Wote tunakumbuka bajeti ya serikali iliyowasilishwa kwa mwaka 2022/23 ni TZS Trilioni 41.48 ikiwa ni ongezeko la 9.2% ukilinganisha na mwaka jana. Sehemu kubwa ya bajeti hii inategemea fedha za ndani (kwa zaidi ya 67%, hili ni jambo la kihistoria na la kipekee).
Baada ya uwasilishwaji wa bajeti ya mwaka 2022/23, wananchi wengi wameonyesha kufurahishwa na mipango ya serikali inayolenga kuboresha maisha ya mtu mmoja mmoja na ustawi wa taifa kwa ujumla, baadhi ya misamaha ya kodi iliyotolewa;
1. Kupunguzwa tozo katika miamala ya simu katika kutuma na kupokea fedha kwa zaidi ya 40%. (Tozo ya juu kabisa imepungua kutoka 7000 hadi 4000).
2. Kupunguzwa kodi(with holding tax) katika tasnia ya filamu kutoka 15% hadi 10%.
3. Kuondolewa kodi (zero rating) kwa bidhaa za mafuta ya kula (edible oils) ili kushusha gharama za bidhaa mbalimbali.
4. Kuondolewa kodi (zero rating) kwa mbolea inayozalishwa hapa nchini na vifaa mbalimbali vinavyotumika katika kupima udongo, net zinazotumika katika kilimo cha maua na mbogamboga pia vifaa vingine vinavyotumika katika horticulture.
5. Kuondolewa kwa kodi katika malighafi zinazotumika kutengeneza mitungi ya gas hapa nchini ili kuwezesha wananchi kupata huduma ya nishati kwa gharama nafuu.
6. Kuondolewa kwa kodi zinazohusisha vifaa/mahitaji muhimu ya viwanda vya usindikaji wa nyama, maziwa na samaki.
7. Kuhakiki madai ya ritani za VAT kidijitali. Hii inalenga kuwezesha sekta binafsi kupewa stahiki za madai yao kwa wakati.
8. Kutambuliwa rasmi kwa njia mbadala za kifedha. Hii inalenga ujumuishi katika huduma za kifedha kwa wananchi.
9. Asilimia 5 ya mapato ya Halmashauri kutumika kuboresha miundombinu ya wajasiriamali.
10. Kuondolewa kwa kodi katika mahitaji ya wakulima kama vile mbegu.
Hii ni baadhi ya misamaha na punguzo zilizowekwa katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kustawisha maisha ya wananchi, kuchochea shughuli za uzalishaji mali na kukuza uchumi wa taifa letu.