mahojiano, yupo wapi?” Wisconsin akauliza maana walikuwa wametingwa sana na hoja za yule mtangazaji na yale yanayotokea mpaka kusahau kabisa kuwa kuna yule binti ambaye naye anaweza kuwa muhimu kwao.

“Sijui,” Karen akajibu. “Mimi ni mdada wa mapokezi tu, siyajui mengi kuhusu mengine.”

“Umewaambia utawala juu ya tishio lako? Umewataarifu polisi?” Wisconsin akaongezea swali.

“Sijamtaarifu yeyote yule,” Karen akajibu. “Hamna atakayeniamini. Najua, hamna atayesadiki maneno yangu. Ni nyie tu!”

Wisconsin akamtazama Mama Brian. Hawakutia neno. Basi Karen akakaribishwa kwenye nyumba ile kulala mpaka hapo atakapohisi kuwa yu salama. Lakini je hilo litamwokoa dhidi ya ahadi ya muuaji?

Mshale wa saa ulipokomea kwenye majira ya saa nane usiku, Brian aligutuka toka usingizi. Hakujua ni nini kilimwamsha, ila alijikuta akihisi upepo wa baridi. Kando yake alikuwa amelala Wisconsin ambaye alimpisha Karen alale kwenye chumba chake.

Brian akaangaza kushoto na kulia, kisha akaamka na kusimamia miguu yake. Akajongea dirisha na kutazama nje. Kulikuwa kimya, kumetulia haswa. Akiwa hapo, akasikia mlango unafunguliwa. Haraka akageuka na kutazama mlango wa chumba chao. Haukuwa huo!

Akasonga na kufungua mlango na kuchungulia kwenye korido kuona ni mlango gani utakuwa umefunguliwa. Macho yakiwa sahihi, akaona mlango wa chumba kile alichokuwa amelala Karen ndicho kipo wazi. Akajawa na shaka.

Akasonga hatua taratibutaratibu akisogelea hicho chumba. Alipofunga mlangoni, akarusha macho yake ndani. Kama macho yake yalikuwa sahihi, alimwona Olivia akiwa kandokando ya kitanda. Mkononi mwake alikuwa ameshikilia kisu kirefu.

Akajikuta akisema, “Olivia!” kwa kunong’oneza. Hamaki, Olivia akageuka na kumtazama. Macho yake yalikuwa yanang’aa kana kwamba taa.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 45*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Akasonga hatua taratibutaratibu akisogelea hicho chumba. Alipofunga mlangoni, akarusha macho yake ndani. Kama macho yake yalikuwa sahihi, alimwona Olivia akiwa kandokando ya kitanda. Mkononi mwake alikuwa ameshikilia kisu kirefu.

Akajikuta akisema, “Olivia!” kwa kunong’oneza. Hamaki, Olivia akageuka na kumtazama. Macho yake yalikuwa yanang’aa kana kwamba taa.

ENDELEA

Brian hajakaa sawa, Olivia akakimbia upesi na kumvamia mpaka chini. Binti huyo akawa anataka kumchoma kisu. Brian akapambana kwa kuudaka mkono wenye kisu akitumia nguvu zote asijeruhiwe.

Ajabu Olivia alikuwa ni mwenye nguvu sana, hata Brian hakuwa anaweza kufua dafu, ncha ya kisu ilikuwa inajongea taratibu kufuata kifua chake. Aling’ata meno akikazana kujitetea, alipoona juhudi zake zinaelekea ukingoni na huku akiwa anashindwa, akajikakamua kwa mwili wake wote kumtupia Olivia kando amweke chini, kisha akadaka mkono wa Olivia wenye kisu, akaubondea ukutani kwanguvu mara tatu , kisu kikadondoka chini!

“Nitakuua, Brian!” Olivia akang’aka. Sauti yake ilikuwa inatetemeka kana kwamba inatoka kwenye ‘tape recorder’. Macho yake yalikuwa mekundu na mdomo wake umekauka kuwa mweusi.

“Olivia, nini kimekutokea?” Brian akauliza. Alimtazama Olivia kwa huruma na mshangao. Katika namna ya ajabu akaanza kudhoofu. Kadiri alivyotazama macho ya Olivia akawa anajihisi kupoteza nguvu mwilini. Mwishowe Olivia akamtupia pembeni na kuteka tena kisu, akamfuata.

“Acha Olivia!” Brian akasihi. “Usifanye hivyo tafadhali!”

Olivia hakusikia, akaendelea kutembaa kumfuata. Brian akiwa chini, akawa anajivuta kusonga mbali na Olivia.

“Tafadhali, Olivia! Wewe ni msichana mzuri, usifanye hivyo,” Brian akaendelea kunena. Olivia asijali, akamsongea na kisha akainama kutaka kumchoma kisu Brian. Alikuwa na nguvu maradufu. Na ubaya ni kwamba Brian alikuwa anaishiwa na nguvu mwilini kila alipomtazama Olivia machoni.

Olivia akacheka. Ila punde akanyong’onyea, akapoteza nguvu zote na kufunga macho yake, alafu akadondokea chini. Brian hakuelewa nini kimetokea.

Alipotazama koridoni, akamwona Wisconsin akiwa amesimama. Mara upesi Wisconsin akamkimbilia na kumuuliza, “Brian, upo sawa?” kabla Brian hajajibu, akamtazama Olivia aliyekuwa pembeni. Alikuwa amelala kama mtu asiye na ufahamu.

“Nipo sawa,” akajibu, alafu akanyanyuka na kusimama. “Nini kimetokea?” Wisconsin akauliza.


**


“Alikuwa amebadilika,” alisema Brian aliyekuwa anatazama dari akiwa amejilaza kitandani. Pembeni yake alikuwa amelala Wisconsin naye akiwa anatazama dari huku akimsikiza Brian kwa umakini. Bado ni usiku, muda mchache baada ya Brian kutoka kupambana na Olivia.

“Macho yake yalikuwa yanawaka. Alikuwa ni mwenye nguvu ajabu. Sijui ni nini kilimtokea.”

Kukawa kimya kidogo kabla ya Wisconsin kuuliza, “Nini kilikuamsha, Brian?”

“Sifahamu,” Brian akajibu. “Nilijikuta nikiwa macho. Baada ya muda mfupi ndiyo nikasikia mlango ukifunguliwa. Nilipoenda kutazama, nikamkuta Olivia akiwa chumbani mwa Karen.”

Wisconsin akamtazama Brian na kumwambia, “Olivia atakuwa alitumwa kutekeleza ujumbe wa Padri Alfonso. Ametumia mwili wake kutekelezea kazi.”

Brian akauliza, “Vipi? Kutakuwa na matatizo juu ya hilo?”

“Sijajua,” Wisconsin akajibu kisha akakaa kimya kwa kama sekunde tatu, alafu akasema, “Sikujua kama kazi hii itakuwa kubwa kiasi hiki. Ni kazi pevu sana. Mategemeo yangu ya kuimaliza ndani ya siku tatu yameshindikana, na hata sasa sijui itakwisha lini. Inabidi nifanye namna Brian.”

“Namna ipi hiyo?” Brian akauliza. Naye akamtazama Wisconsin kwa macho ya udadisi.

Wisconsin akavuta pumzi ndefu alafu kisha akakaa kimya. Macho yake yalikuwa yanaonyesha yu mbali kimawazo.


**


“Amesema hatotaka mtu amsumbue, tumpe muda,” alisema Brian. Walikuwa wameketi mezani wakipata kifungua kinywa. Wote walikuwapo hapo isipokuwa Wisconsin pekee.

“Atakuwa humo mpaka muda gani?” Mama akauliza. Brian akapandisha mabega yake pasipo kusema jambo. Akamtazama Olivia, alafu akamuuliza, “Upo sawa, Olivia?”

Olivia akatikisa kichwa akitafuna. Brian akawaza yale yaliyotokea jana. Ilikuwa ni ajabu hakuna mwingine aliyekuwa anajua chochote isipokuwa Brian na Wisconsin pekee.

Alipomaliza kula, Brian akajiandaa na kwenda shule. Huko akakaa mpaka majira ya mchana wa saa nane ambapo kengele iligonga kuashiria muda umekwisha. Akiwa anatoka, mara akasikia sauti ya kike inamwita, alikuwa ni Wayde.

“Habari, Brian!”

“Njema. Unaendeleaje?”

“Kawaida. Vipi ulipata chochote kumhusu Silvia?”

Brian akatikisa kichwa.

“Brian!” Wayde akaita kisha akauliza, “unajua ni namna gani nilivyo mpweke, Brian? Nimekupoteza wewe, nimempoteza na Silvia, unadhani maisha yangu yapoje?” Wayde alizungumza akiwa na macho mekundu yanayokaribia kumwaga chozi. “Maisha yangu yamekuwa magumu sana, Brian. Nahisi kuchanganyikiwa. Tafadhali … kama kuna jambo naweza kufanya kujisaidia na maisha yangu, nieleze, Brian.”

Wayde akamkumbatia Brian kwanguvu kisha akalia. Brian akamsihi anyamaze na kisha akarejea naye darasani kuteta mambo kadhaa.

“Wayde, ni hatari sana. Mambo haya si kama vile ambavyo unaweza ukawa unawaza. Ni makubwa, na naweza kukushauri tuachane nayo kwa usalama wako, na familia yako.”

“Hapana, Brian!” Wayde akatikisa kichwa. “Nawezaje kuacha haya yapite? Unadhani sihisi kinachoendelea?”

“Unahisi nini, Wayde?” Brian akauliza akimtazama mlengwa. Mara Wayde akasimama na kumwambia, “Twende!”

Wakatoka nje ya darasa kwenda kulikuta gari la Wayde, wakajipaki na msichana huyo kutimka. Brian hakuwa anajua wapi wanaelekea, pia alikuwa na hofu ya kukutwa na baba yake Wayde ambaye ashampiga marufuku ya kuonana na binti yake.

“Wayde, naona hili litakuwa na hatari kwangu.”

“Usijali, baba yangu hayupo,” Wayde akamtoa hofu. Wakaenda na usafiri huo mpaka nyumbani kwa wakina Wayde, nyumba kubwa ya ghorofa mbili. Sakafu ya chini ilikuwa ni ya watoto, ya pili ya wazazi na ile ya tatu ikikaliwa na maktaba.

Wayde akampandisha Brian mpaka juu kabisa kwenye maktaba kisha akamwambia, “Keti hapa.” alafu yeye akarudi chini na muda si mrefu akarejea na funguo, akamwambia Brian, “Nifuate huku.”

Wakaendea chumba fulani ndani ya maktaba. “Chumba hiki ni siri kukiingia. Baba yangu amekuwa akizama humu mara kadhaa tu na kujifungia. Pale nilipopata muda wa kusoma baadhi ya vitabu ambavyo vipo katika maktaba nikaja gundua kuwa upotevu wa watoto ndani ya mji wa Boston ni kitu ambacho kilitarajiwa kwa maana ni adhabu anayotupatia bwana Helo.”

Wayde aliposema hayo, akamtazama Brian na kumuuliza, “Ninachokisema ni uongo?”

Brian akatikisa kichwa. “La hasha.”

“Lakini kwanini hukunambia Brian?” Wayde akauliza. “Ulikuwa unayajua yote hayo, sio?” Brian hakusema jambo. “Ulikuwa unayajua yote hayo na ukaamua kunificha, kwanini Brian?”

Wayde akafungua chumba wakazama ndani, humo kulikuwa na vitabu vingine vya ziada tofauti na vile ambavyo vipo kwenye ukumbi mwingine. Akampatia Brian baadhi ya vitabu na barua kadhaa takribani sita, kisha akamwambia, “visome, nawe uniambie ni nini umeona, Brian.”

Brian akachukua muda kuvipitia. Macho yake yalikuwa mepesi kwakuwa alikuwa mzoefu wa kupenda kusoma. Baada ya muda wa dakika arobaini na tano tu, akawa amaemaliza. Akamuuliza Wayde, “Ina maana baba yako ana mahusiano na seneta yule aliyemuua na kumchoma Helo?”

“Ndio,” Wayde akajibu. “Ni babu yake kabisa mzaa mama.”

“Ajabu!” Brian akatahamaki, kisha akauliza, “Kama ni hivyo, kwanini Helo hajamuua baba yako kulipiza kisasi kabla ya kuamua kuitesa Boston nzima?”

Wayde akanyamaza kidogo, alafu akashusha pumzi na kumuuliza Brian, “Nikikuonyesha kitu, je itakuwa siri baina yangu na wewe?”

“Ndio, naahidi hilo,” Brian akajibu. Basi Wayde akaingiza tena mkono wake mfukoni na kutoa ufunguo wa ziada. Ufunguo mdogo wa shaba. Akafungua mlango mwingine ndani ya chumba hicho cha siri, humo Brian akaona jambo lililomshangaza.

Maiti za watu watatu!

“Wayde, ni nini hicho?” Brian akastaajabu. Wayde akamjibu huku akimtazama, “ni watoto wa Helo!”


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 46*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Ndio, naahidi hilo,” Brian akajibu. Basi Wayde akaingiza tena mkono wake mfukoni na kutoa ufunguo wa ziada. Ufunguo mdogo wa shaba. Akafungua mlango mwingine ndani ya chumba hicho cha siri, humo Brian akaona jambo lililomshangaza.

Maiti za watu watatu!

“Wayde, ni nini hicho?” Brian akastaajabu. Wayde akamjibu huku akimtazama, “ni watoto wa Helo!”

ENDELEA

Brian aliyekuwa amepigwa na tahamaki, akajikaza kisabuni kutazama maiti zile. Hakuwa anazifahamu, na hapo ndipo akagundua ya kuwa, Brewster na Alfonso hawakuwa watoto wa Helo, kitu ambacho alikuwa anakiwaza muda wote huo.

“Nahisi hii ndiyo sababu familia yetu imekuwa salama dhidi ya Helo,” alisema Wayde huku akijongea zile maiti. Zilikuwa zimehifadhiwa kwenye kioo baada ya kukaushwa. Kama maiti hizi zingekuwa zimefungua macho basi ungeweza dhani bado ni watu waliohai.

Wayde akampatia Brian karatasi fulani na kumwambia, “Nadhani unatakiwa kuliona na hili.” Brian akaitazama karatasi aliyopewa. Ilikuwa ni barua ya kale ambayo baba yake Wayde alitumiwa na mwanamke aliyejitambulisha kwa jina la Magreth Woodland. Katika barua hiyo, huyo mwanamke alikuwa anamweleza baba yake Wayde, seneta wa Massachusetts, namna gani anavyompenda lakini pia akiwa hatarini kutokana na mapenzi yake kwake.

Ya kuwa mume wake anaonekana kuyajua mahusiano yao, amemuuliza mara kadhaa akakanusha, inawapasa wawe makini kuanzia muda huo kwa usalama wao kwani asingependa kumharibia picha ya kisiasa ya mwanaume huyo kwani ni mtu mkubwa kwenye siasa za Marekani. Kipindi hicho bado baba yake na Wayde hakuwa seneta, bali mwenye mipango ya kuwa.

Brian akamuuliza Wayde, “Magreth ni nani?” Kabla Wayde hajajibu, akampatia tena Brian barua ya pili, hii ilikuwa fupi tofati na ile ya kwanza, pia ilikuwa imetokea kwa Magreth Woodland akimshukuru baba yake Wayde kwa kumletea zawadi ya mkufu wa thamani.

Wayde akasema, “Nadhani unaweza ukawa unamjua mwanamke huyo.” Brian akatikisa kichwa. “Simfahamu. Wewe unamjua?”

Wayde akaendea kabati dogo lililokuwepo ndani ya chumba hicho akatoa picha aina ya ‘passport’ na kumkabidhi Brian.

“Bado haujamjua?” Wayde akauliza akimtazama Brian aliyekuwa anaikodolea macho picha ile. Punde akasema, “Hii sura si ngeni.”

“Umewahi kuiona wapi?” Wayde akauliza. Kidogo, Brian akapata kumbukumbu. “Niliiona kwenye ofisi ya mkuu wa - ni mke wa Dkt Hamill!”

Wayde akatikisa kichwa. “Ndio, ni yeye.”

“Baba yako alikuwa anatembea na mke wa Dkt Hamill?” Brian akauliza kana kwamba haamini alichopata kuelewa.

“Ndio,” Wayde akajibu. “Kipindi hiko kabla sijazaliwa, miaka mingi iliyopita.” Wayde akaketi kwenye kiti na kuendelea kusema, “Inaelekea baba alikuwa anampenda sana Magreth, hata leo hii hakutoa picha wala barua zake kwenye hifadhi. Najiuliza sana yu wapi huyu mwanamke?”

“Amekufa,” Brian akamjibu na kuongezea, “Dkt Hamill alimuua mkewe. Ameandika hivyo kwenye diary.”

“Kweli?” Wayde akatahamaki.

“Ndio,” Brian akajibu. “Nadhani ni kwasababu ya mahusiano ambayo Magreth alikuwa nayo na baba yako, na huo mkufu ambao Magreth anauongelea kutoka kwa baba yako, itakuwa ndiyo kitu kilichomfanya Dkt Hamill akahakiki mahusiano baina yao. Hata kwenye diary ya Dkt Hamill, mkufu huo ameuweka kwenye karatasi inayokiri kuwa amemuua kwa kumchoma kisu.”

Wayde akashangazwa sana na hizo habari, lakini Brian hakuwa amemaliza kueleza. Akasema pia kuwa Dkt Hamill aliua watoto wake watatu, wote kwa kuwachoma kisu. Hapa kila mmoja akawa na maswali. Hakuna aliyekuwa anajua kwanini Dkt Hamill alifanya tukio hilo la kinyama.

“Naomba niende, Wayde,” akasema Brian. “Tuonane kesho, nadhani nitakuwa na cha kukuambia zaidi.”

“Sawa, acha nikusindikize.” Wayde akafunga kila kitu na kutoka Brian mpaka kwenye usafiri wake, akampeleka kijana huyo nyumbani kwao.


**


“Una uhakika?” Wisconsin aliuliza akiwa anamtazama Brian kwa kukodoa.

“Ndio, kila kitu nimekiona na kuhakikisha,” Brian akajieleza. Wisconsin akatulia kidogo akiwaza. Akanyanyua kikombe cha chai na kunywa mafundo matatu kisha akasafisha koo lake.

“Kwanini Dkt Hamill aliwaua wanae?” Brian akauliza. Bado Wisconsin alikuwa amenyamaza kimya, anatazama huku na kule akiwaza. Baada ya sekunde kadhaa, akasema akinyanyuka, “Twende kwenye nyumba ya Dkt Hamill.”


**

Baada ya dakika kumi na mbili …

“Ndiyo hapa,” akasema Wisconsin. Walikuwa tayari wapo ndani ya nyumba ya marehemu Dkt Hamill upande wa nyuma. Hapo walikuwa wamesimama kwenye kaburi la Magreth Woodland, mke wa Dkt Hamill. Mikononi mwao walikuwa wamebebelea chepeo za chuma na mikono yao imefunikwa na glovu nyeusi.

Wakaanza kuchimba na kuchimba. Wakanyoosha migongo yao, wakakung’uta jasho, na kuendelea kuchimba. Haikuwa kazi nyepesi maana udongo ulikuwa mgumu wenye kujawa na kokoto. Waliweka vituo mara tatu kabla hawajafika chini kabisa. Ajabu hawakukuta kitu, si mabaki wala kitu chochote bali udongo mwekundu tu. Wisconsin akasema, “Dkt Hamill hakuwa amemzika mkewe ndani kama alivyoeleza kwenye diary.”

Brian akauliza, “Sasa atakuwa amemzika wapi?”

Wisconsin akanyamaza kidogo akiweka sawa mambo yake kichwani, alafu akasema, “Ndiyo maana Dkt Hamill aliwapoteza watoto wake, sasa napata maana.” Akamtazama Brian usoni na kusema, “Dkt Hamill atakuwa alienda kumtupia au kumfukia mkewe kule msituni. Na kwasababu hiyo basi, mkewe akaanza kutumika na Helo mpaka pale alipowatoa sadaka watoto wake watatu kumtumikia Helo.”

“Umeyajuaje hayo?” Brian akamuuliza.

“Ni Magreth pekee ndiye aliyeuawa,” Wisconsin akasema akitikisa kichwa. “Na ndiyo maana kaburi lake lipo, au ndiyo maana Dkt Hamill akadanganya kuwapo kwa kaburi lake. Ila kuhusu wanawe, hao hawajauawa, bali walipotea. Hakuna namna nyingine ya kumtuliza Helo isipokuwa kwa sadaka tu, naye Hello aliwatoa sadaka wanawe.”

“Ina maana Brewster na Alfonso si watoto wa Helo,” akasema Brian, “bali ni watoto wa Dkt Hamill?”

Wisconsin akatikisa kichwa. “Ndio. Ni watoto wa Dkt Hamill aliowatoa sadaka.”

“Mbona hawapo vivyo kwenye picha ya familia niliyoiona?” Brian akauliza.

“Brian,” Wisconsin akaita. “Unadhani baada ya Hamill kusema kuwa wanawe wamepotea, wangekuja kuonekana wakiwa na sura zilezile?”

Brian akashusha pumzi. Wisconsin akamsihi watoke ndani ya shimo waende zao nyumbani. Wakiwa njiani kuelekea huko, Brian akamuuliza Wisconsin, “Umepata kile kitu ulichokuwa unasema unakifanyia kazi?”

“Ndio,” akajibu Wisconsin. “Lakini nadhani tutafuata njia mbadala. Binti wa Seneta ammetupatia njia nzuri zaidi.”

“Ipi hiyo?” Brian akauliza. Wisconsin akasimama na kumtazama Brian kisha akamwambia,

“Tutatumia ile miili ya watoto wa Helo. Itatusaidia sana kumaliza kazi moja kwa moja. Mosi, kummaliza Helo, na vibaraka wake. Lakini pili, kuacha pia roho za hao watoto wa Helo nazo zikaenda zake.”

“Unadhani itawezekana?” Brian akauliza.

“Kwa asilimia zote, muhimu kupata tu msaada toka kwa Wayde juu ya miili ile.”

Baada ya maongezi hayo, wakaendelea na safari yao mpaka nyumbani. Hawakumwambia mtu kitu. Walijipumzisha wakiwa wamepanga kesho yake kufanya kila kitu, kuonana na Wayde na kufanya taratibu ya kuhodhi miili ile kwa matumizi.

Ukiwa ni usiku wa kuelekea saa nne, Brian akiwa ameketi sebuleni anatazama runinga, Olivia akamjongea na kumwambia, “Kuna kitu chako nimekiokota.” kisha akaingiza mkono kwenye gauni lake na kutoa mkufu ule wenye kito cha kijani.

“Umeitoa wapi?” Brian akahamaki.

“Nimeiokota,” Olivia akajibu. “Umeiokota wapi? Mbona nakumbuka niliiweka mahali salama?”

“Mimi nimeiokota chini ya kitanda chako,” Olivia akaeleza. Brian akateka mkufu ule na kuutazama akiukagua.

“Brian,” Olivia akaita. “Huo mkufu umeutoa wapi?”

Brian akatabasamu. Akauweka mkufu huo mfukoni mwake na kujibu, “Ni wangu. Kuna mtu tu amenipa.”

“Nani huyo?”

“Rafiki yangu.”

“We ni mwongo,” Olivia akasema akimtazama Brian machoni. Uso wake haukuonyesha masikhara hata kidogo. Brian kidogo akapata shaka.


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom