Simulizi: Penzi ama kaburi?

Simulizi: Penzi ama kaburi?

Unapotea sana jukwaani kama shilingi ya mjerumani...au ushawekwa ndani wasubiria kuchezwa ngoma
Woiiii mimi nimeshawekwa ndani mda we mzee au niwekwe mara ya pili jamani

Kupotea jukwaani kweli nimepotea nahisi sijui ni ubusy au ndio kuwa mtu mzima ebu zidi kuniombea tu nisipotee hivi
 
Nimekumiss pia ndugu jamani uko poa dear

Hahha msome wajina wako alikuwa na tabia nzuri tu baadae ulimwengu umembadilisha
Nimefurahi kusikia uko mzima ndugu.

Huwa ni mvivu kusoma story ila hii ntakwenda nayo pole pole mpaka niimalize Dada.
 
Woiiii mimi nimeshawekwa ndani mda we mzee au niwekwe mara ya pili jamani

Kupotea jukwaani kweli nimepotea nahisi sijui ni ubusy au ndio kuwa mtu mzima ebu zidi kuniombea tu nisipotee hivi
Hahah...

Kama umewekwa ndani tayari basi ruksa kupotea...mimi mzee natoa baraka zote
 
Sehemu ya 66.

Shadya alirudiwa na fahamu akiwa juu ya kitanda, alifumbua macho yake na kuangalia huku na kule, hakuwa na kumbukumbu juu ya mahali alipokuwa muda huo.

Dripu ilikuwa ikining’inia kwa juu ambayo ilikuwa ikipeleka maji katika mshipa wake, akaangalia huku na kule, akagundua alikuwa hospitalini hapo.

Akaanza kuvuta kumbukumbu zake, akaanza kukumbuka kilichokuwa kimetokea.

Majibu ya vipimo vya Ukimwi yakaanza kujirudia kichwani mwake, palepale kitandani akaanza kulia.
Hakuamini, Shadya yeye, msichana mrembo, aliyekuwa na uzuri wa kila aina, leo hii alikuwa ameathirika kwa virusi vya Ukimwi.

Hapo ndipo alipoanza kumtupia lawama Alex, alijua mwanaume huyo ndiye aliyesababisha hayo yote. Hakujua michezo yake kwamba alikuwa akitumika kingono, aliumia, alitamani muda urudi nyuma akarekebishe alipokosea lakini ilishindikana kabisa.

Baada ya dakika kadhaa yule mama aliyempa majibu akaingia, alipomuona, sura yake ikavikwa na simanzi nzito, Shadya alikuwa binti mdogo, aliyekuwa na ndoto kubwa maishani mwake lakini alihisi kila kitu kingeharibika baada ya kuathirika.

“Shadya...” aliita mwanamke huyo kwa sauti ya chini.
“Nimeathirika! Alex ameniua...” alisema huku akiendelea kulia.

“Nisikilize mwanangu! Kuathirika si mwisho wa maisha! Bado una nafasi ya kuendelea kuishi! Kuna watu wengi wanaishi na virusi vya Ukimwi, usikate tamaa, utatakiwa kufuata ushauri wa vyakula nilivyokwambia,” alisema mwanamke huyo.

“Alex ameniua mama....kwa nini Alex ameamua kuniua?” aliuliza Shadya, muda wote alikuwa akilia tu.

Mwanamke huyo alipata kazi ya ziada kumbembeleza kitandani pale na kuendelea kumwambia kuwa na virusi vya Ukimwi haikumaanisha ndiyo ulikuwa mwisho wake.

Alilia lakini hakubembelezeka ila ilivyofika majira ya jioni akaruhusiwa kuondoka na kuambiwa alitakiwa kufika hospitalini hapo mara kwa mara.

Akaondoka, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, hakujua ni kwa namna gani angeendelea kuishi na virusi vya Ukimwi. Moyo wake ulikuwa na maumivu makali na lawama zote zilikuwa kwa Alex.

Huku akimlaumu mwanaume huyo kwa kumtumikisha kingono lakini upande mwingine wa moyo wake ukaanza kumlaumu yeye mwenyewe.
 
Sehemu ya 67.

Alikuwa na mpenzi wake, Ngwali huko Zanzibar, alimpenda na kumthamini lakini baada ya kwenda jijini Dar es salaam kila kitu kikabadilika, starehe zimampata, akakutana na wanaume waliokuwa wakijua kuongea sana na mwisho wa siku kufanikiwa kulala naye.

Akafika bwenini, moyo wake ulikuwa na maumivu makali mno, alishindwa kujua ni kwa namna gani angeweza kuishi na virusi vile.

Huku akiwa akifikiria mambo yote hayo, kitu pekee kilichokuja mbele yake ni kujimaliza tu kwani aliona giza na hakuwa tayari kuona akiusambaza ugonjwa huo kwa watu wengine.
“Siwezi kuishi na virusi vya Ukimwi,” alijisemea.

Kabla ya kufanya kitu chochote kile akampigia simu mdogo wake, Rahim na kuomba kuonana naye, hilo halikuwa tatizo, kijana huyo akafika mahali alipoambiwa kwenda na kuonana na dada yake huyo.

Kwa jinsi alivyomuona tu, alibadilika, hakuwa Shadya yule aliyezoea kumuona, alikuwa na huzuni na macho yake yalikuwa mekundu yaliyoonyesha alitoka kulia sana dakika kadhaa zilizopita.
“Kuna nini Shadya?” aliuliza Rahim huku akimwangalia dada yake huyo.

Shadya alitamani kuzungumza kitu lakini alishindwa kabisa, hakujua ni kwa namna gani ndugu yake angemuelewa kile kilichokuwa kimetokea.
“Niambie kuna nini! Naona unalia tu!” alisema Rahim.

“Nimeathirika!” alimwambia.
Rahim ni kama hakusikia vizuri, alimwangalia ndugu yake huyo kwa macho yaliyomtaka kurudia tena kile alichokuwa amemwambia muda huo.

“Unasemaje?” aliuliza.
“Nimeathirika! Alex ameniua!” alijibu kwa huzuni.

“Yaani sijaelewa, unamaanisha nini?”
Hakuzungumza tena, moyo wake ulimchoma mno, hakutaka kubaki mahali hapo, akasimama na kuondoka zake. Rahim alijaribu kumuita lakini hakuitikia wala kugeuka.

Akamkimbilia na kumshika mkono, Shadya akajitoa, akaanza kuelekea bwenini. Kitu pekee kilichokuja kichwani mwake ni kujiua tu, hakutaka kuendelea kuishi.

Aliyachezea maisha yake, alikuwa na ndoto nyingi mbele yake lakini alihisi zote hizo zisingeweza kutimia kwa sababu tu aliathirika.
 
Sehemu ya 68.

Moyo wake kwa wakati huo uligawanyika mara mbili, kuna upande ulimwambia hakutakiwa kujiua kwa sababu bado angeweza kuishi miaka mingi lakini upande mwingine ulimwambia ni lazima ajiue kwa sababu tu kusingekuwa na maisha zaidi, mbaya kuliko yote, watu wangekuwa wanamcheka tu.

“Yaani watu wakijua umeathirika, hutokaa kwa amani, utachekwa, utanyapaliwa, yaani hutokuwa na maisha ya raha hata kidogo,” aliisikia sauti moyoni mwake.

Hiyo ndiyo ilimtia hofu na kuwa na msimamo wa kutaka kujimaliza tu. Hapo bweni hakukaa sana, akaondoka na kuelekea mtaani ambapo akanunua sumu ya panya na kurudi tena na kukaa kitandani mwake.

“Allah naomba unisamehe!” Hakutaka kusubiri, moyo wake ulikuwa na maumivu makali mno, kila alichokuwa amekipanga alihisi kama kingevurugika kwa kuwa tu aliathirika alipokuwa chuoni.

Akachukua glasi ya maji na sumu ile, akachanganya na kunywa, akajifunika na shuka lake, tumbo likaanza kumkata na hakuchukua dakika nyingi, akatulia, mapovu yakamtoka mdomoni na kufariki dunia.

Hakuna mtu aliyejua kama msichana huyo alifariki dunia, alionekana kama amelala, baada ya masaa matatu ndipo watu walipokuja kugundua.

Kila mmoja alishangaa, taarifa zikaanza kusambaa kwamba Shadya amejiua kwa kunywa sumu akiwa bwenini. Taarifa zilipofika kwa Rahim, hakuamini, alilia mno, hapakuwa na mtu aliyejua sababu zaidi yake, na hakutaka kumwambia mtu yeyote zaidi ya ndugu zake tu.

Mwili wake ukachukuliwa na kupelekwa hospitalini, ukahifadhiwa mochwali baada ya kugundulika alikuwa amefariki dunia.

Wazazi, ndugu, jamaa na marafiki walilia kwa ajili yake, kila mmoja alijaribu kujiuliza sababu ya msichana huyo kuuchukua uamuzi mkubwa namna hiyo lakini hakuna aliyejua lolote lile zaidi ya Rahim ambaye aliamua kuwa kimya kwa sababu maalumu.

Siku iliyofuata mwili ukasafirishwa mpaka Zanzibar. Wazazi wake walihuzunika mno, walijitahidi kutafuta pesa kwa ajili ya binti yao, waliishi maisha ya shida kwa sababu yake na kaka yake, ili wasome tu.
 
Sehemu ya 69.

Watu waliwacheka walipoona wakimsomesha mtoto wa kike kwa kuwa wasichana wengi wa Zanzibar hawakuwa wakipelekwa shule, wao waliamua kuwa tofauti nao, walimsomesha kwa nguvu zote lakini mwisho wa siku Shadya akaja kujimaliza akiwa chuoni, tena alibakiza mwaka mmoja kabla ya kuchukua Diploma yake ya kwanza.

“Kwa nini amejiua?” lilikuwa swali walilojiuliza wazazi wake kila siku, Rahim hakuwajibu kwa kipindi hicho mpaka baada ya mwezi mmoja ndipo akaamua kuwaambia ukweli kile alichoambiwa na Shadya.

“Alikuwa ameathirika!” alisema Rahim kwa unyonge kabisa.
“Aliathirika? Kivipi yaani?”
“Aliniambia hivyo! Akaondoka, baada ya saa kadhaa ndipo nikapata taarifa kwamba alijiua,” alijibu Rahim.

Huo ukawa mwisho wa Shadya, watu walihuzunika kwa sababu ya kifo chake. Alex aliendelea kuishi vizuri japokuwa aliathirika, hakujua kwa kuwa aliogopa kupima.

Kupitia sura yake ya kipole, bado aliendelea kutembea na wanawake wengi chuoni hapo, kila msichana mzuri aliyekuwa akimuona, alijitahidi kumfuata kwa upole na kujifanya mshauri na mwisho wa siku kulala naye na kumwambukiza Ukimwi.

Wanaume kama Alex bado wapo, wana nguvu, wanatembea na wanawake mavyuoni na mitaani. Hawajali kuhusu afya zao, wanaendelea kusambaza virusi vya Ukimwi kwa kila mwanamke watakayelala naye.

Wasichana kama Shadya nao wapo, wanamaliza shule na kujiunga na masomo ya chuo. Wanapofika mwaka wa kwanza, hawajui lolote lile, kila mwanaume anayewafuata na kuwasaidia anaonekana mwema mbele ya macho yao.

Hawafikirii kuhusu ndoto zao, ni kwa jinsi gani wazazi wao wamejinyima kwa ajili yao, wapate elimu bora na kuwaondoka katika giza la umasikini, wanapofika chuoni, maisha ya starehe yanawavamia na kuingia mitegoni na mwisho wa siku kuharibu ndoto zao.

Kumbuka kwamba UKIMWI UPO MAVYUONI, MITAANI NA MAOFISINI. Ikibidi acha ngono, ukishindwa, tumia kondomu.

Ujumbe huu uwafikie vijana wote ambao wanapambana kwa ajili ya maisha yao ya badaye.

MWISHO
-
-
-
NYEMO CHILONGANI.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom