SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 035*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Wakaamka na kuangaza. Lakini kabla hawajafanya kitu wakastaajabu wamezungukwa na maaskari waliobebelea majambia marefu. Askari hawa walikuwa wamevalia sketi ngumu, vifua vyao vikiwa wazi!

Wakawaamuru waweke mikono kichwani na wajieleze wao ni wakina nani na hapo wanafanya nini kabla hawajakatwakatwa na vipande vyao kulishwa papa baharini.

ENDELEA

Kabla hawajasema jambo, mara wakasikia sauti ikisema:

"Waacheni!" Wote wakageuka na kutazama. Wakamwona mzee mmoja aliyevalia joho lililochoka rangi ya grey. Alikuwa na nywele ndefu zinazogota mabegani pamoja na ndevu nyingi zilizojawa mvi.

Miguuni alikuwa peku, na kwenye mkono wake wa kuume alikuwa ameshikilia fimbo ndefu akitembea nayo.

"Waacheni nawafahamu hao!" Mzee huyo akasema akiwakaribia wahusika wake - wanajeshi farasini na wakina Malkia.

"Una uhakika?" Mwanajeshi mmoja akauliza.

"Unadhani mie mwehu?" Akajibu mzee yule. "Kuna faida gani kusema nawajua watu nisiowafahamu?"

Basi mwanajeshi aliyeuliza, ambaye alionekana ndiye mkubwa kwa cheo, akamtazama babu huyo alafu akawatazama na wakina Malkia. Ni kama vile alikuwa na shaka ndaniye lakini akapuuza, akawaamuru wenzake waondoke.

Wakayoyoma.

"Wewe ni nani?" Malkia akamuuliza yule babu. "Kwanini umetusaidia?"

Yule babu akawatazama pasipo majibu, kisha akawaamuru wamfuate. Wakasita. Wakamtazama yule babu akienda zake kisha wakatazamana wao kwa wao. Wakaamua kumfuata.

Wakatembea kwa umbali mrefu kidogo kabla hawajaingia kwenye nyumba fulani kubwa kuukuu, wakawafungia farasi wao nje na wao wakakaketi sebuleni.

Sebule hii ilikuwa hafifu kwa samani. Sakafuni kulikuwa kuna mkeka tu rangi ya zambarau. Waliketi hapo na yule babu akaenda zake chumbani, ndani ya muda mfupi akarejea na kuungana nao mkekani.

Alikuwa sasa ananukia marashi ya tofauti na hapo awali. Bila shaka alikuwa ameenda kuyapaka huko chumbani. Marashi haya yalikuwa ni makali, lakini yanayovumilika.

"Natambulika kwa jina la Waheed," akajitambulisha kwa jina moja. Seth akashtushwa na jina hilo kwani maanaye haikuwa nzuri.

"Waheed si jina langu halisi," akaendelea kufafanua babu huyu. "Lakini ndilo jina ninalotambuka nalo kwa watu wengi waishio hapa. Kwahiyo si mbaya nanyi mkaniita hivyo."

"Kwanini Waheed? Kwanini jina hilo?" Seth akawahi kuuliza. Babu yule akatabasamu kisha akapandisha mabega yake. "Ndivyo walivyoamua kuniita. Wananichukulia mimi ni Waheed. Matendo yangu kwao wanayaona yatoka kwa Waheed. Nami sina muda wa kuwasahihisha, nimewaacha wabaki na mawazo yao hayo."

"Na kwanini umeamua kutusaidia?" Malkia akalirudia swali lake.

"Kwasababu mlikuwa mnahitaji msaada," akajibu Waheed, kisha akatabasamu. "Unadhani nisingewasaidia pale mngekuwa wapi saa hii?"

"Ulijuaje tunahitaji msaada?" Akauliza tena Malkia.

"Watu waliozingirwa na wanajeshi wanahitaji kitu gani zaidi ya msaada?" Waheed naye akauliza.

Kukawa kimya kidogo. Waheed akasema:

"Kabla ya kuniuliza maswali yenu ilibidi mnishukuru kwanza. Sasa hivi mngekuwa ndani, mnangojea maswali mengi sana maana nyie ni wavamizi."

"Nani kakuambia sisi wavamizi?" Seth akawahi kuuliza.

"Mnaonekana nyie ni wavamizi. Hamuonekani kama watu toka Misri. Ama tuseme macho yangu yanawaona nyie sio wa Misri."

Akabinua mdomo wake na kuendelea kueleza:

"Pengine si mimi tu, hata wale wanajeshi waliwatilia hofu kuwakuta mmelala ufukweni. Watakuwa wamedhani mmefika hapo baada ya chombo chenu kwenda mrama ama kupata hitilafu baharini."

"Na wewe unadhanije?" Malkia akauliza. Waheed akacheka kisha akamtazama Malkia kwa macho yake madogo aliyoyafumbua kwa upana.

"Hamjapata hitilafu yoyote baharini. Wala hamjatumia njia ya baharini kufika hapa. Niliona kwa macho yangu mlipotokea pale kimiujiza," alieleza akatabasamu.

"Najua mnaweza mkawa na maswali mengi juu yangu ila mimi nipo hapa kwasababu ya kuwasaidia kufikia lengo lenu."

"Lengo gani?" Malkia akauliza.

"Mwanamke, acha kuuliza maswali mengi. Jua najua kila kitu kuwahusu. Wewe unaitwa Sandarus, huyu ni Seth, Zura, Fluffy na huyo mwingine anaitwa Alk. Bado unadhani kuna kitu sikijui?"

"Wewe ni nani haswa Waheed?" Fluffy akauliza. Wote vichwani walikuwa na swali hilo. Walikuwa wamekubaliana kuwa Waheed hakuwa mtu wa kawaida.

Waheed asiongee jambo, akapasha viganja vyake alafu alafu akawaonyeshea Malkia na wenzake taswira viganjani. Wakajiona walipotokea hadi namna walivyofika hapo.

Waheed alipomaliza kuwaonyesha hayo, akawaambia atawasaidia kuipata hiyo kofia ya Pharaoh waliyokuja kuitafuta. Hapo ndiyo Malkia na wenzake wakachoka.

Hadi hili alijua?

Hawakupata muda wa kuuliza zaidi, Waheed akawataka wapumzike watateta zaidi baadae. Akawapatia chakula na mahali pa kupumzika.

- JE, WAHEED NI MTU WA KUMWAMINI?

- YUKWAPI MTU YULE PEKEE AISHIYE KARIBU NA BAHARI YA MEDITERANIA AMBAYE WAKINA MALKIA WALIAMBIWA WAMTAFUTE?

***

Hii ilikuwa ni siku ya tatu sasa. Siku hii haikuwa ya kawaida kwa Venet, bali siku maalum. Tena maalum sana!

Anga lilikuwa limependezeshwa na picha kamili ya mwezi. Mwezi mweupe ulio kamili ambao unaweza ukadhani unaelekea kugongana na dunia kwa namna unavyoonekana vema na kwa ukaribu.

Siku hii iliyokuwa inangojwa mno na Venet hatimaye iliwadia. Siku ya kafara! Siku ambayo mwezi unaonekana vema.

Venet akiwa ameshaandaa kila kitu katika uwanja wake wa sadaka, kama vile kisu kikali, kaniki nyeupe na nyekundu na kitabu chake cha ulozi juu ya meza, akawasogelea vikongwe pamoja pia na mwili wa Rhoda. Akatabasamu kwa furaha.

"Leo siku imewadia," akawaambia vikongwe. Kufumba na kufumbua akageuka kuwa kundi kubwa la popo lililotawala na kumeza eneo zima!

Wakaruka juu sana na kutengeneza maumbo yasiyoeleweka huko angani. Lakini ajabu Venet akajiri nyuma ya vikongwe aliowaacha chini kisha akaelekea kufuata kitabu chake. Akakifungua na kukitazama kisha akakifunga. Alikuwa tayari ameshakariri cha kusema.

Akanyoosha mikono yake juu alafu akapaza sauti kutamka maneno hayo aliyoyakariri. Akayarudia mara sita. Kila alipoyarudia maneno hayo wale popo waliokuwepo angani wakawa wanadondoka wakiwa wafu. Mpaka anatimiza idadi ya sita, popo wote wakawa wamekwisha angani!

Sasa Venet akaanza kuomba mwili mpya. Akatamka maneno anayoyajua yeye bado akiwa amenyoosha mikono yake juu.

Basi kufumba na kufumbua, wale vikongwe pamoja pia na mwili wa Rhoda ukageuka kuwa kundi kubwa la popo! Wakapanda juu kabisa.

Venet akaanza kuwaita kwa kutumia maneno yake ya kilozi, popo hao wakashuka kwa kasi na kupotelea mwili wake wote! Venet akajihisi mwenye nguvu zaidi.

Akajihisi mpya kama vile ametoka kuzaliwa muda si mrefu.

Akacheka sana. Akafurahi sana. Hakuna siku aliyofurahi maishani mwake kama hii!

Hakupoteza muda, kama mtu asiyeamini, akaanza safari yake ya kwenda himaya ya Goshen. Alijigeuza kuwa kundi kubwa la popo na alipofika mpakani akageuka kuwa Rhoda!

Kama ungelipata bahati ya kumwona usingeliweza kutambua kasoro hata moja kwenye mwili wa mwanamke huyo. Alitembea kwa madaha mpaka yalipo makazi yake, akafurahi sana.

Bado yote haya yalikuwa ni kama ndoto. Hakuamini sasa ametoka kwenye kifungo chake cha maisha. Sasa amekuwa huru!

Akacheka haswa.

Lakini furaha yake hii haikudumu, akasikia sauti huko nje ya nyumba ikimuamuru atoke ndani upesi!

Walikuwa ni wanajeshi wa Phares wapo nje. Walishajua Rhoda amerejea himayani na sasa walikuwa hapo kutekeleza agizo la kumkamata mwanamke huyo mara moja kama vile walivyoagizwa.

- MSALA WA VIKONGWE UNAMUANGUKIA VENET. JE, ATATIWA NGUVUNI?

- TAYARI ISHATAMBULIKA RHODA SI MTU WA KAWAIDA, NINI PONA YA VENET KUKAMILISHA MALENGO YAKE?
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 036*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Akacheka haswa.

Lakini furaha yake hii haikudumu, akasikia sauti huko nje ya nyumba ikimuamuru atoke ndani upesi!

Walikuwa ni wanajeshi wa Phares wapo nje. Walishajua Rhoda amerejea himayani na sasa walikuwa hapo kutekeleza agizo la kumkamata mwanamke huyo mara moja kama vile walivyoagizwa.

ENDELEA

Venet akajiuliza kipi cha kufanya. Akaona ni kheri akaficha makucha yake kwa sasa. Atulie aone mchezo unaendaje hapa. Hakuona haja ya kujifanya mjuaji kwenye ngoma ya kigeni.

Basi taratibu akatoka ndani na kwenda kukutana na rundo kubwa la wanajeshi likiwa limemebelea kila aina ya silaha kana kwamba wamekuja kumkamata mhaini mwenye nguvu isiyo mithilika.

Venet akastaajabu jeshi hili! Asiongee kitu akasukumwa na teke mpaka chini. Akafungwa mikono akidhihakiwa kwa kuitwa mlozi mkubuhu, muuaji na shetani asiyestahili hata tone la huruma!

Japokuwa sifa hizi zilikuwa ni za kweli, Venet akaona amedharauliwa mno. Akajiona ameshushwa na sasa anafanana na taka shimoni. Si mwenye thamani. Lakini bado akavumilia.

Akiwa chini, Alphan akaweka mguu mgongoni mwake akimwambia:

"Ulidhani sitakukamata? Pole sana. Hatimaye mwisho wako umefika. Utatundikwa mbele ya kadamnasi kila mtu aone namna unavyopapatika ukitokwa na roho."

Alafu akamtemea kohozi ptuuh! Venet akatetemeka kwa hasira. Akajihisi moyo wake unasagwa na mche wa kinu. Akang'atameno kwa uchungu akimtazama Alphan kwa jicho la kizandiki, Alphan akatabasamu na kumkebehi.

Akifanya hayo wanajeshi wake wakawa wanashangilia kana kwamba bondia wa nyumbani anamshushia makonde bondia mgeni.

Mwishowe Venet, aliye katika mwili wa Rhoda, akafungashwa safari kuelekea lupango. Huko njiani akavutwa kama ng'ombe. Alikuwa peku akichomwa na miba na kutobolewa na mawe.

Watu njiani wakauliza kulikoni, wakaambiwa ni mlozi huyo. Basi nao wakaokota mawe na kumrushia, kama hayakuwepo wakamwagia mavumbi ama kumtemea mate!

Venet aliwezaje kuyavumilia yote haya?

Muda wote huo akawa anatazama chini akifunikwa na nywele. Alikuwa anautazama udongo anaoukanyaga. Mdomoni kuna kitu alikuwa anateta lakini hakikusikika.

Akafika lupango na kutiwa ndani akisukumiwa humo. Alikuwa peke yake katika chumba hiki, bila shaka walihofia kumchanganya na watu wengine kwasababu za usalama.

"Utakaa humo mpaka utakapokuja kuonja kitanzi!" Akasema Alphan akimuaga.

Basi huko nje kukawa sherehe kwenye kilabu cha pombe. Hatimaye mlozi amekamatwa! Watu wakanywa na kufurahi.

Habari zikasambaa ndani ya himaya nzima kwamba Rhoda ni mchawi na amekamatwa akitokea Tanashe. Habari hizi zikawashtua watu na kuwasisimua.

Mwaname yule mrembo, amekamatwa ulozi? Anhaa... basi ndo maana jengo lake likawa ghofu hivi ghafula? Ndiyo maana biashara yake ikatokomea kusikojulikana?

Watu sasa wakapata majibu. Kila mtu akawa anangoja kesho yake mwanamke huyo atundikwe kunyongwa kwenye uwanja wa hadhara. Wote waende kushuhudia!
**
"Mfalme, tumeshamtia nguvuni!" Akasema Alphan muda mfupi baada ya kuonana na mfalme, usoni akiwa na tabasamu pana.

Mfalme akatahamaki kidogo. Alikuwa yupo juu ya mgongo wa farasi akiwa ametoka safarini. Alimtazama vema Alphan aliyekuwa na pumbazo la furaha usoni, akamuuliza:

"Yupo wapi sasa?"

"Kule chimboni, unataka kumuona?"

"Ndio ila si kwa sasa. Naomba nipumzike kidogo, nadhani unaona nilipotokea."

Alphan akainamisha kichwa chake chini, mfalme akazama ndani alipopata kujimwagia maji na kisha kuketi mezani na mchumba wake, bibie Tattiana.

"Pole kwa safari," mwanamke akamkarimu.

"Ahsante, umeendeleaje hapa na upweke?" Mfalme akauliza kwa uso mtam.

"Upweke?" Tattiana akadakia kwa toni laini. "Sidhani. Nawezaje kuwa mpweke wakati kuna watu wengi hapa?"

Mfalme akatabasamu.

"Kwahiyo ulikuwa na nani akikusaidia kusogeza muda?"

"Watu wengi tu ... Nilikuwa nikiongea na wale wamama."

"Wamama? Unamaanisha wale vijakazi?"

"Sijiskii vizuri kuwaita hivyo. Ni watu wazima kama mama yangu!"

Mfalme akaangua kicheko kisha akamshukuru Tattiana kwa kumfanya afurahi kwani alikuwa ametingwa sana kichwani na hakutegemea kama atapata kuonja hata tabasamu mpaka siku hiyo inakoma.

Habari hiyo ikamvutia Tattiana, akataka kujua nini kilimsibu mfalme. Mbona alitoka na furaha kasrini?

Mfalme akanywa kwanza mvinyo alafu akashusha pumzi ndefu. Akawaamuru vijakazi wake wote wawapatie faragha kabla hajafungua jumba lake la maneno. Wakamtii.

"Kulikuwa na kikao huko himaya ya Mamu. Wafalme wote wa ukanda huu walikuwa wamekutana huko, nami nilipokea ujumbe wa kuhitajika.

Sikutaka kuupuuzia huo wito, nikautii. Lakini niliyokutana nayo huko, yamenitia simanzi na kunitetemesha mwili!"

Tattiana akashindwa kungoja,

"Nini hiko?' Akawahi kuuliza.

Mfalme akaminya mdomo wake akitazama meza. Alafu kwa utulivu akiwa mbali fikirani, akasema:

"Mfalme wa himaya ya Maam anakaribia kufa. Hivi tuongeavyo, yupo hoi taabani kitandani, ni pumzi tu ndiyo wanamhesabia. Hawezi kupona abadani. Anatia huruma sana, haswa nikiwatazama wajane na watoto atakaowaacha bado wakiwa wanamhitaji.

Lakini inaniumiza zaidi na kunikosesha amani kwani kifo chake kina mahusiano na mikono yangu!"

Hapa Tattiana akaogopa. Akatoa macho akikunjama ndita, akamuuliza mfalme kivipi ahusike na kifo cha mfalme wa himaya nyingine? Lini alienda huko akamshikia upanga ama kumtumia maadui wammalize?

Mfalme akamwambia hakuna lolote kati ya hayo aliyoyaainisha amepata kulifanya. Mfalme wa Maam anaweza akawa na maadui ndani ama nje ya himaya yake, hilo halikujalisha. Hakuna mtu anayependwa na wote.

Ila shida inakuja kwamba mfalme huyo amejazwa sumu na tunda la Cedar! Hapa ndipo panamtia hatiani kwani tunda hilo linapatikana ndani ya Goshen pekee!

Ni kivipi tunda hilo likafika huko na hata kutumika kumdhuru mtu huyo mwenye nafasi ya juu ndani ya himaya?

Kwahiyo Goshen inatuhumiwa kwa haya mawili. Mosi, kurudia biashara ya kuuza matunda hayo haramu yaliyopigwa marufuku. Na pili, baya zaidi, kutuhumiwa kufanya jaribio la kumuua mfalme huyo wa Maam kwasabababu zisizojulikana.

"Amah!" Tattiana akaufunika mdomo wake kwa bumbuwazi.

"Kwahiyo hivi tunavyoongea," mfalme akaendelea kumwaga maneno. "Nimepewa takribani siku tano tu kutoa maelezo na ushahidi. Litakaposhindikana hilo, basi hatua stahiki na kubwa zitachukuliwa."

"Zipi hizo?" Tattiana akataka kujua.

"Mosi, Goshen kutengwa na himaya zote na huku wananchi wake wakifanywa kuwa haramu katika kila ardhi watakayokanyaga. Pili, himaya zote kuungana na kuiteketeza Goshen kwenye uso wa dunia. Ama tatu, mfalme wa Goshen kunyongwa mpaka kufa kwenye karamu ya mwaka!

Adhabu itateuliwa kutokana na maelezo yatakayotolewa."

Tattiana akahisi moyo wake umekuwa mzito ghafla. Hata akastaajabu ni kwa namna gani mfalme aliweza kukenua kwa kicheko muda mfupi hapo nyuma.

"Sasa tutaepukaje kikombe hiki?" Akauliza akijawa na woga.

"Kwa njia moja tu," akajibu mfalme. "Nayo ni kumpata mtu aliyepanda, kuchuma na kusafirisha Cedar kwenda huko."

"Hakuna mbadala mwingine!" Akamalizia.

- JE WATAMJUA MTU HUYO KABLA GOSHEN NZIMA HAIJAHUKUMIWA?
- NINI TATTIANA ATAFANYA AKIJA GUNDUA BABA YAKE ANAHUSIKA NA HILI? JE ATAHISI CHOCHOTE?
- VENET ATATIWA KITANZI MBELE YA KADAMNASI?

[emoji91][emoji91][emoji91]
 
Karibia tunaimaliza sandarus
Inabidi utuandalie kitu kingine shunie cha kukonga mioyo maana sandarus ananiburudisha bado najifunza kiswahili maana lugha inayotumika uku inaboresha kiswahili changu lol
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom