Simulizi:Death Of Innocent

Simulizi:Death Of Innocent

*Sehemu ya 11*


Aliposhushwa kituo cha gerezani Isanga abiria wote waligundua kuwa harufu ile ilitokana na yeye, kwani waliona nguo zake zikiwa zimelowa mkojo.
“Hiloooo! Kubwa zima linajikojolea!” mpiga debe wa gari alimzomea.

Belinda aliumia sana moyo wake na kujikuta akilia machozi, hakupenda kuwa alivyokuwa ilikuwa ni bahati mbaya katika maisha, alikuwa ni mtoto wa tajiri kuliko mpiga debe aliyemzomea.

Alichechemea hadi gerezani ambako alijitambulisha kwa maaskari kama mke wa mfungwa Prosper, maaskari walimwambia siku hiyo ilikuwa si ya kuwaona wafungwa lakini alipowaeleza hali halisi iliyotokea na kwamba alikuwa akitokea hospitali maaskari walimwonea huruma na kumwingiza katika chumba alichokutana na Prosper mara kwa mara kabla ya kuugua na kulazwa hospitalini!
“Subiri tumwite!”

“Ahsante nasubiri!” Belinda alijibu.
Dakika chache baadaye Prosper aliingia chumbani akiongozana na mwanaume mwembamba mrefu aliyekuwa amemshika kiunoni, mtu huyo alionekana mgonjwa!

Alikohoa mfululizo na nywele zake zilikuwa nyepesi sana kichwani, alionekana ni kama mgonjwa wa Ukimwi, Belinda alipomwangalia vizuri mtu huyo alimtambua alikuwa ni Savimbi!

Belinda alishindwa kuelewa ni kwanini Savimbi alikuwa amekonda kiasi kile lakini hakutaka kuuliza, yeye na Prosper walikumbatiana na kusalimiana kwa furaha! Ulikuwa umepita muda mrefu sana bila kuonana.

“Huyu ndiye mtoto wako nimemleta umwone! Ila alitaka kunitoa roho, nashukuru Mungu leo niko hai!”

“Pole sana Belinda, ninajua unateseka sana kwa ajili yangu Mungu atakulipia!”
Waliongea mengi yaliyopita katikati yao, wakati Savimbi aliendelea kukohoa mfululizo na jasho jingi likimtoka! Hatimaye aliamua kutoka nje kwenda kupunga upepo.

“Kipenzi changu Pros, nipo nje napunga upepo mama!” Savimbi alisema na kunyanyuka kisha akampiga busu Prosper usoni na kutoka nje.

Belinda alipata uhakika wa kilichokuwa kikiendelea kati ya Prosper na Savimbi, alishindwa kujizuia na kuanza kulia mbele ya Prosper.

“Prosper tafadhali niambie ukweli nini kinaendelea kati yako na Savimbi nimejiuliza maswali mengi sana leo naomba unipe majibu!”

Prosper alimwangalia Belinda kwa macho ya huruma, alionekana mnyonge, alionekana kuwa na kitu moyoni alichotaka kukisema lakini alishindwa aanzie wapi.

“Tafadhali niambie Prosper vinginevyo mimi nakuacha narudi Dar es Salaam kwa baba yangu!”

“Usifanye hivyo Belinda!”
“Basi niambie!”
“Ninaweza kukuambia lakini tafadhali niahidi kitu kimoja!”
“Kitu gani?”

“Kwamba utanifichia siri na hutaniacha!”
“Itategemea Prosper! Lakini ni lazima unieleze vinginevyo naondoka nina wasiwasi kuna uhusiano mbaya kati yako na Savimbi kweli sio kweli?”

“Ni kw...eli Beli...nda! Nisa..mehe Beli..nda, Savi..mbi alinis..hawishi, alijifanya msamaria kwangu akawa ananipa chakula kizuri chenye mafuta, sukari nikafikiri ni mtu mwema lakini siku moja usiku niliamka na kukuta.....!”

Huku akilia machozi Prosper aliendelea kumsimulia Belinda kila kitu kilichotokea kati yake na Savimbi ndani ya gereza, lilikuwa jambo la aibu lakini alilazimika kuliweka wazi kwa sababu Belinda alitoka kufahamu.

“Ni kweli Belinda nisam...ehe mwenz’...angu, nisamehe mke wangu mtarajiwa, ni kweli Savimbi ananifanyia kitendo hiki! Alijifanya mweka kwangu tulipoingia gerezani akawa ananipa chakula kizuri, sukari, maji ya kunywa na kila nilipotaka kupigwa na wafungwa alinikingia kifua kwani mie ndiye nilikuwa mfungwa mdogo kuliko wote kwa wakati huo!

Kumbe alikuwa na nia mbaya ambayo mimi sikuifahamu tangu awali, hakuacha kunisifia eti nilikuwa na sura na umbile zuri, lakini mimi sikujali nilichukulia kitu cha kawaida kumbe alinitamani kimapenzi!”
“Halafu ikawaje?”Aliuliza Belinda kwa mshangao.

“SIku moja usiku nilizinduka usingizini na kumkuta akinipapasa mwili wangu, nilinyanyuka na kukaa huku nikimuuliza ni kitu gani alichotaka kufanya ndipo aliponieleza wazi kuwa alinitaka mapenzi mimi mwanaume mwenzake!”

Belinda alibubujikwa na machozi ya uchungu wakati akisikiliza maelezo ya Prosper jambo alilokuwa akilisikiliza haikuwa mara yake ya kwanza kulisikia alishalisikia kabla na alihisi lingekuwepo kati ya Prosper na Savimbi.

“Siku alipofanya hivyo ilikuwa ni usiku na wafungwa wote walikuwa usingizini, hakuna mtu aliyesikia kitu chochote, nilinyanyuka na kuanza kukimbia kwenda nje ambako Savimbi alinifuata na kuendelea kunishika ili aniingilie kwa nguvu.

“Aliweza?”Belinda hakuwa mvumilivu, alitaka kujua ni kitu gani kilitokea ingawa hakutaka kabisa mwisho wa habari hiyo uwe Prosper kufanya kitendo hicho.
“Hapana!”

“Afadhali, ulifanya kitu gani kujiokoa?”
“Nilichukua ubao mkubwa uliokuwepo na kumpiga nao usoni akaanguka chini na damu nyingi zikamtoka!”
“Kwa hiyo hakukufanya kitu?”
“Siku hiyo ndiyo!

Lakini asubuhi kulipokucha Savimbi alikuwa amenichukia sana hakusema na mimi kitu chochote na aliniambia kuwa ningekiona cha mtema kuni! Asubuhi hiyo sikupata chai aliyokuwa akinipa kila siku pia sikupata chakula wala maji!

Usiku ulipoingia nililala sakafuni kwani alininyang’anya godoro lake, hiyo haikutosha siku iliyofuata alitoa taarifa kwa mkuu wa gereza kuwa mimi nilimpiga kichwani na ubao baada ya kugoma kupasua kuni kitu ambacho hakikuwa kweli, kwa sababu yeye Savimbi alikuwa nyampara alisikilizwa zaidi na mkuu wa gereza kuliko mimi!

“Walikufanya nini baada ya hapo?”
“Nikaadhibiwa kwa kupigwa viboko ishirini na ni Savimbi huyohuyo aliyenichapa., niliumia sana!”Alisema Prosper kwa sauti ya upole.

“Pole sana Prosper sikujua kama ulipata mateso hayo yote sasa kwa nini hukuniambia?”

“Hukuwepo darling wakati huo wewe ulikuwa bado upo shule ulikuwa hujaja hapa Tabora!”
“Kiliendelea kitu gani baada ya hapo?”
“Gereza liligeuka Jehamanu kwangu!

Nilifanyishwa kazi ngumu, niliteswa kwa kunyimwa chakula na hata maji ya kunywa na katika muda wote wa mateso hayo Savimbi akawa anamhudumia kijana mwingine mwenye umri sawa na wangu ambaye aliingizwa gerezani muda mfupi baada ya mimi kukataa.

Kila mara Savimbi alinifuata na kuniambia kuwa nikitaka kuishi vizuri gerezani ilikuwa ni lazima tu nikubaliane na matakwa yake, bado nilikataa!”

“Hongera sana Prosper!”
“Ahsante lakini ngoja kwanza nimalizie kukusimulia kila kitu Darling!”
“Haya endelea?”

“Mwezi mmoja tu baadaye nilishangaa kuona savimbi akirejesha huduma zake kwangu tena! Nilishindwa kukataa kwa sababu ya shida na nikawa nakula chakula kizuri tena, akanipa godoro na kunipunguzia kazi gerezani, maisha yakawa mazuri, hakunieleza tena juu ya kufanya kitendo hicho lakini siku moja alinipa chai ya rangi jioni, baada ya kuinywa chai hiyo mwili ulilegea na nikapitiwa na usingizi na kumkuta Savimbi akinifanyia viba......!” Prosper alishindwa kumalizia sentensi yake na kuanza kulia, belinda nae alishindwa kuvumilia na kuanza kulia akiwa na mtoto wake mkononi!

“Nisamehe sana mke wangu! Nisamehe Belinda! Nililazimika kufanya hivyo kwa sababu ya shida, yalikuwa ni mateso makali mno!”Alisema prosper akiwa ameinamisha kichwa chini.

“Nini kilifuata?”
“Na baada ya hapo tuliendelea kufanya hivyo mara kwa mara, nisamehe belinda lakini pamoja na hayo yote bado nakupenda wewe pamoja na mtoto wangu na nitabadilika!”

“Prosper! Prosper! Ulishindwa nini kuvumilia mpenzi? Huwezi kuwa mwanaume wa kawaida tena!”Alisema Belinda huku akilia.
“Hapana Belinda nipo kawaida na ninakuahidi kubadilika na kama ikatokea nikatoka gerezani tuendelee na maisha yetu!”

“Prosper umeniumiza sana! Na kwa heri ya kuonana!”Alisema Belinda na kuanza kusimama wima alitembea hadi nje bila kugeuka nyuma, machozi yaliendelea kumbubujika na kulowanisha nguo zake, alikuwa ameumia kupita kiasi, hakutegemea kama mwanaume aliyempenda angeweza kutenda jambo hilo! Aliumia kiasi cha kuusahau hata ugonjwa uliokuwa ukimsumbua kwa muda mrefu!

*Je, nini kitaendelea?*
 
*Sehemu ya 12*


“Belinda! Belinda! Belinda! Tafadhali rudi mpenzi nisamehe sitafanya tena jambo hili!” Alimsikia Prosper akisema wakati akitoka nje ya gereza lakini hakutaka hata kuangalia nyuma! Kila alipoikumbuka picha ya Savimbi amemkumbatia mume wake alizidi kupata uchungu zaidi.

“Narudi kwa baba yangu siwezi tena kukaa hapa kama tu anayenisababishia mimi shida hizi ndiye aliyenifanyia ukatili huu!” Alisema Belinda wakati akitoka gerezani.

Hakuwa na nauli ya kulipia usafiri wa gari kutoka gerezani Isanga hadi Tabora mjini na isitoshe hakutaka kusababisha usumbufu kwa abiria kwa harufu aliyokuwa nayo hivyo aliamua kutembea kwa miguu mpaka mjini ulikuwa ni umbali mrefu lakini Belinda hakujali.

Maisha ya Belinda wakati huo yalikuwa tofauti sana na alivyokulia, hakuwahi hata siku moja kutegemea angekuja kuishi maisha ya taabu kiasi hicho wakati nyumbani kwa baba kulikuwa na kila kitu, lakini hiyo ndiyo hali aliyokuwa nayo.

Alitembea kama kilometa tano katika barabara ya vumbi mtoto wake akiwa mgongoni na mfuko wa rambo uliojaa nguo zake ukiwa mkono wake wa kushoto! Miguuni hakuwa na kiatu na miguu yake ilichanika ilikuwa si rahisi hata kidogo kufahamu kuwa Belinda alikuwa ni miongoni mwa watoto wa matajiri nchini Tanzania.

“Piiii! Piiii!Piii!” ilikuwa ni honi ya gari ikipigwa nyuma yake Belinda alikuwa akitembea katikati ya barabara bila kufahamu aliruka na kuangukia pembeni mwa barabara, dereva wa gari lile aliyempakia mwanamke aliyeonekana kuwa mkewe alimuonea huruma Belinda na kulazimika kukanyaga breki gari likasimama ghafla.

“Pole binti!”Alisema dereva baada ya kugundua kuwa alimshtua Belinda.
“Ahsante sana na samahani dereva!” Alisema belinda huku akijaribu kunyanyuka ardhini.

“Unakwenda wapi binti?”
“Nakwenda mjini Tabora!”
“Basi twende!”

“Hapana nyie nendeni tu mimi nitatembea kwani nina matatio!”
Belinda alikataa katakata kupanda ndani ya gari pamoja na dereva aliyeonekana kuwa mzee wa makamo kuendelea kumsisitia Belinda apande kitu cha nyuma cha gari na alipoona Belinda hataki kusikia aliteremka akachukua mzigo wake na kuuingiza ndani kisha akafungua mlango na kumwomba Belinda aingie, alifanya hivyo kwa shingo upande na safari ikaanza.

“Jamani samahani kama hali ya hewa itachafuka kidogo hapa ndani nina tatizo nililolipata wakati nilipojifungua!”
“Tatizo gani?”

“Nilitoboka tundu!”
“Aha! Una VVF siyo?”Mwanamke aliyekaa upande wa kushoto kwa dereva aliuliza.

“Ndiyo!”
“Usijali hili ni tatizo la kawaida tu kwa mwanamke hata mimi linaweza kunipata jisikie vizuri binti mimi naitwa Dk. Zubeda Katunzi ninafanya kazi hospitali ya Kitete wodi ya watoto na huyu ni mume wangu anaitwa Bwana Katunzi Katagile yeye ni afisa mifugo wa mkoa wa Tabora! Pole sana!”

“Ahsante mama!”
“Huyu ndiye mtoto wako wa kwanza?’
“Ndiyo!”

“Alikuwa mkubwa sana wakati wa kujifungua eeh ndiyo sababu akakusababishia tatizo?”
“Hapana alitanguliza mkono!”
“Mkono? hukuhudhuria kliniki wakati wa ujauzito wako?”

“Sikuwahi kwenda hata siku moja!”
“Pole sana na huku umetoka wapi?”
“Nimetoka gerezani ambako baba wa mtoto huyu ameshinikiliwa!”
“Pole sana na alifanya nini?”Mzee Katunzi Kategile aliuliza.
“Wanasema alimuua ma..ma ya....ke!”Belinda alishindwa kujizuia na kuanza kulia tena.

Mzee Katunzi na mke wake waliendelea kumbembeleza wakati gari likiendelea na safari mpaka Belind aliponyamaza. walimuomba awaeleze zaidi juu ya kilichotokea!

“Kwa hiyo wewe ni mtoto wa mzee Thomson.
“Ndiyo!Mimi ndiye mtoto wake wa kwana!”

“Oh my God! Why did Thomson do this?(Oh Mungu wangu kwanini Thomson alifanya jambo hili?) Alisema Dk. Katunzi.

“Hata mimi mwenyewe sifahamu!”
“Tunamfahamu baba yako sana na mara kwa mara huwa tunaonana naye Dar es salaam unataka tukusaidie nini binti?”
“Nataka kurudi kwa baba sitaki kitu kingine tena, nisaidie nauli ya treni ili niondoke siku yoyote kurudi Dar es Salaam!”Aliendelea kusema Belinda huku akilia machozi.

Gari lilikuwa likiingia mjini Tabora mzee Katunzi na mkewe walikuwa kimya gari liliendeshwa hadi nyumbani kwao eneo la Kanyenye mjini Tabora kitu cha kwanza walichofanya baada ya kuuingia ndani ni kumpigia simu mzee Thomson nyumbani kwake Dar es Salaam ili kumuuliza kama alikuwa na mtoot aliyeitwa Belinda.
“Belinda?”

“Ndiyo na tena ana mjukuu wako?”
“Hakuna mtoto mwenye jina hilo hapa kwangu, mzee Thomson alikata simu kwa makusudi ingawa alimfahamu Belinda alikuwa bado na hasira kali kwa Belinda baada ya kupata mimba na alijazwa maneno mengi ya chuki kutoka kwa mama wa kambo wa Belinda.

“Wewe msichana umetudanganya siyo?”
“Kwanini?”
“Mbona mzee Thomson anakataa?”
“Hapana huyo ni baba yangu kabisa!”
“Wewe ni tapeli?”

‘Hapana kama hamuamini nipeni simu mimi niongee naye!”Belinda alisema lakini hakuruhusiwa kuigusa simu.
“Tunasikitika hatuwezi kukusaidia kitu chochote binti!”
“Baba nisaidie tafadhali, nisaidieni kama mtoto wenu!”Alisema Belinda.

Mzee Katunzi na mkewe walimuonea huruma Belinda na kuamua kumsaidia pesa ya nauli kumrudisha Dar es Salaam peke yake na hivyo ndivyo ilivyokuwa kwani siku iliyofuata Belinda alikuwa ndani ya behewa daraja la tatu akielekea Dar njia nzima alilia machozi, aliumia sana kusikia baba yake alimkataa, pamoja na hayo bado alikuwa ameamua kwenda kuonana naye na kuomba msamaha!


Alijingia Dar saa 12 ya jioni na treni la abiria, kwa pesa kidogo iliyokuwa imebaki alikodisha teksi na kwenda moja kwa moja hadi nyumbani kwao.
“Niteremshe hapa hapa!” Alimwambia dereva teksi na kisha akamlipa pesa yake.

Baada ya teksi kuondoka alinyoosha moja kwa moja hadi getini ambako aliingia hadi ndani, watu wa kwanza kukutana nao walikuwa ni kaka zake wa kambo, walimwangalia kwa mshangao, alipowaamkia hakuitikia, waliendelea kucheza mpira wa kikapu katika kiwanja kilichokuwemo ndani ya ngome ya nyumba yao.

“Na wewe hicho kitoto chako unakipeleka wapi?” Walimuuliza Belinda kwa kejeli lakini hakuwajibu kitu alizidi kusonga mbele kuelekea nyumba kubwa waliyoishi.

Alikuwa nyumbani kwao kwa mara nyingine baada ya kukaa na kuteseka nje kwa muda mrefu, hakujua ni kitu gani kingetokea baada ya kukutana na baba yake lakini hilo hakulipa nafasi sana, alichotaka ni kukutana na baba yake na kumuomba msamaha basi!

Kabla hajaingia ndani mlango ulifunguliwa na baba yake alitoka nje na kumkuta, palepale sura yake ilibadilika.


*Je, nini kitaendelea?*
 
*Sehemu ya 13*


Belinda aliendelea kulia 
akiwa amemshika mtoto 
wake Alicia mkononi na Prosper aliendelea kumbembeleza asilie lakini hakusaidia kitu! Kadri alivyobembelezwa ndivyo Belinda alivyozidi kutokwa na machozi, alilia akimwangalia mtoto wake kwa macho ya huruma.

Alikuwa na wasiwasi na hofu kubwa sana moyoni mwake, alijua kama kweli kifo cha Savimbi kilisababishwa na Ukimwi basi hata Prosper alikuwa ameambukizwa! Na kama Prosper alikuwa ameambukizwa Belinda alikuwa na wasiwasi ni lazima na yeye pia alikuwa ameathirika kwa sababu alikutana naye kimwili na matokeo yake yakawa mimba iliyowapa mtoto wao Alicia.

Wasiwasi wake haukuishia hapo ulivuka mpaka hadi kwa mtoto wao, Belinda alijua kama yeye alikuwa ameathirika lazima na mtoto wao pia alikuwa katika hali hiyohiyo!

Hakuna kitu alichokiogopa maishani mwake kama ugonjwa wa Ukimwi! Aliujua ulivyotesa watu kabla ya vifo vyao, roho ilimuuma sana Belinda na kujikuta akimwaga machozi na kumtupia lawama nyingi Prosper.

“Prosper kwanini ulijiingiza katika mchezo huo na Savimbi?” Belinda aliuliza.
Badala ya kujibu swali aliloulizwa Prosper aliinamisha kichwa chini na kuendelea kulia, moyoni mwake alikuwa na maumivu makali na alijuta kwa uamuzi aliouchukua, hakuwa na namna ya kujitetea mbele ya Belinda, aliyoambiwa yote yalikuwa kweli tupu!

“Prosper naomba unijibu swali langu!”
“Darling huu sio wakati wa kunilaumu ninahitaji msamaha wako na msaada mkubwa wa mawazo! Niliingia katika mtego bila kujua hata mimi ninajuta!

Nina uhakika nimeambukizwa na mwisho wa maisha yangu upo karibu, ingawa najua nitanyongwa kwa kesi niliyonayo Mahakamani nisingependa hata kidogo kufa kwa Ukimwi! Nisamehe mke wangu” Alisema Prosper huku akilia.

Maneno ya Prosper yaliuchoma moyo wa Belinda na kumfanya agundue kuwa kweli hakutakiwa kumtupia lawama nyingi kiasi hicho kwa wakati mgumu aliokuwa nao! Hilo alilifahamu lakini bado maumivu yaliendelea kuwepo moyoni mwake, hakutaka kuukubali ukweli kuwa alikuwa ameambukizwa Ukimwi na hakuwa tayari kulipokea jibu hilo hata kama angepimwa.

Moyo wa Belinda haukuwa tayari kwa matokeo ya Ukimwi na alijua angekuwa marehemu siku moja baada ya kupewa majibu ya damu! Jambo ambalo hakutaka kabisa litokee kwa sababu kufanya hivyo kungemaanisha mateso kwa mtoto wake Alicia ambaye angekuwa Yatima tangu siku hiyo.

Alipenda sana kujua hali yake kiafya lakini aliogopa kupima damu! Alichofanya Belinda ni kumshawishi Prosper apime na majibu ambayo angepata ndiyo yangeonyesha kama alikuwa ameambukizwa au la!

“Lakini kuna watu huwa wanatembea na watu wenye virusi vya Ukimwi na hawaambukizwi, acha nisimtupie lawama nyingi sana Prosper mpaka apime damu yake inawazekana hakuambukizwa lakini hata kama ni hivyo nitawezaje kuwa na mwanaume shoga?” Alijiuliza Belinda bila kupata majibu ya maswali yake na machozi yaliendelea kumbubujika.

Muda mfupi baadaye huku Prosper na Belinda wakiendelea kulia mlango wa chumba ulifunguliwa na maaskari Magereza wawili wakaingia hadi ndani ya chumba walichokuwa wameketi Belinda na Prosper.

“Dada muda umekwisha tunakuomba sasa uondoke!” Alisema mmoja wa askari Magereza, mwanamke mwenye umri kati ya miaka ishirini na tano hadi thelathini aliyemwangalia Belinda kwa macho ya huruma.

“Ahsante dada naondoka sasa hivi!” Alijibu Belinda huku akinyanyuka na kumfunga mtoto wake mgongoni kwa kutumia khanga ndogo ya India.
“Belinda umenisamehe mke wangu?”

Prosper aliuliza wakati maaskari wakimnyanyua kutoka sakafuni alipokaa.
Belinda hakulijibu swali hilo alianza kutembea kuelekea nje ya Gereza, kichwani kwake kulijaa mawazo mengi kupita kiasi! Mbele yake aliona giza, kimawazo alijiona tayari yupo kitandani hoi akiugua Ukimwi kwa sababu tu ya uzembe wa Prosper!

“Wanawake wengi sana wanaponzwa na wanaume zao katika suala hili la Ukimwi, nimejitahidi kadri ya uwezo kuwa mwaminifu kwa Prosper lakini ameniangusha!” Aliwaza Belinda akitembea kuelekea kituo cha basi.

Mwili wa Belinda ulikuwa bado ukitoa harufu kwa sababu ya tundu alilolipata wakati wa kujifungua, kabla hajafika kituo cha basi kumbukumbu juu ya matatizo yaliyompata katika mabasi aliyopanda zilimrejea kichwani mwake, hakutaka kuzomewa tena na hakutaka tatizo lake limsumbue wala kumkosesha raha mtu yeyote! Kwa sababu hiyo Belinda aliamua kutembea kwa miguu kuelekea mjini Tabora.
****************

Aliingia Tabora mjini saa nane mchana jua likiwa linawaka kweli kweli, alitafuta kivuli na kuketi huku akitafakari nini cha kufanya, alipofikiria kwenda hospitali ya Kitete moja kwa moja alishindwa kwa sababu zilikuwa zimebaki siku saba kutimiza mwezi kabla hajarudi, alijua manesi wasingempokea mpaka tarehe aliyopewa kurudi hospitali ifike!

Uamuzi uliomwijia akilini mwake wakati huo ni kwenda kijijini Tutuo kusubiri mpaka tarehe ifike ndiyo aende hospitali kurekebishwa tundu lake, alisubiri kwa hamu kubwa sana siku hiyo!

Alitamani sana kupona na kurejea katika hali yake ya kawaida, alikuwa amechoshwa na kuzomewa pamoja na masimango aliyokuwa akiyapata.

“Na hili tundu ni kipimo tosha kama nina virusi vya Ukimwi au la! likipona nitakuwa sijaambukizwa lakini likikataa kupona nitakuwa navyo!” Belinda aliwaza kulingana na taarifa zilizokuwepo mitaani juu ya uponaji wa vidonda vya watu wenye Ukimwi.

Baada ya kuwaza kwa muda mrefu akiwa amekaa chini ya mti wa Mwembe karibu kabisa na shule ya sekondari ya Mihayo, Belinda alinyanyuka na kuamua kutembea hadi kituo cha basi ambako alipanda basi lililomfikisha hadi kijijini Tutuo, mtoto wake Alicia alilia kwa njaa lakini Belinda hakuwa na kitu cha kufanya ilikuwa ni mpaka afike nyumbani kwao na Prosper ndipo apike uji na kumpa.

Alisababisha usumbufu mkubwa sana ndani ya basi lakini hakuna mtu aliyegundua kuwa ni yeye aliyesababisha hali hiyo itokee, alipoteremka kituoni alitembea moja kwa moja hadi nyumbani kwao na Prosper, njiani watu wengi walionekana kumshangaa na hakuelewa sababu ilikuwa ni nini! Aliifananisha hali hiyo na mara ya mwisho alipokuja kijijini na kukuta mama yao Prosper amefariki.
“Sijui kimetokea nini tena leo?” Alijiuliza Belinda.

Mita chache kabla hajafika nyumbani alishangaa kuona ukuta mkubwa wa mabati ukiwa umekizunguka kiwanja chote cha nyumba ya akina Prosper! Belinda alishindwa kuelewa ni nini kilitokea ila alijua lazima kulikuwa na tatizo na aligundua ni kwanini watu walikuwa wakimshangaa.

“Nikusaidie dada?” Aliuliza mtu aliyemkuta mahali pale, aliyeonekana kama mlinzi.

“Nauliza waliokuwa wakiishi hapa wamehamia wapi?”
“Walikiuza kiwanja chao kwa mwarabu mzee Mohamed na sijui wamehamia wapi!”

Belinda aliishiwa nguvu miguuni na kujikuta amekaa chini bila kujua la kufanya, alishindwa kuelewa angekwenda nyumbani kwa nani na kuishi mpaka tarehe ya kwenda hospitali ifike! Kwa hali aliyokuwa nayo na harufu aliyoitoa alijua kusingekuwa na mtu ambaye si ndugu kijijini pale ambaye angevumilia kuishi naye ndani ya nyumba yake.
“Kwani vipi dada?”

“Kwani wewe hunifahamu mimi?”
“Ndiyo nilikuwa nakuona nyumbani kwa Mwarabu Mzee Mohamed lakini sikufahamu vizuri!”

“Nilikuwa naishi hapa na akina Nyamizi na Kasanda kabla sijaanza kazi nyumbani kwa Mwarabu mzee Mohamed, niliacha kazi nilipotakiwa kwenda kujifungua na baada ya hapo nilikwenda nyumbani kwetu Dar es Salaam na sasa nimerudi tena Tutuo nategemeo langu lilikuwa kufikia hapa hapa!”

Alisema Belinda huku akimtoa mtoto wake aliyekuwa akilia mgongoni na kujaribu kumnyonyesha lakini maziwa hayakuwemo kifuani kwake.
“Ukweli ndio huo dada sasa sijui utafanya nini!”

“Kaka yangu nina matatizo makubwa nafikiri hata hapo ulipo unasikia harufu ninayotoa, ni kazi ngumu sana kwa mtu yeyote kuishi na mimi ndani! Ninatakiwa hospitali ya Kitete kutibiwa ugonjwa wangu siku saba kuanzia leo yaani tarehe nne, ninachokuomba kama binadamu mwenzangu mwenye huruma nisaidie niwe naishi hapa ndani mpaka siku hiyo ifike!”

“Dada lakini nyumba hii itabomolewa tarehe tatu! Ninaweza kukusaidia mpaka tarehe mbili baada ya hapo itabidi utafute utaratibu mwingine sababu mzee Mohamed anataka kuweka mashine zake za kusaga”
“Ahsante sana kaka na sijui nikushukuru vipi!”

“Usijali dada yangu matatizo ni ya wote, nyumbani kwangu ni kijiji jirani lakini nitakusaidia chakula mpaka hiyo tarehe mbili, kila nitakacholetewa na mke wangu tutakula pamoja!”

“Mungu akubariki sana kaka yangu!” Alisema Belinda huku akinyanyua mfuko wake wa rambo na kuingia ndani ya ngome ya mabati baada ya mlinzi kufungua mlango.

Nyumba ilikuwa haijabomolewa ila ndani yake hapakuwa na kitu chochote, si kitanda wala jamvi! Kasanda na Nyamizi walishachukua kila kitu, Belinda aliwashangaa sana wasichana hao kwa kitendo chao cha kuuza shamba na kumsahau kaka yao aliyekuwa gerezani.

*Je, nini kitaendelea?*
 
*Sehemu ya 14*


Alichukua kitenge alichokuwa nacho ndani ya mfuko na kukitandika chini na yeye pamoja na mtoto wake wakalala na kujipumzisha, Alicia hakulala sababu ya njaa! Mlinzi ambaye baadaye Belinda alimtambua kwa jina la Juma alikuja ndani kuuliza ni nini kilikuwa kinasumbua.

“Ni njaa! Hajala kitu tangu jana na maziwa kifuani kwangu hayatoshi”
“Subiri nije!”

Mlinzi alitoka nje na aliporudi alikuwa na chupa ya maziwa na kumkabidhi Belinda.
“Mnyweshe hayo maziwa!”
“Ahsante sana kaka! Si ninahitaji kuyachemsha?”

“Ukiweza kufanya hivyo ni vizuri zaidi!”
Belinda aliipokea chupa na kuiweka pembeni alitamani kuyachemsha maziwa hayo lakini kwa sababu hakuwa na sufuria alishindwa na kulazimika kumnyesha Alicia maziwa ya baridi, alijua kulikuwa na magonjwa kama Kipindupindu, Kuhara, Kifua kikuu ambayo hutokana na kunywa maziwa yasiyochemshwa lakini yote hayo alimwachia Mungu.Baada ya kunywa maziwa hayo Alicia alitulia na kulala usingizi.
***************

Belinda alikaa ndani ya nyumba hiyo kwa msaada wa mlinzi Juma mpaka tarehe mbili nyumba ilipobomolewa! Hakuwa na mahali pa kuishi tena ilibidi ampe shukrani zake Juma na kupanda basi lililompeleka moja kwa moja hadi mjini Tabora, siku hiyo alishinda na kulala mtaani na siku iliyofuata saa kumi na mbili za asubuhi alikuwa ameshafika hospitali ya Kitete.

Saa mbili kamili aliingia katika chumba cha daktari aliyefurahi kumwona Belinda tena.

“Belinda mwanangu umerudi?”
“Ndiyo baba!”
“Pole sana najua umeteseka kiasi cha kutosha lakini mateso yako leo yanafikia mwisho!”

“Kweli baba?” Belinda alimuuliza daktari.
“Ndiyo mwanangu!” Alijibu daktari huku akiandika kitu fulani kwenye karatasi, alipomaliza alinyanyuka na kumwomba Belinda amfuate na waliongozana hadi katika chumba kilichoandikwa Laboratory! Wote wawili waliingia hadi ndani.

“Mzee Simba naomba umpime huyu binti damu!”
“Sawa daktari!”
“Daktari!” Belinda aliita.
“Naam Belinda!”

“Unataka kunipima damu?”
“Ndiyo! Ni lazima tujue!”
“Lakini mimi sitaki kufahamu!”
“Hutaki kufahamu nini?”
“Sitaki kufahamu kuwa nina virusi vya Ukimwi!”

“Siyo hivyo Belinda hatukupimi Ukimwi! Tunataka kufahamu una damu kiasi gani kwa sababu utafanyiwa operesheni leo”
“Kama ni hivyo sawa!” Aliitikia Belinda.

Daktari na mzee Simba wote waliangua kicheko kwa woga aliouonyesha Belinda.
“Kwanini mnaogopa sana kupimwa Ukimwi?” Daktari alimuuliza Belinda.
“Basi tu mimi sipendi!”

Usiku wa siku hiyo baada ya majibu kuwa mazuri Belinda alipelekwa chumba cha upasuaji na kurekebishwa kasoro yake akawa mwanamke kamili tena lakini wasiwasi wake uliendelea kuwa juu ya Ukimwi.
*****************

 Mwezi mmoja baadaye:
Hali ya Belinda ilikuwa nzuri kabisa, hakuwa na harufu tena! Furaha ilijaa maishani mwake kasoro pekee iliyomchukulia sehemu ya furaha yake ni tatizo la Prosper! Lakini aliendelea kujipa moyo kuwa huenda Prosper hakuambukizwa virusi vya Ukimwi na Savimbi.

Uhakika pekee angeweza kuupata kwa kuongea na Prosper mwenyewe na kupata taarifa za majibu ya damu aliyomwomba apime! Baada ya kutoka hospitali aliamua kwenda moja kwa moja gerezani Isanga lengo lake likiwa kwenda kuyaona majibu ya damu ya Prosper.
*****************

Prosper alikuwa amekonda na alionekana mwenye mawazo mengi kupita kiasi na muda wote wakati wakiongea aliendelea kulia akimwomba Belinda msamaha kwa yote yaliyojitokeza.

“Prosper nieleze juu ya majibu yako ya damu!” Belinda aliuliza.
Walikuwa watu watatu tu ndani ya chumba Prosper alipoanza kueleza kila kitu kilichokuwa kikiendelea mwilini mwake.

“Nieleze kwanza juu ya majibu, hayo mambo ya homa na kuharisha yaache kwanza, nieleze kwanza juu ya majibu nataka kujua ukweli huo!” Belinda alizidi kumbana.

Dunia ilionekana kubadilika 
na kuwa sehemu ya mateso 
makubwa kwa Belinda. Hakuamini kama binadamu wote waliishi katika shida kama alizokuwa nazo yeye, alibadili matatizo kama nguo! Likitoka hili linaingia jingine, Belinda alihisi kukata tamaa. Baya na lililomsumbua zaidi lilikuwa ni la virusi za Ukimwi ambavyo alihisi Prosper aliambukizwa na Savimbi katika mchezo wa wanaume kwa wanaume kuingiliana gerezani.

Belinda alikuwa ameamua kuufahamu ukweli wa majibu ya damu kutoka kwa Prosper ili auondoe wasiwasi moyoni mwake
“Ulipimwa damu?”Belinda alimuuliza Prosper!
“Ndiyo nilipima Belinda!”
“Majibu yako wapi?”
“Ninayo!”

“Nipe basi niyaone!”
“Naogopa kukupa!”
“Kwa nini? Wewe nipe tu!”
“Sijui kama utaweza kuyakubali!”
“Kwani una virusi katika damu yako Prosper?”

“Nd….i…o Belinda ila nisamahe sana!” Prosper alianza kulia machozi na alishindwa kumwangalia Belinda usoni.

“Kweli?” Belinda aliuliza tena, hakuliamini jibu alilopewa.
“Prosper tafadhali nionyeshe cheti chako cha majibu!” Aliendelea kusisitiza Belinda.
“Niamini na naomba unisamehe sana Belinda!”

“Nipe cheti Prosper siwezi kuamini hivi hivi!” Belinda alisema kwa ukali.
Katika maisha yake Prosper hakuwahi kumwona Belinda katika hali hiyo, ilimlazimu aingize mkono ndani ya kaptura yake, alionekana akivuta kitu fulani ndani ya nguo yake ya ndani na mkono ulipotoka ulikuwa na kikaratasi kidogo kilichokunjwa kikiwa kimelowa jasho alimkabidhi Belinda!”

Huku akitetemeka Belinda alianza kukikunjua kikaratasi hicho na kuanza kukisoma, kadri alivyozidi kusoma ndivyo machozi yalivyozidi k ummiminika hatimaye alijikuta akilia machozi huku kichwa chake akiwa amekiinamisha chini! Kilionyesha tayari Prosper alikwishaambukizwa virusi vya Ukimwi.

“Hivi mimi nina mkosi gani?”
“Wewe huna mkosi hata kidogo Belinda, mwenye mkosi ni mimi niliyewaua wewe na mwanangu bila hatia”
“Prosper ni heri ningekufa mimi kuliko Alicia ana makosa gani mtoto huyu?” Aliongea Belinda huku akizidi kulia.

Prosper alipomwangalia mwanae Alicia mikononi mwa mama yake naye alijikuta machozi mengi zaidi yakimtoka, alijilaumu kwa kila kitu kilichotokea na alijilaumu kwa kuua watu wasio na hatia, alijisikia mkosaji mbele za Mungu na mbele za Belinda na Alicia! Kwa kosa hilo aliamini hakustahili kuishi.

“Prosper nimejitahidi kuwa mwaminifu kwako lakini bado umeniua, nimeacha mambo mengi pamoja na utajiri wa baba yangu kwa ajili yako na ninateseka leo hii tena umenitia virusi vya Ukimwi mwilini mwangu!”

“Belinda ni shetani aliniingia usinilaumu sana Belinda utanifanya nikose sababu ya kuishi!” Prosper alipiga magoti mbele ya Belinda na kuanza kumshika miguu kama ishara ya kumwomba msamaha!
“Hii haitoshi Prosper umekwishaniua basi inatosha!”

“Sikujua itakuwa hivyo Belinda ilitokea kama ajali na kama ningepewa nafasi nyingine nisingefanya hivyo na ninajuta moyoni mwangu nisamahe Belinda kwa kukatisha maisha yako!”

Belinda hakujibu kitu alibaki amesimama wima mtoto wake akiwa mgongoni, alihisi akili yake kuchanganyika, ubongo wake kusimama kufanya kazi sawasawa, alijilaumu kwa kila kitu alichokifanya maishani mwake.

Hakuwa na kimbilio tena maishani kwake na alikiona kifo chake kikija kwa kasi! Katika maisha yake hakuna kitu alichoogopa kama kifo cha Ukimwi kwani kiliwatesa watu wengi na kilionekana kama kifo cha aibu na hakutaka kufa katika jina la umalaya kama jinsi watu wengi walivyokitafsiri kifo cha Ukimwi, Belinda aliamini hakuwahi kuwa malaya katika maisha yake.

*Je, nini kitaendelea?*
 
Back
Top Bottom