Sehemu ya 61.
“Nimekuita lakini!” alisema mwanaume huyo kwa sauti ya upole, Shadya akasimama, alisubiri kusikia akiambiwa nini, japokuwa hakupenda sana kusimama kama alivyofanya.
“Unasemaje?” aliuliza huku akiangalia huku na kule, aliwaogopa watu ila mtu aliyemuogopa zaidi alikuwa Alex kwani alidhani angehisi jamaa huyo alikuwa mtu wake.
“U msichana mzuri sana!” alisema jamaa huyo kwa sauti ya chini, sauti ambayo ilibeba ujumbe mzito ndani yake.
“Ndilo unalotaka kuniambia?” aliuliza huku akionekana kubadilika.
“Ninakupenda sana na ndiyo maana ninataka kukwambia ninalokwambia, upendo wangu kwako ni wa matendo na si maneno. Kama hao unaodhani wanakupenda ingekuwa kweli, basi wangekwambia mapema hili ninalotaka kukwambia,” alisema, Shadya akaanza kupiga hatua, jamaa akamshika mkono.
“Nisikilize kwanza!” alisema kwa upole huku akijaribu kumvuta.
“Nimesema niache! Nitapiga kelele!” alisema msichana huyo kwa hasira.
“Shadya! Si kila mwanaume anayekusimamisha anataka kukutongoza, jaribu kunisikiliza,” alisema, kidogo maneno hayo yakamfanya msichana huyo atulie na kuanza kumwangalia.
“Unataka kuniambia nini?”
“Unajua kitu gani kinaendelea chuoni kuhusu wewe?” aliuliza jamaa huyo.
“Kitu gani?”
“Unahisi umezungukwa na watu sahihi?” aliuliza swali lililomfanya Shadya kumkazia macho.
“Unamaanisha nini?”
“Pole sana!”
“Pole ya nini?”
Kabla jamaa hajajibu, simu ya Shadya ikaanza kuita, akashukuru Mungu, haraka haraka akaitoa na kuangalia jina, alikuwa Alex.
Akasogea pembeni na kuanza kuongea naye, hakuridhika, akatumia njia hiyo kama kumkimbia mwanaume yule, akaanza kupiga hatua kukatiza uwanjani kuelekea katika mabweni ya Magufuli.
“Shadyaaaa...” aliita jamaa, msichana huyo akawa anapiga hatua kusonga mbele.
Hiyo ilikuwa nafasi yake, hakutaka kumuacha msichana huyo, alikuwa na mengi ya kumwambia, akaanza kumfuata lakini naye baada ya kuona anafuatwa, akaanza kupiga hatua zaidi.
“Shadya! Alex anakuharibu!” alisema jamaa huyo baada ya kumfikia, kusikia hivyo, Shadya akasimama.
“Hebu subiri baby nitakupigia,” alisema Shadya kwa sauti nyororo kabisa, akakata simu na kumwangalia mwanaume huyo.
“Shadya! Kitu nitakachokwambia kisikushtue, usichukue uamuzi wowote ule mbaya,” alisema