Sehemu ya 36
“Bosi...bosi...bosi...” ilisikika sauti kutoka upande wa simu ya Razak.
“Unasema Casmir...”
“Yadi inaungua...”
“Unasemaje?”
“Yadi ya magari inaungua bosi...inateketea kwa moto muda huu,” ilisikika sauti ya mfanyakazi huyo.
“Ipi?”
“Hii ya Kinondoni...wahi bosi, inateketea kwa moto...” aliendelea kusisitiza Casmir.
“Moto umean...” alitaka kuuliza swali lakini kabla hilo swali halijakamilika, simu ikakatwa na kubaki akiita tu lakini simu hiyo haikuwa hewani tena.
Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuangalia saa yake, tayari ilikuwa ni saa saba usiku, harakaharaka akakurupuka kutoka kitandani, akawasha taa na harakaharaka kuvaa suruali yake kwa ajili ya kuondoka mahali hapo.
Wakati anajiandaa, Aisha akashtuka kutoka usingizini.
Akapigwa na mshangao, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea mpaka mpenzi wake kuvaa nguo harakaharaka namna ile tayari kwa kuondoka mahali hapo.
“Kuna nini tena?” aliuliza Aisha.
“Yadi inateketea kwa moto...”
“Unasemaje?”
“Nakuja...”
Razak hakutaka kubaki mahali hapo, kwa haraka sana akachomoka chumbani na kuelekea nje, huko, akapanda ndani ya gari lake, mlinzi akafungua geti na kuondoka mahali hapo huku akiwa amechanganyikiwa.
“Yaani yadi inateketea kwa moto, haiwezekanio...haiwezekani...” alisema Razak huku akionekana kuchanganyikiwa kwani miongoni mwa biashara zilizokuwa zikimuingizia kiasi kikubwa cha fedha, ilikuwa hiyo yadi ya magari.
*****
Razak aliendesha gari kwa kasi, alikuwa amechanganyikiwa, taarifa ile ya kuteketea kwa yadi yake ya magari ilimchanganya mno. Kwa kuwa ilikuwa ni usiku sana hakukuwa na foleni barabarani hivyo hakuchukua muda mrefu akawa amekwishafika katika eneo hilo.
Kitu cha ajabu kabisa alichokiona, hakukuwa na dalili za moto wowote ule. Alibaki akishangaa, yadi yake ya magari ilikuwa salama kabisa, sasa kwa nini msimamizi wake wa yadi hiyo alimwambia kwamba yadi yake ya magari ilikuwa ikiteketea kwa moto?
Hakutaka kubaki garini, akateremka na kuelekea ndani ya yadi ile. Ukimya mkubwa ulikuwa umetawala mahali hapo, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
Hakukuwa na mlinzi wala hakuwepo Casmir kitu kilichomshangaza sana kwani haikuwa kawaida hata kidogo. Alichokifanya ni kuanza kuita lakini hakukuwa na mtu aliyeitikia.
Akaanza kuyahesabu agari yaliyokuwa mule ndani, hakukuwa na gari lolote lile lililopungua, yote yalikuwa kama alivyoyaacha, magari mia moja na hamsini.
Hakuridhika, hatua iliyofuata ni kwenda kwenye kibanda cha mlinzi, mlango ulikuwa umefungwa kwa nje na ufunguo kutolea, alichokifanya ni kuanza kuugongwa.
Hakusikia sauti za watu zaidi ya miguno ya watu wawili iliyomfanya kujua kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea humo ndani.
Harakaharaka akaanza harakati za kuuvunja ule mlango, wala hakukuwa na tatizo, mlango ukafunguka, alichokiona ni kwamba mlinzi na Casmir walikuwa wamefungwa kamba na kulazwa chini, akawafungua.
“Kuna nini?” aliwauliza.
“Kuna watu walikuja, wakatufunga kamba...”
“Ni majambazi?”
“Hatujui, ila walikuja na kutufunga kamba kisha kumwambia Casmir aongee nawe maneno waliyoyataka ayaongee huku wakikuita mahali hapa,” alisema mlinzi, wakati huo Casmir alikuwa kimya.
“Ni wakina nani?”
“Bosi...sijawahi kuwaona kabisa, ila walikuja na bunduki...” alisema Casmir.
Wote wakatoka ndani ya kijumba kile, kuhesabu magari haikutosha, walichokifanya ni kuanza kufungua gari moja baada ya jingine ili kuona kama kulikuwa na vifaa vimetolewa, kila gari lilikuwa salama kabisa.
“Labda kuna mtu alitaka kunisumbua tu...nyie endeleeni na kazi, tutazungumza kesho nikija,” alisema Casmir, akaingia ndani ya gari na kuondoka.
Mpaka kipindi hicho, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, alibaki akiwashangaa majambazi hao ambao waliwateka watu wake na kisha kumwamuru Casmir kumpigia simu na kumwambia habari mbaya ambayo haikuwa na ukweli wowote ule.
Alibaki akitabasamu, alitoa kicheko kidogo na kuwaona watu hao kwamba walikuwa wajinga sana.
Hakuchukua muda mrefu akawa amefika nyumbani kwake, kitu kilichomshangaza sana, alianza kupiga honi lakini kitu cha ajabu, mlinzi hakutokea kufungua geti.
“Amelala au?” alijiuliza huku akiteremka.
Akalifuata geti kisha kulifungua, akaingia ndani na kuanza kuelekea katika kibanda cha mlinzi, kilichomshangaza, hakumkuta, hakujua alielekea wapi, hakutaka kujali sana, akalifungua geti, akalirudia gari lake, akaingia kisha kuliingiza.
Alipohakikisha amelipaki sehemu sahihi, hapohapo akateremka na kuelekea ndani. Huko ndipo alipogundua maana ya ile simu aliyokuwa amepigia, walipoingia ndani, kitu kilichomshtua, mpenzi wake Aisha hakuwepo.
Alichanganyikiwa, akaanza kumtafuta huku na kule, alihisi kwamba inawezekana alikwenda nje baada ya kuona ametoka usiku sana huku akiwa amechanganyikiwa, aliita kwenye kila chumba, hakuisikia sauti ya Aisha kitu kilichomfanya kuwafuata wasichana wa kazi.
“Aisha yupo wapi?” aliuliza huku akionekana kuchanganyikiwa.
“SI yupo ndani!”
“Ndani hayupo...hakuja huko kwenu?”
“Wala hakuja...”
Razak akatoka nje, akazunguka katika eneo zima la nyumba yake, alipofika katika bustani ya maua, akakutana na mlinzi akiwa hoi chini, amefungwa kamba huku damu zikimtoka kichwa.
“Kuna nini tena?”
“Tulivamiwa, nimepigwa na watu nisiowajua...” alijibu mlinzi...”
“Wakina nani?”
“Sijui ila walikuja na bastola....wakaingia ndani...”
“Kisha....”
“Sijui ila nilisikia wakilitaja jina la shemeji...” alijibu mlinzi yule.
Hapo ndipo Razak akachanganyikiwa zaidi, akatoka nje mbio na kuanza kukimbia katika barabara huku akiangalia huku na kule. Muda wote mikono yake ilikuwa kichwani, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea.
Alizunguka sehemu kubwa ya Kijitonyama, alikwenda mpaka Tandale na Mwananyamala, kote huko aliambulia patupu hivyo akarudi na kuwapigia simu wazazi wake.
“Unasemaje?”
“Aisha ametekwa...”
“Na nani?”
“Hakuna anayejua....naomba mje...” alisema Razak.
Hakutulia, simu nyingine kupiga ilikuwa ni ya Kituo cha Polisi cha Mabatini, akawaeleza polisi kile kilichotokea, baada ya muda, polisi hao wakafika nyumbani kwake, kitu cha kwanza kabisa wakaanza kuzungumza na mlinzi.
“Walikuwa wangapi?”
“Kama wanne...”
“Kama wanne au wanne?”
“Nasema kama kwa sababu walikuja wawili, wengine nilisikia sauti zao kwa nyuma...”
“Ikawaje?”
“Wakanipiga, wakanifunga kamba na kuingia ndani..”
“Walikuwa na silaha gani?”
“Bastola ndogo...”
“Usoni walivaa vinyago?”
“Hapana...”
“Hukuwatambua?”
“Nilishindwa kuwatambua mkuu...” alijibu mlinzi huyo.
Wakati wote wa mahojiano, Razak alisimama pembeni, alionekana kuwa na hasira mno, alichanganyikiwa, mwili wake ulikuwa ukimtetemeka, alionekana kutokuamini kilichokuwa kimetokea.
Mtu wa kwanza kabisa aliyemfikiria alikuwa msichana Sabrina, alijua hali aliyokuwa nayo na msichana huyo, baada ya kumuomba kuachana naye, aliachana naye na hata msichana huyo aliporudi, tayari alikuwa na msichana mwingine hivyo kuhisi kwamba ili kulipa kisasi, msichana huyo aliamua kumteka Aisha.
“Huyu atakuwa Sabrina tu...haiwezekani, lazima nimtafute...” alisema Razak huku akionekana kuwa na hasira mno.
****
Je nini kitaendelea....