Simulizi: Roho yake inadai

*ROHO YAKE INADAI --- 38*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Ilikuwa ni sauti ya kike. Brian akajaribu kuwaza ni ya nani, upesi akili yake ikamkumbuka yule jirani. Ni yeye ndiye alikuja akagonga mlango muda ule alafu akasema heey!

Ina maana amekuja tena? Brian akawaza. Muda huu?

“Tafadhali,” sauti ikasema mlangoni. “…Naweza kuja kuangalia hicho kipindi?”

ENDELEA

Brian akatoa macho kwa kuduwaa lakini pia kwa woga. Akasonga hatua kadhaa kulifuata dirisha kisha akatupa macho yake nje kutazama mlangoni. Hapo akamwona jirani yao akiwa pia na mtoto wake ambaye ananesanesa kumbembeleza.

Brian akajiuliza zaidi. Akahisi mpaka kichwa chake kinamgonga kwa kuparamiwa na mawazo mengi. Ni namna gani haya mambo yanawezekana? Akaendea dirisha lilikuwepo karibu na runinga akatazama nje kwa jirani yake, akaona ni giza totoro. Sasa ameamkaje pasipo kuwasha taa?

Hodi ikagongwa tena, mara hii sauti ikasema, “Brian, nifungulie niingie!” ilikuwa si ombi bali amri! Brian akaogopa kwenda kufungua, badala yake akaenda mbali na mlango. Akiwa amekaa karibu na korido, akatazama mlangoni. Kulikuwa ni kimya. Aliwaza ni nini kitafuata. Runinga bado ilikuwa inaonyesha lakini hakuwa anaizingatia hivi sasa kama afanyavyo kule mlangoni.

Kukawa kimya kwa kama dakika nne. Brian akawaza pengine kumekuwa shwari, labda mgeni yule atakuwa ameenda zake. Akiwa hapo akijiwazia mema, akasikia mtu akiita jina lake. Haraka akageuza uso wake kutazama kule kwenye runinga. Ilikuwa ni sauti ya kike. Alipoangaza kideoni akaona sura ya mwanamke ambaye alihisi anamfahamu.

Mwanamke huyo alikuwa amevalia sare ya watumishi wa kike kanisani. Gauni jeusi na kiremba chake cheusi. Uso wake ulikuwa mweupe, wenye kutuama kihisia.

Nimemwonea wapi huyu mwanamke? Brian akajiuliza. Yule mwanamke kideoni akakunja sura yake na kutisha, akasema akimnyooshea Brian kidole, “Umeniua. Nami nitakuua!”

Brian ndipo akamkumbuka sasa mwanamke huyu. Alikuwa ni yule Dada aliyeambatana na polisi kule korongoni kanisani. Anasemaje nimemuua? Brian akajiuliza.

“Sijakuua mimi,” akasema kujitetea. Hakuwaza kama anaongea na runinga. “Sihusiki na kifo chako, sijakuua mimi!”

Yule Dada ndani ya runinga akaropoka, “Umeniua!” sauti yake ilikuwa kali na uso wake aliufuma kwa hasira. Alitoa macho na kubinua mdomo wake kana kwamba pakacha. “Nami nitakuua, Brian. Nitakufinyanga mkononi mwangu na kusagasaga mifupa yako kuwa chengachenga. Nitakuua, Brian!”

Punde Brian akahisi kuna mtu nyuma yake. Mwili wake ukapigwa ganzi ya baridi. Akapepesa macho yake akigeuka taratibu kutazama nyuma ya mgongo wake. Mara mkono wa mtu ukamtua begani na kisha sauti ya kiume ikasema, “Brian, bado hujalala?”

Kukurupuka kutazama, akakutana na Wisconsin. Akashusha pumzi ya hofu na mkono wake wa kuume akauweka kifuani kupooza mapigo yake ya moyo.

“Ni wewe!”

“Ndio, ni mimi. Mbona hujalala mpaka saa hii? Ulikuwa unaongea na nani?”

Brian akatazama runinga, ilikuwa kimya na imezima, akastaajabu akiinyooshea kidole, “Kuna mtu … kuna mtu alikuwapo ndani ya runinga!”

“Ulikuwa unatazama runinga mpaka sasa?”

“Hapana! Kuna mtu alikuwepo ndani ya runinga akiongea na mimi!”

Wisconsin akarusha macho kwenye runinga. Hakuona kitu. Akayarudisha kwa Brian. “Una uhakika?”

“Ndio. Kuna mtu alikuwepo kwenye runinga!” Brian akasihi akionyeshea kidole runingani.

“Ni nani?” Wisconsin akauliza. “Alikuwa anasema nini?”

“Alikuwa ni yule Dada aliyekuwa na polisi kule korongoni kanisani! …” Brian akajibu. “ … anadai mimi nimemuua. Anasema naye pia ataniua!”

Wisconsin akakunja ndita za kushangazwa asiseme jambo. Akakagua sebule na kisha akatupa macho yake nje ya dirisha. Hakuona kitu. Akamtaka Brian aende kupumzika.

“Siku ya leo ilikuwa ndefu sana kwako. Umefanya mambo mengi na mazito lakini hujapata muda wa kupumzika. Nenda kalale, Brian. Kapumzishe mwili wako.”

Brian akaendea chumba chake akichechemea. Kweli alikuwa amechoka. Macho yake yalikuwa mekundu na uso wake ukiwa umeelemewa kwa uchovu. Alijitupa kitandani, akasikia sauti ya mlango wa chumba alalacho Wisconsin kikiwa kinafungwa.

Akatazama chumba chake akitafuta usingizi. Muda si mrefu, usingizi ukambeba na kumfanya asijitambue kwa muda. Akalala fofofo akikoroma.

Asubuhi ya saa mbili akaamshwa na sauti fulani ya kipaza sauti. Akajibandua kitandani na kujinyoosha. Mwili wake ulikuwa umejawa na maumivu karibia kila sehemu. Wakati anajinyoosha alijikuta akilalamika kwa maumivu huku akikunja sura kana kwamba amelamba ndimu.

Akasonga dirishani na kuangaza nje. Mwanga wa jua ulikuwa safi, watu walikuwa wanakatiza hapa na pale. Miongoni mwao alikuwa ni mwanaume mzee aliyebebea kipaza sauti akitangaza. Huyu ndiye aliyefanya Brian akaamka.

Brian akatega sikio amsikie ni nini anasema. Alipofanya hivyo akagundua mtu huyo alikuwa akitangaza kuhusu msiba wa mmoja wa wafanyakazi wa muda mrefu wa ofisi ya mtaa wao. Naye si mwingine bali bwana Brewster.

Kwa mujibu wa mtangazaji, Bwana Brewster amekutwa akiwa amefariki nyumbani kwake kwa kile wanachoamini kuwa ni mshtuko wa moyo. Hivyo basi kwakuwa mzee huyo aliitumikia serikali kwa karibu maisha yake yote, basi serikali itasimamia kila kitu msibani. Watu tu wanaomba wafike kumpa heshima zake za mwisho kwenye ardhi ya makaburi.

Bwana huyo akatokomea akitangaza. Akamwacha Brian akiwa na maswali juu ya tangazo hilo. Amekutwa ndani? Mosi. Amekufa kwa mshtuko wa moyo? Pili. Akajiuliza mwenyewe asiwe na majibu. Akatoka hapo dirishani na kwenda sebuleni. Akamkuta Wisconsin, Olivia na Mama wakiwa wamekaa wanapata kifungua kinywa. Baada ya salamu, akawauliza, “Mmesikia tangazo hilo?”

“Lipi?” Mama akauliza.

“La Brewster?” Wisconsin naye akatupa swali lake akimtazama Brian kwa macho ya nje ya kikombe cha chai.

“Ndio la Brewster!” Brian akajibu. Wisconsin akamwambia,

“Ndio, tumesikia. Nadhani itabidi tuhudhurie msiba huo. Nimeshamweleza mama yako hapa.”

“Kwanini?”

“Kwani huwa hamna desturi ya kuhudhuria misiba?”

“Tunayo, ila si kwa mtu kama Brewster!”

“Hastahili kuzikwa? … Brian, kaa chini.”

Brian akaketi akimtazama Wisconsin.

“Umelisikia hilo tangazo, si ndio? Na kwasababu umesikia tofauti na unavyojua ndiyo maana ukakimbilia hapa kuja kutuambia, sio? … sasa kama umesikia usilolijua hapo tu kwenye tangazo, utayasikia mangapi msibani?”

Kabla Brian hajajibu, Wisconsin akanywa fundo moja kubwa la chai na kukiweka kikombe mezani kikiwa kitupu. Akasema, “Tutaenda huko asubuhi. Liweke hilo kwenye ratiba yako, sawa?”

Brian akatikisa kichwa asiseme jambo. Mama akamuuliza, “Nikupatie chai?” napo akatikisa kichwa. “Hapana, niko sawa.”

“Leo hutaenda shule, sio?” Wisconsin akamuuliza.

“Sitaenda,” akajibu na kuongezea, “Nimeshachelewa.”

Wisconsin akasafisha koo lake na kusema, “Mama yako amenambia kilichojiri jana wakati sikuwapo. Ulisema unajua kile kituo cha habari kilipo?”

“Ndio, najua.”

“Basi waweza jiandaa tukaenda huko?”

“Sasa hivi?”

“Ndio, au una kazi ya kufanya?”

Brian akatikisa kichwa.

Basi baada ya nusu saa wakawa tayari wamejiandaa. Wakachukua gari la Mama kuelekea kule kwenye kile kituo ambacho walifanya mahojiano na yule binti aliyepotea na kisha kupatikana. Kwakuwa Brian alikuwa na majeraha, Wisconsin akashikilia usukani.

Mama akawasihi, “Tafadhalini kuweni makini.”

“Usijali,” Wisconsin akamtoa hofu. “Tutafanya hilo kadiri tuwezavyo.” kisha akawasha gari na kutimka.

Wakatembea kwa muda wa takribani lisaa limoja na dakika kumi na saba, ndipo wakafika mbele ya studio ya chombo hicho cha habari. Wakaegesha gari kando na kusonga ofisini.

“Naweza kuwasaidia?” aliuliza mwanadada wa mapokezi. Alikuwa amevalia sare, shati jeupe na kizibao cheusi chenye chapa ya chombo chao cha habari kifuani.

“Tunahitaji kuonana na mwandishi fulani wa habari,” akasema Wisconsin. Brian akadakia, “Yule aliyemfanyia mahojiano mtoto aliyepotea.”

Mdada yule wa mapokezi akawatazama na kuwauliza, “nyie ni wakina nani?” wakati anauliza, akasogeza mkono wake kufuata simu yake ya mezani. Uso wake ulionyesha mashaka.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 39*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Tunahitaji kuonana na mwandishi fulani wa habari,” akasema Wisconsin. Brian akadakia, “Yule aliyemfanyia mahojiano mtoto aliyepotea.”

Mdada yule wa mapokezi akawatazama na kuwauliza, “nyie ni wakina nani?” wakati anauliza, akasogeza mkono wake kufuata simu yake ya mezani. Uso wake ulionyesha mashaka.

ENDELEA

“Sisi ni ndugu zake na yule mtoto,” Brian akawahi kujibu.

“Nani yake?” Dada wa mapokezi akauliza. Brian akamgusa Wisconsin na kusema, “huyu ni mjomba wake,” kisha akajionyeshea kidole na yeye, “mimi ni binamu yake.”

“Kwani hamjui anapokaa?”

“Tunapajua, ila tumekuja hapa kwa ajili ya yule mtangazaji na si mtoto,” akajibu Wisconsin.

Dada yule akawatazama kwa sekunde chache. Mkono wake ulikuwa tayari umeshikilia simu ya mezani. Akauliza,

“Mnamtakia nini bwana huyo?”

Brian akamjibu, “Kuna mambo tunataka kumwambia zaidi ambayo pengine hayafahamu.”

Dada yule baada ya kuwatazama tena kidogo, akatoa mkono wake kwenye simu na kushusha pumzi ndefu. Akawaomba wakina Brian waketi kwenye kiti kwa muda mchache. Brian na Wisconsin wakatii, wakaendea sofa lililokuwapo hapo, wakaketi kungoja.

Yule dada akaongea na simu kwa dakika moja kisha akarejesha simu mezani na kuendelea na kazi yake. Baada ya dakika kama tatu, simu ikaita, akapokea na kuongea nayo kwa kama dakika moja na nusu kisha akawaita wakina Brian.

“Mtu mnayemhitaji, hayupo kwa sasa. Tulitarajia atakuja kazini lakini imeshindikana. Mnaweza kwenda mkarejea siku nyingine.”

Dada aliposema hayo, akaendelea na kazi yake ya kushika makaratasi. Brian na Wisconsin wakatazamana kwa maulizo kisha Brian akauliza, “Samahani, unaweza kutuambia alipo? Tunaweza kumfuata maana tuna usafiri.”

Basi baada ya kumbembeleza huyo dada, akakubali na kuwapatia anwani ya makazi ya huyo mtangazaji. Wakamshukuru na kwenda zao kufuata chombo kilichowaleta, wakatimka kuelekea katikati ya mji wa Boston. Walipotembea kwa takribani robo saa, wakawa wamewasili mbele ya jengo la ghorofa ambapo hapo waliegesha gari lao na kuanza safari ya kwenda kwenye chumba walichoelekezwa.

Hili lilikuwa ni miongoni mwa maghorofa ya muda mrefu hapa Boston. Yalikuwa ni maghorofa mapacha yaliyopakana, ila hili walilopo wakina Brian lilikuwa ni refu zaidi.

Wakasonga na ngazi mpaka kwenye sakafu ya tano, hapo wakaendea upande wao wa kushoto na kukomea kwenye mlango uliopachikwa nambari 455. Wakagonga mara tatu.

Kimya.

Wakagonga tena na tena, bado kimya. Brian akachungulia kwenye tundu la komeo kama ataona ufunguo, haukuwepo. Akakagua chumba hicho kwa kupitia kitundu hicho, hakumwona mtu. Vitu vilikuwa vuruguvurugu.

Na kwakuwa kitundu ni kidogo, hakuona vema chumba kizima. Alitamani atazame zaidi. Akiwa anachungulia akagundua kuwa dirisha, kule upande wa mbali ukutani, lilikuwa wazi. Akaona ni fursa nzuri ya kutazama chumba hicho.

“Tuzunguke kwa nyuma,” akamwambia Wisconsin.

“Kufanya nini?”

“Dirisha lipo wazi. Twenda tukatazamie chumba huko!”

Wakiwa hapo wanateta, kuna jirani mmoja, mwanamke mzee, alikuwa anawatazama tangu mwanzo. Bibi huyo, akatokea kuwahisi vibaya. Alidhani huenda wakawa wezi kwa namna walivyokuwa wanahangaika mlangoni pale.

Na alivyowaona wakina Brian wakielekea upande wa nyuma ya jengo, akapata mashaka zaidi. Alitazama kando na kando amwambie mtu yeyote juu ya mashaka yake lakini hakukuwapo na mtu. Chumba kizima alikuwa mwenyewe.

“Unaona,” Brian akasema wakiwa wanatupa macho ndani ya chumba. Kitanda kilikuwa kimevurugwa, kuna vikombe chini na sahani iliyopasuka. Walipotazama vema, wakagundua hata mashuka yale yalikuwa yamechanika.

“Kuna nini kimetokea humu ndani?” akauliza Wisconsin kwa kuduwaa kisha akasema “inaoyesha mwenyeji hajatoka humu ndani, umeona viatu vyake …” akaonyeshea kidole pembeni ya mlango, hapo kulikuwa na viatu, kimoja kimesimama wakati kingine kikiwa kimelala.

Brian akauliza, “Vipi kama ana viatu vingine?” Wisconsin akamwonyeshea stendi ya viatu na kumwambia, “basi vile angekuwa kavirejeshea mahala pake.”

Punde kidogo, Brian akaropoka, “Ona kule!” alikuwa amenyooshea mlango wa bafu. Mlango huo ulikuwa ni wa kioo kinachohakisi kwa uhafifu. Kwa chini yake, ilionekana kitu kama damu.

Wisconsin akasema, “yatupasa tuingie ndani. Ukute amekufa, hakuna mtu anayejua!”

Basi kwa kupitia dirisha, wakazama ndani. Kabla hawajapekuapekua, wakanyookea moja kwa moja bafuni kutazama damu ile inatokea wapi. Huko wakakuta mwili wa mtangazaji wanayemtafuta ukiwa upo chini umevuja damu lukuki toka kichwani.

Bafu zima limejawa na damu. Mkononi mwa mwanaume huyo alikuwa ameshikilia sabuni ya kuogea akiwa uchi wa mnyama.

“Amedondoka!” akasema Brian akiwa ametumbua macho. Wisconsin akatikisa kichwa, “Hapana, ameuawa!” Kisha wakatoka ndani ya bafu na kutazama mule chumbani, “Kama angekuwa ameanguka huko bafuni, kwanini shuka limechanwa na vyombo vikapasuliwa? … tazama!” Wisconsin akaonyeshea mlangoni mwa bafuni. “Hata viatu vyake vya kuogea, hakuvaa!”

Brian akauliza, “Sasa nani atakuwa amemuua?”

“Mtu mwenye matumizi naye,” akajibu Wisconsin na kuongezea, “mtu ambaye hataki awe hai.”

“Nani huyo?”

“Brian,” Wisconsin akaita na kumtazama kijana huyo, akamuuliza, “Leo umeona tangazo la watoto kupotea?”

“Hapana!” Brian akatikisa kichwa.

“Basi huyo anayepoteza watoto, atakuwa alikuwa hapa usiku.” kitendo cha Wisconsin kumaliza kuongea kauli hiyo, dirisha likacheza baada ya upepo kupuliza ghafla. Wote wakalitazama.

Kabla hawajafanya kitu, mara dirisha likajifunga na kujitia ‘lock’. ilikuwa ni ajabu kwani hakukuwa na mtu aliyefanya hivyo. Dirisha lilijibana vema kana limesogezwa na mtu. Na kama haitoshi, pazia nalo ambalo lilikuwa wazi, likasonga na kujifunika.

Ndani kukawa na giza!

Brian akamshika mkono Wisconsin wakiwa wamestaajabu. Ndani ya muda mfupi, wakasikia sauti ya maji yakiwa yanamiminika huko bafuni kisha ikafuatiwa na sauti ya mtu akiwa anapiga mluzi.

Moyo wa Brian ukaanza kwenda mbio. Wisconsin naye akatetemeshwa na wakisikiacho. Haraka wakaendea mlango na kujaribu kuufungua, haukufunguka. Wakatazama kuutafuta ufunguo, mara ufunguo ukarushwa tokea bafuni.

Haraka Brian akauchukua na kuchokonolea mlango, bado mlango haukufunguka! Brian akapayuka, “Si wenyewe!” huku akimtazama Wisconsin kwa macho ya hofu.

Kidogo tena, ufunguo ukarushwa tokea chini ya mlango wa bafuni. Brian kabla hajauokota, akamtazama kwanza Wisconsin kana kwamba anahitaji ruhusa alafu haraka akaukwapua ufunguo ule na kuchokonolea mlango.

Bado haukufunguka.

Akiwa anahangaika, ufunguo mwingine ukarushwa, wa tatu sasa kwa idadi, lakini nao haukufungua mlango. Sasa wakawa hawana matumaini na funguo zile zirushwazo.

Maandishi yakaandikwa kwenye kioo cha mlango wa bafuni. Kwakuwa kulikuwa na unyevu wa maji, yakaonekana vema japo yaliandikwa kwa ndani. Maandishi hayo yalisomeka,

“Hakuna Ufunguo Wa Kuwatoa Mkiwa Hai.”

Walipoyasoma, mkono ukayafuta na mara mlango ukaanza kufunguka taratibu. Brian na Wisconsin wakaanza kusonga mbali kusogelea dirishani. Mlango ukakoma kufunguka, na ghafla humo ndani akatoka kiumbe ambacho hawakukitambua. Kilikuwa ni cheusi, chenye mwili mpana na mrefu.

Kikamjia Wisconsin na kumkaba kwanguvu. Kikamnyanyua juu na kumtupia ukutani ambapo alijibamiza na kudondoka chini. Kichwa kikamgonga na punde akazirai. Kiumbe kile kikamgeukia Brian!

Brian akatoa macho na kuhisi anakosa pumzi.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 40*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Kikamjia Wisconsin na kumkaba kwanguvu. Kikamnyanyua juu na kumtupia ukutani ambapo alijibamiza na kudondoka chini. Kichwa kikamgonga na punde akazirai. Kiumbe kile kikamgeukia Brian!

Brian akatoa macho na kuhisi anakosa pumzi.

ENDELEA

Haraka akanyakwa koo na kunyanyuliwa juu, kisha kama Wisconsin alivyofanywa, naye akatupwa kana kwamba unyonya. Akabamiza ukutani na kudondoka chini! Mbaya akakita kiuno chake kwenye kingo ya kitanda. Akalalama kwa maumivu makali aliyoyapata!

Yule kiumbe, ambaye bado hakumtambua, akamjongea tena upesi alafu kama mpshi akagawanyika na kumvaa Brian puani na mdomoni. Brian akaanza kukohoa kana kwamba anakata roho. Akatoa macho akikohoa. Mpaka mishipa ya damu ikamsimama kichwani akipambana kudaka shingo yake.

Alikuwa anaelekea kufa!

Ni kheri muda kidogo mlango ukabamizwa na punde ukafunguliwa kwa kuvunjwa! Wakaingia ndani wanaume wawili waliovalia sare za polisi, hamaki wakawaona Brian na Wisconsin wakiwa kwenye hali mbaya. Haraka, katika namna ya ajabu, Brian akajikuta anapata ahueni na lile fukuto lililokuwa linamkaba na kuminya viungo vyake vya hewa likamwacha akiwa anapambania pumzi kana kwamba mwana mroho aliyeona chakula baada ya miaka kenda.

Polisi wakapiga simu kwa watoa huduma za afya za dharura, baada ya muda mfupi wakawasili na kuwapatia huduma Wisconsin na Brian. Maiti iliyokuwepo ndani ikachukuliwa na kusafirishwa kwenda hospitali kwa matunzo.

Wisconsin aliporejea kwenye fahamu zake na Brian pia kupata unafuu wa kumwezesha kuongea, wakahojiwa na polisi.

“Tulimkuta akiwa amekufa,” alisema Brian, “Inaonekana alikufa tangu usiku wa kuamkia leo hii, na ajabu ni kwamba muuaji bado alikuwepo ndani ya eneo.” wakati akizungumza, polisi alitega sikio lake vema akimtazama Brian kwa umakini.

Polisi huyu alikuwa ndiye yule ambaye alimfanyia mahojiano Mama Brian baada ya lile tukio la mapolisi wawili kuuawa mbele ya nyumba yake na mtu asiyejulikana. Kwa jina polisi huyu aitwa Afisa Randall.

Akauliza, “Mnaweza kumtambua muuaji huyo?” Brian akatikisa kichwa na kujibu, “hapana. Hakuwa anaonekana usoni. Alikuwa ni kiumbe cha ajabu hakika!”

Afisa Randall akashusha pumzi na kutikisa kichwa chake. “Umesema unaitwa Brian, sio?”

“Ndio.”

“Brian,” afisa Randall akaita na kusema, “Hatufanyi maigizo hapa bwana Brian. Hii ni kesi kubwa. Kesi ya mauaji. Tafadhali nipatie taarifa zenye mantiki.”

Wisconsin akadakia kwa kusema, “Anachosema ni ukweli mtupu.” Sasa afisa Randall akamtazama Wisconsin aliyekuwa amekaa pembeni ya Brian.

“Tuliukuta mwili wa marehemu ukiwa bafuni, umelala mfu. Mkononi mwake kulikuwa na sabuni kavu na kwenye mlango wa bafu kukiwa na viatu vya kuogea ambavyo hakuvitumia. Chumba chake kilikuwa shaghalabaghala. Alipambania roho yake chumbani kabla hajapelekwa kuuawa huko bafuni!”

Afisa Randall akauliza, “na ninyi mliingiaje ndani kwake ingali palifungwa?”

“Kwakupitia dirishani,” Brian akawahi kujibu. “dirisha lilikuwa wazi. Baada ya kuchungulia kwenye tundu la mlango tulibaini hilo na kuamua kutumia njia hiyo kuzama ndani.”

“Kutokana na hicho mlichokifanya, nikiwaita ninyi ni wezi ama wauaji nitakuwa nimekosea? Vipi kama ni ninyi ndiyo mliomuua na kisha mkatengeneza mazingira?”

“Hatujamuua. Hatuna sababu ya kumuua!” Brian akajitetea.

Afisa Randall akabinua mdomo wake na kuuliza, “mlivyoona kuna dalili za hatari, kwanini hamkutoa taarifa polisi badala ya kuvunja na kuzama ndani mwa watu pasipo ruhusa?”

Swali hili likawa gumu. Afisa Randall akawatazama na kisha akasema akitazama kushoto kwake kwa mbali, “mnamwona yule bibi? … ndiye ambaye alitoa taarifa juu yenu baada ya kuwahisi vibaya … mnadhani alikosea?”

“Hapana,” Wisconsin akasema na kujitetea, “Hatukuwa na namna ya karibu ya kuwasiliana na polisi kwa-”

“Vipi kuhusu majirani?” Afisa Randall akamkatisha. Na asisubirie majibu akanyanyuka na kuwataka Wisconsin na Brian wazame ndani ya gari waende kituo cha polisi kwani wana kesi ya kujibu. Tena kesi ya mauaji.

Wakiwa wameduwazwa, wakazamishwa ndani ya chombo na kutimka.

Baada ya masaa matatu ..

Ngo ngo ngo ngo!

“Nakujaa!” Mama Brian akapayuka. Alikuwa jikoni akifuta vyombo alivyotoka kuviosha akiwa pamoja na Olivia. Kwa ishara ya kichwa, akamonyeshea Olivia njia na kumwambia, “nenda katazame ni nani.”

Olivia akaenda zake. Baada ya sekunde chache, akarudi na kumwambia mama, “Ni polisi.”

“Polisi?” Mama Brian akauliza kana kwamba hakusikia, Olivia akamjibu kwa kutikisa kichwa. Akajifuta maji akiwaza nini kitakuwa kimetokea. Taratibu akaenda sebuleni na uso kwa uso akakutana na Afisa Randall. Sura ya afisa huyo aliikumbuka vema.

“Karibu.”

“Ahsante.”

Mama Brian akaketi na kisha akamtazama afisa kwa macho ya maulizo. Kunani?

Baada ya maongezi mafupi, wakajikuta hapa …

“Walisema wanaenda kwenye kituo fulani cha habari kuonana na mmoja wa watangazaji,” Mama Brian akasema akiwa na taharuki usoni mwake. Afisa Randall akamuuliza, “Mtangazaji gani na kwasababu gani?”

Mama Brian akaeleza sababu aijuayo yeye ya kwamba walihitaji maelezo zaidi juu ya yule mtoto aliyepotea na kuonekana tena. Habari hizo zikamsisimua Afisa. “Wakakueleza nini juu ya hilo?” akauliza.

“Hamna kitu,” Mama Brian akajibu. “Tangu walipotoka hapa sijapata kuwaona mpaka sasa.”

Afisa akamtaka mwanamke huyo ajiandae waongozane wote kwenda kwenye kituo hicho cha habari ambapo ndipo alipodai Brian na Wisconsin walimuaga kuendea. Basi baada ya muda mfupi, Mama huyo akawa tayari kuongozana na afisa.

“Nakuja muda si mrefu, sawa?” akamwambia Olivia kisha akambusu kwenye paji lake la uso kumuaga.


**

“Unadhani tutafungwa?” akauliza Brian. Alikuwa amejikunyata ndani ya chumba cha mahabusu, pembeni yake akiwa amekalia Wisconsin. Ndani ya chumba hicho kulikuwa na watu wanne kwa idadi. Kila mmoja alionekana ana lake.

“Kama hawatatuamini, basi tutafungwa,” akasema Wisconsin. “Unajua Brian, kuna dunia za aina mbili, ule ambapo upo kitabuni na ule ambao upo fikirani. Ule ambao upo mwangani na ule wa gizani. Polisi na mahakama wanatambua ulimwengu mmoja tu, ule wa kitabuni, waasadiki wanachokiona na kukigusa.

Wapo kwenye mwanga, hivyo hawataki kuamini kama kuna giza. Lakini mwanga utakujaje pasipo ya giza? Ni giza ndiyo inafanya kuwapo kwa mwanga. Na mwanga ufanya kuwepo kwa giza.”

“Unajaribu kumaanisha nini?” Brian akauliza. Wisconsin akamtazama kijana huyo, kabla hajasema kitu, wakasikia sauti za vishindo, wakatazama nje ya mahabusu. Punde wakamwona polisi ambaye alifungua lango na kuwataka watoke na kuongozana naye.

**

Baada ya lisaa limoja na nusu.

Gari lilikuwa njiani kuelekea nyumbani, ndani yake alikuwapo Mama Brian, Wisconsin na Brian. Mama alikuwa ameshikilia usukani, Wisconsin akiwa ameketi kiti cha kando na dereva na Brian amekalia nyuma peke yake.

Ukimya haukudumu muda mrefu, Wisconsin akauliza, “Yule binti alisemaje kule polisi? Mbona imekuwa rahisi kututoa mule?”

Mama Brian akajibu akitazama mbele waelekeapo, “alisema yale yote ambayo yalimwondolea mashaka afisa Randall kuwa ninyi hamhusiki na yale mauaji.”

“Yapi hayo?” Wisconsin akaongezea swali.

“Ni hivi,” Mama Brian akaanza kueleza, “Tangu binti yule aliyekuwa amepotea kupatikana, mtangazaji yule alianza kumfuatilia akitaka taarifa zake. Alipompata na kukubali kufanya kipindi, akapokea vitisho toka kwa mtu asiyejulikana kwa njia za barua, na isitoshe mtu huyo akamwambia mpaka na muda ataokuja kumuua.

Akapuuzia na kuendelea na kazi yake, japo alifikisha mashtaka yake hayo kwa ofisi za uongozi. Ajabu ni kwamba, aliuawa kama ambavyo aliambiwa, muda na siku ileile.”

“Mmejuaje kama ni muda uleule?” Wisconsin akauliza.

“Kwa mujibu wa chunguzi za marehemu, mwili wake ulipoteza moto kwa makadirio ya masaa sita nyuma kabla ya kupambazuka.”

“Vipi kuhusu barua hizo?” akauliza Brian. “Wameshindwa kujua zilitumwa toka anwani gani?”

Mama akanyamaza kidogo na kisha akasema, “wamegundua zimetokea wapi. Japo mwandishi hakufahamika, ila mtindo wa bahasha ulionyesha zilipotokea.”

Wisconsin akauliza upesi, “Ni wapi huko?”

“Kanisani,” Mama akajibu.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 41*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Mama akanyamaza kidogo na kisha akasema, “wamegundua zimetokea wapi. Japo mwandishi hakufahamika, ila mtindo wa bahasha ulionyesha zilipotokea.”

Wisconsin akauliza upesi, “Ni wapi huko?”

“Kanisani,” Mama akajibu.

ENDELEA

“Kanisani?” wakaduwaa. Mama akatikisa kichwa na kusema. “Ndio, kanisani. Hata kwetu ilikuwa ngumu kuamini, ila ndivyo ushahidi ulivyokuwa unasema. Uzuri barua zote ambazo bwana yule mtangazaji alizopokea, alizikabidhi ofisini kwa hiyo yule dada aliziwasilisha na zote zikasomwa pale.”

“Sasa polisi wanafanyaje?” Brian akauliza.

“Wanalifuatlia hivi sasa,” Mama akajibu. “Kesho tutarudi tena kituoni nadhani tutakuwa tumepata majibu toka huko.”


**


“Ni afisa wa polisi,” alisema Dada Magdalena punde baada ya kuingia kwenye chumba cha padri Alfonso. Mwanaume huyo akakunja uso wake kuonyesha mashaka, alafu akasema, “mruhusu aingie.”

Kabla Dada Magdalena hajaenda, akamuuliza, “Una uhakika?”

“Usijali, hamna shida,” Padri akamtoa hofu. Basi Dada Magdalena akaenda zake na punde Afisa Randall akaingia na kuketi kitini. Mkononi mwake alikuwa na bahasha rangi ya kaki. Wakasalimiana na Padri na kueleza haja iliyomleta hapo.

“Samahani sana kwa ujio wangu wa ghafla,” akasema huku akifungua bahasha alokuja nayo. “Nimelazimika kuja hapa kwa mara nyingine kwasababu zisizozuilika.” akatoa barua zile mfukoni mwa bahasha alafu akaziweka mezani na kumtazama Padri Alfonso usoni. Akamuuliza, “Unazijua hizo barua?”

Padri Alfonso akaziteka kwa mkono wake na kuzikagua. Hakuwa na miwani. Akafungua droo na kuitoa, akaivesha usoni na kuendelea kukagua. Muda kidogo akabinua mdomo wake na kumtazama afisa Randall, “hapana, sizitambui,” akajibu na kuuliza, “Ni wapi umezitoa?”

“Kabla hujaanza kuniuliza, inabidi umalize maswali yangu kwanza,” Afisa akamtanabaisha na kisha akamuuliza, “Umeona chapa kwenye kona ya bahasha?”

“Ndio nimeona la--”

“Ni ya nani?” Afisa akamkatisha kidoomo. Alikuwa anamtazama machoni asitake kupoteza hata sekunde moja mbali.

“Ni-ni ya kanisa,” akasema Padri Alfonso, “Ila si--”

“Imefikaje hapo kwenye bahasha?”

“Sitambui!” Padri Alfonso akatahamaki. “Kama ilivyo kwako, nami sitambui!”

Afisa Randall akamtazama kwa sekunde chache kisha akamtaka awasilishe bahasha za kanisa zilizopo ofisini. Padri Alfonso akatii amri. Akanyanyuka na kuendea kabati kisha akatoa ‘package’ ya bahasha mpya na kumpatia Afisa. Afisa akasema,

“Nahitaji pia na zile ambazo zimeshatumika.”

Kidogo Padri Alfonso akasita, ila hakuwa na budi kutoa. Akainamisha mgongo wake na kumpatia kifurushi hicho Afisa.

Kwa muda kidogo afisa Randall akakagua hivyo vifurushi alafu akamwambia Padri Alfonso, “Bila shaka huwa unatunza kumbukumbu ya barua zako.”

“Ndio,” Padri akajibu akitikisa kichwa. “Huwa nafanya hivyo.”

Afisa akamwambia, “naomba na hizo rekodi kama hutojali.” hapa Padri Alfonso akasita tena. Wakatazamana na Afisa kwa sekunde mbili kabla hajafungua droo ya mezani na kumtolea rekodi za barua. Afisa akaendelea kukagua.

Akatumia kama dakika tano, kisha akaweka vitu kando na kumuuliza Padri Alfonso, “Kuna barua ambayo huwa unaandika na kutuma pasipo kuweka rekodi?”

Padri akatikisa kichwa. “Hapana, ni kinyume na utaratibu wa matumizi ya mali za kanisa.”

“Vema,” Afisa akatikisa kichwa na kuuliza tena, “Kuna mtu yeyote ambaye huandika barua mbali na wewe?”

“Ndio,” akajibu Padri. “Ila afanyavy hivyo basi lazima niwe na taarifa kama kiongozi.”

“Na rekodi hutunzwa?”

“Ndio. Ni lazima itunzwe.”

“Vema. Sasa mbona kuna barua tatu ambazo zimetoka pasipo rekodi?” Afisa akauliza akimkazia macho Padri Alfonso. Padri akawaka, “Barua gani hizo?”

Ndipo Afisa Randall akamwambia kwa mujibu wa kifurushi kipya cha bahasha, huwa ndani kunakuwa na bahasha sitini kwa mkupuo, lakini kifurushi kile ambacho kimetumika, kwa mahesabu, bahasha ishirini na tatu zimeshatoka, ila kwenye rekodi, ni bahasha ishirini na tatu tu ndizo zenye maelezo ya kubeba na kutuma barua. Sasa swali likaja,

“Hizo bahasha tatu zimeenda wapi?” afisa Randall akauliza, Padri Alfonso akakosa cha kujibu. Akadaka vile vifurushi vya bahasha pamoja pia na rekodi zake akaanza kuvikagua upya kuhakikisha kile ambacho afisa Randall amekisema.

Afisa akampatia muda huo. Akahangaika kwa takribani dakika kumi, hamna cha tofauti. Bahasha tatu hazikujulikana zimeenda wapi. Jasho likamtoka.

“Afisa, huenda kuna mtu ambaye atakuwa ametumia bahasha hizo,” akajitetea.

“Ila ulisema lazima kuwe na rekodi,” Afisa akamkumbushia na kisha kuongezea, “Na kama kulitokea tukio la wizi basi ungekuwa umetoa taarifa polisi tukalifahamu.”

Padri akakosa la kusema. Akatoa leso yake na kujifuta jasho. Afisa akamtazama na kumwambia, “Naomba kukagua eneo.”

“Eneo gani, afisa?”

“Ulalapo, kanisani … na pia kule korongoni.”

“Korongoni? … si mlishapakagua?”

“Nitakapakagua tena leo hii.”

“Sawa,” akasema Padri Alfonso na kisha akamwita Dada Magdalena. “Utaongozana na afisa hapa kwenye ukaguzi” akaagiza, ila Afisa akapinga na kusema, “Tutakuwa wote. Naomba tuongozane pamoja, giza linakaribia.” Padri Alfonso akatazama na Dada Magdalena pasipo kusema jambo.

Majira yalikuwa ni ya saa kumi na moja. Jua lilianza kusinyaa na kupoteza nguvu yake. Ndege waoga walishaanza kurejesha mbawa zao kwenye viota.

Basi Padri Alfonso, kwa kufuata maagizo, akaambatana na Afisa kwenda kanisani. Wakakagua na kuona kila kitu ni chema. Baada ya hapo, wakaenda chumbani mwa Padri Alfonso, napo wakakagua na kuona kila kitu ni chema. Sasa kukawa kumebakia kule korongoni.

“Kutakuwa na giza sasa, utaona kweli?” Padri Alfonso akauliza. “Nimekuja na kurunzi, usijali.” Afisa Randall akamjibu na kisha wakaeleka kwenye gari alilokuja nalo, huko wakamkuta afisa mwingine wa polisi, kwa jina Williamson, akampatia Afisa Randall kurunzi kubwa na kumuuliza, “Vipi twende wote?”

“Hapana, sitachukua muda mrefu,” Afisa Randall akajibu alafu akiongozana na Padri wakaelekea na kuzama korongoni. Kiza kilikuwa kimeshaanza kujijenga humo kutokana na uwingi wa miti. Afisa Randall akatazama huku na huko akirusha kurunzi.

Wakatembea kwa takribani dakika sita, wakawa wamezama kabisa kwenye moyo wa korongo. Hakukuwa na kitu ambacho Afisa Randall alikiona. Akasema, “Turudi.”

Wakiwa wanarudi, baada ya kutembea kwa dakika moja na nusu, afisa akamulika kitu fulani kwenye kingo ya korongo. Kitu hicho kilikuwa kinang’aa mithili ya kioo. Akakisogelea kwa ukaribu akitazame.

Akagundua ni bangili. Akafukuafukua kwa kutumia mkono wake, akaja kugundua bangili hiyo ilikuwa pamoja na kiatu kidogo cha kike. Akapata hamu ya kufukua zaidi. Akatumia mkono wake, kwakuwa udongo ulikuwa mlaini basi haikuwa tabu.

Akafukua zaidi na zaidi, mwishowe akakutana na mkono wa mtoto mdogo. Akastaajabu. Akamtazamia Padri na kumtaka watoke korongoni humo.

“Sihusiki na hicho kitu!” Padri akajitetea wakiwa wanatembea kutoka korongoni. “Sitambui kimefikaje huko. Kanisa halihusiki!”

Afisa hakusikiliza, akaendelea kutembea zake. Walipofika kwenye gari, akaudumbukiza mkono ule kwenye mfuko mwepesi wa nailoni na kuuhifadhi. Kisha akamwambia Padri Alfonso, “Nakuhitaji kesho asubuhi na mapema kituoni.” kisha wakawasha gari na kwenda zao.

Padri Alfonso akang’ata meno yake akitazama gari hilo likiishia. Muda si mrefu Dada Magdalena akaungana naye kutazama mapolisi hao wakiyoyoma, akauliza, “Sasa tunafanyaje?”

Padri Alfonso akawa kimya. Akavuta na kushusha pumzi ndefu pasipo kutia neno. Dada Magdalena akamuliza, “Kwanini haukummalizia kulekule korongoni?”

Padri akamtazama na kumrudishia swali, “huoni ingekuwa hatari? … kummalizia kule korongoni kungetuweka wazi kuwa sisi ndiyo tumemuua polisi.”

“Sasa tunafanyaje na ameondoka na vitu vile?” Dada Magdalena akauliza akiwa na shaka. Padri Alfonso akatabasamu, “tunafanyaje? Yani unauliza tunafanyaje? Kwani hujui huwa tunafanyaje?”

Dada Magdalena naye akatabasamu.

Hawakutia tena neno lingine.


**
 
*ROHO YAKE INADAI --- 42*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Sasa tunafanyaje na ameondoka na vitu vile?” Dada Magdalena akauliza akiwa na shaka. Padri Alfonso akatabasamu, “tunafanyaje? Yani unauliza tunafanyaje? Kwani hujui huwa tunafanyaje?”

Dada Magdalena naye akatabasamu.

Hawakutia tena neno lingine.

ENDELEA

Basi afisa Randall akaenda kuonana na familia ya wakina Brian na kuwapa mrejesho wa kilichotokea, nao akawaambia wafike kituo cha polisi kesho asubuhi na mapema, alafu akaenda zake kupumzika.

Afisa Williamson alimshushia nyumbani na kutokomea kwenda kulaza usafiri wa polisi. Randall alikuwa amechoka sana kutokana na kazi za siku nzima. Baada ya kuingia nyumbani kwake, akala na kutulia kidogo sebuleni pamoja na mkewe, alafu muda si mrefu akaenda kupumzika kwa kujimwaga kitandani.

Hata hakuoga. Na muda si muda, akasombwa na usingizi kwa mkupuo. Hakusikia hata mkewe alipozima kila kitu na kuja kulala. Alikuwa usingizini haswa akikoroma na kuachama kinywa.

Kwa mujibu wa saa yake ya sebuleni, mshale ukasonga na kujongea kwenye kituo cha nane usiku. Ulipofika hapo, Afisa Randall akajikuta anaamka toka usingizini asijue nini kimemwamsha kwani bado alikuwa na usingizi mzito.

Akatazama kushoto kwake, akamwona mkewe akiwa amejilalia. Taa ilikuwa imezimwa na hali ilikuwa imetulia tuli kabisa. Hakusikia sauti ya kingine chochote kile zaidi ya pumzi ya mkewe ambaye aliyekuwa anahema kwa uzito.

Akarudisha kichwa chake kitandani na kufumba macho aendelee kulala, usingizi haukuja. Akajitahidi kuyafumba macho kwanguvu, lakini bado hakukuwa na kitu. Macho yaligoma kudaka usingizi abadani,

Muda si mrefu, akasikia harufu fulani ambayo ilimfanya afungue macho na kutazamatazama chumbani. Ni kama kitu kinaungua ila kinanukia. Akanusanusa kama paka jikoni apate kutambua kitu hicho ni nini lakini hakufanikiwa.

Na kadiri muda ulivyokuwa unasonga, akajikuta anahisi harufu hiyo zaidi na zaidi. Akamuita mkewe, “Hey, hey.” akimsukuma bega kistaarabu, ndo’ kwanza mwanamke akageukia kando na kuendelea kulala.

Akataka kuendelea kumwamsha ila akasita. Acha apumzike, akajisemea, kisha akaweka shuka kando na kushuka toka kitandani. Akasikia dirisha linatetemeka, haraka akatazama. Ulikuwa ni upepo. Akapuuzia na kuuendea mlango, akafungua na kutoka chumbani.

Ila punde akarejea na kutwaa bunduki yake kwa dharura ya kiusalama. Akaikoki vema, ndaniye kulikuwa na risasi tatu. Zinatosha kabisa. Akaanza kufuata harufu kwa kudaka korido aende sebuleni na kisha jikoni.

Alipofika sebuleni, akawasha taa. Akatazama kwa kurusha macho yake huku na huko, hakuona jambo. Basi akaelekea kule jikoni. Napo akawasha taa. Akakaguakagua, hakukuwa na kitu. Sasa harufu inatoka wapi?

Dirisha la jikoni likatetemeka, akarusha macho yake kutazama. Ulikuwa ni upepo. Pazia lilichezacheza na mwishowe upepo ulipopita, likatulia. Afisa Randall akafungua droo zote za jikoni na kutazama ndani kama kuna kitu kimeoza, hakuona kitu. Hapo ndipo pua yake ikamwambia harufu ilikuwa inatokea nje.

Akahisi na kuamini kabisa itakuwa inatokea nje. Basi akaona asijisumbue kwenda huko. Kama haipo ndani, basi hana haja ya kujisumbua. Ila kabla hajajirudisha chumbani, akaona haitachukua nguvu sana kutazama nje kwa kupitia dirisha. Huenda akaona wapi harufu inatokea.

Alipotupa macho yake, upande wa mashariki mwa jiko, bustanini, akaona mbwa wawili wakiwa wakiwa wanatafuna. Kwakuwa alikuwa mbali, hakuona mbwa hao wanatafuna nini, ila walichokuwa wanakula kilikuwa kinatoka kwenye mfuko wa nailoni. Si kwamba aliuuona, bali alisikia sauti yake.

Akatazama kwa umakini aone ni nini kile ambacho mbwa hula, hakuweza kuona. Akajiuliza na kustaajabu, ni hicho ndicho hutoa harufu aliyoisikia mpaka kule chumbani?

Dirisha la sebuleni likatikisika. Akatupa macho yake upesi kutazama, hakuona kitu. Ulikuwa ni upepo. Pazia lilicheza na kisha kutulia. Aliporudisha macho yake kule nje, hakuona tena wale mbwa! Wameenda wapi? Akarusha macho yake kutazama na kuwatafuta, hakuwaona.

Akiwa hapo anabung’aa, akasikia sauti za mbwa hao wakiwa wananguruma na kugombana. Walibweka na kunguruma kwa fujo kana kwamba wanagombea kitu, sauti zao zikawa kero na bughudha.

Afisa Randall alipotaka kuachana nazo, zikaendelea pasipo kukoma. Hapo akaona hana budi kuwafukuza mbwa hao kabla watoto wake hawajaamka. Akafungua mlango, akiwa ameshikilia bunduki yake vema mkono wa kuume, akatoka na kurusha macho yake kuwatafuta wale mbwa.

Hakuwaona. Akasonga hatua nane mbele na kisha akatazama tena, hakuwaona! Sasa kulikuwa kimya, ni sauti ya upepo tu wa taratibu ndiyo ambao ulikuwa unasikika.

Wale mbwa wameenda wapi?

Basi kwakuwa aliwakosa na tayari ameshatoka nje, akaona ni kheri akatazame pale bustanini kuona kitu gani ambacho wale mbwa walikuwa wanakula.

Akasonga na kutazama, hakukuta kitu. Ule mfuko haukuwepo, na mbali na hilo, hata alama za miguu ya mbwa, haikuwapo ardhini! Akiwa hapo, bado anaperuzi, kwa nyuma yake mlango aliotokea ukarudi taratibu na kujifunga iiiiiiiiiiiipp .. kisha, tas-tas! Sauti ya komeo ikaita na kumshtua!

Haraka akatoka pale alipo na kukimbilia mlangoni, akagonga na kusema, “Hey, nipo nje! Hey nipo nje!” mlango haukufunguka. Akagonga tena na tena akiita, mlango haukufunguliwa. Akajaribu kuuvuta pasipo mafanikio, mlango ulikuwa umefungwa!

Mlango huu wa jikoni ulikuwa umesanifiwa kwa chuma kizito na kioo kigumu kinachohakisi ndani kwa uhafifu. Na kwakuwa jikoni taa ilikuwa inawaka, kioo hiki kilionekana cheupe kana kwamba mwezi angani.

Basi Afisa alipoona juhudi zake za kugonga mlango hazikuzaa matunda, akatengeneza mduara kiooni kwa kutumia bapa za viganja vyake ili apate kutazama ndani kama kuna mtu ama mlango umejifungwa kwa makosa.

Alipofanya hivyo, akaona kuna mtu ndani, lakini hakuweza kumtambua mtu huyo kwani kioo kile cha mlango hakikuwa chepesi kuonyesha hivyo mtu huyo alikuwa anaonekana kana kwamba kivuli tu.

Randall akabamiza tena mlango na kuita. Akastaajabu, mbona mtu yule hakuwa anamfungulia? Hapa akapata shaka. Huenda ni jambazi! Basi haraka akatoka hapo mlangoni na kwenda kwenye madirisha ya sebuleni, akatupa macho yake ndani.

Hakumwona mtu. Ila kabla hajatoka hapo akiwa amelenga kwenda kwenye mlango wa sebule kujaribu kufungua, akaona kitu fulani koridoni. Kilikuwa ni kitu cheusi kirefu chenye umbo la binadamu, ila hakina sura. Afisa akadhani ni macho yake. Punde taa ya sebuleni ikazima!

Akashtuka.

Ikabakia taa moja tu ya kule jikoni ambayo mwanga wake ukawa unajimwayamwaya kwa uhafifu mpaka huku sebuleni. Hapo ndipo Afisa Randall akaona kile kitu ambacho kipo koridoni, kikiwa na umbo kama la binadamu, kikiwa kinawaka macho mithili ya paka. Moyo wake ukapata mshtuko sana. Akakodoa na kuachama akiwa haelewi kile anachokiona. Alitamani awe ndotoni, ila hapana, ilikuwa ni uhalisia!

Kabla hajavuta hata pumzi tatu, katika ule mwanga ambao ulikuwa unatokea jikoni kufika sebuleni, akaona kivuli cha mtu. Alikuwa ni mwanamke amevalia gauni. Mwanamke huyo alikuwa anacheza mienendo ya bluzi akinyanyua pindo la gauni lake na kusonga kusonga kushoto, kulia.

Akayarudisha macho yake kule koridoni, ajabu hakumwona tena yule kiumbe aliyekuwa anawaka macho kama taa. Akiwa anaangaza ajue yupo wapi, akastaajabu ameshikwa bega na mkono wa baridi kana kwamba barafu. Alipotazama, uso kwa uso akakutana ni kiumbe yule mwenye macho ya taa. Kiumbe mweusi na mrefu!

Akahisi moyo wake umeongeza makasia. Akapatwa na baridi kavu mwilini wake. Alijawa na kihoro haswa, upesi akanyanyua bunduki yake na kutupa risasi zote tatu kwa mkupuo, mara kiumbe yule akapotea!

Afisa akiwa amekodoa, anahema kama aliyekimbizwa, punde kidogo akaguswa tena begani na mkono wa baridi zaidi. Alipogeuka kutazama, akakutana na mwanamke aliyevalia gauni jeusi. Alikuwa amefunga kiremba kichwani kilichoziba mpaka uso wake.

Afisa akajaribu tena kufyatua risasi, hazikuwapo, ziliisha. Basi akawehuka na kuanza kukimbia akipiga makelele kuomba msaada.


**

Saa tatu asubuhi …


Kulikuwa na magari matatu ya polisi na nyumba ya afisa Randall ilikuwa imezungushiwa utepe wa rangi ya manjano na nyeusi kukataza watu wasiohusika kukatiza hapo.

Mbali na hivyo, watu kadhaa, haswa majirani, walikuwa wametoka nje ya makazi yao wakitazama eneo la tukio kwa macho ya maulizo na nyuso za mashaka. Kulikuwa na zogo fulani midomoni mwao.

Muda si mrefu gari ya wagonjwa ikawasili eneoni na kujitengenezea vema. Kutoka ndani ya nyumba, ikatolewa miili mitatu ambayo imefunikwa gubigubi, ikatiwa ndani ya gari la wagonjwa na kisha gari hilo kutimka.


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom